Riwaya: Afisa usalama

Riwaya: Afisa usalama

RIWAYA: AFISA USALAMA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 21
ILIPOISHIA
Ofisi ya Rais ilimpa kazi Mr Paul Siafu kuchunguza na kubaini wahalifu wanaofanya mauaji na kuacha kitambaa chenye maandishi yanayosomeka ‘very sorry marehemu’. Alipewa muda wa miaka mitatu, miaka hiyo imeisha na inasemekana Mr Paul Siafu ameshakamilisha kazi hiyo na ameshaandaa ripoti maalumu ya kuwasilisha ofisi ya Rais”

ENDELEA

Colotilda akauliza kwa shauku

“Unamaanisha Mr Paulo Siafu Siafu aliandaa ripoti yenye majina ya wahalifu, ripoti yenye ufafanuzi wa wahalifu wa kundi la The Devil?”

Mr Hamisi Ernest akamshika kichwa Colotilda kisha akamwambia

“Una akili sana ndio maana nikaamua kukuingiza ndani ya idara hii, akili yako nyepesi sana kufikiria”

Akatoa mkono kwenye kichwa cha Colotilda kisha akaendelea

“Ndio, kuna ripoti yenye majina hayo, kitu kinachonishangaza Mr Paulo Siafu kauliwa kipindi ambacho alitakiwa kuwasilisha ripoti hiyo ofisi ya Rais na ikiwezekana apandishwe cheo kama alivyoahidiwa kuwa mkuu wa idara ya Usamala wa Taifa kanda ya Magharibi”

Akapiga mwayo mrefu kisha akaendelea

“Tuliokuwa tunajua habari hii ya marehemu kufanya kazi ya kutafuta majina ya wahalifu ni viongozi wakubwa wa idara, Maafisa Usalama mwengine hawakushirikishwa jambo hili. Sasa nani atakua amemuua kama sio kiongozi mwenzetu wa idara hii? Na kama jibu ni ndio basi kiongozi huyo wa idara atakua anashirikiana na kundi hilo la majambazi sugu”

Akatazama saa yake ya mkononi, ikamuonesha ni saa saba mchana akapuuzia kisha akaendela

“Ripoti aliyoiandaa ndio itakuwa chanzo cha kifo chake”

Colotilda akainamisha kichwa chini akatafakari kwa muda wa kama sekunde tatu kisha akainua kichwa chake, akasema

“Kati yenu viongozi wa juu kuna msaliti anayeendesha kundi hilo au anayeshirikiana na magaidi hao, ugumu unakuja jinsi ya kumfahamu kiongozi huyo”

Mr Hamisi Ernest akaendelea kumfafanulia Colotilda

“Nimekabidhiwa kazi ya kufatilia kifo cha Mr Paulo Siafu ili kumbaini au kuwabaini wahalifu, sasa najua nafatiliwa kila hatua ninayopiga”

Akatazama saa kwa mara nyingine kisha akaendelea

“Nakukabidhi kazi hii ufatilie juu chini mpaka tubaini nani anaongoza kundi hilo la majambazi, pia tujue taarifa kamili kuhusu ripoti aliyoiandaa Mr Paulo Siafu yenye majina ya wahalifu. Hutakiwa kumshirikisha yeyote ndani na nje ya idara yetu kwa sababu hatufahamu nani mwema na nani adui”

Akameza mate funda moja kisha akaendelea

“Najua umemzoea sana Magoela lakini naomba uelewe kuwa hata yeye hutakiwi kumwambia lolote. Kazi yako ya ushushushu imeanzia hapa, japokuwa kazi hii ni ngumu lakini ndio kipimo halisi cha ukomavu wako”

Colotilda alikua kimya akimsikiliza kwa makini Mr Hamisi Ernest, mzee yule akaendelea

“Utakua unaripoti kwangu kila hatua utakayopiga kwenye kazi hii, kumbuka lazima tushirikiane kila kitu ili kazi iishe haraka iwezekanavyo”

Mapigo ya moyo ya Colotilda yakaongeza kasi kama mtu aliyekimbia riadha, akili yake ikafikiria haraka sana, sasa akaona anaingizwa kwenye mdomo wa kifo. Atakataa vipi kuifanya kazi hiyo wakati ndio taaluma aliyoandaliwa kuifanya? Atakataa vipi wakati anamuheshimu sana Mr Hamisi Ernest na ndio baba yake aliyebakia kwenye ulimwengu huu uliokithiri machafuko na maafa?. Colotilda akamtazama usoni Mr Hamisi Ernest kisha akamwambia

“Wewe ni mzee wangu, nina kuhakikishia kuwa lazima nifahamu kila kitu kuhusu kazi uliyonipatia. Huyo anayejifanya Afisa Usalama mkubwa kumbe ni jambazi lazima afahamike kabda hali haijawa mbaya zaidi”

Maneno hayo yalimfurahisha Mr Hamisi Ernest, akaamini Colotilda ameiva hasa hasa kwenye idara hiyo. Mr Hamisi Ernest aliona uoga wote wa Colotilda aliokua nao utotoni sasa umetoweka, Colotilda amekua mpya. Msichana mrembo mwenye roho ya simba. Mr Hamisi Ernest akamwambia Colotilda

“Wewe ni Silent Notorious kama ulivyoitwa tangu ulipokua mtoto, lazima udhibitishe hilo. Vile vile ukichunguza kwa umakini unaweza ona kuna uhusiano mkubwa kati ya hawa wauaji na vifo vya familia yako”

Kauli hiyo ikamuongezea hasira Colotilda akachukua kitambaa toka kwenye mfuko wa jinzi aliyovaa kisha akajifuta chozi jembamba lililokua likitengeneza mfereji katika shavu lake la kulia. Baada ya dakika kumi Colotilda alimuaga Mr Hamisi Ernest Ernest kisha akaenda kwa mzee Calist alipofikia baada ya kuwasili Tanzania. Kipindi Mr Hamisi Ernest na Colotilda walipokua wakiongea na kupanga jinsi ya kupambana na maadui waliomuua Mr Paulo Siafu, upande wa pili wa shilingi ndani ya chumba namba 17 katika hoteli maarufu ya kifahari mkoani Kigoma inayoitwa ‘Hill Top’ walikuwemo Mr Aloyce Ndosi na Magoela. Mr Aloyce Ndosi alifikia katika hoteli hiyo siku aliyofika mkoani Kigoma kutokea Dar es salaam. Kikao kizito cha siri kilikuwa kikiendelea kati ya Mr Aloyce Ndosi na Fortunatus Magowela . Mr Aloyce Ndosi akamwambia Magowela

“Kuna kazi nataka kukupa, kazi itakayokufanya kuwa na uadui na Mr Hamisi Ernest”

Kauli hiyo ilimshtua kidogo Mago, akamtazama vizuri Mr Aloyce Ndosi kisha akauliza

“Nimesikia vibaya au ndivyo ulivyokusudia?”

Mr Aloyce Ndosi akacheka kinafiki kisha akamwambia Magoela

“Najua mliandaliwa kuja kulitetea Taifa la Tanzania lakini kuna kipindi lazima uangalie maslahi yako binafsi, usiwe mjinga kiasi kwamba ukasahau umasikini uliokua nao”

Mr Ndosi akachukua maji yaliyokua kwenye glasi akamwa fundo nne mfululizo kisha akaendela

“Nilikupigania uwe Afisa Usalama kwa sababu lengo langu lilikua uje kunisaidia kwenye mambo yangu, mambo ambayo yanahitaji umakini wa hali ya juu. Umri wangu umekwenda sana nahitaji kijana kama wewe wa kusimamia kila hatua”

Akili ya Magoela ilikua bado ikifikiria juu ya suala la kuwa adui wa Mr Hamisi Ernest, mzee ambaye alikua kama mzazi wake siku zote za masomo na mafunzo yake ya Uafisa Usalama, sasa itakuaje amlipe kwa ubaya?. Mr Aloyce Ndosi akaendelea

“Kama unavyojua nilikua mkuu wa idara ndani ya mkoa wa Dar es salaam lakini sasa nimeletwa mkoani Kigoma, siku yoyote nitakabidhiwa ukuu wa idara ndani ya mkoa huu. Kwa lugha nyepesi ninahamishwa toka Dar es salaam kuja Kigoma"

Akapumzika sekunde mbili, akaendelea

“Mkuu wa idara mkoani hapa alitakiwa awe mkuu wa idara wa kanda nzima ya magharibi lakini ndio kaishatangulia kwa Mungu, hilo sio tatizo bali tatizo limekuja baada ya kifo chake”

Magoela akauliza kwa shauku kutaka kujua zaidi

“Tatizo gani?”

Mr Aloyce Ndosi akainuka kwenye kiti alichokua amekaa akaanza kutembea tembea ndani ya chumba hicho huku akiongea

“Nasikia marehemu ameacha ripoti yenye majina ya watu wanaosadikika ni waharifu, watu wanaohujumu uchumi na kufanya matukio mengine yenye kutishia usalama wa nchi. Nataka ufatilie kuhusu ripoti hiyo, nataka inifikie kabla haijamfikia kiongozi yeyote wa idara hii. Hapo ndipo uadui wa wewe na Mr Hamisi Ernest unapoanzia, kwa sababu na yeye lazima afatilie pia kuhusu ripoti hiyo ili akamilishe kazi aliyopewa”

Magoela akamtazama kwa makini Mr Aloyce Ndosi kisha akamuuliza swali lingine ili apate ufafanuzi zaidi

“Kwanini unapingana na Mr Hamisi Ernest?”

Mr Ndosi akamjibu Mago huku akimtazama usoni kwa macho yake makavu

“Kwa sababu nataka siku za usoni uje kurithi mikoba yangu, nataka uje kuongoza kundi langu, kundi lenye matawi yake karibu kila kona ya nchi hii. Nataka upambane na Mr Hamisi Ernest kwa sababu anajifanya anajua kufatilia haki anasahau duniani hakuna haki kabisa, haki tutaikuta kwa Mungu tu”

Maneno hayo yakazidi kumchanganya Magoela, maswali mengi yakajazana kwenye kichwa chake. Akaamua kuuliza swali moja kati ya maswali hayo

“Una maanisha wewe ndiye uliyemuua Mr Paulo Siafu?”

Mr Aloyce Ndosi akatabasamu kidogo, meno yake yaliyoathirika na moshi wa sigara yakaonekana vizuri, akamjibu Magoela

“Hapana! Bali vijana wangu ndio waliomuua”

Akachukua tena glasi yake ya maji akanywa mafundo matatu kisha akaendelea

“Kiherehere chake ndicho kilichosababisha atangulie kwa Mungu. Naona Mr Hamisi Ernest anataka kumfuata Mr Paulo Siafu”

Mr Aloyce Ndosi akamueleza Magoela kuwa yeye ndie mmiliki wa kundi la majambazi wanaoua na kutelekeza kitambaa chenye maandishi yanayosomeka ‘Very sorry marehemu’. Hakuishia hapo bali alimueleza pia kuwa alimuua Mr Paulo Siafu baada ya kiongozi kutaka kutoa ripoti yenye kufichua maovu yake hadharani, lakini baada ya kumuua waliitafuta ripoti hiyo bila mafanikio. Uchunguzi ndani ya nyumba ya Mr Paulo Siafu uliendelea taratibu ndipo walipofanikiwa kukuta kijitabu kidogo ndani ya droo ndogo ya kitanda, ndani ya kijitabu hicho ilikutwa picha ndogo ya pasipoti saizi (passport size). Walipoigeuza nyuma picha hiyo walikua imeandikwa maneno machache yaliyosomeka “Ripoti kwa Rais”. Mr Aloyce Ndosi akamalizia maji yaliyokua kwenye glasi kisha akaendelea

“Baada ya kuona picha hiyo yenye ujumbe huo kazi ikabadilika. Sura ya kijana aliyekua kwenye picha ilikua ngeni kwa kila mmoja wetu lakini nashukuru Mungu nina vijana wengi kila sekta. Juzi nimeletewa taarifa na kijana wangu anayefanya kazi katika jeshi la polisi kuwa amebaini kijana huyo yupo gerezani, gereza la bangwe”.

Mr Aloyce Ndosi akapumzika kidogo kisha akaendelea

“Inasemekana ana miaka miwili gerezani, anatumikia kifungo cha miaka sita baada ya kukutwa na kesi ya kupanga kulipua jengo la mahakama mojawapo inayopatikana jirani na uwanja wa mpira wa Lake Tanganyika. Hapo nashindwa kuelewa kidogo, yaani inakuaje mtu mwenye ripoti hiyo yenye majina ya wahalifu awe gerezani wakati muda wa kuwasilishwa ripoti hiyo umeshafika?”

Akili ya Magoela ikazunguka haraka, ikashindwa kuhimili maswali yaliyojengeka kichwani kwake akaamua kuuliza ili kupunguza mrudikano wa maswali hayo.

“Kama huyo muhusika yupo gerezani kwa hiyo una maanisha nimfuate huko? Namfuata vipi wakati mimi sio mfungwa?”

Mr Aloyce Ndosi akatabasamu kwa maswali aliyoulizwa na Magoela, aliona katika maswali aliyowahi kuulizwa na kijana huyo maswali ya sasa ni rahisi kujibika, akamjibu huku akimpiga piga begani.

“Polisi aliyeniletea taarifa ya kijana tunayemtafuta anafanya kazi katika gereza la bangwe, vile vile hufanya kazi katika kituo cha polisi kilichopo jirani na mahakama ya mkoa. Hivyo basi suala la wewe kutengenezewa kesi na kuingizwa moja kwa moja gerezani pasipo kupitia mahakamani ni jambo dogo sana”.

Mago alifikiria suala hilo akaona hana jinsi zaidi ya kufanya kazi iliyo mbele yake, aliifikiria familia yake aliyoiacha jijini Dar es salaam akaona jinsi ilivyoathiriwa na umasikini uliokithiri. Akajiona yeye ndiye msaada pekee anayetegemea, sasa lazima achukue maamuzi magumu ili atengeneze pesa nyingi zaidi zitakazoweza kuwasaidia wazazi pamoja na ndugu zake. Japokua alikua akipewa pesa nyingi zilizoweza kukidhi mahitaji yake ipasavyo lakini alitamani maisha aishiyo yeye waishi jamii yake yote ya Dar es salaam. Kichwani kwake aliapa hataweza kumuua Mr Hamisi Ernest hata kama ukitokea ugumu wa namna gani katika kazi iliyo mbele yake, alimfikiria Colotilda pia akaona kuna ugumu katika kazi yake. Kwa akili yake ya ajabu akahisi Colotilda anaweza kuwa nyuma ya kazi ya Mr Hamisi Ernest, sasa aliona vita kati yake na Colotilda, alifikiria atafanyaje ili kukwepana kukutana ana kwa ana na Colotilda. Colotilda alikua kama dada yake wa tumbo moja, sasa aliona ugumu wa kazi iliyo mbele yake. Mago akamwambia Mr Aloyce Ndosi

“Kazi iliyo mbele yangu ni ngumu sana kwa sababu nahisi Colotilda atakua amevaa viatu vya Mr Hamisi Ernest , sasa akijua nipo gerezani kila kitu kitakua kigumu kwa sababu najua uwezo wake wa uchunguzi na utafiti”

Mr Aloyce Ndosi akakuna kichwa chake, kichwa kiwaka moto, awali hakufikiria kabisa uwepo wa Colotilda. Jambo aliloambiwa na Magoela aliona lina ukweli asilimia zote. Kama ilivyo kawaida yake roho ya ukatili ikamwingia, yakamtoka maneno makali yaliyomchanganya zaidi Magoela

“Kila atakayeibuka kuwa kipingamizi kwenye jambo hili atakua amejiingiza mwenyewe kwenye mlango wa kifo, sitaki siri yangu ifichuke”.

Magoela aliona ukatili halisi wa mzee huyo, akaona kweli amezamilia kufanya ukatili wowote kwa lengo la kukinga siri zake zilizo njiani kufichuka. Suala la kumuangamiza Colotilda nalo lilileta taswira mpya katika akili yake yake, akamueleza Mr Aloyce Ndosi

“Kumbuka Colotilda ni kama dada yangu wa tumbo moja, nimekua nae toka utotoni na tumesaidiana vitu na mambo mengi mpaka tumefanikiwa kufika hapa tulipo. Sasa nitawezaje kumdhuru endapo akiwa kikwazo katika suala hili?”

Sura ya Mr Aloyce Ndosi ikabadilika, makunyanzi yakaishambulia sura yake iliyotawaliwa na ndevu nyingi mashavuni. Akamuangalia Magoela kwa macho makali kisha akamwambia kwa sauti ya juu kidogo

“Huyo Colotilda umemjua baada ya kukutana Afrika Kusini, huna undugu nae hata kidogo umesikia? Ndugu zako umewaacha Dar es salaam”

Mr Aloyce Ndosi alikua kama mzazi kwa Magoela hivyo basi Magoela hakuwa na jinsi zaidi ya kukubali kufanya kazi hiyo kama alivyosisitizwa. Roho ngumu ikamwingia Magoela akaona pesa za kutosha na Mr Aloyce Ndosi na familia yake ndio kila kitu kwake. Akamtazama Mr Aloyce Ndosi kisha akamwambia

“Mzee hakuna siri itakayovuja”

Kauli hiyo ikaibua tabasamu mororo katika mashavu yaliyofunikwa na ndevu, Mr Aloyce Ndosi akamkumbatia kijana wake kisha akamwambia

“Kuhusu pesa usiwe na shaka, kazi zetu hutengeneza pesa nyingi. Nakuahidi ndani ya muda mfupi utakua kijana tajiri katika nchi hii na hakuna atakaye kutilia mashaka kwa sababu atakaye thubutu atalichungulia kaburi”

Akameza mate fundo moja kisha akavuta pumzi ndefu ndani akairuhusu itoke nje kwa nguvu, akaendelea na maneno yake.

“Fanya uwezalo kazi ianze mara moja”

Waliongea mengi sana na kukubaliana lazima kazi ya kumfatilia Colotilda na Mr Hamisi Ernest ianze siku inayofuata.

YUPO WAPI GOD MOTHER?

NAFIKIRI TUSUBIRI KITABU SASA. SITAPOST TENA RIWAYA HII KATIKA UKURASA HUU.

KAMA UNAHITAJI KITABU TUMA JINA NA NAMBA YAKO KWENYE NAMBA 0758 195 890 ILI NAKALA YAKO IANDALIWE.

LEO NAFUNGUA GROUP LA WHATSAPP TUTAKALOKUWA TUNAPEANA MREJESHO KUHUSU RIWAYA HII, LINI KITABU KITATOKA NA NSHU ZINGINE ZINAZOHUSU KAZI HII.

ASANTE.
kazi na dawa, umeeleweka mkuu
 
Tusubiri kitabu ndg
Sawa ndugu lkn wengine huwa ni wapenzi wa soft copy hasa kwa issue ya ubebaji na utunzaji waandishi wenzio huwa wanautaratibu wakuuza hata softcopy. Shida ya nakala ngumu ni pale mtu anapoazima haitarudi kama ulivyompatia. Wengine tunàhifadhi katika electronic library hivyo unapaswa na sisi kutufikiria. Ndiyo maana hata amazon huwa tunanunua sana vitabu
 
Sawa ndugu lkn wengine huwa ni wapenzi wa soft copy hasa kwa issue ya ubebaji na utunzaji waandishi wenzio huwa wanautaratibu wakuuza hata softcopy. Shida ya nakala ngumu ni pale mtu anapoazima haitarudi kama ulivyompatia. Wengine tunàhifadhi katika electronic library hivyo unapaswa na sisi kutufikiria. Ndiyo maana hata amazon huwa tunanunua sana vitabu
Ndg nitafute kwa namba 0758 195 890 tuongee, tutaelewana tu
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 01

David alimtaza mpenzi wake aliyekuwa akihesabu hela iliyokuwa juu ya meza yao chakavu, meza iliyopoteza rangi yake ya asili, mpenzi aliyeishi nae kama mke pasipo vigezo vyovyote. Mwanamke yule aliipata idadi kamili ya pesa, akamwambia David

"Imebaki mia saba hamsini mpenzi"

Kichwa cha David kilikuwa moto kwa mawazo hakujuwa afanye nini kwa wakati huo ili apate pesa ya matumizi na pesa atakayotumia kwenye huduma za kujifungua kwa mpenzi wake huyo. Mwanamke wake alikuwa na mimba ya miezi tisa, walitegemea siku yoyote anaweza kujifungua. Aliwaza kuomba msaada kwa ndugu na jamaa lakini aliamini hawezi kusaidiwa kwa sababu ameshawachosha kwa uombaji wake wa pesa. Alikuwa akinuka madeni. Upande wa mwanamke wake aliyefahamika kwa jina la Winnie hakukuwa na namna yoyote wangeyoweza kuitumia ili kuupata msaada wao, kwa sababu upande ule haukuridhia kabisa David kuishi na mtoto wao, hivyo basi walimzira mwanao na kumfukuza moja kwa moja wakimwambia asije kugeuza kichwa nyuma kuwatazama.

David aliinamisha kichwa chini kama kobe anayetunga sheria kisha akakiinua, tayari alikuwa ana majibu ya nini alichopaswa kufanya. Alimwambia Winnie

"Acha nitoke niende mtaani kutafuta pesa, lazima pesa ipatikane kwa sababu siku yoyote unaweza kupata uchungu wa kujifungua"

Ilikuwa ni kauli nzuri kwenye masikio ya mpenzi wake lakini bado ilimpa mashaka na taharuki za kutosha. Ilibidi kuuliza ili apate ufafanuzi zaidi

"Unaenda wapi kutafuta pesa?"

David alishindwa kumjibu mpenzi wake, aliamini akimwambia akiwazacho akilini mwake lazima apate pingamizi kali toka kwa Winnie. Aliapa kutokuwambia kabisa. Swali la Winnie lilikuwa na maana sana kwa sababu David hakuwa na kazi yoyote baada ya kufukuzwa kazi yake ya ulinzi aliyokuwa akiifanya katika kampuni ya ujenzi ya mchina. David aligeuza kichwa chake akamwambia mpenzi wake

"Ukimzaa mwanangu utamwita jina langu, endapo akiwa wa kike utamwita jina lako au jina la marehemu mama yangu. Utachagua kati ya majina hayo"

Kauli ya David ilikuwa ngumu kueleweka katika kichwa cha mpenzi wake. Alijiuliza maswali kadhaa akilini mwake.

Anataka kunitoroka na kuniacha peke yangu? Anataka kujiua? Anawaza nini kichwani kwake?

Hakika alikosa majibu ya maswali yote. Alipoinua kichwa chake ili aulize maswali yake lakini hakubahatika kumuona David, David alikuwa ameshatoka ndani ya nyumba hiyo. Hofu ikampanda Winnie, mawazo yakazidi maradufu kichwani. Uchungu wa uzazi ukachukua nafasi yake. Alianza kulia kwa uchungu, kilio kile kilifanikiwa kuyafikia masikio ya David aliyekuwa nje akivaa viatu tayari kwa kuondoka. Alirudi ndani haraka akamkuta mpenzi wake akilalamika kwa uchungu. Macho yalimtoka pima David.

Alimbeba mikononi mpenzi wake mpaka barabarani, bahati ilikuwa upande wake kwa sababu alifanikiwa kuiona bajaji na kuisimamisha. Haraka kwa sauti ya kitetemeshi alimwambia dereva wa bajaji

"Tupeleke hospitali ya Maweni haraka"

Dereva alipoona hali ya Winnie na uharaka waliokuwa nao aliamini hapo ndipo pa kupatia pesa, aliamini dau lolote atakalosema lazima wakubali. Aliongea

"Utanipa elfu kumi ndugu yangu"

David hakuwa na muda wa kujibizana na dereva, alimpandisha mpenzi wake kisha akapanda. Hata hakuelewa alichoambiwa na dereva, akili yake ilikuwa ikiwaza maumivu aliyokuwa akiyapitia mpenzi wake. Safari ilianza kwa mwendo kasi kwa sababu David alikuwa akimshinikiza dereva bajaji awahi ili kunusuru maisha ya mpenzi wake. Walifika hospitali, Winnie akachukuliwa na manesi haraka wakampeleka wodi namba moja, wodi maalumu kwa masuala ya uzazi. David alibaki na mwenye bajaji. Alijisachi mfukoni kama mtu atafutaye pesa lakini hakuwa na kiasi chochote mfukoni. Akakumbuka hata ile mia saba hamsini ya akiba imebaki katika chumba alichopanga, akili ikawaza moto. Akamtazama dereva wa bajaji kisha akamuuliza

Hivi ulisema shilingi ngapi?"

Dereva hakupendezwa kabisa na swali lile, aliamini kitakachofata ni usumbufu kwa sababu alishuhudia jinsi David alivyokuwa akihangaika kujisaji mifukoni pasipo kupata chochote. Akamjibu kwa hasira

"Elfu kumi jamaa"

David alishtuka kama mtu aliyeona au kusimuliwa kitu cha ajabu au chenye kutisha. Alikataa katakata akimwambia dereva yule kuwa hawezi kumlipa pesa kubwa kiasi kile, sehemu ambayo kwa kawaida hulipa elfu mbili mpaka tatu. Mzozo ukaibuka. Kipindi mzozo ukiendelea mara mmoja kati ya manesi waliompokea Winnie alifika eneo lile na kuwatuliza kwa maneno ya upole. Walipotulia akamuuliza David

"Bila shaka wewe ndiye uliyekuja na yule dada mwenye uchungu aliyevaa gauni lekundu?"

David alijibu kwa haraka kwa sauti ya kuhema hema kutokana na majibizano aliyokuwa nayo na dereva wa bajaji

"Ndio dada yangu, wala hujakosea"

Sasa ilikuwa ni zamu ya nesi kuongea lakini alisita kidogo, akamkazia macho David aliyekuwa na hofu pamoja na taharuki ya kutaka kufahamu nini kinachoendelea. Nesi akaongea

"Mwanamke uliyemleta ana njia ndogo ya kujifungua, sio nzuri kwa mtu anayehitaji kujifungua kwa njia ya kawaida. Daktari na manesi wapo wanajaribu uwezekano lakini lolote laweza kutokea. Ikishindikana kabisa atajifungua kwa upasuaji. Waweza kujiandaa kwa gharama za upasuaji pia japokuwa hatuombei apasuliwe"

Akili ya David ilimpaa kabisa akawa kama anaota huku amesimama wima, alishindwa kuongea wala kujibu chochote. Kwa mbali alisikia kelele za dereva wa bajaji, kelele zilizosisitiza kulipwa elfu kumi yake ya nauli.

ITAENDELEA
86666ba97e3f48699485bb3052748b15.jpg
 
Mkuu wenzako asilimia kubwa wanao leta story zao wanazimaliza kabisa, ila umekuwa mtu kuzikatisha story zako mapema, watakuja wengine kuzisoma ila nakushauri inabidi uimalize hata stori yako moja mkuu.
 
Mkuu wenzako asilimia kubwa wanao leta story zao wanazimaliza kabisa, ila umekuwa mtu kuzikatisha story zako mapema, watakuja wengine kuzisoma ila nakushauri inabidi uimalize hata stori yako moja mkuu.
Asante sana kwa ushauri, nafikiri hii itaisha. Lakini yakupasa kukumbuka utunzi wa story ndio kazi niliyochagua, so niki'offer story yote nitakosa hata pesa ya bundle ya ku'post story zingine, ndio maana natoa kitabu nikihitaji support yenu.
 
Asante sana kwa ushauri, nafikiri hii itaisha. Lakini yakupasa kukumbuka utunzi wa story ndio kazi niliyochagua, so niki'offer story yote nitakosa hata pesa ya bundle ya ku'post story zingine, ndio maana natoa kitabu nikihitaji support yenu.
Wenzako huwa wana sacrifice hata story moja kwanza, watu wanaona potential yako kwenye utunzi, hivi vitu huwa ni automatically motivated
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 02

David aliona jinsi maji yalivyozidi unga. Hakuwa na jibu lolote kwa nesi wala dereva wa bajaji. Akili yake ikaikumbuka kauli ya rafiki yake kipenzi, kauli iliyomsisitiza kuwa jasiri ili afanikiwe kimaisha. Sasa aliona ni wakati wa kukubaliana na kauli ile. Nesi alivyoona ukimya wa David alimpuuza na kuondoka zake eneo lile. Mzozo wa David na dereva wa bajaji ukaanza upya, safari hii dereva alikuwa moto sana. David ilibidi awe mpole kama mtoto aombaye pesa ya ada kwa mzazi wa kambo. Akamwambia dereva wa bajaji

"Mimi ni mwanaume mwenzako naomba unielewe, sina pesa ya kukulipa ndugu yangu. Nimevurugwa hapa".

Kauli hiyo ilikuwa kama tusi kwenye masikio ya dereva yule. Kelele zikaongezeka maradufu. Watu wakajaa kushuhudia nini kilichokuwa kikiendelea, vile vile hata walinzi wenye kazi ya kudumisha ulinzi na usalama wa hospitali walifika haraka. Walijaribu kuwasikiliza wote, makosa yakaangukia kwa David japokuwa na dereva alikosolewa kwa bei aliyoitaja. Baadhi ya raia walimtetea David wakiamini atakuwa amevurugwa na hali ya mwanamke wake. Dereva alizidi kuwa mkali akihitaji pesa yake. Kelele zilivyozidi zilikuwa kero, David akaamua kuondoa kero hilo, alikuwa tayari kujizalilisha ili maneno yaishe. Alimwambia dereva yule kuwa ampe saa, mkanda na viatu alivyovaa ili awe amelipa deni lake.

Dereva alikubali haraka sana, aliamini vitu hivyo vina thamani kubwa kuliko pesa anayodai. Lakini kabda David hajavua chochote, ilisikia sauti nyororo ikisema

"Usimdhalilishe mwanaume mwenzako, muache aondoke zake nitamlipia deni lake"

David aligeuka nyuma kumtazama aliyeongea, hakika alikuwa ni mrembo. Alikutanisha macho na mtoto mwenye asili ya kiarabu akimtazama kwa huruma. Binti yule alitoa noti mbili za shilingi elfu kumi, moja akamkabidhi dereva wa bajaji na nyingine akamkabidhi David kisha akamwambia

"Utafanya nauli ya kurudi kwako"

David alimshukuru sana dada yule aliyekuwa kama malaika aliyetumwa na Mungu aje kumuokoa na aibu ya dunia. Dereva wa bajaji hakuwa na neno la kuongeza, hakumuaga yeyote wala hakuhitaji kumbeba tena David kwa sababu walikuwa wameshatibuana vibaya. David baada ya kumuaga binti yule wa kiarabu aliondoka ndani ya jengo la hospitali haraka huku akili yake ikiwaza mpango alioambiwa na rafiki yake. Japokuwa alipewa pesa ya nauli lakini aliamua kutembea kwa miguu, aliamini akitumia pesa hiyo kwa wakati huo hatopata pesa nyingine. Mawazo yakarudi kumfikiria mpenzi wake aliyemuacha wodini, akazifikiria gharama alizoambiwa

"Eti gharama za upasuaji"

Alimini lazima aingie kwenye kazi aliyoikataa awali ili apate pesa ya haraka. Kipindi akipiga hatua kuelekea kwa rafiki yake, akili nyingine ilimkumbusha umuhimu wa kuandaa chakula cha Winnie. Alibadilisha mawazo ya kwenda kwa rafiki yake. Aliona bora aende kwenye nyumba aliyopanga amuombe mpangaji mwenzake amsaidie kuandaa chakula cha mpenzi wake ili akipeleke hospitali. Ndivyo alivyofanya. Alimpatia Edna ile elfu kumi aliyopewa na dada yule mwenye asili ya kiarabu. Edna hakuwa na hiyana alikubali kuandaa chakula cha Winnie, alienda dukani kisha sokoni akanunua mahitaji ya Winnie kisha akaingia jikoni na kuanza kupika. Kipindi upishi ukiendelea, David alihisi akizidi kuchelewa kwenda kwa rafiki yake mwenye kazi za kijasiri. Aliondoka kimya kimya pasipo kumuaga Edna. Edna alipomaliza kuandaa chakula hakumuona David, alipojaribu kumpigia simu iliita pale pale alipokuwepo. David aliiacha simu yake makusudi.

Alimsubiri pasipo mafanikio, masaa ya kuona wagonjwa yalipofika Edna aliamua kubeba chakula mwenyewe na kuelekea hospitali. Kitendo kile kilimuudhi sana Edna na kilimshangaza sana kwa kuona David aliondoka bila kumuaga na kuelekea pasipo julikana wakati anafahamu hali ya mwanamke wake. Edna alifika hospitali na kapu lake la chakula. Mungu sio Athumani, alikuta Winnie amejifungua salama kwa njia ya kawaida mtoto wa kike. Lakini kitendo cha Edna kupeleka chakula pasipo uwepo wa David kilimpa sana mashaka Winnie aliyekuwa amembeba mtoto wake kipenzi mikononi. Alipomuuliza Edna ndio alizidi kuchanganyikiwa zaidi na kupandwa na taharuki. Kipindi akiendelea kupambana na mshangao wake mara aliletewa risiti ya malipo ya huduma zote alizokuwa ameshahudumiwa hospitali hapo.

Alipoitaza kilikuwa ni kiasi kikubwa kulingana na hali waliyokuwa nayo, alijiuliza David amepata wapi pesa hiyo haraka hivyo? Kwanini risiti iletwe na nesi? David yupo wapi?

Winnie akamuuliza nesi aliyemkabidhi risiti ile

"David yupo wapi?"

Jibu la nesi lilimuacha Winnie mdomo wazi, nesi alijibu

"Aliyenipa risiti alijitambulisha kwa jina moja la Zimwi sio David. Kijana mwenye rasta fupi, alisema kuwa ni mdogo wako mnayefatana"

Jibu la nesi lilimvuruga zaidi Winnie, eti mdogo wake wanayefatana wakati yeye ndiye mtoto wa mwisho katika familia yao. Alihisi kuna kitu hakipo sawa. Alimfikiria David, sasa aliamini atakuwa ameenda kufanya kazi aliyomkataza kujihusisha nayo. Aliiona hatari mbele yake.

ITAENDELEA

KUJIUNGA NA GROUP LANGU LA WHATSAPP
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 03

Zilikuwa zimepita siku mbili tangu Winnie aruhusiwe kutoka hospitali, mtoto wake wa kike aliyempa jina la Lucia, jina la marehemu mama yake na David alikuwa na afya nzuri kabisa. Siku zote hizo hakufanikiwa kumuona David. Hofu na hali ya sitofahamu vilizidi kuchanganya akili ya Winnie, alishangaa sana siku zilivyozidi kusonga pasipo kumuona kipenzi chake aliyekuwa akitamani kuwa naye kila dakika. Alijiuliza maswali akajijibu mwenyewe. Alishangazwa na kitendo cha David kushindwa kwenda kumuona mwana wake. Siku zilisogea kama kawaida, maisha ya shida yalikuwa ni rafiki yake. Siku moja jioni ya saa kumi na mbili alipokea mgeni aliyekuwa hamfahamu kabisa, mgeni huyo alikuwa akinukia marashi ya bei ghari sana, mgeni alijitambulisha kuwa ametumwa na mama yake ampelekee zawadi ya kujifungua. Winnie alishangaa sana kusikia taarifa kutoka kwa mama yake mzazi aliyemkana na kumkataa baada ya kuamua kuishi na David.

Mgeni yule alimkabidhi begi dogo Winnie alilomuhakikishia kuwa limetoka kwa mama yake kipenzi. Mgeni aliaga na kuondoka zake pasipo kujitambulisha kuwa yeye ni nani haswa. Winnie hakujali hilo, yeye alifurahishwa na zawadi toka kwa mama yake mzazi. Baada ya kumaliza shughuli zake za nyumbani, Winnie alifungua begi lile kwa lengo la kuangalia zawadi toka kwa mama yake. Alipata mshangao mkubwa na mapigo ya moyo yakaongezeka maradufu, haikuwa zawadi toka kwa mama yake kama alivyoambiwa bali ilikuwa ni zawadi toka kwa mpenzi wake, David. Begi lilikuwa na picha ya David, kipande kidogo cha karatasi pamoja na noti za elfu kumi zenye thamani ya shilingi za Kitanzania laki moja na elfu sabini. Alisoma kipande kile cha karatasi kilichokuwa na ujumbe uliosema

"Napambana na ajili yako na mwanangu. Chunga sana maisha yenu, uhai wenu ndio uhai wangu"

Sasa Winnie alielewa fika kuwa aliyempa begi hilo atakuwa sehemu moja na David, na aliamini aliamua kumpa pesa zile kwa njia ile kwa sababu aliogopa kuulizwa maswali mengi kuhusu mpenzi wake. Moyo ulimuuma sana na kujilaumu kwanini hakufungua zawadi yake mbele ya mgeni wake. Alitamani asiitumie pesa ile kwa kuamini itakuwa haramu yenye damu za watu lakini aliikosa jeuri hiyo, hali ngumu ya maisha aliyokuwa nayo ilimwambia kuwa pesa zile ni halali kabisa. Siku zilisogea kama kawaida, siku mara wiki mbili zikapita pasipo kumuona David. Lakini suala la kupata pesa katika mazingira ya kutatanisha liliendelea kama kawaida. Kuna siku aliamka na kukuta mfuko wenye pesa mlangoni kwake, siku zingine watoto wadogo wa mtaani kwake walimpelekea bahasha ya kaki yenye hela na alipowauliza wamepewa na nani walimjibu hawamjui kabisa, hawajawahi kumuona mtaani kwao. Vile vile aliendelea kupokea ujumbe tofauti tofauti wenye kumsisitiza kujitunza yeye pamoja na kumtunza mtoto.
***********
Ulikuwa ni usiku wa maneno, nyota zilikuwa zimelipamba anga kila kona ya dunia. Mji ulikuwa kimya huku raia wengi wakiendelea kuota jonzi njema za mafanikio. David alikuwa kazini. Alikuwa amevaa begi dogo la mkanda mmoja, ndani ya begi hilo kulikuwa na madawa ya kulevya aina ya heroine aliyokuwa akiyapeleka katika pwani ya ziwa Tanganyika, sehemu maarufu kwa jina la forodhani. Sehemu maalumu ambayo wavuvi huegesha vyombo vyao vya majini. Alihakikishiwa kuwa akifika eneo lile atakutana na kijana mweusi mwenye miraba minne, amkabidhi begi hilo kisha aondoke zake. Ndivyo ilivyokuwa. Alifanikiwa kumuona kijana huyo wa miraba minne akamkabidhi begi lile kisha wakaagana. Kijana mwenye mwili wa miraba minne aliwasha boti lake la mwendo kasi kisha safari ya kuelekea nchini Congo ikaanza. David alibaki akijiuliza

"Atawezaje kuingia na mzigo wa madawa nchini Congo?"

Hakika David alikuwa hajakomaa kwenye biashara hiyo. Taratibu akageuka na kuanza kurudi alipotoka. Lakini Mungu hakuwa upande wake, ghafla alishangaa mwanga mkali wa tochi ukimpiga usoni. Alibabaika kwa hofu. Kabda hajachukua hatua yoyote alisikia sauti kali ya kukwaruza ikimshurutisha kusimama na kuweka mikono juu. Hakika kilikuwa ni kitendo cha haraka sana kilichomchanganya. Alibaki akitetemeka kama mtoto na alishindwa kutii amri ile kwa sababu hakuelewa kabisa alichoagizwa kufanya. Taswira ya mpenzi wake akiwa na mimba ikamjia kichwani. Moyo ukamuuma sana kuona anaelekea kwenye shimo la hewa. Shimo litakalo mtenga na familia yake. Mwanaume aliyemshurutisha awali akaipaza sauti yake kwa mara ya pili

"Naitwa kapteni Mussa toka jeshi la polisi, upo chini ya ulinzi kwa kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya"

Mwanzo David alimurikwa na tochi moja, lakini muda huo alikuwa akimurikwa na matochi zaidi ya saba kitu kilichomaanisha aliyepaza sauti hakuwa peke yake.

ITAENDELEA
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI (Mwandishi Phiri)
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 04
Mwanga uliongezeka maradufu machoni, macho ya David yakashindwa kuvumilia kabisa akajikuta akiukinga uso wake kwa mikono ili kupambana na mwanga huo, lakini alihisi kuna miale ya mwanga iliendelea kupenya. Alitamani ageuke nyuma ili atimue mbio lakini alijihakikishia kitendo hilo lazima kimpeleke kuzimu, aliamini lazima apigwe risasi za mgongo kisha kifo kichukue nafasi yake. Akili ilikataa, aliona bora aende gerezani kwa sababu atapata wasaa wa kuonana na mwanae pamoja na mpenzi wake, Winnie. Alibaki amesimama wima kama mlingoti wa umeme huku mikono yake ikiendelea kupambana na mwanga uliokuwa ukimshambulia pasipo huruma.

Vijana zaidi ya saba waliokuwa na matochi yenye mwanga mkali walimfuata David taratibu, hakika walikuwa wakijihakikishia usalama wao.Walipomfikia hawakuwa na jambo la kuuliza wala kuongea. David alipigwa kitako cha bunduki kichwani, alishindwa kuvumilia maumivu yake, mikono iliyokuwa usoni ikipambana na mwanga ilihamia kichwani mahali aliposhambuliwa. Alipiga kelele zilizomaanisha alikuwa akipitia maumivu makali, kijana mwenye sauti kali ya kukwaruza hakujali kilio cha David, alipaza sauti

"Kaa kimya mpuuzi wewe, unaleta utoto hapa"

Hakika sauti ile ilipenya vizuri katika masikio ya David, alijikuta akikaa kimya pasipo kupenda, kwa mbali alisikika akilia kilio cha kwikwi. David aliinua kichwa chake kisha akawatazama vijana wenye matochi, alijihakikishia walikuwa zaidi ya saba, hakuna hata mmoja aliyekuwa amevaa mavazi ya polisi japokuwa walikuwa na silaha za moto, walikuwa wamevaa mavazi ya kisasa yanayopendwa na vijana wenye miaka kuanzia kumi na sana mpaka thelathini na sita au arobaini. Hakujali muonekano kwa sababu polisi sio lazima awe jezi zake, kuna baadhi ya kazi humlazimu kuvaa kiraia.

David alijaribu kujitetea lakini vijana wale hawakuwa na muda wa kumsikiliza. Walimfunga pingu mikononi kisha akavishwa soksi usoni, soksi iliyomzuia kuona chochote. Sasa alikuwa akiona giza mbele yake. Aliinuliwa kwa nguvu na kuanza kuongozwa njia, hakujuwa walikuwa wakielekea wapi kwa sababu soksi aliyovishwa ilitoa kipingamizi cha kutosha. Alijutia maamuzi yake ya kujiunga katika kundi haramu linalosambaza na kuuza madawa ya kulivya ndani na nje ya nchi, alikumbuka mara kadhaa alivyokatazwa na mpenzi wake kuhusu kujiingiza kwenye mtandao huo. Aliuona usaliti wake, usaliti uliomponza sasa. Akajisemea moyoni

"Nisamehe Winnie wangu, sikusikiliza kauli yako. Acha dunia inifunze"

Hakika hakusikiliza kauli ya mpenzi wake lakini angefanya nini wakati alikuwa akihitaji pesa za haraka kwa ajili ya kumsaidia mpenzi wake pamoja na mtoto?

Safari yao ya kibubu bubu ilishia ndani ya gari, David aliingizwa garini kisha akalisikia likiondoka kwa mwendo wa wastani. Hakujuwa ni aina gani ya gari na walikuwa wakielekea kituo gani cha polisi, alichojuwa yeye walikuwa ndani ya gari linaloelekea kituo cha polisi. Alijisemea na kujiapiza ndani ya moyo wake kuwa hatawataja wenzake anaofanya nao kazi, aliamini hata apigwe namna gani hatofungua mdomo wake kuwataja wenzake. David alihofia usalama wa familia yake, aliamini endapo akiwataja wenzake atakuwa ameihatarisha familia yake. Aliamini lazima waishambulie na kuiteketeza kabisa. Hakutaka kusikia suala la kifo cha mpenzi wake wala mtoto. Aliamini yeye ndiye wa kuwatetea kwa sababu hawakuwa na msaada sehemu nyingine. Hakika alitaka kosa alilolifanya limuhukumu mwenyewe.
***********************

Jogoo waliendelea kuwika, hakika walipaza sauti zao haswa hali iliyoonesha walikuwa na hadhi na vigezo vyote vya kuitwa madume ya mbegu. Sauti zile za jogoo zilisikika maradufu katika masikio ya David kwa sababu siku hiyo hakupata wasaa wa kulala hata dakika moja. Sio kwamba alikosa kitanda cha kulalia, hapana, alikuwa juu ya kitanda na chumba safi zaidi ya alichokuwa akikimiliki chumbani. Usingizi ulimpaa siku hiyo, nafasi ya usingizi ilijazwa na mawazo tele. Usiku kucha alijiuliza maswali pasipo majibu, kila swali lililomjia kichwani lilikosa majibu sahihi. Maswali yaliyomchanganya zaidi yalikuwa

"Hapa ni wapi?, mbona sio polisi? Au walionikamata sio mapolisi? Ni akina nani sasa?"

Kichwa kiliwaka moto kwa mawazo. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha kuwa ni saa moja kasoro dakika kumi asubuhi, akajisachi mfukoni ili atoe simu yake yenye chapa ya Samsung lakini hakuiona. Simu hiyo alinunuliwa na kundi lake linalojihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya baada ya kuiacha simu yake nyumbani. Kitendo cha kuikosa simu yake mfukoni kilimaanisha ilichukuliwa na watekaji ili asiweze kufanya mawasiliano na mtu yeyote. Alijiuliza mara mbili mbili

"Waliichukua saa ngapi? Mbona sijalala kabisa?"

Alikosa majibu ya maswali yake, sasa aliamini yupo chini ya watu hatari zaidi asiojuwa kama ni polisi au laah!. Kipindi akiendelea kupambana na mawazo kichwani, ghafla mlango wa chumba alichomo ukafunguliwa kisha akaingia kijana wa makamo, kijana mwenye umri wa miaka isiyozidi ishirini na saba. Kijana yule alikuwa mtanashati sana mwenye kunukia vizuri, kichwani alikuwa na rasta fupi zilizopendezesha kichwa chake kilichobeba sura nzuri. David alimkazia macho kijana yule aliyekuwa akipita hatua taratibu kama mtu anayelazimishwa kwenda mahala alipo, alijihakikishia sio mmoja wa wachache aliofanikiwa kuona sura zao usiku uliopita kipindi akikamatwa. Kijana mtanashati alifika mbele ya David akajitambulisha huku sura yake ikiwa na bashasha ya furaha na uchangamfu uliotukuka

"Naitwa Zimwi, karibu katika maskani hii"

ITAENDELEA
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 05

Sio jina tu bali hata sura ya Zimwi ilikuwa ngeni katika utashi wa David, alibaki kamkodolea macho kama mtu aliyehitaji maelezo zaidi. Zimwi aliyekuwa amekaa kwenye moja ya viti vilivyopatikana ndani ya chumba hicho alielewa hali ya David lakini hakujali chochote, bali aliendelea na ufafanuzi wake

"Mimi ndiye niliyefanya malipo ya huduma alizopatiwa mpenzi wako kipindi alipokuwa hospitali kwenye nshu yake ya kujifungua"

David alipata mwanga wa nani aliyefanya malipo ya huduma za mpenzi wake kwa sababu awali yeye na watu wake aliokuwa akishirikiana nao kwenye nshu za madawa ya kulevya walishindwa kuelewa nani aliyelipa. Kijana aliyekuwa akisambaza pesa kwa Winnie hakukuta deni lolote la matibabu siku aliyoenda maalumu kwa kulipa deni hilo. Hawakuelewa Winnie alilipaje, mwisho wa siku waliamini atakuwa alisaidiwa na wapangaji wenzake. Hawakujuwa nyuma ya pazia kuna mtu alikuwa akifatilia maisha ya David. Zimwi akaendelea

"Mpenzi wako na mwanao wapo salama kabisa wala usiwe na hofu yoyote lakini mbele ya siku za usoni wanaweza wakawa sehemu mbaya zaidi...tumegundua huwa mnampelekea pesa za matumizi kwa njia zenu za kijambazi, hakika wote mtaingia mikononi mwetu tu"

Ujasiri ukamvaa David baada ya kujihakikishia huyo sio polisi bali ni mtekaji, ujasiri uliohitaji kumfahamu zaidi

"Wewe ni nani haswa? Mbona sikuelewi"

Kijana aliyejitambulisha kwa jina la Zimwi wala hakuonesha dalili yoyote ya kushangazwa na maswali ya David, hakika alitegemea kuulizwa maswali hayo toka awali. Akimtazama David usoni kisha akamjibu kwa sauti ya kujiamini

"Kama nilivyokwambia naitwa Zimwi, lakini hilo sio jina langu kamili. Hilo ni jina la kazi zangu, kazi kama hii inayoendelea"

Sasa David aliamini atakuwa kwenye mikono ya maadui wa kundi lake analolitumikia, aliamini hivyo kwa sababu mara kadhaa makundi yanayojishuhurisha na masuala ya kuuza na kununua madawa ya kulevya hugeukana yenyewe kwa yenyewe, hali hiyo hutengeneza uadui kati yao. Uadui ambao hupelekea vita kali ya kuuwana. Hakika alijiona yupo kwenye mikono ya Zimwi halisi aliyetumwa kuchukua roho yake. Kijana yule mtanashati mwenye rasta kichwani akaendelea na ufafanuzi zaidi

"Jina langu kamili naitwa Alimas Jumbe, nafanya kazi katika kitengo cha siri kinachopambana na kudhibiti uuzaji na usambazaji wa madawa ya kulevya nchini"

Utambulisho huo ulimaanisha David hakuwa kwenye mikono salama japokuwa hakuwa kwenye mikono ya wahalifu aliowafikiria awali. Aliamini kitendo cha yeye kukamatwa na watu wanaojihusisha na shughuli za kupiga vita madawa ya kulevya kilikuwa hakina nafuu yoyote. Utofauti mkubwa aliouona ni kuwa, akiwa chini ya watu hao hawatamuua bali watampeleka mahakamani kisha kifungo kitachukua mkondo wake. Zimwi aliendelea na maelezo yake

"Tulifatilia nyendo zako muda mrefu baada ya kugundua una ujamaa na wauzaji wa madawa ya kulevya, tukatega mitego yetu. Siku, wiki na miezi ikapita pasipo kukutia mtegoni, tulikuona ukiwa bize na kazi yako ya ulinzi katika tenda za wachina. Upelelezi uliendelea kimya kimya mpaka siku tuliyojihakikishua kuwa u miongoni mwa wasambazaji wa madawa ya kulevya"

Hofu ilizidi kupanda katika mwili wa David, mwili ukamtetemeka sana, akahisi kama yupo ndotoni lakini ubongo wake ukakataa. Ukamuhakikishia kuwa haoti ndoto yoyote. Akafikiria maneno aliyoambiwa kuwa alikuwa kwenye rada muda mrefu. Akamkumbuka rafiki yake aliyemshawishi kuingia kwenye biashara hiyo eti kwa lengo la kumsaidia kiuchumi, hapo ndipo akili yake ilipomuhakikishia kuwa atakuwa alionwa akiongozana au kuongea na mtu huyo ambaye ni tishio kwa matukio ya kihalifu ndani ya mipaka ya Tanzania. Mtu ambaye anatafutwa usiku na mchana ili adhibitiwe pasipo mafanikio. Picha ya mpenzi wake akiwa kwenye hali ya uchungu ikamjia David kisha akakumbuka kauli aliyoambiwa na Zimwi kuwa ndiye aliyemlipia gharama za huduma alizopatiwa hospitali. Swali likajengeka kichwani kwake

"Kwanini alilipa deni hilo?"

Alikosa majibu sahihi. Midomo iliendelea kumtetemeka kama mtu aliyekuwa sehemu yenye baridi kali huku akilini mwake akijihakikishia kuwa haoni njia yoyote ya kukwepa gereza. Kipindi David akiendelea kupambana na mawazo, akashitushwa na kauli ya Zimwi, kauli iliyosema

"Tazama picha ya mtu huyu kisha uniambie yupo wapi na njia sahihi ya kumpata?"

David aliipokea simu ya Zimwi huku mikono ikimtetemeka sana, akaitazama picha ile iliyokuwa kwenye simu. Hakika haikuwa sura ngeni hata kidogo, ilikuwa ni sura aliyoifahamu vizuri miaka mingi sasa, ilikuwa ni sura ya rafiki yake aliyemshawishi ajiunge kwenye biashara ya madawa ya kulevya. David aliinua kichwa chake akamtazama Zimwi aliyekuwa makini akisubiri majibu ya swali yake, midomo ya David iliendelea kutetemeka, sasa ilitetemeka zaidi ya awali. Hofu ilimjaa moyoni akashindwa kuchukua maamuzi yoyote akabaki kamtumbulia macho Zimwi huku kichwa chake kikitafakari jibu la kutoa.

Lakini kabda hajatoa jibu lolote, alishuhudia mtu mwingine akiingia ndani ya chumba hicho. Alimkazia macho vizuri ili kujihakikishia kama alikuwa akimfananisha au ndiye yule yule aliyemuona siku zilizopita. Akili yake ilimuhakikishia kuwa ni yule binti mrembo aliyemlipia pesa ya bajaji aliyokuwa akidaiwa na dereva yule mkorofi kisha akampatia shilingi elfu kumi nyingine ya nauli, binti mwenye asili ya kiarabu. Macho ya binti yule yalipokutana na macho ya David akaachia tabasamu angavu, sio kwamba binti yule alifurahi mpaka akaachia tabasamu, hapana, ilikuwa ni njia ya kumlaghai mateka wake

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom