Riwaya: 'hofu'

Riwaya: 'hofu'

HOFU
ARUSHA
III

Ilikuwa saa mbili na nusu asubuhi. Peter Gerrit alikuwa anazungumza na maafisa wa Uhamiaji na Ushuru wa Forodha wa upande wa Tanzania. Alidai alikuwa anakwenda Arusha kuhudhuria mkutano wa wapigania uhuru. Paspoti yake ilimtambulisha kama Askofu Peter Jackson kutoka Zimbabwe. Alipitishwa haraka haraka bila kushukiwa. Wakati ule ule Mike Maina alikuwa na mazungumzo ofisini kwa Mkurugenzi wake ofisini.

"Kama Willy yuko Arusha, basi wasiwasi wangu umekwisha", Mike alisema.

"Kwa vipi?".

"Kwa sababu hawa wageni wa Peter ni majasusi wa makaburu na tayari wako Arusha. Aidha Peter yuko Arusha ambako ndiko alikokimbilia ili kuungana na wenziwe".

"Sawa kabisa. Sasa?", Mkurugenzi aliuliza.

"Sasa naomba umwalifu mwenzako huko Dar es Salaam kuwa mimi niko njiani kwenda kuungana na Willy na wenzake. Hii ni lazima kwani nilimwahidi marehemu Mwaura kwamba nitalipiza kisasi dhidi ya Peter Gerrit", Maina alisema.

"Unayo ruhusa", Mkurugenzi alisema. "Heri uende kuongeza nguvu dhidi ya majahili haya yenye nia ya kuhujumu mkutano wa ukombozi kusini mwa Afrika".

"Ahsante, mzee", Maina alishukuru.

"Nakutakia kila la heri".

"Nashukuru".

"Ukifika Arusha utamkuta Willy New Arusha Hoteli. Atakuwa na habari zako. Matayarisho mengine yako tayari kama kawaida", Mkurugenzi alimalizia.

Mike aliondoka. Wakati anatelemka ngazi alianza kumfikiria Will Gamba.

Walikuwa wamefanyakazi pamoja huko Angala kwa mara ya mwisho.

"Mbona itakuwa hatari", alijisemea huku akimwemwesa. Aliangalia saa yake ilionyesha kuwa ni saa tatu asubuhi.

"Chakula cha mchana leo nitakula mjini Arusha". Maina alijisemea tena.

ITAENDELEA
 
HOFU
ARUSHA

IV

"Hallo, naomba kuzungumza na ndugu Hamisi".

"Wewe ni nani?", sauti ya Katibu Muhtasi ilisikika.

"Mwambie ni mdogo wake aitwaye Willy".

"Mbona yeye analo jina la Ki-islamu na wewe na Kikristo? Utakuwaje mdogo wake".

"Kamwulize".

"Haya, babasubiri".

Baada ya muda kitambo Willy alisikia sauti kwenye simu. "Hallo, Hamisi hapa".

"Willy. Shikamoo, mzee".

"Marahaba. Vipi unaingia mji wa watu bila kuwaona wenyeji?".

"Hivi sasa ndio nawaeleza wenyeji kuwa nipo", Willy alisema.

"Sawasawa. Vipi, sasa unakuja?".

"Nisubiri. Nitakuwa ofisini kwako mnamo dakika tano zijazo".

"Willy alikuwa amepiga simu kutoka kwa rafiki yake karibu tu na ofisi ya upelelezi ya mkoa. Hivyo haikumchukulia muda mrefu kufika ofisi hapo.

"Eh, wewe binti ndiye unayetaka kujua ndugu za mkubwa wako wa kazi? Haya niulize vizuri au umeshamwuliza?", Willy alimwambia Katibu Muhtasi.

Msichana yule alimwangalia Willy kwa jicho la kuibia. Alimwona ni mvulana mwenye sura ya kupendeza na nadhifu. Roho ilimdunda.

"Aha, wewe ndiye Willy", aliuliza.

"Bila shaka", Willy alijibu.

"Kaka yako anakusubiri. Amesema ukifika uingie moja kwa moja", yule msichana alisema huku akilembua macho.

Willy naye alimtolea tabasamu la mwaka akamwacha amebung'aa.

Alifungua mlango na kuingia ndani ya ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa.

"Lo! Mwanaume huyu anaweza kukutia kiwewe. Anavutia hasa", yule msichana alibaki anajisemea kimoyomoyo.

Willy alifungua mlango na kuingia ndani ya ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa mkoa.

"Karibu, Willy", Hamisi alitoa tabasamu.

"Ahsante, mzee", Willy alimjibu Hamisi.

"Kazi iliyofanyika jana usiku nimearifiwa".

"Vizuri".

"Sijui watu hawa wameweza vipi kuingia maana polisi na sisi pia tulifanya tulivyoweza kuhakikisha kwamba watu wanaostahili tu ndio wale wanaingia nchini".

"Mzee Hamisi, lazima ufahamu kuwa watu hawa ni majasusi wa hali ya juu. Hivyo usione ajabu jinsi walivyoingia kwani hiyo ni moja ya kazi yao".

"Ni kweli Willy. Mimi nimeogopa sana. Jana usiku mpigania uhuru mmoja aliuawa kati ya saa tisa na saa kumi huko Maunti Meru Hoteli. Alikuwa chumbani kwake. Hii inaonyesha kwamba, kutokana na kazi mliyofanya, ni dhahiri kwamba siyo hao tu. Kuna kundi kubwa la majasusi tayari liko hapa mjini. Hivi sasa tunakabiliwa na upinzani mkubwa wa kutisha. Ingawa hata wewe uko hapo".

"Hii ni kazi na sisi tuko hapa kwa ajili ya kazi hii. Tunachokiomba ni Mungu atusaidie tuweze kuyasaka na kuyaangamiza majahili hayo, ili mkutano uanze hapo kesho kama ulivyopangwa. Lakini nakubaliana na wewe kwamba kazi kubwa lazima ifanyike, na tutaomba ushirikiano wenu".

"Sisi tuko hapa masaa ishirini na nne na hatutalala".

"Vizuri. Sasa ningependa kujua kama mmekagua hoteli zote ili kuhakikisha kuwa wageni wote waliojiandikisha kulala kwenye hoteli hizi wanatambuliwa sawasawa?".

"Hilo limefanyika baada tu ya kukuta Wazungu wamefariki". Hamisi alijibu. "Polisi pamoja na vijana wangu wamefanya ukaguzi wa hoteli na nyumba za kulala wageni. Ajabu ni kwamba hata wale Wazungu waliouawa walikuwa hawakujiandikisha kulala mahali popote".

"Basi hii ina maana hawalali hotelini wala katika nyumba za kulala wageni. Hivyo tunabaki na jibu moja; Majasusi hawa wanaishi nyumbani kwa mtu". Willy aliongeza.

"Sasa huyo atakuwa ni mtu gani?", Hamisi aliuliza.

"Hiyo ndio kazi yetu. Ninyi na sisi lazima tutafute watu hawa wanaishi nyumba gani. Ila tu nasema hii itawezekana kama vijana wenu watafanyakazi vizuri. Ili kuwa na uhakika naomba warudie kufanya ukaguzi kwenye hoteli hizo".

"Sawa, tutafanya hivyo. Lakini ikiwa ni nyumbani kwa mtu itakuwa ni vigumu", Hamisi alisema. "Kukagua nyumba hadi nyumba litakuwa jambo la ajabu".

"Sikiliza mzee", Willy alidakia. "Nyinyi hapa mnajua ni watu gani ambao mnahisi wanaweza kununuliwa kwa pesana kufanya kitendo kama hicho, watu mnaowashuku sharti kuwapeleleza usiku na mchana ili kufahamu ni nani wanaingia au kutoka kwenye nyumba zao. Kama mkihisi au kugundua kitu chochote, tafadhali tunaomba mtujulishe".

"Mawazo yako ni sawa kabisa. Hata hilo pia nitalitekeleza", Hamisi aliitikia."

"Kuna habari nilizoleta ofisini kwako kuhusu magari mawili ili yachunguzwe ni ya aikina nani, sijui kama umepata majibu?", Willy aliuliza.

"Ndio, lile walilokuwa wanaendesha wale Wazungu linaonekana halikusajiliwa hapa Arusha. Wala popote nchini Tanzania. Ni jambo la ajabu sana kwani namba za injini siyo namba za gari ya aina hiyo iliyoingia hapa nchini, bali gari aina ya Peugeot 505 na muundo wa karibuni. Tumepeleleza na kushirikiana na wenzetu wa Kenya nao wanasema nambari hiyo hawana", Hamisi alieleza.

"Basi anchana nalo. Je, na lile gari lenye namba ARKK 5677?".

"Gari hilo linamilikiwa na kampuni ya kitalii ya Nyota Tours and Safari ya hapa mjini Arusha. Lakini tumechunguza na wenye gari hilo. Wao wanasema gari hilo halikwenda uwanja wa ndege jana. Aidha ni watu tunaowaamini sana hapa mjini. Mwenye Kampuni hii ni Mhindi mmoja tajiri sana ajulikanaye kwa jina la Feroz Kassam; mtu ambaye anaaminiwa sana hapa mjini. Ni Mhindi wa aina yake hapa nchini.

Willy alikumbuka habari kuhusu Mhindi huyo. Alikuwa ameelezwa sifa zake siku nyingi. Hasa alisifika kutokana na misaada yake na utiifu wake kwa Chama na Serikali.

"Aha, ni nani aliyetoa majibu haya? Ni F.K mwenyewe, kama mnavyomwita, au ni mtu mwingine", Willy aliuliza.

"Hapana. Ni meneja mkuu wa kampuni hiyo anaitwa Chris Tondo".

"Huyo ni nani?".

"Nilisema ni Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo".

"Nina maana ya kuuliza ni mtu wa namna gani kutokana na mwenendo wake kiusalama?".

"Huyu amewahi kuwa afisa wa cheo cha juu katika Jeshi la Polisi na alistaafu kwa manufaa ya umma miaka iliyopita. Hatua hiyo ilichukuliwa kutokana na tuhuma kwamba alikuwa anasaidia wafanya magendo kuvusha mali nje ya nchi. Lakini toka siku hizo mpaka leo rekodi yake ni nzuri sana. Hajawahi kuwa na tatizo kiusalama wala katika maisha ya kawaida".

Willy alifikiri kidogo halafu akauliza tena. "Je, katika jalada lenu kuna habari kuhusu ilikuwaje mpaka akafanyakazi kwa F.K?".

"Hapana, bali tulifikiri aliombewa hiyo kazi na rafiki zake".

Willy alikuwa hakuridhika juu ya Chris Tondo. Aliinuka na kuaga akisema. "Nafikiri wewe tekeleza hayo mambo tuliyozungumza halafu tuonane baadaye".

"Sawa", Hamisi aliitikia.

Waliagana na Willy aliondoka kwa kupitia mlango wa Katibu Muhtasi.

"Wewe unaitwa nani?", Willy aliuliza.

"Naitwa Carol!" Yule msichana alijibu huku moyo wake ukimdunda.

"Iko siku Carol", Willy alimwambia Carol huku akifungua mlango na kupotea.

Alimwachia Carol kiu ya maelezo zaidi Willy alipoondoka pale ofisini aliamua kwenda Nyoka Tours and Safaris.

ITAENDELEA...
 
HOFU
ARUSHA

V

P.G aliwasili nyumbani kwa F.K kwa miguu baada ya teksi kumtelemsha karibu na ofisi ya mbao. Alisema amedai ndiko alikokuwa akienda ili kununua mbao za kununua. Alitembea kwa tahadhari kubwa. Ilikuwa saa nne na nusu alipojipenyeza kwenye ua wa nyumba ya F.K na kubisha hodi. F.K ndiye aliyefungua mlango. Alishangaa kumwona P.G.

"Hakuna mtu aliyekuona unakuja huku?", F.K alimwuliza huku uso wake ukionyesha huzuni na mashaka.

"Hakuna, F.K".

"Karibu ndani, P.G".

"Ahsante".

F.K alimwongoza P.G mpaka kwenye chumba cha siri. Majasusi wengine walikuwa ndani wanapumzika. Walipomwona walipomwona tu P.G wote walikaa kitako huku wakihisi kuna tatizo limetokea.

"Hebu tupe habari", F.K aliomba.

P.G alieleza yote yaliyotokea usiku ule na jinsi alivyokuwa ameamua kuja kuwaongezea nguvu wenzake baada ya kupoteza watu wake wote na kubaki yeye na mtu mmoja tu.

"Hivi nimemwacha Smith Namanga. Ataingia hapa mchana huu. Nimeona siyo vizuri sisi wote wawili kuja pamoja mchana huu", alisema P.G.

"Pole sana", walimjibu kwa pamoja.

Baadaye F.K naye alimweleza mambo yaliyokuwa yamewatokea.

"Hii ina maana kwamba mpaka sasa hivi mambo hayaendi vizuri. Lakini nina hakika tutashinda maana sasa tunajua nguvu za adui; na yeye hajui nguvu zetu wala maskani yetu". F.K alieleza.

"Sasa mipango ikoje", P.G aliuliza.

"Mipango iko kama ifuatavyo", F.K alieleza. "Usiku tutagawanyika mafungu mafungu. Kwanza lazima tuwamalize hawa watu watatu sababu ni kwamba sasa tunafahamu vyumba vyao na hoteli. Vile vile sasa tunafahamu mienendo yao. Muda mfupi tu uliopita Chris alinipigia simu. Amesema kwamba amepata habari kuwa Willy Gamba amemwambia Mkuu wa Upelelezi kwamba hakuridhika na maelezo kuhusu gari letu nambari ARKK 567. Ameongeza kuwa Willy angeendelea kufanya uchunguzi kuhusu gari hilo. Hivyo nimemwasa Chris ajaribu kumkwepa Willy maana huyo ndiye mtu hatari zaidi. Yeye ndiye aliyefanya mauaji ya jana".

"Je, huyu Mkuu wa Upelelezi yuko upande wetu?". P.G aliuliza.

"Ndio na hapana", F.K alijibu. "Huyu Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa ni mtu ambaye tumemsaidia sana kifedha. Zaidi ya hayo yeye anaamini kwamba sisi ni watu wanaotii sana Serikali. Kutokana na misaada yetu kwake, neno lolote linaloweza kutudhuru sisi yeye atatusaidia kwa kila njia. Lakini akijua ukweli katika swala kama hili, lazima atatuuza. Kutofanya hivyo kunaweza kuwa na yeye kupoteza kazi yake au hata kupewa adhabu kali ya kifo kama mhaini. Kusema kweli wanamwogopa sana Willy".

"Hao viongozi wa wapiganian uhuru watakaohutubia mkutano wameshaisha fika".

"Watatu wamefika na wengine wawili watafika jioni hii, kuhusu wale ambao wamefika tayari tumechukua habari juu yao. Mienendo yao pia tumeisha ifahamu. Hata wale wawili wakiingia tutapata habari zao. Kama ujuavyo P.G, mimi naaminika hapa kama mwanamapinduzi. Habari zozote ninazozitaka nazipatamoja kwa moja kutoka kwa watayarishaji wenyewe wa mkutano huo. Hivyo lazima tuwafungie kazi hawa viongozi leo usiku, halafu tuone kama mkutano utafunguliwa", F.K, alisema.

F.K alisema. "Sasa hivi natoka ili nikamilishe mipango ya usiku kwa kupata habari zaidi. Na wewe Peter, George atakupa mipango yote ambayo tumeifanya kwa ajili ya usiku. Kwa vile na wewe umeongezeka. ni dhahiri kwamba tutashinda. Tutatenda kitendo ambacho kitaiacha dunia nzima inagwaya".

"Vizuri. Mimi nitaelewana na George halafu nitapumzika maana mpaka sasa sijalala. Wewe kakamilishe mipango hiyo kuhusu kazi", P.G alijibu huku yeye na George wakielekea chumba kingine

ITAENDELEA
 
HOFU
ARUSHA

VI

Willy alikaribia ofisi za Nyota Tours and safaris. Hapo hapo alimwona msichana mrembo sana akitoka nje ya ofisi hiyo. Kila wakati Willy alipokutana na wasichana warembo namna ile aliwaona kama sumu kwake kwani alikuwa mgonjwa sana juu yao.

Willy alibana kwa mbali kidogo ili aweze kuyapa nafasi macho yake yapate chakula chake. Alipenda amwone vizuri mrembo huyu ambaye aliumbwa ili wanaume wajisikie raha. Willy aligundua kwamba hakuwa yeye peke yake aliyekuwa anamwangalia, bali wanaume wengine pia walikuwa wanalisha macho yao kwa chati.

Msichana huyu alitembea mpaka kwenye gari moja. Alitoa funguo kwenye pochi yake na kusimama ili afungue mlango. Willy alijuwa kuwa gari hiyo mpya aina ya Toyota KE 30, ilikuwa ya huyo msichana. Lakini hakushangaa kwani msichana mrembo kama yule angeweza kumpata mtu yeyote mwenye pesa akamnunulia kitu chochote. Hata gari angemnunulia ili mradi tu aridhike.

Wakati huyo msichana anaingiza funguo kwkenye tundu la kufuri katika mlango wa gari. Ghafra akatokea kijana. Alikwapua pochi yake halafu akakimbia. Huku akiwa ametoa jisu kali alitisha mtu yeyote ambaye angethubutu kumfuata. Yule msichana wa watu alitoa sauti kali yenye kutia hofu halafu akaanguka chini. Watu waliokuwa karibu walisambaa kwa kuogopa hilo jisu kali.

Willy ambaye alishuhudia kitendo hicho cha kijambazi, alianza kumfukuza yule kijana. Alipoona kuwa watu wote wamesambaa isipokuwa mtu mmoja tu aliyekuwa bado anamsakama, yule kijana alisimama kumsubiri Willy apambane nae ana kwa ana.

"Hunijui mimi eh? Mji mzima wananijua mimi ni nani... sogea nikukate kichwa ", alitamba yule jambazi kijana.

willy alimwendea kwa tahadhari kubwa huku watu wote wakipiga makelele kumsihi arudu nyuma kusalimisha maisha yake. "Rudi, rudi! Kimbia! huyo ni mwuaji! Anamaliza watu hapa".

Kama kwamba hasikii Willy alizidi kumsogelea yule jambazi. Mara yule jambazi alimvamia Willy kama mchezo vile. Willy alikwepa shambulizi la kwanza na lile jisu. Alimnasa mkono wake na kumkata mkono mmoja wa karate kwenye bega lile jisu lilianguka. Willy alilipiga ngwala lile jambazi mpaka chini. Kuona vile yule msichana alikimbia mpaka pale. Huku akiwa ameshikilia kiatu chake mkononi alimpiga na kisigino yule jambazi. Hapo ndipo watu wengine walipofika pamoja na polisi wa doria. Akiwa ameshika pochi aliyoporwa, Willy alimvuta kando yule msichana.

"Ahsante sana", msichana alimwambia Willy. "Ahsante bwana. Sijui nikushukuru vipi kwa kujitolea maisha yako ili kuokoa mali yangu".

"Sijali", Willy alisema. Kwa mtoto kama wewe. Kila mwanaume kamili yuko tayari kujitoa mhanga maisha yake".

Polisi alimfuata Willy akimtaka akatoe maelezo ya wizi huo katika kituo cha polisi. Lakini Willy alimnong'oneza Polisi huyo naye akamwacha huru. Huku amemfunga pingu jambazi yule na kundi la watu walimfuata. Polisi alianza safari kuelekea kituo cha polisi. Alimwacha Willy akizungumza na yule msichana hapo pembeni mwa barabara. Yule msichana alianza kutokwa na hofu na kurejea katika hali ya kawaida. Sasa alimwangalia yule kijana aliyekuwa ameokoa mali yake. Alikuwa kijana mwenye sura ya kupendeza sana. Vile vile alikuwa na kitu kingine ambacho ilikuwa vigumu kukieleza. Huyo kijana alisisimua damu yake.

"Ehe, unaitwa nani?", Willy alimwuliza.

"Naitwa Nyaso", msichana alijibu.

"Nyaso tu, basi?".

"Ndio, Nyaso tu basi! Na wewe waitwaje?".

"Mimi naitwa Willy".

"Oh, vizuri. Sijui nikupe nini Willy!".

"Usijali, sasa hivi nina shughuli. Tunaweza kuonana jioni mnamo saa kumi na mbili hivi, angalau kwa muda mfupi, niweze kukununulia kinywaji", Willy alimwuliza.

Nyaso alifikiri sana kwanza. Alimwogopa sana F.K. angechukia ikiwa angejua alitoka nje na mtu, hasa mtu mgeni. Hali hii aliipima na jinsi F.K. alivyokuwa hataki kumwona siku hizi kwa kisingizio eti alikuwa na shughuli nyingi. Alifikiria sana jinsi F.K. alivyokuwa amemkaripia eti kwa kumpigiapigia simu nyumbani kwake wakati yeye alikuwa na kazi nyingi. Kama namna moja ya kumkomoa F.K. Nyaso alikubali mwaliko wa huyu kijana ambaye alimsisimua damu.

"Sawa, una miadi!" Nyaso alijibu.

"Arusha, Oke, nichukue hapo New Arusha saa kumi na mbili kamili", Willy alisema.

"Nitafika bila kukosa", Nyaso aliahidi.

Huku akitingisha matako yake huku na huku, alielekea kwenye gari lake na kumwacha Willy ameshikwa na butwaa. Alipoingia ndani ya gari Nyaso alimrushia busu Willy ambaye alisikia kama vile moyo wake umekosa pigo moja. Nyaso alipopotea ndipo Willy alipokumbuka safari yake ya kwenda kwenye ofisi ya Chris Tondo, ambayo ilikuwa karibu na hapo alipokuwa. Vile vile ndipo alipogundua kwamba Nyaso alikuwa anatokea kwenye ofisi ile ile wakati alipovamiwa.

Chris Tondo alikuwa katika pilika pilika humo ofisini kwake. Alikuwa akikusanya makaratasi na kutatunza kwenye visanduku. Alifanya shughuli hii haraka ili atoke ofisini. Alikuwa ameambiwa na F.K kufanya hivyo ili Willy asije kumkuta.

Wakati huo huo Willy alifika kwenye ofisi za Nyoka Tours and Safaris.

"Habari za leo", Willy alimsalimia kijana mmoja aliyekuwa kwenye ofisi ya nje.

"Nzuri, mzee. Nikusaidie nini?".

"Naomba kumwona ndugu Chris Tondo".

"Una miadi naye".

"Yupo?", Willy aliuliza.

"Ndiyo yupo, lakini huwezi kumwona huna miadi", kijana alisema

"Mimi ni rafiki yake. Ukinirudisha bila kumwona halafu akasikia umefanya hivyo ujuwe wewe huna kazi", Willy alitishia huku akielekea kwenye ofisi iliyoandikwa Meneja Mkuu.

Aliwaacha wafanyakazi wote kwenye ofisi ile wakimwangalia wasijue la kufanya. Alifungua mlango na karibu wagongane na Chris Tondo ambaye pia alikuwa anafungua mlango huo ili atoke nje.

"Oh, pole sana", Willy alisema.

Tondo alipogundua huyo alikuwa Willy, alisikia moyo wake unapiga haraka na akashindwa kupumua sawasawa.

"Karibu", Tondo alijikuta amebabaika.

"Ahsante", Willy aliitika huku akifunga mlango nyuma yake.

"Hawa vijana hawakunieleza kuna mgeni", Tondo alisema huku akionyesha kukasirika.

"Samahani, kwa kweli wao hawana kosa kwani ni mie ambaye sikuwasikiliza", Willy alijibu.

"Ehe, nikusaidie nini ndugu...?".

"Willy Gamba", Willy alimalizia.

Tondo alishangaa kumsikia Willy akijitambulisha kwa jina lake la kweli kwani alifikiri angejificha. Hii ilimtia hofu zaidi."Ya, nikusaidie nini ndugu Gamba?".

"Natumaini wewe ni ndugu Tondo. Meneja Mkuu wa Kampuni hii?", Willy alimwuliza huku akimtazama machoni.

Moyoni Tondo alijua mambo yameanza kutibuka. Alijisikia kujuta kwani alifahamu jinsi gani Willy aliweza kusoma mawazo ya mtu aliyezungumza naye. Kitu hicho ndicho kilichomfanya Willy kufanikiwa katika kazi yake ya upelelezi. Tondo alitafakari alipoulizwa vile.

"Ndio", Tondo alitumia uzoefu wake wa kipolisi kujibu swali hilo. Kwani alifahamu majibu mafupi yalikuwa mazuri kwa mtu anayehojiwa.

"Mimi ni afisa usalama kutoka Dar es Salaam. Nimefika hapa kwa shughuli za kiserikali. Nimeshawishika kuzungumza na wewe niliposikia uliwahi kuwa afisa wa cheo cha juu katika idara ya polisi".

"Vizuri", Tondo alijibu huku akishangaa kuona jinsi Willy alivyokuwa akijieleza.

"Sijui uliwahi kufika kwenye uwanja wa ndege jana usiku?", Willy aliuliza.

Mate yalimkauka Tondo alipofikiri juu ya uwezekano kwa kwamba Willy alikuwa amemwona wakati anatoa upepo ndani ya gari. Tondo alijuwa watu kama hawa walikuwa hatari.

Baada ya kusita kidogo, alijibu kwa sauti hafifu. "Hapana!".

"Nasikia gari nambari ARKK 567 ni lenu?", Willy alimpachika swali Tondo.

"Ndio".

"Nani huwa analiendesha mara kwa mara?".

"Unajua sisi tunafanya kazi ya kuhudumia watalii. Hivyo tunayo magari mengi na madereva wengi. Hatuna dereva maalum kwa gari fulani", Tondo alijibu.

"Nani alikuwa anaendesha gari hilo jana?".

Tondo alisita kujibu kwani alijua jibu la swali hili lilikuwa muhimu sana kwa Willy.

"Jana halikutoka", Tondo hatimaye alijibu.

Willy alijua alikuwa ameongopa tena.

"Kwa nini, lilikuwa bovu?".

"Wakati tunapokuwa hatuna kazi nyingi, magari yetu hufungiwa tu katika gereji".

"Gereji yenu iko wapi?".

"Iko nyuma tu ya ofisi hii", Tondo alijibu.

"Kwa hiyo gari haliwezi kutoka bila ruhusa kamili", Willy alipendekeza.

"Kabisa".

"Oke, ndugu Tondo, vizuri. Samahani kwa kuchukua muda wako", Willy alisema huku akiwa amesimama tayari kuondoka.

"Hivi kuna jambo gani kuhusu hilo gari? Naona sina budi niulize", Tondo aliuliza.

"Wewe umekuwa afisa wa polisi kwa muda mrefu, kwa hiyo ni lazima unaelewa mambo haya", Willy alimjibu. "Wakati mwingine tunapata habari fulani fulani. Inatubidi kuchunguza na kuthibitisha, vinginevyo watu wanaweza wakaumia bure".

"Ni kweli", Tondo alijibu.

"Oke, kwaheri".

"Karibu tena, ndugu Gamba".

"Willy alifungua mlango na kutoka ofisi ya nje. Aliwaaga wale wafanyakazi wa ofisi ile.

Tondo alirudi akaa kitako kitini mwake na kuanza kufikiri.

Willy alipotoka tu nje alitembea haraka sana na kuzunguka nyuma ya ile ofisi. Huko aliona lango la kuingilia katika gereji. Alibisha hodi maana lilikuwa limefungwa. Mara mlinzi alifungua. "Tukusaidie nini, mzee", aliuliza yule mlinzi.

"Jana nilipewa lifti na ndugu Tondo. Lakini kwa bahati mbaya nilisahau miwani yangu ndani ya gari lake. Sasa amenishauri nije nikaangalie kama bado imo iwapo gari hilo halijatoka", Willy alijibu.

"Ahaa, gari alilokuwa anaendesha jana. Si ni lile ARKK 567?".

"Nafikiri", Willy alijibu.

"Basi, limetoka kwenda kujaza mafuta kwenye kituo chetu", alijibu mlinzi.

"Siyo kitu, nitamwambia yeye anitazamie miwani hiyo wakati gari likirudi".

"Haya, kwaheri", mlinzi alijibu huku akirudisha lango.

"Kwaheri", Willy alijibu huku akimwemwesa.

ITAENDELEA
 
HOFU
ARUSHA

VII

Ilikuwa saa saba na nusu za mchana. Willy, Bon na Rocky walikuwa wakila chakula pale pale New Arusha Hoteli. Ilikuja simu ambayo ilimhitaji Willy.

"Wewe mzee ndiye Willy Gamba?", mhudumu mmoja alimwuliza Willy.

"Ndio".

"Kuna simu yako".

"Sawasawa", Willy alisema huku akiweka kisu na uma kwenye sahani.

Alikwenda kusikiliza simu.

"Hallo, Willy hapa", Willy alisema baada ya kuunyakua mkono wa simu na kuupachika katika sikio lake la kushoto.

"Hapa ni mapokezi. Kuna mgeni wako ngoja uzungumze naye".

Hallo, Mike Maina", sauti ilisikika.

"Wewe unafanya nini hapa", Willy aliuliza kwa mshangao kwani alikuwa hakumtegemea.

"Nimekuja kukutafuta. Kwani wewe unafanya nini hapa", Maina aliuliza.

Willy alifahamu kwa nini Chifu alikuwa amemtafuta; Maina alikuwa ameletwa ili kuongeza nguvu.

"Njoo kwenye ukumbi wa maakuli. Utatukuta kwani nafikiri una njaa", Willy alimwambia.

"Nitakuja kwa haraka kama jeti", Maina alijibu.

Maina alimkuta Willy na wenzake wakiendelea kula chakula.

"Hallo Maina, karibu", Willy alimkaribisha Maina huku wenzake wakisimama.

"Ahsante Willy, mambo?", Maina aliuliza.

"Mambo ni segemnege", Willy alijibu huku akivuta kiti na wote wakakaa.

"Hebu nikujulishe kwa hawa ndugu zetu hapa. Naamini hamfahamiani", Willy alisema. "Huyu ni Bon Sipele wa wapigania uhuru na huyu ni Rocky Malele wa Zimbabwe".

Kisha Willy alimgeukia Maina na kusema. "Na huyu jamani ni Mike Maina kutoka Kenya".

Wote walisalimiana.

"Nilipata habari zake Angola alipokuwa naye. Mlifunga kazi takatifu", Bon alisifia.

"Basi, huyu ndiye Mike Maina", Willy alisisitiza.

Mhudumu alifika mezani na Maina akaagiza chakula.

Wakati huo Willy, kwa sauti ya chini, alikuwa anaeleza sifa za kipelelezi za kila mmoja.

"Basi mambo yanazidi kujipa", Rocky alisema.

"Sasa Mike, tupe habari za huko Nairobi. Nikisoma sura yako nahisi kuna mambo", Willy alichokoza.

"Haya, nisikilize kwa makini halafu na nyinyi baadaye mnijulishe mambo ya hapa", Mike alisema.

Mike aliwaeleza yaliyotokea Nairobi huku akiendelea kula chakula. "Nilipopita mpakani leo nilishangaa. Nilikuta rafiki yangu Peter Gerrit kaishapita. Alitumia jina la Peter Anderson na kudai yeye alikuwa ni Askofu kutoka Zimbabwe akija kuhudhuria mkutano wa wapigania uhuru. Kwa sababu hiyo maafisa usalama na uhamiaji wakampitisha haraka. Hivyo yuko hapa na mnaweza kuona wenyewe hali ya mambo".

"Kwa hiyo rafiki zangu", Willy alimalizia. "Mji huu umeingiliwa na balaa. Bila shaka damu itamwa

gika. Tuwe tayari kujitoa mhanga ili wale watakaobaki wawezi kufaidi matunda ya uhuru. Uhuru ni kitu muhuimu kwetu na kwa vizazi vijavyo".

Bon alisema. "Na sisi watu wa Afrika Kusini tunaamini kwamba kabla ubaguzi wa rangi haujatokomezwa ni lazima damu ya wazalendo itamwagika. Tuko tayari kwa yote hayo. Kama mnavyosikia, hata vijana wadogo wameamua kujitoa mhanga ili kutokomeza utawala wa Makaburu kwa faida ya walio wengi. Kwa hiyo Willy, mimi niko tayari kufa kwa ajili ya nchi yangu. Lakini kabla sijafa, nitahakikisha nao wanakiona cha mtema kuni".

"Kwa sasa hivi mipango gani?", Mike aliuliza.

"Kwanza kabisa nimempigia simu mtu wetu hapa, ambaye ni Mkuu wa Upelelezi Mkoa, Ndugu Hamisi", Willy alieleza. "Ameweka vijana wa kumfuatilia Chris Tondo. Ninayo imani kuwa yeye anaweza kutufikishia walipo hawa majasusi. Sina shaka mtu huyu anahusika nao kwa namna fulani".

"Kama inao uhakika", Mike alishauri. "Kwanini tusimufuate sisi wenyewe, ikibidi tumsakame mpaka atueleze tu? Wewe mwenyewe unajua kuwa tuna uwezo wa kumfanya mtu hata mwenye kichwa ngumu kama, atatapika maneno".

"Hapana, tusifanye haraka, maana watu kama hawa wanazo mbinu nyingi", Willy alieleza. "Lakini hata sisi tunazo mbinu zetu. Tunaweza kumfanya akatueleza mahali walipo bila kutumia nguvu zetu nyingi. Unajuwa bado tunahitaji nguvu zetu hasa kwa kupambana na hawa majahili", alieleza Willy, halafu akaanza kuwapa mipango kwa ajili ya usiku ule".

"Sisi tutasimama badala ya hawa viongozi wa wapigania uhuru. Sisi pamoja na wao ndiyo wanaowindwa. Hivyo kuanzia saa tatu tutajipoteza maana watu hawa watakuwa wanatuvinjari".

"Tumekuelewa barabara", Rocky alidakia. "Na ninaamini mipango yako ni sawasawa kabisa".

"Mike, kula", Willy alishauri mara mhudumu alipoleta chakula. Mhudumu alipoondoka. Willy na wenzake waliendelea na mazungumzo yao.

ITAENDELEA
 
HOFU
ARUSHA

VIII

Ilikuwa saa nane za mchana wakati F.K aliporudi. Alikuta wenzake wamelala. Walihitaji usingizi kwani usiku huo walitarajia kuwa macho. Alienda moja kwa moja kwenye chumba ambamo Peter Gerrit, George na Dave walikuwa wamepumzika.

"Karibu, F.K", George alimkaribisha. Yeye tu ndiye aliyekuwa hajalala. "Una mapya yapi?".

"Ninayo mengi", F.K alijibu. Wakati huo huo Peter na Dave wakazinduka kutoka usingizini.

"Kwanza Tondo nimemkuta ofisini?", F.K aliuliza. "Anasema kuwa Hamisi alimpigia simu na kumweleza kuwa Willy alimshauri aweke vijana wa usalama kumfuatilia na kuripoti mienendo yake yote. Hivyo nimemshauri akitoka ofisini aende moja kwa moja nyumbani kwake na asitoke".

Aliposikua hivyo George aliinuka kitandani.

"Hapana F.K", George alisema na kuinuka kitandani. "Tondo lazima auawe".



"Auawe? Hapana, mtu huyu ametusaidia sana", F.K alimtetea Tondo. "Lazima aishi ili naye aweze kufurahia ushindi. Bila yeye mimi nisingeweza kufanya yote niliyofanya hapa nchini. Taarifa zote za kijasusi nilizoleta ni kutokana na msaada wake, kwani yeye alikuwa afisa wa cheo cha juu katika jeshi la polisi. Hapana, George, Chris Tondo lazima aishi ili afaidi matunda ya ushindi wetu. Vile vile nimeamua kwenda naye Afrika Kusini baada ya kazi ya hapa".

Wale majasusi wengine walimwangalia kwa macho makali yenye kutoa onyo.

"Nafikiri litakuwa jambo la busara kwako kufanya hivyo", P.G. alimwasa F.K.

ITAENDELEA
 
HOFU
ARUSHA

X

Wakati wenzake walipokuwa wamepumzika, mnamo saa kumi za mchana, Willy alimpigia simu ndugu Mbeki. Mbeki alikuwa Mwenyekiti wa kamati ya kutayarisha mkutano. Alikuwa amefikia Maunt Meru Hoteli.

"Hallo. Maunt Meru hapa", mpokeaji simu alisikika akisema.

"Nipe chumba 321", Willy alisema.

"Subiri".

"Hallo, Mbeki hapa".

"Aha, nimepata habari kuwa unanitafuta".

"Sawasawa, naomba uje tuonane hapo kwenye klabu ya Kituo cha mikutano ya Kimataifa. Unaifahamu?", Willy aliuliza.

"Basi, jitahidi uwe pale katika muda wa dakika kumi zijazo".

"Haya".

Willy aliweka simu chini na kutelemka chini.

Alichukua teksi na kuelekea AICC Klabu.

Alipofika alisubiri kidogo na Mbeki akawasili. Willy alikuwa anajulikana sana mahali hapo. Aliongozana na Mbeki mpaka kwenye kibanda kimoja, halafu wakaagiza vinywaji.

"TUmekuwa na wasiwasi sana baada ya matukio makubwa ya jana", Mbeki alianza.

"Hiyo ndiyo sababu imetuleta hapa", Willy alijibu.

"Ulinzi wa Polisi unaonekana ni dhaifu sana", Mbeki alisema. "Viongozi wote wanawasili leo jioni, tayari kwa mkutano wa kesho. Sasa mimi ninao wasiwasi. Kuna mtu ambaye anatoa habari zetu nje, lakini hatujui ni nani".

"Mimi nashauri kuanzia sasa mtoe habari kwa mtu yeyote. Ikibidi punguzeni watu hata kwenye kamati ya matayarisho. Bakizeni watu tunaowafahamu fika. Sasa nisikilize kwa makini. Nataka ufanye kama nitakavyokueleza. Usikose hata chembe, kwani ukikosea, kutatokea balaa isiyoelezeka", Willy alitahadharisha.

Alianza kumweleza Mbeki juu ya mipango yote ya usalama wa mkutano kuanzia dakika ile mpaka mwisho wa mkutano. Alimweleza mipango ya ulinzi wa wajumbe, na viongozi mashuhuri wa wapigania uhuru.

ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA NANE

NYASO

Ilikuwa saa kumi na mbili juu ya alama, Nyaso alipoegesha gari lake hapo New Arusha Hoteli. Willy alikuwa anaranda pale nje ya hoteli akimsubiri.

"Nimeamini kuwa unajuwa kuweka ahadi mtoto we, Wasichana wengi wa Kiafrika hawaweki muda maanani", Willy alisema huku akifungua mlango wa gari na kuingia ndani.

"Wacha kutuonea, siku hizi tumebadilika, hujui kuwa wakati huu unajulikana miaka ya elekttroniki! Watu lazima kwenda kwa wakati", Nyaso alijibu huku akiondoa gari.

"Unanipeleka wapi?", Willy aliuliza.

"Nilipiga simu 'Kambi ya Fisi' na kuomba watuwekee nyama ya kuchoma", Nyaso alijibu.

"Hiyo ni maridadi", Willy aliitikia aliitikia halafu akaendela. "Vipi maisha hapa".

"Mwenyezi Mungu anatusaidia".

"Umeishi hapa Arusha kwa muda mrefu?".

"Miaka mitano hivi".

"Mimi nakuja hapa mara kwa mara lakini sijawahi kukuona, sijui huwa unajificha wapi?".

"Mbona maswali mengi? Unajuaje, huenda mwenzio nimewekwa kinyumba?", Nyaso alimtolewa Willy jicho la kiwiziwizi.

"Unasema kweli, hebu nisiulize maswali mengi kwani ninaweza kujiumiza roho bure".

"Pole sana".

Waliendelea na safari mpaka 'Kambi ya Fisi'.

Walipowasili Willy aligundua kuwa wahudumu wa pale walikuwa wanamfahamu sana Nyaso. Hiyo ilitokana na kwamba walipowasili Willy aliona wahudumu wakimkimbilia Nyaso na kuwapa mahali pazuri pa kukaa.

"Nyama uliyoagiza karibu itakuwa tayari", mhudumu alisema. "Utasubiri kidogo tu".

"Hakuna tabu", Nyaso alijibu wakati wakikaa kwenye viti.

Watu wengi walikuwa pale ambapo pia walikuwa wamekuja kuchoma nyama.

"He, leo ni maajabu! Umemwona Nyaso kaja na mwanaume! Siyo maajabu haya?", kijana mmoja aliwauliza vijana wenzake wapatao watano.

"Huenda ni kaka yake", kijana mwingine alisema. "Huoni kuwa hata kijana mwenyewe anayo sura nzuri".

"Watu wanasema eti Nyaso hana ndugu, sasa huyo kaka katoka wapi", kijana wa kwanza alidadisi.

"Ya nini kuingilia maisha ya watu? Ndio sababu nyinyi waswahili hamwendelei. Mnapenda kuchunguza maisha ya wengine huku yale ya kwenu yanawashinda. Kama huyo kijana kaka yake au bwana yake nyinyi inawahusu nini? Iwapo mtu anavutiwa si heri akatafute nafasi yake halafu abahatishe tu? Vinginevyo kama Nyaso kapata bwana mwingine na kumwacha F.K hicho ni kilio chake F.K", kijana mwingine aliyeonekana kuwa mkubwa kidogo kuliko wengine aliwaasa wenzake. Hivyo iliwabidi kujali yaliyowaleta.

"Unafanya kazi wapi?", Willy alimwuliza Nyaso wakati wakinywa vinywaji baridi.

"Sasa hivi sifanyi kazi yoyote, ila naadaa kitabu".

"Eh, kitabu kuhusu nini?".

"Kinahusu uchumi wa nchi yetu"."Wewe ni mtaalam wa mambo ya uchumi?".

"Ndiyo. Ninayo shahada ya kwanza katika uchumi".

"Ahaa vizuri sana. Hata mimi ni hivyo hivyo".

"Na wewe unafanya kazi gani?".

"Mimi niko Dar es Salaam ambako ninafanya biashara".

"Na hapa Arusha umekuja kufanya nini?".

"Mimi ni shabiki wa siasa, hivyo nimekuja kusikiliza mkutano wa hawa wapigania uhuru".

Nyaso alimwangalia bila kuamini masikio yake.

"Mkutano kama huu utakusaidia nini na wewe ni mfanya biashara?", Nyaso aliuliza.

"Nimekwambia kuwa mimi ni shabiki wa siasa. Madhumuni ya shabiki wa kitu chochote siyo kupata faida ya mali, bali kufanya mioyo yao ifurahi".

"Lakini wewe huelekei kuwa mtu wa kushabikia kitu hivi hivi tu".

"Sijui sasa", Willy alijibu kisha akaendelea. "Mimi nilifikiri unafanya kazi Nyoka Tours and Safaris maana kabla hujavamiwa na yule jambazi nilikuona unatoka kwenye ofisi zao".

"Hapana, mwenye kampuni hiyo ndiye bwana yangu", Nyaso alijibu huku akiangalia chini.

Willy alisikia damu inamsisimka.

"Una maana ya F.K au Chris?", Willy aliuliza.

"Ni nani katika nchi hii ambaye hamjui F.K? Yule ni mtu maarufu sana".

"Basi, ni huyo F.K".

"Hongera, Nyaso kwani kwa mara ya kwanza nimeona msichana wa Kiafrika ambaye ni binti wa mvulana wa Kihindi kiwaziwazi bila kujificha".

"Nimekwambia Willy dunia inageuka.

Willy aliisifu tena nyota yake, kwani kama kweli msichana huyu alikuwa bibi yake F.K, basi bila shaka alimfahamu sana Chris Tondo. Ilikuwa ni bahati kwamba Willy, kama alivyofikiri, angejua mengi kutoka kwa Nyaso.

"Bahati yangu mbaya. Mimi nilifikiri nimepata mchumba kumbe wameisha niwahi", Willy alinung'unika.

Nyaso alimwangalia Willy na kumhusudu. Alifikiri ingekuwa furaha iliyoje kama angeolewa na kijana mzuri kama yule. Akimlinganisha Willy na F.K, Nyaso alijilaumu. Alijua alikuwa anaishi na F.K kwa sababu ni yeye tu amabaye aliweza kumtimizia mahitaji yake kipesa, hakuwa na mapenzi yoyote juu ya F.K. Lakini sasa matayarisho ya mpango wake yalikuwa yanakaribia kukamilika. Nyaso alikuwa na nyumba tayari. Alikuwa na gari na pesa pia. Hivyo angeweza kuanza opereshani wakati wowote. Alipofikiri hayo, Nyaso alijisikia machozi yanamlengalenga.

"Nini sasa, dada umekuwa nini?", Willy aliuliza alipomwona msichana huyu akitokwa na chozi la hudhuni. Na ilikuwa ajabu kwamba Nyaso alipotokwa na machozi ndiyo alivyozidi kupendeza.

"Usijali, kila mtu huwa na matatizo yake. Nimekumbuka jambo ambalo limenigusa moyoni, lakini siyo kutokana na wewe".

"Basi, pole".

"Ahsante".

Kutokana na uzoefu wake wa siku nyingi kuhusu wasichana, Willy aligudua kwamba Nyaso hakuwa na furaha katika uhusiano wake na bwana yake. Hivyo aliamua kutumia nafasi hiyo ili aweze kujua mengi zaidi juu ya Chris Tondo na F.K.

"Wewe na F.K mnakaa pamoja", Willy aliuliza.

"Hapana".

"Wewe unakaa wapi?".

"F.K alininunulia nyumba huko Kijenge, na yeye anaishi kwenye jumba lake huko Themi Hill".

"Anasubiri nini asikuoe msichana mrembo hivi. Anafikiri watu wengine hawakuoni?", Willy alimtolea Nyaso tabasamu la kumlainisha.

"Hiyo ni shauri yake".

"Au ni kwamba wazazi wako hawataki wewe uolewe na Mhindi?", Willy aliongeza. Mara aliona machozi yanamlengalenga Nyaso mara ya pili.

"Hapana", Nyaso alijibu.

Willy alihisi wazo fulani lilimjia akilini mwake.

"Nyaso, wazazi wako wako wapi?".

Nyaso hakumjibu Willy. Wote wawili walikaa kimya kwa muda mpaka nyama ilipoletwa.

"Basi, sahau yote hayo unayofikiria ili tule nyama na kufurahi", Willy alimshauri Nyaso.

"Uliniambia jina lako ni Willy nani?", Nyaso aliuliza kwa unyonge.

"Willy Gamba".

"Nimewahi kusikia jina kama hilo mahali fulani", Nyaso alisema.

"Kama siyo redioni, basi ni kwenye magazeti".

"Sijui, labda ni mtu mwingine. Kama ujuavyo, baadhi ya watu wanayo majina yanayofanana".

"Willy sijui nianzie wapi", Nyaso alisema halafu akasita.

"Naona kama kuna kitu kinakukera rohoni", Willy alisema. "Nakushauri ukiseme tu. Mimi ni kijana mwenzako. Unajua Nyaso, kama kuna jambo linalokukera moyoni, dawa ya kuleta nafuu ni kumwambia mtu. Ni vizuri zaidi ukamwambia mtu kama mimi ambaye hatufahamiani. Hivyo itasaidia sana kwani huwezi kuwa na wasiwasi kwamba nitawaambia watu wengine. Mimi sijui marafiki zako na wewe hujui marafiki zangu".

"Willy, nitakupa siri yangu ya maisha ambayo hakuna mtu mwingine anayeijua isipokuwa mimi mwenyewe. Pamoja na mwito wako wa kutaka nikueleze, huenda nisingekueleza. Lakini kwa kuwa wakati wa kutekeleza mpango umekaribia, nitakueleza tangu mwanzo.

Mara mhudumu alifika kwenye meza yao.

"Nyama ya hapa ni safi sana", Willy alinena.

"Ndiyo sababu ilinifanya nikulete hapa hapa", Nyaso alidakia.

"Msee, hapa nyama ni safi kabisa kabisa", mhudumu aliongeza.

"Wewe ni Mchagga?", Willy aliuliza.

"Ndiyo".

"Biashara kweli mnaijua", Willy alimsifia.

"Utafanya nini, babangu?", mhudumu aliitikia halafu akaondoka zake.

"Hebu endelea", Willy alimkumbusha Nyaso.

"Mimi nilizaliwa miaka ishirini na sita iliyopita nikiwa ni mtoto wa tatu wa Dk. Soni", Nyaso aliendelea. Baba yangu alikuwa daktari wa mifugo na mama yangu alikuwa muuguzi. Miaka saba baada ya mimi kuzaliwa tulivamia na majambazi wakati wa usiku, huko nyumbani Moshi. Majambazi hayo yalivunja nyumba na kuua watu wote wa familia yangu isipokuwa mimi tu. Mtumishi wetu wa nyumbani, akiwemo mlinzi wetu waliuawa pia. Hata mimi nilidhaniwa kuwa niliuawa. Majambazo yalipompiga mapanga dada yangu mkubwa aliniangukia na sote wawili tulianguka chini. Majambazi walifikiri kuwa nami nilikuwa tayari nimekufa".

Aliposema hayo, Nyaso alinyamaza kidogo huku machozi yakimtoka.

Willy ambaye alikuwa akimsikiliza Nyaso kwa makini na mshangao alimshauri asilie.

"Unajuwa kuwa hapa tuko hadharani, hivyo nakuomba usilie".

"Sawa", Nyaso alijibu, halafu akaendelea. "Walipoamini kuwa wameua kila mtu, ndipo alipotokea yule mtu ambaye alikua amekodi majambazi. Lengo lake lilikuwa kuhakikisha kwamba kazi aliyowatuma ilikuwa imetekelezwa ndipo awalipe ujira wao. Mtu huyo nilimwona na kumtambua. Halafu nafikiri nilizirai, kwani nilipopata fahamu nilijikuta hospitali huku nimezungukwa na wauguzi pamoja na askari polisi. Baada ya siku mbili niliruhusiwa kutoka hospitali. Nilichukuliwa na polisi kisha niliulizwa maswali mengi. Ni ajabu kwamba sikuweza kukumbuka jambo lolote. Mwisho wake waliniachia kisha nikachukuliwa na Masista wa madhehebu ya Kikatoliki. Wao ndio walionitunza na kunipekeka shule hadi nilipomaliza kidato cha sita".

Nyaso alinyamaza ili kumeza mate ya kulainisha koo.

"Ulisema huyo mtu ulimwona na kumtambua, lakini ulipopata fahamu ukawa hospitali hukuwa na kumbukumbu tena?", Willy aliuliza.

"Ndiyo, lakini hebu nikwambie jambo nililotaka ulisikie: Kwa sababu hiyo, mimi sina baba wala mama, sina hata ndugu yeyote. Ndugu wa pande mbili za wazazi wangu walikaa kimya. Hakuna hata mmoja wao aliyejitokeza kunichukua kutoka kwa masista ili anitunze. Ufahamu Willy kwamba mimi nilikuwa mdogo hivyo sikujua mambo mengi. Ndio sababu naitwa Nyaso tu, basi!".

Nyaso alinyamza kidogo na kisha akaendelea. "Maisha yangu ya utoto yalikuwa ya ukiwa ingawaje wafadhili wangu walinipa kila kitu nilichohitaji. Sasa jambo la ajabu ni kwamba, nilipokuwa nasoma Kidato cha Sita, wanafunzi wa shule ya sekondari ya Kibosho tulipatwa na ajali. Baada ya kumaliza muhula wa kwanza shule ilifungwa. Tulikodishiwa gari litupeleke mjini Moshi tayari kwa safari ya kwenda likizo. Lakini humo njiani, kabla ya kufika mjini, gari lilipinduka. Mimi nilikuwa mmoja wa wanafunzi waliopata majeraha kichwani, hivyo nikalazwa K.C.M.C. Nilipokuwa nimelazwa niliota ndoto kuhusu siku ile ya mauaji ya familia yetu. Ndoto hiyo ilinionyesha mambo yote yaliyokuwa yametokea siku hiyo; mpaka mtu yule aliyekodi majambazi yaliyoteketeza familia yangu. Niligutuka toka usingizini na kujikuta nimezungukwa na madaktari na huku jasho likinitoka mwili mzima".

"Nilipoulizwa na madaktari nilikuwa najisikia vipi, niliwajibu kuwa nilikuwa najisikia salama wote walishangaa! Hapo hapo muuguzi mmoja alinieleza kwamba wakati nikiwa usingizini nilikuwa napiga kelele na kuhangaika. Alisema kwamba hata wao walikuwa na wasiwasi kuwa huenda nilikuwa karibu kukata roho".

"Ina maana njozi ile njozi hiyo ilikufanya umkumbuke yule mtu aliyekodi majambazi", Willy aliuliza kwa shauku kubwa.

"Ndiyo, na siku hiyo hiyo niliruhusiwa nikatoka hospitali nikiwa mzima kabisa. Mtu yule nilikuwa namfahamu tangu nikiwa mtoto, kwanza alikuwa rafiki yake marehemu baba yangu", Nyaso alisema na kuanza kulia tena.

"Jikaze ili uweze kunimalizia kisa hiki", alidakia Willy.

"Je, ukimwona sasa unaweza kumtambua".

"Ndiyo, kwani mara nilipotoka usingizini nilimkubuka barabara. Zaidi ya hayo, mtu huyo anaishi hapa hapa Arusha na ni mtu mkubwa sana. Wakati huo nilipata wazo la kwenda polisi kueleza kisa hicho, lakini nilijuwa hakuna hata mtu mmoja ambaye angeniamini. Kwanza miaka mingi ilikuwa imepita, na pili, mtu huyo alikuwa tayari kizito. Watu wangefikiri mimi nimekuwa kichaa kwa sababu ya ajali".

"Wewe uliamua kufanya nini", Willy aliuliza.

"Nilifikiri sana juu ya hali hii, halafu nikaamua kulipiza kisasi".

"Niliamua kuchukua hatua mimi mwenyewe, kwani Serikali ilishindwa kuwakamata na kuwaadhibu wauaji hao. Niliona ni bora kuendelea na masomo kwanza, kitu ambacho nimefanya mpaka nikahitimu elimu ya Chuo Kikuu. Baada ya masomo niliwaomba ruhusa masista ambao walinitunza ili niweze kufanya kazi serikalini. Waliniruhusu na kunitakia kila la heri. Lakini mpaka sasa huwa ninakwenda kuwajulia hali kwa sababu nawaona kama wazazi wangu. Unaelewa, wakati nikiwa shuleni nilikuwa naitwa Nyaso wa masista".

"Sasa wewe umeamua kulipiza kisasi kwa njia gani?", Willy aliendelea kuuliza.

"Usiniulize swali hilo. Tangu nimeota ndoto ile sasa yapata miaka minane. Kwa muda huo nilikuwa nikipanga na kupangua. Sasa naamini nimefikia uamzi sahihi juu ya namna gani nitalipiza kisasi. Jukumu hili ni langu mwenyewe. Willy. Najua nitafanya nini. Kulipiza kisasi ni lazima".

"Nilipohitimu masomo ya Chuo Kikuu nilipangwa kufanya kazi katika Wizara ya Uchumi na Mipango. Niliomba kituo changu cha kazi kiwe Arusha, kwani hapo ndipo alipo mbaya wangu".

"Je, mtu huyo anajuwa kuwa wewe ni mtoto wa Dk. Soni?".

"Hapana. Hawezi kujua kwa sababu mimi situmii jina hilo. Najulikana kama Nyaso wa masista, basi. Na hii imeweza kunisaidia sana, kwani huyu mtu naonana naye mara nyingi, lakini hawezi kunitambua. Yeye ni mtu maarufu hapa, hivyo ni rafiki wa watu maarufu kama akina F.K".

"Ahaa, kwa hiyo urafiki wako na F.K una uhusiano na mtu huyo?".

"Siyo hivyo. Urafiki wangu na F.K ulitokana na sababu tofauti kidogo".

"Kuhusu mpango wangu wa kulipiza kisasi, mimi nilihitaji uwezo mkubwa kipesa. Ilinibidi nifanye kila liwezekanalo ili nipate mtu anayeweza kunipa uwezo huo. F.K ndiye aliyeonekana kuwa mtu wa kukidhi haja yangu. Hivyo nilitupa ndoano yangu, na F.K akanasa. Kwa hiyo lengo langu limetimizwa; fedha za kuendeshea operesheni yangu sasa ninazo. Ninaweza kuanza pole pole kutekeleza mpango wangu. Sasa najisikia nafuu kwani nimemweleza mtu historia yangu".

Willy alimwangalia Nyaso kwa makini na mshangao vilevile. Mara alikumbuka maneno aliyoambiwa na mama yake mzazi: Mwanangu Willy kila mara jihadhari na wasichana warembo kwani wana mambo.

"Lo, kumbe Nyaso umeishi maisha ya taabu sana, lakini napenda nikushauri kuwa siyo vizuri kulipiza kisasi kwani matokeo yake yanaweza kuwa mabaya zaidi; janga linazua janga. Hivyo ninaku....".

"Ngoja ngoja, Willy", Nyaso alimkata kilimilimi. "Mahali nilikofikia siyo pa kurudi nyuma. Janga gani linaweza kunitokea mimi zaidi ya kufa? Mie siogopi kufa. Unajua kwa nini familia yangu ilipouawa Mungu alininusuru? Alifanya hivyo ili niweze kulipiza damu ya familia yangu ambayo ilimwagika bila makosa".

"Je, unajua kwanini mtu huyu alipanga familia yako iangamizwe?".

"Ndiyo, najua lakini siwezi kukwambia. Nimekwambia mambo mengi ambayo nafikiri yanakutosha. Najua wasiwasi wako unatokana na kuwaza kwamba nikauawa pia. Mimi niko tayari kufa ili niungane na familia yangu huko peponi. Kula nyama uondoke wala usiniangalie kwa masikitiko hivyo".

Pale pale Willy alijuwa kuwa Nyaso alikuwa amepania kutekeleza matakwa yake. Lakini alimsikitikia sana msichana yule kwani alijua kwamba alikuwa mgeni katika mambo kama hayo. Hivyo alijua kwa vyovyote Nyaso angekuwa na mwisho mbaya, hata kama mipango yake ilikuwa mizuri. Hata hivyo Willy alimwona Nyaso alikuwa msichana jasiri na kwa sababu hiyo alimheshimu sana. Kutokana na hali hiyo, Willy aliamua kumpasha mambo ambayo yangemfanya msichana huyu awe tayari kusaidiana naye, hasa kuhusu Chris Tondo na F.K.

"Sikiliza Nyaso", Willy alisema. "Tangu nilipokuona mara ya kwanza nilijua wewe ni mtu wa aina gani. Wewe ni msichana mwenye sura nzuri sana. Ninathubutu kusema umependelewa sana jinsi ulivyoumbika. Vile vile wewe una akili nyingi sana na usafiri kinyume cha wasichana wengi. Unao uwezo wa kumdu mapambano".

"Hebu wacha kunipamba na sifa nyingi". Nyaso alimkatiza. "Mimi nimeshasikia nikipewa sifa za kila aina".

"Sikiliza, Nyaso. Sifa ambazo umezisikia ni kutoka kwa wanaume walaghai wenye kukutaka mapenzi. Nia yangu siyo hiyo, la hasha. Kama hali ya mapenzi ikitokea kati yangu na wewe, basi itakuwa katika hali ya kawaida na siyo kwa kughilibu. Kitu ninachotaka kusema ni kwamba nilikuwa sijaona msichana aliyebarikiwa kama wewe mpaka akawa na akili nyingi, sura nzuri isiyoelezeka na pia hekima na ujasiri. Kwa sababu ya yote hayo. nimekuheshimu. Ndiyo sababu nami nimeamua kukueleza juu ya maisha yangu mwenyewe na kwanini niko hapa".

Willy alimtolea Nyaso jicho la mahaba.

"Usiniangalie hivyo na kuniumiza roho", Nyaso alilalamika. "Sema tu unavyotaka kusema".

"Kama nilivyokwambia hapo awali", Willy alisema. "Mimi naitwa Willy Gamba. Watu wengi wananijua kama mfanyabiashara. Lakini ukweli ni kwamba mimi ni mpelelezi katika Idara ya Upelelezi Tanzania".

"Kweli", Willy alimthibitishia.

"Nimewahi kusikia tetesi kama hizo", Nyaso alidakia. "Ndiyo sababu nikakwambia nimewahi kusikia jina lako. Lakini watu wengine husema kuwa habari zote kuhusu jina hilo huwa ni hadithi tu na wala hakuna mtu wa namna hiyo ambaye anaishi hapa duniani. Lakini tangu nilipokuona kwa mara ya kwanza, niliona vitendo vyako vinafafana na vile vya huyo Willy anayesifika. Sasa naamini kwamba ni wewe hasa. Nafikiri ninayo bahati kubwa kukufahamu. Sina shaka wewe utakuwa mwali wangu katika operesheni ninayotarajia kuendesha ili kullipiza kisasi".

"Usijali, ngoja kwanza nikueleze kilichonileta hapa", Willy alimwambia Nyaso. "Baadaye utaona kwamba mambo mengine pamoja na hayo ya kwako ni kama mchezo".

"Sawa, Willy, ninakusikiliza".

"Basi tega masikio nikueleze toka mwanzo hadi mwisho".

Willy alimweleza Nyaso yote yaliyokuwa yametokea, kwanini alikuwa Arusha na tuhuma zake dhidi ya Chris Tondo na huenda F.K vile vile.

"Kwa hiyo Nyaso", Willy alimaliza. "Ninakuomba unisaidie kwa kunipa habari ambazo zinaweza kunisaidia katika mapambano dhidi ya majasusi wa Afrika Kusini. Ushindi wetu ni wako vile vile".

Nyaso aliyekuwa anamsikiliza Willy kwa makini, alimtolea tabasamu la mwaka kisha akasema. "Usiwe na wasiwasi, Willy. Mtu kama wewe ndiye nilikuwa natafuta tokea siku nyingi. Tangu sasa hivi mimi niko mikononi mwako. Msaada wowote utakaohitaji kutoka kwangu hesabu kuwa umepata".

Willy alijisikia joto la mwili likipanda, lakini akaamua kutoruhusu hali hiyo iendelee mpaka hapo kazi iliyokuwa mbele yao itakapokuwa imemalizika.

"Nyaso", Willy alisema. "Ninakuomba unieleze yote kuhusu maisha ya F.K pamoja na shughuli zake kibiashara. Yale yanayohusu maisha yenu kama bibi na bwana unaweza kuyaacha".

Nyaso alimweleza Willy yote anayojuwa kuhusu F.K., Chris Tondo pamoja na shughuli za Nyoka Tours and Safaris.

"Kama unahisi hapa majasusi wamejificha mahali, basi ni nyumbani kwa F.K", Nyaso alisema. "Kama nilivyokueleza mimi na F.K tumekuwa marafiki kwa muda mrefu. Lakini nimefika nyumbani kwake mara chache. Nyumba yenyewe imejengwa kinamna, kwani White House ni Wihite house hasa. Ni kama Ikulu; hata sijui unaweza vipi kuingia ndani ya jumba hilo".

"Je, F.K hajawahi kukueleza kitu chochote ambacho kinaweza kunisaidia kuingia ndani ya jumba hilo?".

"Kitu ninachokumbuka ni kwamba, wakati penzi letu lilipokuwa bado moto moto, F.K alinichukua ili nikalale kwake. Hii ilikuwa moja ya safari tatu tu ambazo nimewahi kulala kwake. Wakati tulipokuwa tunazungumza, nilionyesha wasiwasi wangu kuhusu yeye kuishi peke yake katika jumba kubwa vile. Nilimweleza kuwa angeweza kushambuliwa na majambazi kwani alijulikana kuwa ni mtu tajiri sana. Lakini yeye alinihakikishia nisiwe na wasiwasi kwani jumba lake lilikuwa limejengwa kwa namna yake. Aliongeza kusema kuwa kama angevamiwa, angweza kutumia njia za siri ambazo ziko chini kwa chini mpaka akatokea nje ya seng'enge, ili akawajulishe polisi. Kwanza nilifikiri alikuwa anajigamba tu. Unajuwa wanaume wengi hupendelea kujionyesha mbele ya wanawake kwamba wao ndio wenyewe. Lakini baada ya kusikia tuhuma dhidi yake, naamini alikuwa anasema kweli".

"Sehemu yake ina eneo gani?", Willy aliuliza.

"Ekari kumi na mbili", Nyaso alijibu.

Willy aliangalia saa yake na kuona ilikuwa saa mbini na nusu usiku.

"Nyaso", Willy aliomba. "Hebu twende ukanionyeshe kwa Chris Tondo. Ningependa nizungumze naye kidogo".

"Sawa Willy, lakini huenda tusitumie gari langu kwani linajulikana sana. Hapo nyumbani kwangu kuna gari la rafiki yangu kutoka Nairobi, aliliacha pale halafu alipanda ndege kwenye Dar es Salaam. Heri tukatumie gari hilo".

"Mawazo yako ni sahihi. Je, lina namba za Kenya?".

"Ndio".

"Haya twende. Si wewe mwenyewe unataka pilika pilika? Sasa basi zimeanza", Willy alimtania Nyaso.

Waliunuka toka vitini na kuondoka.

ITAENDELEA
 
Willy Gamba nakupa 5. Asante sana mkuu kula like kubwa hap kaka. Umenikumbusha mbali sna. Chonde chonde naomba uimalize yote usiiche nusu ukapotea.
 
Willy Gamba 1 kula like kwa jinsi unavyoshusha nondo kwa mkupuo mkupuo.
 
Last edited by a moderator:
Aisee.. Willy Gamba 1 asante sana umeshusha nondo ya uhakika mkuu salute sana sana! chonde hakikisha unamalizia hii kitu
 
Last edited by a moderator:
dah yaani sjalala ndo namaliza kusoma muda huu. kazi nzuri sana W. Gamba
 
HOFU
NYASO

II

Chris Tondo alikuwa anaishi sehemu inayojulikana kama 'Corridor Area! Wakati Willy na Nyaso walikuwa wanaelekea huko kupitia barabara ya Haile Sellasie, walipishana gari dogo aina ya Datsun.

"Gari hilo ni la F.K. na anaendesha mwenyewe. Kwa kawaida huwa haliendeshi gari hilo. Mara nyingi huwaachia watumishi wake na yeye anatumia ile Benz yake, kwani anazo gari tatu hapo nyumbani kweke", Nyaso alimwambia Willy mara walipopishana na ile Datsun.

F.K. alikuwa hakuwatambua.

"Huenda amechoka kuendesha magari makubwa", Willy alisema.

"Nyumba ya Chris Tondo ni ya nne kutoka nyumba hiyo hapo".

"Basi, egesha mahali pazuri na mimi nitatoka kwa muda wa robo saa", Willy alimwambia Nyaso.

"Mimi nitaingia katika nyumba hii kumwona rafiki yangu", Nyaso alisema "Nitatoka baada ya robo saa ambapo wewe pia utakuwa tayari. Tafadhali Willy, kama watu hawa ni hivyo unavyohisi, basi ni watu wabaya, ni vizuri kuchukua tahadhari wasije wakakudhuru".

"Usijali, tutaonana baada ya dakika hizo", Willy alisema huku akitokomea gizani.

Nyaso aliyekuwa anamwangalia Willy huku akimwemwesa alijikuta anajisemea kimoyomoyo. "Jinsi nilivyomzoea! Utafikiri tumeishi naye miaka mingi. Hivi sasa ninavyojisikia ovyo kumkosa hiyo robo saa".

Nyaso aliondoka akaenda kubisha hodi mlangoni kwa rafiki yake.

Willy aliambaa kwenye nyufa za nyumba jirani na ile ya Chris Tondo. Aliwaona vijana wawili kwa mbali wakipotea kwenye giza la michongoma ya nyumba iliyotazamana na ile ya Chris Tondo. Mara alitambua wale walikuwa vijana wa Hamisi. Kwa kuwa hakutaka wamwone, Willy alijipeneyza kwenye sehemu ya kushoto ya ua. Kwa ustadi kama wa paka Willy alipanda ukuta na kudondoka uwani bila kishindo.

Aliangaza huku na kule na kwa bahati nzuri aliona dirisha kwa upande huo liko wazi. Aliona taa ilikuwa inawaka kwenye chumba upande wa sebule. Willy alihisi kilikuwa chumba cha kulala cha Chris. Basi alijinyanyua, akakwea hadi ndani ya nyumba kupitia dirishani. Huku bastola ikiwa mkononi mwake. Willy alijikuta kadondoka bafuni. Alipofungua mlango taratibu alijikuta yuko kwenye njia nyembamba iliyokuwa inatenganisha vyumba. Aliamua kwenda sebuleni ambako alihisi Chris angekuwepo.

Willy alifungua mlango kwa ghafla ili asimpe nafasi Chris ya kuwa tayari kujihami. Lakini alishangaa kukuta chumba kile kilikuwa kitupu. Taa ya mle chumbani ilikuwa inawaka na Willy aliona jinsi chumba kile kilivyokuwa cha fahari isiyo kifani. Alijongea na kuelekea kwenye chumba kingine ambacho kilikuwa kinawaka taa pia. Hata hivyo, Willy alishangazwa na ukimya uliokuwa ndani ya jumba hilo.

Alifikiri labda walipopishana na gari la F.K. Nyaso alikuwa hakuona vizuri kwani huenda hata Chris alikuwa kwenye gari lile lile. Wakati anafikiri yote hayo, aliamua kuendelea na mpango wake. Kwa kasi kama umeme Willy alifungua mlango wa chumba hicho. Kumbe loo mle ndani alikuta maiti tatu! Baada ya kuangalia vizuri aligundua kuwa watu watatu hao waliuawa kwa kupigwa risasi. Walikuwa ni Chris Tondo, msichana mmoja mrembo sana ambaye Willy alihisi kuwa alikuwa binti yake Chris pamoja na mlinzi mmoja kutokana na mavazi yake..

"Bila shaka kazi hii ni ya F.K.; ameniwahi", Willy alijisemea kwa uchungu.

Bila kupoteza muda, alitoka nje kwa kupitia njia aliyokuwa ameingilia. Alipokuwa nje alimwona Nyaso naye anatokea kwenye lango la nyumba ya rafiki yake, walipoingia ndani ya gari, Willy alimwambia Nyaso.

"Hebu endesha gari haraka ili tutoke kwenye sehemu hii. Chris, mlinzi wake pamoja na binti yake wameuawa. Nipeleke hotelini kwangu kwani sasa kazi imeanza", Willy alimwambia Nyaso.

"Huyo ni F.K. Willy, ndiyo sababu tulikutana naye akitoka huku", Nyaso alisema.

"Bila shaka", Willy alikubaliana na Nyaso.

"Masikini Betty kauawa bure mtoto wa watu. Mimi ndiye niliyemfahamisha kwa Chris, oh Betty! Willy uliyohisi ni kweli. F.K. utakiona ", Nyaso alisema kwa uchungu. Aliendesha kuelekea New Arusha Hoteli. Willy alipoangalia saa ilikuwa saa tatu na robo. Alikuwa amechelewa robo saa lakini alikuwa amejua mengi.

ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA TISA

KABLA YA USIKU WA MANANE

Wakati Willy na Nyaso walipokuwa wanaelekea New Arusha Hoteli. F.K. alikuwa amewasili nyumbani kwake. Alikuwa akiwaeleza wenzake kazi aliyokuwa ameifanya.

"Kazi mliyonituma nimeimaliza tayari", F.K alisema.

"Vema", George alijibu.

"Sasa ni saa tatu na dakika kumi, mipango yetu itaanza saa ngapi?", P.G aliuliza.

"Hebu nisikilize kwa makini", George alieleza. "Nilikuwa kwenye chumba cha habari na nimewasiliana na Kamanda wa KULFUT huko Afrika ya Kusini. Nilipompa habari kuwa tayari tumepoteza watu wawili alikasirika sana na kuniambia kwamba asingependa kusikia kitu kama kile tena. Alisema jambo hilo lilikuwa kinyume cha nia ya matakwa ya Serikali ya Afrika Kusini ambayo ni kuleta 'hofu' isiyoelezeka dhidi ya wapigania uhuru, nchi zilizokuwa mstari wa mbele na Afrika huru kwa ujumla.

"Ameongeza kuwa usiku wa leo lazima uwe usiku wa kazi. Hapo kesho Kamanda anataka kusikia habari za kilio kutoka Tanzania na Afrika nzima. Kama mjuavyo mkutano wa wapigania uhuru umepangwa kuanza kesho saa tatu. Lakini amri tuliyopewa ni kwamba mkutano huo usiwepo, na badala yake kuwe na vilio. Wale watakaokuwa wamesalimika watakuwa wanaikimbia Tanzania bila mpangilio wowote. Wakati dunia nzima itakapokuwa inalaani kipigo tutakachokitoa kwa Tanzania, majeshi yetu ya Serikali ya Afrika Kusini yatavamia Msumbiji, Botswana, Zambia, Zimbabwe na Angola hapo kesho. Watu wa nchi hizo watabaki wamechanganyikiwa. Wakati dunia nzima inagwaya, jeshi letu la polisi litafyekelea mbali watu weusi wenye kuleta ghasia ndani ya Afrika Kusini. Tutawachinja kama kuku na hivyo kuzima kabisa maasi wanayoita ukombozi".

"Ndio mnaona umuhimu wa kushinda katika mapambano yetu. Kamanda wetu amenipa majina ya viongozi wanne wa wapigania uhuru. Ameongeza kwamba hao wakiuawa wote kwa siku moja, itakuwa ni kipigo cha kutosha hata kuzima vugu vugu la maasi katika Afrika kwa muda mrefu. Majina ya viongozi hao ni Mbeki, Jamana, Ntamazi na Basweka. Je, F.K una habari kuwa watu hawa wamewasili?".

"Ndiyo, wote hawa wamefikia Maunt Meru Hoteli na namba za vyumba vyao ni hizi hapa", F.K alisema huku akimpa kijikaratasi chenye maelezo kamili juu ya viongozi wake.

"Umefanya kazi nzuri, F.K", George alimpongeza F.K.

"Ahsante, kazi nzuri lazima ifanyike George ili lengo letu liweze kutimizwa", F.K alisema.

"Sina shaka", George alisema. "Viongozi hawa wanalindwa sana. Askari polisi, maafisa usalama na hao wapelelezi mashuhuri watatu wamewazunguka viongozi hao, hasa kutokana na mambo yaliyotokea jana. Tumshukuru F.K kwa kuhakikisha usalama wetu na kukaa bila adui kujua tuko wapi huku tukipata habari bila matatizo".

"Hayo yote ni matunda ya mafunzo yako thabiti, kama Mwalimu wangu", F.K alijibu kwa unyenyekevu.

"Hivyo", George alieleza. "Mpango ni kama ifuatavyo; kwanza kabila lazima tuwakorofishe hawa wapelelezi watatu. Bila kufanya hivyo, kazi yetu ya kuwafyekelea mbali viongozi hawa itakuwa ngumu. Kwa hiyo, mimi nimepanga kwamba ni lazima Willy Gamba auawe leo kabla ya usiku wa manane, inaonekana huyu ndiye ngao ya wengine waliobaki. Yeye akiuawa wenzake watabaki wamegwaya na kuchanganyikiwa wasijue la kufanya. Hawataweza kuchukua hatua yoyote kwa leo kwani watahitaji muda mrefu kutayarisha mpango mpya, bila kuwa na Willy Gamba. Hii itatupatia muda sisi kufunga kazi, Kabla ya jua kuchomoza, kazi yetu itakuwa imekamilika".

"Mtu huyu atauawa vipi", P.G aliuliza.

"Mpango wa kumuua Willy utakuwa kama ifuatavyo, F.K na vijana watatu watakwenda nyumbani kwa mzee Hamisi. F.K alieleza kwamba familia ya mzee Hamisi iko likizo, hivyo yeye anakaa peke yake kwa wakati huu. Vile vile tunafahamu kuwa Willy na mzee Hamisi wanafanya kazi bega kwa bega, kwani habari zote kutoka kwa bosi wa Willy zinapitia ofisini kwa mzee Hamisi. Hivyo F.K na wenzake watamlazimisha mzee Hamisi amwite Willy Gamba kwa simu toka hapo hotelini kwake. Mzee Hamisi atalazimishwa kumwambia Willy aje nyumbani kwake ili ampe habari muhimu sana kutoka kwa bosi wake. Bila shaka Willy atakuja na mtego wetu utamnasa. Atauawa tu", George alisema huku akitabasamu alipoona nyusa za wenzake zimejaa furaha baada ya kusikia mpango wake.

"Kweli naamini unastahili kuwa kiongozi wetu", Dave alisema. "Kwenye mtego kama huu hata mimi ningenasa tu".

"Lakini vijana watatu hawatoshi, mtu huyu ni mbaya sana", F.K alisema kwa sauti ya woga.

"Oke, nitakwenda nao mimi mwenyewe", Dave alijigamba.

"Hapana", George aliingilia kati. "F.K atakwenda na hao vijana, bali tu tutamwongeza mmoja zaidi ili wawe wanne. Wewe mwenyewe Dave unajuwa kwamba vijana wetu wanao ujuzi mkubwa. Vile vile mfahamu kuwa wakati Willy akiitwa kwa mzee Hamisi hatachukua tahadhari kubwa, kwani hatahisi kitu chochote kibaya. Hivyo kazi yao itakuwa rahisi kama mtelemko. Mara tu baada ya mzee Hamisi kumwita Willy, naye lazima auawe. Baada kumuua Willy vijana wetu watarudi huku haraka kwa kazi nyingine ya baada ya usiku wa manane. Mimi, P.G na vijana wawili tutakwenda kukagua mazingira Maunt Meru Hoteli na vile vile jumba la Kimataifa ambamo mkutano unatarajiwa kufanyika. Tunataka kutega mabomu ya masaa kwenye sehemu hiyo. "Kwa hiyo F.K, baada ya kumwita Willy na kumuua Hamisi, kazi nyingine utawaachia vijana. Wewe utachukua gari la Hamisi kwani litahakikisha usalama zaidi, halafu utufuate Maunt Meru Hoteli ili utuonyeshe chumba cha mikutano ambamo tunatarajia kutega mabomu. Baada ya kumuua Willy. Vijana warudi huku haraka kwa gari lako. Wewe Dave utabaki hapa na vijana watatu mkisubiri kazi yenyewe ya usiku wa manane. Mipango zaidi nitawajulisha saa tano usiku wakati tukijitayarisha kwenda kwenye mapambano yenyewe. Naamini nyote mmenielewa?".

"Mpango ni barabara kabisa", Dave alisema huku akijinyoosha nyoosha.

"Hivi ni kwanini mnataka kutega mabomu? Si hawa watu tutawaangamiza usiku huu ili mkutano usifanyike kesho?", P.G aliuliza.
"Katika kazi hii hakuna kuacha mwana hata kidogo, kama hatukufanikiwa kuwauwa wote kwa leo, basi wale watakaodiriki kuendelea na mkutano kesho, nao watauawa vile vile", George alijibu huku akitabasamu.

"Baada ya kufunga kazi sisi tutaondoka vipi hapa?", Dave aliuliza.

"Usiwe na wasiwasi", George alijibu. "Mipango yote imeshakamilishwa na F.K; ukipata muda ingia chumba namba kumi".

"Haya, twende kazini vijana. Mungu atusaidie", P.G alisema.

"Amin!", wengine walijibu kwa pamoja huku wakiinuka na kujitayarisha kuondoka.





HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

II

Ilikuwa yapata muda wa saa tatu na nusu usiku, Willy na Nyaso walibisha hodi kwenye chumba cha Willy baada ya kujua kwamba wenzake walikuwa wanamsubiri ndani. Willy na Nyaso walikuwa wamefika pale chumbani kwa kupitia njia tofauti kama walikuwa hawafahamiani. Willy alikuwa amepanda kwa kutumia ngazi, wakati Nyaso alitumia lifti.

"Nani", Bon aliita kwa sauti.

"Willy".

Bon alifungua mlango huku akiwa na bastola mkononi. Alipomuona msichana Bon alirudisha mlango haraka haraka.

"Na wewe woga umezidi, karibu ndani Nyaso", Willy alimkaribisha huku akirudisha mlango baada ya Nyaso kuingia ndani.

"Maama", Mike alisema kwa mshangao.

"Nini?", Willy aliuliza kwa kebehi.

"Wewe huwa unawatoa wapi hawa?".

"Malaika huyu ama mwanadamu?", Mike aliendelea kushangaa.

"Wewe unafikiri vipi?", Willy alimuuliza.

"Malaika", Mike alijibu huku wote chumbani wakimwemwesa.

"Subiri sasa niwafahamishe kwa huyu 'malaika'. Mtoto huyu anaitwa Nyaso. Ni Nyaso tu. Msiulize zaidi. Nyaso hawa ndiyo rafiki zangu niliokuwa nikikueleza. Yule maneno mengi ni 'Kikuyu' toka Kenya. Huyu ni Bon toka Afrika Kusini na yule pale anayejifanya mkimya ni Rocky kutoka Zimbabwe", Willy alisema.

"Nashukuru kuwafahamu", Nyaso alijibu.

"Sisi ndiyo tunapaswa kushukuru kwani kumfahamu mtoto mzuri kama wewe ni fahari ati", Mike alisema.

"Willy kweli watanzania mnatoa watoto, mimi sina hata maneno. Hivi vijana wa hapa mtaweza kujenga?, Mtoto kama huyu akisema umpe mshahara wako wote wa mwezi unaweza kukataa? La hasha rocky alisema.

"Ahsante kwa sifa ulizonipa", Nyaso aliitika.

"Sikia sauti yake nyororo", Bon aliongeza.

"Wacha sauti na sura, Nyaso anayo mengi zaidi", Willy aliasa.

"Haya Willy, umemleta huyu mrembo ili tukusifu ama unayo mengine zaidi?". Mike aliuliza.

"Wacha maneno mengi, nyinyi wakenya mkijua kiswahili kadiri, sisi watanzania huwa watufui dafu", Willy alisema.

"Hayo ndio maendeleo", Mike aliongeza.

"Hebu jamani, nisikilize kwa makini. Sikuja na msichana huyu ili kuwakoga. Kusema kweli mambo yamepamba moto tayari na ni lazima na sisi tuwemo kazini", Willy alisema halafu aliwaeleza juu ya mazungumzo yake na Nyaso, juu ya F.K na mwisho jinsi walivyokwenda kwa Chris na kukuta ameuawa.

"Tunao uhakika kuwa F.K ndiye aliyefanya mauaji hayo. Mimi ninahisi amekuwa na wasiwasi baada ya kusikia kwamba mimi nimemhoji sana Chris. Kwa hiyo aliamua kutumia mbinu zile zile za siku zote: Yaani maiti hawana maneno. Hii ina maana kwamba fumbo limefumbuliwa tayari. Majasusi tunaowatafuta wamejificha kwa F,K. Kutokana na maelezo ya Nyaso kuhusu jumba la F.K. lilivyo ni dhahili kwamba majasusi hao wako mle ndani, hivyo kazi imebaki kwetu", Willy alisema.

"Sasa mipango iko vipi bosi?", Bon alimwuliza Willy.

"Kwanza kabisa mimi na Nyaso tutakwenda kufanya uchunguzi kwenye jumba la F.K. kama nilivyowaeleza, jumba hilo linazo njia za chini kwa chini. Na kama hivyo ndivyo, basi mle kuna sehemu nyingi ambazi ni za siri. Kwa sababu hiyo mimi naona ni bora niende na Nyaso ambaye atanionyesha mahali jumba hilo lilipo. Baada ya kufanya utafiti, nitarudi hapa ili tujadili jinsi gani ya kuwakabiri hao majasusi usiku huu, ama mnasemaje?", Willy aliuliza.

"Hisia zetu ni sahihi. Sasa kwa nini sisi sote tusivamie jumba hilo mara moja na kufunga kazi", Mike alipendekeza.

"Hapana Mike, huenda kazi yenyewe isiwe rahisi kama unavyofikiri. Haitakuwa vizuri sisi sote kujitumbukiza bila kufanya uchunguzi. Uwezekano wa kuangamia sisi sote upo, na hilo litakuwa pigo kubwa kwa Afrika huru na kwa wapigania uhuru wa Afrika Kusini. Hivyo utakuwa ushindi kwa makaburu. Amini usiamini, mapambano yanayoendelea huko Afrika Kusini, kwa kiwango kikubwa, yanategemea ushindi wetu", Willy alijibu.

"Mimi nakubaliana na wewe kabisa", Bon alisema halafu akaendelea, "Kusema kweli, vita kamili vimeanza ndani ya Afrika Kusini. Ushindi wetu hapa utawatia hamasa vijana wa kizalendo ambao wanapambana na askari wa makaburu. Nia ya makaburi ni kutuvuruga sisi huku na kufanya wana-ukombozi walio ndani na nje ya Afrika Kusini kuchanganyikiwa. Vita vya Ukombozi tayari vimevuka hatua ya kutumia mawe na marungu. Awamu hii ni ya kutumia silaha za moto. Hivyo, na sisi tuwe tayari kujitoa muhanga ili matunda ya uhuru yapatikane kwa watu wetu", Bon alisema.

Willy alikuwa karibu kuzungumza jambo fulani, mara simu ililia. Wote waliangaliana halafu Willy aliamua kusikiliza simu.

"Hallo", Willy aliitikia.

"Mimi ni mzee Hamisi, naomba kuzungumza na Willy", sauti ya mzee Hamisi ilisikika.

"Mwenyewe nazungumza, habari za saa hizi mzee", Willy alijibu.

"Habari ni nzuri, Willy nakuhitaji uje hapa nyumbani kwangu haraka kwani nina habari muhimu sana", Hamisi alisema, Willy alisita kidogo halafu akamjibu.

"Sawa, nakuja", halafu alikata simu bila kusema maneno zaidi.

"Huyo ni nani?", Mike aliuliza.

"Ni mzee Hamisi, anasema ni lazima niende nyumbani kwake kwani ana habari muhimu", Willy alibu.

"Hivi sasa itabidi mimi, Rocky na Nyaso tuandamane mpaka kwenye jumba la F.K. Sisi tutafanya utafiti halafu turudi hapa", Bon alishauri.

"Hiyo ni sawa, wewe Mike huna budi kubaki hapa. Kama kuna habari zozote, tutawasiliana. Bon na Rocky ni lazima kuchukua tahadhari kubwa kwani katika mazingira ya jumba kama lile, kunaweza kukatokea jambo lolote", Willy aliasa.

"Huyu Hamisi anakaa wapi?", Nyaso aliuliza.

"Anakaa kwenye nyumba za maafia huko Kijenge, karibu na barabara iendayo Themi Hill. Kwa hiyo tutaondoka wote halafu nyinyi mtaniacha barabarani. Baada ya kuzungumza na mzee Hamisi, mimi nitatafuta njia yangu mwenyewe ya kurudi ili tukutane hapa tena. Sasa Nyaso, wewe telemka chini na kutusubiri kwenye gari", Willy alielekeza.

Wote watatu walichukua silaha ambazo walifikiri wangezihitaji. Willy pia, ingawa alikuwa anakwenda kwa mzee Hamisi, alichukua silaha akiwa tayari kwa lolote. Wanaume walishajuwa kwamba walikuwa wanawinda na huku wakiwindwa. Mike ambaye alikuwa na jukumu la kubaki pale hotelini, naye alikaa tayari na silaha zake. Walipokuwa tayari, walielekea kwenye gari huku kila mmoja akitumia njia tofauti na wenzake.

HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

III

"Ahsante". F.K. alimwambia mzee Hamisi baada ya kuzungumza na Willy.

"Hebu ondoa huo mtutu wa bunduki kwenye kichwa changu. Unajua mimi ni mzee sana na kuniweka katika hali hii kunaweza kunisababisha nipate ugonjwa wa moyo. Kazi uliyotaka nimekufanyia, zaidi unataka nini", mzee Hamisi aliuliza.

"Ha ha", F.K. aliangua kicheko kwa jeuri halafu akaendelea, "Mzee Hamisi sina budi nikushukuru kwa yote uliyonifanyia, maana bila kupata habari ulizonipa mipango yangu isingefikia hatua hii. Wewe ni mtu mwenye ujuzi na uzoefu katika shughuli za usalama. Sina shaka umeshahisi kitu gani kinatendeka baada ya kuona unavamiwa na kundi la Wazungu. Hawa ni askari kutoka Afrika Kusini. Ufahamu fika kwamba wewe ni msaliti wa nchi yako. Hii imetokana na nyinyi watu wenye vyeo Serikalini kupenda pesa. Pesa nilizokupa zilikufanya uisaliti nchi yako. Ha ha! Uchu wa pesa utaimaliza Afrika. Je, unajua adhabu ya usaliti ni nini", F.K. aliuliza kwa kebehi.

"Usiniue F.K. kwani hata ukiniua, Willy atakumaliza...", Hamisi alisema huku akipapatika.

"Stumke, fanya kazi yako", F.K. aliamrisha, mzee Hamisi aliinuka na kabla hajachukua bastola yake kutoka kwenye koti, alipigwa risisa ya paja na kichwani na kufa papo hapo.

"Sasa msubiri Willy. Nina imani kazi yenu itakuwa rahisi", F.K. alisema huku akimpa Stumke swichi ya gari lake. Stumke alikuwa kiongozi wa yale majasusi yaliyomvamia mzee Hamisi, na ambayo sasa yalikuwa yakimsubiri Willy. Baadaye F.K. alichukua funguo za marehemu Hamisi kutoka mezani kwake na kuaga.

"Stumke, tuonane nyumbani. Lakini nawashauri mkae macho sana. Ingawaje Willy atakuja bila tahadhari, ni mtu hodari kupindukia. Msimpe mwanya bali mtumie mbinu zote mnazozifahamu", F.K. alionya.

"Usiwe na wasiwas, F.K. mimi nilikwisha ongoza kundi hili hili na kuteketeza kikosi kizima huko Namibia. Itakuwaje tushindwe mtu mmoja?, Huyo mfute kutoka kwenye orodha ya adui walio hai. Labda asitokee!", Stumke alijigamba.


HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

IV

Willy na wenzake walikuwa wanaingia kwenye barabara kuu iendayo Themi Hill. walipishana na F.K. ambaye alikuwa akiendesha gari la Hamisi na kuelekea mjini. Si F.K. wala Nyaso ambaye alimtambua mwenzake kwani wote walikuwa wanaendesha magari ambayo hayakuwa yao. Lakini Willy aligeuka na kuliangalia gari hilo ambalo lilikuwa linakwenda kasi na kupotea gizani.

Hilo ni kama gari la mzee Hamisi", Willy alisema baada ya kugutuka.

"Itakuwaje akuite halafu atoke", Bon aliuliza kwa mshangao.

"Hapo sasa", Willy aliitikia.

"Kama una hakika ni lenyewe, basi hilo siyo jambo la kawaida", Rocky alisema.

"Huenda ameona nimechelewa hivyo akaamua anifuate", Willy alijibu.

"Lakini hatujachelewa hata kidogo", Rocky alijibu.

Wakati huo walikuwa wamekaribia sehemu ya Kijenge ambako Hamisi alikuwa anakaa.

"Nyaso! Simama hapo pembeni", Willy alisema, Nyaso alijisikia raha kwani alijua yeye alikuwa msichana peke yake aliyepata fursa ya kuwaendesha wapelelezi mashuhuri wa Afrika, hasa wakiwa katika harakati za mapambano. Alisimamisha gari pembeni mwa barabara na Willy akatelemka.

"Haya nendeni lakini jihadharini sana. Huko mwendako panaweza kuwa moto. Nawatakia kila la kheri", Willy alisema.

"Ahsante", Bon na Rocky walijibu kwa pamoja.

Nyaso aliendesha kuelekea Themi Hill baada ya kumwacha Willy. Willy naye taratibu aliambaa kwa kufuata ua wa sehemu hii kuelekea nyumbani kwa Hamisi. Nyumbani kwa marehemu mzee Hamisi Stumke alikuwa amepanga watu wake tayari.

"Mtu huyu akiingia sharti auawe pale pale. Hakuna kusubiri. Yeyote atakayekuwa kwenye sehemu nzuri ya kumuua lazima afanye hivyo mara moja. Kama tulivyokwisha ambiwa, mtu huyu ni hatari sana. Kila mtu awe macho", Stumke aliwaonya wenzake.

Stumke alitokomea gizani. Aliambaa kwenye ua huku akielekeza macho na mawazo yake kwenye lango la nyumba. Majasusi wengine wawili walikuwa wamejibanza kwenye ua. Mmoja wao mwingine alikaa langoni kwani yeye ndiye ambaye angemfungulia Willy. Kila wakati waliposikia muungurumo wa gari, walijiweka tayari lakini hakuna gari lililojitokeza pale nyumbani. Gari la Nyaso liliposimama Stumke kutokana na uzoefu wa kazi yake, alihisi huenda mtu wao angeweza kuteremshwa njiani na kuingia pale kwa kutembea. Hivyo aliwashauri watu wake wawe macho kama mtu huyo angeingia kwa miguu.

Kengere ya ilani ilizidi kulia kichwani mwa Willy baada ya kila hatua aliyopiga kuelekea kwenye nyumba ya Hamisi. Ilikuwa kawaida yake kwamba kila hali hiyo ilipotokea, Willy alichukua tahadhari ya hali ya juu. Wakati huo huo Willy alimua kupita mlango wa nyuma badala ya mbele ya nyumba ile. Alizunguka ua wa nyumba huku akinyatia kama nyani. Aliruka ua huo wa michongoma na kutua ndani kwa kishindo kidogo.

Jasusi aliyekuwa upande wa kulia aligutuka kidogo halafu akaamua kuja kuangalia kuna nini. Alikuja kwa mwendo wa kunyatia kiasi kwamba hakutoa sauti yoyote. Lakini kwa kuwa masikio ya Willy yalikuwa na uzoefu kama wa mnyama awindwaye porini, aliweza kusikia mtu anajongea. Willy aliinuka mara moja na kujibanza kwenye pembe ya kulia ya nyumba. Aliangalia kwa chati na kuona yule kaburu anasogea huku bastola ikiwa mkononi. Macho ya Willy kama ya wale majasusi yalishazoea giza. Hivyo aliweza kuona vizuri.

Willy alikuwa na bastola mkononi, mara akaamua kuirejesha mahali pake, akajitayarisha kumkabiri jasusi yule kwa mikono. Pale pale akijuwa kuwa kuitwa kwake kulikiwa ni mtego na kwa hiyo ilibidi awe tayari kwa mapambano. Yule jasusi alisogea karibu kabisa na pale Willy alipokuwa amejibanza. Willy alimwacha afike kabisa kwenye usawa alipokuwa amesimama. Ndipo alipomrukia na kumkaba koo kiasi kwamba yule jasusi hakuwa na muda wa kuweza hata kukohoa. Willy alivunja shingo ya yule jasusi ambaye alikata roho bila kutoa sauti. Taratibu Willy aliilaza chini maiti yake.

Jasusi mwingine alipoona mwenzake anakawia kurudi, alitoa ishara kwa yule aliyekuwa kwenye lango. Alikuwa anamjulisha kuwa anaelekea nyuma ya nyumba. Wakati huo damu ya Willy ilikuwa tayari imechemka kwa hali ya vita. Mara alimwona jasusi mwingine anakuja mbio. Willy alimsubiri huku akimwemwesa kwani alikuwa anakwenda hovyo bila tahadhari yoyote. Lakini alipokaribia mahari Willy alipokuwa, yule jasusi alisimama kana kwamba alikuwa amegutushwa na jambo fulani. Willy alijua kuwa kama angesubiri, bila shaka angeonekana. Kama risasi, Willy alifyatuka na kumrukia yule jasusi pale alipokuwa amesimama. Alimkata mkono wa karate na kumpasua kichwa. Wote walianguka chini.

Walianguka kwa kishindo ambacho kilimshitua Stumke na yule jasusi aliyekuwa kwenye lango. Wakiwa kama watu waliotiwa ufunguo walikimbia kuelekea mahali alipokuwa, mmoja akipitia kushoto na mwingine akipita kulia. Hapo hapo Willy aligundua kuwa jasusi yule alikuwa kafa, hivyo aliinuka haraka. Aliruka kama nyani na kukamata sehemu ya juu ya ukuta. Alijipinda na kupanda juu ya paa akajibanza. Mara tu baada ya kupanda juu ya paa ya nyumba, Stumke na mwenzake walifika sehemu ambayo Willy alikuwa amesimama muda kitambo. Walikuta wenzao wawili wamekufa. Waliingiwa na woga sana.

"Grande, mtafute haraka tumuue, unasikia", Stumke alimwamrisha mtu wake wasiwasi mwingi.

"Willy, uko wapi? njoo tuonane uso kwa uso kama kweli wewe ni mwanaume", Grande alisema kwa sauti. Willy ambaye alikuwa amelala juu ya paa alijisikia raha alipoona majasusi yale yanapaparika kwa woga. Mara aliinuka na kwa spidi kubwa Willy alijirusha katikati yao. Lakini wakati akiwa bado yuko hewani aliipiga teke bastola ambayo Grande alikuwa nayo mkononi. Silaha hiyo ilianguka upande wa pili wa ua. Stumke ambaye alikuwa ameangalia upande mwingine aligeuka na kufyatua risasi. Wakati ule ule Willy alijiviringisha chini na risasi zile zikampata Grande.

"Stumke, umeniua! Aibu", Grande alilalamika halafu akakata roho pale pale. Willy aliamka na kumwahi Stumke. Aliipiga teke bastola yake ambayo iliruka na kutua juu ya paa ya nyumba. Mara mapambano makali yakaanza.

Stumke alimpiga Willy teke la tumbo ambalo lilimpata barabara na kumwangusha chini. Kabla hajaweza kusimama, Stumke alimwongeza teke jingine la ubavuni. Halafu aliamua kumrukia ili ammalize kabisa. Kumbe Stumke alikuwa amefanya makosa. Wakati huo huo Willy alijiviringisha kidogo na Stumke akamkosa. Willy alijipinda na kusimama. Alikuwa amejisikia damu yake imeanza kwenda mbio kutokana na kupigo. Hasira zilikuwa zimempanda. Angeweza kummaliza Stume pale pale, lakini Willy alimpa nafasi naye ainuke. Jambo hilo lilimshangaza sana Stumke.

"Simama kaburu mshenzi, wee! Ulichokuja kutafuta leo utakipata. Kama mlifikiri mkutano hautafanyika mlijidanganya. Wakati ukiwa jehanamu mkutano utakuwa unaendelea", Willy alisema kwa hasira.

Stumke alikuwa bingwa wa karate katika jeshi la KULFUT. Hivyo alimsikitikia Willy kwani alifikiri angeweza kumamliza mara moja. Aliamini kwamba hakukuwepo mtu yeyote kutoka katika nchi za Afrika ambaye angediriki kupigana naye. Stumke alikuwa mwoga kila mapambano yalipokuwa sura ya kutumia silaha kama vile bastola. Lakini kama mtu alipambana naye kwa kutumi mbinu za karate, basi Stumke alimhesabu mtu huyo kuwa ni marehemu.

"Utajijutia leo", Stumke alisema. Mara alimrukia Willy na kutoa mapigo matatu ya karate ambayo hata Willy hakutarajia kamwe. Stumke alishangaa kwani Willy aliyazuia yote. Ni mara chache ambazo Stumke alikuwa ametumia mapigo ya namna hiyo wakati wa mapambano. Na kila alipoyatumia ni watu wachache ambao waliweza kuyazuia. Jambo ambalo alikuwa hajui Willy alikuwa Ninja.

Stumke alibadili mbinu na kutumia zile za hali ya juu kabisa. alitoa pigo la kwanza ambalo Willy alilikwepa. Alitoa pigo na pili na Willy alilizuia. Alipotoa pigo la tatu Willy alimkamata mkono ghafla. Aliukata kwa kiganja chake nao ukavunjika. Hata hivyo Stumke alijirusha na kumpiga Willy teka farasi ambalo lilimwangusha chini. Wakati huo huo Stumke aliguna kutokana na maumivu ya mkono wake uliovunjika. Alimtupita teke la mauti Willy lakini alikuta patupu! Willy alikuwa amejipinda kama swala na kuushika mguu wa Stumke akiwa bado hewani. Aliupinda na kufyatua mfupa wa goti.

Willy alimsukumiza Stumke kwenye ukuta ambapo aligonga kichwa chake na kuona nyota. Fahamu zilimpotea. Willy alimfuata kasi na kumkata karate iliyoacha mkono wake wa pili bila kuwa na kazi. Alimtingisha huku akisubiri fahamu zimrudie. Stumke alipopata fahamu, alijuwa kuwa ameshindwa. Hivyo kama lile jasusi Paul lilivyokuwa limefanya, Stumke alitoa ulimi wake nje na kuukata haraka kwa meno. Kwa haraka, Willy alimtia ngumi moja Stumke halafu akamwacha akate roho kwa kutokwa na damu.

"Ama kweli majasusi hawa ni watu wa ajabu. Kujiua kwa kujikata ulimi ni jambo geni kabisa", Willy alijisemea huku akielekea ndani ya nyumba. Mle ndani alikuta maiti ya mzee Hamisi. Hapo hapo akagudua kuwa mzee hamisi alikuwa amelazimishwa kumwita ili aje auawa kama yeye. Vile vile Willy aligundua kuwa kama majasusi hawa waliweza kuutumia uhusiano wake na Hamisi, basi tayari walikuwa na habari nyingi juu yao. Willy alijipongeza, bahati yake nzuri kwani mtego waliokuwa wamemwekea ilikuwa bahati kuukwepa.

Mara wazo likamjia. Alifikiri jinsi F.K. alivyokuwa anaaminiwa hapo Arusha kuwa mtu mwaminifu kwa Serikali na Chama. Kama kweli anahusika, bila shaka ndiye anayetayarisha mpango mzima. Mzee Hamisi asingeweza kumhisi kitu F.K. Ndio sababu waliweza kumwingia kwa urahisi. Mzee Hamisi alikuwa anajulikana kama mtu matata. Isingekuwa rahisi kwake kuuawa 'kike' hivyo. Willy aliamua kurudi alipokuwa amelala Stumke. Alimkuta bado hajakata roho kabisa. Alimpapasa ili kuona kama angepata kielelezo chochote. Hakukuta kitu bali funguo za gari. Alizichukua na kuelekea sehemu ya mbele ya nyumba.

Alikuta gari aina ya Benz. Alichukua kalamu yake ambayo ilikuwa na tochi vile vile, na kumulika kwenye karatasi ya bima iliyokuwa imebandikwa katika kioo cha mbele cha gari. Bima hiyo ilikuwa imechukuliwa kwa jina la Feroz Kassam. Kwa kutumia funguo zile zile, Willy alifungua mlango wa gari na kuingia ndani. Aliwasha gari lile na kuondoka. Wakati akiendesha Willy alijikuta akisema.

"We gari, nipeleke nyumbani kwenu, na leo hii bwana yako atanitambua!".
HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

V

"Jumba lenyewe ni lile pale", Nyaso aliwaonyesha mara walipofika kwa F.K.

"Seng'enge yote ile mnayoiona imezunguka eneo la jumba hilo", waliangalia eneo hilo kwa makini kwani kila sehemu ilikuwa inawaka taa.

"Hili ni jumba hasa", Rocky alisema.

"Wacha kulishangaa kwa nje. Ndani yake ni zaidi. Siku moja mimi nililala humo. Mara nilisikia mlio wa vitu fulani kutoka chini. Nilipomwuliza nini ilikuwa, F.K alijibu huku akiwa mwenye nusu usingizi.

"Hao ni watu wanafanyakazi huko chini, wewe lala usiwe na wasiwasi. Mambo haya hayakufai! Siku hiyo ndiyo nilijuwa jumba hilo lilikuwa na vyumba chini ya ardhi. Siku nyingine F.K alifurahi sana halafu akanieleza kwamba, kama lingetokea jambo la dharura, jumba lile lina njia mbili za kutokea nje kupitia chini kwa chini. Aliongeza kusema kwamba njia moja ilitokea Magharibi na nyingine ilitokea Kusini mashariki mwa jumba hilo. Alinieleza pia kwamba kwa nje mtu yeyote angefikiri labda sehemu ya nje ni mahali palipofunikwa tu. Aidha mfuniko wa njia ulionekana kama ule wa machafu", Nyaso alieleza huku akiendesha pole pole.

"Mimi naona usimame hapa. Sasa hivi ni saa nne kamili. Sijui utaegesha wapi halafu utasubiri, tusingependa waone gari lako", Bon alimwambia Nyaso.

"Itawachukua muda gani?", Nyaso aliuliza.

"Tupe nusu saa. Ukikuta hatujarudi, ujuwe mambo yameharibika. Hivyo utakwenda Hotelini na kumweleza Willy", Bon alijibu.

"Una maana gani?", Nyaso aliuliza.

"Usiniulize maswali, fanya kama nilivyokwambia kwani hiyo itakuwa rahisi kwako", Bon alijibu kwa sauti kali kidogo.

"Haya bwana, mimi nakwenda kwa rafiki yangu hapo juu kwenye nyumba za wasabato. Saa nne na nusu juu ya alama nitakuwa hapa", Nyaso alijibu.

"Sawa, tutakuwa tumejibanza kwenye mti ule pale", Bon alieleza na halafu wakatelemka. Nyaso aliondoka huku roho ikimdunda.

Kufuatana na maelezo ya Nyaso, jumba hili linazo njia mbili za kuingilia kwa chini. Moja iko magharibi na nyingine iko kusini mashariki, wewe utaingilia magharibi na mimi nitapita kusini mashariki. Kama hatukuonana ndani basi tukutane mahali petu kabla ya saa nne na nusu", Bon alimweleza Rocky.

Wote walitazamana kwa hisia zao zilizowajulisha kwamba walikuwa wanaingia mahali pa hatari. Huku wakiwa wamejidhatiti, walipeana mikono na kuingia kazini. Rocky alikuwa wa kwanza kuona mfuniko ulioziba mlango wa njia. Aliuinua taratibu na kuona ngazi za kutelemkia chini. Aliuweka kando mfuniko ule ili wakati wa kutoka nje usije ukampa tabu. Baada ya kufanya hivyo, alichukua tochi yake yenye saizi ya kalamu akamulika na kutelemka ngazi jambo ambalo Rocky hakufahamu ni kwamba wakati mfuniko ule ulipofunguliwa ulikuwa unapeleka miale ya ilani, ambayo ambayo ilionekana kwenye televisheni iliyokuwa chumbani, kwa ajili ya usalama.

Dave alikuwa ndani ya chumba cha kumi akiangalia helikopta ya namna yake ambayo ilikuwa chumbani tayari kwa ajili ya kuwachukua majasusi baada ya kufanya maovu yao. Mara alisikia jasusi mmoja kwa jina la Terre akimwita. Terre na wenzake wawili walikuwa wamejinyoosha kwa mapumziko. Aligutushwa na makelele kutoka kwenye televisheni pamoja na picha ya mtu aliyeonekana akiingia kwenye njia ya siri upande wa magharibi. Dave alipofika na kuona picha hiyo, aligundua mara moja kwamba yule alikuwa Rocky kutoka Zimbabwe. Dave aliweza kumtambua Rocky kwa sababu alikuwa ameonyeshwa picha za wapelelezi mashuhuri wa Afrika, majina yao na nchi walizotoka.

"Haya sasa, kazi imebaki kwenu. Huyu amejileta mwenyewe badala ya sisi kumtafuta. Terre na Gary nendeni kwenye mlango ule. Akifungua tu nataka mmalize mara moja. Sisi tunamwona lakini yeye hatuoni. Hivyo kazi yenu itakuwa rahisi. Hakuna haja yangu mimi kuhangaika. Nitakuwa nawaangalia kwenye televisheni. Sitaki mtumie bastola bali mikono yenu. Hapo ndipo watu hawa watatambua sisi ni nani", Dave aliamrisha huku furaha imemjaa. Dave na Howe walikaa tayari kushuhudia mapambano ambayo yangefuatia.

"Huyu ni chakula chetu", Terre alijibu huku akiondoka pamoja na Garry. Walikuwa wamepandwa na mori kwani walitaka kuonyesha uhodari wao, pia kuwa mtu wa kwanza kumuua mpelelezi mashuhuri wa Afrika. Bila kujua kuwa alikuwa anaonekana kwenye televisheni, Rocky aliendelea taratibu kwa tahadhari kubwa sana. Alipomaliza ngazi za kwanza, aliufikia mlango. Upande wa pili wa mlango, Terre na Garry alikuwa wakisubiri tayari.

Ili wamsaidie kuingia kwenye mtego, walikuwa wamefungua mlango na kuuacha umerudishiwa tu. Rocky alipojaribu kufungua mlango alikuta umerudishiwa. Kutokana na uzoefu wake wa kazi wa muda mrefu. Rocky alifungua mlango ghafla na kwa nguvu. Terre na Garry walitarajia Rocky angefungua taratibu na kuendelea kutembea. Badala yake alijirusha chini kwenye njia. Alifanya kitu ambacho hakikutarajia mpaka wakashindwa kufanya yale waliyokuwa wamepanga. Alijiviringisha chini na kujipinda huku akichukua bastola yake. Alifyatua risasi mfululizo ambazo zilimpata Terre na Garry. Wote wawili walikufa pale pale.

Dave na Howe ambao walikuwa wanafuatilia mapambano kwenye televisheni, walishangazwa na kitendo hicho cha Rocky chenye kuonyesha ujuzi wa hali ya juu.

Howe, twende tukamkabiri kwani naona mtu huyu ni hatari sana. Chukua bastola na mimi nipatie moja", Dave alimwagiza Howe.

"Wewi ni Ninja, huyu atakuwa nini kwako?", Howe alimpambisha Howe moto.

"Unasema kweli, kama hujaniona basi leo utaniona", Dave alijigamba huku wanaelekea kwenye mlango katika njia ambayo Rocky alikuwa akitokea.

"Dave, nafikiri tusisogee kwenye mlango kwani mtu huyu anaweza kutufanya kama Terre na Garry. Heri tumsubiri hapa. Kwa kuwa chumba hiki ni kipana kiasi cha kutosha, hata kama akijirusha bila shaka ataimba tu", Howe alisema huku akijitayarisha na kumwangalia Rocky kwenye televisheni kwa mara ya mwisho. Rocky aliendelea kunyata na kuusogelea mlango wa chumba kile cha mapumziko.

Mlango wa sita wa maarifa ulimjulisha Rocky kwamba chumba alichokuwa akisogelea kilikuwa cha hatari zaidi. Hivyo alichukua tahadhari zaidi. Alikuwa tayari amepandwa na mori wa kupigana. Kwa hiyo alijiona kuwa alikuwa na uwezo wa kupabana katika hali yoyote ile. Dave ambaye alikuwa amesimama pembeni karibu na mlango ule, alitarajia Rocky angejirusha chini baada ya kufungua. Badala yake Rocky aliruka hewani na kuufungua mlango kwa kuupiga teke akitumia miguu yake miwili. Wakati bado akiwa hewani, Rocky alijipinda na kutua njiani nyuma yake. Howe aliyekuwa anasubiri Rocky kwa hamu alifyatua risasi tatu ambazo zote zilikosa Rocky. Kitendo cha sasa cha Rocky kilikuwa hakikutarajiwa pia.

Dave alimtolea ishara Howe ili amfuate Rocky. Howe alijiviringisha chini kwenye njia huku akifyatua risasi ambayo ilimpata Rocky kwenye mkono wa kushoto karibu na bega. Wakati huo huo Rocky aliachia risasi ambayo ilimpata Howe kwenye paji la uso. Alikata roho pale pale. Akiwa anasikia maumivu makali. Rocky alikimbia mpaka nyuma ya mlango kulikokuwa na maiti ya Terre na Garry. Alirudisha mlango huo. Alichana shati lake mwenyewe na kujifunga mkono ili kuzuia damu isitoke kwa wingi. Dave alijuwa Rocky alikuwa ameumia hivyo alimfuata na kufungua mlango ule. Rocky alikuwa ameweka bastola yake chini. Dave aliruka na kumkumba Rocky na wote wakajiviringika chini.

"Rocky! Unakufa sasa", Dave alisema kwa sauti ya juu. Rocky alikuwa anasikia maumivu makali lakini hali halisi ilimfanya asahau maumivu hayo. Aliinuka haraka akiwa tayari kukabiliana na jasusi hilo. Hapo mapambano makali yalianza. Dave alimshambulia Rocky kwa mapigo safi yapatayo saba lakini yote yalizuiwa. Hapo ndipo Dave alipogundua kuwa alikuwa anapambana na mtu mwenye ujuzi zaidi ya vile alivyotarajia. Hivyo aliamua kutumia mafunzo ya U-Ninja. Vile vile Rocky aligundua kuwa Dave alikuwa na ujuzi wa hali ya juu. Hivyo ilimbidi atumie mbinu kali kuweza kumshinda adui.

Dave alitupa ngumi lakini Rocky aliikwepa nayo ikagonga ukuta na kulitoa tofari moja lililoangukia upande wa pili. Wakati huo huo Rocky alichukua nafasi hiyo kumtia mapigo makali Dave ambayo yalimfanya aanguke chini. Hapo aliamua kuchukua bastola yake kwani aliamini kuwa mtu huyu hakuwa saizi yake. Hivyo alijirusha lakini kabla hajawahi kuichukua bastola yake iliyokuwa chini, Dave naye aliruka na kumwahi Rocky hewani alipompiga teke la kichwa. Rocky alipoteza fahamu na kuanguka chini kwa kishindo.

Bon alikuwa amenyatia toka chumba hadi chumba wakati alipofika kwenye chumba cha televisheni alimwona Dave anampiga Rocky teke la kichwa. Bon aligundua kwamba Rocky alipigwa teke la ki-Ninja ambalo asingeweza kulistahamili.

Bon alikimbia haraka kuelekea kwenye njia ambayo aliamini ndiko walikuwa wakipigania huku hasira na chuki zimemjaa. Rocky alikuwa anapigana kishujaa. Bon alipofungua mlango na kuingia kwenye chumba walichokuwa wanapigania, kumbe alikuwa amechelewa. Dave alikuwa amemrukia Rocky na kumpiga teke la moyoni ambalo lilimuua pale pale Rocky.

"Kufa mbwa mweusi, we!" Dave alitukana. Mara aliona mlango unafunguliwa ghafla na Bon akiingia ndani.

"Mbwa we, umemuua Rocky, nawe utaambatana naye mpaka peponi", Bon alisema kwa uchungu huku machozi yakimtoka. Bon alikuwa na bastola mkononi. Angeweza kumpiga risasi Dave. Lakini badala yake aliitupa kando. Dave alishangazwa na kitendo cha Bon. Vile vile alimwonea huruma kwani aliamini hakuna mtu mweusi ambaye angepambana naye kwani yeye alikuwa ni Ninja.

"Pole sana mbwa mweusi! Na wewe umejileta kwenye kaburi lenu", Dave alijibu kwa dharau. Bila kuchelewa Bon alimrukia Dave na kumpiga vipigo, moja baada ya kingine mpaka akaanguka chini. Lakini alijiviringisha na kuinuka haraka tayari kumkabiri Bon. Bon hakumpa nafasi kwani kabla hajasimama sawa sawa Dave alipewa vipigo kadhaa ambavyo vilimtatanisha. Pale pale alijuwa kwamba alikuwa anapambana na Ninja kama yeye mwenyewe, Bon aliruka na kumtia Dave teke la ubavuni na kumzidishia hasira.

Bon alimwahi Dave na kumpiga teke moja la shingoni na jingine la kichwani kwa wakati ule ule, ambayo yalimfanya Dave achanganyikiwe. Bon alipima hali ya Dave na kuona mbaya. Hivyo alichukua nafasi hiyo na kumtia pigo takatifu la kifuani ambalo lilikibomoa na kufanya damu ifumke na kutapakaa kila mahali. Kabla dave hajaanguka chini, Bon alimwonyesha kiganja na kama kusema. 'pigo linalofuata ni kisasi cha Rocky! Alimzibua tumbo na kuyatoa matumbo ya Dave nje'.

"Kufa Kaburu mshenzi, we!" Bon alisema kwa hasira. Dave alianguka chini akiwa maiti. Bon aliangalia saa yake. Ilikuwa saa tano kasoro dakika tano.

HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

VI

Ilikuwa yapata saa tano hivi wakati Willy alipokuwa anaegesha gari la F.K karibu na ofisi za mjini za mauzo ya General Tyre. Alikwenda haraka kwenye hoteli yake. Alibisha hodi kwenye chumba chake Mike akamfungulia.

"Vipi mwenzetu, mbona umenuna", Mike alimwuliza Willy.

"Hatari, akina Bon hawajarudi?", Willy aliuliza.

"Bado, mimi nina wasiwasi mkubwa", Mike alisema, "Je, umeonana na mzee Hamisi?".

"Mzee Hamisi ameuawa. Sasa hivi mtu wetu ni F.K. Hivi ninavyokueleza, nimeshaua makaburu wanne", Willy alisema na kisha alianza kumsimulia Mike yote yaliyotokea.

"Hivyo Mike, hapa mjini kuna kundi kubwa la makaburu wenye ujuzi mkubwa wa kupigana", Willy alimalizia.

"Kama ni hivyo, mimi napendekeza tulivamie jumba hilo kwani bila shaka majasusi wako humo. Nashauri kwamba kama ikibidi, tuombe msaada wa polisi ama jeshi", Mike alisema.

"Hapana Mike, kazi ya kupambana na majasusi haistahili kuhusisha polisi ama jeshi, kwani wao wanaweza kutumia mbinu za kijeshi tu na kusababisha maafa makubwa. Inatubidi sisi wenyewe tufunge vibwebwe na".... kabla hajamaliza sentensi, alisikia mtu anabisha hodi kwa kugonga mlango. Bastola za wanaume hawa zikawa tayari mikononi. Kwa tahadhari kubwa. Willy alifungua mlango huku bastola yake mkononi.

"Ni mimi....", Nyaso alisema kwa hofu alijikuta amekabiliana na mtutu wa bastola.

"Pole, usiwe na wasi wasi", Willy alisema huku akimvuta Nyaso ndani na kuurudisha mlango.

"Wenzako wako wapi?", Mike alimwuliza Nyaso huku akitweta.

"Waliniambia niwapitie saa nne na nusu. Nilipokwenda kwenye sehemu tuliyoagana, sikuwakuta. Hapo mwanzo walikuwa wamenieleza kwamba kama nisingewakuta basi ilibidi nije moja kwa moja huku ili niwaambie nyinyi", Nyaso alijibu huku machozi yakimlenga. Willy aliangalia saa yake na kuona kwamba ilikuwa saa tano na dakika kumi za usiku.

"Nyinyi subirini hapa. Mimi nitakwenda kuchunguza nini kimetokea, maana tukiondoka wote tunaweza kupishana nao, hivyo tutakuwa tumewachanganya. Nipeni mpaka saa sita na nusu, kama hamkuniona basi mjuwe mambo yameiva hivyo njooni", Willy aliwaambia.

"Hapana Willy, tuondoke wote. Nyaso atabaki hapa ili kama akina Bon wakirudi atawaambia watufuate", Mike alisisitiza.

"Hapana Mike, Willy halielewi sawa sawa lile jumba. Sharti nifuatane naye ili nimwelekeze", Nyaso alisema.

"Sawa Mike, utabaki hapa nami nitafuatana na Nyaso. Akisha nionyesha atarudi hapa. Kama ikifika saa sita na wewe hujaniona, basi nifuate", Willy alitamka.

"La hasha, mimi nitabaki huko na wewe....", Nyaso alisema na huku Willy akimkatisha.

"Nyamaza! Wewe unajuwa watu wale pamoja na bwana yako ni wauaji. Je, unataka kufa ama nini", Willy alisema kwa ukali.

"Hebu usiniambia kuwa bwana yangu ni muuaji! Kuna tofauti gani kati yake na wewe. Nyote wauaji tu. Kwani mimi nilifahamu kuwa yeye ni muuaji?", Nyaso alijibu kwa hasira. Willy alishikwa na hasira nusura ya kumnasa kibao Nyaso. Lakini Mike aliingilia kati.

"Basi basi, acheni hayo. Tunapoteza muda wetu. Wewe Nyaso usipende kugombana na wanaume. Utaumia. Mpeleke Willy kama alivyokwambia.

Nyaso alimtazama Willy kwa macho ya upendo. Alimkimbilia na kujilaza kifuani kwake huku akisema kwa sauti nyororo.

"Samahani Willy, sikuwa na maana hiyo. Nakupenda, tafadhali jihadhari", Willy alimvuta na wote wakatoka nje.

"Nawatakia kila la heri", Mike alisema.

"Ahsante!", Willy na Nyaso walijibu kwa pamoja wakati wakitoka nje.

HOFU
KABLA YA USIKU WA MANANE

VII

Mnamo muda wa saa tano na robo za usiku F.K, PG, George na vijana wao walikuwa wanarudi Themi Hill nyumbani kwa F.K. Hii ilikuwa baada ya kutega mabomu kwenye ukumbi wa mikutano wa AICC.

"Kesho Afrika itagwaya", P.G alisema.

"Kesho, watu hawa watatambua nguvu zetu. Tanzania imezidi kuzihamasisha nchi zilizo mstari wa mbele lakini baada ya kesho serikali itawafukuza wapigania uhuru wote kutoka nchini. Hiyo inatokana na kwamba baada ya pigo la kesho, tutatoa tangazo kuwa kama wataendelea kuwasitiri wapigania uhuru, tutaingia Ikulu na kutia kipigo", George alijigamba huku F.K akiegesha gari mbele ya nyumba yake. Walipotelemka walishangaa kuona kwamba gari la F.K lilikuwa bado halijawasili.

"Lo, hii ina maana kuwa Stumke na wenzake bado wanamsubiri Willy?", George aliuliza.

"Sidhani..." P.G alisema kwa sauti yenye kuonyesha wasiwasi kwamba kuna jambo ambalo halikwenda sawa. Waliingia ndani kwa kupitia mlango wa mbele. Walikwenda moja kwa moja mpaka kwenye chumba cha mapumziko walipokuwa wamemwacha Dave na wenzake. Walifungua mlango na kuingia ndani. Walipoangalia kwenye televisheni waliona maiti zimelala njiani.

"Mungu wangu", wote walisema kwa pamoja huku wakikimbilia yalipokuwa maiti.

"Mambo makubwa haya", F.K aligwaya.

"Sasa kazi imeanza", George alisema huku akiangalia maiti ya Dave na yale ya Rocky.

"Nakubali kwamba hawa watu siyo wa kawaida, njooni hapa niwaeleze", George aliwaita F.K na PG. waliokuwa wakiangalia maiti kwa mshangao. "Kazi hii ni ya Ninja", George alimaliza kusema na kwa mara ya kwanza alijisikia hofu.

"Dave, nitalipiza kisasi kwa ajili yako rafiki yangu", George alisema huku akichukuwa shuka na kuifunika maiti ya Dave. Mara wote walirudi chumbani na kukaa ili kupanga nini wafanye kwani mambo yalikuwa yamebadilika.

"Jamani, mmeona wenyewe jinsi mambo yalivyobadilika. Mimi nahisi Stumke na wenzake wameshauawa. Hata hivyo ni lazima tushinde vita hivi. Hatuwezi kushtushwa na haya yaliyotokea. Kulingana na habari tulizonazo ni kwamba Willy na Bon bado wangali hai. Kuanzia sasa ni wao wawili dhidi yetu watatu na vijana wetu wawili. Ninayo hakika watatufuata hapa kwani wameshajuwa siri yetu. Ni heri tuwasubiri hapa ili tuweze kuwamaliza watu hawa kwanza, tulijiamini kupita kiasi na kuwadharau wao. Lakini askari hawezi kufanya kosa lile lile mara mbili...", George alieleza.

"Maneno yako ni mazuri. Lakini mimi napendekeza tuwafuate kwa kuwa wanajuwa mahali tulipo. Kuna uwezekano wakatafuta msaada wa polisi na hata jeshi ili kutuvamia. Huo utakuwa mwisho wa kazi yetu ambayo bado haijamalizika na ushindi bado. Hatuwezi kuruhusu hali hiyo itokee kwani lazima kazi yetu ikamilike", P.G alishauri.

"Hapana P.G, tukifanya hivyo ujuwe tumekwisha. Kwanza tunajuwa watu hawa wako New Arusha Hoteli. Lakini baada ya mambo yaliyotokea ni vigumu kubashiri wao wako wapi. Hatimaye tutaanza kutafutana tusikutane hadi kesho asubuhi. Hiyo ina maana kazi yetu itakuwa haikumalizika usiku huu kama ilivyopangwa. Pili lazima tufahamu kwamba watu hawa ni wapelelezi wa muda mrefu. Wanaelewa sheria ya mchezo huu. Hivyo, amini usiamini, hawawezi kutumia polisi wala jeshi. Watatuwinda wao wenyewe. Muda siyo mrefu watakuja hapa maana mchezo umebadilika. Hivi sasa, sisi ndio wawindwa. Wao wanazo habari kamili kuhusu sisi kama sisi tulivyo na habari juu yao. Lililopo ni kujiweka tayari kupambana nao", George alisisitiza.

"Mimi nakubaliana na maneno yako George. Kama nilivyokueleza hapo mwanzoni, imetokea ghafla tu. Viongozi wa vyama vya ukombozi hawalali kwenye hoteli walizopangiwa. Tena hata polisi hawajui lolote kuhusu viongozi hao. Habari kuhusu viongozi hawa zimekuwa nyeti. Ni wapelelezi hawa tu ambao wanajuwa viongozi hawa wamepelekwa wapi. Nasi tutawaulia mbali washenzi hawa, wasije wakaharibu kazi yangu, ambayo imetokana na mpango wa muda mrefu wa kuleta hofu katika nchi hii. Lazima ushindi ni wetu", F.K aliwatia mori wenzake. Baada ya hapo George alianza kuwaeleza mpangilio wa kujiweka tayari wakati wakisubiri wapelelezi maarufu wa Afrika wakiongozwa na Willy Gamba.

HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

VIII

Wakati George alipokuwa anawaelekeza wenzake. Willy alikuwa anaagana na Nyaso karibu na nyumba hii.

"Willy, tafadhali jihadhari sana. Nakupenda sana Willy. Tafadhali...", Nyaso alisema kwa sauti ya unyonge.

"Tulia mtoto, usinililie mimi kwani nakwenda kazini. Lakini nitachukua tahadhari na tutaonana baadaye", Willy alisema huku akimvuta Nyaso na kumbandika busu moto moto. Kisha Nyaso alianza kumpa maelezo kuhusu jumba la F.K.

"... Upande wa kushoto kuna madirisha mawili makubwa", Nyaso alimaliza kueleza.

"Unasema Bon na Rocky walipita kwenye njia za siri ulizowaeleza?", Willy aliuliza.

"Bila shaka maana baada ya kuwaelekeza, wote walitoa ishara ya kukubali kwa kutumia vichwa vyao", Nyaso alijibu.

"Oke, mpenzi! Kwa heri", Willy alisema huku akimvuta Nyaso na kumbusu tena.

"Willy tafadhali... tafadhali...", Nyaso alibembeleza huku machozi yakimlenga.

"Usinitilie uchuro, mtoto we!", Willy alisema huku akiyeyuka na kutokomea gizani.

Roho ya Nyaso ilikuwa nzito sana lakini aliwasha gari na kurudi hotelini.

Willy alipanda na kuruka seng'enge akaingia uani. Kwa kuwa taa zilikuwa zinawaka kuzunguka eneo hilo, ilimbidi aende huku ameinama. Kwa kujificha kwenye vivuli vya miti mingi mizuri iliyopandwa kuzunguka nyumba hiyo. Willy hakuonekana na mtu. Alifika kwenye ukuta wa kushoto wa jumba hilo. Alijibanza na kisha kutambaa ili aweze kuona upande wa mbele wa nyumba. Alipofika tu kwenye kona ya jumba hilo, aliliona gari la mzee Hamisi limeegeshwa mbele karibu na mlango. Mara Willy alihisi mambo mawili. Kwanza, Majasusi wa makaburu walikuwa ndani wakimsubiri. Pili, kwamba Bon na Rocky walikuwa wameuawa na ndio sababu walikuwa hawakurudi. Aligundua kwamba alikuwa katika hatari kubwa. Hivyo ilibidi achukue tahadhari zaidi.

Akiwa sasa amelala chini Willy alisikia kishindo. Aligeuka na kuangalia upande huo lakini hakuona kitu. Aliamua kusubiri. Alijua fika kwamba katika mchezo huo, subira ni jambo muhimu. Kumbe aligundua kuwa kile kishindo kilikuwa cha mmoja wa askari wawili waliobakia kwani alimwona anatokea kwenye mti. Alikuwa amepangiwa kukaa juu ya mti huo na kutoa ishara kama angekitilia kitu chochote mashaka. Ajabu ni kwamba askari huyo alikuwa hakumwona Willy wakati alipoingia. Hivyo alikuwa ameamua kutelemka na kupanda mti mwingine. Kutokana na woga baada ya kuona wenzake walivyokufa askari huyo alikuwa anatembelea kwa uangalifu mkubwa. Willy alimwona askari yule karibu naye huku akinyata.

Alimsuburi mpaka walipokuwa sambamba ndipo Willy alipomrukia kwa spidi ya umeme na kumbana mdomo. Alimkata mkono wa shingo na kumuua pale pale. Kisha alimburuza taratibu na kumlaza alipokuwa yeye. Willy aliamua kuingia ndani ya nyumba kwa kupitia dirisha la kushoto. Baada ya kuangaza huku na kule na kuona kwamba kila kitu kilikuwa shwari, alijongea mpaka kwenye dirisha mojawapo na kulikagua. Alikuta limefungwa. Willy alichukua kisu chake maalumu chenye ncha ya almasi na kukata kipande cha kioo kutoka kwenye dirisha. Alipitisha mkono wake kwenye tundu na kufungua dirisha. Kisha alikwea dirishani na kutumbukia ndani ya chumba kilichokuwa giza. Baada ya kusimama tu alisikia sauti inasema.

"Shenzi kabisa". Halafu alisikia kitu kinamgonga kichwani. Willy alidondoka chini na kupoteza fahamu pale pale.

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom