Riwaya: Matanga ya rohoni

Riwaya: Matanga ya rohoni

SEHEMU-43


[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Dr.Pesambili alitua barani Afrika nchini Tanzania kwa mara ya kwanza akiwa mtu mzima tokea achukuliwe akiwa ni mtoto mdogo kutoka kule nchini Kenya. Aliwasili Tanzania katika nchi ya asili ya wazazi wake, bila yeye mwenyewe kufahamu. Alikuwa amepata kibarua katika taasisi ya Afya yenye makao makuu nchini Marekani inayoitwa "The Centers for Disease Control and Prevention (CDC)", iliyo na matawi yake katika nchi mbalimbali duniani. Taasisi hiyo ilikuwa na miradi ya Afya nchini Tanzania, Mkoani Morogoro hivyo Dr.Trezguet au ukipenda Dr.Pesambili alikuwa ni mmoja wa Wafanyakazi kwenye taasisi hiyo. Alivyopangiwa kituo hicho kipya cha kazi, Dr.Pesambili alijawa na furaha sheshe. Furaha hiyo ilitokana na tamaa yake ya kwenda kuzuru nchi Kenya, sehemu ambayo alipewa taarifa na baba yake mlezi, Mr.Lorenzo kuwa ndipo alipochukuliwa kutoka kwenye kituo cha watoto yatima.

Dr.Pesambili baada ya kumaliza mafunzo yake ya vitendo alimzuru baba yake mlezi gerezani na kumdadisi vya kutosha kutaka kujua wapi ilipo asili yake. Ndipo Mr.Lorenzo bila kupepesa macho akamchana waziwazi kuwa alichukuliwa na msafara wa Papa John Paulo (II) kutoka kwenye kituo cha watoto yatima, Jijini Nairobi. Tokea hapo Dr.Pesambili akaanza kusaka nafasi za kazi kwenye Taasisi za Kimataifa kwa kutumia mtandao akilenga hasa maeneo ya nchi za Afrika Mashariki. Chambilecho mgaagaa na upwa hali wali mkavu, juhudi zake zikajibu akapata kazi nchini Tanzania. Furaha yake ya kupata kazi Tanzania ilitokana na kuwa kupitia somo la Jiografia alijua fika Tanzania na Kenya ni nchi majirani, wanaounda Jumuiya moja ya Afrika Mashariki, hivyo itamuwia wepesi kwake kukanyaga ardhi ya Kenya akitokea Tanzania, ili kuisaka asili yake. Taasisi ya "The Centers for Disease Control and Prevention (CDC)" mkoani Morogoro walikuwa wanajishughulisha na kutoa huduma za Afya majumbani, kwa kutumia magari maalumu, hospitali inayotembea kwa kuwapatia vipimo vya magonjwa bure na kuwapa matibabu. Nguvu kubwa ya hospitali inayotembea 'mobile hospital' ilielekezwa vijijini, sehemu ambazo kulikuwa na shida ya uwepo wa hospitali za kisasa.

Shirika la Afya Duniani 'WHO' kwa kawaida linapendekeza, daktari 1 atibu wagonjwa 300, lakini kwa Tanzania hali ilikuwa ni mbaya, daktari 1 huwa anatibu wagonjwa zaidi ya 20,000, hivyo Taasisi ya "The Centers for Disease Control and Prevention (CDC)" ikaonelea bora iwekeze nguvu vijijini kwenye upande wa kuboresha Afya. Kijiji alichokuwa anafanyia kazi Dr.Pesambili ndio kijiji ambacho alikuwa anaishi Mjomba Kobelo.


Mjomba Kobelo, alishahama zake kutoka kijiji cha Mikongeni na kuhamia kijiji cha Nyandira Mgeta wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro. Mkewe yule mkorofi sana aliyekuwa haishi kumshushia vipigo shadidi na mateso Deborah alifariki kifo cha ghafla siku chache tu baada ya Mjomba Kobelo kupokea malipo yake ya fidia ya kuhamishwa eneo walilokuwa wanaishi. Alikufa kutokana na mshtuko wa moyo baada ya Mjomba Kobelo siku moja kurudi nyumbani amelewa akija na stori za kuibwa pesa zote za fidia. Baada ya maziko tu, haukupita siku nyingi Mjomba Kobelo akahama kijiji na binti zake pamoja na dada yake mgonjwa, mama Deborah kuhamia kijiji kipya. Ndipo Dr.Pesambili katika mapito yake ya shughuli za kikazi akajikuta anafika katika nyumba ya Mjomba Kobelo. Akafanikiwa kumuona mama Deborah akiwa kwenye hali mbaya ya kupooza mwili. Dr.Pesambili kwa jinsi alivyokuwa na uchungu wa kukosa mama, alihuzunika sana kumuona mama Deborah wamemtelekeza, hapati huduma stahiki. Hima hima akamuanzishia matibabu, na kumuanzisha pia mazoezi ya viungo. Baada ya miezi kama mitatu (3), mama Deborah taratibu akaanza kuimarika afya yake. Kutokana na huduma mbovu nyumbani kwa Mjomba Kobelo, ikabidi Dr.Pesambili ajitolee kukaa nae mgonjwa wake nyumba moja na yeye.

Kwa Mjomba Kobelo kiroho safi akakubali, kwake ikawa ni nafuu kubwa kitendo cha Dr.Pesambili kumchukua mama Deborah na kuishi nae chini ya paa moja. Mgonjwa zamani hali yake ilikuwa mbaya sana kutokana na kukosa faraja toka kwa wauguzi wake. Lakini sasa chini ya mikono ya Dr.Pesambili alikuwa anapata lishe bora, huduma bora za afya na ushauri nasaha wenye kumpa matumaini mapya katika maisha yake. Baada ya kupita miezi sita (6) mama Deborah akaanza kutembea kwa kuchechemea kwa msaada wa fimbo. Ila kitu kibaya zaidi, homa ile ya kupooza ilimfanya mama Deborah asahau kumbukumbu nyingi sana maishani mwake.

Ilikuwa inakadiriwa kuwa itamchukua kama muda wa mwaka mmoja na nusu kuweza kufanikiwa kurudisha kumbukumbu zake za miaka ya nyuma. Mbaya zaidi Mjomba Kobelo akahama tena toka kijiji kile na kutokomea kusipojulikana huku Binti zake wote wakiwa wameshaolewa wanaishi na waume zao, kila mtu na lake bila hata kumpa taarifa Dr.Pesambili. Maendeleo ya Kiafya ya mama Deborah kila uchao yalikuwa yanampa faraja kubwa sana Dr.Pesambili, sasa mama Deborah kwake akageuka ndio kama mama yake mzazi. Akaajiri mtumishi maalumu wa kumpa huduma zote mama Deborah. Lakini Dr.Pesambili alikuwa anamlea mama yake wa kambo bila kufahamu. Mama Deborah nae alikuwa hajui kitu chochote kama Dr.Pesambili huyu mfadhili wake na daktari wake, mama yake mzazi ni Recho, ambaye ndio hasimu wake mkubwa, aliyemdhulumu mali za marehemu mumewe Bosi Minja na kumsababishia msongo wa mawazo uliosababisha mpaka apooze mwili. Mungu aliamua kumtumia Dr.Pesambili kumfanyia wema mama Deborah ili kufuta ubaya wa mama yake mzazi alioufanya kwa mama Deborah.

Mkataba wa kazi ulipoisha, Dr.Pesambili hakutaka kuongeza tena kandarasi yake. Aliamua rasmi makazi yake kuyafanya yawe Jijini Dar es Salaam. Alipolipwa mafao yake tu akanunua nyumba maeneo ya Mikocheni na kuhamia rasmi akiambatana na mama Deborah, ambaye kadri siku zilivyokuwa zinasonga alikuwa anazidi kuimarika kiafya. Sasa rasmi akazindua harakati za kumtafuta mama yake mzazi, kwa udi na uvumba. Ikabidi apange safari ya kuelekea Jijini Nairobi, Nchini Kenya kwenye kituo cha kulelea watoto yatima cha Cheryls Childrens Home and Learning Centre. Kituo hicho kinachomilikiwa na mtu binafsi, Mr.Ochieng kilikuwa kipo Katika mtaa wa Dagorretti Corner hatua chache kutoka barabara ya Ngong, Jijini Nairobi. Wakaagana vizuri na mama Deborah huku mama Deborah akimtakia kila la heri kwenye safari yake hiyo. Miadi walipeana kuonana baada ya wiki 2, ndipo Dr. Pesambili atarejea Jijini Dar es Salaam, hivyo akamuacha nyumbani na mtumishi wa kumpa huduma.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Alex na Deborah baada ya kumaliza mambo ya kesi, sasa walikuwa wanapika na kupakua pamoja, wanalala kitanda kimoja, wakijifunika shuka moja. Walikuwa ni wapenzi rasmi wapendanao 'Love Birds' wasiojificha tena, kila kitu hadharani. Muda wa kazi ulikuwa unapoisha tu, basi popote utakapomuona Alex basi Deborah yupo nae sako kwa bako. Wale wenye vijiba vya Roho, mahasidi wasiopenda kuona watu wakipendana mapenzi ya kweli, roho zao zilikuwa zinakaribia kuwachomoka kwa wingi wa chuki katika mioyo yao.

Chuki zilianzia Ofisini kwake Alex, wapo wasichana waliokuwa wanajiona wana sifa na vigezo vya kuwa wapenzi wa Alex kutokana na uvaaji wao nadhifu wa nguo za gharama na namna wanavyojua kwenda na wakati, lakini tahamaki Alex kadondokea kwa Deborah. Mwanamke ambaye kwa mtazamo wao ni mshamba, nywele zake anasuka mtindo wa twende kilioni. Magauni yake ya mshono wa mfuko wa mashineni kama muimba kwaya kanisani, na ngozi yake ya asili haipakwi cha ziada zaidi ya mafuta ya mgando. Walichokuwa hawakifahamu ni kuwa Alex alikuwa anatafuta mke mwema na sio gubegube linalojishebedua kwa uzuri wake.

Baada ya miezi mitatu (3), majibu ya Deborah ya kidato cha 6 yakatoka, huku akiwa amepata ufaulu wa daraja la kwanza. Alikuwa amechaguliwa kujiunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam 'UDSM' kusomea Uhandisi wa Chakula 'Food Engineering'. Alijawa na furaha chekwachekwa kwa kuchaguliwa kozi hiyo ambayo ingempa wigo mpana wa kujiajiri mwenyewe kwa kufungua kiwanda cha kusindika vyakula hasa katika zama ambazo ajira rasmi zilikuwa ni finyu sana. Lakini furaha yake hiyo ilitumbukia nyongo baada kutokupata mkopo toka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi Tanzania 'Higher Education Student's Loan Board'(HESLB). Vigezo vyote vya kuweza kupatiwa mkopo alikuwa anakidhi lakini Mrs.Tonny ndio aliyechafua hali ya hewa. Kumbuka alimpa ahadi ya kumfadhili kwenye elimu ya juu hivyo Deborah katu hakujishughulisha na kujaza fomu za maombi ya mkopo huo. Lakini mpenzi wake Alex akatekeleza msemo wa ukipenda boga penda na ua lake, hivyo akajivika rasmi mzigo wa kumsomesha. Alex hakutaka kufuata maneno ya mtaani ya kuwa mchumba hasomeshwi utakuja kulia kilio cha kusaga na meno. Alimuamini Deborah zaidi ya hata anavyoiamini nafsi yake, ya kuwa hawezi kamwe kuja kumgeuka pindi atakapohitimu masomo yake ya Chuo Kikuu.

Kwa kutumia mshahara wake, Alex akakopa pesa za kumlipia ada Deborah na matumizi ya kujikimu chuoni. Muda wa kuripoti Chuoni ulipowadia, Alex akamsindikiza Deborah mpaka Chuoni. Wakakamilisha taratibu zote za Chuo zinazohitajika na Deborah akapangiwa kuishi Hosteli za Mabibo zilizopo barabara ya Mandela jirani na eneo la Ubungo. "Mpenzi Deborah, nakutakia masomo mema, kikubwa kumbuka kulinda ahadi yetu, ya kuwa tutakuja kuoana pindi utakapomaliza Chuo. Jitahidi kujilinda na vishawishi vya kila aina. Upo ndani ya Jiji la Dar es Salaam lenye watu wa kila sampuli, wenye uwezo hata wa kukuhonga nyumba na magari ili mradi wavuruge penzi letu. Lakini kumbuka pia maisha ya Chuo ni matamu sana lakini ni mafupi mno, ukivuruga muelekeo wako ndani ya miaka 4, utakuja kujutia maisha yako yote, hivyo akili kumkichwa chako" alizungumza Alex kwa hisia kali, nasaha ambazo zilimtoa machozi Deborah pindi walipokuwa wanaagana hapo Mabibo Hosteli.


Deborah hakuwa na maneno mengi zaidi ya kushukuru kwa hisani ya kusomeshwa na mpenzi wake, kipindi ambacho aliona kabisa ndoto yake ya kielimu inataka kutoweka. "Nakuahidi sitokuangusha, nitalilinda penzi letu kwa hali na mali, na nitasoma kwa bidii ili kuhakikisha ninapata maarifa stahiki. Nakuahidi pindi nikimaliza Chuo nitafungua kiwanda cha kusindika nyanya kule kule Mzumbe, na hutojuta kwa pesa ulizonilipia ada, tutakuwa matajiri wakubwa tu. Nataka siku moja tukae meza moja na hasimu wetu Mrs.Tonny tukiwa tunaongea lugha moja ya uwezo wa kipesa" aliongea Deborah kwa furaha huku akimpa matumaini makubwa mpenzi wake Alex.

Wakaachana, siku zikaanza kusonga, miezi kadhaa ikakauka, huku Deborah akijihesabia kuwa yupo sasa yupo salama salimini, ndani ya mikono ya mtu makini kama Alex. Likizo ndogo zote alikuwa lazima arejee Mzumbe kwa Alex. Nae Alex kwa upande wake, majukumu ya kazi yaliongezeka hivyo kumfanya muda mwingi awe anautumia ofisini. Akitoka saa 1 asubuhi kurudi kwake ni saa 1 usiku. Sana sana mapumziko yake rasmi yalikuwa ni siku ya Jumapili, hali ambayo ilimlazimu kuajiri mtumishi wa kike wa kuja na kuondoka kwa ajili ya usafi wa nyumba, kufua nguo na kupika chakula. Kabla ya kuajiri mtumishi huyo, alipata baraka zote za Deborah hasa baada ya kuthibitisha uzito wa majukumu aliyo nayo mpenzi wake hivi sasa.

Lakini kama ujuavyo ya kuwa Deborah ni mtu wa mikosi, daima hawezi kupata starehe ya kukesha mpaka che, lazima tu kitokee kitu cha kuchafua hali ya hewa, akajikuta anaingia kwenye mgogoro wa mapenzi na Alex. Mgogoro ambao ulisababisha penzi lao lisambaratike vipande vipande, na kumuacha Deborah yupo njia panda hajui cha kufanya.

Mgogoro wao ulianza wakati wa likizo ndogo ya karibu na mapumziko ya Sikukuu ya Pasaka, Deborah akiwa ndio kwanza amerejea toka Chuoni, ghafla yule dada wa kazi za ndani akatoweka bila taarifa. Simu yake ikawa kila ikipigwa ili kufahamu ana tatizo gani lililomfanya asije kazini ikawa haipatikani. Wakakubali matokeo kuwa huenda kazi imemshinda au kapata sehemu nyingine yenye maslahi zaidi ya hapo.
Asubuhi yake iliyofuatia, wakati Alex yupo kazini hana hili wala lile, Deborah akiwa kwenye harakati za usafi wa nyumbani akaifuma barua iliyokuwa imesokomezwa chini ya sofa ukumbini. Kichwa cha habari juu ya bahasha ya barua hiyo, alipokisoma tu kilimpa mshtuko mkubwa Deborah. Jasho jekejeke likaanza kumtiririka mwilini mwake huku mapigo ya moyo wake yakienda mbio. Akajikuta anaishiwa nguvu na kuamua kukaa kitako chini ya sakafu ili aisome vizuri barua hiyo mbaya. Akajikuta ghafla anatetemeka mwili mzima kama mgonjwa aliyepigwa na homa kali. Vidole vya mikono vilikuwa vinamtetemeka mithili ya mnywaji gongo aliyekubuhu. Kwa ufupi Deborah alijihisi kufa kufa.

Hakuamini mtu aliyemwamini na kumthamini kama Alex angeweza kumtenda kiasi hicho. Kilichokuwa kinampa mawazo ni kuwa ataiweka wapi sura yake kwa mashosti zake wa Chuoni ambao kutwa kucha alikuwa anawatambia kuwa amepata mpenzi mwenye kujiheshimu na anayempenda kwa dhati. Licha ya wenzake kumtahadharisha kuwa asiweke matumaini asilimia 100% kwa mwanaume, lakini Deborah alikuwa anamkingia kifua Alex. Sasa leo kupitia barua hiyo alikuwa anaonjeshwa asali kwa ncha ya kisu. Deborah akajikaza Kisauni na kujitutumua kuifungua barua hiyo.


Barua ambayo juu ya bahasha kulikuwa na maandishi ya herufi kubwa, "KWAKO MPENZI ALEX". Ndani ya barua sasa kulikuwa kunasomeka kama ifuatavyo; "Mpenzi Alex, nimeamua kukuachia ujumbe huu kama nilivyokuelekeza kwenye meseji ya simu yako kuwa utaukuta chini ya sofa lako unalopenda kukalia. Nimeamua kupotelea kusipojulikana kutokana na shinikizo lako la kutaka nitoe mimba uliyonipa ili mchumba wako asijue kama nina mimba yako. Nakutakia kila la heri katika maisha yako na huyo mchumba wako unayempenda sana kuliko mtoto wetu aliye tumboni mwangu. Nitamlea peke yangu bila kuhitaji msaada wako wowote lakini hesabia huna mtoto na mimi". Deborah alipomaliza kusoma barua hiyo alijikuta anajiona anaishiwa nguvu na kujilaza kwenye zulia la pale sebuleni. Kifua chake kilikuwa kinafukuta fukuto la joto la hasira dhidi ya Alex. Mawazo lukuki yalimvamia kichwani mwake, huku Ibilisi akimpandia kichwani na kumshadidia ajiondoshe uhai wake. Alijilaumu sana kukubali kuwa mpenzi wa Alex bila hata kupata nafasi ya kumchunguza tabia zake kiundani.

"Ina maana kipindi chote nipo Chuoni, huyu dada wa kazi alikuwa ndio alikuwa anajinafasi, ama kweli paka akitoka panya hutawala" alijisemea kimoyomoyo Deborah na kuamua kuinuka pale alipojilaza. Akili yake ilimuambia aifiche ile barua, ili aone mwisho wa sinema hiyo mpya kwake ya mapenzi baina ya Alex na dada wa kazi. Deborah akiwa hana hili wala lile, akashtukia mlango wa barazani unafunguliwa kwa kishindo, kisha Alex akaingia ndani ya sebule. Bila kuzungumza na mtu yoyote akaenda kukaa kwenye sofa lile lile aliloelekezwa kuna barua yake.

"Kulikoni mbona salamu unatuvamia, umepatwa na maswaibu gani mwenzangu mbona unanitisha..!" alisema Deborah huku akijikaza kutokumuuliza chochote kuhusiana na barua ile ili amuone kama atakuwa mkweli na kueleza kinagaubaga bila mficho. "Aaaah....take easy hamna kitu nimekuja kunywa chai tu, tayari umepika..?" aliongea Alex huku akilazimisha tabasamu. "Tayari ipo mezani, ingawa hukunipa taarifa kama utakuja kunywa chai nyumbani maana huna kawaida hiyo ukiwa kazini" Deborah alizidi kumfunga Alex ili kumtengenezea mazingira ya kuelezea kitu kinachomsumbua. "Hapa si nyumbani kwangu? usiwe na mashaka nimeamua tu kukufanyia surprise..twende basi tukapate wote staftahi" alijibaraguza Alex huku ameuviringisha mkono wake kwenye kiuno cha Deborah. "Ahsante mpenzi, lakini mie nimeshakunywa, sasa naenda kujipumzisha chumbani sijisikii vizuri, nimekunywa dawa za kutuliza maumivu " alisema Deborah huku akiutoa mkono wa Alex kiunoni mwake na kuelekea moja kwa moja chumbani kwao. "Pole sana, kapumzike unono..." alisema Alex huku akimuangalia Deborah namna anavyomalizikia kuelekea chumbani kwao.

Alex alivyomuona Deborah ameshamalizikia kuingia chumbani akarudi kwa kasi pale sebuleni mpaka kwenye sofa lake analopenda kukalia. Akalinyanyua kuitafuta barua aliyoelekezwa na mtumishi wake aliyetoweka. Alex tokea alipopata ujumbe wa kwenye simu ya mkononi, alikosa amani kabisa ya kuendelea kufanya kazi ofisini. Alijutia kitendo cha kumkubalia kuwa mtumishi wake wa nyumbani, mpaka akamuingiza kwenye mtego uliosababisha atembee nae kimapenzi. Siku ya kwanza Alex kumuona dada huyo alivyokuwa kuomba kazi hakuamini kama kweli dada huyo anatafuta kazi za ndani hasa kutokana na urembo wake wa shani. Urembo ambao ulimbabaisha Alex vilivyo na kumkubalia ombi lake, huku akijifanya kuomba ushauri kwa mpenzi Deborah ili kuondosha fikra potofu. Mpaka anavyopokea ujumbe huo wa simu alishakuwa ametembea nae si chini ya mara mbili. Lkini anachokumbuka ni kuwa mara zote alizofanya nae mapenzi alitumia kondomu, hakufanya ngono uzembe sasa mimba hiyo amepataje, ni kitu kilichokuwa kinamfanya achanganyikiwe vilivyo.

"Kama Deborah aking'amua nitambeba na mbeleko gani apate kunielewa kuwa ni shetani tu amenipitia..! " alijisemea peke yake Alex kimoyomoyo huku akiwa anaendesha lile sofa alilonyanyua. Deborah mchezo wote anaoufanya Alex wa kuitafuta barua chini ya sofa alikuwa anaushuhudia kupitia upenyo wa mlango wa chumbani. Alipojifanya anaenda kulala, ilikuwa ni janja ya nyani tu, ili kumpa nafasi Alex ya kujitawala sebuleni. Deborah akajithibitishia mubashara bila chenga kuwa Alex ni kweli kambandika mimba dada wa kazi kutokana na juhudi zake za kutaka kuinyakua barua hiyo. Deborah akajikokota kinyonge mpaka kitandani na kujitupa kama furushi la mwizi. Macho yake yalikuwa yanabubujikwa machozi bila ukomo, huku akiwaza na kuwazua maamuzi ya kufanya juu ya penzi lao. Mawazo mengine yakimshawishi aachane na Alex aanze maisha yake upya katika ulimwengu wa huba, lakini kikwazo kikaja kwenye suala la kusomeshwa, nani atakuwa tayari kumlipia ada ya Chuo Kikuu na gharama zingine kama anavyofanya Alex. Akajiona kabisa analazimika kuwa mtumwa wa Alex kwa sababu tu za kiuchumi lakini tayari alishamfuta thamani kwenye moyo wake.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Koh...Koh....Koh....Koh....fungua mlango...!" ilikuwa sauti nzito iliyoshiba ikishinikiza yeyote aliyekuwa ndani ya nyumba ya Alex afungue mlango. Deborah akiwa jikoni anakarangiza maakuli ya jioni, wito huo ukamshtua kidogo. Akawa anasikilizia wito huo akijaribu kutaka kutanabahi sauti hiyo ni ya nani. Alipozidi kusikia wito huo ukitaka mlango ufunguliwe, ikabidi akurupuke na kanga moja kwenda kufungua mlango huo kujua kulikoni. Alipoufikia mlango huo na kuufungua mshtuko wa ghafla ulimshika. Alihisi mapigo ya moyo wake kama yanataka kusimama kwa ghafla. Akajikuta miguu yake haina ushirikiano na sehemu ya juu ya mwili wake, ikaanza kushindwa kuhimili uzito wake, akajikuta anachegama mlango huo ili kupata msaada wa kuegemeza mwili.

Alimuona Alex akiwa amefungwa pingu za mikononi huku machozi yanamtiririka machoni mwake. Deborah alikuwa anatamani afungue mdomo wake aulize kulikoni lakini akajikuta anapatwa na gagaziko la ulimi hawezi kuongea chochote. "Ingia ndani, unatuchelewesha fisadi mkubwa wewe" aliongea yule mtu mwenye sauti nzito aliyekuwa anagonga mlango. Walikuwa ni askari kanzu wawili wameambatana na Mtendaji kata wakimleta Alex nyumbani kwake. Majirani nao waliokuwa wamebakia nyumbani muda huo nao wakaanza kujongea kutaka kujua kulikoni.

"Dada habari yako, sisi tumekuja kufanya upekuzi nyumbani kwa mtuhumiwa huyu Bwana Alex kutokana na tuhuma za kuomba rushwa ya ngono kwa mwanafunzi wake. Hivyo tumekuja kukagua mitihani ya wanafunzi wake aliyosema amehifadhi nyumbani kwake ili wana usalama iwasaidie kwenye taftishi yao dhidi ya mhadhiri Alex. Hivyo kuwa na amani kwa sababu tumekuja kisheria" alisema Mtendaji Kata nia na madhumuni ya ujio wao pale nyumbani. "Sawa hamna shida, kwani amefanyaje mpaka mnamtia pingu kama jambazi? " alijitutumua Deborah kuuliza kwa tabu akitaka adadavuliwe kwa undani tuhuma hizo. "Dada usichoelewa kitu gani, huyu jamaa yako tumemkata ofisini kwake leo saa 9 alasiri akijiandaa kufanya mapenzi na mwanafunzi wake ofisini kwake..! " aliongea yule askari kwa kufoka huku akimhimiza Alex asonge ndani ya nyumba hiyo akaonyeshe mahali anapohifadhi nyaraka za wanafunzi wake. Deborah akabaki amesimama mlangoni amebung'aa kwa mshangao anawasindikiza kwa macho. Alex wakati wote alikuwa anatikisa kichwa kuonyesha hakubaliani na tuhuma hizo, ukweli halisi wa tukio hilo alikuwa anaujua Alex na huyo mwanachuo aliyetoa taarifa kwa vyombo vya dola juu ya kusumbuliwa rushwa ya ngono ili apewe maksi za kumfaulisha kwenye somo analofundisha Alex.

Baada ya nusu saa ukaguzi wao ukakamilika huku wakiondoka na mitihani ya wanafunzi waliyoikuta nyumbani kwa Alex. "Naomba umfahamishe mama yangu mzazi tukio lote..!" aliongea Alex kumpa maagizo Deborah huku akikwepesha macho hataki kuangaliana uso kwa uso na Deborah. Alichofanya Deborah ni kuitikia kwa kichwa, kuonyesha kuwa atatekeleza maagizo hayo. "Mshahara wa dhambi ni mauti, umeumbuka Alex, umempa mimba dada wa kazi na leo leo kabla jua halijakuchwa unapigwa kofi lingine la rushwa ya ngono, Ahsante sana kwaheri..!" alisema Deborah baada kulisogelea gari la wazi lililotumika kumbeba Alex kwa upande wa nyuma. Alex hakuwa na kitu cha kujibu, soni ilimjaa usoni kwake, macho yake yamemwiva wekundu.

"Kumbe barua chini ya sofa kaichukua Deborah..!, ama kweli siku ya kufa nyani miti yote" hizo zilikuwa ndio fikra za Alex wakati huo. Gari hilo likaondoka eneo hilo kwa manjonjo likiwaacha majirani midomo wazi kila mtu anasema lake. Deborah haraka haraka akaingia ndani ya nyumba na kujifungia kwa komeo. Alijua majirani wale habari kuuzwa ndio wakati wao muafaka wa kuja kuchokonoa mambo ya watu. Watamuingia kwa gia za kumpa pole kisha waanze kumdadisi undani wa tukio la Alex. Alipoingia ndani Deborah akatuma meseji kwa mama yake mzazi Alex akimuelezea tukio zima kisha akazima simu yake kukwepa maswali, baada ya hapo akaanza kupanga nguo zake na vifaa vyake mbalimbali kwenye begi lake la safari. Alishajua penzi lake na Alex ndio limekufa rasmi, kwani lazima atafungwa jela kwa kosa la kuomba rushwa ya ngono.

Moyoni mwake aliyakinisha asilimia 100% kuwa Alex amehusika hasingiziwi hasa akirejea tukio la kumtundika mimba dada wa kazi. Pia hata kama angeendelea kukaa hapo lazima angetimuliwa katika nyumba na Uongozi wa Chuo cha Mzumbe ili kupisha watumishi wengine wasio na makazi. Kilichokuwa kinambangua kichwa ni kuwa anaelekea wapi akitoka hapa nyumbani kwa Alex, na nani atamlipia ada Chuoni na kumpa pesa za matumizi hali ya kuwa ni kesho kutwa tu Chuo kinafunguliwa. Chakula chake alichokuwa anakipika jikoni hakuwa na hamu nacho tena, akakitekeleza huko huko. Akiwa na begi lake pembeni akaa juu ya sofa sebuleni anatafakari. Muda ulikuwa inayotoka, magharibi ilikuwa inakaribia, muda muafaka aliopanga kuondoka huku kukiwa na kigizagiza kukwepa fedheha mbele ya majirani. Ghafla bin vuu akakurupuka kwenye sofa na kuanza kufungua begi na kuchambua vitu vyake pembeni ya begi kana kwamba kuna kitu anatafuta. Akaunda tabasamu jepesi baada ya kukiona kitu alichokuwa ananitafuta. Alikuwa anatafuta kadi yenye anuani na namba za simu za mfadhili wake mpya Timammy alizompa siku alipomchomoa mikononi mwa Mrs.Tonny kule mahakamani kwa kumuwekea dhamana. Tokea siku ile alipomtafuta mara moja na hakumpatana hewani hakujisumbua tena kumtafuta. Lakini leo alikuwa ametumbukia kwenye dhiki yenye kuhitaji utatuzi wa haraka hakuwa na jinsi zaidi ya kumtafuta tena, kama ujuavyo mficha ugonjwa mauti humuumbua. Sakata lake lilimfikisha mahali pa kuchagua kusuka ama kunyoa, hivyo ampige pande Timammy afukuzwe Chuo kwa kukosa ada au amtafute Timammy amuombe tena msaada wa kusomeshwa ili aweze kuhitimu Chuo.

Deborah alijawa na matumaini kuwa atamuelezea kila kitu Timammy kuwa Mrs.Tonny ndio alimuingiza chaka asiombe mkopo kwa kujimwambafai kuwa atamsomesha akaishia kumtelekeza machakani. Akatoa simu yake kwenye pochi la mkononi, na kuanza kuingia namba kwa ajili ya kuipiga simu ya Timmamy. Bila mafanikio yoyote namba zote za Timammy zilizokuwa zimeorodheshwa kwenye kadi ile zilikuwa hazipatikani. Jasho jekejeke likaanza kumvuja Deborah huku machozi yakianza kumlengalenga upya machoni mwake. Matumaini yake aliyaona kabisa mithili ya mshumaa uliowashwa kwenye uelekeo wa upepo mkali. Akaanza kuvuta tafakuri jadidi ya maisha yake upya tokea azaliwe mpaka leo yupo Chuo Kikuu akajiona kabisa hajawahi kabisa kuishi maisha ya kula bata kama walivyo wenzake, yeye kila siku kidagaa kinamuozea yeye tu. Machozi sasa yakaanza kumtiririka kwa wingi bila kizuizi na kilio cha kwikwi. Ghafla akanyamaza kulia, akatoa hanchifu yake kwenye pochi yake na kujifuta machozi yote. Akachomoa noti ya sh.5,000/= na kufungua mlango wa sebuleni atoke nje. Alipanga kwenda duka la dawa kununua vidonge ili avibugie afilie mbali. Alishakata tamaa ya kuishi, hakuona tena thamani ya maisha ya dunia, kwake aliona bora awafuate wazazi wake waliotangulia jongomeo. Kabla hajanyonga kitasa cha mlango, simu yake ikaanza kuita kwa fujo. Akairudia alipoangalia ilikuwa ni namba binafsi 'private number' akaikata na kuizima simu kabisa kisha akairudisha kwenye kipochi tena.

Akachomoka mbio mbio kuelekea duka la dawa, bila kutanabahi kuwa ile simu aliyoikata ni ya mfadhili wake Timammy aliyekuwa anamtafuta kwa udi na uvumba muda mchache uliopita. Ama kweli hasira hasara, Deborah alikuwa kama vile anapiga teke furushi la pesa, anapishana na ngekewa. Baada ya dakika takribani 10 Deborah akawa anarejea akiwa na tembe zake mkononi. Akiwa meta chache kabla ya kufika nyumbani akashtuka kuona gari la kifahari aina ya 'Vanguard' limeegeshwa upenuni kabisa mwa nyumba ya Alex. Akasita kwenda mbele akasimama, akiwa ameshtushwa roho yake kuwa huenda amekuja kukamatwa yeye sasa. Akiwa bado amepigwa na mzumbao akaliona lile gari limeamshwa linageuzwa na kuanza kuja uelekeo wake pale aliposimama. Deborah hakuwa na simile tena, akageuka, akavitupa vile vidonge na kutaka kuanza kutimua mbio, tayari alikuwa ameshachanganyikiwa, anaona kabisa penzi lake na Alex linampiga pute furaha yake katika maisha. Kichwa chake kilikuwa ni kama dampo ya mawazo machafu ya kila aina. Tahamaki lile gari likawa limefunga breki karibia kabisa na miguu yake, Deborah akaanguka mpaka chini kutokana na kiwewe cha hofu iliyomsonga moyoni mwake. Akaharakisha kunyoosha mikono yake juu anahema kwa kutweta kuonyesha kuwa anahitaji amani amesalimu amri. Lile gari lilifungwa vioo vyeusi lisivyoruhusu kumuona aliyekuwa ndani ya gari. Kioo cha gari upande wa siti ya mbele ya abiria kikaanza kushushwa taratibu mpaka aliyekaa siti ile akaonekana dhahiri.

"Deboraaaah.....usikimbie ni mimi Timammy nimekufuata...!" aliongea mtu aliyekuwa amekaa siti hiyo akiwa amevaa miwani yenye vioo vyeusi. Akaivua miwani yake na kufungua mlango wake akashuka chini na kumsogelea Deborah pale alipokaa kwenye mchanga. Akanyoosha mkono wake mrefu kutaka kumpa msaada Deborah wa kuinuka toka ardhini. Deborah alinyoosha mkono wake lakini kwa wasiwasi bado akiwa amepigwa na butwaa kaachwa mdomo wazi. Hofu yake ilikuwa haamini kama kweli huyu ni Timammy alidhania labda ni mzuka wake Timammy. "Haiwezekani mtu niliyempigia simu robo saa iliyopita tena sikumpata hewani ghafla awe amefika mpaka kwenye nyumba ninayoishi" aliwaza Deborah. "Najua unajiuliza maswali kibao na hupati majibu kuhusu ujio wangu, kwa ufupi sakata la mchumba wako kuomba rushwa ya ngono limetangazwa mapema sana kwenye redio na televisheni, na mie nilikuja kijiji cha Mlali hapo jirani na Mzumbe nikiwa kwenye harakati za kutafuta eneo la kufungua kiwanda cha kusindika nyanya ndio nikaonelea nichepuke mara moja kuja kuangalia usalama wako..! " aliongea Timammy kwa kujiamini bila kupepesa macho wala kutafuna maneno, kauli ambayo kidogo iliondosha hofu katika moyo wa Deborah. Kama ujuavyo ukiwa kwenye dhiki na shida hata akili inapunguza uwezo wake wa kuchanganua mambo kwa upana. Mtu mwenye njaa anafikiria kwa msaada wa tumbo lake, kichwa chake kinaenda likizo.

Deborah akajinyanyua ardhini na kujikung'uta mavumbi kwenye sketi yake. Baada ya maongezi mafupi ya kusafiana nyoyo baina yao, Deborah akaingia ndani kufuata begi lake aweze kuondoka na Timammy. Moyo wa Timammy ulijawa na furaha fokofoko kutokana na kukaribia kutimiza ndoto yake ya kumfanya Deborah awe mke wake wa kufanya nae maisha. Msichana ambaye amemsubiria kwa zaidi ya miaka 6 na ushee ili aweze kumtia kwenye himaya yake. Timammy ndio aliyeandaa mipango yote ya maangamizi kwa Alex bila Alex na Deborah kutanabahi kuwa ni adui yao. Baada ya Timammy na dereva wake kumkosa Deborah kule shuleni na kuelekezwa kuwa yupo Morogoro. Katika juhudi zao za kumsaka wakafanikiwa kuelekezwa kuwa anafanya kazi dukani kwa Mrs.Tonny. Walipofika hapo dukani ndio wakapata hadithi ya Deborah kuwekwa ndani rumande kwa kosa la wizi wa vito vya thamani. Kwa jinsi Timammy anavyomfahamu Deborah kwa tabia zake njema, moja kwa moja akajua ni zengwe tu lililosukwa na Mrs.Tonny, mwanamke ambaye anamjua kinagaubaga kuwa ni tajiri lakini ana tabia za kikhabithi sana.

Uzuri wake Mrs.Tonny alikuwa anamuogopa vibaya sana Timammy kutokana na mtifuano mkali waliowahi kuzozana katika kugombea tenda mbalimbali zenye ulaji serikalini. Ndio maana ikawa rahisi kwa Timammy kumaliza kesi ya Deborah kiulaini kama kumsukuma mlevi. Kikwazo pekee kilichokuwa kimebakia mbele Timammy alikuwa ni Alex. Akaitafuta mbinu iliyoenda shule ili kumchomoa Deborah kwa Alex, hakutaka kutumia mbinu ambazo Deborah zitamfanya amgundue yeye kama ndio mpishi faraka katika penzi lake na Alex kwa kutumia kuni za fitina. Timammy Kwa ujuba wake uliotopea angeweza kumuua Alex au kumtia kilema chochote ili ajitwalie kirahisi Deborah ila akaamua kutumia njia za kisayansi ambazo itakuwa ngumu Deborah kugundua kuwa yeye ndio mhusika wa matatizo ya Alex.

Akatumia fursa ya upweke wa Alex pindi mpenziwe alipokuwa Chuoni kumpenyeza dada wa kazi ambaye ni mrembo wa haja kumtia mtegoni Alex, akafanikiwa kunasa. Ndipo ukasukwa mpango yule dada ajisingizie amepata ujauzito na apotee kimoja ila ahakikishe taarifa zinavuja kwa Deborah. Ramani ya tukio zima ikachorwa kiustadi mkubwa kuwa siku hiyo hiyo inayovuja habari ya ujauzito wa dada wa kazi kabla jeraha la moyo wa Deborah halijakauka, atoneshwe tena ili amchukie kimoja Alex. Ndipo akapangwa msichana mrembo, mmoja wa wanafunzi wa Alex aingie ofisini kwa Alex kisha askari kanzu wavamie wamkamate Alex kwa kigezo cha kuomba rushwa ya ngono. Waandishi wa habari na wapiga picha wakapewa chao kuhakikisha wanaripoti tukio la Alex kiufasaha na kwa kuongeza chumvi zaidi ili kuzidi kuchafua hali ya hewa. Sasa mipango ya Timammy ilikuwa inakaribia kutimu, Deborah anaingia kwenye himaya yake kiulaini mithili ya mbwa mbele ya chatu.

Punde si punde Deborah akatoka na begi lake, kisha akaacha funguo za nyumba ya Alex kwenye nyumba ya jirani huku akimpa maelekezo kuwa mama yake Alex atakuja kuufuata ufunguo hapo, kisha akaingia kwenye gari la Timammy na kutokomea zao, usiku mbichi huo wa saa moja na robo usiku. Deborah mchezo aliokuwa anaucheza wa kutaka auni toka kwa Timammy ilikuwa ni kama kurudisha tende Manga, kamwe asingepata faraja anayoitarajia. Auni iliyokuwa inatolewa na Timammy kwa Deborah ilikuwa ni kwa malengo maaalumu.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
SEHEMU-44



[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
SURA YA KUMI NA NANE
"Umesema ni mwaka 1990 eeh....ngoja niangalie faili la mwisho, tukikosa taarifa zako humo ndio basi tena, sina jinsi ya kukusaidia rafiki yangu" aliongea Bwana Joram Peter Ochieng Mkurugenzi wa kituo kikongwe cha yatima Jijini Nairobi kinachojulikana na kwa jina la Cheryls Childrens Home and Learning Centre. Walikuwa wamejifungia kwenye ofisi ya kisasa yenye ukubwa wa wastani iliyopambwa kwa samani nzuri za kuvutia, huku kiyoyozi kikifanya kazi barabara na kuzalisha hali ya hewa ya kuvutia.

"Sawa nitashukuru ukinisaidia" aliongea kinyonge Dr.Pesambili akionyesha dalili za kukata tamaa ya kupata taarifa zake zilizosajiliwa kwenye kituo hicho pindi alipokuwa analelewa kwenye kituo hicho cha yatima kwenye miaka hiyo ya 90's. Alikuwa ameshakaa ofisini hapo kwa zaidi ya dakika 45 wakizisaka nyaraka zenye taarifa zake. Kibaya zaidi mmiliki wa kituo mstaafu Mzee Peter Ochieng ambaye ndio alimpokea Dr.Pesambili akiwa kinda wa miaka 2 alikuawa ameshastaafu, anajilia zake pensheni yake huko maeneno Kisumu.

"Mmmhhhhh..........kuna hii karatasi ya usajili inaonyesha jina la mtoto wa kiume ni Pesambili, mlemavu wa miguu aliokotwa na mlinzi wa klabu ya starehe ijulikanayo kama 'Nairobee BY Night Club'" aliongea kwa mshawasha yule Mkurugenzi huku akiwa ananyofoa hiyo karatasi kutoka kwenye faili hilo alilokuwa ameliinamia kitambo kirefu na kumkabidhi Dr.Pesambili. Dr.Pesambili alipoipitia kwa umakini machozi ya huzuni yakaanza kumtiririka akivuta hisia za kulijua kwa mara ya kwanza jina lake halisi la utotoni la Pesambili. Siku zote tokea apate akili anajijua anaitwa 'Trezguet Lorenzo' na ndio jina la kwenye hati yake ya kusafiria na alilolitumia kwenye vyeti vya shuleni. "Huyu ndio mimi kabisa....! " alisema kwa msisitizo mkubwa Dr.Pesambili tena kwa lugha ya kiswahili fasaha kutokana na kuishi kwake Tanzania kitambo kirefu pia baba yake na babu yake mlezi nchini Italia nao walikuwa fasaha wa lugha ya kiswahili.

"Lakini hapo inaonyesha mtoto alikuwa ni mlemavu wa miguu na wewe ni mzima, hapo inashangaza kidogo" aliuliza Mkurugenzi yule swali la kidadisi huku akiyaweka sawa masikio yake kutaka kulisikia jibu maridhawa toka kwa Dr.Pesambili. "Ni hadithi ndefu, lakini kwa ufupi nimefanyiwa operesheni ya kurekebisha mifupa ya miguu nikiwa mtoto kabisa" aliongea kinyonge Dr.Pesambili. Baada ya mazungumzo mafupi, Dr.Pesambili akachomoa kitabu chake cha hundi akaandika cheki ya Ksh.10,000/= kama msaada wake kwa kituo huku akiahidi kukitafutia wafadhili mbalimbali kituo hicho.

Akatoka nje ya Ofisi na kufanya ziara fupi katika mabweni wanayotumia watoto hao kuishi, akaongea nao na kuwapa nasaha fupi zenye kuleta matumaini katika maisha yao ya siku za usoni. Watoto wale wakafurahi sana kuona mwenzao kama wao aliyepitisha maisha yake hapo kituoni ametoboa maisha. Akapiga nao picha ya pamoja, kisha akaagana nao na kuingia mtaani rasmi kumsaka mlinzi wa klabu ya "Nairobee BY Night" ambaye taarifa rasmi zinasema yeye ndio alimuokota.


"Naomba unipeleke klabu moja inaitwa Nairobee BY Night...!" alisema Dr.Pesambili kumuambia dereva taksi mmoja aliyekuwa ameegesha gari yake mtaani jirani kabisa na kituo cha watoto yatima alichotoka. "Wewe ni mgeni Jijini Nairobi eeeh...?" aliuliza kwa mshangao mkubwa yule dereva huku akimuangalia usoni Dr.Pesambili. "Eeeh...sio mwenyeji hapa Nairobi..!" alijibu Dr.Pesambili huku akisubiri jibu muafaka. "Hamna Klabu yenye jina hilo inayosema, nina miaka 5 Jijini Nairobi, naijua mitaa na vichochoroni vyote yakiwemo majumba ya starehe lakini sijawahi kuisikia hiyo Klabu unayoitaja" alisema yule dereva huku akimchangamkia mteja mwingine aliyekuwa anahitaji taksi.

Dereva yule akaondoka zake na mteja mpya, akimuacha Dr.Pesambili kwenye mataa asijue la kufanya. Akaanza kutembea kwa miguu barabarani akipasua mitaa kuelekea katikati ya Jiji huku akitafakari kitu cha kufanya akifika huko Mjini. Kwa upande wake maji yalishazidi unga, hajui hata cha kufanya huku uoga ukimtawala kuwa kama hiyo Klabu ni kweli haipo basi kumpata Mlinzi wa Klabu aliyemuokota itakuwa ni kama kamari ya kumtafuta mwanamke bikira ndani ya wodi ya wazazi. Alishaanza kukata tamaa kama kweli atafanikiwa kuipata asili ya wazazi wake. Dr.Pesambili alikuwa anauchapa wa fisi katika mitaa ya Jiji la Nairobi hataki taksi wala nini, kuanzia mitaa ya Moi Avenue, Tom Mboya, Kimathi, Biashara na kwingineko kote aliivuruga akiulizia kila anayekutana nae kuhusu Nairobee BY Night Club, lakini hakuwa anapata ushirikiano wowote. Katika Jiji la Nairobi kila mtu alikuwa anajali hamsini zake, watu wake sio marafiki kama walivyo Watanzania.

Harakati zake hizo zikamfanya atiliwe mashaka na na kuanza kumulikwa na vyombo vya Dola bila yeye mwenyewe kufahamu. Kenya ilikuwa imetoka kwenye Uchaguzi Mkuu wa tarehe 27/12/2002, uchaguzi ambao ulimuingiza madarakani Rais mpya Mheshimiwa Mwai Kibaki kupitia chama cha "National Rainbow Coalition (NARC)". Uchaguzi ambao ulishuhudia anguko la chama kikongwe barani Afrika cha "Kenya African National Union" (KANU) kilichokuwa madarakani tokea nchi ya Kenya kupata Uhuru mwaka 1963. Kwa kuwa siasa za Kenya zilikuwa zimetawaliwa na ukabila, wapo waliokuwa hawapendi nchi itawaliwe na Mheshimiwa Mwai Kibaki toka kabila kubwa la Kikuyu, kabila ambalo lilikuwa linapendelewa tokea enzi za utawala wa Mkoloni hivyo kulikuwa na tetesi za watu wa makabila madogo madogo kama Luhya, Luo, Kalenjin, Kamba, Kisii na mengineyo kuwa na mikakati ya kujipanga upya kuhakikisha wanachukua madaraka kwa njia ya kufa au kupona katika Uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 2007. Hivyo katika kutaka kulidhibiti jambo hilo lisitokee mashushushu walikuwa wamemwaga mitaani kama utitiri kunusanusa njama zozote za wahalifu wenye nia ya kuleta machafuko nchini Kenya.

Dr.Pesambili akiwa amejipumzisha kwenye Mkahawa mmoja wapo uliopo Jijini Nairobi anapoza koo kwa kupata soda baridi ili aendelee na harakati zake, akastukia anawekwa chini ya ulinzi mkali na maaskari kanzu lukuki. Alipofanyiwa taftishi ya kutosha na kutakiwa aonyeshe hati yake ya kusafiria na nyaraka zingine Nyeri akajikuta hanayo hata moja. Kijasho chembamba kilimvuja juu ya paji lake la uso kwa hofu kubwa. Kumbe alidondosha baadhi ya nyaraka zake kule kwenye kituo cha watoto Yatima alipotoka cha Cheryls Childrens Home and Learning Centre". Alipoteza nyaraka hizo akiwa katika harakati za kujumuika nao watoto yatima katika shughuli mbalimbali za kupiga nao picha, kupata nao maakuli ya pamoja na nyinginezo. Mashushushu wale kusikia hana nyaraka zozote halali, yupo yupo tu wakageuka mbogo dhidi yake na kumgombania mithili ya mpira wa kona, tayari wameshamhisi ni mtu hatari kwa usalama wa nchi ya Kenya.

Dhana zao ziliwatuma kuwa ni mmoja wa mamluki toka Mataifa kibeberu ya Ughaibuni aliyetumwa kupandikiza chokochoko nchini Kenya. Akiwa anashangaa hajui kinachoendelea dhidi yake akastukia anavikwa pingu mikononi na kufunikwa na mfuko mweusi usoni kisha akatupwa kwenye gari na kupelekwa kusipojulikana. Njia nzima alikuwa anapokea kichapo kitakatifu cha mbwa mwizi huku anahojiwa kwa kuulizwa alichokuja hasa kukifanya nchini Kenya akitokea huko kwao Italia. Walipoona hana chochote cha maana anachokiongea wakaacha kumtesa, Dr.Pesambili akasikia tu wanaongelea kuhusu "Shimo la Tewa".

Dr.Pesambili alijawa na hofu furifuri moyoni mwake hajui wapi anapopelekwa, hasa akichukulia amekuja nchini Kenya kwa amani kabisa, yeye wala sio mhalifu kwenye maisha yake hajawahi hata kumwaga damu ya mdudu mdogo kama mbu sembuse mwanadamu.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3585][emoji3586]
Mbweku Jr alipozinduka alijikuta yupo wodini ndani ya gereza la Segerea. Gereza hilo la mahabusu lilikuwa ni gereza ambalo watuhumiwa wengi hawapendi wapelekwe huko. Walikuwa wanakufananisha na Jahanamu kutokana na shida na madhira yanayopatikana huko. Wale watuhumiwa wenye nguvu ya kipato walikuwa wanahangaika huku na kule kwa njia za panya na kupenyeza mlungula kwa Maafisa wasio waadilifu ili mradi ndugu zao wapelekwe gereza la Keko lakini sio Segerea. Segerea kipindi hicho Mbweku Jr ametupwa huko, kulikuwa na shida ya maji balaa. Hali ambayo ilisababisha mahabusu waugue magonjwa ya ngozi maarufu kwa jina la 'burudani'.

Pia Segerea kulikuwa na msongamano wa mahabusu wa kutisha, gereza lilikuwa na uwezo wa kuhifadhi watu takribani 750 lakini kuwa wakati walikuwa wanafurika mahabusu zaidi ya 2,000 hali iliyokuwa inapelekea mahabusu kulala watatu watatu kwenye godoro moja kwa mtindo wa "mchongoma". Mtindo ambao ulimtaka mtuhumiwa kila baada ya masaa matatu kupita ndio anaruhusiwa kujigeuza kitandani kulalia ubavu mwingine.

Jambo la yeye kutupwa Segerea lilimpa mashaka makubwa Mbweku Jr kama kweli rafiki yake Timammy wapo pamoja na yeye kwenye shida na raha. Alitegemea Timammy kwa umaarufu wake alionao ahangaike juu chini ili apelekwe gereza lenye nafuu kidogo, lakini aliona kama ametelekezwa. Kingine kilichomsikitisha ni kitendo cha kutoletewa huduma zozote za kibinadamu na Timammy kipindi chote cha msoto akiwa gerezani. Mahabusu alikuwa anaruhusiwa kuletewa chakula na bidhaa mbalimbali kama sabuni, dawa ya meno, na miswaki lakini tokea atupwe Segerea hakuona hata mche mdogo tu wa sabuni ya kufulia unaouzwa Sh.1,000/= uliotoka kwa rafiki yake Timammy wakati yeye Mbweku Jr alikuwa anaamini ana hisa kibao tu katika utajiri anaomiliki Timammy.

Mbweku Jr akatumia busara na hekima, hakutaka kumhukumu moja kwa moja rafiki yake kuwa amemfungia vioo ametupa jongoo na mti wake, akampa udhuru kuwa huenda ametingwa na majambo mbalimbali ya harakati za kimaisha anaziweka sawa kwanza kisha atamrudia yeye. Baada ya wiki kadhaa kuyoyoma akaanza kuyazoea maisha ya jela. Maisha ya kuamka na kula kwa filimbi, unakula unachopewa na sio unachokitaka. Unafungiwa selo kulala kwa amri ya Afisa magereza hata kama hauna usingizi. Ikabaki kazi ya kupelekwa mahakamani na kurudishwa mahabusu wakati kesi yake ikitajwa na kupangiwa tarehe.
.

Kilichomshtua Mbweku Jr na kujua kuwa hawapo pamoja na Timammy ni kitendo cha kushindwa hata kumuwekea Wakili wa kumtetea mahakamani, mpaka serikali ikampatia Wakili wa kumtetea. "Hisia zangu kutoka kwenye sakafu ya mtima wangu wa moyo sasa zinanituma Timammy, rafiki yangu kipenzi hanitaki tena nirudi uraiani, na huenda yeye ndio amenichomea utambi pale Mahakamani kwa Hakimu kuhusu kesi hii ninayohangaishwa nayo siku tumeonana na nikamuomba anilipie faini. Ama kweli duniani wewe tenda wema nenda zako usingoje shukrani, na fadhila ya punda ni mateke daima dawamu...!" aliwaza kwa hasira Mbweku Jr huku amekunja ndita kwenye paji lake la uso anapigapiga ngumi zake nzito kwenye kiwambaza cha selo. Akaanza kukumbukia siku aliyomkabidhi burungutu sufufu la fedha za kigeni Timammy, alizopora kwenye gari ya Bosi Recho . Ngwenje ambazo zimempa heshima Timammy kutoka mtu asiyejulikana mpaka kuwa mtu mahashumu katika Nchi, akiongea kila mtu anamtetemekea.

Kwa kuwa alikuwa hana jinsi ya kufanya, akafunika kombe mwanaharamu apite kwa kunyanyua mikono juu na kumshukuru Jalia kwa yote yaliyomfika huku akisubiri hatima yake ya hukumu atakayopewa. Baada msoto wa takribani mwaka mmoja na nusu gerezani wa kupigwa danadana kesi yake, sasa ikaanza kusikilizwa. Hapo ndipo likaibuka zengwe jipya kabisa lililozidi kumkata maini na kumtibua nyongo, Mbweku Jr. Mawakili tofauti wanaomtetea yeye wakaanza wimbi la kujitoa kumtetea bila kutoa sababu zenye mashiko mbele ya Mheshimiwa Jaji. Jambo ambalo lilimfikirisha vilivyo Mbweku Jr akitaka haswa kujua kindakindaki sababu za hao Mawakili kumkacha bila mafanikio.

Mungu si Athumani, ndipo mmoja wa Wakili wake wa mwisho kujitoa alipojivika mabomu na kumpasulia ukweli bayana, kinagaubaga bora bila kupepesa macho kuwa wanashinikizwa na tajiri Timammy wajitoe kwenye kesi kwa tishio la hata kupotezwa uhai wao kama wakijifanya vichwa ngumu. Hapo sasa Mbweku Jr ndipo alipoyakinisha kweli isiyo na chembe ya mashaka kuwa kikulacho ki nguoni mwako, na Timammy kweli ni zaidi ya Ibilisi adui nnasi kwa ususi wa vitimbi na vibweka vyake dhidi yake mtawalia visivyo na ukomo.

" Natangaza vita yenye kishindo kikuu na Timammy, nitatoroka gerezani kwa mbinu yoyote ile, nikimpata ama zake ama zangu, lazima nimuonyeshe cha mtema kuni, nimtie adabu mpaka akijue kilichomtoa kanga manyoya...! " alikula yamini ya moyo Mbweku Jr huku mishipa ya shingo imemsimama dede kwa hasira dhidi ya Timammy. Kiapo hicho kiliashiria kuvunjika rasmi kwa usuhuba baina yao uliodumu kwa miaka kadhaa tokea wakiwa maskani kule Kigamboni, na sasa Mbweku Jr alimtangaza Timammy ndani ya serikali yake ya moyo kuwa ni hasimu wake namba moja. "Nitamuangamiza Timammy na uzao wake wote, sitobakisha mbwa yoyote mwenye mafungamano nae, dawa ya moto ni moto na daima wapambanapo mafahali wawili ziumiazo ni nyasi, mie sitolijali hilo" alizidi Mbweku Jr kula yamini ya moyoni akiwa peke yake juu ya godoro amejipumzisha mchana mmoja wapo ndani ya gereza hilo la Segerea.

Lakini Timammy nae hakuwa zumbukuku ulimwengu upo huku, alikuwa anamjua fika rafiki yake Mbweku Jr ni mtata haswa hawezi kukubali kuishia gerezani, lazima atalala mbele akiona giza limezidi mbele yake hamna mapambazuko. Na kama akifanikiwa kuchoropoka kuja uraiani patakuwa hapakaliki, lazima pachimbike hivyo nae alijipanga kwa mbinu madhubuti za Kimafia kumuangamiza Mbweku Jr huko huko akiwa gerezani. Hivyo ngoma ikawa droo, mchuzi moto ugali moto, Mbweku Jr anawindwa bila mwenyewe kung'amua kuwa roho yake imewekwa rehani, Timammy ameipandia dau.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
SEHEMU-45



️[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Siku moja ilipofika majira ya magharibi, mahabusu wote wakiwa tayari wameshakula mlo wa chajio na wameshafungiwa ndani ya selo kikasikika kishindo kikubwa cha mlipuko kama wa bomu kisha umeme ukazimika gereza zima, likageuka giza totoro. Kilikuwa ni kishindo cha mlipuko wa transfoma linalohusika na kusambaza umeme maeneo ya Segerea karibia na gereza na maeneo ya jirani. Mpaka giza likawa limeanza kutamalaki mawinguni, umeme ukawa bado haujarudishwa na TANESCO, hali iliyojulisha kuwa hitilafu ya umeme iliyotokea ni kabambe isiyo ya kitoto.

Ghafla tu Mbweku Jr akajikuta amebanwa na haja ndogo anahitaji kutabawali kwa haraka sana ili kibofu chake cha mkojo kipate unafuu kwa kutoa uchafu mwilini. Akajizoa toka kwenye godoro lake la ulimi wa ng'ombe alilokuwa amebahatika kulala peke yake na kushika uelekeo wa msalani. Akaambaa na korido mpaka akajitokeza kwenye eneo maalumu lililotengwa kwa ajili ya vyoo na mabafu lililopo ndani ya Selo hiyo hiyo. Wakati anazidi kwenda mbele akiwa gizani, machale yakaanza kumcheza Mbweku Jr, nywele zake zikaanza kumsisimuka, vinyweleo vya nywele ya ngozi yake vikamsimama dede, akageuka nyuma yake kuangalia kama kuna mtu anamfuatilia ili apate kuchukua tahadhari mapema. Akahisi kama kuna mtu amejificha nyuma ya moja ya tanki kubwa la kuhifadhia maji alilolipita nyuma yake baada tu ya yeye kugeuka nyuma.

Mbweku Jr akazidi kupatwa na ushawishi wa kutaka kumjua ni nani anayemfuatilia kizani kwa kutumia mwangaza wa mbalamwezi. Tayari damu ilianza kumchemka mwilini, mikono yake ikimchezacheza akipandwa shauku ya kutaka kumvunja mtu. Akamgeuzia mgongo adui na kuanza kuchanganya mwendo huku mkono wake wa kushoto umekamatia juu ya suruali kwenye maeneo ya sehemu za siri kujionyesha amezidiwa na mkojo, akakunja kulia kuelekea kwenye vyoo akiyaacha mabafu yakiwa yamejipanga upande wa kushoto kwake. Akapishana na mtu mmoja tu aliyekuwa anatokeza upande wa vyooni, Mbweku Jr akainamisha sura yake asijulikane, alishapanga kumshikisha adabu huyo mjuba anayemfuatilia.

Alipokata tu upande wa kulia mbele yake kulikuwa na pipa la plastiki la kuhifadhia maji ya kujitawadhia pindi ukiwa chooni. Mbweku Jr kama umeme akajitumbukiza ndani ya pipa hilo lililokuwa na maji robo kwa mtindo wa kupiga mbizi, huku akiacha kichwa tu kikiwa kinaelea juu juu. Baada ya muda wa nusu dakika akasikia vishindo vya miguu ya yule jamaa anakuja wangu wangu bila kuchukua tahadhari yoyote akasimama jirani kabisa na pipa lile la maji anaangaza usalama wake kabla hajavamia vyooni kumsaka Mbweku Jr. Mbweku Jr kama mzimu vile akaibuka kutoka kwenye pipa la maji akiwa nyuma ya mgongo wa yule jambazi kisha akajikohoza kidogo, yule jamaa mkononi akiwa ameshika bastola akageuka nyuma, macho yakamtoka kama mjusi aliyebanwa na mlango. Alishikwa na kihoro akiwa haamini kama ameingizwa mkenge kwenye mtego wa Mbweku Jr kaingia mzima mzima.

Mbweku Jr bila kuchelewesha habari, akajirusha mzima mzima kama samaki mkizi akitokea kwenye pipa na kumkumba yule mjuba wote wakaanguka sakafuni kwa mlio wa pwataaaaah. Kikiri kakara ikaanza baina yao wakiviringishana mieleka wakipimana nguvu ya ugali. Bastola ikawa imemponyoka mkononi na kuangukia meta kadhaa kutoka walipokuwa wanapimana ubavu. Wote wakanyanyuka kwa pamoja toka sakafuni na kuanza mtifuano mkali wa kukata na shoka baina yao. Mbweku Jr akawa anavurumisha mvua ya makonde kadhaa lakini yakawa yanayeyukia hewani, yanashindwa kumlenga sawa sawa adui yake, dalili za kukosa umakini kutokana na kuacha mazoezi kwa muda mrefu.

Mbweku Jr akajikuta kibao kinamgeukia yeye anaanza kuchakazwa ngumi mfululizo za usoni. Ndani ya muda mchache tu tayari alishapasuliwa chini ya jicho la kushoto. Akazuga kama amezidiwa na kipigo kile kumbe hamna mtu sugu duniani kama yeye. Vile amejiinamia chini yule adui akaanza kuelekea ilipo bastola yake akiifuata ili aje ammalize Mbweku Jr akiwa amempa kisogo Mbweku Jr. Hilo likawa ni kosa kubwa kwake la kufungia uhai wake, Mbweku Jr alijirusha hewani kama chui anayevizia mawindo yake na kumkaba shingo yake kwa nguvu kisha bila ajizi akaizungusha na kunyonga hapo hapo. Yule jamaa akapoteza uhai wa wake pale pale bila hata kuomba maji ya kunywa ya kupunguzia uchungu wa sakarati mauti wakati Malaika wa kifo anapochomoa roho ya mtu.

Himahima akaanza kumfanyia speksheni mwilini, kwenye suruali yake yule mjuba akakutana na vipisi visivyo idadi vya sigara bwege maarufu kwa jina la bangi pamoja na kikaratasi kidogo cheupe. Akamchomolea simu yake mfukoni yule adui kwa msaada wa mwangaza wa tochi ya simu akaanza kukisoma kile kikaratasi. Akabakia amepigwa na mzumbao wa sekunde kadhaa baada ya kusoma ujumbe ulioandikwa kwenye kikaratasi kile. Kilikuwa kinasomeka kama ifuatavyo;
"MBWEKU JR SELO NO. 06[emoji777]". Akakifinyanga kikaratasi hicho na kukitupia kwenye shimo la choo. Mbweku Jr haraka haraka bila kulaza damu akamburuza adui yule mpaka kwenye moja ya vyoo na kumfungia humo akiwa amemkamatisha kabisa bastola yake kukamilisha ushahidi. Baada ya hapo akajisaidia zake na kujiweka sawa kwa kuosha eneo lenye mpasuko usoni mwake kabla hajarejea selo kwa kutumia msaada wa nuru ya mwezi.

Akashukuru Mungu kwa kuwa hamna mtu hata mmoja aliyeshuhudia tukio lile la mauaji alilolifanya. Akarudi zake Selo kulala huku akisubiria mapambazuko yafike ili mbivu na mbichi za mhusika zijulikane. Usiku mzima Mbweku Jr alilala usingizi wa mang'amung'amu, anaweweseka kutokana na mpambano wake na mjuba yule aliyekosa chembe ya junaya mpaka anamfuata na bastola jela. Mbweku Jr alikuwa anawaza huyu adui yake aliyemuua muda mfupi uliopita katumwa na nani na kwa maslahi gani. Kilichokuwa kinambangua kichwa zaidi ni kitendo cha huyo adui kufanikiwa kuingia jela tena akiwa na silaha ya moto. Akajikuta anajisumbua bure kujifikirisha bila kupata majibu ya haraka kwenye maswali anayojiuliza.


"Tabia ya ukweli huwa haujifichi, hata kama ukiufunika ipo siku utajiweka uchi hadharani, adui yangu anashirikiana na baadhi ya Maafisa magereza wasio waaminifu kutaka kuniangamiza...!" aliwaza Mbweku Jr akijipa moyo wa kumfahamu mtu aliyemtuma mapema iwezekanavyo. Huyu jambazi alikua ni mtu wa pili kuuliwa na Mbweku Jr katika maisha yake, wa kwanza akiwa ni Kibopa Mfanyabiashara wa kiarabu wa Kariakoo, Bwana Mwinyi Fuad aliyetaka kumlawiti kinguvu wakati yupo chokoraa mtaani.
Kulipokucha tu tayari habari za kifo cha yule mtu zilisambaa kama upepo. Kilichowashangaza watu ni namna alivyoingia gerezani chini ya ulinzi mkali hali ya kuwa sio mahabusu. Ikagundulika kuwa askari magereza wawili waliokuwa lindoni usiku wametoweka, hawajulikani walipo. Hivyo dhana za Mbweku Jr dhidi ya Maofisa wa Magereza hazikuangukia patupu. Askari Magereza walitoroka baada ya kula njama na Timammy za kumuingiza mhalifu ndani ya gereza, hivyo njama zao zilivyofeli ikabidi walale mbele kukwepa mkono mrefu wa sheria.

Timu ya wapelelezi toka polisi makao makuu wakiwa na wapelelezi bobezi wakatua gerezani kuchunguza lengo la mhalifu huyo kuingia gerezani. Baada ya uchunguzi wao ikaonekana mhalifu huyo ameuliwa na mmoja wa mahabusu baada ya kuzidiwa nguvu katika kujitetea zake. Msako kabambe wa mule mule ndani ya gereza ukaanza wa kumtafuta mahabusu aliyehusika na mauaji hayo. Mpaka giza linazama walishindwa kumbaini mhusika zaidi ya mahabusu kadhaa kutiliwa mashaka akiwemo Mbweku Jr kutokana na majeraha aliyokutwa nayo. Ikatolewa amri mahabusu hao wahamishwe, kupelekwa kwenye magereza mengine. Ndipo Mbweku Jr akahamishiwa usiku usiku katika gereza la Ukonga. Moyoni Mbweku Jr kusikia anapelekwa Ukonga alijawa na furaha fokofoko isiyoelezeka. Furaha yake ilitokana na mchanyato wa mambo mengi, ikiwemo mazingira mazuri ya kuishi na uwezekano wa yeye kutoroka gerezani na kurejea mtaani. Sala na dua zake alikuwa anaombea kila kitu kiende anavyotegemea iwe. Pia pale Segerea alikuwa amejitahidi kutafuta penyenye za baba yake mzazi aliyemuacha gereza la Ukonga kabla hajazamia nchini Afrika ya Kusini lakini hakuambulia kitu. Hivyo huko Ukonga akategemea huenda atapata habari hizo anazozisaka.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Timammy safari hii hakutaka kufanya makosa ya kiufundi kabisa, alipanga kufa au kupona lazima amuoe Deborah. Aliamua kumtengeneza kwa kutumia kamati ya ufundi. Lengo lake namba moja lilikuwa ni kumuachisha Chuo moja kwa moja abakie nyumbani ili iwe rahisi kumuoa. Alijua akimpa sera za kumuachisha Chuo, itakuwa ni kumtafuta muhali Deborah hivyo lazima ajiongeze kwa kutumiwa uchawi ili aache chuo apende au asipende. Akaamua kumuendea kwa Mganga, gwiji wa ulozi ajulikanaye kama Bi.Havijawa. Huyu Bibi alikuwa anaishi katika kisiwa cha Kwale. Kwale ni kisiwa kidogo katika Bahari Hindi mbele ya pwani ya Tanzania upande wa kaskazini wa delta ya mto Rufiji. Kisiwa hicho ni sehemu ya kata ya Kisiju kwenye wilaya ya Mkuranga katika Mkoa wa Pwani.


Kwale imetambuliwa na wataalamu wa akiolojia kuwa kati ya vituo vya awali vya biashara ya pwani iliyokuwa chanzo cha utamaduni wa Uswahilini. Kwa hiyo mambo yote ya kiswahili swahili unayoyajua wewe na usiyoyajua huko ndio chimbuko lake. Yale sijui masuala ya mtu kugeuzwa paka, kujaza tumbo la mwizi wako kwa kutumia pampu ya baiskeli mpaka tumbo lake linamaanisha huko yalikuwa mambo madogo sana. Bi. Havijawa utaalamu alirithishwa na Baba yake mzazi.

Baba yake alivuma sana siku alivyoaga dunia, ndio watu wengi nchini Tanzania walimfahamu. Inasemekana kuna Shambaboi mmoja wa shamba la mzungu huko Rufiji alituhumiwa kesi ya ubakaji enzi za Mkoloni. Baba mzazi wa Bi.Havijawa akamfanyia dawa ya kumgeuza jinsia yule mtuhumiwa. Mahakamani Hakimu akamuachia huru mtuhumiwa baada ya kuthibitika pasina mashaka kuwa ni mwanamke hivyo hana uwezo wa kubaka kutokana na jinsia yake. Furaha ya mtuhumiwa huyo wa kiume aliyegeuzwa jike ilimtumbukia jongo baada ya kutoka Mahakamani na kuelekea moja kwa moja kwenye Kisiwa cha Kwale na kupishana na jeneza la mganga wake, baba yake Bi.Havijawa akipelekwa makaburini. Ikabidi amwage kilio cha karne na kutoboa siri baina yake na marehemu Mganga kuwa amempa jinsia ya kike nae anataka arudishie jinsia yake ya kiume. Hivyo sasa mikoba yote ya Uganga alikuwa ameachiwa Bi.Havijawa, Mapredeshee na Viongozi mbalimbali walikuwa wanamiminika Kisiju kwa Bi.Havijawa.

Timammy akapeleka jina la Deborah na la mama yake mzazi Deborah kwa Bi. Havijawa, akamfunga vilivyo kwa makafara ya kishetani na kumpa ahadi ya kuwa Chuo ndio kwaheri Deborah hatosoma tena.
Timammy akajitutumua kifaurongo kujitia kumlipia ada ya Chuo na pesa ya matumizi Deborah hali ya kuwa anamnanga kisogoni, akijua kabisa ya kuwa Chuo ndio kwaheri kwa Deborah. Aliporudi chuoni Deborah akaanza kukumbana na mauzauza ya kuogofya na kutisha Anatoka zake hosteli vizuri salama salimini lakini kosa lake akiingia tu darasani. Macho yake yanakosa nuru kabisa anakuwa mpofu na kiziwi kabisa. Akitolewa nje ya darasa mzima kabisa hana shida yoyote. Timammy alipoletewa mashtaka hayo na Deborah akajitia kuzunguka nae mahospitalini mpaka Nairobi wakafika, lakini kila aliporudi Chuo mambo yakawa yanabaki vile vile salama ya balawa. Ndipo Deborah rasmi akasalimu amri na kuacha Chuo.

Sasa ndio ikawa nafasi rasmi ya Timammy kutupa ndoano yake, ambayo bila ajizi ikamnasa mzima mzima Deborah. Ilikuwa ni ngumu kwa Deborah kumkataa tena Timammy hasa ukichukulia wema aliomtendea usio na kifani. Deborah alianza kupima tokea kulipiwa ada ya kwanza ya kuanza elimu ya sekondari, kuokolewa na kifungo cha jela kilichotaka kumkumba kutoka kwa Mrs.Tonny, na kulipiwa ada na kupewa hifadhi pindi ambapo mpenzi wake Alex alipotiwa ndani kwa tuhuma za kuomba rushwa ya ngono. Pia Timammy akamlipia gharama za Chuo Kikuu na bila kuchoka kazunguka nae kwenye tiba ya macho bara na visiwani mpaka Jijini Nairobi. Hakuona fadhila ya kumlipa Timammy zaidi ya kumkubalia matakwa yake.

Timammy akawa na furaha sheshe iliyopitiliza mipaka kutokana na kufanikiwa kumtia katika milki yake Deborah. Timammy roho yake ilikuwa imesuuzika vilivyo, akatokea kumtunuku chochote anachokihitaji Deborah. Sasa Deborah akageuka kuwa mwanamke tajiri 'BossLaddy' akishirikishwa kwa ukaribu katika biashara zote za Timammy kiufasaha. Katika kukata kiu yake ya kielimu aliyoshindwa kuipata Chuo Kikuu cha Dar es Saalam akajiunga na Chuo Kikuu Huria 'Open University of Tanzania' akawa anajisomea akiwa nyumbani. Katika harakati zao za kujivinjari penzi lao jipya, Deborah akajishtukia amenasa ujauzito. Ikabidi harakati za kufunga ndoa baina yao zianze kusukwa.

Timammy akamshinikiza Deborah kuwa lazima abadili dini yake ili wafunge ndoa ya Kiislamu. Baada ya mvutano wa hapa na pale na hasa ukichukulia Timammy ndio alishika mpini huku Deborah akiwa ameshika makali, ikabidi abadili dini kwa shingo upande ili mradi tu ndoa ipite. Moyo wa mwanadamu umeumbwa kumpenda yule mwenye kuutendea wema, kutokana na wema alioufanya Timammy kwa Deborah alishafanikiwa kuuteka moyo wa Deborah vilivyo. Kila alichokuwa anakiamrisha Timammy kinatekelezwa kama kumsukuma mlevi vile. Timammy aljiona amekuwa jabali wa maisha kayapatia vilivyo kwa kumzidi kete adui yake namba moja kwa sasa ambaye ni Mbweku Jr.


Siku moja asubuhi Timammy akiwa yupo nyumbani amejipumzisha, anasubiria kupata habari tamu kupitiliza kwa njia ya simu ili ajihakikishie kuishi maisha ya raha mustarehe na Deborah wake bila bughudha ya mtu yoyote, akajikuta anapigwa simu yenye maudhui ya kukera. "Hellow...Hellow...Bosi Bosi mambo sio mazuri, kijana tuliyemtuma gerezani akammalize Mbweku Jr amezidiwa nguvu kauliwa na Mbweku Jr. Hapa sasa kuna hekaheka za kuwahamisha baadhi ya wafungwa ili watawanywe magereza tofauti, na Mbweku Jr yupo katika orodha ya wafungwa hao, nitakujuza anapelekwa wapi kwaheri...!" taarifa ilitoka kwa mmoja wa askari magereza mshirika wa Bosi Timammy akimpa taarifa ya tukio zima.

Taarifa hiyo ikamsababishia shinikizo la damu Bosi Timammy na kupelekea kukimbizwa hospitalini kwa ajili ya huduma ya kwanza. Alishaanza kukihofia kivuli cha Mbweku Jr, alishamuona ameshindikana kuuliwa kwa njia za kawaida.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
SURA YA KUMI NA TISA
Dr.Pesambili alikuja kutupwa katika gereza linaloitwa Shimo la Tewa lililopo Mjini Mombasa, Kenya. Hili lilikuwa ni moja ya gereza linalotumika kuhifadhia magaidi tokea milipuko ya Balozi za Marekani nchini Kenya na Tanzania. Alipowasili hapo na kuvuliwa mfuko mweusi usoni alijaribu kuyazungusha macho yake kama dira kuangalia mandhari isiyovutia ya gereza lile. Baada ya kupokelewa tu, wakamtupia ndani ya selo kwa mtindo wa varange kama mnyang'anyi vile.

Selo hiyo iliyokuwa haipitishi mwangaza wa kutosha, alifungiwa kwa muda wa siku mbili mtawalia bila kutolewa nje. Selo ambayo sakafu yake ilikuwa ya mchanga yabisi kama ardhi ya jangwani. Riha mbaya ya mikojo na vinyesi ilisikika ndani ya selo ile dalili za kuonyesha unajisaidia mume mule ndani. Harufu ile ilimchefua chefu chefu na kumkoroga tumbo lake na kusababisha aanze kutapika bila breki. Paa lake lilikuwa ni refu sana, lililopambwa na utando wa nyumba za buibui, pamoja na ukoko wa kutosha wa vumbi.

Panya walikuwa wanakimbizana kwenye mbao za paa utasema wapo kwenye mashindano fulani. Selo ile ilikuwa na vidirisha vidogo sana, vilivyo juu na kupitisha mwangaza wa jua hafifu. kuonyesha Chakula chake pia kilikuwa cha kudonoa, akipewa kombe la uji asubuhi, uji ambao haina chumvi wala sukari anapewa mlo wa mwingine wa aina ya kipara cha babu chafuka moshi kwa kutowezea maharage mabovu saa 9 alasiri hiyo ndio nitolee mpaka kesho yake. Maharage hayo hayana dawa ya mboga wala hayajaungwa na kitunguu.

Alishikwa na msongo mkubwa wa mawazo hatima yake itakuwaje, Akianza kujiona yu kama mfu. Alitamani abebwe na kwenda kutupwa kwenye mtungi usioisha maji, huko akaliwe na samaki wakubwa kama papa na nyangumi iwe mwisho ya maisha yake ya ulimwenguni. Alitamani mfukoni awe na zile njiti ambazo ukikuna kichwa chake tu kinakupa moto aweze kuunguza selo yote iwe hadithi tena.

Kwa hali mbaya ya gereza lile alianza kuomba Mungu asiwekwe muda mrefu, vinginevyo ataanza kucheza gitaa bila kuujua wimbo wenyewe, kutokana na kupatwa na ukurutu wa ngozi. Alishangazwa sana na ufanyaji kazi wa Wanausalama wa nchi za Kiafrika kwa kutanguliza mateso kwanza kabla ya kujihakikishia kuwa huyo mtu ni mhalifu. Wanausalama hao walikuwa na nafasi ya kujiridhisha usahihi wa taarifa kupitia Ubalozi wa Italia nchini Kenya kwa sababu Dr.Pesambili alikuwa ni raia wa Italia. Matumaini yake pekee yalibakia kwa Bwana Joram Peter Ochieng Mkurugenzi wa kituo cha kulelea yatima cha Cheryls Childrens Home and Learning Centre alipopoteza nyaraka zake muhimu. Alitumaini huenda atazichukua nyaraka hizo na kuzipeleka polisi ili mwenye nazo atafutwe.

Siku zote mbili alikuwa hajafanyiwa mahojiano yoyote zaidi ya kula na kulala tu. Ilipofika siku ya tatu alfajiri na mapema akaja kutolewa kule selo, wakamfungua pingu alizofungwa miguuni na mikononi, kisha akapewa kifungua kinywa cha kutosha tu, chai ya mkandaa iliyojazwa fori fori kwenye kikombe cha plastiki na nusu mkate uliopakwa siagi. Dr.Pesambili akaanza kukibwakia bwaku kile chakula utasema anaishi kwenye kambi za wakimbizi kwenye shida ya chakula.

Aliona miujiza imemtembelea, watu ambao wenye roho za kishetani kwa zaidi ya siku tatu wanampa mateso shadidi bila sababu yoyote kisha ghafla bin vuu tu wanabadilisha gia angani na kujigeuza kuwa malaika, wanaanza kumtendea wema. Baada ya kumaliza kula akaletewa maji ya kuoga yaliyochemshwa chem chem na bwerasuti za michezo mpya za kubadilisha. Huko bafuni wakati anaoga ilibidi awe anajishikiza ukutani, vinginevyo Parr! mpaka Makka! na meno unavunja kutokana kubingirika bingiri bingiri bingiri na sakafuni. Weusi ulitanda ukutani na chini kutokana na uchafu uliorundikana kwa miongo kadhaa. Maji machafu bafuni kule yalikuwa yanachiririka chiriri chiriri, yakisambaa kila kona ya jengo.

Hofu ikaanza kumtawala moyoni mwake Dr.Pesambili kutokana na wema anaotendewa kwa ghafla tena bila kupewa maelezo yoyote. Alishawahi kusomaga taarifa za nchi za Afrika namna zinavyowajali wafungwa wanaotaka kunyongwa kwa kuwapikia chakula kizuri ili kuwaondosha mawazo. Sasa aliona hiyo hali ndio kama inataka kumtokea yeye ya kufanywa kama jogoo, mchana analishwa mchele, jioni anachinjwa cha kisha analiwa kwenye wali mezani.

"Ondoa hofu kijana tunakupeleka kwa Mkuu wa Polisi, Kaunti ya Mombasa, yeye ndio ataamua hatima yako kama kukuachia huru au kutupa amri tuendelee kukushikiria" aliongea mmoja wa askari wale waliofanana kwa sare zao na maumbile mfano wa njiti za kiberiti. Alipofikishwa mbele ya Mkuu yule mambo yakajipa, akaachiwa huru bila masharti yoyote huku akisindikizwa kwa msafara wa polisi mpaka alipofikia. Yule Mkuu wa Polisi, alikuwa Mzee mtu mzima, rangi ya nywele zake kichwani utasema amejitwika machicha ya nazi, anayesubiria miezi michache tu kustaafu utumishi wake wa umma. Shamba lake la meno kinywani mwake lilianza kukauka halitoi matunda, kutokana na mapengo dalili ya kuelekea kuwa kibogoyo miaka michache ijayo.

Mkuu huyo kabla ya kuhamishiwa Mombasa alikuwa anafanya kazi Jijini Nairobi kwa miaka mingi. Hivyo aliposoma maelezo ya Dr.Pesambili akavutiwa kuonana nae kutokana na maelezo yake kuonyesha kuwa baba yake mzazi Dr.Pesambili, Mr.Martin Tenga alikuwa ni rafiki yake miaka hiyo. Huyu ndio polisi ambaye alimfukuza Recho, mama yake Dr.Pesambili kwa mbinu chafu akishirikiana na Mr.Martin Tenga ili wapore mali zake zilizopo Jijini Nairobi. "Mama yako ni Mchaga, raia wa Tanzania, aliondoka Kenya miaka mingi sana. Alikuwa anatokea Mkoa wa Arusha au Kilimanjaro sikumbuki vizuri sana, na kabla ya kuja Jijini Nairobi aliwahi kuajiriwa kwenye Shirika moja linaitwa Peace-Corps Tanzania ", maelezo hayo ya Mkuu yule wa polisi, yalikuwa ni kama dawa inayotibu maradhi yake yote ya msongo wa mawazo wa kumkosa mama yake.

Akaamini maneno ya wahenga ya kuwa tumbo la shari huzaa heri, akawashukuru sana kimoyomoyo Askari Kanzu waliomkamata mtaani kule Jijini Nairobi. Kutokana na shari yao ya kumkamata imemlaimishia njia ya kufahamu sehemu alipo mama yake kiurahisi kabisa. Bila kupoteza muda baada ya kufikishwa Jijini Nairobi akarejea kule kwenye kituo cha watoto yatima kufuata nyaraka zake. Kwa bahati nzuri alikuta wamezihifadhi sehemu salama huwa wakiwa na matarajio kuwa lazima atarudi tena kuzifuata nyaraka zake hizo.

Siku ya pili yake tu akakwea pipa kurejea zake Jijini Dar es Salaam tayari kwa kujipanga upya kuanza msako rasmi dhidi ya mama yake mzazi. Aliyaona gerezani kule Shimo la Tewa alipewa onyo ayafutike futi moyoni mwake asimsimulie mtu, vinginevyo atajikuta matatizoni. Maana hamna aliyeingizwa humo akatoka salama salimini, ni yeye tu alipata bahati ya mtende kuota jangwani.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Aliporejea Jijini Dar es Salaam, Dr.Pesambili akajikuta anafuraha mbili bila kutarajia. Alimkuta mama Deborah ambaye anaishi nae chini ya paa moja, afya yake imeimarika vilivyo kuliko kawaida. Pia alishaanza kurudisha kumbukumbu zake kichwani taratibu. Akaanza kumkumbuka binti yake wa pekee kwenye hii dunia Deborah pamoja na ndugu na jamaa zake akina Mjomba Mkude. Akapatwa sana na tashiwishi na wahaka wa kutaka kufahamu wapi walipotokomea mpaka akaokotwa na Dr.Pesambili.

Ikabidi Daktari amkalishe kitako na kumuelezea mkasa wake mzima wa kuugua kwake mpaka alivyofanya maamuzi ya kumbeba jumla jumla. Swali la wapi alipo Deborah likakosa majibu toka kwa Dr.Pesambili, hivyo wakaweka adhima afya yake itakapotengamaa wataanzisha operesheni ya kumsaka Deborah popote alipo aweze kuungana na mama yake. Siku zilivyokuwa zinazidi kusonga ndipo alipozidi kunawiri na kutakata, mpaka akaacha kabisa kutembelea gongo akawa anatembea kwa kuvuta mguu kwa mbali. Katika mazungumzo yao kama mama na mwana, ndipo Dr.Pesambili akagundua kuwa mama Deborah ni nesi kwa fani yake. Jambo hilo lilimfurahisha sana Dr.Pesambili kwani aliona ndoto zake za kutaka kufungua hospitali kubwa ya kisasa itatimia kwa urahisi kutokana na kuwa karibu na mtu mzoefu wa shughuli za hospitali.

Dr.Pesambili kwa vijisenti vyake alivyodunduriza wakati anafanya kazi Morogoro akafanikiwa kununua kiwanja maeneo ya Tuangoma, Kigamboni ekari 20 mahususi kwa ujenzi wa hospitali. Mipango ya Dr.Pesambili sasa ikawa akitoka tu kumtafuta mama yake mzazi Jijini Arusha na Kilimanjaro basi ahamishie nguvu zake kwenye ujenzi ili aanze hata walau na jengo moja. Wawili hao sasa ikawa kiba kibandika kiba kibandua kila wakati wanatembea pamoja, wasiojua kitu baina yao walidhania ni mama na mwana kwa jinsi walivyoshibana.

"Mama nitaomba kesho unisindikize Jijini Arusha, ninaelekea kwenye ofisi za 'Peace-Corps Tanzania'......hivyo ingekuwa bora tuambatane wote kwa pamoja na wewe upate kuchangamsha mwili" alisema Dr.Pesambili wakiwa wapo wawili tu mesini ndio kwanza wamemaliza mlo wao wa usiku. Mama Deborah kusikia Peace Corps Tanzania moyo wake ulimlipuka kama taa ya chemli iliyoishiwa mafuta inavyolipuka.

Mawazo yake yakarudi kisengerenyuma sana mpaka yakafikia mwaka 1986, akikumbukia mumewe alivyopata madaraka makubwa ya kuongoza shirika hilo, na mpaka madaraka hayo kuwa ndio sababu ya kifo chake kuuliwa na majambazi. "Mama mbona hunijbu kitu umebaki umeshangaa tu kulikoni, upo mzima?" aliuliza Dr.Pesambili akiwa ameshashikwa na hofu huenda afya ya mama Deborah inataka kuanza kubadilika.

"Nipo fiti mwanangu kuwa na amani, nimekumbuka tu miaka ya nyuma nimewahi kufika Jijini Arusha, mume wangu anafanyakazi shirika hilo hilo ulilolitaja" aliongea kiunyonge mama Deborah huku akijiweka sawa kutaka kufahamu anachokwenda haswa kukitafuta Dr.Pesambili huko kwenye ofisi za 'Peace-Corps Tanzania'. "Nilipokuwa Jijini Nairobi katika harakati za kumsaka mama yangu mzazi, nimepata penyenye za kuaminika zisizo na hata chembechembe ya mashaka kuwa mama yangu mzazi ni Mtanzania na yupo Jijini Arusha au Moshi, nikaambiwa amewahi kufanya kazi kwenye ofisi hizo, ndio maana nimeamua kuanzia taftishi yangu hapo..!" alisema Dr.Pesambili sasa akiwa ana amani ya moyoni baada ya kuondokwa na hofu yake dhidi ya afya ya mama Deborah ambaye sasa alikuwa anamuona ni kama mama yake rasmi.

Mama Deborah mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda mbio, baada ya kusikia kuwa mama yake Dr.Pesambili amewahi kufanya kazi Peace-Corps Tanzania tena katika miaka ambayo mumewe alikuwa ndio Bosi hapo. "Ina maana huyu Dr.Pesambili ndio mtoto wangu wa kambo kwa Bi mdogo wa mume wangu?" alijiuliza hilo swali nafsini mwake mama Deborah, lakini akalipuuzia kwa muktadha kwamba Dr.Pesambili kampa taarifa kuwa baba yake mzazi amefariki gerezani nchini Italia hivyo kwa vyovyote vile hawezi kuwa ni mtoto wa mumewe Bosi Minja.

Wakaendelea na maongezi yao usiku huo huku mama Deborah akiweka nia ya kuelekea Marangu kwa wakwe zake kuwasalimis kutokana na kupotezana na kwa miaka mingi. Mpaka ilipofika saa 4:00 usiku wakaagana kwenda kulala, kuipumzisha miili yao wakijiandaa kwa safari ya kesho yake asubuhi kuelekea Jijini Arusha. Usiku kucha mama Deborah hakupata usingizi mtamu, alishikwa na kimuhemuhe cha kwenda kuwatembelea ukweni kwake Marangu, ili akamjue haswa mtoto wa kiume wa Bosi Minja ni nani na yupo wapi kwa sasa.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
Back
Top Bottom