HII HAPA SEHEMU YA 15
ILIKUWA safari iliyojaa katika kichwa chake ghafla baada ya vita ile ya usiku iliyoondoka na uhai wa watu watatu ambapo mmoja kati yao alikuwa ni kiongozi wao kwa mujibu wa maelezo yao.
Martin Nguzu ambaye sasa hakuwa akiushangaa uwezo wake wa kukabiliana na maadui alikuwa amewaangusha wengine watatu huku akifanikiwa kuwapokonya bunduki tatu pamoja na risasi za kutosha kabisa.
Hakutaka kulala baada ya kuhakikisha ameitelekeza ile miili mbali na ngome ya mzee Majenga. Alimwamsha mzee Majenga na kumweleza kwa ufupi juu ya kilichotokea.
Tofauti na matarajio yake kuwa taarifa ile itamtisha sana Majenga, hii ilikuwa kinyume. Mzee Majenga akatokwa na kicheko kidogo kisha akampigapiga kifuani Martin Nguzu na kumwita kwa jina la babu yake.
"Ngengekuzenza Nguzu umezaliwa upya..." Kauli ile ilimtoka na kumwacha Martin Nguzu katika pumbazo asielewe ni kitu gani bwana yule alimaanisha.
"Mimi nimezeeka kijana wangu, niliisubiri sana hii vita kwa muda mrefu lakini imekuja nikiwa mzee tayari. Nenda ukapambane hii ni vita yako na inakuhusu. Nakuachia haya maandishi niliyoyaandika bila kuongeza wala kupunguza neno kutoka katika kinywa cha hayati babu yako anayeishi sasa katika nafsi yako. Hakikisha unayamaliza yote kabla haujaivaa hiyo vita...... mimi nitakuwa salama kabisa na tutakutana nikiwa hai, na hata nikifariki ni kwa sababu ya uzee tu..." Aliongea kwa ujasiri mkuu. Kisha akachechemea hadi ndani na kuchukua makaratasi yaliyoandikwa kwa kalamu akamkabidhi Martin.
"Nilikuwa napenda sana kuandika na babu yako alikuwa anapenda sana kunisimulia, nadhani ni maneno hayo kwa ufupi yatakupa jawabu nilikutana vipi na babu yako." Majenga alitoa kauli ile na Martin akaipokea lakini alikuwa na swali la ziada.
"Niliokoka vipi katika ule moto jijini Dar es salaam?"
"Mzee wako asingeweza kukuacha uangamie. Wazee wa zamani hawakuwa wa kawaida, akinuia jambo linakuwa kama lilivyo, nadhani ni kutokana na kutenda dhambi chache nd'o maana Mungu alikuwa akiwasikiliza." Alifafanua na kuzidi kumvuruga Martin.
Akagundua mvurugano ule, akaongezea "Kasome haya yote kabla hujaamua wapi pa kuanzia"
Maongezi yakaishia hapo.
MAANDISHI YA NGENGEKUZENZA.
Ubaya ni kwamba wakati wa ukoloni, sisi watu wa rangi nyeusi hatukuishia tu kunyanyaswa na ngozi nyeupe katika uhai wetu, hata ulipokuja ustaarabu wa kuhifadhi maiti zetu sisi tuliwekwa katika kundi la mbwa koko aliyefia jaani baada ya kukabwa na mfupa aliodhani ni mnofu.
Ukipata bahati sana unafukiwa, ila ni waafrika wachache waliokuwa na bahati, wengi tulitunukiwa nuksi.
Ukiwa na nuksi unaachwa hapohapo ulipofia ama unasogezwa kidogo porini, ukawe chakula kwa wanyama wenye tabia ya uvivu katika suala la kuwinda na ndege wanaoona sifa kudonoa donoa.
Hata babu yangu alikuwa na nuksi vilevile baada ya kufariki alitupwa, akaipata bahati akiwa maiti tayari waafrika kadhaa wakamfukia.
Baada ya kuupata uhuru wetu nikawa naitembelea ile sehemu niliyoaminishwa kuwa babu yangu alifukiwa pale, pakawekwa alama nami nikawa naenda kumsalimia na kuzungumza naye bila kujali ananisikia ama la!
Sasa yule mwanahizaya baada ya kuona haitoshi kumchukua kiharamia mke wangu na kuniacha katika jitimai, akaona hata! hii haitoshi huyu bwege bado anapata raha. Akaanza kuniandama kivingine, najua aliwatuma mashushu wake waliokiamini na kukiabudu chama chao kuliko Mungu wa mbinguni na miungu ya porini.
Hawa wakamfikishia habari kuwa ninayo furaha nyingine, furaha ya kuzungumza na babu yangu makaburini.
Ikapita ajenda katika siku nisiyoijua na baadaye ikawa ni amri bila kutahadhalishwa.
Eneo lile lilipaswa kupandwa miti, mara lilitakiwa kupita barabara.
Sikuelewa hata kidogo, na hakuna aliyesubiri nielewe.
Kwani Ngengekuzenza nani mpaka aelewe?
Lile nililoamini kuwa ni kaburi likavunjwa na huyu mkoloni mshenzi mwenye rangi kama yangu huku akiiga miondoko ya wazungu na afro yake kichwani akiipaka kalikiti na kuwa laini kama nywele za mkoloni.
Lugha yake pia ilifanana na yao.
Poor Joseph Kazeze!
Kama ni kunipiga, hapa alinipiga na mjeledi wa chuma nikaangukia pua huku mikono yangu ikishika makaa ya moto.
Huyu mjinga aliniweza hakika!
Uchungu wangu ule nikamshirikisha mwanangu Salama nikamweleza kuwa Jose anataka kuvuka mipaka ambayo ameivuka tayari, yaani sielewi anachotaka.
Salama alinisihi niachane naye, nikaona hajui uchungu ninaoupitia kwa kupokonywa mke na kisha hapohapo nikapokonywa furaha yangu.
Babu yangu!
"Salama, nikiachana naye akagundua nina furaha kuwa na wewe atakuchukua na wewe pia...." nilimwambia Salama. Wazo hili likamkuna na kuiona hatari ya waziwazi.
"Sasa utamfanya nini?"
"Yule ni mjinga tu kwangu, nataka nimfanyie yale mambo ambayo wajanja huwafanyia wajinga wanaodhani pesa nd'o ujanja." nilimweleza huku nikiona wazi kuwa hanielewi.
"Unataka upigane naye?" aliniuliza.
"Nikipigana naye wote tutakuwa levo ileile ya ujinga, nataka nimpige ili tuunde daraja katika ya nani mjinga na nani mjanja."
"Lakini baba, huyu ana pesa na cheo atakusumbua sana. Yaani nina uhakika hautafikia hata nusu ya azma yako."
"Kwanini unasema una uhakika." nilimuuliza salama.
"Si kila kitu kipo wazi, ana pesa na vyeo."
"Sikiliza mwanangu Salama na uliweke hili milele katika maisha yako, hapa duniani kuna kitu kimoja tu nd'o cha uhakika vingine vyote si vya uhakika. KIFO pekee ndo jambo la uhakika, kila mtu atakufa hii haina mjadala. Ujiue, unyweshwe sumu, ugongwe na gari ama hata ukilala usiamke. Vyote vina maana moja tu ya uhakika.... asije akakudanganya mtu kuwa jambo hili ni uhakika... anakulaghai nawewe unayemsikiliza na kumkubalia unakuwa upande wa mjinga. Sipendi uwe mjinga siku moja...." Nilimsomea mambo yale. Yakamuingia na kumpa ujasiri naye akanibariki katika uamuzi wangu na hiyo ilikuwa ni mnamo mwaka elfu tisa mia themanini na tatu ama nne kama sijasahau.
Sijui itakuwaje miaka ya huko mbele lakini enzi zetu hizi hapakuwa na ulinzi wa kutosha kwa viongozi, ulinzi huo tuliusikia tu na kuuona walipokuja viongozi kutoa nje, Mwalimu Julius Nyerere alihamasisha sera za kuishi kijamaa, nasi tukaamua kuishi kama ndugu.
Hapakuwa na wa kumpinga kirahisi mwalimu. Ukitaka kumpinga sisi tunakwambia nenda ukapambane kuileta Tanganyika huru ndipo ujilinganishe na mtaalamu huyu.
Hivyo tuliishi kijamaa sana, halikuwa jambo la ajabu kukutana na mwalimu Nyerere barabarani. Sasa vipi kuhusu mjinga huyu anayeitwa Joseph Kazeze?
Sidhani kama kwa miaka yenu huko mbeleni itakuwa hivi. Nahisi hata balozi naye atatafuta ulinzi...
Nilikueleza awali kuwa tangu nilipokuwa mtoto nilikuwa nina uwezo mkubwa sana darasani, hata akili yangu haikuwa ndogo katika kufikiri.
Nikaamua kuitumia akili yangu kumwonyesha yule bwana nini maana ya mwanaume kutoa machozi.
Kwakweli nilimkosesha amani!
Kwanza nilifurahia kile kitendo cha mwalimu Nyerere kutowafukuza wazungu baada ya kutupatia uhuru, hivyo upatikanaji wa silaha hadi miaka ya themanini bado ulikuwa ni mwepesi sana, unaweza kuipata bunduki hata kwa kubadilishana na gunia la mahindi pekee.
Zilikuwa zimezagaa.
Nami nikajipatia bunduki yangu, uzuri nilipitia jeshini hivyo sikuhitaji kufundishwa lolote.
Nikamuaga mwanangu kuwa naanzisha mapambano rasmi.
Sikuwahi kuua ila nilijeruhi sana.
Nilianza na baba yake mzazi, akiwa katika mizunguko yake. Nikamteka na kumpiga kipigo cha mbwa mwizi, akavunjika mkono.
Sikumtumia salamu Jose Kazeze kama ni mimi ili aendelee kuhadaika.
Akafuata mdogo wake, huyu nilimfungia safari hadi Morogoro, nikamkamata na kumfunza adabu asiweze hata kuiona sura yangu.
Jose Kazeze kitu alichosahau ni kwamba sisi tulikuwa marafiki na nilimfahamu vyema yeye na familia yake.
Niliendelea kumpa presha bwana yule kwa kufikia hatua ya kuvamia kwake nikarusha risasi zikavunja vioo vya nyumba aliyokuwa akiishi lakini sikumdhuru mtu na sikutaka kumdhuru.
Uwezo wangu katika kupanga matukio ulianza kunishangaza hata mimi, kila nikilala na kuamka nawaza pigo jingine.
Jose akaanza kukonda!
Mara akaachana na yule mwanamke aliyenipokonya.
Nami sikurudiana naye mjinga yule aliyekosa hata nukta ya akili.
Nilikuwa nina hasira kali.
Baadaye baba yake alifariki, kwa magonjwa mengine sijui kama na kile kipigo kilichangia.
Siku mbili baada ya kuzikwa nikaenda makaburini, huku nikaweka bomu nililolipata kwa bei nzuri tu.
Likafanya mlipuko uliotikisa nchi.
Hakuna kilichobaki zaidi ya jeneza kusambaratika huku na kule.
Hili lilikuwa pigo kubwa zaidi, wanandugu wakalundikana nyumbani kwa Jose Kazeze kujadiliana nini kinaendelea.
Nikavamia na huko na kurusha bomu jingine katika choo kilichokuwa mbali kidogo na nyumba na hii ni baada ya kuhakikisha hapakuwa na mtu ndani yake.
Mparangano uliojitokeza nilijikuta nacheka mwenyewe.
Amakweli mtenda akitendwa....
Jose akazidi kuzorota kiafya.
Ni hapa ndipo nikaamua kumweleza bayana ili kama ni kufa kwa mshtuko afe tu, who cares?
Hakufa!
Ila alipagawa vibaya mno, na hapo ndipo ikaanzishwa oparesheni ya Ngengekuzenza Nguzu anasakwa auwawe.
Kisa ni jambazi, yakaundwa matukio ya kushangaza kunihusu mimi na hapo nikaanza kusakwa rasmi.
Nilijua kuwa hali ni mbaya, nikaraejea kwa mwanangu... usiku wa mwisho kumwona mwanangu.
Akanieleza kuwa yu mjamzito, nikamweleza kuhusu kinachoandikwa na magazeti ya serikali huku nikimweleza kuwa moyo wangu u radhi kuwa nimemuweza yule bwana.
Zaidi ya hayo nikamsihi kuwa iwapo atazaa mtoto wa kiume basi amwite Nguzu!
Tulikumbatiana huku sote tukishindwa kuyazuia machozi.
Nikaondoka na kuja kwako Majenga unihifadhi nikusimulie ya kuandika kama ulivyohitaji wewe kijana wangu.
Na nimejitahidi sana kukusimulia.
Maandishi yale yaliacha nafasi kubwa kisha ikafuata aya ambayo mwandishi wake alikuwa ni Majenga.
Mnamo mwaka 1988 mwezi wa kumi na moja mzee Ngengekuzenza mwenye msongo wa mawazo kwa kuishi maisha ya mashaka kila kukicha aliniaga kuwa anakwenda msalani, ilikuwa majira ya usiku. Hakurejea mapema nikalazimika kutoka pamoja na mbwa kwenda kumtafuta.
Nilimtafuta sana hadi pambazuko likanikuta nikiwa namtafuta, mbwa asiyechoka ndiye alinihimiza kumdaka mzee wangu nimpendaye.
Hatimaye nikaufikia mti ambao alikuwa amejitia kitanzi.
Nasikitika kuwa sikuwahi kukiri kuwa ninamfahamu mzee yule kwa sababu za kiusalama, alikuwa anasakwa sana na jeshi la polisi kama jambazi sugu.
Niliporejea ndani nikakutana na karatasi katika kitanda alichokuwa akilalia. Haikuwa na maneno mengi sana aliniandikia kama nilivyokuwa nimefanya tayari.
"Umenihifadhi kwa moyo wote wa upendo, wewe ni kijana wangu nikupendaye. Ninaomba uendelee kunitunzia maneno yangu..... utawapatia wajukuu zangu ili wajifunze kuwa babu yao hakuwahi kuwa mtu dhaifu hata kama nilionewa, babu yao sikuwahi kuwa jambazi hata kama watayaona maandishi hayo, pia kwa imani yangu kuu naamini kuwa sijafa kirahisi rahisi. Mizimu ya mababu zangu waliouwawa kifedhuli utumwani imeniambia kuwa najipumzisha ila ipo siku nitazaliwa na nitazaliwa katika damu yangu mwenyewe. Ninapumzika Majenga ila nikizaliwa tena usishangae. Naamini mizimu hii kulikoni dini walizotuletea wakoloni, dini zilizotuongopea kuwa Mungu ni mzungu, zikaenda mbali na kusema kuwa Mungu anaishi katika majengo yao waliyoyajenga.
Dini za kishenzi zilizonipatia jina la kishenzi, Frolian na kunipokonya jina la kishujaa kutoka kwa babu yangu.
Dini zilizotulaghai kuwa kila asemacho yule mzee mweupe anayesimama mbele yetu basi ni sawa, anatuona tunateseka na anasema tumwachie Mungu, nasi tukijaribu kupambana anasema tena sisi ni watu wabaya sana na hatufai kuwekwa kundi la wanadamu.
Dini zao hazijaniambia kuwa siku moja nitarejea, lakini wazee wangu ambao tuliwalilia njaa wakatusikia katika miti, tuliwaomba kila kitu na walikuwa wakweli.
Wazee hawahawa wamesema nami, acha nipumzike ila ipo siku nitarejea na sitakuwa wa kujificha tena.
Kwaheri mjukuu wangu!"
Kisha akwakeka hitimisho Majenga kwa wino mzito.
"MNAMO MWAKA 1988 BABU YETU Ngengekuzenza aliaga dunia na ni mwaka huohuo mwanaye Salama alipata kujifungua... yule mtoto akaitwa NGUZU"
______
NGUZU alibaini kuwa alikuwa anatetemeka baada ya kuimaliza sentensi ile ya mwisho.
Akaituliza akili yake na kutaka kumaizi ni kitu gani kimempa majibu katika maandishi yake.
Kwanza, aliamini katika mizimu na kimyakimya akakiri kuwa mzimu wa babu yake ungali ndani yake.
Pili, Jose kazeze yawezekana aliweka kisasi cha kudumu, baada ya familia yake kunyanyaswa akaisambaza ile chuki kwa wajukuu na vitukuu kama wapo.
Hivyo yawezekana mmoja kati ya kitukuu ama mjukuu alikuwa akilishambulia jina la Nguzu popote atakapokutana nalo hivyo naye alikuwa ameshambuliwa.
Mambo haya mawili yakamwacha katika sintyofahamu nyingine mpya.
Akajaribu kulitaja jina la Inspekta Kobo...... akatazama kisa chake hadi kuja kumchomea ndani ya nyumba yake.
Hili akaliweka katika mabano, yawezekana kuna watu wengine walihusika katika hili jambo.
Akayakumbuka maneno ya yule kiongozi wa waliotumwa kumkamata Majenga.
Akakumbuka kuwa yule bwana ndiye aliyemueleza juu ya Inspekta Kobo kuwa yungali rumande akituhumiwa kwa kesi mbaya kabisa inayoweza kumtokomeza uraiani, lakini alimtajia jina la kiongozi wao mkuu ambaye hata wao hawakuwahi kumwona hapo kabla.
Zumbe!
Nguzu akafuatilia katika mitandao mbalimbali kutazama huyu mtu ni nani katika serikali ili ajue je? ana uhusiano na ukoo wa Kazeze? na kama hana uhusiano ni kitu gani anataka?
Kichwa kikamuuma alipojikuta anayo orodha kubwa sana katika kichwa chake.
Na kadri basi lilivyoikaribia ardhi ya jijini Dar es salaam,mara moyo wa Nguzu ukapiga kwa nguvu sana.
Kuna kitu alikuwa amekisahau kwa muda mrefu.
Koplo Zubeda!
Mungu wangu! Akahamanika kutokana na hali ile ambayo ilimtokea naye asijue ni kwanini imekuwa hivyo ghafla wakati analikaribia jiji na si wakati yupo mbali?