Riwaya: Kiguu na njia

SURA YA ISHIRINI NA TATU

Mtwara; Tumaini Lilirorejea

Masaibu ya maisha yanaweza kukupangia jambo ambalo hata hukupata kulifikiria. Mfano mzuri ukiwa wangu mwenyewe. Maishani mwangu sikukusudia kuwa mhalifu wala sikupata kutarajia kamwe kujikuta nikiishi gerezani kama mfungwa. Lakini ufungwa nao una yake. Ufungwa wangu ulianza kugeuka kuwa utalii.
 
SURA YA ISHIRINI NA NNE

Dar es Salaam, jiji la Raha na Karaha

Dar es Salaam niliiona chungu. Watu, majengo, magari na kila nilichokiona mbele yangu kilinitisha na



Nikapata basi lililonipeleka Stesheni.

























 
SURA YA ISHIRINI NA TANO

Tanganyika, Ziwa Lenye neema

Nadhani nilikuwa mtu wa kwanza kufika Stesheni kati ya wasafiri wa siku hiyo. Nilinunua magazeti mawili ya Kiswahili, moja la Kiingereza na kuketi kwenye lile benchi la mbao kujisomea. Kama kawaida zilikuwa habari zilezile za kukatisha tamaa; Mzee ajinyonga kwa madeni; Msichana akamatwa kwa kutupa kichanga jalalani; Achomwa moto kwa kuiba fuko lenye nepi za mtoto, na nyingine kama hizo. Kurasa za mbele zilipambwa na habari za wakubwa; Rais aenda Uingereza; Waziri Mkuu akutana na Balozi mpya Japan; Hotel mpya kujengwa ufukoni. Upande wa michezo nao ulitawaliwa na habari za vilabu vilevile ambavyo nimekuwa nikivisikia toka mwaka wa 47; Yanga yasajili kinda; Simba kwenda mahakamani; Ligi kuu yahairishwa na kadhalika na kadhalika.

Ziko wapi habari za vijijini? Nilijiuliza. Nilikua na kiu kubwa ya kufahamu chochote juu ya vijiji. Moja ya habari kubwa iliyonigusa sana nilipokuwa gerezani ni ile ya operesheni ya vijiji vya Ujamaa, kwamba serikali ilikuwa imeamua watu wote waende katika vijiji vilivyopimwa kwa ajili ya kupatiwa huduma muhimu za kimaendeleo kama maji, barabara na zahanati. Kwa machache tuliyosikia huko gerezani operesheni ilileta songobingo kubwa kwa wananchi, kiasi kwamba baadhi waliliwa na wanyama wakali huko porini walikohamishiwa, baadhi walidaiwa kujinyonga wakipinga uamuzi huo.

Mimi nilikuwa mmoja kati ya waathirika wa maamuzi hayo. Kwa jinsi ukoo wangu ulivyojitenga, toka mababu na mababu na kujenga nyumba kandokando ya mashamba yetu, kwa vyovyote vile tungekuwa waathirika wa kwanza katika operesheni hiyo. Safari hii ya kurudi nyumbani ilinitatiza kwa hilo. Sikujua wazazi wangu watakuwa wamehamishiwa wapi. Sikuwa na mawasiliano ya aina yoyote nao. Hivyo, sikujua nitaanzia wapi niishie wapi katika kuwatafuta. Kwa bahati mbaya, vyombo vya habari havikutoa walao fununu juu ya hilo.

Wasafiri walianza kufurika Stesheni hapo. Mmoja wao akiwa yule mama wa Kizungu na lundo lake la mizigo. Aliponiona alitabasamu, akanifuata. Nilimsaidia kuweka mizigo yake vizuri, kabla hajaketi na kuniuliza habari za usiku uliopita.

“Ulipata mahali pa kulala?”

“Naam,” nilimjibu.

“Mjini hapahapa?”

“Hapana. Nje kidogo ya mji.”

Alisita kidogo kabla hajageuka na kuniuliza tena, “Unajua jana hatukuambiana majina? Mie naitwa Jane, Jane Goodhall.”

Jane! Halikuwa jina geni sana masikioni mwangu. Nilipata kulisikia mahala. Wapi vile, sikuweza kukumbuka mara moja. “Nimepata kulisikia jina hilo, lakini sikumbuki wapi,” nilimwambia.

“Bila shaka.” Alijibu. “Nimepata kuandikwa mara nyingi katika magazeti na majarida yanayojihusisha na masuala ya maliasili hasa wanyama pori. Nipo Kigoma katika hifadhi ya Gombe. Najihusisha na utafiti wa sokwe,” alifafanua.

“Bila shaka!” nilitamka kwa furaha. “Uko Gombe, kilometa zipatazo kumi na tano hivi, mwambao wa ziwa Tanganyika kuelekea kaskazini, sawa?”

“Naam,” alikubali, kiasi akiwa ameshangaa. “Kwa kweli, ni mwendo wa kilomita kumi na sita.” Aliongeza.

“Uko na mtu anayeitwa Hugo Van Lawick. Mpiga picha za wanyama ambaye ametengeneza filamu nyingi za wanyama,” niliongeza.

Mama huyo alizidi kushangaa, “Ni kweli kabisa. Hugo ni mume wangu. Alinikuta kule wakati naendelea na kazi yangu, yeye akifanya yake. Tukapendana, tukaoana. Umejuaje yote hayo?” aliniuliza.

“Nasoma sana. Nasikiliza redio. Habari za wanyama siku zote hunivutia sana. Habari zako za sokwe nimekuwa nikizifuatilia kwa karibu. Umekwishajua lugha yao?”

Jane alicheka. Kisha akafafanua, “Sokwe, kama wanyama wengine hawana lugha. Wanawasiliana kwa ishara tu ya sauti na miili. Mimi wamenikubali baada ya kunizoea. Tunaelewana nao. Lakini mnyama ni mnyama tu.”

Wakati akimzungumzia sokwe niliona jinsi Jane alivyobadilika. Macho yake yaling’ara, sauti yake ikiwa wazi zaidi. Ilikuwa dhahiri kuwa mapenzi ya mama huyu kwa sokwe hayakuwa na kifani.

Haikuwa uongo. Historia fupi niliyokuwa nayo juu ya msichana huyu ni kwamba alikuwa ameingia katika misitu hiyo ya Gombe mara baada ya uhuru, akiwa mdogomdogo tu, ndio kwanza amemaliza elimu ya sekondari. Jane alifanya maajabu kwa kuweza kuishi peke yake msituni, akiwafuata sokwe kila wanapokwenda, wakati mwingine akilala nao porini, hadi wakamzowea. Alifungua kituo maalumu ambapo sokwe huja na kupata mahitaji yao hasa ndizi ambazo walizipenda sana. Jane aliweza kumfuatilia sokwe toka anazaliwa, anakua, anabalehe hadi naye anapata mtoto, alinukuu mwenendo na tabia zao, chakula chao, tiba zao na hulka zao mmoja baada ya mwingine. Alimfahamu kila sokwe na kila familia ya sokwe vilivyo, kiasi cha kujua nani kiongozi wao, nani anapinduliwa uongozi na nani kapindua. Utafiti makini wa aina yake duniani ambao tayari umempatia shahada ya udaktari.

“Unajua hujaniambia jina lako?” Alinizindua.

“Naitwa Petro Mtukwao Kionambali,” nilimjibu.

Jane alifahamu Kiswahili kidogo sana. Kati ya machache aliyoyafahamu jina la ‘Mtukwao’ au ‘Kionambali’ lilimpa maana fulani, lakini hakuweza kuifafanua mara moja. Aliyataja majina hayo mara mbili tatu, akikosea, kabla hajakata tamaa na kuniuliza maana yake, “Petro bila shaka ni Peter kwa Kiingereza. Ni jina lenye asili ya Kigiriki likiwa na maana ya mwamba au jabali. Hii Kionambali au Mtukwao ina maana gani?”

Jane alinitazama , “Ni la Kiebrania,” nilimjibu. “Lina maana ya Mungu ni mwenye fadhila sio?” nilimuuliza kabla ya kumjibu.



Jane alionyesha mshangao. Nadhani hakutegemea kuwa pamoja na hali niliyokuwa nayo ningeweza kufahamu mambo mengi kama ilivyokuwa. “Ni kweli kabisa,” alijibu baada ya tabasamu fupi, “Kiona mbali?” alisisitiza.

Wazazi wangu hawakupata kuniambia maana hasa ya majina yangu. Nadhani yalitolewa na babu kwa sababu zake. Hata hivyo nilimweleza Jane hili na lile juu ya maana ya majina hayo.

Sidhani kama aliridhika. Mara nilimwona akibadilika ghafla kama mtu aliyekumbuka jambo “Kionambali…. Mtu kwao… nadhani nilipata kuyasikia majina hayo kabla ya leo,” alisema.

Nikacheka.

“Unacheka nini?”

“Nina hakika hujawahi kulisikia mahala popote. Ni jina dogo sana katika nchi hii. Sijawahi kuandika kitabu wala kucheza mpira hata nijulikane.”

“Hapana, nimelisikia likitajwa. Si mara moja si mara mbili,” alisisitiza.

Sikuamini. Nikijua kuwa alitokea kwao Uingereza, akakaa Kenya kwa muda kabla ya kuja nchini sikuona vipi angeweza kukutana na jina langu. Hasa ikizingatiwa kuwa muda mwingi nilikuwa gerezani.

“Unakwenda wapi?” alinihoji.

“Kigoma.”

“Nyumbani kwenu?”

“Ndiyo.”

“Kwa hiyo, safari yetu moja.”

“Bila shaka.”

Alisita kwa muda kabla hajauliza swali jingine, “Kwa hiyo, unakwenda likizo?”

“Ndiyo na hapana,” nilimjibu.

“Una maana gani?”

“Nina maana kuwa ndiyo nakwenda nyumbani; hapana siendi likizo.”

Jibu langu lilimshangaza Jane, “Kwani unatokea wapi?”

Sikuona sababu ya kumficha, “Jela.”

Kiasi nilimwona akishtuka. Lakini, akiwa mwanamke mwenye roho ya chuma, anayeweza kuishi na kuvumilia hasira za ghafla za wanyama hatari kama sokwe, alijirekebisha mara moja. Badala yake aliniuliza kwa upole, “Nini kilitokea?”

Alikuwa binadamu wa kwanza uraiani aliyetaka kujua masaibu yangu toka nilivyofungwa hadi kufunguliwa. Akawa binadamu wa kwanza niliyepata kumsimulia, kwa tuo, yote yaliyonitokea hadi nikatupwa gerezani kwa miaka mingi. Sijui kwa nini niliamua kuwa wazi kwake. Nadhani ni kwa kuwa sikuwa na shaka kuwa ni mtu mwenye huruma sana. Kama anaweza kuishi na sokwe, vipi binadamu mwenzake?

Nilipofika sehemu ambayo nilimtaja Dakta Leakey kama mwajiri wangu pekee ambaye niliishi naye kwa muda mrefu nilimuona Jane akishtuka. Mara akanikatiza kwa kuuliza, “Leakey yupi?”

“Leakey unaemjua wewe. Na mke wake Mary… wagunduzi wa fuvu la kale zaidi nchini,” nilimjibu.

Jane aliinuka na kunikodolea macho ya mshangao. “Sasa nimefahamu wapi nilisikia jina lako kwa mara ya kwanza,” alisema baadaye.

“Wapi?”

“Kwa akina Leakey. Walikuwa hawaachi kukutaja. Walishangazwa sana na kutoweka kwako ghafla, bila kuaga, mtu ambaye walidai kuwa walimtegemea sana katika shughuli zao.”

Ikawa zamu yangu kushangaa, “Unawafahamu?”

“Vizuri sana,” Jane alinijibu. “Walipata kuniajiri pia. Kutokana na mapenzi yangu kwa wanyama na mazingira Leakey alinishawishi kwenda kwenu Kigoma kufanya utafiti wa wanyama wale, binamu zetu.”

Sikuwa na la kusema, nikauliza, “Hawajambo?”

“Nani?”

“Akina Leakey.”

Jane akacheka, “Wazima sana. Kwa nini ulifanya vile?”

“Kufanya nini?”

“Kufungwa. Kukubali kufungwa bila kuwaarifu. Wangeweza kukusaidia.”

Ilikuwa wazi kuwa Jane hajui maana ya kufungwa, hasa katika nchi zetu za dunia ya tatu. Mnyama anayefugwa ana uhuru mara mia zaidi ya mfungwa.

Wakati nikizungumza na Jane nilimwona msichana mmoja, msafiri kama sisi, akinitazama sana. Nilimtupia macho. Nikamwona akiyakwepa macho yangu kwa namna ya haya kiasi. Kitu fulani kilinifanya nipate hisia kuwa namfahamu. Wazo ambalo nililipuuza mara moja. Jana tu nimetoka jela, nitamjulia wapi msichana huyu?

Kitu kimoja kilinivutia kumtazama msichana huyu alikuwa ana tofauti kubwa na wasichana wengine wengi niliowaona jijini hapo. Alikuwa Mwafrika halisi. Nywele zake zilikuwa fupi, ambazo hazikupata kuathiriwa na madawa. Ngozi yake laini maji ya kunde, pia haikuwa na dalili zozote za kuathiriwa na madawa hayo. Hata mavazi yake yalikuwa ya heshima. Gauni jekundu lililomkaa vizuri lilimfunika hadi miguuni.

Lakini kuna kitu cha ziada ambacho kilinivutia zaidi kwa msichana huyu. Halikuwa umbile lake wala mavazi yake. Kilikuwa kitu fulani. Kwa bahati mbaya sikuweza kubaini mara moja ni kipi hasa kilichonivutia zaidi kwake. Ningeweza kukisoma kitu hicho katika macho yake, lakini tayari aliyakwepa macho yangu na kutazama upande mwingine.



Honi ya treni iliyokuwa ikiingia stesheni iliniokoa kujibu swali la Jane pamoja na kuendelea kusumbua fikra zangu juu ya msichana yule. pilikapilka za kuingia katika mabehewa zikaanza. Mimi nikiwa sina mzigo wowote nilifanya kazi ya kumsaidia kupakia vitu vyake katika chumba cha daraja la pili alicholipia. Mimi, nikiwa sina namba ya kiti, nilipata debe moja la msafiri mwenzangu na kulikalia. Roho yangu ilipumua pale dakika ishirini baadaye treni ilipoanza safari ya kuelekea bara.

Jing... jang… jing… jang… tuliuacha mji na kuingia Buguruni. Jing… jang… jing… jang … vingunguti. Jing… jang… jing… jang… Karokota. Taratibu tukauacha mkoa wa Dar es Salaam na kuingia Pwani. Tulizipita stesheni za Soga, Ruvu na Magindu kabla hatujaiacha Pwani na kuingia Morogoro katika stesheni za Kidugalilo, Ngerengere, Mikesa na hatimaye Morogoro mjini.

Wakati huo usiku ulikwishaingia. Sikuweza kuziona vizuri stesheni za Mkata, Kimamba na ile ya Kilosa. Toka hapo tuliingia stesheni ya mpaka wa Morogoro na Dodoma, Kidete kabla ya kufika Godegode, Gulwe na Kikombo. Tulifika Dodoma alfajiri ya siku ya pili.

Jane alikuwa akinitafuta. Alinikuta nikiwa nimeegemea mlango nikijaribu kupata chochote ambacho ningeweza kupata juu ya mji wa Dodoma, makao makuu ya serikali baada ya kuhamishwa toka Dar es Salaam. Zaidi ya majengo kadhaa, barabara pana zaidi na watu wa kutosha zaidi bado Dar es Salaam niliyoiacha jana ilifanya Dodoma ionekane kama mzaha kuiita makao makuu.

“Unajisikiaje?” Jane aliniuliza

“Safi kama chuma cha pua,” nilimjibu

Akacheka. “Twende tukapate kifungua kinywa,” aliniambia.

“Wapi?”

“Mgahawa wa humu ndani.”

Nikamfuata. Tulipita mabehewa kadhaa kabla ya kufikia behewa la chakula. Tukaketi. Aliagiza chapati mbili, supu ya kuku na chai kwa kila mmoja wetu. Kwangu ulikuwa mlo ambao sitapata kuusahau kwa muda mrefu. Toka nilipopata chai na maharage ya ‘mama ntilie’ kula Manzese tumbo langu lilikuwa halijaonja chakula zaidi ya karanga za mia moja nilizonunua humo ndani.

Tulikula taratibu. Kila mara Jane akinidodosa juu ya mipango niliyokuwa nayo baada ya kutoka gerezani. Hakunielewa pale nilipomwambia kuwa nilikuwa na mpango mmoja tu katika akili yangu, ambao haukuwa ziadi ya kufika nyumbani, kumwona babu na wazazi wangu, kama wako hai.”

“Bila shaka ulitoka kwenu mikono mitupu… unataka kurudi mikono mitupu?” alinihoji.

“Sina jinsi.”

“Kwa nini?”

Asingeweza kuelewa. Asingeelewa hata kidogo hata kama ningemwelewesha vipi. Kwamba lazima nikaombe radhi kwa kupoteza hirizi! Kwamba nina hakika mikosi na balaa nyingi ninazopata zilitokana na kuipoteza baraka ile, hivyo lazima nioshwe kwa kutemewa mate usoni. Mzungu, mwenye utamaduni tofauti na wangu angeelewaje? Sikujisumbua kumwelewesha.

Jane akaamua kuifichua siri iliyokuwa moyoni mwake. Alinitaka twende wote Gombe nimsaidie kazi. Kwamba alikuwa na mipango ya kufungua kituo kingine cha sokwe kusini mwa ziwa Tanganyika, katika milima ya Mihale, kilometa zipatazo 120 toka mjini Kigoma. Kwa mujibu wa Jane milima hiyo ilikuwa na sokwe waliokadiriwa kuwa 700 katika makundi kama kumi na mitano. “Siwezi kufanikisha peke yangu. Lazima niwe na mtu mwaminifu, mwadilifu na pia tunayeelewana lugha vizuri,” alisema

“Halafu,” aliongeza. “Mume wangu ana mpango wa kutengeneza filamu kubwa, itakayojumuisha vivutio mbalimbali vya Tanzania. Kwa historia yako na uzoefu wako hakuna mtu ambaye atamfaa zaidi yako.”

Hili la pili lilinivutia zaidi. Ningependa sana kuwa sehemu ya historia ya mtu atakayefanikisha kazi hiyo. Lakini nilikwishajiwekea nadhiri ya kutojihusisha na jambo lolote kabla ya kufika kwetu. Ama niwaone wazazi wangu, ama niyaone makaburi yao.

Nilimweleza hivyo Jane. Bado hakunielewa. Lakini hilo lilikuwa tatizo lake, halikuwa langu.

Safari ya mchana ilivutia zaidi. Tulisimama dirishani mimi na Jane tukiangalia nje, kituo baada ya kituo. Nkungu, Nala, Bahi, Kintinku, Saranda, hatimaye tukaingia Manyoni. Watu na mazingira maeneo yote haya havikunifurahisaha sana. Ardhi ilijaa vumbi, mtu mmoja hapa na pale. Hali iliyonifanya hisia za nusu jangwa zinijie akilini. Hali kadhalika hali za wakazi wengi iliashiria umasikini mkubwa. Mavazi ambayo wengi wao walivaa, baadhi wakitembea bila hata kandambili. Ilikuwa dalili tosha ya umasikini. Hata wale waliokuwa na bidhaa, bidhaa zao ziliashiria kuganga njaa tu. Mtu mzima akiwa na vichane vitatu vya ndizi, mwingine akiwa na chupa moja ya asali, yule sinia la karanga! Kwa gari moshi ambalo hupita hapo mara mbili tatu kwa wiki sikuona kama biashara hizo zilikuwa na namna yoyote ya kuwaondoa katika vibanda vya tembe tulivyokuwa tukiviona toka tunaingia Dodoma hadi tunaiacha.

Stesheni ya Manyoni ilishamiri kwa biashara ya kuku, walio hai kwa waliokaangwa. Takribani kila mtu alikuwa na sinia yenye mapaja ya vidari vya kuku wanaotamanisha kuwala. Bila shibe ya mlo alionipa Jane ningejikongoja kununua paja moja. Ingawa baadhi ya watu hudai kuwa hawa si kuku wa kawaida kwa ajili ya wingi wao. Wanadai baadhi ya tunaowadhania kuku waliokaangwa ni kunguru na ndege wengine wa porini waliozagaa katika maeneo hayo. Kwa kweli, ulikuwa mzaha wa watani wa Wanyaturu na Wanyiramba.

Toka Manyoni tuliingia Itigi, kaskazini hadi Malingwe. Jua likaanza kuzama. Jane alirudi chumbani kwake kujisomea kitabu mimi nikaendelea kuranda ndani ya mabehewa hayo mengi. Tukafika Nyama, tukaingia Igagula. Saa mbili za usiku tulifika Tabora. Hapo tulichukua muda mrefu kutokana na pilikapilika nyingi za kubadili mabehewa, kukagua vichwa vya treni na pengine kufanya ukarabati.

Nilitamani kuutumia muda huo kuchepuka kidogo nikautupie macho, walao kidogo mji wa Tabora, ambao uko kidogo nje ya stesheni hiyo. Hata hivyo kwa kuchelea kuachwa sikuthubutu. Niliishia kuchungulia tu nje ya stesheni ambako niliiona ile miembe iliyozeeka lakini bado ilikuwa ikipamba na kuzaa embe tamu za dodo na bolibo.

Niliona pia kundi kubwa la mbuzi wasio na mlinzi wakirandaranda kando ya barabara hiyo. Mbuzi wa Tabora? Nilijiuliza nilipokumbuka simulizi ya mji wa Tabora kuwepo na mbuzi wengi wasio na mmiliki ambao hutembea ovyo mitaani bila kubugudhiwa, mbuzi ambao inaaminika kuwa kwa namna moja au nyingine wanahusiana na ama ushirikina ama laana fulani. Mwenyewe alifariki zamani na kufanya wawe hawana mwenyewe, lakini kila mtu ambaye huthubutu kuwala hudhurika na hata kupoteza maisha. Jambo ambalo lilisababisha hata wezi wa mjini hapo wawaogope.

Honi ya kuashiria safari ikapigwa. Nikarudi au kuparamia behewa lolote lililokuwa karibu. Dakika tano baadaye safari ikaanza. Ilikuwa awamu ya mwisho ya safari hiyo ndefu ya kilometa 2600 toka Dar es Salaam hadi Kigoma.

Hamu niliyokuwa nayo ya kufika nyumbani ikaanza kuingia nyongo. Hofu ikaanza kuchukua nafasi. Hofu ya kutojua lipi nitalikuta huko nyumbani. Habari za kufurahisha au kuhuzunisha, heri au shari. Hali kadhalika, aibu ya kurudi mikono mitupu kama nilivyoondoka, baada ya miaka nenda rudi ya kuhangaika pia ilinitesa sana. Sio siri, nilitamani garimoshi hilo lipate ajali, mtu mmoja tu apoteze maisha; Petro Kionambali.

Haikuwa. Treni iliendelea kukata mbuga. Ikiwa safari ya usiku sikuweza kuona mabadiliko ya ardhi toka ile ya nusu ukame. Ya Dodoma hadi Tabora hadi ile yenye rutuba nyingi ya kutokea Tabora hadi Kigoma. Kelele za wasafiri kila tulipofika stesheni ndizo ziliniashiria tuko wapi; Usoke, Kaliua, Suinge, Malagalasi, Uvinza, Simbo, Luiche na hatimaye Kigoma

Ulikuwa mkesha wa aina yake. Pilikapilika za kuingia katika mabehewa kila stesheni zilikuwa kubwa na za fujo kubwa. Mizigo ilirushwa ndani ikifuatiwa na wababe; wake kwa waume. Ilikuwa rahisi kwa mgeni kufikiria kuwa watu wa Kigoma wana asili ya vurugu. Lakini kamwe mwenyeji asingeweza kufikiria hivyo. Watu hawa hawakuwa na njia nyingine yoyote ile ya usafiri. Maeneo mengi hayakuwa na barabara iliyowaunganisha na upande mwingine wa dunia zaidi ya treni. Hivyo, kuachwa na usafiri huo kulimaanisha kuharibikiwa kwa mipango yako ya safari pengine kwa wiki nzima au zaidi. Hivyo, kutumia nguvu na ubabe lilikuwa jambo la lazima.

Tulifika Kigoma saa moja na nusu za asubuhi, lakini kwa sababu za kijiografia ndio kwanza jua lilikuwa likichomoza. Miale yake ilipenya milima ya Bangwe na kutuangazia pale stesheni, kando kabisa mwa Pwani ya ziwa Tanganyika. Ziwa ambalo liliupokea mwanga huo, likaujumuisha na maji yake yasiyo na rangi na kufanya limeremete kwa mchanganyiko wa nuru ya rangi ya dhahabu toka angani na buluu toka katika lindi la maji na kutoa sura ya kusisimua sana.

Nilishuka na kusimama kwa muda hapo nje nikitazama huku na kule kana kwamba siamini kuwa nimerejea nyumbani. Macho yangu yalivutwa na jengo imara la stesheni hiyo, lililojengwa na Mjerumani toka enzi zile. Zaidi ya ukarabati wa rangi na pengine bati jengo lile lilikuwa imara kama walivyoliacha. Wala halikuwa na dalili zozote za kupoteza uimara wake katika siku za usoni.

Nikahamisha macho kwenye jengo na kuyatupa ziwani. Kwa mbali, niliweza kuona mitumbwi na mashua za wavuvi wakirejea Pwani baada ya shughuli zao za usiku kucha, lakini kilichovutia zaidi macho yangu ni meli kubwa, yenye rangi nyeupe iliyotia nanga katika bandari hiyo. Jina lake liliweza kusomeka hapo niliposimama, MV LIEMBA.

Hii ni mali yenye historia ya pekee duniani. Kwanza, inaaminika kuwa ni meli ya kale kuliko zote duniani ambayo bado inafanya kazi. Pili, imezitumikia enzi zote muhimu za historia ya Tanganyika ikiwa imeletwa na kuunganishwa na Wajerumani miaka ya 1914 na kupewa jina la Graf Von Goetzen. Mjerumani alipozidiwa katika vita ya pili aliizamisha katika lindi la ziwa Tanganyika wa nia ya kumkomoa Mwingereza aliyechukua madaraka. Lakini wao walifanya kila jitihada kuiibua majini na kuitengeneza. Ikaanza kazi kwa jina jipya la SS Liemba. Tanganyika ilipopata uhuru wake Liemba ilikarabatiwa tena na mitambo yake badala ya kutumia mvuke ikawa ikitumia dizeli, hivyo ikaitwa MV Liemba. Meli hiyo hadi sasa ni tegemeo kuu la usafiri katika mwambao wa ziwa Tanganyika hadi bandari za Mpulungu Zambia, Bunjumbura, Burundi na Kelemie Kongo.

Upande wa pili wa ziwa hilo macho yangu yalivutwa na baadhi ya milima ya nchi hizo. Burundi kwa upande wa kaskazini na Kongo ilionekana mbele yangu, magharibi ya nchi yetu. Hali ya hewa ikiwa safi, anga likiwa angavu niliweza kuiona milima ya nchi hizo kwa uwazi kabisa.

Sijui ningesimama hapo kwa muda gani kama nisingeshikwa bega na nilipogeuka nikakutana na uso mpole wa yule msichana aliyenivutia pale stesheni ya Dar es Salaam. Sura yake ilikuwa iliyojaa haya. Hata hivyo, alijitahidi na kuniuliza kwa sauti yake ya upole, “Samahani kaka. Hivi unaitwa Petro Kionambali?”

“Naam,” nilimjibu.

“Ulipata kuishi katika maeneo ya Bonde la Ufa?” aliongeza swali jingine ambalo pia nililikubali. Nikamwona akibadilika sura. Kwanza alitabasamu. Kisha tabasamu lake likamezwa na uso uliojaa huzuni, machozi yakimlengalenga machoni.

“Vipi kwani?” nilimwuliza kwa mshangao.

“Petro… Hunikumbuki?”

Sikuweza kuelewa anachozungumza. “Nakumbuka kukuona juzi pale stesheni, Dar es Salaam, kwa mara ya pili nakuona leo hapa Kigoma,” nilimjibu

Pamoja na machozi yake nilimwona akitabasamu kisha alisema, “Petro wewe ulipata kuokoa maisha yangu kwa kuhatarisha yako. Ulinichukua hadi Singida ambako ulinipeleka misheni ambako walinilea kiimani na kielimu. Sasa hivi nina kazi nzuri hapa Kigoma.”

Akili zangu zilikimbia na kunirejesha nyuma zaidi ya miaka ishirini iliyopita. Nikamwona yule msichana wa Kimasai aliyekuja katika kambi yangu huku akitetemeka. ‘...Nisaidie ...Naogopa’ Nilikumbuka jina lake, “Nashifa sio?”

Nilimwona akichangamka. “Unalikumbuka hata jina langu? Hata hivyo nilibatizwa na kupewa jina jipya la Maria. Lakini sijaliacha jina langu la asili. Nimefurahi sana kukuona Petro. Siku zote nilikufikiria usiku na mchana. Nilikuwa na hakika kuwa ingetokea siku nikakutia machoni. Imetokea…” alisita kuzungumza na kuangua kilio.

Sikujua kilichotokea nilijikuta nimemkumbatia kwa namna ya kumfariji huku yeye pia akinikumbatia na kukilaza kichwa chake juu ya kifua changu akiendelea kulia huku akinong’ona maneno fulani ambayo sikuyasikia vizuri. Nilisikia machache tu, “Uliokoa maisha yangu… kwa gharama ya kuharibu yako… sikupata kujisamehe kwa kitendo kile…”

Nilicheka kidogo kabla ya kumnong’oneza vilevile, “Maisha yangu ni hadithi nyingine. Masaibu yako hayahusiani hata kidogo na yale yaliyotokea. Yangu nayajua mimi na Mungu wangu.”

Tulikuwa bado tumekumbatiana. Kama si macho ya wapita njia kututazama kwa mshangao sijui tungekaa katika hali hiyo kwa muda gani. Macho yao yalifanya nijikumbuke na kujitazama. Nilitoa picha ya kuchekesha sana kwa mavazi yangu ambayo hayakuwa zaidi ya midabwada, kumkumbatia msichana huyu mtanashati ambaye sasa alivaa vitenge vilivyomkaa kana kwamba alizaliwa navyo. Nikajikwanyua toka mikononi mwake na kumtaka radhi.

“Samahani ya nini? Hujui nilivyofarijika Petro.” Alisema.

“Lakini tayari njia zetu zimetofautiana sana. Mimi ni ndege wa jela asiyestahili kukukumbatia hadharani. Tazama nilivyo,” nilisema nikijitenga naye zaidi ili anione vizuri zaidi.

Kwa mshangao wangu alicheka kabla ya kusema, “Najua yaliyokusibu. Nilikuwa nikifuatilia kwa karibu maongezi yako na yule mama wa Kiingereza. Anaitwa nani vile, Jane siyo?”

Nilikubali kwa kichwa.

“Hivyo huna haja ya kuniambia chochote zaidi. Najua umerudi kwenu. Najua umerudi mikono mitupu. Usijali. Nitakusaidia kadri ya uwezo wangu. Uliniokoa kwenye mvua mimi pia nitakuokoa kwenye jua.”

Alitia mkono wake kwenye pochi lake la mkononi na kutoa kadi ambayo alinikabidhi. Ilikuwa na majina yake na namba za simu. Kilichonivutia zaidi ni cheo chake. Afisa uhamiaji wa mkoa! Niliduwaa.

“Matunda ya wema wako hayo.” Alinifafanulia.

“Wamisheni wale walinipa elimu bora hadi chuo kikuu. Mara kadhaa nimepelekwa nje kuongeza ujuzi. Huu ni mkoa wangu wa tatu toka nilipopanda cheo.”

Nilizidi kuduwaa. Safari hii aliniondoa mshangao kwa kunishangaza zaidi. Alitia tena mkono wake mfukoni na kunipa kitita cha fedha. Kwa hesabu za haraka haraka zilipata kuwa shilingi laki moja.

“Za nini?” nilimuuliza.

“Zitakusaidia kidogo. Najua una matatizo mengi. Fika nyumbani, wasalimu wazazi halafu njoo mjini tushauriane.”

Nilitamani kulia. Kwa nini siku zote maisha yangu yamekuwa ya kukutana na binadamu wenye roho mbaya kama shetani na wale wenye roho nzuri mfano wa malaika? Nilijiuliza huku nikiwa nimemkodolea macho. Unajua wewe ni malaika. Unajua utafika mbinguni? Nilitamani kumwabia hivyo. Nilishindwa. Badala yake nilijikongoja kumwuliza, “Umeshaolewa?”

Alinipa jibu jingine ambalo liliniacha taabani zaidi, “Nilikuwa nikikusubiri wewe.” Nilipomtazama, aliyaepuka macho yangu na kutazama chini. Mara nikaelewa kilichonivutia zaidi juu yake. Haya! Pamoja na elimu yake, pamoja na cheo chake, bado alikuwa msichana wa kiafrika halisi, mwenye uso wa soni tofauti kabisa na wasichana wengi wa kileo.

“Sina budi kuondoka,” aliseme. “Tafadhali tuwasiliane. Sawa Petro Kionambali?”

“Bila shaka.” Nilimjibu

Akaifuata gari ambayo muda wote ilisimama nje ya stesheni ikimsubiri. Akaingia upande wa pili wa dereva na kupunga mkono wakati gari ikitiwa moto na kuondoka.

Mara alipotoweka machoni mwangu, nilihisi upweke wa pekee ambao sikupata kuujua huko nyuma.

Nilizihesabu tena fedha alizonipa. Nilikuwa na laki moja na hamsini. Sikuhitaji kufikiria sana. Niliendea duka la karibu la nguo na kununua shati mbili, suruali mbili na shuka la kujifunika.

Nilikuwa na mfuko wa nguo mpya mkononi ndiyo kwanza nilijiona nilivyochakaa. Nilikuwa nanuka!. Niliweza hata kuisikia harufu chafu ya mwili wangu mimi mwenyewe. Jasho la joto la Dar es Salaam na vumbi la Dodoma, purukushani za Tabora na malazi mabaya ndani ya behewa lililotoa mchanganyiko wa kutisha. Nikaamua kuiacha bandari na kuufuata ufukwe nikielekea Mtanga hadi nilipopata sehemu faragha ambayo nilivua nguo zangu na kujitupa ziwani. Sikuwa na sabuni wala mswaki. Nilitumia mchanga na vidole kujisugua. Nikapiga mbizi mara mbili tatu. Kweli, aliyeogelea hafi maji, kwani nilijikuta nikielea juu ya maji kana kwamba maisha yangu yote nilikuwa ziwani humo.

Nilipotoka majini nilijihisi mtu mpya. Hisia fulani ziliniambia kuwa kwa kuoga katika ziwa hili lenye historia ya pekee nilikuwa nikisafisha mikosi na mikasa yote iliyoniandama na kuanza maisha mapya.

Pengine haikuwa uongo. Ziwa Tanganyika lilikuwa mwujiza mwingine wa dunia. Kwanza lilikuwa refu kuliko maziwa yote duniani. Pia, kina chake kwenda chini kilivunja rekodi ya maziwa yote ya ulimwengu. Likiwa limeenda chini kwa takribani meta 2400 toka kilele cha milima ya Mahele iliyopo kilometa 150 toka Kigoma mjini au meta 1500 toka ardhi ya kawaida ya mkoani humo mwisho wa kina hicho uliwiana na usawa wa bahari kwa miji ya Dar es Salaam na Zanzibar. Inaaminika kuwa kuwepo kwa ziwa hilo ni matokeo ya mabadiliko makubwa yaliyopata kuitokea dunia, kama matetemeko ya ardhi au volkano ambayo pia yanaaminika kuibua vitu kama Bonde la Ufa. Walikotokea samaki ainaaina na viumbe wengine hai waliomo tele ziwani humo ni fumbo jingine ambalo mwanadamu hajapata kulipatia ufumbuzi.

Sikuhitaji gari kutoka kigoma hadi Mwanga. Mwendo wa dakika ishirini kwa mguu uliniwezesha kufika katikati ya mji huo. Mwanga ilichangamka. Vijana waliokuwa wakifanya kazi za kushevu walikuwa tele katika ofisi zao zinazovutia kwa vioo na viyoyozi. Niliingia katika kimojawapo cha vibanda hivyo na kukinga kichwa changu.

“Nywele na ndevu,” nilisema.

“Utahitaji tukuwekee na super black, kaka?” niliulizwa na kijana huyo

“Kwa nini?”

“Mvi zinakuanza. Unaona hapa?” alielekeza.

Nikajitazama katika kioo. Kweli, kulikuwa na mvi mbili tatu katikati ya kichwa changu. Nazeeka! niliwaza kwa mshtuko kidogo. Kuzeeka kabla ya kufanya jambo lolote ambalo familia, jamii na nchi yangu itaweza kujivunia haikuwa dhamira yangu hata kidogo.

“Hapana, shevu tu,” nilimwambia. Sikuona haja ya kuficha shahada ya umri wangu.

“Ndevu unashevu kwa mashine au magic?”

“Ndiyo nini hiyo mejiki?

Akanionyesha dawa fulani. “Hii inafanya kidevu kiwe kama cha mtoto mdogo,” Alifafanua.

“Na bei yake?”

“Iko juu kidogo.”

“Kama ni hivyo tumia mashine.”

Muda mfupi baadaye nilikuwa mtu mwingine kabisa, mtu anayependeza kwa usafi hasa kwa kijana huyo kunipaka mafuta ambayo yalilainisha ngozi yangu. Nilijitazama kwenye vioo vyake, mbele na nyuma, kwa muda kabla ya kumlipa na kuondoka.

Niliuliza magari ya kwenda Kasulu. Niliambiwa kuwa nimekwishachelewa, kwamba lilikuwepo basi moja tu la Mwarabu ambalo huondoka saa kumi na mbili za asubuhi kila siku. Pia, nilidokezwa kuwepo kwa malori ya mizigo ambayo huondoka asubuhi hadi saa tatu. Nilipoitazama saa yangu iliitimu saa nne na nusu za asubuhi. Nikaamua kutafuta hoteli ya bei nafuu ili nijipumzishe hadi hiyo kesho.

Kabla ya kuchukua chumba niliamua kuuvinjari kidogo mji wa Mwanga. Kama miji mingine nchini Mwanga ilipanuka sana. Maeneo kama Vumilia na Majengo ambayo zamani yaliogopwa na kudharaulika sasa viwanja vyake vilioneka lulu. Majengo yalikuwa yakiota kama uyoga. Kwa bahati mbaya sana, kama yalivyokuwa maeneo mengi mapya, maeneo haya pia yalikosa huduma muhimu. Hayakuwa na mifereji ya maji machafu, hayakuwa na mfumo wa maji safi, umeme wa barabarani ilikuwa ndoto na hata barabara zilijaa na kujitunza zenyewe. Hali iliyopelekea mafuriko na uchafu kuivuruga dhamira nzima ya wamiliki.

Nilienda Mwanga Katubuka. Nikaingia Sokono. Macho yangu yalikuwa yakiwatafuta samaki niliowazoea na wale ambao nimekuwa nikisikia sifa zao toka utotoni; nonzi, wale samaki wakubwa wanaofanana na ndege, kuhe, samaki mtamu ambaye ana hadhi; singa, samaki mnono aliyejaa mafuta mwili mzima, nika, samaki mwenye nguzu za umeme ambaye kumshika lazima utumie mdomo wake wa chini vinginevyo utarushwa na kumwachia; kuvungwe, anayeitwa nguruwe wa majini kwa umbile na masharubu yake.

Ningependa pia kuwaona kungura, ndubu, kambale na wengineo. Sikuwa na bahati hiyo. Samaki niliowaona sokoni humo siku hiyo ni migebuka ambayo ilikuwa imekufa kwa wingi. Ndubu? Siku hizi hapatikani sana. Kibonde? Alikuwepo mmoja tu leo, amegombewa kama mpira wa kona. Nikakata tamaa. Nikaenda soko la dagaa ambamo kulikuwa na dagaa wabichi wenyewe wakiwaita “mteke” na samaki wadogo wadogo walioitwa “Masembe.”

Nilipochoshwa na ziara hiyo nilitafuta hoteli na kuagiza chakula. Ningekula nini zaidi ya ugali wa muhogo kwa migebuka iliyokaangwa kwa mafuta ya mawese? Ulikuwa mlo mtamu uliofanya nijisikie shibe isiyo na kifani.

Baadaye nilipanda basi kwenda Ujiji. Sikujisikia kuondoka Kigoma bila kuuona mji huo wa kihistoria. Mji ambao ulikuwa na uzito mmoja na ile ya Bagamoyo, Zanzibar na Kilwa. Lakini mara niliposhuka kilima cha kutoka Mnarani na Mawemi matumaini yangu ya kuiona Ujiji inayosisimua ilizimika. Macho yangu yalipokelewa na mji wa kale, kama ulivyokuwa enzi za kina Tip Tippu na Livingstone. Mji uliomezwa na nyumba nyingi ambazo ziliezekwa kwa nyasi au bati kuukuu. Baadhi ya nyumba zilikuwa kuukuu zikiashiria jambo lilelile ambalo nimekuwa nikiliona huku na huko toka nilipotoka kifungoni; Umasikini.

Hali ya mitaa mingi pia ilitia huzuni. Kwa mtu aliyetoka katika miji inayokua, hata Mwanga tu, Ujiji ingeweza kumtoa machozi. Mitaa mingi ilimezwa na majani. Baadhi ya mitaa majirani walianza kulima mahindi na maharage. Kuna nini? Nilijiuliza. Yako wapi magari yachangamshe mitaa? Wako wapi watu waitie uhai? Nini kimetokea hapa?

Nikafikia uamuzi. Bila shaka biashara ya utumwa ilikuwa na laana. Vinginevyo mji huu ambao Dakta Livingstone alitia kambi miaka ya 1871 wakati akifanya utafiti katika nchi za Kongo na Malawi. Mji ambao Novemba 10, mwaka huohuo Henry Stanley, baada ya kutumwa kumtafuta alikutana naye ufukweni na kusema “Dr livingstone…! I presume…” mwaka mmoja kabla ya kifo chake. Ukiwa njia na kituo kuu cha wafanyabiashara wa Arabuni, Ulaya na Amerika katika kujipatia bidhaa za meno ya tembo na ile biashara haramu ya watumwa. Mji ambao huwezi kuandika historia ya Afrika bila ya kuutaja! Hadi leo uko hivi! Kama si laana ni nini?

Nilishuka kwenye basi, nikaifuata barabara ya Livingstone ambayo ilinifikisha Pwani ya Ujiji, pale Livingstone alipokutana na Stanley kwa mara ya kwanza. Palijengwa nguzo ya kumbukumbu yenye maelezo ya hafla yao ile. Nikatupa macho yangu ziwani na kuziona boti za jahazi ya wavuvi waliokuwa katika pilikapilika za safari, ama kuondoka ama ndio kwanza wanafika toka maeneo hayo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Nikarejea Mwanga na kuanza kutafuta hoteli ya kulala. Ujiji haikuwa na nyumba ya aina hiyo. “Nenda Mwanga… nenda Kigoma mjini. Hapa utalala nje bure,” niliambiwa na msamaria mwema, mtu mzima aliyevaa kanzu na baragashia. Mkewe alivalia baibui lililomfunika gubigubi isipokuwa sehemu ndogo ya macho na miguu. Wazee hao walinikumbusha Bagamoyo na Pangani.

Wakati azana ya kuwakumbusha waumini kuwasili zinaanza kutoka misikiti mbalimbali mimi nilikuwa nikipanda basi kurudi Mwanga.







SURA YA ISHIRINI NA SITA

Hirizi Iliyopotea Na Maajabu Yake

Pengine kwa ajili ya safari ndefu ya wima toka Dar es Salaam, pengine kwa ajili ya chumba murua chenye hewa safi nilicholala nilijikuta nimechelewa kuamka. Hivyo, basi la Mwarabu liliniacha. Nilioga harakaharaka, nikanywa chai kwa dagaa wa mteke, kisha huyoo, nikawahi malori ya mizigo. Nilipata moja lililokuwa likipakia mabati na vifaa vingine vya ujenzi. Kwa namna ya muujiza nilipata kiti cha mbele, tukiwa abiria wawili tu na dereva. Muda mfupi baadaye gari liliondoka.

Nikiwa nimekaa dirishani nilipata fursa nzuri ya kutazama nje, macho yangu yalivutwa na ardhi nyekundu, mimea ya asili, mashamba ya wenyeji na zaidi ya yote watu. Toka Mwanga hadi Gungu na baadaye Mwandiga yalikuwa maeneo ya watu, nyumba ambazo hazikutofautiana sana na zile za Mwanga na Ujiji. Hii hapa ikiwa imejengwa kwa saruji bati na samani nyingine zikiwa zimeipamba; ile ikiwa nyumba ya tope, ilijengwa kwa matete na mianzi na kuezekwa kwa nyasi.

Toka Mwandinga mambo yalibadilika zaidi. Nyumba duni zilianza kutamalaki huku zile za afadhali zikizidi kupungua. Watu pia walibadilika. Wengi walivalia mavazi duni, baadhi yakiwa yamechanikachanika. Ilikua rahisi sana kumshuku mtu kuwa ni mwendawazimu kutokana na hali hiyo. Lakini pale unapoona idadi kubwa zaidi iko katika hali hiyo, hasa watoto ambao wengi wao walitembea nusu watupu, miguu iliyojaa vumbi jekundu ikiwa pekupeku, unajikuta ukiondokana na wazo lako na kupata jibu mara moja, rahisi; umasikini.

Nyuso za watu wengi zilionyesha dalili ya kukata tamaa. Walicheka ndio, lakini kicheko hicho kilionekana mdomoni tu, moyoni ungeweza kusoma kitu kingine kabisa. Walizungumza pale ulipozungumza nao, lakini sauti zao ziliashiria kuifadhi jambo fulani ambalo hawakuwa na uwezo wa kulifafanua. Sura hizi za msiba, majengo mengi ya maombolezo na ardhi nzuri ambayo haikuwa ikichekelea kwa pamba na kahawa kama nilivyoizowea utotoni ni jambo ambalo lilinitia hofu badala ya shahuku ya kufika nyumbani. Nilihisi huzuni ikinigubika katika fikra zangu katika safari hiyo nzima.

Ndiyo, nchi yetu ni masikini. Lakini umasikini huu unazidiana kati ya mkoa na mkoa. Pengine iko mikoa iliyo taabani zaidi ya Kigoma, hilo halikunisumbua. Kilichonisumbua ni kwa nini Kigoma iwe katika kundi hilo? Kigoma haikuwa na sababu yoyote ya kuwa kama ilivyo. Ni mkoa uliojaaliwa kila ambacho binadamu anahitaji. Ardhi ilikuwa na rutuba tele, mali asili zikiwa zimefurika katika misitu na ardhini. Mito, mabwawa na baba lao; ziwa Tanganyika vikiwa vimejaa samaki tele ambao ladha yake ina uwezo wa kumshangaza mtu yeyote duniani zaidi ya hiyo Kigoma ni lango muhimu kwa nchi za Kongo, Burundi na hata Zambia. Ukweli huo pekee wa kijiografia ni rasilimali tosha. Historia ya Kigoma, hasa Ujiji pia ni rasimali nyingine muhimu ambayo kuitumia vyema kungeweza kuubadili mkoa kiuchumi.

Kitu gani kimetokea hata mkoa uwe ukirudi nyuma badala ya kwenda mbele? Kitu gani kimesahauliwa? Nani alaumiwe? Nilijiuliza hili na lile. Yako mengi ambayo hayakuhitaji utafiti wa kina kuyaona. Moja la haraka likiwa usafiri. Ilikuwa rahisi zaidi kutoka Kigoma kwenda Burundi au Kongo kuliko kwenda Tabora au Mwanza, achilia mbali Dar es Salaam. Wakati huu wa Kilimanajaro au Arusha anaweza kutoka Dar es Salaam hadi kwao na akarudi jioni au kesho yake ilimchukua mtu wa Kigoma wiki mbili au zaidi kufanya safari hiyo, hali ambayo muuza nyanya au samaki ataishia kuiona bidhaa yake ikioza mbele ya macho yake.

Barabara ilikuwa tatizo la kwanza lisilohitaji mjadala barabara pia lilikuwa tatizo la pili. Kigoma ulikuwa mmoja kati ya mikoa iliyo kimya sana. Pamoja na kukisiwa kuwa na eneo la kilometa za mraba 37,037 mkoa wa Kigoma ulikuwa hauna kiwanda hata kimoja. Hata wale samaki, aina ya migebuka ambao katika misimu fulani huliwa kwa mamilioni huishia kuharibika bure na kutupwa badala ya kusindikwa; achilia mbali dagaa wanono wenye sifa zote.

Hata mafuta ya mawese, yatokanayo na michikichi ambalo ni zao linalostawi sana mkoani humu hayajapata kujengewa kiwanda cha kuyasindika ili yauzwe kimataifa. Nani atafikiria kufanya mradi kama huo mahala ambapo hakuna hata barabara?

Barabara pekee ambayo haikuaminika sana ya kutoka Kigoma kwenda nje ya mkoa ni hiyo tuliyokuwa tukiitumia. Sehemu ndogo sana zilikuwa na lami. Sehemu kubwa ikiwa Changarawe na tope ambalo lilifanya safari iwe shughuli kubwa badala ya starehe. Lakini hilo halikuwa tatizo kubwa. Tatizo hasa lilikuwa mzunguko wa njia hiyo ulioifanya kuwa ndefu kupita kiasi. Ili kwenda Dar es Salaam au Tabora miji iliyoko mashariki ya mkoa ulilazimika kwenda kaskazini, upite Kasulu, Kibondo hadi Biharamulo kabla hujageuka kuelekea kusini ili ufike Kahama na Nzega kabla ya kuingia Tabora. Toka Tabora unapanda kaskazini tena na kurudi Nzega kabla ya kwenda Igunga, Iramba, Singida hadi Manyoni. Toka hapo utafika Dodoma na kutelezea Gairo, Morogoro, Chalinze na baadaye Dar es Salaam! Pema hapo?

Ndiyo, Kigoma kuna uwanja mdogo wa ndege. Ndege ndogondogo vilevile huja na kuondoka mara mbili au tatu kwa wiki. Licha ya ukweli kuwa hazitoshi, bado nauli kubwa ya ndege imefanya ziwe na wenyewe badala ya kila mtu. Si kila mtu mwenye laki mbili au tatu kwa safari ya saa nne kwenda na kurudi.

“Vipi unashukia wapi?” dereva alinizindua. “Naona uko mbali sana kimawazo,” aliongeza.

Nikapekecha macho yangu kwa kidole changu cha shahada kabla ya kumuuliza, “Kwani hapa ni wapi?”

“Tumeshapita Simbo. Hapa ni Kitawe. Baada ya hapa tunaingia Mayange. Toka hapo ni moja kwa moja hadi Kasulu, mwisho wa safari yetu.”

Sikujua nimjibu nini. Kwa kweli, sikujua hata mahala pa kushuka. Niliondoka nikiwa mdogo sana. Kumbukumbu nilizokuwa nazo zilionyesha kuwa hatukuwa mbali sana na mji wa Kasulu. Lakini udogo, mabadiliko makubwa ya mazingira na hasa kutoweka kwa misitu mingi ambayo ningeweza kuikumbuka kulifanya nisijue wapi pa kuanzia upelelezi wangu wa kutafuta chochote nitakachoweza kupata juu ya wazazi wangu.

Nadhani dereva alizisoma hisia zangu. Kwani alirahisisha kazi yangu pale alipouliza, “Yaelekea wewe ni mgeni sana huku?”

“Nadhani, maana niliondoka nikiwa mdogo sana. Hata sifahamu nianzie wapi kuwatafuta wazee wangu,” niliropoka bila kutegemea.

Kwa wakazi wa mkoa ambao hauna ajira za kutosha, ambao mkoloni aliutumia kama shamba la kuchukulia manamba wakakate mkonge huko Tanga na Kilimanjaro maelezo yangu hayakumshangaza dereva huyo hata kidogo. Alihitaji maelezo mafupi tu; niliondoka lini. Tulikuwa tukiishi wapi, ukoo wangu ni upi na mengineyo. Nilipomweleza juu ya hofu yangu juu ya vijiji vya Ujamaa alinielewa mara moja. Akanishauri nishuke katika kijiji kinachofuata, kinachoitwa Mayange, ambacho ni kikubwa na kilikusanya familia mbalimbali toka maeneo mengi.

“Walisema kingekuwa kijiji cha mfano kwa maendeleo,” alisema akicheka kwa kebehi. “Hebu katazame hayo maendeleo halafu utatuambia.”

Nikaafikiana na ushauri wake. Tulipofika Mayenge nililipa nauli yangu, nikateremka na kuanza kazi ya kutafuta ‘kwetu’.

Kama nilivyotegemea kijiji cha Mayange kilikuwa kinyume kabisa na matarajio ya awali kama ilivyokuwa kwa vijiji vingine vyote tulivyovipita njiani, Mayange ilitoa taswira ileile, umasikini unaonuka. Karibu watoto wote walichakaa miili na mavazi, wakifanya kazi ndogondogo kama kubeba mizigo ya wasafiri kwa mikokoteni yao ya miti au kuomba tu kwa wapita njia. Baadhi walivaa sare za shule. Lakini sare nyingi kati ya hizo hazikufanana kabisa na malengo ya wizara kwa kuchoka na kuchakaa.

Watu wazima nao walikuwa na yao. Wengi wao walikuwa taabani, suruali zikiwa zimejaa viraka, shati zikiwa zimepasukapasuka, miguu iliyokuwa peku ikiwa imebadilika rangi kutokana na vumbi jekundu lililowapiga pindi wakihangaikia mkono kwenda kinywani.

Waliahidiwa huduma muhimu kama barabara; hazikupata kujengwa au kukarabatiwa. Waliahidiwa maji ya bomba; hawakupata kuyaona. Waliahidiwa umeme; ilikuwa ndoto za mchana. Waliahidiwa huduma ya matibabu; sasa ilibidi kuyalipia kwa fedha ambazo huna. Kwa ujumla, ahadi zote zilizotumiwa ili kuwaondoa katika makazi ya baba na babu zao ziligeuka hewa. Jambo hilo lilifanya nyuso za kila mtu unayekutana naye zitangaze dalili zote za kukata tamaa.

Kazi ya kuitafuta familia moja, kati ya familia zaidi ya mia saba zilizohamishiwa hapo toka maeneo tofauti haikuwa ndogo. Nilitumia zaidi ya saa mbili kabla ya kumpata mzee mmoja ambaye alimfahamu babu, “Familia ya Kionambali, sio? Wala usihangaike. Wako humuhumu. Mtoto wake Karimanzira huwa namwona mara kwa mara.”

Nikapata matumaini. “Ni babu? Kionambali mwenyewe?” niliuliza.

“Huyo sina habari zake. Sijui kama bado yuko hai au tayari ametangulia,” mzee alinijibu. Laiti angejua kauli yake ilivyonishtua.

Nikiwa na matumaini mapya nilianza awamu ya pili ya kuwatafuta wazazi wangu. Zikiwa safari za mguu, katika kijiji kikubwa kisicho walao na jina la mtaa ilinichukua saa moja na nusu kabla ya kuonyeshwa kwa mbali nyumba iliyoaminika kuwa ya baba.

Ilikuwa nyumba iliyofanana na nyingine nyingi kijijini hapo; tofali za tope ambazo zilichakaa kabla ya kupata lipu, achilia mbali rangi. Juu nusu iliezekwa bati kuu kuu nusu nyasi. Sakafu ilikuwa ardhi ileile waliyoikuta palepale.

Nje ya nyumba hiyo alikuwepo bibi mmoja mchovu kama wengine wote kijijini hapo, akisuka ukili. Nilisogelea na kumwamkia. Kisha niliuliza kama hapo palikuwa nyumbani pa mzee Karimanzira. Swali langu lilimfanya bi mkubwa huyo ainuke na kunitazama kwa makini. Mara nikamwona akianza kutetemeka. Machozi yakianza kumtoka.

“Wewe ni Mtukwao!... Mwanangu! Umerudi…” alisema akinijia na kunikumbatia kwa nguzu zake zote.

Alikuwa mama! Mama yangu kipenzi! Fuko nililokuwa nalo mkononi lilidondoka pwaa, mikono yangu pia ikamkumbatia kwa nguvu. Masikioni nilisikia sauti nzito ya kiume ikilia! Kilio cha kwikwi. Ilinichukua muda kubaini kuwa ilikuwa ni mimi niliyekuwa nikilia.

Mara mzee mmoja akatoka nje ya nyumba hiyo. Alikuwa mchovu vilevile. Umbile lake refu lilipinda kwa mbele, ndevu zenye mchanganyiko na mvi zilimeza kidevu na kichwa chake kizima. Akitetemeka miguu na mikono yeye pia alinijia na kunikumbatia, machozi yakimlengalenga.

Baba! Amezeeka kabla hajapata kuwa kijana!

Dakika mbili tatu baadaye nyumbani palifurika. Watu waliotoka huko na huko walijazana kushangilia ujio wangu. Kila mtu alisema lake, ingawa mada ilikuwa ileile; Mwana mpotevu karejea!

Niliingizwa ndani, nikapewa kiti cha kifalme; kigoda cha baba. Fumba fumbua togwa tamu ikaletwa. Nikapewa kata kubwa iliyojaa. Kabla haijaisha nililetewa mihogo mitamu, huko nje nikiwaona vijana wakikimbizana na jogoo.

Baba na mama hawakubanduka ubavuni mwangu. Walikuwa na mengi ya kuniuliza mengi ya kunisimulia. Kwa bahati mbaya, hali haikuruhusu. Watu walikuwa tele, wakinishangaa kana kwamba nimetoka mwezini. Kelele pia zilishamiri. Watoto ambao hata sikuwafahamu walijipenyeza na kukaa miguuni mwangu, wakijitahidi sana kunikumbatia, walao miguu.

Kwa kweli sikutarajia mapokezi makubwa kama haya. Nikiwa mtu aliyepotea kwa zaidi ya miaka thelathini, mtu aliyerudi akiwa mikono mitupu kama nilivyokuwa, nilitarajia kupokelewa kwa kejeli au dharau. Si vicheko na kushangiliwa kwa takribani kijiji kizima kama ilivyokuwa. Hata hivyo, nilijihisi kama mtu aliyeutua mzigo mzito uliomlemea. Nilijihisi kama ambaye nilifutiwa madhambi yangu yote hata kabla ya kuomba radhi.

Kitu kimoja tu kilikuwa kikinisumbua. Mtu niliyetamani kumwona pengine kabla ya wengine wote hakuwa katika kundi la watu waliojitokeza kunilaki. Mtu huyohuyo nilihitaji sana kumwomba radhi kwa kumwamgusha katika matarajio aliyokuwa nayo juu yangu na kumpotezea hirizi yake muhimu. Nilimtegemea awe katika mjumuiko huo, aniite kando ambako tungeketi peke yetu na kuteta kama mtu na baba yake. Sikumwona. Wala sikuthubutu kuuliza harakaharaka kwa kuchelea kupewa jibu ambalo lingeweza kunitia ugonjwa wa moyo; Babu yake! Mbona alikufa zamani?

Kuku alikwishachinjwa na kupikwa. Ugali mweusi wa nyangwe uliletwa mbele yangu kwa kitoweo cha kuku huyo. Bila kuambiwa wageni walianza kupungua ili kuniachia faragha ya kufaidi chakula changu. Nilishindwa kujizuia. Kabla ya kumega tonge la kwanza nilimuuliza baba, “Babu yuko wapi?” nilisubiri jibu lake kwa hofu kubwa, moyo ukinidunda. Lakini nilipomwona baba akitabasamu kabla hajanijibu hofu ilitoweka moyoni mwangu.

“Babu yako kwani humjui?” baba alisema. “Aligoma katakata kuhama. Jeshi la polisi, jeshi la mgambo na hata sungusungu walishindwa kabisa kumtoa. Hivi sasa yuko peke yake ndani ya msitu mkubwa wa yaliyokuwa makazi yake. Kila wiki huwa nakwenda kumjulia hali.”

Nikapumua. “Bibi?” niliuliza.

“Yeye hatuko naye tena. Alitutoka miaka mitatu iliyopita. Alipatwa na ugonjwa wa malale uliokataa kila aina ya dawa.”

Ladha ya kuku ikaniishia palepale.

* * *​

“Nilijua utarudi salama… nilikuwa nikikusubiri… nisingeweza kufa kabla hujarudi, mjukuu wangu,” ilikuwa kauli ya kwanza ya babu mara aliponitia machoni na kunipapasa kichwani.

Sikuweza kuyastahimili machozi yaliyomiminika toka machoni mwangu. Babu alinikumbatia, huku mkono wake ukiendelea kunipapasa kichwani kwa namna ya kunibembeleza. Kitendo hicho kilizidisha uchungu moyoni mwangu na kunifanya nizidi kulia. Kwa mara ya kwanza, hakunishutumu kwa kitendo hicho. Niliinua uso na kumtazama kwa wizi. Yeye pia alilowa macho kwa machozi.

Babu analia, chuma cha pua!

Kwangu, alikuwa zaidi ya babu. Alikuwa kila kitu; baba, babu, rafiki, mwalimu na zaidi ya hayo. Hayo nilibaini na kuyahakikisha muda huo ambao mzee hataweza kustahimili kabisa kuficha udhaifu wake kwangu! Nitamsimuliaje malaika huyu kuwa jitihada zake zote za kupita mabonde, milima na misitu yenye hatari zote za dunia, hadi kunifikisha nchi ya Wahaya ili nipate elimu zilikuwa kazi bure? Nitaanzaje kumwambia kuwa ile hirizi yake, urithi pekee alioniachia ilipotea kwa uzembe? Niliteseka vibaya sana akilini nilipowaza hayo.

Nilikuwa nimemlazimisha baba alfajiri tu ya siku iliyofuata aniongoze kuja kumwona babu. Yeye akisisitiza kuwa ningepumzika walao siku mbili kabla ya kufanya safari hiyo. Jambo ambalo sikuafikiana nalo.

Kwa kutokuwa na uhakika wa kuwapata wazazi wangu, wakiwa hai nilifika nyumbani mikono mitupu. Hivyo, nilipopata fursa ya faragha ya kumkabidhi baba shilingi 50,000 kati ya zile laki moja nilizobakiwa nazo nilionekana shujaa mkubwa. Baba alianza mipango ya ‘kumaliza bati’ mama aliongea juu ya kulimisha shamba. Ilikuwa kama nimetoa milioni hamsini.

Tulimkuta babu akifunga mbuzi wake nje ya nyumba. Alivaa nguo zake zile alizozipenda, kaptula na shati nyeupe. Ziling’ara kama nilivyoziacha! Miguuni alitilia buti zake ambazo nazo ziling’ara kwa kiwi, ingawa zilianza kuchoka. Alikuwa peke yake katikati ya pori, isipokuwa kwa mifugo mingi ya mbuzi, kuku na bata. Watu wa pwani wangeweza kuapa kuwa ni jini jeupe linalokaa peke yake msituni. Babu alikuwa ametusikia toka mbali. Hivyo, alimfunga mbuzi yule harakaharaka na kusimama akitukodolea macho. Alipotuona alitukimbilia na kunidaka juujuu. Angeweza kunibeba… angeweza kunitia mweleka…. Babu alikuwa na nguvu zake. Ilikuwa kama ni binadamu pekee aliyebishana na uzee. Binadamu ambaye hakukubali kusalimu amri kwa kifo.

Pamoja na baba tulikuwa na vijana wengine wawili ambao nilielekezwa kuwa ni ndugu zangu. Vijana hao walipewa amri ya kumkamata beberu mkubwa kuliko wote na kumchinja. Akachunwa. Moto ukawashwa. Muda mfupi baadaye, tulikuwa tukimla mbuzi yule, wa kuchoma. Babu, akiwa na meno yake yote alitafuna mguu mzima wakati wengine tukishika shika hapa na pale.

Baadaye babu aliwataka baba na wale wenzetu wengine kuondoka kwa maelezo kuwa alikuwa na mengi ya kuzungumza na mjukuu wake faragha. Usiri wangu na babu halikuwa jambo geni kwa baba, toka utoto wangu. Hivyo, hakutia ubishi, walichukua nyama ya kula nyumbani wakaondoka zao kwa ahadi ya kunifuata kesho.

Nikapata wasaa wa kuchomoa zile elfu hamsini nilizobakiza na kumkabidhi babu. “Zawadi pekee niliyoweza kukuletea ni hii,” nilisema kwa masikitiko.

Babu hakuzipokea. Badala yake alicheka kabla ya kusema, “Sidhani kama nazihitaji. Za nini? Kaa nazo, zitakufaa wewe zaidi. Naamini bado unasafari nyingine ndefu, yenye mafanikio makubwa zaidi. Halafu, bado tuna mengi ya kuzungumza, mimi na wewe.”

“Bila shaka. Niliitikia.

“Miaka mingapi vile toka tumetengana?” Babu aliniuliza.

“Mingi sana. Ni aibu kuitaja.” Nilimjibu.

“Aibu ya nini? Mwanaume anayeonea aibu masaibu yake hafai. Kwa nini ufanye jambo ambalo utalijutia maishani mwako?”

Nilijua darasa la babu limeanza. Sikuwa tayari kwa darasa lolote wala somo lolote kabla ya kumtaka radhi. Hivyo nikajikongoja na kumwambia, “Babu ningeomba nianze kwa kukutaka radhi.”

“Radhi ya nini?”

“Hirizi.”

“Ilifanyaje?”

“Ilipotea!”

Nilitarajia babu abadilike, akasirike. Lakini kwa mshangao nilimwona akiachia tabasamu jembamba. “Nisubiri kidogo,” alisema akiinuka na kuingia ndani, aliporejea alikuwa na hirizi mkononi.

“Hirizi hii siyo?”

Niliitazama kwa makini. Nisingeweza kuisahau. Ilikuwa ileile!

Sikuyaamini macho yangu. Nikamkodolea babu macho ya mshangao.

“Hii ndiyo inayokusumbua?” babu aliongeza baada ya kicheko kingine. “Usiwe na wasiwasi. Ilipotea ikatafuta njia, ikarudi nyumbani kukusubiri.”

Bado sikuweza kuelewa. Hirizi hiyo ilipotea porini katika purukushani za kuikimbiza isianguke mikononi mwa padri. Yule kimbelembele, Byabato, alinihakikishia kuwa aliiokota tena na kumrudishia padri Backhove ambaye aliichoma, ikakataa kuungua. Kwamba baadaye ilitupwa baharini. “Ilifikaje kwako?” nikamuuliza.

“Ni hadithi ndefu. Ili kuifanya fupi pengine nikuambie tu kuwa ililetwa.”

“Na nani?” nilizidi kumbana babu.

“Na mizimu ya babu zetu.”

Bado nilikuwa sijamwelewa. Nikamwambia hivyo.

“Mizimu ina njia nyingi ya kuwalinda wahanga wake,” alifafanua. “Chochote kilichokutokea hadi hirizi hii kutengana nawe wahanga walikuwa wakiona. Ama kwa kujigeuza ndege, ama kwa kuwatuma ndege, hirizi hii ililetwa hadi katika mikono yangu.”

Babu alipoona kuwa bado sijaridhika na ufafanuzi huo aliamua kuwa wazi zaidi. Alisema kuwa jioni moja alikuwa akiwinda katika mwambao wa mto Malagalasi. Mara akaona kundi kubwa la ndege aina ya hondohondo wakitua hatua chache toka alipokuwa. “Walikuwa wengi. Kama elfu moja hivi. Waliponiona waliruka kunikimbia. Lakini mwenzao mmoja hakuweza kuruka. Alikuwa akipigapiga mabawa kwa nia ya kupaa lakini hakuweza. Nikamsogelea kuona kapatwa na nini. Nikabaini kuwa shingo yake ilikabwa na kamba nyeusi ambayo ilinasa kwenye kichaka cha mti. Nilipomshika ili kumkwamua ile kamba nilishangaa kuona kuwa ilikuwa hirizi ile niliyokupa. Nikaitoa na kumwacha ndege ambaye alipaa kuwaendea wenzake waliokuwa wakihangaika angani kumsubiri.”

Ilikuwa habari ya ajabu kwangu. Hirizi yangu, iliyopotea zaidi ya miaka thelathini iliyopita imerejea mikononi mwangu. Niliipokea, nikaipapasa. Ilikuwa ileile, kwa rangi na uzito. Kwamba imerudi mikononi mwangu halikuwa jambo la ajabu sana, ni namna iliyoifanya irudi ambayo kichwa changu hakikuweza kupokea.

Falsafa nyingi zilipita kichwani mwangu. Kama kweli ilitupwa ziwani bila shaka ingeweza kuoza. Kama hilo halikutokea ni wazi kuwa ilimezwa na samaki ambaye huenda alivuliwa na kuliwa. Kama ilikuwa hivyo hirizi itakuwa ilitupwa kama sehemu ya uchafu wa matumbo ya samaki wanayotayarishwa kwa ajili ya minofu kusafirishwa Ulaya na “mapanki” kuvamiwa na akina baba na mama ntilie. Inawezekana kuwa katika jitihada za kujitafutia chochote ndege yule alijikuta ameivaa hirizi ile na kuisafirisha bila kujua? Kama ni kweli kwa nini ailete hadi miguuni mwa babu?

Katika pitiapitia yangu vitabuni nilikuwa nimesoma mahala tabia za ndege. Moja ya tabia zao za ajabu ni ile ya kuhama au kusafiri safari za mbali kila ifikapo msimu fulani. Mara nyingi ndege hao wanaweza kusafiri safari za mbali toka Marekani au Ulaya hadi Afrika. Inaaminika kuwa wengi uhama katika vipindi vya hali fulani ya hewa na kurudi hali inapotengemaa. Inaaminika pia huko ambako huenda ndiko ambako ndege huzaliana na kurejea likiwa kundi kubwa zaidi. Inawezekana kabisa kuwa hondohondo aliyebeba hirizi yangu alikuwa katika msafara huo. Anaweza kuwa alikuwa akitoka zake Ulaya au nchi za Kiarabu na kuelekea Afrika Kusini!

Babu alikuwa kama anayeyasoma mawazo yangu. Alikohoa kidogo kabla ya kusema, “Naona na wewe tayari umeambukizwa yale maradhi yenu.”

“Maradhi gani?

“Maradhi ya kisomi. Naona unavyoona shida kuamini kuwa mizimu ya babu wa babu zako imekurejeshea hirizi hii! shauri lako. La msingi ni kwamba hirizi yako imerejea na tangu leo utaivaa tena. safari hii milango yote uliyoshindwa kuifungua itafunguka,” alisema akinivisha hirizi hiyo na kisha kunitemea mate kichwani na kifuani.

“Kuna jambo la pili.” Alisema akiinuka tena na kurudi ndani. Aliporejea alikuwa na bahasha tatu mkononi. Alinikadhi. Ilikuwa barua. Juu ziliandikwa jina lake na anuani ya kijiji chake. Ilielekea barua hizo zilitoka nje ya nchi, kwani stempu zote zilikuwa na picha ya malkia au wafalme wazungu, muhuri ukisomeka waziwazi “Stockholm-sweden”. Tarehe kwenye mihuri hiyo zilionyesha kuwa zilitumwa zaidi ya miaka kumi na mitano iliyopita!

“Barua!” Niliropoka.

“Ndiyo,” babu alijibu “Mbona hazijafunguliwa? Ni za zamani sana,” nilisaili.

Babu naye akaonyesha mshangao wake kwangu, “Mjukuu wangu, zinalekea kuwa ni barua muhimu sana. Unadhani ningeweza kumpelekea mtu yeyote asome siri zangu na kuanza kunitangaza? Nilikuwa nakusubiri, nilijua ungerudi salama.”

“Ni wewe peke yako utakayekuwa wa kwanza kuelewa chochote kilichoandikwa humo.”

“Zilifikaje hapa?” Niliuliza nikianza kufungua moja niliyoiona ya zamani zaidi.

“Zililetwa. DC alileta kwa mkono wake mwenyewe. Alinishawishi kufungua lakini nilikataa katakata.”

Baada ya maelezo hayo babu alikunjua kiti chake cha uvivu, kilichotengenezwa kwa ngozi ya nyati na kujilaza kimya kwa namna ya kunipa wasaa wa kusoma barua hizo kwa tuo.

Barua ya kwanza ilikua ndefu kidogo. Ilianza kwa salamu za siku nyingi, ikaendelea kwa taarifa ya kuipongeza kazi yake alipokuwa nchini humo, “Tumetengeneza filamu mbili za ile michezo uliyoshiriki kuicheza. Filamu hizo zimependwa sana Ulaya nzima zinanunuliwa kama peremende. Taarifa tuliyoichapisha hapa chini ni malipo yako ya mrabaha hadi sasa. Tunaomba ufanye kila uwezalo kuwasiliana nasi ili upokee malipo yako,” ilieleza barua hiyo.

Sehemu ya pili ya barua hiyo ilikuwa na mahesabu ya idadi ya mikanda iliyouzwa na televisheni zilizonunua hakimiliki na hakishiriki. Kwa hesabu za harakaharaka asilimia ya babu ilionyesha kama dola 227,000. Sikuyaamini macho yangu. Nikainua macho kumtazama. Alikuwa amesinzia, tabasamu likiwa mdomoni.

Nikafungua barua ya pili. Hii iliandikwa mwaka mmoja baadaye. Ilisisitiza, umuhimu wa babu kwenda haraka au kumtuma mrithi wake yeyote anayeaminika. Iliongeza kuwa iwapo kuna tatizo lolote la vitambulisho mwakilishi huyo alichotakiwa ni kwenda na ile hirizi ambayo ilikuwa haibanduki shingoni mwake. “Benki yetu tayari imearifiwa juu ya hilo. Usiwe na wasiwasi,” iliongeza barua hiyo.

Barua ya tatu iliambatanishwa na hundi. Hesabu zilizoandikwa juu ya hundi hiyo zilinitatanisha dola 812,000! Barua ilisisitiza fedha hizo kuchukuliwa. Ikiongeza kuwa benki yao tayari imefungua matawi nchini katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza, haikuwepo haja ya kusafiri hadi Ulaya tena.

Mara nikaanza kupata njozi za mchana. Nilijiona nikiandika kitabu, ambacho kiliyahusu maisha yangu mwenyewe. Niliyaumba na kuyaumbua matukio, mikasa na visa vyote vilivyonikumba toka katika safari zangu kuu mbili safari ya kimaisha iliyonifikisha kila pembe ya nchi na ile ya kimaumbile ambayo ilinitoa utotoni na kuniingiza ukubwani. Nilihisi hata jina la kitabu likinijia akilini; Kiguu na Njia.

Zikanijia njozi nyingine. Katika njozi hizi nilijiona nikiwaelekeza watu wa masuala ya filamu wapi pa kuelekeza kamera zao, katika filamu niliyokua nikiitengeneza. Niliwataka ihusishe maeneo yote muhimu ya nchi yetu, mbuga za wanyama, maziwa na mito yote ambayo haikupata kutangazwa vizuri. Kwa njozi niliona mikanda ya filamu hiyo ikigombewa na kuwafanya watazamaji waone hazina kubwa iliyosahauliwa ambayo walijaliwa na Muumba.

Nikaona jinsi nilivyokuwa nikiishi na mke wangu Nashifa kwa furaha. Watoto wetu wawili wenye afya njema wakicheka na kufurahi…

Halafu nikamkumbuka mwenye fedha zake, ambazo zingeniwezesha kufanikisha ndoto hiyo. Nikageuka.

“Babu!” niliita tena nikimtazama.

Alikuwa bado amelala vilevile kwenye kiti chake cha uvivu. Tabasamu lake lilikuwa bado limesahauliwa palepale usoni kama mtu aliyekuwa katika dimbwi la starehe. Niliinuka na kumshika bega. Nikamtikisa taratibu, baadaye kwa nguvu kidogo, “Babu… babu… babu…!”

Kimya! Kimya!

Nikashtuka. Alikuwa kama hapumui! Nikamshika kifua kusikiliza mapigo ya moyo. Hayakuwepo. Hata mwili wake tayari ulikuwa umepoa. Ndio kwanza nikabaini kuwa babu hatukuwa naye tena duniani! Tabasamu lake lililobakia palepale kama ishara ya ushindi kwa jambo zito lililokuwa likimsumbua kwa muda mrefu.

Nilitetemeka mwili mzima. Nguvu zikaniishia, furaha, faraja na matumaini makubwa niliyoyapata mara baada ya kuisoma barua yake, ikatumbukia nyongo.
 
Natanguliza shukrani wapendwa, nimefikia mwisho wa riwaya hii lakini kwa sababu kadha wa kadha, nimelazimika kuiondoa baadhi ya vipande ili kukwepa wezi wa kazi za watu. Kwa comment yoyote ushauri tafadhali usisite kuitupia hapa. kwa wale wanaohitaji vitabu vya Mtobwa tafadhali tupigie kwa namba 0712504985.
 
Natanguliza shukrani wapendwa, nimefikia mwisho wa riwaya hii lakini kwa sababu kadha wa kadha, nimelazimika kuiondoa baadhi ya vipande ili kukwepa wezi wa kazi za watu. Kwa comment yoyote ushauri tafadhali usisite kuitupia hapa. kwa wale wanaohitaji vitabu vya Mtobwa tafadhali tupigie kwa namba 0712504985.
Ndio hadithi imefika tamati?
 
Natanguliza shukrani wapendwa, nimefikia mwisho wa riwaya hii lakini kwa sababu kadha wa kadha, nimelazimika kuiondoa baadhi ya vipande ili kukwepa wezi wa kazi za watu. Kwa comment yoyote ushauri tafadhali usisite kuitupia hapa. kwa wale wanaohitaji vitabu vya Mtobwa tafadhali tupigie kwa namba 0712504985.
asante saana kwakweli ni kama iendelee hivi mkuu amna part 2 yake like ?
 
SURA YA ISHIRINI NA TANO

Tanganyika, Ziwa Lenye neema

Nadhani nilikuwa mtu wa kwanza kufika Stesheni kati ya wasafiri wa siku hiyo. Nilinunua magazeti mawili ya Kiswahili, moja la Kiingereza na kuketi kwenye lile benchi la mbao kujisomea. Kama kawaida zilikuwa habari zilezile za kukatisha tamaa; Mzee ajinyonga kwa madeni; Msichana akamatwa kwa kutupa kichanga jalalani; Achomwa moto kwa kuiba fuko lenye nepi za mtoto, na nyingine kama hizo. Kurasa za mbele zilipambwa na habari za wakubwa; Rais aenda Uingereza; Waziri Mkuu akutana na Balozi mpya Japan; Hotel mpya kujengwa ufukoni. Upande wa michezo nao ulitawaliwa na habari za vilabu vilevile ambavyo nimekuwa nikivisikia toka mwaka wa 47; Yanga yasajili kinda; Simba kwenda mahakamani; Ligi kuu yahairishwa na kadhalika na kadhalika.

Ziko wapi habari za vijijini? Nilijiuliza. Nilikua na kiu kubwa ya kufahamu chochote juu ya vijiji. Moja ya habari kubwa iliyonigusa sana nilipokuwa gerezani ni ile ya operesheni ya vijiji vya Ujamaa, kwamba serikali ilikuwa imeamua watu wote waende katika vijiji vilivyopimwa kwa ajili ya kupatiwa huduma muhimu za kimaendeleo kama maji, barabara na zahanati. Kwa machache tuliyosikia huko gerezani operesheni ilileta songobingo kubwa kwa wananchi, kiasi kwamba baadhi waliliwa na wanyama wakali huko porini walikohamishiwa, baadhi walidaiwa kujinyonga wakipinga uamuzi huo.

Mimi nilikuwa mmoja kati ya waathirika wa maamuzi hayo. Kwa jinsi ukoo wangu ulivyojitenga, toka mababu na mababu na kujenga nyumba kandokando ya mashamba yetu, kwa vyovyote vile tungekuwa waathirika wa kwanza katika operesheni hiyo. Safari hii ya kurudi nyumbani ilinitatiza kwa hilo. Sikujua wazazi wangu watakuwa wamehamishiwa wapi. Sikuwa na mawasiliano ya aina yoyote nao. Hivyo, sikujua nitaanzia wapi niishie wapi katika kuwatafuta. Kwa bahati mbaya, vyombo vya habari havikutoa walao fununu juu ya hilo.

Wasafiri walianza kufurika Stesheni hapo. Mmoja wao akiwa yule mama wa Kizungu na lundo lake la mizigo. Aliponiona alitabasamu, akanifuata. Nilimsaidia kuweka mizigo yake vizuri, kabla hajaketi na kuniuliza habari za usiku uliopita.

“Ulipata mahali pa kulala?”

“Naam,” nilimjibu.

“Mjini hapahapa?”

“Hapana. Nje kidogo ya mji.”

Alisita kidogo kabla hajageuka na kuniuliza tena, “Unajua jana hatukuambiana majina? Mie naitwa Jane, Jane Goodhall.”

Jane! Halikuwa jina geni sana masikioni mwangu. Nilipata kulisikia mahala. Wapi vile, sikuweza kukumbuka mara moja. “Nimepata kulisikia jina hilo, lakini sikumbuki wapi,” nilimwambia.

“Bila shaka.” Alijibu. “Nimepata kuandikwa mara nyingi katika magazeti na majarida yanayojihusisha na masuala ya maliasili hasa wanyama pori. Nipo Kigoma katika hifadhi ya Gombe. Najihusisha na utafiti wa sokwe,” alifafanua.

“Bila shaka!” nilitamka kwa furaha. “Uko Gombe, kilometa zipatazo kumi na tano hivi, mwambao wa ziwa Tanganyika kuelekea kaskazini, sawa?”

“Naam,” alikubali, kiasi akiwa ameshangaa. “Kwa kweli, ni mwendo wa kilomita kumi na sita.” Aliongeza.

“Uko na mtu anayeitwa Hugo Van Lawick. Mpiga picha za wanyama ambaye ametengeneza filamu nyingi za wanyama,” niliongeza.

Mama huyo alizidi kushangaa, “Ni kweli kabisa. Hugo ni mume wangu. Alinikuta kule wakati naendelea na kazi yangu, yeye akifanya yake. Tukapendana, tukaoana. Umejuaje yote hayo?” aliniuliza.

“Nasoma sana. Nasikiliza redio. Habari za wanyama siku zote hunivutia sana. Habari zako za sokwe nimekuwa nikizifuatilia kwa karibu. Umekwishajua lugha yao?”

Jane alicheka. Kisha akafafanua, “Sokwe, kama wanyama wengine hawana lugha. Wanawasiliana kwa ishara tu ya sauti na miili. Mimi wamenikubali baada ya kunizoea. Tunaelewana nao. Lakini mnyama ni mnyama tu.”

Wakati akimzungumzia sokwe niliona jinsi Jane alivyobadilika. Macho yake yaling’ara, sauti yake ikiwa wazi zaidi. Ilikuwa dhahiri kuwa mapenzi ya mama huyu kwa sokwe hayakuwa na kifani.

Haikuwa uongo. Historia fupi niliyokuwa nayo juu ya msichana huyu ni kwamba alikuwa ameingia katika misitu hiyo ya Gombe mara baada ya uhuru, akiwa mdogomdogo tu, ndio kwanza amemaliza elimu ya sekondari. Jane alifanya maajabu kwa kuweza kuishi peke yake msituni, akiwafuata sokwe kila wanapokwenda, wakati mwingine akilala nao porini, hadi wakamzowea. Alifungua kituo maalumu ambapo sokwe huja na kupata mahitaji yao hasa ndizi ambazo walizipenda sana. Jane aliweza kumfuatilia sokwe toka anazaliwa, anakua, anabalehe hadi naye anapata mtoto, alinukuu mwenendo na tabia zao, chakula chao, tiba zao na hulka zao mmoja baada ya mwingine. Alimfahamu kila sokwe na kila familia ya sokwe vilivyo, kiasi cha kujua nani kiongozi wao, nani anapinduliwa uongozi na nani kapindua. Utafiti makini wa aina yake duniani ambao tayari umempatia shahada ya udaktari.

“Unajua hujaniambia jina lako?” Alinizindua.

“Naitwa Petro Mtukwao Kionambali,” nilimjibu.

Jane alifahamu Kiswahili kidogo sana. Kati ya machache aliyoyafahamu jina la ‘Mtukwao’ au ‘Kionambali’ lilimpa maana fulani, lakini hakuweza kuifafanua mara moja. Aliyataja majina hayo mara mbili tatu, akikosea, kabla hajakata tamaa na kuniuliza maana yake, “Petro bila shaka ni Peter kwa Kiingereza. Ni jina lenye asili ya Kigiriki likiwa na maana ya mwamba au jabali. Hii Kionambali au Mtukwao ina maana gani?”

Jane alinitazama , “Ni la Kiebrania,” nilimjibu. “Lina maana ya Mungu ni mwenye fadhila sio?” nilimuuliza kabla ya kumjibu.



Jane alionyesha mshangao. Nadhani hakutegemea kuwa pamoja na hali niliyokuwa nayo ningeweza kufahamu mambo mengi kama ilivyokuwa. “Ni kweli kabisa,” alijibu baada ya tabasamu fupi, “Kiona mbali?” alisisitiza.

Wazazi wangu hawakupata kuniambia maana hasa ya majina yangu. Nadhani yalitolewa na babu kwa sababu zake. Hata hivyo nilimweleza Jane hili na lile juu ya maana ya majina hayo.

Sidhani kama aliridhika. Mara nilimwona akibadilika ghafla kama mtu aliyekumbuka jambo “Kionambali…. Mtu kwao… nadhani nilipata kuyasikia majina hayo kabla ya leo,” alisema.

Nikacheka.

“Unacheka nini?”

“Nina hakika hujawahi kulisikia mahala popote. Ni jina dogo sana katika nchi hii. Sijawahi kuandika kitabu wala kucheza mpira hata nijulikane.”

“Hapana, nimelisikia likitajwa. Si mara moja si mara mbili,” alisisitiza.

Sikuamini. Nikijua kuwa alitokea kwao Uingereza, akakaa Kenya kwa muda kabla ya kuja nchini sikuona vipi angeweza kukutana na jina langu. Hasa ikizingatiwa kuwa muda mwingi nilikuwa gerezani.

“Unakwenda wapi?” alinihoji.

“Kigoma.”

“Nyumbani kwenu?”

“Ndiyo.”

“Kwa hiyo, safari yetu moja.”

“Bila shaka.”

Alisita kwa muda kabla hajauliza swali jingine, “Kwa hiyo, unakwenda likizo?”

“Ndiyo na hapana,” nilimjibu.

“Una maana gani?”

“Nina maana kuwa ndiyo nakwenda nyumbani; hapana siendi likizo.”

Jibu langu lilimshangaza Jane, “Kwani unatokea wapi?”

Sikuona sababu ya kumficha, “Jela.”

Kiasi nilimwona akishtuka. Lakini, akiwa mwanamke mwenye roho ya chuma, anayeweza kuishi na kuvumilia hasira za ghafla za wanyama hatari kama sokwe, alijirekebisha mara moja. Badala yake aliniuliza kwa upole, “Nini kilitokea?”

Alikuwa binadamu wa kwanza uraiani aliyetaka kujua masaibu yangu toka nilivyofungwa hadi kufunguliwa. Akawa binadamu wa kwanza niliyepata kumsimulia, kwa tuo, yote yaliyonitokea hadi nikatupwa gerezani kwa miaka mingi. Sijui kwa nini niliamua kuwa wazi kwake. Nadhani ni kwa kuwa sikuwa na shaka kuwa ni mtu mwenye huruma sana. Kama anaweza kuishi na sokwe, vipi binadamu mwenzake?

Nilipofika sehemu ambayo nilimtaja Dakta Leakey kama mwajiri wangu pekee ambaye niliishi naye kwa muda mrefu nilimuona Jane akishtuka. Mara akanikatiza kwa kuuliza, “Leakey yupi?”

“Leakey unaemjua wewe. Na mke wake Mary… wagunduzi wa fuvu la kale zaidi nchini,” nilimjibu.

Jane aliinuka na kunikodolea macho ya mshangao. “Sasa nimefahamu wapi nilisikia jina lako kwa mara ya kwanza,” alisema baadaye.

“Wapi?”

“Kwa akina Leakey. Walikuwa hawaachi kukutaja. Walishangazwa sana na kutoweka kwako ghafla, bila kuaga, mtu ambaye walidai kuwa walimtegemea sana katika shughuli zao.”

Ikawa zamu yangu kushangaa, “Unawafahamu?”

“Vizuri sana,” Jane alinijibu. “Walipata kuniajiri pia. Kutokana na mapenzi yangu kwa wanyama na mazingira Leakey alinishawishi kwenda kwenu Kigoma kufanya utafiti wa wanyama wale, binamu zetu.”

Sikuwa na la kusema, nikauliza, “Hawajambo?”

“Nani?”

“Akina Leakey.”

Jane akacheka, “Wazima sana. Kwa nini ulifanya vile?”

“Kufanya nini?”

“Kufungwa. Kukubali kufungwa bila kuwaarifu. Wangeweza kukusaidia.”

Ilikuwa wazi kuwa Jane hajui maana ya kufungwa, hasa katika nchi zetu za dunia ya tatu. Mnyama anayefugwa ana uhuru mara mia zaidi ya mfungwa.

Wakati nikizungumza na Jane nilimwona msichana mmoja, msafiri kama sisi, akinitazama sana. Nilimtupia macho. Nikamwona akiyakwepa macho yangu kwa namna ya haya kiasi. Kitu fulani kilinifanya nipate hisia kuwa namfahamu. Wazo ambalo nililipuuza mara moja. Jana tu nimetoka jela, nitamjulia wapi msichana huyu?

Kitu kimoja kilinivutia kumtazama msichana huyu alikuwa ana tofauti kubwa na wasichana wengine wengi niliowaona jijini hapo. Alikuwa Mwafrika halisi. Nywele zake zilikuwa fupi, ambazo hazikupata kuathiriwa na madawa. Ngozi yake laini maji ya kunde, pia haikuwa na dalili zozote za kuathiriwa na madawa hayo. Hata mavazi yake yalikuwa ya heshima. Gauni jekundu lililomkaa vizuri lilimfunika hadi miguuni.

Lakini kuna kitu cha ziada ambacho kilinivutia zaidi kwa msichana huyu. Halikuwa umbile lake wala mavazi yake. Kilikuwa kitu fulani. Kwa bahati mbaya sikuweza kubaini mara moja ni kipi hasa kilichonivutia zaidi kwake. Ningeweza kukisoma kitu hicho katika macho yake, lakini tayari aliyakwepa macho yangu na kutazama upande mwingine.



Honi ya treni iliyokuwa ikiingia stesheni iliniokoa kujibu swali la Jane pamoja na kuendelea kusumbua fikra zangu juu ya msichana yule. pilikapilka za kuingia katika mabehewa zikaanza. Mimi nikiwa sina mzigo wowote nilifanya kazi ya kumsaidia kupakia vitu vyake katika chumba cha daraja la pili alicholipia. Mimi, nikiwa sina namba ya kiti, nilipata debe moja la msafiri mwenzangu na kulikalia. Roho yangu ilipumua pale dakika ishirini baadaye treni ilipoanza safari ya kuelekea bara.

Jing... jang… jing… jang… tuliuacha mji na kuingia Buguruni. Jing… jang… jing… jang … vingunguti. Jing… jang… jing… jang… Karokota. Taratibu tukauacha mkoa wa Dar es Salaam na kuingia Pwani. Tulizipita stesheni za Soga, Ruvu na Magindu kabla hatujaiacha Pwani na kuingia Morogoro katika stesheni za Kidugalilo, Ngerengere, Mikesa na hatimaye Morogoro mjini.

Wakati huo usiku ulikwishaingia. Sikuweza kuziona vizuri stesheni za Mkata, Kimamba na ile ya Kilosa. Toka hapo tuliingia stesheni ya mpaka wa Morogoro na Dodoma, Kidete kabla ya kufika Godegode, Gulwe na Kikombo. Tulifika Dodoma alfajiri ya siku ya pili.

Jane alikuwa akinitafuta. Alinikuta nikiwa nimeegemea mlango nikijaribu kupata chochote ambacho ningeweza kupata juu ya mji wa Dodoma, makao makuu ya serikali baada ya kuhamishwa toka Dar es Salaam. Zaidi ya majengo kadhaa, barabara pana zaidi na watu wa kutosha zaidi bado Dar es Salaam niliyoiacha jana ilifanya Dodoma ionekane kama mzaha kuiita makao makuu.

“Unajisikiaje?” Jane aliniuliza

“Safi kama chuma cha pua,” nilimjibu

Akacheka. “Twende tukapate kifungua kinywa,” aliniambia.

“Wapi?”

“Mgahawa wa humu ndani.”

Nikamfuata. Tulipita mabehewa kadhaa kabla ya kufikia behewa la chakula. Tukaketi. Aliagiza chapati mbili, supu ya kuku na chai kwa kila mmoja wetu. Kwangu ulikuwa mlo ambao sitapata kuusahau kwa muda mrefu. Toka nilipopata chai na maharage ya ‘mama ntilie’ kula Manzese tumbo langu lilikuwa halijaonja chakula zaidi ya karanga za mia moja nilizonunua humo ndani.

Tulikula taratibu. Kila mara Jane akinidodosa juu ya mipango niliyokuwa nayo baada ya kutoka gerezani. Hakunielewa pale nilipomwambia kuwa nilikuwa na mpango mmoja tu katika akili yangu, ambao haukuwa ziadi ya kufika nyumbani, kumwona babu na wazazi wangu, kama wako hai.”

“Bila shaka ulitoka kwenu mikono mitupu… unataka kurudi mikono mitupu?” alinihoji.

“Sina jinsi.”

“Kwa nini?”

Asingeweza kuelewa. Asingeelewa hata kidogo hata kama ningemwelewesha vipi. Kwamba lazima nikaombe radhi kwa kupoteza hirizi! Kwamba nina hakika mikosi na balaa nyingi ninazopata zilitokana na kuipoteza baraka ile, hivyo lazima nioshwe kwa kutemewa mate usoni. Mzungu, mwenye utamaduni tofauti na wangu angeelewaje? Sikujisumbua kumwelewesha.

Jane akaamua kuifichua siri iliyokuwa moyoni mwake. Alinitaka twende wote Gombe nimsaidie kazi. Kwamba alikuwa na mipango ya kufungua kituo kingine cha sokwe kusini mwa ziwa Tanganyika, katika milima ya Mihale, kilometa zipatazo 120 toka mjini Kigoma. Kwa mujibu wa Jane milima hiyo ilikuwa na sokwe waliokadiriwa kuwa 700 katika makundi kama kumi na mitano. “Siwezi kufanikisha peke yangu. Lazima niwe na mtu mwaminifu, mwadilifu na pia tunayeelewana lugha vizuri,” alisema

“Halafu,” aliongeza. “Mume wangu ana mpango wa kutengeneza filamu kubwa, itakayojumuisha vivutio mbalimbali vya Tanzania. Kwa historia yako na uzoefu wako hakuna mtu ambaye atamfaa zaidi yako.”

Hili la pili lilinivutia zaidi. Ningependa sana kuwa sehemu ya historia ya mtu atakayefanikisha kazi hiyo. Lakini nilikwishajiwekea nadhiri ya kutojihusisha na jambo lolote kabla ya kufika kwetu. Ama niwaone wazazi wangu, ama niyaone makaburi yao.

Nilimweleza hivyo Jane. Bado hakunielewa. Lakini hilo lilikuwa tatizo lake, halikuwa langu.

Safari ya mchana ilivutia zaidi. Tulisimama dirishani mimi na Jane tukiangalia nje, kituo baada ya kituo. Nkungu, Nala, Bahi, Kintinku, Saranda, hatimaye tukaingia Manyoni. Watu na mazingira maeneo yote haya havikunifurahisaha sana. Ardhi ilijaa vumbi, mtu mmoja hapa na pale. Hali iliyonifanya hisia za nusu jangwa zinijie akilini. Hali kadhalika hali za wakazi wengi iliashiria umasikini mkubwa. Mavazi ambayo wengi wao walivaa, baadhi wakitembea bila hata kandambili. Ilikuwa dalili tosha ya umasikini. Hata wale waliokuwa na bidhaa, bidhaa zao ziliashiria kuganga njaa tu. Mtu mzima akiwa na vichane vitatu vya ndizi, mwingine akiwa na chupa moja ya asali, yule sinia la karanga! Kwa gari moshi ambalo hupita hapo mara mbili tatu kwa wiki sikuona kama biashara hizo zilikuwa na namna yoyote ya kuwaondoa katika vibanda vya tembe tulivyokuwa tukiviona toka tunaingia Dodoma hadi tunaiacha.

Stesheni ya Manyoni ilishamiri kwa biashara ya kuku, walio hai kwa waliokaangwa. Takribani kila mtu alikuwa na sinia yenye mapaja ya vidari vya kuku wanaotamanisha kuwala. Bila shibe ya mlo alionipa Jane ningejikongoja kununua paja moja. Ingawa baadhi ya watu hudai kuwa hawa si kuku wa kawaida kwa ajili ya wingi wao. Wanadai baadhi ya tunaowadhania kuku waliokaangwa ni kunguru na ndege wengine wa porini waliozagaa katika maeneo hayo. Kwa kweli, ulikuwa mzaha wa watani wa Wanyaturu na Wanyiramba.

Toka Manyoni tuliingia Itigi, kaskazini hadi Malingwe. Jua likaanza kuzama. Jane alirudi chumbani kwake kujisomea kitabu mimi nikaendelea kuranda ndani ya mabehewa hayo mengi. Tukafika Nyama, tukaingia Igagula. Saa mbili za usiku tulifika Tabora. Hapo tulichukua muda mrefu kutokana na pilikapilika nyingi za kubadili mabehewa, kukagua vichwa vya treni na pengine kufanya ukarabati.

Nilitamani kuutumia muda huo kuchepuka kidogo nikautupie macho, walao kidogo mji wa Tabora, ambao uko kidogo nje ya stesheni hiyo. Hata hivyo kwa kuchelea kuachwa sikuthubutu. Niliishia kuchungulia tu nje ya stesheni ambako niliiona ile miembe iliyozeeka lakini bado ilikuwa ikipamba na kuzaa embe tamu za dodo na bolibo.

Niliona pia kundi kubwa la mbuzi wasio na mlinzi wakirandaranda kando ya barabara hiyo. Mbuzi wa Tabora? Nilijiuliza nilipokumbuka simulizi ya mji wa Tabora kuwepo na mbuzi wengi wasio na mmiliki ambao hutembea ovyo mitaani bila kubugudhiwa, mbuzi ambao inaaminika kuwa kwa namna moja au nyingine wanahusiana na ama ushirikina ama laana fulani. Mwenyewe alifariki zamani na kufanya wawe hawana mwenyewe, lakini kila mtu ambaye huthubutu kuwala hudhurika na hata kupoteza maisha. Jambo ambalo lilisababisha hata wezi wa mjini hapo wawaogope.

Honi ya kuashiria safari ikapigwa. Nikarudi au kuparamia behewa lolote lililokuwa karibu. Dakika tano baadaye safari ikaanza. Ilikuwa awamu ya mwisho ya safari hiyo ndefu ya kilometa 2600 toka Dar es Salaam hadi Kigoma.

Hamu niliyokuwa nayo ya kufika nyumbani ikaanza kuingia nyongo. Hofu ikaanza kuchukua nafasi. Hofu ya kutojua lipi nitalikuta huko nyumbani. Habari za kufurahisha au kuhuzunisha, heri au shari. Hali kadhalika, aibu ya kurudi mikono mitupu kama nilivyoondoka, baada ya miaka nenda rudi ya kuhangaika pia ilinitesa sana. Sio siri, nilitamani garimoshi hilo lipate ajali, mtu mmoja tu apoteze maisha; Petro Kionambali.

Haikuwa. Treni iliendelea kukata mbuga. Ikiwa safari ya usiku sikuweza kuona mabadiliko ya ardhi toka ile ya nusu ukame. Ya Dodoma hadi Tabora hadi ile yenye rutuba nyingi ya kutokea Tabora hadi Kigoma. Kelele za wasafiri kila tulipofika stesheni ndizo ziliniashiria tuko wapi; Usoke, Kaliua, Suinge, Malagalasi, Uvinza, Simbo, Luiche na hatimaye Kigoma

Ulikuwa mkesha wa aina yake. Pilikapilika za kuingia katika mabehewa kila stesheni zilikuwa kubwa na za fujo kubwa. Mizigo ilirushwa ndani ikifuatiwa na wababe; wake kwa waume. Ilikuwa rahisi kwa mgeni kufikiria kuwa watu wa Kigoma wana asili ya vurugu. Lakini kamwe mwenyeji asingeweza kufikiria hivyo. Watu hawa hawakuwa na njia nyingine yoyote ile ya usafiri. Maeneo mengi hayakuwa na barabara iliyowaunganisha na upande mwingine wa dunia zaidi ya treni. Hivyo, kuachwa na usafiri huo kulimaanisha kuharibikiwa kwa mipango yako ya safari pengine kwa wiki nzima au zaidi. Hivyo, kutumia nguvu na ubabe lilikuwa jambo la lazima.

Tulifika Kigoma saa moja na nusu za asubuhi, lakini kwa sababu za kijiografia ndio kwanza jua lilikuwa likichomoza. Miale yake ilipenya milima ya Bangwe na kutuangazia pale stesheni, kando kabisa mwa Pwani ya ziwa Tanganyika. Ziwa ambalo liliupokea mwanga huo, likaujumuisha na maji yake yasiyo na rangi na kufanya limeremete kwa mchanganyiko wa nuru ya rangi ya dhahabu toka angani na buluu toka katika lindi la maji na kutoa sura ya kusisimua sana.

Nilishuka na kusimama kwa muda hapo nje nikitazama huku na kule kana kwamba siamini kuwa nimerejea nyumbani. Macho yangu yalivutwa na jengo imara la stesheni hiyo, lililojengwa na Mjerumani toka enzi zile. Zaidi ya ukarabati wa rangi na pengine bati jengo lile lilikuwa imara kama walivyoliacha. Wala halikuwa na dalili zozote za kupoteza uimara wake katika siku za usoni.

Nikahamisha macho kwenye jengo na kuyatupa ziwani. Kwa mbali, niliweza kuona mitumbwi na mashua za wavuvi wakirejea Pwani baada ya shughuli zao za usiku kucha, lakini kilichovutia zaidi macho yangu ni meli kubwa, yenye rangi nyeupe iliyotia nanga katika bandari hiyo. Jina lake liliweza kusomeka hapo niliposimama, MV LIEMBA.

Hii ni mali yenye historia ya pekee duniani. Kwanza, inaaminika kuwa ni meli ya kale kuliko zote duniani ambayo bado inafanya kazi. Pili, imezitumikia enzi zote muhimu za historia ya Tanganyika ikiwa imeletwa na kuunganishwa na Wajerumani miaka ya 1914 na kupewa jina la Graf Von Goetzen. Mjerumani alipozidiwa katika vita ya pili aliizamisha katika lindi la ziwa Tanganyika wa nia ya kumkomoa Mwingereza aliyechukua madaraka. Lakini wao walifanya kila jitihada kuiibua majini na kuitengeneza. Ikaanza kazi kwa jina jipya la SS Liemba. Tanganyika ilipopata uhuru wake Liemba ilikarabatiwa tena na mitambo yake badala ya kutumia mvuke ikawa ikitumia dizeli, hivyo ikaitwa MV Liemba. Meli hiyo hadi sasa ni tegemeo kuu la usafiri katika mwambao wa ziwa Tanganyika hadi bandari za Mpulungu Zambia, Bunjumbura, Burundi na Kelemie Kongo.

Upande wa pili wa ziwa hilo macho yangu yalivutwa na baadhi ya milima ya nchi hizo. Burundi kwa upande wa kaskazini na Kongo ilionekana mbele yangu, magharibi ya nchi yetu. Hali ya hewa ikiwa safi, anga likiwa angavu niliweza kuiona milima ya nchi hizo kwa uwazi kabisa.

Sijui ningesimama hapo kwa muda gani kama nisingeshikwa bega na nilipogeuka nikakutana na uso mpole wa yule msichana aliyenivutia pale stesheni ya Dar es Salaam. Sura yake ilikuwa iliyojaa haya. Hata hivyo, alijitahidi na kuniuliza kwa sauti yake ya upole, “Samahani kaka. Hivi unaitwa Petro Kionambali?”

“Naam,” nilimjibu.

“Ulipata kuishi katika maeneo ya Bonde la Ufa?” aliongeza swali jingine ambalo pia nililikubali. Nikamwona akibadilika sura. Kwanza alitabasamu. Kisha tabasamu lake likamezwa na uso uliojaa huzuni, machozi yakimlengalenga machoni.

“Vipi kwani?” nilimwuliza kwa mshangao.

“Petro… Hunikumbuki?”

Sikuweza kuelewa anachozungumza. “Nakumbuka kukuona juzi pale stesheni, Dar es Salaam, kwa mara ya pili nakuona leo hapa Kigoma,” nilimjibu

Pamoja na machozi yake nilimwona akitabasamu kisha alisema, “Petro wewe ulipata kuokoa maisha yangu kwa kuhatarisha yako. Ulinichukua hadi Singida ambako ulinipeleka misheni ambako walinilea kiimani na kielimu. Sasa hivi nina kazi nzuri hapa Kigoma.”

Akili zangu zilikimbia na kunirejesha nyuma zaidi ya miaka ishirini iliyopita. Nikamwona yule msichana wa Kimasai aliyekuja katika kambi yangu huku akitetemeka. ‘...Nisaidie ...Naogopa’ Nilikumbuka jina lake, “Nashifa sio?”

Nilimwona akichangamka. “Unalikumbuka hata jina langu? Hata hivyo nilibatizwa na kupewa jina jipya la Maria. Lakini sijaliacha jina langu la asili. Nimefurahi sana kukuona Petro. Siku zote nilikufikiria usiku na mchana. Nilikuwa na hakika kuwa ingetokea siku nikakutia machoni. Imetokea…” alisita kuzungumza na kuangua kilio.

Sikujua kilichotokea nilijikuta nimemkumbatia kwa namna ya kumfariji huku yeye pia akinikumbatia na kukilaza kichwa chake juu ya kifua changu akiendelea kulia huku akinong’ona maneno fulani ambayo sikuyasikia vizuri. Nilisikia machache tu, “Uliokoa maisha yangu… kwa gharama ya kuharibu yako… sikupata kujisamehe kwa kitendo kile…”

Nilicheka kidogo kabla ya kumnong’oneza vilevile, “Maisha yangu ni hadithi nyingine. Masaibu yako hayahusiani hata kidogo na yale yaliyotokea. Yangu nayajua mimi na Mungu wangu.”

Tulikuwa bado tumekumbatiana. Kama si macho ya wapita njia kututazama kwa mshangao sijui tungekaa katika hali hiyo kwa muda gani. Macho yao yalifanya nijikumbuke na kujitazama. Nilitoa picha ya kuchekesha sana kwa mavazi yangu ambayo hayakuwa zaidi ya midabwada, kumkumbatia msichana huyu mtanashati ambaye sasa alivaa vitenge vilivyomkaa kana kwamba alizaliwa navyo. Nikajikwanyua toka mikononi mwake na kumtaka radhi.

“Samahani ya nini? Hujui nilivyofarijika Petro.” Alisema.

“Lakini tayari njia zetu zimetofautiana sana. Mimi ni ndege wa jela asiyestahili kukukumbatia hadharani. Tazama nilivyo,” nilisema nikijitenga naye zaidi ili anione vizuri zaidi.

Kwa mshangao wangu alicheka kabla ya kusema, “Najua yaliyokusibu. Nilikuwa nikifuatilia kwa karibu maongezi yako na yule mama wa Kiingereza. Anaitwa nani vile, Jane siyo?”

Nilikubali kwa kichwa.

“Hivyo huna haja ya kuniambia chochote zaidi. Najua umerudi kwenu. Najua umerudi mikono mitupu. Usijali. Nitakusaidia kadri ya uwezo wangu. Uliniokoa kwenye mvua mimi pia nitakuokoa kwenye jua.”

Alitia mkono wake kwenye pochi lake la mkononi na kutoa kadi ambayo alinikabidhi. Ilikuwa na majina yake na namba za simu. Kilichonivutia zaidi ni cheo chake. Afisa uhamiaji wa mkoa! Niliduwaa.

“Matunda ya wema wako hayo.” Alinifafanulia.

“Wamisheni wale walinipa elimu bora hadi chuo kikuu. Mara kadhaa nimepelekwa nje kuongeza ujuzi. Huu ni mkoa wangu wa tatu toka nilipopanda cheo.”

Nilizidi kuduwaa. Safari hii aliniondoa mshangao kwa kunishangaza zaidi. Alitia tena mkono wake mfukoni na kunipa kitita cha fedha. Kwa hesabu za haraka haraka zilipata kuwa shilingi laki moja.

“Za nini?” nilimuuliza.

“Zitakusaidia kidogo. Najua una matatizo mengi. Fika nyumbani, wasalimu wazazi halafu njoo mjini tushauriane.”

Nilitamani kulia. Kwa nini siku zote maisha yangu yamekuwa ya kukutana na binadamu wenye roho mbaya kama shetani na wale wenye roho nzuri mfano wa malaika? Nilijiuliza huku nikiwa nimemkodolea macho. Unajua wewe ni malaika. Unajua utafika mbinguni? Nilitamani kumwabia hivyo. Nilishindwa. Badala yake nilijikongoja kumwuliza, “Umeshaolewa?”

Alinipa jibu jingine ambalo liliniacha taabani zaidi, “Nilikuwa nikikusubiri wewe.” Nilipomtazama, aliyaepuka macho yangu na kutazama chini. Mara nikaelewa kilichonivutia zaidi juu yake. Haya! Pamoja na elimu yake, pamoja na cheo chake, bado alikuwa msichana wa kiafrika halisi, mwenye uso wa soni tofauti kabisa na wasichana wengi wa kileo.

“Sina budi kuondoka,” aliseme. “Tafadhali tuwasiliane. Sawa Petro Kionambali?”

“Bila shaka.” Nilimjibu

Akaifuata gari ambayo muda wote ilisimama nje ya stesheni ikimsubiri. Akaingia upande wa pili wa dereva na kupunga mkono wakati gari ikitiwa moto na kuondoka.

Mara alipotoweka machoni mwangu, nilihisi upweke wa pekee ambao sikupata kuujua huko nyuma.

Nilizihesabu tena fedha alizonipa. Nilikuwa na laki moja na hamsini. Sikuhitaji kufikiria sana. Niliendea duka la karibu la nguo na kununua shati mbili, suruali mbili na shuka la kujifunika.

Nilikuwa na mfuko wa nguo mpya mkononi ndiyo kwanza nilijiona nilivyochakaa. Nilikuwa nanuka!. Niliweza hata kuisikia harufu chafu ya mwili wangu mimi mwenyewe. Jasho la joto la Dar es Salaam na vumbi la Dodoma, purukushani za Tabora na malazi mabaya ndani ya behewa lililotoa mchanganyiko wa kutisha. Nikaamua kuiacha bandari na kuufuata ufukwe nikielekea Mtanga hadi nilipopata sehemu faragha ambayo nilivua nguo zangu na kujitupa ziwani. Sikuwa na sabuni wala mswaki. Nilitumia mchanga na vidole kujisugua. Nikapiga mbizi mara mbili tatu. Kweli, aliyeogelea hafi maji, kwani nilijikuta nikielea juu ya maji kana kwamba maisha yangu yote nilikuwa ziwani humo.

Nilipotoka majini nilijihisi mtu mpya. Hisia fulani ziliniambia kuwa kwa kuoga katika ziwa hili lenye historia ya pekee nilikuwa nikisafisha mikosi na mikasa yote iliyoniandama na kuanza maisha mapya.

Pengine haikuwa uongo. Ziwa Tanganyika lilikuwa mwujiza mwingine wa dunia. Kwanza lilikuwa refu kuliko maziwa yote duniani. Pia, kina chake kwenda chini kilivunja rekodi ya maziwa yote ya ulimwengu. Likiwa limeenda chini kwa takribani meta 2400 toka kilele cha milima ya Mahele iliyopo kilometa 150 toka Kigoma mjini au meta 1500 toka ardhi ya kawaida ya mkoani humo mwisho wa kina hicho uliwiana na usawa wa bahari kwa miji ya Dar es Salaam na Zanzibar. Inaaminika kuwa kuwepo kwa ziwa hilo ni matokeo ya mabadiliko makubwa yaliyopata kuitokea dunia, kama matetemeko ya ardhi au volkano ambayo pia yanaaminika kuibua vitu kama Bonde la Ufa. Walikotokea samaki ainaaina na viumbe wengine hai waliomo tele ziwani humo ni fumbo jingine ambalo mwanadamu hajapata kulipatia ufumbuzi.

Sikuhitaji gari kutoka kigoma hadi Mwanga. Mwendo wa dakika ishirini kwa mguu uliniwezesha kufika katikati ya mji huo. Mwanga ilichangamka. Vijana waliokuwa wakifanya kazi za kushevu walikuwa tele katika ofisi zao zinazovutia kwa vioo na viyoyozi. Niliingia katika kimojawapo cha vibanda hivyo na kukinga kichwa changu.

“Nywele na ndevu,” nilisema.

“Utahitaji tukuwekee na super black, kaka?” niliulizwa na kijana huyo

“Kwa nini?”

“Mvi zinakuanza. Unaona hapa?” alielekeza.

Nikajitazama katika kioo. Kweli, kulikuwa na mvi mbili tatu katikati ya kichwa changu. Nazeeka! niliwaza kwa mshtuko kidogo. Kuzeeka kabla ya kufanya jambo lolote ambalo familia, jamii na nchi yangu itaweza kujivunia haikuwa dhamira yangu hata kidogo.

“Hapana, shevu tu,” nilimwambia. Sikuona haja ya kuficha shahada ya umri wangu.

“Ndevu unashevu kwa mashine au magic?”

“Ndiyo nini hiyo mejiki?

Akanionyesha dawa fulani. “Hii inafanya kidevu kiwe kama cha mtoto mdogo,” Alifafanua.

“Na bei yake?”

“Iko juu kidogo.”

“Kama ni hivyo tumia mashine.”

Muda mfupi baadaye nilikuwa mtu mwingine kabisa, mtu anayependeza kwa usafi hasa kwa kijana huyo kunipaka mafuta ambayo yalilainisha ngozi yangu. Nilijitazama kwenye vioo vyake, mbele na nyuma, kwa muda kabla ya kumlipa na kuondoka.

Niliuliza magari ya kwenda Kasulu. Niliambiwa kuwa nimekwishachelewa, kwamba lilikuwepo basi moja tu la Mwarabu ambalo huondoka saa kumi na mbili za asubuhi kila siku. Pia, nilidokezwa kuwepo kwa malori ya mizigo ambayo huondoka asubuhi hadi saa tatu. Nilipoitazama saa yangu iliitimu saa nne na nusu za asubuhi. Nikaamua kutafuta hoteli ya bei nafuu ili nijipumzishe hadi hiyo kesho.

Kabla ya kuchukua chumba niliamua kuuvinjari kidogo mji wa Mwanga. Kama miji mingine nchini Mwanga ilipanuka sana. Maeneo kama Vumilia na Majengo ambayo zamani yaliogopwa na kudharaulika sasa viwanja vyake vilioneka lulu. Majengo yalikuwa yakiota kama uyoga. Kwa bahati mbaya sana, kama yalivyokuwa maeneo mengi mapya, maeneo haya pia yalikosa huduma muhimu. Hayakuwa na mifereji ya maji machafu, hayakuwa na mfumo wa maji safi, umeme wa barabarani ilikuwa ndoto na hata barabara zilijaa na kujitunza zenyewe. Hali iliyopelekea mafuriko na uchafu kuivuruga dhamira nzima ya wamiliki.

Nilienda Mwanga Katubuka. Nikaingia Sokono. Macho yangu yalikuwa yakiwatafuta samaki niliowazoea na wale ambao nimekuwa nikisikia sifa zao toka utotoni; nonzi, wale samaki wakubwa wanaofanana na ndege, kuhe, samaki mtamu ambaye ana hadhi; singa, samaki mnono aliyejaa mafuta mwili mzima, nika, samaki mwenye nguzu za umeme ambaye kumshika lazima utumie mdomo wake wa chini vinginevyo utarushwa na kumwachia; kuvungwe, anayeitwa nguruwe wa majini kwa umbile na masharubu yake.

Ningependa pia kuwaona kungura, ndubu, kambale na wengineo. Sikuwa na bahati hiyo. Samaki niliowaona sokoni humo siku hiyo ni migebuka ambayo ilikuwa imekufa kwa wingi. Ndubu? Siku hizi hapatikani sana. Kibonde? Alikuwepo mmoja tu leo, amegombewa kama mpira wa kona. Nikakata tamaa. Nikaenda soko la dagaa ambamo kulikuwa na dagaa wabichi wenyewe wakiwaita “mteke” na samaki wadogo wadogo walioitwa “Masembe.”

Nilipochoshwa na ziara hiyo nilitafuta hoteli na kuagiza chakula. Ningekula nini zaidi ya ugali wa muhogo kwa migebuka iliyokaangwa kwa mafuta ya mawese? Ulikuwa mlo mtamu uliofanya nijisikie shibe isiyo na kifani.

Baadaye nilipanda basi kwenda Ujiji. Sikujisikia kuondoka Kigoma bila kuuona mji huo wa kihistoria. Mji ambao ulikuwa na uzito mmoja na ile ya Bagamoyo, Zanzibar na Kilwa. Lakini mara niliposhuka kilima cha kutoka Mnarani na Mawemi matumaini yangu ya kuiona Ujiji inayosisimua ilizimika. Macho yangu yalipokelewa na mji wa kale, kama ulivyokuwa enzi za kina Tip Tippu na Livingstone. Mji uliomezwa na nyumba nyingi ambazo ziliezekwa kwa nyasi au bati kuukuu. Baadhi ya nyumba zilikuwa kuukuu zikiashiria jambo lilelile ambalo nimekuwa nikiliona huku na huko toka nilipotoka kifungoni; Umasikini.

Hali ya mitaa mingi pia ilitia huzuni. Kwa mtu aliyetoka katika miji inayokua, hata Mwanga tu, Ujiji ingeweza kumtoa machozi. Mitaa mingi ilimezwa na majani. Baadhi ya mitaa majirani walianza kulima mahindi na maharage. Kuna nini? Nilijiuliza. Yako wapi magari yachangamshe mitaa? Wako wapi watu waitie uhai? Nini kimetokea hapa?

Nikafikia uamuzi. Bila shaka biashara ya utumwa ilikuwa na laana. Vinginevyo mji huu ambao Dakta Livingstone alitia kambi miaka ya 1871 wakati akifanya utafiti katika nchi za Kongo na Malawi. Mji ambao Novemba 10, mwaka huohuo Henry Stanley, baada ya kutumwa kumtafuta alikutana naye ufukweni na kusema “Dr livingstone…! I presume…” mwaka mmoja kabla ya kifo chake. Ukiwa njia na kituo kuu cha wafanyabiashara wa Arabuni, Ulaya na Amerika katika kujipatia bidhaa za meno ya tembo na ile biashara haramu ya watumwa. Mji ambao huwezi kuandika historia ya Afrika bila ya kuutaja! Hadi leo uko hivi! Kama si laana ni nini?

Nilishuka kwenye basi, nikaifuata barabara ya Livingstone ambayo ilinifikisha Pwani ya Ujiji, pale Livingstone alipokutana na Stanley kwa mara ya kwanza. Palijengwa nguzo ya kumbukumbu yenye maelezo ya hafla yao ile. Nikatupa macho yangu ziwani na kuziona boti za jahazi ya wavuvi waliokuwa katika pilikapilika za safari, ama kuondoka ama ndio kwanza wanafika toka maeneo hayo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Nikarejea Mwanga na kuanza kutafuta hoteli ya kulala. Ujiji haikuwa na nyumba ya aina hiyo. “Nenda Mwanga… nenda Kigoma mjini. Hapa utalala nje bure,” niliambiwa na msamaria mwema, mtu mzima aliyevaa kanzu na baragashia. Mkewe alivalia baibui lililomfunika gubigubi isipokuwa sehemu ndogo ya macho na miguu. Wazee hao walinikumbusha Bagamoyo na Pangani.

Wakati azana ya kuwakumbusha waumini kuwasili zinaanza kutoka misikiti mbalimbali mimi nilikuwa nikipanda basi kurudi Mwanga.







SURA YA ISHIRINI NA SITA

Hirizi Iliyopotea Na Maajabu Yake

Pengine kwa ajili ya safari ndefu ya wima toka Dar es Salaam, pengine kwa ajili ya chumba murua chenye hewa safi nilicholala nilijikuta nimechelewa kuamka. Hivyo, basi la Mwarabu liliniacha. Nilioga harakaharaka, nikanywa chai kwa dagaa wa mteke, kisha huyoo, nikawahi malori ya mizigo. Nilipata moja lililokuwa likipakia mabati na vifaa vingine vya ujenzi. Kwa namna ya muujiza nilipata kiti cha mbele, tukiwa abiria wawili tu na dereva. Muda mfupi baadaye gari liliondoka.

Nikiwa nimekaa dirishani nilipata fursa nzuri ya kutazama nje, macho yangu yalivutwa na ardhi nyekundu, mimea ya asili, mashamba ya wenyeji na zaidi ya yote watu. Toka Mwanga hadi Gungu na baadaye Mwandiga yalikuwa maeneo ya watu, nyumba ambazo hazikutofautiana sana na zile za Mwanga na Ujiji. Hii hapa ikiwa imejengwa kwa saruji bati na samani nyingine zikiwa zimeipamba; ile ikiwa nyumba ya tope, ilijengwa kwa matete na mianzi na kuezekwa kwa nyasi.

Toka Mwandinga mambo yalibadilika zaidi. Nyumba duni zilianza kutamalaki huku zile za afadhali zikizidi kupungua. Watu pia walibadilika. Wengi walivalia mavazi duni, baadhi yakiwa yamechanikachanika. Ilikua rahisi sana kumshuku mtu kuwa ni mwendawazimu kutokana na hali hiyo. Lakini pale unapoona idadi kubwa zaidi iko katika hali hiyo, hasa watoto ambao wengi wao walitembea nusu watupu, miguu iliyojaa vumbi jekundu ikiwa pekupeku, unajikuta ukiondokana na wazo lako na kupata jibu mara moja, rahisi; umasikini.

Nyuso za watu wengi zilionyesha dalili ya kukata tamaa. Walicheka ndio, lakini kicheko hicho kilionekana mdomoni tu, moyoni ungeweza kusoma kitu kingine kabisa. Walizungumza pale ulipozungumza nao, lakini sauti zao ziliashiria kuifadhi jambo fulani ambalo hawakuwa na uwezo wa kulifafanua. Sura hizi za msiba, majengo mengi ya maombolezo na ardhi nzuri ambayo haikuwa ikichekelea kwa pamba na kahawa kama nilivyoizowea utotoni ni jambo ambalo lilinitia hofu badala ya shahuku ya kufika nyumbani. Nilihisi huzuni ikinigubika katika fikra zangu katika safari hiyo nzima.

Ndiyo, nchi yetu ni masikini. Lakini umasikini huu unazidiana kati ya mkoa na mkoa. Pengine iko mikoa iliyo taabani zaidi ya Kigoma, hilo halikunisumbua. Kilichonisumbua ni kwa nini Kigoma iwe katika kundi hilo? Kigoma haikuwa na sababu yoyote ya kuwa kama ilivyo. Ni mkoa uliojaaliwa kila ambacho binadamu anahitaji. Ardhi ilikuwa na rutuba tele, mali asili zikiwa zimefurika katika misitu na ardhini. Mito, mabwawa na baba lao; ziwa Tanganyika vikiwa vimejaa samaki tele ambao ladha yake ina uwezo wa kumshangaza mtu yeyote duniani zaidi ya hiyo Kigoma ni lango muhimu kwa nchi za Kongo, Burundi na hata Zambia. Ukweli huo pekee wa kijiografia ni rasilimali tosha. Historia ya Kigoma, hasa Ujiji pia ni rasimali nyingine muhimu ambayo kuitumia vyema kungeweza kuubadili mkoa kiuchumi.

Kitu gani kimetokea hata mkoa uwe ukirudi nyuma badala ya kwenda mbele? Kitu gani kimesahauliwa? Nani alaumiwe? Nilijiuliza hili na lile. Yako mengi ambayo hayakuhitaji utafiti wa kina kuyaona. Moja la haraka likiwa usafiri. Ilikuwa rahisi zaidi kutoka Kigoma kwenda Burundi au Kongo kuliko kwenda Tabora au Mwanza, achilia mbali Dar es Salaam. Wakati huu wa Kilimanajaro au Arusha anaweza kutoka Dar es Salaam hadi kwao na akarudi jioni au kesho yake ilimchukua mtu wa Kigoma wiki mbili au zaidi kufanya safari hiyo, hali ambayo muuza nyanya au samaki ataishia kuiona bidhaa yake ikioza mbele ya macho yake.

Barabara ilikuwa tatizo la kwanza lisilohitaji mjadala barabara pia lilikuwa tatizo la pili. Kigoma ulikuwa mmoja kati ya mikoa iliyo kimya sana. Pamoja na kukisiwa kuwa na eneo la kilometa za mraba 37,037 mkoa wa Kigoma ulikuwa hauna kiwanda hata kimoja. Hata wale samaki, aina ya migebuka ambao katika misimu fulani huliwa kwa mamilioni huishia kuharibika bure na kutupwa badala ya kusindikwa; achilia mbali dagaa wanono wenye sifa zote.

Hata mafuta ya mawese, yatokanayo na michikichi ambalo ni zao linalostawi sana mkoani humu hayajapata kujengewa kiwanda cha kuyasindika ili yauzwe kimataifa. Nani atafikiria kufanya mradi kama huo mahala ambapo hakuna hata barabara?

Barabara pekee ambayo haikuaminika sana ya kutoka Kigoma kwenda nje ya mkoa ni hiyo tuliyokuwa tukiitumia. Sehemu ndogo sana zilikuwa na lami. Sehemu kubwa ikiwa Changarawe na tope ambalo lilifanya safari iwe shughuli kubwa badala ya starehe. Lakini hilo halikuwa tatizo kubwa. Tatizo hasa lilikuwa mzunguko wa njia hiyo ulioifanya kuwa ndefu kupita kiasi. Ili kwenda Dar es Salaam au Tabora miji iliyoko mashariki ya mkoa ulilazimika kwenda kaskazini, upite Kasulu, Kibondo hadi Biharamulo kabla hujageuka kuelekea kusini ili ufike Kahama na Nzega kabla ya kuingia Tabora. Toka Tabora unapanda kaskazini tena na kurudi Nzega kabla ya kwenda Igunga, Iramba, Singida hadi Manyoni. Toka hapo utafika Dodoma na kutelezea Gairo, Morogoro, Chalinze na baadaye Dar es Salaam! Pema hapo?

Ndiyo, Kigoma kuna uwanja mdogo wa ndege. Ndege ndogondogo vilevile huja na kuondoka mara mbili au tatu kwa wiki. Licha ya ukweli kuwa hazitoshi, bado nauli kubwa ya ndege imefanya ziwe na wenyewe badala ya kila mtu. Si kila mtu mwenye laki mbili au tatu kwa safari ya saa nne kwenda na kurudi.

“Vipi unashukia wapi?” dereva alinizindua. “Naona uko mbali sana kimawazo,” aliongeza.

Nikapekecha macho yangu kwa kidole changu cha shahada kabla ya kumuuliza, “Kwani hapa ni wapi?”

“Tumeshapita Simbo. Hapa ni Kitawe. Baada ya hapa tunaingia Mayange. Toka hapo ni moja kwa moja hadi Kasulu, mwisho wa safari yetu.”

Sikujua nimjibu nini. Kwa kweli, sikujua hata mahala pa kushuka. Niliondoka nikiwa mdogo sana. Kumbukumbu nilizokuwa nazo zilionyesha kuwa hatukuwa mbali sana na mji wa Kasulu. Lakini udogo, mabadiliko makubwa ya mazingira na hasa kutoweka kwa misitu mingi ambayo ningeweza kuikumbuka kulifanya nisijue wapi pa kuanzia upelelezi wangu wa kutafuta chochote nitakachoweza kupata juu ya wazazi wangu.

Nadhani dereva alizisoma hisia zangu. Kwani alirahisisha kazi yangu pale alipouliza, “Yaelekea wewe ni mgeni sana huku?”

“Nadhani, maana niliondoka nikiwa mdogo sana. Hata sifahamu nianzie wapi kuwatafuta wazee wangu,” niliropoka bila kutegemea.

Kwa wakazi wa mkoa ambao hauna ajira za kutosha, ambao mkoloni aliutumia kama shamba la kuchukulia manamba wakakate mkonge huko Tanga na Kilimanjaro maelezo yangu hayakumshangaza dereva huyo hata kidogo. Alihitaji maelezo mafupi tu; niliondoka lini. Tulikuwa tukiishi wapi, ukoo wangu ni upi na mengineyo. Nilipomweleza juu ya hofu yangu juu ya vijiji vya Ujamaa alinielewa mara moja. Akanishauri nishuke katika kijiji kinachofuata, kinachoitwa Mayange, ambacho ni kikubwa na kilikusanya familia mbalimbali toka maeneo mengi.

“Walisema kingekuwa kijiji cha mfano kwa maendeleo,” alisema akicheka kwa kebehi. “Hebu katazame hayo maendeleo halafu utatuambia.”

Nikaafikiana na ushauri wake. Tulipofika Mayenge nililipa nauli yangu, nikateremka na kuanza kazi ya kutafuta ‘kwetu’.

Kama nilivyotegemea kijiji cha Mayange kilikuwa kinyume kabisa na matarajio ya awali kama ilivyokuwa kwa vijiji vingine vyote tulivyovipita njiani, Mayange ilitoa taswira ileile, umasikini unaonuka. Karibu watoto wote walichakaa miili na mavazi, wakifanya kazi ndogondogo kama kubeba mizigo ya wasafiri kwa mikokoteni yao ya miti au kuomba tu kwa wapita njia. Baadhi walivaa sare za shule. Lakini sare nyingi kati ya hizo hazikufanana kabisa na malengo ya wizara kwa kuchoka na kuchakaa.

Watu wazima nao walikuwa na yao. Wengi wao walikuwa taabani, suruali zikiwa zimejaa viraka, shati zikiwa zimepasukapasuka, miguu iliyokuwa peku ikiwa imebadilika rangi kutokana na vumbi jekundu lililowapiga pindi wakihangaikia mkono kwenda kinywani.

Waliahidiwa huduma muhimu kama barabara; hazikupata kujengwa au kukarabatiwa. Waliahidiwa maji ya bomba; hawakupata kuyaona. Waliahidiwa umeme; ilikuwa ndoto za mchana. Waliahidiwa huduma ya matibabu; sasa ilibidi kuyalipia kwa fedha ambazo huna. Kwa ujumla, ahadi zote zilizotumiwa ili kuwaondoa katika makazi ya baba na babu zao ziligeuka hewa. Jambo hilo lilifanya nyuso za kila mtu unayekutana naye zitangaze dalili zote za kukata tamaa.

Kazi ya kuitafuta familia moja, kati ya familia zaidi ya mia saba zilizohamishiwa hapo toka maeneo tofauti haikuwa ndogo. Nilitumia zaidi ya saa mbili kabla ya kumpata mzee mmoja ambaye alimfahamu babu, “Familia ya Kionambali, sio? Wala usihangaike. Wako humuhumu. Mtoto wake Karimanzira huwa namwona mara kwa mara.”

Nikapata matumaini. “Ni babu? Kionambali mwenyewe?” niliuliza.

“Huyo sina habari zake. Sijui kama bado yuko hai au tayari ametangulia,” mzee alinijibu. Laiti angejua kauli yake ilivyonishtua.

Nikiwa na matumaini mapya nilianza awamu ya pili ya kuwatafuta wazazi wangu. Zikiwa safari za mguu, katika kijiji kikubwa kisicho walao na jina la mtaa ilinichukua saa moja na nusu kabla ya kuonyeshwa kwa mbali nyumba iliyoaminika kuwa ya baba.

Ilikuwa nyumba iliyofanana na nyingine nyingi kijijini hapo; tofali za tope ambazo zilichakaa kabla ya kupata lipu, achilia mbali rangi. Juu nusu iliezekwa bati kuu kuu nusu nyasi. Sakafu ilikuwa ardhi ileile waliyoikuta palepale.

Nje ya nyumba hiyo alikuwepo bibi mmoja mchovu kama wengine wote kijijini hapo, akisuka ukili. Nilisogelea na kumwamkia. Kisha niliuliza kama hapo palikuwa nyumbani pa mzee Karimanzira. Swali langu lilimfanya bi mkubwa huyo ainuke na kunitazama kwa makini. Mara nikamwona akianza kutetemeka. Machozi yakianza kumtoka.

“Wewe ni Mtukwao!... Mwanangu! Umerudi…” alisema akinijia na kunikumbatia kwa nguzu zake zote.

Alikuwa mama! Mama yangu kipenzi! Fuko nililokuwa nalo mkononi lilidondoka pwaa, mikono yangu pia ikamkumbatia kwa nguvu. Masikioni nilisikia sauti nzito ya kiume ikilia! Kilio cha kwikwi. Ilinichukua muda kubaini kuwa ilikuwa ni mimi niliyekuwa nikilia.

Mara mzee mmoja akatoka nje ya nyumba hiyo. Alikuwa mchovu vilevile. Umbile lake refu lilipinda kwa mbele, ndevu zenye mchanganyiko na mvi zilimeza kidevu na kichwa chake kizima. Akitetemeka miguu na mikono yeye pia alinijia na kunikumbatia, machozi yakimlengalenga.

Baba! Amezeeka kabla hajapata kuwa kijana!

Dakika mbili tatu baadaye nyumbani palifurika. Watu waliotoka huko na huko walijazana kushangilia ujio wangu. Kila mtu alisema lake, ingawa mada ilikuwa ileile; Mwana mpotevu karejea!

Niliingizwa ndani, nikapewa kiti cha kifalme; kigoda cha baba. Fumba fumbua togwa tamu ikaletwa. Nikapewa kata kubwa iliyojaa. Kabla haijaisha nililetewa mihogo mitamu, huko nje nikiwaona vijana wakikimbizana na jogoo.

Baba na mama hawakubanduka ubavuni mwangu. Walikuwa na mengi ya kuniuliza mengi ya kunisimulia. Kwa bahati mbaya, hali haikuruhusu. Watu walikuwa tele, wakinishangaa kana kwamba nimetoka mwezini. Kelele pia zilishamiri. Watoto ambao hata sikuwafahamu walijipenyeza na kukaa miguuni mwangu, wakijitahidi sana kunikumbatia, walao miguu.

Kwa kweli sikutarajia mapokezi makubwa kama haya. Nikiwa mtu aliyepotea kwa zaidi ya miaka thelathini, mtu aliyerudi akiwa mikono mitupu kama nilivyokuwa, nilitarajia kupokelewa kwa kejeli au dharau. Si vicheko na kushangiliwa kwa takribani kijiji kizima kama ilivyokuwa. Hata hivyo, nilijihisi kama mtu aliyeutua mzigo mzito uliomlemea. Nilijihisi kama ambaye nilifutiwa madhambi yangu yote hata kabla ya kuomba radhi.

Kitu kimoja tu kilikuwa kikinisumbua. Mtu niliyetamani kumwona pengine kabla ya wengine wote hakuwa katika kundi la watu waliojitokeza kunilaki. Mtu huyohuyo nilihitaji sana kumwomba radhi kwa kumwamgusha katika matarajio aliyokuwa nayo juu yangu na kumpotezea hirizi yake muhimu. Nilimtegemea awe katika mjumuiko huo, aniite kando ambako tungeketi peke yetu na kuteta kama mtu na baba yake. Sikumwona. Wala sikuthubutu kuuliza harakaharaka kwa kuchelea kupewa jibu ambalo lingeweza kunitia ugonjwa wa moyo; Babu yake! Mbona alikufa zamani?

Kuku alikwishachinjwa na kupikwa. Ugali mweusi wa nyangwe uliletwa mbele yangu kwa kitoweo cha kuku huyo. Bila kuambiwa wageni walianza kupungua ili kuniachia faragha ya kufaidi chakula changu. Nilishindwa kujizuia. Kabla ya kumega tonge la kwanza nilimuuliza baba, “Babu yuko wapi?” nilisubiri jibu lake kwa hofu kubwa, moyo ukinidunda. Lakini nilipomwona baba akitabasamu kabla hajanijibu hofu ilitoweka moyoni mwangu.

“Babu yako kwani humjui?” baba alisema. “Aligoma katakata kuhama. Jeshi la polisi, jeshi la mgambo na hata sungusungu walishindwa kabisa kumtoa. Hivi sasa yuko peke yake ndani ya msitu mkubwa wa yaliyokuwa makazi yake. Kila wiki huwa nakwenda kumjulia hali.”

Nikapumua. “Bibi?” niliuliza.

“Yeye hatuko naye tena. Alitutoka miaka mitatu iliyopita. Alipatwa na ugonjwa wa malale uliokataa kila aina ya dawa.”

Ladha ya kuku ikaniishia palepale.

* * *​

“Nilijua utarudi salama… nilikuwa nikikusubiri… nisingeweza kufa kabla hujarudi, mjukuu wangu,” ilikuwa kauli ya kwanza ya babu mara aliponitia machoni na kunipapasa kichwani.

Sikuweza kuyastahimili machozi yaliyomiminika toka machoni mwangu. Babu alinikumbatia, huku mkono wake ukiendelea kunipapasa kichwani kwa namna ya kunibembeleza. Kitendo hicho kilizidisha uchungu moyoni mwangu na kunifanya nizidi kulia. Kwa mara ya kwanza, hakunishutumu kwa kitendo hicho. Niliinua uso na kumtazama kwa wizi. Yeye pia alilowa macho kwa machozi.

Babu analia, chuma cha pua!

Kwangu, alikuwa zaidi ya babu. Alikuwa kila kitu; baba, babu, rafiki, mwalimu na zaidi ya hayo. Hayo nilibaini na kuyahakikisha muda huo ambao mzee hataweza kustahimili kabisa kuficha udhaifu wake kwangu! Nitamsimuliaje malaika huyu kuwa jitihada zake zote za kupita mabonde, milima na misitu yenye hatari zote za dunia, hadi kunifikisha nchi ya Wahaya ili nipate elimu zilikuwa kazi bure? Nitaanzaje kumwambia kuwa ile hirizi yake, urithi pekee alioniachia ilipotea kwa uzembe? Niliteseka vibaya sana akilini nilipowaza hayo.

Nilikuwa nimemlazimisha baba alfajiri tu ya siku iliyofuata aniongoze kuja kumwona babu. Yeye akisisitiza kuwa ningepumzika walao siku mbili kabla ya kufanya safari hiyo. Jambo ambalo sikuafikiana nalo.

Kwa kutokuwa na uhakika wa kuwapata wazazi wangu, wakiwa hai nilifika nyumbani mikono mitupu. Hivyo, nilipopata fursa ya faragha ya kumkabidhi baba shilingi 50,000 kati ya zile laki moja nilizobakiwa nazo nilionekana shujaa mkubwa. Baba alianza mipango ya ‘kumaliza bati’ mama aliongea juu ya kulimisha shamba. Ilikuwa kama nimetoa milioni hamsini.

Tulimkuta babu akifunga mbuzi wake nje ya nyumba. Alivaa nguo zake zile alizozipenda, kaptula na shati nyeupe. Ziling’ara kama nilivyoziacha! Miguuni alitilia buti zake ambazo nazo ziling’ara kwa kiwi, ingawa zilianza kuchoka. Alikuwa peke yake katikati ya pori, isipokuwa kwa mifugo mingi ya mbuzi, kuku na bata. Watu wa pwani wangeweza kuapa kuwa ni jini jeupe linalokaa peke yake msituni. Babu alikuwa ametusikia toka mbali. Hivyo, alimfunga mbuzi yule harakaharaka na kusimama akitukodolea macho. Alipotuona alitukimbilia na kunidaka juujuu. Angeweza kunibeba… angeweza kunitia mweleka…. Babu alikuwa na nguvu zake. Ilikuwa kama ni binadamu pekee aliyebishana na uzee. Binadamu ambaye hakukubali kusalimu amri kwa kifo.

Pamoja na baba tulikuwa na vijana wengine wawili ambao nilielekezwa kuwa ni ndugu zangu. Vijana hao walipewa amri ya kumkamata beberu mkubwa kuliko wote na kumchinja. Akachunwa. Moto ukawashwa. Muda mfupi baadaye, tulikuwa tukimla mbuzi yule, wa kuchoma. Babu, akiwa na meno yake yote alitafuna mguu mzima wakati wengine tukishika shika hapa na pale.

Baadaye babu aliwataka baba na wale wenzetu wengine kuondoka kwa maelezo kuwa alikuwa na mengi ya kuzungumza na mjukuu wake faragha. Usiri wangu na babu halikuwa jambo geni kwa baba, toka utoto wangu. Hivyo, hakutia ubishi, walichukua nyama ya kula nyumbani wakaondoka zao kwa ahadi ya kunifuata kesho.

Nikapata wasaa wa kuchomoa zile elfu hamsini nilizobakiza na kumkabidhi babu. “Zawadi pekee niliyoweza kukuletea ni hii,” nilisema kwa masikitiko.

Babu hakuzipokea. Badala yake alicheka kabla ya kusema, “Sidhani kama nazihitaji. Za nini? Kaa nazo, zitakufaa wewe zaidi. Naamini bado unasafari nyingine ndefu, yenye mafanikio makubwa zaidi. Halafu, bado tuna mengi ya kuzungumza, mimi na wewe.”

“Bila shaka. Niliitikia.

“Miaka mingapi vile toka tumetengana?” Babu aliniuliza.

“Mingi sana. Ni aibu kuitaja.” Nilimjibu.

“Aibu ya nini? Mwanaume anayeonea aibu masaibu yake hafai. Kwa nini ufanye jambo ambalo utalijutia maishani mwako?”

Nilijua darasa la babu limeanza. Sikuwa tayari kwa darasa lolote wala somo lolote kabla ya kumtaka radhi. Hivyo nikajikongoja na kumwambia, “Babu ningeomba nianze kwa kukutaka radhi.”

“Radhi ya nini?”

“Hirizi.”

“Ilifanyaje?”

“Ilipotea!”

Nilitarajia babu abadilike, akasirike. Lakini kwa mshangao nilimwona akiachia tabasamu jembamba. “Nisubiri kidogo,” alisema akiinuka na kuingia ndani, aliporejea alikuwa na hirizi mkononi.

“Hirizi hii siyo?”

Niliitazama kwa makini. Nisingeweza kuisahau. Ilikuwa ileile!

Sikuyaamini macho yangu. Nikamkodolea babu macho ya mshangao.

“Hii ndiyo inayokusumbua?” babu aliongeza baada ya kicheko kingine. “Usiwe na wasiwasi. Ilipotea ikatafuta njia, ikarudi nyumbani kukusubiri.”

Bado sikuweza kuelewa. Hirizi hiyo ilipotea porini katika purukushani za kuikimbiza isianguke mikononi mwa padri. Yule kimbelembele, Byabato, alinihakikishia kuwa aliiokota tena na kumrudishia padri Backhove ambaye aliichoma, ikakataa kuungua. Kwamba baadaye ilitupwa baharini. “Ilifikaje kwako?” nikamuuliza.

“Ni hadithi ndefu. Ili kuifanya fupi pengine nikuambie tu kuwa ililetwa.”

“Na nani?” nilizidi kumbana babu.

“Na mizimu ya babu zetu.”

Bado nilikuwa sijamwelewa. Nikamwambia hivyo.

“Mizimu ina njia nyingi ya kuwalinda wahanga wake,” alifafanua. “Chochote kilichokutokea hadi hirizi hii kutengana nawe wahanga walikuwa wakiona. Ama kwa kujigeuza ndege, ama kwa kuwatuma ndege, hirizi hii ililetwa hadi katika mikono yangu.”

Babu alipoona kuwa bado sijaridhika na ufafanuzi huo aliamua kuwa wazi zaidi. Alisema kuwa jioni moja alikuwa akiwinda katika mwambao wa mto Malagalasi. Mara akaona kundi kubwa la ndege aina ya hondohondo wakitua hatua chache toka alipokuwa. “Walikuwa wengi. Kama elfu moja hivi. Waliponiona waliruka kunikimbia. Lakini mwenzao mmoja hakuweza kuruka. Alikuwa akipigapiga mabawa kwa nia ya kupaa lakini hakuweza. Nikamsogelea kuona kapatwa na nini. Nikabaini kuwa shingo yake ilikabwa na kamba nyeusi ambayo ilinasa kwenye kichaka cha mti. Nilipomshika ili kumkwamua ile kamba nilishangaa kuona kuwa ilikuwa hirizi ile niliyokupa. Nikaitoa na kumwacha ndege ambaye alipaa kuwaendea wenzake waliokuwa wakihangaika angani kumsubiri.”

Ilikuwa habari ya ajabu kwangu. Hirizi yangu, iliyopotea zaidi ya miaka thelathini iliyopita imerejea mikononi mwangu. Niliipokea, nikaipapasa. Ilikuwa ileile, kwa rangi na uzito. Kwamba imerudi mikononi mwangu halikuwa jambo la ajabu sana, ni namna iliyoifanya irudi ambayo kichwa changu hakikuweza kupokea.

Falsafa nyingi zilipita kichwani mwangu. Kama kweli ilitupwa ziwani bila shaka ingeweza kuoza. Kama hilo halikutokea ni wazi kuwa ilimezwa na samaki ambaye huenda alivuliwa na kuliwa. Kama ilikuwa hivyo hirizi itakuwa ilitupwa kama sehemu ya uchafu wa matumbo ya samaki wanayotayarishwa kwa ajili ya minofu kusafirishwa Ulaya na “mapanki” kuvamiwa na akina baba na mama ntilie. Inawezekana kuwa katika jitihada za kujitafutia chochote ndege yule alijikuta ameivaa hirizi ile na kuisafirisha bila kujua? Kama ni kweli kwa nini ailete hadi miguuni mwa babu?

Katika pitiapitia yangu vitabuni nilikuwa nimesoma mahala tabia za ndege. Moja ya tabia zao za ajabu ni ile ya kuhama au kusafiri safari za mbali kila ifikapo msimu fulani. Mara nyingi ndege hao wanaweza kusafiri safari za mbali toka Marekani au Ulaya hadi Afrika. Inaaminika kuwa wengi uhama katika vipindi vya hali fulani ya hewa na kurudi hali inapotengemaa. Inaaminika pia huko ambako huenda ndiko ambako ndege huzaliana na kurejea likiwa kundi kubwa zaidi. Inawezekana kabisa kuwa hondohondo aliyebeba hirizi yangu alikuwa katika msafara huo. Anaweza kuwa alikuwa akitoka zake Ulaya au nchi za Kiarabu na kuelekea Afrika Kusini!

Babu alikuwa kama anayeyasoma mawazo yangu. Alikohoa kidogo kabla ya kusema, “Naona na wewe tayari umeambukizwa yale maradhi yenu.”

“Maradhi gani?

“Maradhi ya kisomi. Naona unavyoona shida kuamini kuwa mizimu ya babu wa babu zako imekurejeshea hirizi hii! shauri lako. La msingi ni kwamba hirizi yako imerejea na tangu leo utaivaa tena. safari hii milango yote uliyoshindwa kuifungua itafunguka,” alisema akinivisha hirizi hiyo na kisha kunitemea mate kichwani na kifuani.

“Kuna jambo la pili.” Alisema akiinuka tena na kurudi ndani. Aliporejea alikuwa na bahasha tatu mkononi. Alinikadhi. Ilikuwa barua. Juu ziliandikwa jina lake na anuani ya kijiji chake. Ilielekea barua hizo zilitoka nje ya nchi, kwani stempu zote zilikuwa na picha ya malkia au wafalme wazungu, muhuri ukisomeka waziwazi “Stockholm-sweden”. Tarehe kwenye mihuri hiyo zilionyesha kuwa zilitumwa zaidi ya miaka kumi na mitano iliyopita!

“Barua!” Niliropoka.

“Ndiyo,” babu alijibu “Mbona hazijafunguliwa? Ni za zamani sana,” nilisaili.

Babu naye akaonyesha mshangao wake kwangu, “Mjukuu wangu, zinalekea kuwa ni barua muhimu sana. Unadhani ningeweza kumpelekea mtu yeyote asome siri zangu na kuanza kunitangaza? Nilikuwa nakusubiri, nilijua ungerudi salama.”

“Ni wewe peke yako utakayekuwa wa kwanza kuelewa chochote kilichoandikwa humo.”

“Zilifikaje hapa?” Niliuliza nikianza kufungua moja niliyoiona ya zamani zaidi.

“Zililetwa. DC alileta kwa mkono wake mwenyewe. Alinishawishi kufungua lakini nilikataa katakata.”

Baada ya maelezo hayo babu alikunjua kiti chake cha uvivu, kilichotengenezwa kwa ngozi ya nyati na kujilaza kimya kwa namna ya kunipa wasaa wa kusoma barua hizo kwa tuo.

Barua ya kwanza ilikua ndefu kidogo. Ilianza kwa salamu za siku nyingi, ikaendelea kwa taarifa ya kuipongeza kazi yake alipokuwa nchini humo, “Tumetengeneza filamu mbili za ile michezo uliyoshiriki kuicheza. Filamu hizo zimependwa sana Ulaya nzima zinanunuliwa kama peremende. Taarifa tuliyoichapisha hapa chini ni malipo yako ya mrabaha hadi sasa. Tunaomba ufanye kila uwezalo kuwasiliana nasi ili upokee malipo yako,” ilieleza barua hiyo.

Sehemu ya pili ya barua hiyo ilikuwa na mahesabu ya idadi ya mikanda iliyouzwa na televisheni zilizonunua hakimiliki na hakishiriki. Kwa hesabu za harakaharaka asilimia ya babu ilionyesha kama dola 227,000. Sikuyaamini macho yangu. Nikainua macho kumtazama. Alikuwa amesinzia, tabasamu likiwa mdomoni.

Nikafungua barua ya pili. Hii iliandikwa mwaka mmoja baadaye. Ilisisitiza, umuhimu wa babu kwenda haraka au kumtuma mrithi wake yeyote anayeaminika. Iliongeza kuwa iwapo kuna tatizo lolote la vitambulisho mwakilishi huyo alichotakiwa ni kwenda na ile hirizi ambayo ilikuwa haibanduki shingoni mwake. “Benki yetu tayari imearifiwa juu ya hilo. Usiwe na wasiwasi,” iliongeza barua hiyo.

Barua ya tatu iliambatanishwa na hundi. Hesabu zilizoandikwa juu ya hundi hiyo zilinitatanisha dola 812,000! Barua ilisisitiza fedha hizo kuchukuliwa. Ikiongeza kuwa benki yao tayari imefungua matawi nchini katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza, haikuwepo haja ya kusafiri hadi Ulaya tena.

Mara nikaanza kupata njozi za mchana. Nilijiona nikiandika kitabu, ambacho kiliyahusu maisha yangu mwenyewe. Niliyaumba na kuyaumbua matukio, mikasa na visa vyote vilivyonikumba toka katika safari zangu kuu mbili safari ya kimaisha iliyonifikisha kila pembe ya nchi na ile ya kimaumbile ambayo ilinitoa utotoni na kuniingiza ukubwani. Nilihisi hata jina la kitabu likinijia akilini; Kiguu na Njia.

Zikanijia njozi nyingine. Katika njozi hizi nilijiona nikiwaelekeza watu wa masuala ya filamu wapi pa kuelekeza kamera zao, katika filamu niliyokua nikiitengeneza. Niliwataka ihusishe maeneo yote muhimu ya nchi yetu, mbuga za wanyama, maziwa na mito yote ambayo haikupata kutangazwa vizuri. Kwa njozi niliona mikanda ya filamu hiyo ikigombewa na kuwafanya watazamaji waone hazina kubwa iliyosahauliwa ambayo walijaliwa na Muumba.

Nikaona jinsi nilivyokuwa nikiishi na mke wangu Nashifa kwa furaha. Watoto wetu wawili wenye afya njema wakicheka na kufurahi…

Halafu nikamkumbuka mwenye fedha zake, ambazo zingeniwezesha kufanikisha ndoto hiyo. Nikageuka.

“Babu!” niliita tena nikimtazama.

Alikuwa bado amelala vilevile kwenye kiti chake cha uvivu. Tabasamu lake lilikuwa bado limesahauliwa palepale usoni kama mtu aliyekuwa katika dimbwi la starehe. Niliinuka na kumshika bega. Nikamtikisa taratibu, baadaye kwa nguvu kidogo, “Babu… babu… babu…!”

Kimya! Kimya!

Nikashtuka. Alikuwa kama hapumui! Nikamshika kifua kusikiliza mapigo ya moyo. Hayakuwepo. Hata mwili wake tayari ulikuwa umepoa. Ndio kwanza nikabaini kuwa babu hatukuwa naye tena duniani! Tabasamu lake lililobakia palepale kama ishara ya ushindi kwa jambo zito lililokuwa likimsumbua kwa muda mrefu.

Nilitetemeka mwili mzima. Nguvu zikaniishia, furaha, faraja na matumaini makubwa niliyoyapata mara baada ya kuisoma barua yake, ikatumbukia nyongo.

Safi sana...

Simuliz hii kila kipengele kinafundisha...

Chapter Closed...


Cc: mahondaw
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom