Riwaya: Konstebo Zungu

Riwaya: Konstebo Zungu

Mwanzo zilikuwa double double, mwendo kasi, sasa hivi ni speed ya Gari za makongo juu
 
HII HAPA SEHEMU YA 15

ILIKUWA safari iliyojaa katika kichwa chake ghafla baada ya vita ile ya usiku iliyoondoka na uhai wa watu watatu ambapo mmoja kati yao alikuwa ni kiongozi wao kwa mujibu wa maelezo yao.
Martin Nguzu ambaye sasa hakuwa akiushangaa uwezo wake wa kukabiliana na maadui alikuwa amewaangusha wengine watatu huku akifanikiwa kuwapokonya bunduki tatu pamoja na risasi za kutosha kabisa.
Hakutaka kulala baada ya kuhakikisha ameitelekeza ile miili mbali na ngome ya mzee Majenga. Alimwamsha mzee Majenga na kumweleza kwa ufupi juu ya kilichotokea.
Tofauti na matarajio yake kuwa taarifa ile itamtisha sana Majenga, hii ilikuwa kinyume. Mzee Majenga akatokwa na kicheko kidogo kisha akampigapiga kifuani Martin Nguzu na kumwita kwa jina la babu yake.
"Ngengekuzenza Nguzu umezaliwa upya..." Kauli ile ilimtoka na kumwacha Martin Nguzu katika pumbazo asielewe ni kitu gani bwana yule alimaanisha.
"Mimi nimezeeka kijana wangu, niliisubiri sana hii vita kwa muda mrefu lakini imekuja nikiwa mzee tayari. Nenda ukapambane hii ni vita yako na inakuhusu. Nakuachia haya maandishi niliyoyaandika bila kuongeza wala kupunguza neno kutoka katika kinywa cha hayati babu yako anayeishi sasa katika nafsi yako. Hakikisha unayamaliza yote kabla haujaivaa hiyo vita...... mimi nitakuwa salama kabisa na tutakutana nikiwa hai, na hata nikifariki ni kwa sababu ya uzee tu..." Aliongea kwa ujasiri mkuu. Kisha akachechemea hadi ndani na kuchukua makaratasi yaliyoandikwa kwa kalamu akamkabidhi Martin.
"Nilikuwa napenda sana kuandika na babu yako alikuwa anapenda sana kunisimulia, nadhani ni maneno hayo kwa ufupi yatakupa jawabu nilikutana vipi na babu yako." Majenga alitoa kauli ile na Martin akaipokea lakini alikuwa na swali la ziada.
"Niliokoka vipi katika ule moto jijini Dar es salaam?"
"Mzee wako asingeweza kukuacha uangamie. Wazee wa zamani hawakuwa wa kawaida, akinuia jambo linakuwa kama lilivyo, nadhani ni kutokana na kutenda dhambi chache nd'o maana Mungu alikuwa akiwasikiliza." Alifafanua na kuzidi kumvuruga Martin.
Akagundua mvurugano ule, akaongezea "Kasome haya yote kabla hujaamua wapi pa kuanzia"
Maongezi yakaishia hapo.

MAANDISHI YA NGENGEKUZENZA.
Ubaya ni kwamba wakati wa ukoloni, sisi watu wa rangi nyeusi hatukuishia tu kunyanyaswa na ngozi nyeupe katika uhai wetu, hata ulipokuja ustaarabu wa kuhifadhi maiti zetu sisi tuliwekwa katika kundi la mbwa koko aliyefia jaani baada ya kukabwa na mfupa aliodhani ni mnofu.
Ukipata bahati sana unafukiwa, ila ni waafrika wachache waliokuwa na bahati, wengi tulitunukiwa nuksi.
Ukiwa na nuksi unaachwa hapohapo ulipofia ama unasogezwa kidogo porini, ukawe chakula kwa wanyama wenye tabia ya uvivu katika suala la kuwinda na ndege wanaoona sifa kudonoa donoa.
Hata babu yangu alikuwa na nuksi vilevile baada ya kufariki alitupwa, akaipata bahati akiwa maiti tayari waafrika kadhaa wakamfukia.
Baada ya kuupata uhuru wetu nikawa naitembelea ile sehemu niliyoaminishwa kuwa babu yangu alifukiwa pale, pakawekwa alama nami nikawa naenda kumsalimia na kuzungumza naye bila kujali ananisikia ama la!
Sasa yule mwanahizaya baada ya kuona haitoshi kumchukua kiharamia mke wangu na kuniacha katika jitimai, akaona hata! hii haitoshi huyu bwege bado anapata raha. Akaanza kuniandama kivingine, najua aliwatuma mashushu wake waliokiamini na kukiabudu chama chao kuliko Mungu wa mbinguni na miungu ya porini.
Hawa wakamfikishia habari kuwa ninayo furaha nyingine, furaha ya kuzungumza na babu yangu makaburini.
Ikapita ajenda katika siku nisiyoijua na baadaye ikawa ni amri bila kutahadhalishwa.
Eneo lile lilipaswa kupandwa miti, mara lilitakiwa kupita barabara.
Sikuelewa hata kidogo, na hakuna aliyesubiri nielewe.
Kwani Ngengekuzenza nani mpaka aelewe?
Lile nililoamini kuwa ni kaburi likavunjwa na huyu mkoloni mshenzi mwenye rangi kama yangu huku akiiga miondoko ya wazungu na afro yake kichwani akiipaka kalikiti na kuwa laini kama nywele za mkoloni.
Lugha yake pia ilifanana na yao.
Poor Joseph Kazeze!
Kama ni kunipiga, hapa alinipiga na mjeledi wa chuma nikaangukia pua huku mikono yangu ikishika makaa ya moto.
Huyu mjinga aliniweza hakika!
Uchungu wangu ule nikamshirikisha mwanangu Salama nikamweleza kuwa Jose anataka kuvuka mipaka ambayo ameivuka tayari, yaani sielewi anachotaka.
Salama alinisihi niachane naye, nikaona hajui uchungu ninaoupitia kwa kupokonywa mke na kisha hapohapo nikapokonywa furaha yangu.
Babu yangu!
"Salama, nikiachana naye akagundua nina furaha kuwa na wewe atakuchukua na wewe pia...." nilimwambia Salama. Wazo hili likamkuna na kuiona hatari ya waziwazi.
"Sasa utamfanya nini?"
"Yule ni mjinga tu kwangu, nataka nimfanyie yale mambo ambayo wajanja huwafanyia wajinga wanaodhani pesa nd'o ujanja." nilimweleza huku nikiona wazi kuwa hanielewi.
"Unataka upigane naye?" aliniuliza.
"Nikipigana naye wote tutakuwa levo ileile ya ujinga, nataka nimpige ili tuunde daraja katika ya nani mjinga na nani mjanja."
"Lakini baba, huyu ana pesa na cheo atakusumbua sana. Yaani nina uhakika hautafikia hata nusu ya azma yako."
"Kwanini unasema una uhakika." nilimuuliza salama.
"Si kila kitu kipo wazi, ana pesa na vyeo."
"Sikiliza mwanangu Salama na uliweke hili milele katika maisha yako, hapa duniani kuna kitu kimoja tu nd'o cha uhakika vingine vyote si vya uhakika. KIFO pekee ndo jambo la uhakika, kila mtu atakufa hii haina mjadala. Ujiue, unyweshwe sumu, ugongwe na gari ama hata ukilala usiamke. Vyote vina maana moja tu ya uhakika.... asije akakudanganya mtu kuwa jambo hili ni uhakika... anakulaghai nawewe unayemsikiliza na kumkubalia unakuwa upande wa mjinga. Sipendi uwe mjinga siku moja...." Nilimsomea mambo yale. Yakamuingia na kumpa ujasiri naye akanibariki katika uamuzi wangu na hiyo ilikuwa ni mnamo mwaka elfu tisa mia themanini na tatu ama nne kama sijasahau.
Sijui itakuwaje miaka ya huko mbele lakini enzi zetu hizi hapakuwa na ulinzi wa kutosha kwa viongozi, ulinzi huo tuliusikia tu na kuuona walipokuja viongozi kutoa nje, Mwalimu Julius Nyerere alihamasisha sera za kuishi kijamaa, nasi tukaamua kuishi kama ndugu.
Hapakuwa na wa kumpinga kirahisi mwalimu. Ukitaka kumpinga sisi tunakwambia nenda ukapambane kuileta Tanganyika huru ndipo ujilinganishe na mtaalamu huyu.
Hivyo tuliishi kijamaa sana, halikuwa jambo la ajabu kukutana na mwalimu Nyerere barabarani. Sasa vipi kuhusu mjinga huyu anayeitwa Joseph Kazeze?
Sidhani kama kwa miaka yenu huko mbeleni itakuwa hivi. Nahisi hata balozi naye atatafuta ulinzi...
Nilikueleza awali kuwa tangu nilipokuwa mtoto nilikuwa nina uwezo mkubwa sana darasani, hata akili yangu haikuwa ndogo katika kufikiri.
Nikaamua kuitumia akili yangu kumwonyesha yule bwana nini maana ya mwanaume kutoa machozi.
Kwakweli nilimkosesha amani!
Kwanza nilifurahia kile kitendo cha mwalimu Nyerere kutowafukuza wazungu baada ya kutupatia uhuru, hivyo upatikanaji wa silaha hadi miaka ya themanini bado ulikuwa ni mwepesi sana, unaweza kuipata bunduki hata kwa kubadilishana na gunia la mahindi pekee.
Zilikuwa zimezagaa.
Nami nikajipatia bunduki yangu, uzuri nilipitia jeshini hivyo sikuhitaji kufundishwa lolote.
Nikamuaga mwanangu kuwa naanzisha mapambano rasmi.
Sikuwahi kuua ila nilijeruhi sana.
Nilianza na baba yake mzazi, akiwa katika mizunguko yake. Nikamteka na kumpiga kipigo cha mbwa mwizi, akavunjika mkono.
Sikumtumia salamu Jose Kazeze kama ni mimi ili aendelee kuhadaika.
Akafuata mdogo wake, huyu nilimfungia safari hadi Morogoro, nikamkamata na kumfunza adabu asiweze hata kuiona sura yangu.
Jose Kazeze kitu alichosahau ni kwamba sisi tulikuwa marafiki na nilimfahamu vyema yeye na familia yake.
Niliendelea kumpa presha bwana yule kwa kufikia hatua ya kuvamia kwake nikarusha risasi zikavunja vioo vya nyumba aliyokuwa akiishi lakini sikumdhuru mtu na sikutaka kumdhuru.
Uwezo wangu katika kupanga matukio ulianza kunishangaza hata mimi, kila nikilala na kuamka nawaza pigo jingine.
Jose akaanza kukonda!
Mara akaachana na yule mwanamke aliyenipokonya.
Nami sikurudiana naye mjinga yule aliyekosa hata nukta ya akili.
Nilikuwa nina hasira kali.
Baadaye baba yake alifariki, kwa magonjwa mengine sijui kama na kile kipigo kilichangia.
Siku mbili baada ya kuzikwa nikaenda makaburini, huku nikaweka bomu nililolipata kwa bei nzuri tu.
Likafanya mlipuko uliotikisa nchi.
Hakuna kilichobaki zaidi ya jeneza kusambaratika huku na kule.
Hili lilikuwa pigo kubwa zaidi, wanandugu wakalundikana nyumbani kwa Jose Kazeze kujadiliana nini kinaendelea.
Nikavamia na huko na kurusha bomu jingine katika choo kilichokuwa mbali kidogo na nyumba na hii ni baada ya kuhakikisha hapakuwa na mtu ndani yake.
Mparangano uliojitokeza nilijikuta nacheka mwenyewe.
Amakweli mtenda akitendwa....
Jose akazidi kuzorota kiafya.
Ni hapa ndipo nikaamua kumweleza bayana ili kama ni kufa kwa mshtuko afe tu, who cares?
Hakufa!
Ila alipagawa vibaya mno, na hapo ndipo ikaanzishwa oparesheni ya Ngengekuzenza Nguzu anasakwa auwawe.
Kisa ni jambazi, yakaundwa matukio ya kushangaza kunihusu mimi na hapo nikaanza kusakwa rasmi.
Nilijua kuwa hali ni mbaya, nikaraejea kwa mwanangu... usiku wa mwisho kumwona mwanangu.
Akanieleza kuwa yu mjamzito, nikamweleza kuhusu kinachoandikwa na magazeti ya serikali huku nikimweleza kuwa moyo wangu u radhi kuwa nimemuweza yule bwana.
Zaidi ya hayo nikamsihi kuwa iwapo atazaa mtoto wa kiume basi amwite Nguzu!
Tulikumbatiana huku sote tukishindwa kuyazuia machozi.
Nikaondoka na kuja kwako Majenga unihifadhi nikusimulie ya kuandika kama ulivyohitaji wewe kijana wangu.
Na nimejitahidi sana kukusimulia.
Maandishi yale yaliacha nafasi kubwa kisha ikafuata aya ambayo mwandishi wake alikuwa ni Majenga.
Mnamo mwaka 1988 mwezi wa kumi na moja mzee Ngengekuzenza mwenye msongo wa mawazo kwa kuishi maisha ya mashaka kila kukicha aliniaga kuwa anakwenda msalani, ilikuwa majira ya usiku. Hakurejea mapema nikalazimika kutoka pamoja na mbwa kwenda kumtafuta.
Nilimtafuta sana hadi pambazuko likanikuta nikiwa namtafuta, mbwa asiyechoka ndiye alinihimiza kumdaka mzee wangu nimpendaye.
Hatimaye nikaufikia mti ambao alikuwa amejitia kitanzi.
Nasikitika kuwa sikuwahi kukiri kuwa ninamfahamu mzee yule kwa sababu za kiusalama, alikuwa anasakwa sana na jeshi la polisi kama jambazi sugu.
Niliporejea ndani nikakutana na karatasi katika kitanda alichokuwa akilalia. Haikuwa na maneno mengi sana aliniandikia kama nilivyokuwa nimefanya tayari.
"Umenihifadhi kwa moyo wote wa upendo, wewe ni kijana wangu nikupendaye. Ninaomba uendelee kunitunzia maneno yangu..... utawapatia wajukuu zangu ili wajifunze kuwa babu yao hakuwahi kuwa mtu dhaifu hata kama nilionewa, babu yao sikuwahi kuwa jambazi hata kama watayaona maandishi hayo, pia kwa imani yangu kuu naamini kuwa sijafa kirahisi rahisi. Mizimu ya mababu zangu waliouwawa kifedhuli utumwani imeniambia kuwa najipumzisha ila ipo siku nitazaliwa na nitazaliwa katika damu yangu mwenyewe. Ninapumzika Majenga ila nikizaliwa tena usishangae. Naamini mizimu hii kulikoni dini walizotuletea wakoloni, dini zilizotuongopea kuwa Mungu ni mzungu, zikaenda mbali na kusema kuwa Mungu anaishi katika majengo yao waliyoyajenga.
Dini za kishenzi zilizonipatia jina la kishenzi, Frolian na kunipokonya jina la kishujaa kutoka kwa babu yangu.
Dini zilizotulaghai kuwa kila asemacho yule mzee mweupe anayesimama mbele yetu basi ni sawa, anatuona tunateseka na anasema tumwachie Mungu, nasi tukijaribu kupambana anasema tena sisi ni watu wabaya sana na hatufai kuwekwa kundi la wanadamu.
Dini zao hazijaniambia kuwa siku moja nitarejea, lakini wazee wangu ambao tuliwalilia njaa wakatusikia katika miti, tuliwaomba kila kitu na walikuwa wakweli.
Wazee hawahawa wamesema nami, acha nipumzike ila ipo siku nitarejea na sitakuwa wa kujificha tena.
Kwaheri mjukuu wangu!"
Kisha akwakeka hitimisho Majenga kwa wino mzito.
"MNAMO MWAKA 1988 BABU YETU Ngengekuzenza aliaga dunia na ni mwaka huohuo mwanaye Salama alipata kujifungua... yule mtoto akaitwa NGUZU"
______
NGUZU alibaini kuwa alikuwa anatetemeka baada ya kuimaliza sentensi ile ya mwisho.
Akaituliza akili yake na kutaka kumaizi ni kitu gani kimempa majibu katika maandishi yake.
Kwanza, aliamini katika mizimu na kimyakimya akakiri kuwa mzimu wa babu yake ungali ndani yake.
Pili, Jose kazeze yawezekana aliweka kisasi cha kudumu, baada ya familia yake kunyanyaswa akaisambaza ile chuki kwa wajukuu na vitukuu kama wapo.
Hivyo yawezekana mmoja kati ya kitukuu ama mjukuu alikuwa akilishambulia jina la Nguzu popote atakapokutana nalo hivyo naye alikuwa ameshambuliwa.
Mambo haya mawili yakamwacha katika sintyofahamu nyingine mpya.
Akajaribu kulitaja jina la Inspekta Kobo...... akatazama kisa chake hadi kuja kumchomea ndani ya nyumba yake.
Hili akaliweka katika mabano, yawezekana kuna watu wengine walihusika katika hili jambo.
Akayakumbuka maneno ya yule kiongozi wa waliotumwa kumkamata Majenga.
Akakumbuka kuwa yule bwana ndiye aliyemueleza juu ya Inspekta Kobo kuwa yungali rumande akituhumiwa kwa kesi mbaya kabisa inayoweza kumtokomeza uraiani, lakini alimtajia jina la kiongozi wao mkuu ambaye hata wao hawakuwahi kumwona hapo kabla.
Zumbe!
Nguzu akafuatilia katika mitandao mbalimbali kutazama huyu mtu ni nani katika serikali ili ajue je? ana uhusiano na ukoo wa Kazeze? na kama hana uhusiano ni kitu gani anataka?
Kichwa kikamuuma alipojikuta anayo orodha kubwa sana katika kichwa chake.
Na kadri basi lilivyoikaribia ardhi ya jijini Dar es salaam,mara moyo wa Nguzu ukapiga kwa nguvu sana.
Kuna kitu alikuwa amekisahau kwa muda mrefu.
Koplo Zubeda!
Mungu wangu! Akahamanika kutokana na hali ile ambayo ilimtokea naye asijue ni kwanini imekuwa hivyo ghafla wakati analikaribia jiji na si wakati yupo mbali?
 
Mwanzo zilikuwa double double, mwendo kasi, sasa hivi ni speed ya Gari za makongo juu
Mwanzo Zilikuwa episode nyingi zimeshaandikwa.Ila sasa tumefika ile sehemu ambayo inaandikwa Leo na kuwekwa Leo Leo.
 
Daa

nimeipenda hataree..

nimeenda kwenye application ya hadithi kuitafuta sijaipata, naona hapa nitacheleweshwa ama kutomaliziwa kabisa.
 
Mwanzo Zilikuwa episode nyingi zimeshaandikwa.Ila sasa tumefika ile sehemu ambayo inaandikwa Leo na kuwekwa Leo Leo.
Jamani kama wewe sio mwandishi niambie unaitoa wapi niifate hukohuko
 
SEHEMU YA 16

MAJIRA YA saa saba usiku Martin Nguzu alikuwa akirandaranda katika kona mbalimbali za jiji la Dar es salaam kusaka hoteli ambayo angeweza kulala kama si kupumzika mpaka patakapokucha na kuutaza uelekeo ambao anapaswa kuanza nao.
Hakuwa na mashaka yoyote ya kuufichaficha uso wake, habari zake zilikuwa zimesambaa lakini si picha yake.
Wasambaze picha yake kwa cheo chake cha u-konstebo kwani hawana mambo mengine ya kuandika.
Alifanikiwa kupata hoteli ya bei ya wastani, akafanya malipo na kujiandikisha kwa jina batili.
Akakabidhiwa chumba.
Alipoingia na kuufunga mlango akaiwasha taa, akakiona kioo kikubwa jirani na mlango.
Akajitazama jinsi alivyokuwa, kimaumbile alijiona yungali vilevile lakini ndani ya mwili wake alijihisi yupo ngangali sana tofauti na awali.
Bila kutarajia akajikuta akimuwaza tena Zubeda.
Akiwa palepale mkabala na kioo alifikiria ule ukaribu wao jinsi ulivyokuwa ukimpa raha ya kipekee, raha iliyomfanya ajikute akimwonea wivu inspekta ambaye alisemekana kummiliki Zubeda, kuna kipindi alikuwa akitamani hata kumdhuru yule inspekta ambaye ndiye kikwazo pekee kilichokuwa kati yake na penzi la uhuru baina yake na Zubeda.
Nguzu alikuwa akitamani kumtambulisha Zubeda kwa marafiki zake kama shemeji yao, ukiachana na kuufurahisha moyo wake na pia kuuweka wazi udhibiti wake dhidi ya Zubeda, Sifa pia kilikuwa ni kigezo cha kutamani uhuru ule.
Nani ambaye angeacha kumsifia kuwa anamiliki 'mtoto mkali'
Zubeda alikuwa mzuri, urembo wake haukufichika hata alipojitundika katika gwanda zake za kazini.
Askari wengi walikiri kuwa binti huyu alikuwa wa aina yake, na hii ni sifa waliyoitoa huku akiwa katika gwanda zake.
Nguzu alikuwa amepata fursa ya kuziondoa zile gwanda kisha akamvesha kanga moja nyepesi mwanadada huyu na kisha kuambatana naye maliwatoni.
Macho yake mawili yenye nguvu yakifanikiwa kutazamana ana kwa ana na mzigo wa matiti ambayo yalikuwa yamevuka kidogo ule muda maarufu wa 'saa sita' lakini hayakuwa mbali sana kufananishwa na muda huo hasahasa yakipewa msaada mdogo wa sidiria.
Macho ya Zubeda yangeuamuru mwili wa mwanaume yeyote atakayemtilia maanani kujikuta ukisisimka na donge la hamu kumshika.
Macho yake makali angali akiwa kazini yalikuwa yanatepeta wakiwa wawili na Nguzu na kumfanya Nguzu ashangazwe na hali hii.
"Huyu mtu aliupata vipi ukoplo wa polisi? Kwa macho haya tepevu?" Haya ni baadhi ya maswali aliyojiuliza kabla hajachoshwa na mikono laini ya Zubeda. Mikono ambayo hakuamini hata kama inao uwezo wa kuzishika pingu na kumlazimisha mtuhumiwa azivae.
Ajabu Zubeda alisifika kwa kuwahenyesha watuhumiwa.
Kuhenyesha watuhumiwa??
Ilishangaza!
Lakini Nguzu naye akajikuta anahenya kupambana na msisimko uliokuwa ukimkumba kila mara mikono ile ilipomgusa.
Na hapo akakiri kuwa hata yeye ni mtuhumiwa pia na alikuwa anahenyeshwa wawapo chumbani wawili.
Kweli Zubeda ni kiboko!
Kumbukumbu hizi zikajirejesha nyuma kwa kasi ya ajabu, Nguzu akakumbuka jinsi alivyokutana na Zubeda jijini Mwanza.
Akaukumbuka utambulisho wake wa kijivuni dhidi ya Zubeda ambaye hakuwa na cheo chochote wakati ule na hata jeshini alikuwa hapajui.
"Naitwa Martin, Konstebo Martin Nguzu!"
Tabasamu likamponyoka na kujikuta akipiga saluti ya kihuni.
Akakiendea kitanda na kujirusha hapo kwa fujo zote.
Kitanda kikahimili kishindo!
Na hapo kikaanza kuufyonza ule uchovu wote na kuugeuza kuwa raha ya kipekee.
Usingizi ukampitia.....
_____
MAHAKAMA kuu ya Tanzania ilikuwa imesheheni haswa, maaskari walikuwa wanafanya kazi ya ziada kuwazuia watu waliozidi kumiminika pale mahakamani.
Punde ikasikika amri ya kumaanisha kuwa jaji na baraza zima la wazee lilikuwa linaingia pale mahakamani.
Kimya kikuu kikatanda ikiwa ni ishara ya kuheshimu mahakama.
Akiwa na pingu miguuni na mikononi kisha pingu hizo za miguu na mikono zikaunganishwa na mnyororo mgumu aliongozwa hadi katika kizimba.
Alipofikishwa kizimbani akafunguliwa zile pingu, akaingia akiwa huru kizimba kikafungwa.
Macho yake yaliyozama ndani na kuzidi kuonekana kuwa ni makubwa yaligeuka huku na kule, safari hii hakuwa na uoga tena alikuwa ameikubali hali halisi.
Macho yake yakatua katika kiti alichokuwa ameketi mama yake aliyepooza upande mmoja.
Licha ya kwamba alikuwa amelia sana hadi machozi kumkauka aliweza kuhisi machozi ya moyoni yakimlowanisha.
Wakagonganisha macho yao, akamwona mama yake akizungumza maneno yasiyoweza kusikika hata kidogo huku machozi yakimtoka kwa wingi.
Aliamini kuwa mama yake alikuwa akimwombea kwa Mungu ili kesi ile ipate muujiza wa yeye kushinda.
Uchungu uliomshika alitamani angepewa walau nafasi moja tu ya upendeleo naweze kuzungumza na mama yake, amkumbatie na kumfariji.
Jicho lile likaendelea kubarizi pale ndani ili aweze kuwaona watu wengine ambao huenda anawajua.
"Marafiki hawana maana!" Alijisemea baada ya kuhakikisha kuwa hakuna rafiki yake hata mmoja aliyefika mahakamani hapo.
"Kwa hiyo wameogopa kuwa nitawachoma ama?" alijiuliza.
Hakupata muda wa kujiuliza zaidi wakati jicho lake likitua katika kiti kingine upande wa kushoto.
Macho yakagongana tena na huyu mkaaji wa kiti hicho.
Zubeda!
Walitazamana kwa sekunde kadhaa kabla Martin Nguzu hajakwepesha macho yake.
Hakutaka kumwangalia binti huyu aliyekonda sana na kuonekana wazi alikuwa akitawaliwa na uchungu mkubwa.
Alipomaliza kuzungusha macho yake akamwona jaji akitoa ruhusa ya mwendesha mashtaka kumuuliza maswali mshtakiwa.
Maswali yalikuwa magumu sana, akayajibu kadri alivyoweza. Mengi alikuwa ameyasahau kabisa.
Miaka sita mahabusu bila kesi kusikilizwa, angekumbuka nini sasa.
Wakati wote huu alikuwa akishangaa kumwona wakili kwa ajili ya kumtetea.
"Lakini nilimkataza mama kuhangaika kuweka wakili." Martin Nguzu alijiuliza huku akitikisa kichwa chake kama namna ya kusikitika.
Akakiri kuwa katika ulimwengu huu mzazi ni mzazi lakini mama ni bora zaidi kuliko baba. Mama anaumia sana akimwona mwanaye katika wakati mgumu wakati baba huhesabu ugumu ule kama changamoto na kusema 'kijana wangu amekua na atatatua changamoto hizo' mama huinama chini na kusema 'mtoto wangu anateseka'
Ni hii tofauti aliikiri katika kesi yake hii. Mama mzazi aliyepooza mwili alikuwa mahakamani kushuhudia kile kiumbe alichokileta duniani baada ya suluba ya miezi tisa, kisha kuhangaika katika malezi.
Hakujali kupooza kwake, hakujali kuwa yawezekana mwanaye akahukumiwa kifungo cha maisha gerezani ama kunyongwa kabisa kwa jinsi kesi ilivyokuwa.
Alichokifuata pale ni kumwona mwanaye kwa jicho lake mwenyewe. Kama alivyomuona wakati amemzaa, alihitaji kumwona tena katika ugumu huu, ugumu wa kukondeana kwa sababu ya mateso na lishe duni, ugumu wa kuwaza kufia jela.
Mama alibaki kuwa shuhuda wa mwisho!
Ni nani kama mama kwani?
Wakili alisimama na kutema vifungu vya sheria ili kumnusuru Martin Nguzu kutoka katika janga lile.
Alionekana kuijua vyema sheria lakini upande wa mashtaka ulionekana kuwa imara zaidi, sura nyingi zilitawaliwa na hasira kali. Hasira hii iliboreshwa zaidi na mavazi yao, walifanania na kundi la mafia ambalo limemshukia mwenzao baada ya kuwasaliti na sasa wanataka kumpa adhabu ya kumzika huku akiwa hai akaupiganie uhai wake akiwa chini ya ardhi.
Nguzu akamgeukia jaji ambaye alionekana mwingi wa chuki kuliko haki.
Jaji alipounyanyua uso wake Nguzu akajikuta anagundua kitu kipya kabisa. Ile sura ya jaji haikuwa njgeni machoni mwake hata kidogo.
Hofu ikamjaa ya kutotendewa haki juu ya kesi ile ambayo alitambua wazi kuwa ni vile tu amekosa mashahidi lakini haikuwa ikimuhusu kabisa na alitakiwa kuwa mtu huru.
Jaji yule akaanza kusoma vipengele kimoja baada ya kingine kwa utulivu sana.
Ni kama aliyeelekea kutoa hukumu, hii ilimshangaza sana Martin.
Hukumu inatoka vipi kirejereja hivi bila kesi ile kupewa muda wa baraza la wazee kuipitia na kutoa mitazamo yao.
Jaji alisoma taratibu huku kila mahali akijaribu kumbana Nguzu.
Na hatimaye kauli ikamtoka.
"UTANYONGWA MPAKA UFE"
Mungu wangu! Nguzu akamwona mama yake mzazi akitua chini kama mzigo, watu wakakimbilia alipokuwa ili kumwokoa.
Palepale akawaona askari wanne wenye ghadhabu wakisogea katika kile kizimba na pingu kwa ajiri ya kumchukua na kumpeleka katika mahabusu ya mahakama kabla hawajampeleka gereza la Ukonga.
Gereza pekee ambalo washtakiwa waliohukumiwa kunyongwa mpaka wafe huhifadhiwa huko mpaka siku ya hukumu yao.
Kuwaona watu wale kukamchanganya Nguzu, na jaji alikuwa amefunga mjadala tayari.
Nguzu akaona haiwezekani, akawahi kujirusha akaidaka silaha ya askari mmoja na mara moja akaielekeza alipokuwa yule jaji.
Jaji akakodoa macho yake alipojikuta anatazama ana kwa ana na bunduki iliyoshikwa na mtu asiyekuwa na masihara hata chembe.
Akafyatua risasi kiufundi lakini yule jaji akawahi kujificha chini ya meza.
Na hapohapo Nguzu akaisikia sauti ya kike ikimpigia kelele kumtahadhalisha.
Ilikuwa sauti ya Zubeda!
Akageuka na kukuta amechelewa tayari, bunduki nyingine ilikuwa inaelekea kufyatuliwa ili yeye adhurike.
Ilielekezwa kifuani pake.
Akajikuta anapiga mayowe ya hofu huku akikiziba kifua chake kwa mikono yake.
Bunduki ikacheua.
"Mamaaaa nakufaaa!" alipiga kelele kubwa sana na hapo akajikuta akibiringita kama chaguo lake la mwisho.
Akashangaa kujikuta anaelea hewani. Akaanza kutapatapa akirusha miguu huku na kule.
Hatimaye akasimama wima tena.
Hakuwa mahakamani! alikuwa amesimama katika kitanda huku akiwa amejifumbata mikono yake katika kifua chake.
Ndoto!
Jasho lilikuwa linamwagika vibaya mno, bado moyo ulikuwa unapiga kama unaotaka kutoka nje ya kifua chake.
Alikuja kutulia baada ya dakika kumi na hapo ndipo akakiri kuwa ile ilikuwa ni ndoto lakini ndoto ya ajabu sana.
"Yule jaji yule! Yule jaji ni nani!? Jaji, jaji...." Nguzu alibaki kusema kama ambaye anajaribu kulazimisha kung'amua vitu kutoka katika ile ndoto ya ajabu ambayo hakutaka kuamini eti ilikuwa ndoto ya kawaida.
Alihisi yule ni babu yake anasema naye. Hofu ikatanda alipokumbuka kuwa alihukumiwa kunyongwa katika ndoto yake.
Hofu ya kifo ikamjaa, akaanza kuhofia uwepo wake katika jiji la Dar es salaam.
Jiji ambalo ipo ile mahakama ya ndotoni na pia lile gereza wanalohifadhiwa wafungwa wa adhabu ya kunyongwa mpaka kufa.
Hiki nini? alijiuliza.
Bado hofu iliishi naye, akamkumbuka mama yake alivyokuwa akimlilia na hata alivyoanguka baada ya hukumu ile kutolewa.
Hofu ya kifo ikiwa haijaisha ikapanda hofu nyingine.
Hofu ya kumpoteza mama yake mzazi pindi atakaposhuhudia matatizo yakimpata.
Nguzu akakiri kuwa huu mpambano ulikuwa maji ya shingo kwake naye alikuwa hajui kuogelea vyema. Akaamini kuwa alikuwa anahitaji watu watakaosimama pamoja naye.
Kwa mara nyingine tena jina Zubeda likakiandama kichwa chake.
"Kwanini Zubeda?" alijikuta katika swali hili.
Hisia mbili zikaanza kupambana, mojawapo ilikuwa hisia za mapenzi. Nguzu akakiri kuwa alikuwa akihangaishwa na jina Zubeda kwa sababu tu aliwahi kumpa burudani ambayo ilikatishwa ghafla bila kufika ukingoni.
Pili alihisi kuwa anahitaji kupata msaidizi na msaidizi wa kweli katika vita hii ni koplo Zubeda.
Kujua hisia ipi ni ya kweli nd'o ukawa mtihani mzito.
"Ngoswe penzi kitovu cha uzembe" Usingizi ulimkuta Nguzu akiwa katika uchambuzi hafifu wa kitabu hiki maarufu , alianza kwa kumpa kongole mwandishi Edwin Semzaba kwa kuandika kitabu hiki, kisha akahamia kwa Ngoswe na Mazoea na hadi anasinzia alikuwa amefikia mahali ambapo Mazoea ameanza kuzoeana na Ngoswe! Hii ni baada ya Ngoswe kumuhadaa kuwa atamtorosha waende wote mjini......
Alisinzia akiwa anatabasamu, bila shaka ni vile visa vya Ngoswe vilimpa tabasamu.
 
Hongera sana kaka yani we hukoseagi yani daaa tuna subiri mwendelezo bonge moja la RIWAYA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom