Wote tulitazamana. Macho yangu yalikutana na yale ya Byabato ambayo yalinitazama kwa namna ya kunisuta na kunidhihaki. Macho yaliyokuwa yakisema, “Unajua kuwa najua kuwa ni yako!”
ENDELEAAAAA...
“Nitauliza kwa mara ya tatu,” Padri aliendelea. “Nani kati yenu aliyedondosha hirizi hii jana?”
Macho ya Byabato yalikuwa yameganda juu ya macho yangu, yakinicheka. Sikuweza kustahimili zaidi. Niliinua mkono wangu juu na kisha kusimama huku nikijibu taratibu, “Ni yangu, Padri.”
Si Padri wala wanafunzi wenzangu walioamini masikio yao. Kwa darasa langu, kwa shule nzima na hata jamii nzima ya eneo hilo mimi nilikuwa mfano bora zaidi kimasomo na kikanisa. Nilikuwa hata nikiwasaidia mashemasi katika huduma ndogo ndogo za kanisa.
“Ni yako?” Padri aliniuliza tena, kana kwamba alitaka nibadili kauli na kuikana hirizi yangu. Sikuwa tayari kwa hilo.
“Unajua kuwa mwili wako ni hekalu la Mungu? Aliniuliza Padri.
“Najua!”
“Kwa nini basi unavaa uchafu? Kwa nini unahifadhi dhambi na kuishi nayo? Hutaki kuingia katika ufalme wa Mungu?”
Sikumjibu.
“Sio neno,” Padri aliendelea. “Leo Bwana amefanya muujiza kwa ajili yako. Ameifichua hirizi hii chafu, ambayo umeivaa kwa muda mrefu, ili ujitakase upya. Tutawasha moto hapo nje, utaichoma hirizi hii kwa mkono wako mwenyewe. Kisha tutakuombea na kukubariki kwa kitendo hicho cha kuachana na upagani milele.”
Tulitolewa nje. Zikaletwa kuni, moto ukawashwa. Huku wenzangu wakiimba pambio mbalimbali, mimi na Padri Backhove tulisimama mbele ya kadamnasi hiyo, mikononi mwake akiwa na Biblia na hirizi yangu.
“Wakati nikianza kusali, ichukue hirizi hii uitupe ndani ya moto ukitamka maneno yafuatayo ‘Shetani nakuteketeza sasa na milele, kwa jina la Yesu’ Umeelewa?”
Niliitikia kwa kichwa.
Nyimbo zilipamba moto. Sauti ya Padri akisoma sala ilisikika waziwazi. Lakini mkono wangu uliokuwa na hirizi uliishiwa nguvu huku nikitetemeka mwili mzima. Niliishikilia kwa zaidi ya dakika mbili, nikiining’iniza juu ya miale murua ya moto huo lakini vidole vyangu vilielekea kunigomea. Hisia zangu zilikwenda mbali sana toka hapo. Zilisafiri hadi usiku ule tulipoagana na babu uchochoroni. Masikio yangu yalisafiri pia. Yalikuwa pamoja nami huko uchochoroni, gizani, yakimsikia babu akisema;
Hii ni hirizi ya bahati. Ilinde nayo itakulinda maishani mwako. Sauti hiyo ilikuwa wazi wazi kabisa masikioni mwangu.
“Ichome!” Padri alikatiza sala na kuniambia kwa ukali.
“Siwezi!” Nilimjibu.
“Huwezi nini?” aliniuliza kwa mshangao. “Tupa uchafu huo ndani ya moto!” nilishindwa kabisa kuviamini vidole vyangu kufanya hivyo. Mara nikageuka na kuanza kuondoka. Padri hakuyaamini macho yake. Akanifuata na kujaribu kunishika. Nikamsukuma.
Padri Backhove alikuwa mtu mnene na mzito sana. Lakini hakuwa na nguvu nyingi. Nilimsukuma kidogo tu, lakini akaanguka chali, kama gunia. Sehemu ya kanzu yake ndefu, iliyofika miguuni iliangukia ndani ya moto huo na kuanza kuungua.
“Nakufa!” Padri alipiga kelele akijiviringisha huku na kule katika jitihada za kujizoa ainuke toka mavumbini hapo.
Nilishikwa na hofu kubwa. Wakati wenzangu wakihangaika kuzima moto katika mwili wa padri, wengine wakijaribu kuinua mwili wake wenye zaidi ya kilo mia na sitini mimi nilianza kukimbia kwa nguvu zangu zote huku nikihisi sauti za watu wanaonifuata wakizomea nyuma yangu. Sikugeuka wala kusimama hadi nilipofika vichakani, mbali sana, ambako niliamini mtu yeyote asiye na uwezo wa kukimbia kama mimi na ujuzi wa mambo ya porini kama mimi, asingeweza kunipata.
* * *
Nilijipumzisha kwa muda chini ya kivuli cha mti aina ya mvule, ulioonekana kupevuka sana. Nikaketi na kuegemea shina lake huku nikiitumia akili yangu kutafakari mustakabali wa maisha yangu baada ya tukio lile. Moyo wangu ulijaa kiza, hofu kubwa ikiwa imetanda katika nafsi yangu kwa kufikiria tu uzito wa mkasa ule.
Sikuwa na hakika kama padre Backhove alikuwa hai au la kwa moto na mweleka ule. Hata hivyo, hakika niliyokuwa nayo ni kwamba alikuwa ameathirika sana kimwili na kisaikolojia. Kwa vyovyote vile kama angenitia mkononi adhabu ambayo ningeipata isingekuwa kifani. Wazo ambalo lilinifanya nisahau kabisa ndoto ya kurudi shuleni pale na kuomba msamaha.
Zaidi ya hayo, hata kama ningerudi na kusamehewa ningeishi maisha gani shuleni pale bila kuwa kituko na kichekesho kwa kila mtu kwa miaka nenda miaka rudi? Sikuwa radhi kwa hilo.
Halafu, hata kama ungetokea muujiza nirejee shule na yote mengine yasahauliwe, jambo moja tu lisingeweza kusahauliwa kamwe. Hirizi. Kwa vyovyote vile msamaha wangu na kutakasika kwangu kungeendana na kuiteketeza hirizi ile hadharani, hirizi ambayo ni urithi wangu pekee! Kiungo cha mwisho kati yangu na familia yangu!
Mara nikaikumbuka hirizi hiyo! Iko wapi? Nilijiuliza nikitia mkono wangu mfukoni kuitafuta. Haikuwemo. Nilikagua mifuko yangu yote na kujipapasa mwili mzima, wapi. Hirizi yangu ilikuwa imepotea, bila shaka katika zile purukushani za kukimbia!
Nilihisi nikiishiwa nguvu. Kwa muda nilipoteza mapigo kadhaa ya moyo, huku macho yakiingia kiza. Hirizi yangu ambayo ilikuwa kila kitu maishani mwangu. Hirizi ambayo ilisababisha nipoteze kila kitu maishani mwangu!
Imepotea!
Wanasema binadamu katika uhai wake, anaweza kufa kidogo! Kama madai hayo ni ya kweli basi mimi Petro Kionambali, siku hiyo, chini ya mti ule wa mvule nilikufa kidogo.
Na hata pale uhai uliponirejea sikuwa mtu yuleyule tena. Sikuwa na pa kwenda. Nisingeweza kurudi Kashozi kwa mzee Buberwa na kumsimulia kuwa nimeshindwa shule kwa ajili ya hirizi. Kadhalika, nisingeweza kurudi kwetu Buha na kumwambia babu na wazazi wangu kuwa nimeacha shule kwa ajili ya hirizi ambayo haipo tena. Shule nako kusingeendeka.
Iko wapi hirizi tuichome? Ningeulizwa kabla ya mengine yote.
Imepotea! Lingekuwa jibu langu. Nani ambaye angeniamini? Zaidi nani ambaye angenithamini? Haikuwepo namna.
Ghafla nikajiona yatima. Hapana, nilikuwa mwana mpotevu, asiye na mbele wala nyuma.
Nikainuka na kujitazama. Tayari nilikuwa kijana mrefu kuliko watu wote katika familia yangu. Nilikuwa mwembamba lakini mkakamavu. Mikono yangu ilikuwa na nguvu, miguu yangu ikiwa na uwezo. Zaidi ya kaptula, shati na viatu nilivyovaa sikuwa na chochote mkononi wala mfukoni mwangu. Nilikuwa masikini. Lakini nilijiamini. Afya yangu, elimu yangu na ari yangu vilifanya niamue jambo moja; sirudi kwetu wala sirudi shule. Nitapiga mguu, kutafuta maisha upya. Hata kama nitafika mwisho wa dunia!
* * *
Nilipiga mguu kuelekea Kanazi. Nilifika usiku sana. Kwa kuhofia kuwa habari zangu zilishafika hapo nililala porini, juu ya mti. Alfajiri nilianza tena safari. Kiguu na njia hadi Muhutwe. Hapo niliomba hifadhi kwa wavuvi waliokuwa wamejenga vibanda vyao pwani. Hawakuwa na hiyana, ingawa mavazi ya shule niliyoyavaa yalifanya wanishuku kuwa nimetoroka shule. Sikukosa uwongo wa kuwaambia hata mashaka juu yangu yakaisha.
Katika elimu yangu fupi shuleni nilikuwa nimepata ufahamu wa kutosha wa Jiografia. Baada ya kughairi kurudi kwetu au kwenda kwa mzee Buberwa niliamua kwenda nchi ya Wasukuma. Mengi yalikuwa yakizungumzwa juu ya nchi hiyo ambayo nilitamani kuyaona kwa macho.
Zilikuwepo hadithi za Msukuma aliyeitwa Ng’wanamalundi ambaye alisemekana kuwa mganga aliyewashinda wachawi wote kwa kutumia ngoma zake. Mtu huyo wa miujiza alisemekana pia kuwa alikuwa na macho yenye nguvu za ajabu, ambayo yaliweza kukausha miti na hata binadamu aliowakazia macho, jambo lililopelekea awe akitembea huku akiwa amejifunga kitambaa usoni kufunika macho yake. Mtu huyo alidaiwa kuwa katika moja ya hafla zake alipata kukausha msitu mkubwa na mamia ya watu waliokuwa mbele yake. Jambo hilo liliifanya serikali ya mkoloni imkamate na kumhukumu kunyongwa. Lakini hakuna aliyethubutu, kwani kabla ya hukumu hiyo kutekelezwa alifungwa katika kimojawapo cha visiwa vidogovidogo vilivyo baharini katika pwani ya Bahari ya Hindi, huko Dar es Salaam. Hata hivyo, ilielezwa kuwa Ng’wanamalundi huyo kila jioni alionekana katika vilabu vya pombe Dar es Salaam akiwa amevuka bahari kwa kutembea juu ya maji. Wakoloni wakalazimika kumwachia.
Sifa nyingine ya nchi ya Wasukuma ni zile hadithi kuwa kulikuwa na milima ya mawe, ama majini ama nchi kavu. Baadhi ya milima hiyo ilielezewa kuwa ilikuwa katika maumbile ya binadamu, ikiwa imesimama miaka nenda rudi kama inayosubiri mwujiza fulani utokee, ili ipate uhai na kuanza kutembea kama binadamu wengine.
Nchi hiyo pia ilikuwa ikisifiwa sana kwa ukubwa wa ardhi na wingi wa rutuba yake. Kilimo cha mazao ya chakula na yale ya biashara kama pamba na katani kilielezewa kuwa hakikupata kumtupa mtu. Kwa bahati mbaya, mimi sikupata kuwa mkulima wa haja. Wala sikuona kama ningeweza kuwa na ustahimilivu wa kulima leo kusubiri mavuno miezi au miaka kadhaa baadaye. Mimi nilikuwa mtu wa maji. Mtu wa kutupa nyavu na kuzitupa huku tayari zimejaa samaki! Hivyo, sababu kubwa iliyonipa msukumo wa kutamani kufika huko hasa lilikuwa ziwa. Jiografia yangu ilionyesha kuwa Wahaya na Wasukuma walichangia ziwa hili. Wakati Wahaya wakiwa Magharibi wakilitumia kwa shughuli zilezile.
Kwa kuzingatia hali yangu ya kutokuwa na kazi wala ujuzi wowote wa kuweza kupata ajira nyingine nililichukulia ziwa hili kuwa mkombozi wangu pekee. Nilitegemea ziwa liniajiri, linilee, kwani taaluma ya uvuvi niliyoipata katika likizo zangu ilitosha kabisa kunipatia ajira hiyo.
Ni kwa mtazamo huo ndipo nilipojikuta nikijiunga na vikundi mbalimbali vya uvuvi kwa lengo la kujipatia fedha. Siku zote za uvuvi wangu nilifuata ziwa kuelekea upande wa kushoto kwangu badala ya upande wa kulia. Kama ningeelekea kushoto, ningelazimika kufika Uganda na baadaye Kenya, kabla ya kuingia Tarime, Musoma, Bunda hadi kufika Mwanza. Ingekuwa safari ndefu isiyo na sababu yoyote.
Mimi nilielekea kulia. Nilivua katika pwani na visiwa mbalimbali kama Bambire, Iroba, Rubondo na Nyamiende. Ilikuwa safari ndefu na ngumu sana. Takribani mwaka mzima uliishia njiani. Ama nilikwamishwa na ukosefu wa majahazi yanayoelekea huko nilikokuwa nikielekea, ama upepo mkali wa siku kadhaa ziwani ulifunga kabisa njia. Msimu wa masika ulioambatana na mvua kubwa za radi na mingurumo ya kutisha ni miongoni mwa sababu nyingine iliyonichelewesha njiani. Nililazimika kusubiri kwa zaidi ya miezi minne katika kijiji fulani huko Biharamulo.
Urefu huo wa safari ulikuwa na faida moja. Kwanza, ulinipa fursa ya kupata ukomavu na uvumilivu mkubwa katika pilikapilika za ziwani na nchi kavu. Ningeweza kuvumilia mvua ya siku mbili au tatu ikinipiga mwilini, niliweza kustahimili jua kali linalochoma kama mkaa wa moto. Niliweza pia kuipuuza njaa kwa muda mrefu. Zaidi, mwili wangu ulijenga uwezo mkubwa wa kuyashinda maradhi madogomadogo kama homa au tumbo bila haja ya kutumia dawa za madukani au mitishamba tele niliyopata kuelekezwa na babu.
Faida nyingine kubwa niliyoipata kutokana na urefu wa safari hiyo ilikuwa udugu. Nilikutana na watu mbalimbali, nikashirikiana nao kwa hili na lile na kujikuta nimepata ndugu na marafiki tele, ambao kila nilipoondoka kuendelea na safari yangu walisikitika sana, lakini haikuwa kabla ya kunitakia kheri na baraka za safari.
Nilikosa raha kiasi pale tulipofika kisiwa cha Kome tukikaribia kabisa Mwanza. Rafiki zangu hao walishauri tubadili mwelekeo na kwenda kwanza Ukerewe. Tulifika Nansio. Tukafanya shughuli zetu za uvuvi hapa na pale, katika kijiji hiki na kile hadi tukajikuta tumeingia katika kisiwa kingine kidogo kiitwacho Ukara.
Ulipata kuona au kusikia juu ya mawe yanayocheza muziki? Kama hujapata hata kusikia mwenzio niliyaona kwa macho yangu katika kisiwa hicho cha Ukara. Kisiwa hicho kina mawe yaliyokaa kiajabu ajabu. Mtu anaweza kufikiria kuwa yalipangwa na binadamu, kwani baadhi yako juu ya mengine, yakiwa yamegusana kwa sehemu ndogo sana lakini hayadondoki si kwa mawimbi wala dhoruba la ziwani. Nilikuwa nikiyakodolea macho mara kwa mara mawe yale hadi mwenzangu mmoja aliposema, “Unashangaa kuyaona yalivyokaa, jee ukiyaona yanacheza?”
Nilidhani ni mzaha. Tulipobishana jamaa hawa walinipeleka katika kijiji cha Kome, ambako tulipata mwenyeji aliyetupeleka eneo la Kululibha yalipo mawe haya ya ajabu. Mwenyeji wetu alitoa amri kwa lugha yake ya Kikara. Mara mawe hayo yakaanza kucheza kama watoto mapacha moja juu ya jingine. Hadi leo sijui ni kitu gani kilichotokea hadi mawe hayo yamtii binadamu.
Lakini huo si muujiza pekee wa Ukara. Pale kijijini kuna kisu chenye makali pande mbili. Unapotokea uhalifu wa aina yoyote watuhumiwa hupelekwa kwa mtaalamu na kuamriwa kukalia kisu hicho. Lakini si kwa mhalifu. Yeye hukatwa mara moja, hata awe amevaa nguo nzito kiasi gani. Kwa yale niliyoyaona, ya mawe kucheza, sikuwa na ubishi wowote kwa jambo hilo.
Maajabu mengine ambayo niliyaona kwa macho yangu, ni mti mmoja kijijini Chilabi huko Ukara. Mti huo ulipigwa na radi ukang’oka. Wenyeji wakaanza kujipanga ili waupasue mbao na kuni. Wakati kabla kazi hiyo haijaanza, mti huo ulisimama na kuota tena palepale ulipokuwa awali. Hata hivyo, haukuwa na majani. Mti huo upo hadi leo. Niliutazama, nikaupapasa. Unaonekana mkavu lakini unaishi.
Maajabu hayo yalifanya tulipoanza tena safari ya Mwanza niwe nimechangamka zaidi.