Riwaya: 'hofu'

Riwaya: 'hofu'

Willy Gamba 1 uko wapi?? Watu wana kiu ya kufa Huku
 
Hali ya ukimya ikiendelea inabidi niingilie kati kumsaidi isije ikawa ametekwa na Makaburu!

mi nakushangaa maana mwenyewe alishatoa ruksa kuwa kama kuna anayeweza kumsaidia afanye hivyo. sasa tunakutegemea wewe
 
H O F U

SEHAMU YA KUMI

MAMBO BADO

Ilikuwa yapata saa sita kasoro dakika kumi wakati Bon alipobisha hodi kwenye chumba cha Willy, huku akiwa na bastola mkononi tayari. Mike alikwenda kufungua. Akiwa tayari kabisa, aliruka haraka upande.

"Lo! Mungu wangu vipi?", Mike aliuliza baada ya kumwona Bon".

"Willy yuko wapi?", Bon aliuliza kabla ya kujibu.

"Amewafuata", Mike alijibu.

"Kama nusu saa hivi. Nyaso amempeleka na atarudi si muda mrefu. Rocky yuko wapi?", Mike aliuliza.

"Mike. Rocky ameuawa", Bon alijibu.

"Hapana", Mike alisema bila kuamini.

"Ukweli ni kwamba watu hawa ni majasusi wa hali ya juu. Twende tumfuate Willy. Huko njiani nimeona gari likielekea nyumbani kwa F.K. likiwa limejaa watu. Iwapo Willy yuko peke yake, atapata matatizo. Heri tumfuate kwani hatuwezi kumpotenza na Willy pia. Mambo mengine nitakueleza njiani. Kwani hatuna muda. Nyaso akirudi anaweza akatusubiri hapa hapa", Bon alisema.

Bila kusema neno Mike alichukua zana zake na wanaume wakatelemka chini. Mbele ya hoteli walipungia taksi na kupanda.

"Tupeleke Themi Hill", Bon alimwamrisha dereva. wakaondoka.


Willy alipopata fahamu kidogo akajikuta ndani ya chumba kikubwa. Alikuwa amefungwa kwenye mti mfano wa msalaba uliokuwa katikati ya chumba. Ingawa Willy alikuwa amepata fahamu huku akiumwa sana na kichwa, hakuonyesha kama amepata fahamu. Alifanya hivyo 'kununu muda' Alishangaa kukuta majasusi walikuwa bado hawajamuua. Hapo hapo aligundua kuwa walikuwa na sababu ya kumweka hai. Kwa kutumia sababu hiyo aliweza kununua muda zaidi. Alijikuta amefungwa barabara kiasi kwamba asingeweza hata kujitingisha.

Mara alisikia mlango unafunguliwa na taa kali zaidi zinawashwa na kuelekeza mwanga wake kwake. Pale pale Willy alitambua kuwa chumba kile kilikuwa chumba cha mateso. Alikuwa amevuliwa nguo zake zote na kubaki na chupi tu.

"Hecke, bila shaka umempiga sana mtu huyu, nusura umwue. Unajuwa mtu huyu tunamhitaji sana angalau kwa muda wa dakika tano zaidi akiwa hai", F.K alisema. Willy aliyasikia maneno hayo.

"Mtu huyu ni hatari sana F.K. Hecke alichofanya ni sawa sawa", mtu mmoja alisema na Willy akamsikia.

"Sharti turudishe fahamu yake maana yule mwenzake anaweza kuwa anajongea kwa wakati huu", F.K. alisema.

"P.G yuko nje tayari kumfungia kazi. Hecke na wewe nenda nje ukamsaidie P.G. kama ikibidi. Akidiliki kupitia njia ile ya chini kama alivyofanya mwanzo, huo ndio utakuwa mwisho wake, kwani nimemtegeshea bomu moja safi", George alijigamba.

"Hebu kwanza Hecke, nenda ukawashe ile swichi ya umeme ili umshitue mbwa huyu kwani amezirai muda mrefu", F.K. alimwamrisha Hecke. Willy akajiweka tayari huku akili yake ikifanya kazi haraka haraka. Hecke alikwenda akawasha swichi. Umeme ulimshitua Willy naye akajifanya kaupata fahamu tayari ili asiumizwe zaidi. Alipofungua macho alimwona F.K. amesimama mbele yake pamoja na George. Kule pembeni alimwona Hecke.

"Karibu kwetu Willy Gamba. Ni jambo lisilofurahisha kukukaribisha hapa nyumbani kwangu katika hali hii. Lakini umeyataka mwenyewe na kama ujuavyo msiba wa kujitakia hauna kilio. Haya, huyu hapa ni mwenzetu na kiongozi wetu Geoge ambaye anaongoza kikundi cha 'KULFUT' kilichotumwa kuja kuifundisha adabu Tanzania", F.K alisema akiwa anamtazama Willy. Baadaye alimgekia George.

"George, huyu ndiye Willy Gamba kama umewahi kumsikia. Ni bahati yake mbaya kwamba amekutana na wewe", F.K. alisema.

"Hata mimi nimefurahi kumwona, nimesikia habari zake nyingi. Nasikitika kumwona katika hali hii, hata anapokuwa amefikia mwisho wa maisha yake haya yote yametokana na nchi ya Tanzania kujiweka kimbelembele na kujiingiza kwenye mambo yasiyowahusu", George alijigamba.

Aliposikia hayo Willy alianza kuzungumza ilimradi aweze kusukuma wakati.

"F.K... ni lazima umweleze kaburu huyu swala la ukombozi Kusini mwa Afrika ni swala la Afrika huru nzima. Hivyo kwa watu kufa ili vizazi vilivyobaki viweze kuwa huru ni jambo takatifu. Kwa hiyo mimi sina wasiwasi na kufa".

"Hecke, hebu nenda huko nje ukamsaidie P.G. kumumaliza huyo mbwa mweusi mwingine kwani naona hawa wana vichwa vigumu kama vya paka", George alimrisha.

"Kitu kimoja ambacho unapaswa kuweka maanani Willy ni kwamba, mtu mweusi hawezi kujitawala. Sana sana atapata uhuru wa bendera lakini uchumi wenu utatawaliwa na mtu mweupe daima. Chukua mfano wa Tanzania ni nani anayefaidi matunda ya uhuru hapa kama siyo mzungu na mhindi?, Mhindi akiendesha Benz ni halali yake; thubutu mtu mweusi aendeshe Benz kama hakutiwa msukosuko. Sasa, kisa gani hata kupoteza maisha yenu kwa kupigania uhuru wa bendera ambao huna faida? kweli mtu mweusi hawezi...", F.K. alisema na kukatizwa.

"F.K. unazungumza maneno ya kitoto. Nchi huru za Afrika zinapigana dhidi ya ubaguzi kwa sababu hazitaki ubaguzi. Nyinyi wahindi mnaonekana kama watanzania machoni mwa watanzania. Mawazo yako katika kuhusu uhitilafiana kimapato ni jambo lililopo Ulimwenguni kote. Amini usiamini, kama usaliti wako utagunduliwa, hata kama mimi nitakuwa nimekufa, wahindi wenzako watakuwa wa kwanza kutamani kukurarua. Siyo wahindi wote wenye mawazo finyu kama yako", Willy alimwambia F.K.

"F.K. unamchelewesha huyu mtu. Hebu muulize atupe habari zetu halafu... Usiku unakwenda haraka sana", George alimwambia F.K.

"Kusema kweli Willy nilipenda kifo chako kije haraka. Hata hivyo huo ni uamzi wako. Kama utajibu swali langu, utakufa haraka bila kupata mateso. La hasha, utakufa pole pole na kwa uchungu mkubwa. Chumba hiki kina kila aina ya vifaa vya kutesea. Sina haja ya kukueleza kwani wewe mwenyewe ni mwenyekiti katika shughuli hii. Sasa jibu swali langu: Viongozi wa wapigania uhuru wamefichwa wapi?", F.K. aliuliza. Mara Willy aligundua kwamba mpango wa kuwaficha viongozi wa wapigania uhuru ulikuwa wa busara sana.

"Sijui. Kawatafute wewe mwenyewe. Kwani sisi tulipogundua hawa makaburu ulipowaficha ulituambia?", willy alijibu kwa kiburi. Jibu hilo liliwafanya wahamaki. George alimrukia Willy na kumtia makonde ya haraka haraka mpaka Willy akapoteza fahamu kwa muda.

"Sisi hatutaki mchezo. Tumekuja Tanzania kuwatia hofu na kiwewe. Jibu lako litatusaidia kuua viongozi peke yake kuliko kufagilia mbali umati wa watu na mji mzima wa Arusha. Kipigo tutakachotoa kitasikika mpaka huko ahera. Nyumba hii imejaa silaha za kisasa za kuweza kuuteketeza mji mzima. Sasa sema ama hakika utaumia", F.K. alisema kwa hasira. Willy alifahamu fika kwamba hakuna mtu ambaye angethubutu kumuua, kwani alijuwa wao walitaka kufahamu viongozi wa wapigania uhuru wako wapi. Hilo ndilo jambo muhimu lililokuwa limewaleta.

"Sijui walipo, fanya unavyotaka", Willy alijibu.

"Umeyataka mwenyewe", F.K. alijibu huku akitoa kitu mfano wa saa kutoka kwenye mfuko wa shati na kukiwasha. Mara Willy alijisikia moto unamchoma kutoka kwenye ncha ya kidole mpaka utosini. Alijaribu kuvumilia. Lakini uchungu ulizidi na Willy akaanza kupoteza fahamu. Bila ya kujifahamu Willy alitoa sauti kali.

"Aaaaaa! Nitakuelezeaaa!".

Wakati F.K na George wanamkabiri na kumtesa Willy katika kile chumba cha mateso, Bon na Mike walikuwa wamefika kwenye seng'enge ya jumba la F.K. tayari kwa mapambano makali.

"Tusipite kwa chini maana wanayo televisheni watatuona. Tupite njia ya kawaida ila tujuwe kuwa wanatusubiri", Bon alisema.

"Sawa", Mike alijibu.

"Pande zote mbili, kushoto na kulia zinayo madirisha makubwa. Jambo la kufanya ni kujitahidi kuingia na sisi tuonane huko ndani", Bon alimweleza Mike. Wote waliangaliana ili kupeana moyo.

"Jihadhari sana", Mike alimweleza Bon.

"Na wewe vile vile", Bon alijibu huku akimkumbuka marehemu Rocky aliyekuwa amemuaga kwa namna ile.

"Jambo la kwanza ni kuangalia kama Willy angali hai. Nina wasi wasi juu ya maisha yake", Bon alimnong'oneza Mike huku wakiachana. Mike alimuonyesha ishara ya kumwelewa Bon. Wakiwa wamejificha kwenye vivuli wanaume hao wawili walilisogelea jumba la F.K. kwa tahadhari na hamasa kubwa.

Mike aliambaa ambaa katika upande wake; mara alisimama kimya na kwa tahadhari alijaribu kusikia kila aina ya jambo ambalo lingetokea. P.G alikuwa upande wa kaskazini wa jumba lile. Mara alimwona Hecke aliyekuwa achunge upande wa kushoto wakati yeye P.G akichunga upande wa kulia.Wakati P.G alipokuwa anaambaa na ukuta wa kulia huku bastola mkononi. Mike naye alishafika kwenye ukuta ule ule akiangalia akiangalia namna ya kufungua dirisha bila kuwashitua watu waliokuwa ndani.

Mara P.G. alisikia jasho jembamba likimtoka. Pale pale alijuwa kuwa alikuwa katika hali ya hatari kwani hali hiyo humtokea mara tu hatari inapobisha hodi. Mike ambaye alikuwa amevaa nguo nyeusi alisogea mbali kidogo kutoka alipokuwa kwani naye alihisi kitu kinatembea karibu na ukuta ule. Alibana chini ya mti huku macho yake yamezoea giza. Mara alikia kitu kama mti kinakatika! Alipoangalia umbali wa mita mbili kutoka chini ya mti alipokuwa amesimama aliona kitu kinatingishika. Alipoangalia vizuri aliona mtu anasogea. Mike alisimama kama mti mkavu. P.G. naye alikuwa ananusa nusa huku na kule kama mbwa wa polisi huku bastola yake tayari kufyatuliwa wakati wowote.

Alipotembea na kufika sehemu ya mita moja kutoka mahali Mike alipokuwa amesimama, naye alisimama. Wakati huo huo Mike aliruka kama risasi. Alimkumba P.G. na wote wawili wakaanguka chini. Bastola ya P.G. ilianguka kando na kuzitema risasi zake. mlio wake haukusikika ndani ya jumba kwa sababu bastola ile ilikuwa na kiwambo cha kuzuia sauti. Walipoinuka, Mike alimtambua P.G. mara moja.

"Ni bahati iliyoje kwangu P.G.? Nilidhani umenikimbia huko Nairobi. Sasa mimi na wewe", Mike alisema na kumshangaza P.G. ambaye hakutarajia kukutana na Mike Arusha.

"Umejileta wewe mwenyewe kwenye kifo chako Mike Maina. Baada ya kukumaliza wewe nitarudi Nairobi. Kisha nitajibadilisha na kuhakikisha vile vikaragosi vyako kwenye ofisi yenu ambao walitaka kuharibu kazi yangu nawafagilia mbali. Kwa kutumia uwezo wangu wa kipesa, nitahakikisha Masoga anakuwa mkuu wa idara yenu..." P.G. alisema. Kisha alikatisha sentesi ili amchukue Mike kwa ghafla ili amtie 'mapigo ya kifo', kama yeye alivyokuwa anayaita. Lakini P.G. alipotupa mapigo yake hayo Mike aliyazua yote kwa ufundi wa hali ya juu.

"Nilimwahidi Mwaura kwamba nitalipa kisasi chake kwa mikono yangu mwenyewe. Sasa P.G. umekufa", Mike alisema na pale pale aliona sura ya maiti ya Mwaura ilivyokuwa imepigwa risasi. Mori ulimpanda. Alijisikia akipata nguvu zisizo kifani. Mike alimtia pigo la kifuani P.G. ambalo karibu lingemdondosha. Lakini alijitahidi na kurudishia mapigo makali sana. Mike aliteleza mpaka chini. P.G alivuta upanga wake ili ammalize Mike. Upanga ulikuwa umefichwa kiunoni. Huku akiamsha upanga, tayari kumkata Mike P.G. alisema.

"Burian Mike!", wakati huo huo Mike alijiviringisha na upanga ukamkosa, P.G. alijirusha na kujitayarisha tena kumkata Mike. Alimkosa mara ya pili na mara ya tatu. Mike aliruka na kuumpiga teke mkono ule wenye upanga ambao ulianguka chini. Mkono wa P.G. ulikuwa umevunjika. Maumivu yalikuwa makali na Mike alichukua nafasi hiyo. Mike alimtia P.G. kipigo cha mbavu ambazo zilivunjika. P.G. aliamua kujikakamua lakini akawa amezidiwa mbinu.

"P.G. Afrika itashinda na Afrika Kusini itaondokana na udhalimu wa ubaguzi wa rangi na kuwa huru chini ya wazalendo walio wengi. Ukiwa huko ahera utaona kuwa unyama wenu haufui dafu kwa wapigania haki. Hata Mwenyezi Mungu yuko kwenye upande wa wanyonge", Mike alimwambia P.G. ambaye alikuwa anatokwa damu puani na masikioni. Alijua alikuwa amekaribia mwisho wake lakini aliamua kama ni kufa ilibidi afe kiume. Alikusanya nguvu zake zilizobakia na kumrukia Mike. Lakini Mike alikuwa tayari. Hivyo alimpisha P.G. ambaye alijigonga kwenye ukuta na kuanguka chini. Mike alichukua ule upanga wa P.G. na kuutumia kumkata kichwa.

"Malipo ya dhambi ni mauti", Mike alisema huku akiwa ameinua upanga na kuangalia maiti ya P.G. Akiwa bado amepandwa na mori alivunja dirisha kwa kutumia upanga akiwa tayari kwa mapambano makali.

"Leo ni leo. Liwalo na liwe. Sisi na washenzi makaburu ", Mike alisema huku akipanda dirisha ili ajitose ndani.
 
Kidi kudi lete mkuu, huyu Gamba kabanwa huyu. lete hata chp 2 tu wakati tunasubiri.
 
H O F U

MAMBO BADO

IV

Baada ya kumtelemsha Willy, Nyaso alielekea New Arusha Hoteli huku akiwa na mawazo mengi sana juu ya Willy. Kitu kimoja kilimshangaza sana na jinsi alivyokuwa ametokea kumpenda kijana huyo. Alikuwa amempenda ghafra kiasi cha kuhatarisha maisha yake wakati alikuwa hamjui sawa sawa kijana huyu.

"Kweli dunia ni msongamano", Nyaso alijisemea huku akiegesha gari karibu na hoteli.

"Mtoto huyo", dereva mmoja wa taksi kati ya wale walioegesha nje ya New Arusha alimnong'oneza mwenzake.

"Sijui mtoto huyo ana nini. Labda F.K. amesafiri kwani namwona anayo njemba moja hivi", dereva mwingine alijibu.

"Ni kweli hata mimi njemba huyo nimemwona. Jamaa mwenyewe mkali na vitu anavyoweka toka chini mpaka juu ni vya ukali tupu", dereva wa tatu alisema.

"Yule ni saizi yake siyo huyo F.K. ambaye anafuja mtoto wa watu bure", dereva wa pili aliongeza huku wakichekelea. Wakati huo Nyaso alishatoka kwenye gari na alikuwa anapotea hotelini. Macho ya watu hao yakimfuata yeye.

"Ama kweli Mungu ana upendeleo angalau kwa kiumbe yule", kijana mmoja wa mapokezi alimnong'oneza mwenzake baada ya Nyaso kuwapita na kusimama akisubiri lifti.

"Huyo msichana mimi simwangalii kwa sababu nikifanya hivyo najisikia msisimko. wakati najuwa fika kwamba hata nishitakie mbingu, siwezi kumpata", mwenzake alijibu.

"Si lazima kupata kila kitu ukipendacho. Hata macho pekee yanatosha kuangalia tu. Mimi ninapoona sura yake humsifia Mungu muumba; halafu kusema kwamba kuna wanaume duniani waliobahatiwa", yule kijana wa kwanza alisema kwa masikitiko.

Bila kujuwa kuwa watu walikuwa wanauguwa roho kutokana na sura yake murua. Nyaso alipanda lifti. Alikuwa na wazo moja tu kwamba kama angekuta akina Bon wamerudi angewataka wamfuate Willy. Alifikiri kwamba kama kweli F.K. amemuua Tondo hata Willy atauawa kama hakujihadhari.

Nyaso alifika kwenye chumba cha Willy. Alibisha hodi lakini hakupata jibu. Alibisha mara ya pili lakini kukabaki kimya. Aligonga tena mara hii kwa nguvu lakini bado hakujibiwa. Mara alitokea kijana mmoja mhudumu katika hoteli alisema huku akitabasamu.

"Samahani dada, nimeona jamaa wanaondoka haraka haraka".

"Wangapi", Nyaso aliuliza.

"Wawili", yule mhudumu alijibu.

"Ahsante", Nyaso aliitikia huku nusu akitembea nusu akikimbia, alielekea kwenye ngazi. Alikuwa na wazo la kuwafuata akina Bon na Mike huko kwa F.K. kwani aliamini Willy alikuwa kwenye hatari. Yule mhudumu alimwangalia Nyaso kwa butwaa.

"Ama kweli duniani kuna wanaume! Mimi nikiwa na miadi na msichana kama huyu siwezi kutoka hata itokee nini. Labda niambiwe mama yangu kafariki", yule mhudumu alijisemea mwenyewe.


Wakati mapambano makali yalipokuwa yanaendelea kati ya Mike na P.G. Bon alikuwa anafanya kazi ya kuingia ndani ya jumba la F.K. Hakupata kipingamizi kikubwa. Alipofika kwenye ile sehemu ya kushoto, aliona maiti ya yule askari aliyeuawa na Willy. Aligundua kuwa Willy alikuwa amepitia njia hiyo. Wakati anaangaza ili kuona Willy alikuwa ameingilia dirisha gani, alimwona yule askari mwingine akija. Bon alibana sawa sawa na ukuta akimwangalia askari anasogea kwa wasiwasi na hofu kubwa. Hofu yake iliweza kumfanya yule askari afike mahali alipokuwa Bon bila kuhisi kitu.

Bon aliyekuwa amebana mithili ya kinyonga afanyavyo kunasa inzi, alisubiri mpaka wote wakawa sambamba. Alimvuta na kumtia kabari kisha akamnyang'anya bastola. Alimpekuwa na kukuta hana kitu. Pale pale akimwamrisha.

"Kama unataka kuishi zaidi, nipeleke alipo Willy Gamba. Najuwa yuko ndani", Bon alibahatisha. Hofu ni kitu kibaya sana. Binadamu anaposhikwa na woga, hupoteza uwezo wa kuamua, hivyo akatenda yale ambayo asingeyafanya katika hali ya kawaida.

"Usiniue, twende nikuonyeshe", Hecke alisema kwa hofu.

Hecke alijua hiyo ndio ilikuwa nafasi yake ya mwisho. Alijuwa angemfikisha Bon kwa George, basi huo ndio ulikuwa mwisho wake hivyo Hecke alimwongoza Bon mpaka kwenye chumba cha mateso.
 
H O F U
SEHEMU YA KUMI NA MOJA

FUNGA KAZI

"Hapa", sema sasa nakupa sekunde moja", F.K. alimwambia Willy. Willy ambaye alikuwa amejitahidi kupitisha muda akitafuta njia ya kujiokoa alijuwa kuwa sasa amepatikana. Mara wazo lilimjia ghafla ... F.K. alikuwa ameshika chombo mkononi. Kazi ya chombo hicho ilikuwa ni kuendesha (kwa mbali), mashine ya umeme ambayo ilikuwa kwenye mti ambao Willy alikuwa amefungwa..... Kama angeweza kukata umeme huo kwa njia yoyote ile, basi mfumo mzima wa chumba kile ungeathirika.

Huku akijifanya kana kwamba alikuwa hajapata fahamu sawa sawa, alichunguza kwa chati ile nguzo alikokuwa amefungiwa. Aligundua kuwa ilikuwa na magurudumu chini. F.K. na George walikuwa hatua moja mbele yake. Hivyo Willy aliamua kutenda jambo ambalo wasingeweza hata kufikiria maisha yao yote. Lakini kwa bahati Willy hakupata nafasi ya kutenda kitendo hicho kwani vitu viwili vilitokea ghafla.

Mlango wa nyuma ulifunguka ghafla na kwa nguvu Bon alimsukumiza ndani Hecke. Hecke alimkumba George na F.K. kutoka kwa nyuma na wote wakaingukia ile nguzo alikofungiwa Willy. Kukatokea kishindo kikubwa.

"Kisanduku hicho hapo juu", Willy alipiga kelele.

Kana kwamba walikuwa wamepanga shambulizi hilo kutoka kushoto. Mike alivunja dirisha kubwa la kioo. Huku akiwa na rungu na upanga mikononi, alitumbukia ndani kupitia dirishani. Alikuwa amekatwa na vipande vya kioo lakini alionekana kutotambua. Vitendo hivyo vilitokea ghafla mno kiasi kwamba George na F.K. walipoteza sekunde mbili ama tatu kabla ya kujua nini kilikuwa kimetokea.

Hapo hapo Bon na Mike walichukua nafasi hiyo kufanya kitendo kimoja kwa haraka. Mike alikata kamba alizokuwa amefungiwa Willy kwa kutumia upanga mkali. Bon alikipiga risasi kile kisanduku kama alivyoelezwa na Willy. Mara chumba kikawa giza. Kisanduku kile ndicho kilikuwa kikitumika kuendesha vyombo vya chumba kizima cha mateso.

Kitu cha kwanza ambacho George na F.K. walifanya ilikuwa kujihami. Kama njiwa, George aliruka na kupitia kwenye diridha ambalo Mike alikuwa ameingilia. Lakini pamoja na vurugu hilo Willy alikuwa amemwona. Alitenda vitendo karibu kwa wakati mmoja. Alifungua kamba na kuruka dirishani akimfuata George.

F.K. alijiviringisha na kumkumba Bon mpaka chini. Halafu alipitiliza mpaka kwenye mlango na kukimbilia ukumbini. Bon aliinuka na kumfuata. Hecke aliliwahi lile rungu aliloingia nalo Mike. Alihamaki na kumpiga Mike akaenda chini. Upanga ulimtoka Mike mkononi.

Hecke aliukimbilia ule upanga, lakini kabla hajaushika Mike alimpiga teke la farasi ambalo lilimpeperusha mpaka akaenda chini. Wakiwa wanaonana vyema kutokana na mwanga uliokuwa unatoka kwenye chumba cha pili. Mike alimrukia tena Hecke na kumtia dhoruba ya kichwa wakati Hecke alipokuwa anajaribu kusimama. Hata hivyo, wote wawili walianguka chini. Dhoruba ya Mike ilimfanya Hecke aone nyota na barabara iendayo ahera. Mike alisimama haraka na kuchukua upanga wake. Kama alivyofanya P.G. aliikata shingo ya Hecke na kichwa chake kikaanguka chini.

"Makaburu wenzako watakaposikia juu ya staili ambayo umechinjwa, bila shaka watagwaya, kamwe hawatathubutu kuichezea Afrika huru", Mike alijisemea kimoyomoyo. Akiwa na upanga wake mkononi. Mike alitoka mbio na kuwafuata wenzake ili afahamu ni kitu gani kilikuwa kikifanyika.

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom