Riwaya: Konstebo Zungu

Riwaya: Konstebo Zungu

SEHEMU YA KUMI NA NANE

"Nipo mwenyewe.... nipo mwenyewe usiniue."
"Amekuagiza nani?"
"Inspekta.... Inspekta Kobo." Alijibu kwa utulivu.
Nguzu akaishiwa hamu! hakutarajia jibu lile.
Huu ukawa ni mkanganyiko mpya kutoka katika majibu ya muhariri na huyu bwana mlinzi.
Akamtazama kwa jicho lililotangaza chuki ya waziwazi kabla hajamtundika swali jingine katika namna ya kisharishari.
"Muonekano wake upoje huyo bwana wa kuitwa Kobo.
Huku akikumbuka kuwa akijifanya hajasikia swali lile basi kifuatacho ni kubamizwa ngumi na kuulizwa swali la kukera safari hii aliwahi kujibu.
Akauelezea wajihi wa inspekta Kobo.
Nywele ndefu nyeupe zinazojaribu kuuficha uwalaza wake, ndevu fupi zenye uwiano sawia na nywele zake katika rangi.
Umri wake ukichezea miaka sitini hadi sitini na nane.
Konstebo Nguzu akachoka upya!
Huyu hakuwa inspekta Kobo aliyekuwa akimfahamu yeye.
Lakini kilichomjaza nguvu upya ni ule utambulisho ulikaribiana na ule ambao alielezwa na muhariri wa gazeti baada ya kumbana vizuri.
Konstebo akiwa anajiandaa kumuuliza tena yule bwana swali jingine, akafanya kosa kuitazama anga kama anayefikiria aulize kwa namna gani nyingine ili apate mwanga mkali anaouhitaji katika giza lile nene.
Yule muhanga alitokwa na teke kali likatua vyema katikati ya mapaja ya Nguzu, teke lile likamfanya Nguzu ainame.
Naam! adui alihitaji hivyo.
Uso ukawa jirani naye, akatokwa na teke kali sana lililoongezewa uzito na kiatu kigumu alichokuwa amevaa.
Uzito huu ukatua barabara katika uso wa Nguzu.
Ilikuwa mchana ghafla ukawa usiku kwa Nguzu pekee. Pigo lile lilimsukuma mpaka mlangoni.
Akaingia na ule mlango, kiuno kikapokea maumivu stahiki.
Konstebo Nguzu akajaribu kurejea katika mapambano lakini giza lilikuwa linamuharibia, hakumwona adui yake. Sanjari na hilo alikuwa akipambana kuilamba damu iliyokuwa inamtoka puani.
Adui alikuwa amechachamaa.
Alijaribu kutapatapa lakini adui hakumwachia nafasi, ni kama alimaanisha kutaka kuondoka na roho ya Nguzu na hakuhitaji kumuuliza swali lolote lile.
Nguzu alibaki kuikumbatia sakafu wakati mateke yasiyokuja kimpangilio yakimwandama.
Pumzi zikaanza kumsaliti, na hapa akajaribu kwa mara ya mwisho kuusaka uhai wake ambao yule bwana alitaka kumpokonya angali hajamaliza shughuli yake.
Akaituliza akili katika maumivu. Kitu ambacho wanadamu wachache sana wanaweza.
Kasumba ya mwanadamu akisikia mlio wa risasi anaanza kukimbia asijue kama anaikimbia ama anaikimbilia risasi.
Nguzu akautafuta uelekeo wa yale mateke makali yaliyomaanisha kuua. Akaupata uelekeo wa mpigaji, na jinsia livyokuwa anapiga hovyo akatambua bayana kuwa anatumia zaidi hasira na hapohapo anapoteza muhimili wa umakini.
Teke lilipomwingia akajitutumua na kusimama wima, na kujirusha kulekule katika uelekeo wa adui yake.
Karata sahihi!
Akamsomba yule bwana na kutua naye chini.
Majogoo mawili yaliyochoka haswa yalikuwa yamelaliana.
Na heri tele kwa jogoo lililomlalia mwenzake.
Martin Nguzu alikuwa juu.
Hakuweza kurusha ngumi, kuchimba mikwara wala lolote lililoonyesha umwamba. Wote walikuwa wanahema juu juu.
Martin akapambana na kufanikiwa kuyafumbua macho yake.
Likafumbuka jicho moja kwa shida sana.
Akamwona adui yake akiwa mdomo wazi, anahema juu juu!
Akaiona shingo ikiwa wazi.
Akajitutumua akaifikia na kuikaba, anayekabwa akaanza kurusha mikono kuzuia kitendo kile.
Hakika walikuwa wamechoka!
Vishindo vilisikika kwa mbali, Nguzu akahisi hatari kubwa inakuja mbele yake.....
Uwezo wa kupambana kwa wakati ule hakuwanao, kama huyu aliyechoka anashindwa hata kummalizia vipi hao wanaokuja huku wakiwa na nguvu mpya.
Akajigeuza na kutua chini kisha ukaanza mpambano mpya wa kila mmoja kujaribu kusimama.
Nguzu akajaribu akaanguka, mwenzake naye yakamkuta yaleyale.
Nguzu akakerwa na hali hii ya kujikuta mnyonge angali oparesheni ikiwa mwanzo kabisa.
Hali ikazidi kuwa mbaya alipomwona yule mlinzi akifanikiwa kusimama wima, akayafuatilia macho yake yakiwa yanaangaza huku na kule hatimaye kwa pamoja wakajikuta wakiitazama bastola iliyokuwa imetulia sakafuni ikisubiri yeyote ajuaye kuitumia na aitumie.
Nguzu alitamani nguvu zimjae na akimbilie kule kuiwahi lakini hakuwa na nguvu za kutosha na alikuwa katika maumivu bado.
Kifo kikanukia katika namna ya kukera. Yule mlinzi akaanza kujivuta kwa kasi kuifuata bastola ile, Nguzu akaanza kujiona yu mjinga kukisubiri kifo chake bila dalili zozote za kupambana.
Akapitiwa na fikra za harakaharaka juu ya hayati babu yake, aliyemrithisha jina hilo lenye maana kubwa.
Nguzu 'chikichia' hapa hapafai tena! alijionya huku akiangaza lilipo kimbilio.
Hakuliona kimbilio kabla hajamwona yule mlinzi akigeuka huku akiwa na bastola mkononi.
Akafyatua hovyo kwa mara ya kwanza, bastola isiyokuwa katika kiwambo cha kuzuia sauti ikatoa mlio mkubwa.
Mlio huu ukamuhamasisha Nguzu kujitutumua na kukimbia.
Alikimbia ndani ya ile nyumba huku akiamini kuwa ataukuta wazi ule mlango aliokuwa anaufahamu ili aweze kutokea upande mwingine.
Hofu ya kifo ilizidi kujenganaye urafiki, alijitutumua akaufikia mlango.
Mungu wangu!! ulikuwa umefungwa kwa kutumia mnyororo.
Hakuwahi kuiona hali kama hii hapo kabla. Huku nyuma akawa anamsikia yule mlinzi akitoa matusi yote huku kila mara akimaanisha kuwa iwe isiwe lazima amuue.
Nakufa! Hatimaye Nguzu akakiri, lakini hakubaki kibwegebwege afe bila kupambana.
Akausukuma mlango wa chumba cha Zubeda ambacho enzi zile alikuwa akiingia huku amebebwa mgongoni na koplo yule mwenye asili ya Tanga lakini akiishi zaidi Mwanza.
Sasa aliingia katika chumba hiki huku akiwa anasota, jicho moja likiwa linaona kwa tabu huku lile jingine likiwa limefumba kabisa.
Hamadi! mlango ulikuwa umezuiwa na kitu kwa ndani.
Hofu ya kichwa chake kusambaratishwa na risasi ikamfanya Nguzu ajitupe mzima mzima na kufanikiwa kukisogeza kizingiti.
Akajikuta ndani ya chumba.
Sauti ya yule mlinzi nayo ikazidi kutapatapa ikitishia kuua.
Chumba kilimkaribisha Nguzu katika hali ya utulivu, utulivu ule ulimtisha zaidi, akajaribu kufikiri ni wapi atajificha ili kumkwepa mshika bunduki.
Uvunguni! hili lilikuwa wazo la kizembe lakini walau naye aliwaza.
Akaanza kujitutumua aingie uvunguni, akaanza kujivuta kwa kutumia tumbo.
Hakuzama sana kabla hajabamizwa ghafla na kitu kigumu katika paji la uso wake.
Ile anajaribu kujiweka sawa akatandikwa teke kali usoni, akajikuta yungali nje ya ule uvungu huku akiwa nusu hai nusu mfu.
Alikuwa amepiga magoti damu zikimvuja.
Hazikupita sekunde nyingi kiumbe akauona mdomo wa bunduki ukitangulia kutoka katika ule uvungu.
Nipokee baba nakufa mimi Nguzu! alijifanyia dua upesiupesi.
Na hapo mlango ukasukumwa akamsikia yule mlinzi akiendelea kuropoka.
Nguzu akatambua kuwa nyuma yake palikuwa na mtutu na pia mbele yake alijionea waziwazi.
Swali likabaki juu ya nani atakayekuwa wa kwanza kufyatua ili auondoe uhai wake.
Yule wa uvunguni akawa wa kwanza kufyatua.
Risasi ikapenya jirani kabisa na sikio la Nguzu, ikafanya mlio kama wa nyuki mwenye hasira.
Kisha kishindo kikafuatia, Nguzu akatua chini akiangukia tumbo.
Kichwa chake kikawa jirani kabisa na ule mdomo wa bunduki iliyotokea uvunguni.
Na hapo akaviringika na kutoa uvunguni mshambuliaji yule aliyemkosa Nguzu maksudi na kumlipua aliyekuwa nyuma yake.
"Nilijua kuwa umekufa duniani, lakini si katika moyo wangu. Nikaamini tutakutana mbele ya haki, sijui kama ni mahali sahihi tulipokutana Martin, konstebo Martin Nguzu." Sauti imara ya kike ilizungumza.
Nguzu hakuhitaji macho yake katika hili, masikio pekee yalitosha kutambua kila kitu. Hatimaye kinywa kizito kikajitutumua na kuzungumza.
"Koplo Zuu!"
"Nihakikishie kuwa sitakiwi kukulipua kwa sababu u mmoja kati yao..."
"Si..sijui kitu hapa. Usilipue koplo." Alisihi Nguzu.
Zubeda akamdaka na kumsimamisha. Nguzu akakosa muhimili akataka kuanguka, Zubeda akatega mgongo wake kama alivyokuwa akiutega zama zao za furaha.
Nguzu akatua juu yake.
Zubeda akaanza kupiga hatua kutafuta uelekeo, Nguzu akiwa anakoroma.
Hali yake ilikuwa mbaya sana. Zubeda naye alikuwa anajitutumua, mguu wake mmoja ulikuwa haujaimarika..
Zubeda akiwa ndiye anayetegemewa alijaribu kufikiria juu ya uwepo wao pale ndani. Hapo kabla alikuwa amefanikiwa kuua na kisha kumpokonya bunduki mtu aliyewekwa kwa ajiri ya kumlinda asiweze kuleta bughudha yoyote.
Walimpatiliza kwa sababu ya miguu yake kuwa na mushkeli.
Dharau zao zikawafanya wapunguze ulinzi na kumwacha mbabe mmoja.
Yakamtokea puani!
Wakati Zubeda akiendelea kufikiria ni nini kilitokea hadi akabadilishiwa ulinzi ghafla, kutokea ule ulinzi aliowekewa na inspekta Kobo hadi ulinzi huu wa ajabuajabu. Akalishuhudia geti likifunguliwa na gari ikaingia huku askari watano waliovalia sare wakitangulia mbele.
Balaa!
Akajaribu kumshirikisha Nguzu aliyekuwa bado hoi. Nguzu hakuwa na la kuchangia.
Askari yule imara ndani kwa ndani na legelege kwa umbo la nje alitoweka mpaka chooni. Huku aliweza kuona kila kitu kilivyokuwa kinaendelea nje.
Alimtua Nguzu na kumsihi anywe maji yanayotoka katika bomba ili aweze walau kupata nguvu kiasi. Wakati huo akiendelea kuilazimisha akili yake ifanye kazi kwa kasi zaidi kuhusu tukio linalokuja mbele yao, alifahamu fika kuwa hakuna namna ya kuwa salama angali mle ndani kuna maiti mbili.
Kwa namna yoyote yeye na Nguzu watayamalizia maisha yao gerezani.
Maji yalikuwa msaada mkubwa sana kwa Martin Nguzu. Hayakumfanya kuwa imara sana lakini walau macho yake yaliweza kuona na aliweza kupumua vyema kwa sababu aliweza kuyaondoa mabonge ya damu yaliyounda uzio mbele ya pua zake na kumsababisha apumue kwa mdomo badala ya kutumia pua.
"Martin, Martin!" Zubeda aliita kwa kunong'ona.
Konstebo Martin akaupokea wito ule kwa kutulia akimsikiliza.
"Askari wote wanatuzingira." alimweleza kana kwamba Nguzu alikuwa anafahamu tayari juu ya uwepo wa ugeni ule..
"Akina nani? wako wapi?"
Zubeda hakumjibu badala yake alimsaidia kunyanyuka na kisha akamwelekeza kila alichokuwa akikiona kwa nje.
Walichoka!
____
BAADA ya kukataa kata kata kubadili maelezo yake, amri ilitolewa ya kwenda kupekua nyumba ya inspekta Kobo ili iweze kubainika kama anayo mawasiliano yoyote aliyowahi kufanya na kikosi cha majambazi kilichoinyanyasa Shinyanga kwa wakati ule huku askari kadhaa wakiangushwa na kupoteza maisha.
Msako wa kwanza haukuzaa matunda yoyote waliyoyatarajia.
Walikata tamaa huku wakianza kuamini yawezekana kuwa inspekta Kobo aidha hajuani na lile kundi ama la ni mafia aliyefuzu mafunzo yote stahiki.
Yaani hata umkate mguu akisema sijui ni sijui. Anameza maneno yake na kuingia nayo kaburini...
Wakiwa wanakaribia kuondoka, askari mmoja akafika na kitu kipya.
Akamtupia swali Kobo.
"Hii nyumba unayoishi ni mali ya nani?"
"Binafsi." Alijibu kwa sauti iliyokata tamaa.
"Umeijenga mwaka gani na umeanza kuishi humu lini?"
"Huu ni mwaka wa kumi sasa naishi humu."
Jibu lile likamfanya askari yule afanye tabasamu hafifu kabla hajamtundika pagumu bila yeye kujua.
"Umejenga nyumba nyingine tofauti na hii?"
"Hapana!"
"Mtu akifika hapa kukutafuta na asikupate je? ni wapi zaidi anaweza kukupata?"
"Kazini kwangu."
Jibu la sasa likayafanya meno ya yule askari yaonekane kwa sababu ya kicheko kidogo.
Na hapo akayabwaga makaratasi kadhaa mbele ya maaskari wenzake na Kobo akayashuhudia.
Alikuwa ni mnyonge lakini haya yalimtia unyonge zaidi.
Mikataba!
Mikataba baina yake na mmiliki wa nyumba aliyokuwa akiishi hawara yake.
Koplo Zubeda!
Alitamani ardhi ifunguke atumbukie humo, alijiona waziwazi kuwa alikuwa anaelekea pabaya.
Kwanza alidanganya kuwa hana makazi mengine zaidi ya hayo, pili mikataba yote aliiandikisha kwa majina yake na si ya Zubeda.
Mkataba wa mwisho aliuandikisha miezi miwili tu iliyopita.
Anakwepa vipi rungu la sheria?
Watamuhesabu kama mnyang'anyi ambaye analo eneo la siri kwa ajiri ya kufanyia shughuli zake haramu.
Inspekta Kobo akaumia zaidi kwa sababu alikuwa anakwenda kumweka Koplo Zubeda na maaskari aliowaweka kumlinda matatani.
Wote hawa watahesabika kuwa ni chama kimoja cha kimafia na wataminywa kama alivyominywa yeye hadi kufikia hapo alipo.
Akaunganisha meno yake kwa uchungu mkubwa.
"Tunaenda moja kwa moja hadi katika nyumba hii. Ukithubutu kutudanganya utajutia uongo wako" Akachimbwa mkwara, akamtazama yule bwana kwa jicho kali, akajilaumu sana kwa sababu alikuwa na pingu, vinginevyo angefanya shambulizi kwake.
Hakupendelea masuala ya kuchimbwa mkwara!
Inspekta Kobo akawaelekeza nyumba ile inapopatikana, na hata asingewaelekeza bado kuna namba ya nyumba iliorodheshwa katika ile mikataba.
Bila kusahau kiherehere cha mmiliki wa nyumba ile kuweka nambari yake sahihi kabisa ya simu ya mkononi
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom