Riwaya: Afisa usalama

Riwaya: Afisa usalama

SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: immaphiri

SEHEMU: 06

Msichana yule wa kiarabu aliyekuwa amepambwa kwa tabasamu maridhawa, tabasamu lililosababisha David kuona meno yake mazuri yaliyopangwa na kupangika mahala pake alikuwa amevaa mavazi yenye asili na tamaduni za Kihindi. Kichwani alikuwa amefunga mtandio mrefu uliofika mpaka mgongoni. Akiwa alikuwa ni binti mwenye asili ya kiarabu akiwa Uhindini. Macho ya David yaliendelea kumtazama mpaka alipofika mbele yake. Msichana yule akavuta kiti, akakaa jirani zaidi ya David aliyekuwa juu ya kitanda. Sasa walikuwa ana kwa ana kimtazamo lakini kiakili David alikuwa amesafiri mbali zaidi, hakika hakuwa mahala pale. Alishindwa kuelewa matukio yote yaliyomtokea, alifikiria kauli ya Zimwi kuwa ndiye aliyelipa gharama za matibabu ya mpenzi wake kisha akakumbuka alivyolipiwa pesa ya nauli na msichana aliye mbele yake.

Sasa aliamini alikuwa akifatiliwa muda mrefu kama alivyoambiwa na Zimwi, aliamini familia yake itakuwa bado ikiendelea kufatiliwa ili wafatiliaji wapate wanachokihitaji kwa haraka. Aliiona hatari. Mawazo na maswali vilipishana akilini mwake akashindwa ashike kipi na aache kipi. Hakika alivurugwa. Kipindi akiendelea kuandamwa na mawazo na maswali huku akimtazama mtoto wa Kiarabu aliyekuwa mbele yake ghafla akashitushwa na salamu

"Hujambo David Samson?"

Hakushangazwa na kitendo cha msichana yule kufahamu jina lake kamili kwa sababu walikwisha mfatilia muda mrefu. Japokuwa alishitushwa na salamu iliyomtowa mawazoni lakini hakuna alichosikia zaidi ya jina lake, alibaki kamtumbulia macho kama mtu anayeulizia

"Umesemaje?"

Msichana wa Kiarabu hakujali hali ya David, aligeuza kichwa chake akamtazama Zimwi aliyekuwa kimya baada ya binti huyo kuingia kisha akamwambia

"Unaweza kutupisha tafadhari"

Zimwi hakuwa na neno lolote, aliinuka alipokuwa amekaa kisha akatokomea pasipojulikana. Kitendo kile kilirudisha mawazo ya David mahala pale, sasa aliamini kuwa jambo linaenda kutokea baada ya kumshuhudia Zimwi akiondoka chumbani mule. Kwakuwa kichwa cha David kilikuwa mbali kimawazo hivyo basi hata kauli aliyoambiwa Zimwi hakuielewa, sio kwamba hakuisikia, hapana, aliisikia kama kelele tu masikio kwake. Akili yake ikajiuliza

"Anaelekea wapi?"

Lakini akili hiyo ilikosa jawabu kamili. Msichana wa kiarabu akafungua mdomo wake kwa mara nyingine kisha akaongea

"Umeanza lini kujihusisha na biashara ya kuuza na kusambaza madawa ya kulevya?"

Safari hiyo David alielewa alichouliza lakini jawabu la swali lilikuwa gumu kutoka, sio kwamba alikuwa hajui jawabu la swali hilo la hasha, bali aliamini huo sio wakati na mahala sahihi pa yeye kuongelea maswala hayo. Akili yake ilimwambia lazima akajieleze katika ofisi zao na sio mafichoni namna hiyo. Hakika alijifanya jeuri na kiburi mbele ya binti mzuri. Binti yule wa kiarabu akamuuliza David kwa mara ya pili, safari hiyo aliongeza sauti tofauti na awali

"Umeanza lini kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya?"

David aliyejawa na ujasiri wa ajabu, ujasiri mwenye dalili ya kukata tamaa ya maisha akamjibu binti yule wa Kiarabu

"Hapa sio mahala sahihi pa kujielezea, nifikisheni ofisini kwenu nitaongea kila kitu"

Binti wa Kiarabu akauona ujasiri wa David. Sasa aliona kama akichezewa mwili wake na mwanaume asiyempenda pasipo ridhaa yake. Hasira zikapanda kichwani. Urembo wa sura yake ukapotea ghafla baada ya kuruhusu makunyanzi ya hasira, dimpo zake zikawa ndita. Hakika hakuwa mrembo wa dakika kadhaa zilizopita. Hali ile ilimuogopesha sana David lakini alijikaza kiume ili aelewe ukweli kamili kuhusu watu wao. Bado akili yake ilikuwa na hofu ya kuwaamini kama ni watu wa kitengo cha siri kinachopambana na wauzaji wa madawa ya kulevya.

Msichana yule wa Kiarabu akasimama wima, akaanza kupiga hatua moja baada ya nyingine ndani ya chumba kile. Akili yake ilikuwa ikiwaza kitu cha kufanya, kitu kitakachokomoa jeuri ya David. Akili yake ikakosa cha kufanya, sasa hasira zikachukua nafasi, hasira zikapata kitu cha kufanya. Akatafuta jina katika simu yake, alipolipata akapiga. Aliyepigiwa alipopokea simu msichana yule wa kiarabu akampa maelekezo mazito

"Naona huyu mpuuzi analeta ubishi wa kujielezea, hatuna haja ya kumbembeleza. Nenda kamkamate mpenzi wake na mwanae uwalete hapa mara moja"

Kauli hiyo ilisikia vizuri katika masikio ya David, sasa aliamini familia yake ipo matatani kwa ajili yake. Alibabaika kama mtoto, akataka kuongea akasita. Akashuka kitandani haraka mpaka aliposimama msichana wa Kiarabu, akapiga magoti huku akisema kwa sauti ya kitetemeshi

"Samahani sana dada yangu, naomba msiiguse familia yangu. Nitaongea kila kitu mnachohitaji kujua kutoka kwangu"

Simu ya binti yule ilikuwa bado ipo hewani na sikioni kwake lakini aliisikia vizuri kauli ya David. Akimtazama David aliyekuwa amepiga magoti mbele yake kisha moyo wake ukatabasamu baada ya kuamini wanaelekea kushinda vita yao kama walivyopanga. Akabadilisha kauli yake, lakini bado haikuwa na nafuu kwa David bali iliendelea kumuumiza kama ile kauli ya awali, binti yule alimwambia aliyekuwa akiongea nae

"Amekubali kuwa ataongea kila kitu lakini kutokana na dharau, jeuri na usumbufu alionionesha yatupasa tumfunze adhabu. Waweza kumuacha mpenzi wake lakini mchukue mtoto wake uje nae hapa"

Baada ya kauli hiyo binti yule wa kiarabu akakata simu. Sura yake ya awali ikarudi mahala pake, urembo wake ukajihidhirisha kwa mara nyingine. David alimshika miguu huku akimbembeleza kuwa yupo tayari kwa lolote lakini wasiiguse familia yake. Hakika alikuwa ameshachelewa. Binti yule hakumtazama hata usoni bali sauti yake ilisikika katika masikio ya David

"Baada ya nusu saa nitaingia na mtoto wako ndani ya chumba hiki. Nafikiri ndiyo utaongea vizuri bila kubembelezwa"

Baada ya kauli hilo alijitoa kwenye mikono ya David kisha akatokomea nje kama Zimwi alivyofanya muda mfupi uliopita.

ITAENDELEA
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: mwandishi.phiri

SEHEMU: 07

Ukimya ulitawala katika chumba alichokuwa David, ukimya huo haukumaanisha chochote katika akili yake, kichwani alizisikia kelele, kelele zilizokinzana zenyewe kwa zenyewe, kelele zenye majuto ndani yake.Hakika kelele hizo zilistahili kuitwa mawazo mazito yaliyoelemea kichwa cha David. Muda wote macho ya David yalikuwa yakiutazama mlango wa chumba hicho akisubiri kuona ahadi aliyopewa, ahadi ambayo ni adhabu upande wake, ahadi ya kutekwa kwa mtoto wake. Mlango ulikuwa wazi kabisa, pasipo kufungwa. Akili yake ilimwambia ajaribu kufanya jaribio la kutoroka lakini akili hiyo hiyo ikamsisitiza kuwa watekaji hawakuwa wajinga kuacha mlango wazi namna ile. Aliamini ulikuwa ni mtego, mtego ungeoweza kumuongezea adhabu endapo akifanya jaribio la kutoroka alafu akakamatwa. Akaamua kutulia tuli.

Akatazama saa yake ya mkononi ikamuonesha nusu saa aliyoambiwa kuwa mtoto wake atakuwa mbele yake imeshapita muda mrefu, sasa ilikuwa imepita saa na dakika kadhaa. Hakujua nini kilichokuwa kikiendelea na nini hasa hatima ya familia yake. Kipindi akiendelea kupambana na mawazo mazito kichwani kwake alimuona binti wa Kiarabu akiingia chumbani humo akiwa na mtoto mchanga mikononi. Mtoto alikuwa akinyonya maziwa yaliyokuwa kwenye chupa lenye chuchu ya bandia. Macho yalimtoka pima David, sasa aliamini kuwa watu wale hawakutania kuhusu ahadi yao, akili ya David ikamfikiria mpenzi wake, Winnie, hakujuwa atakuwa kwenye hali gani baada ya kunyang'anywa mtoto wake mchanga aliyekuwa akihitaji huduma ya mama yake ya karibu. Alihisi kuchanganyikiwa.

Alitamani kuinuka lakini miguu ilikataa akataki akimtazama binti yule wa kiarabu huku midomo yake ikimtetemeka kwa hofu na uwoga. Tabasamu halikuisha kutawala katika sura ya mrembo aliyembeba mtoto wa David, alikuwa akipiga hatua huku akimpapasa mtoto yule kichwani. Mrembo yule alipofika kwenye kiti alichokuwa amekaa awali alikaa tena kisha pasipo salamu yoyote akamwambia David

"Nafikiri hujawahi kumshika mwanao, leo nimemleta ili uweze kumshika na yeye ahisi mikono ya baba yake"

Kauli hiyo ilimtoka binti wa kiarabu huku akimkabidhi David mtoto wake wa pekee. David alimpokea kwa mikono miwili malaika wake aliyepewa jina la marehemu mama yake. Alimtazama usoni, hakika aliiona sura ya marehemu mama yake. Hakupata muda wa kumtazama sana mwanae kwa sababu alishitushwa na swali

"Ulianza lini kujihusisha na kundi linalouza na kusambaza madawa ya kulevya?"

Macho ya David yaliyokuwa akimtazama mtoto wake alirudi kumtazama binti wa kiarabu aliyekuwa makini akisubiri jibu la swali lake. David hakuwa na pingamizi wala ubishi wowote, aliamini akifanya hivyo atakuwa amenunua majanga katika familia yake. Alimjibu mrembo wa kiarabu

"Siku niliyompeleka mpenzi wangu hospitali kwa ajili ya kujifungua ndio siku hiyo hiyo niliyoingia rasmi katika mtandao huo"

Binti wa kiarabu alionesha dalili ya kutoridhishwa na majibu ya David, aliamini kulikuwa na uongo ndani yake kwa sababu alikwisha muona David na mmoja wa wauza madawa ya kulevya mkubwa miaka kadhaa iliyopita, kitu kilichomaanisha walikuwa na uhusiano wa karibu tangu miaka mingi iliyopita. Binti yule akamkazia macho David kisha akamwambia

"Unataka kuniaminisha kuwa umemfahamu Aman Collence ndani ya kipindi hiki kifupi kilichopita?"

Sasa David alielewa nini maana ya swali aliloulizwa awali, alielewa binti wa kiarabu alitaka kusikia kauli gani. David akamjibu

"Aman Collence ni rafiki yangu wa muda mrefu, tulikutana mtaani tukazoeana miaka mingi iliyopita, japokuwa maisha yetu yapo tofauti sana kwenye suala la pesa na kipato"

Binti wa kiarabu akamchukua mtoto aliyekuwa mikononi mwa David kisha akaendelea kuuliza maswali ili kupata ufafanuzi zaidi

"Ilikuwaje mpaka mkawa marafiki?"

Lilikuwa ni swali gumu kwa David, alifikiria sababu iliyopelekea kuwa na urafiki na Aman Collence hakuiona kabisa kwa sababu kijana yule wa kitajiri aitwaye Aman Collence hakuwa na marafiki wengi kipindi walipoanza urafiki wao, alikuwa mkimya na mtu wa kujitenga sana.David alimtazama binti wa kiarabu kisha akamjibu

"Nilijikuta nipo ndani ya urafiki na Aman Collence, urafiki nilioshindwa kuelewa chanzo chake halisi. Nafikiri yeye ndiye aliyehitaji urafiki na mimi, yeye ndiye atakuwa na majibu sahihi"

Binti wa kiarabu alitabasamu, akamtazama mtoto wa David aliyekuwa mikononi mwake akiishambulia ile chuchu ya bandia, akarudisha macho kwa David kisha akamuuliza

"Unayapenda maisha ya mwanao? Kama jawabu ni ndiyo, basi hutakiwi kunificha chochote...sisi sio wahalifu wala wauaji, tunapambana na wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya. Sasa inapotokea adui anakuwa mbishi kutoa ushirikiano lazima tumuoneshe umuhimu wa ushirikiano wake, lazima atoe ushirikiano kwa njia yoyote ile tutakayohisi itatusaidia"

Binti yule wa kiarabu akaitazama saa iliyokuwa kwenye mkono wake wa kulia kisha akarudisha macho kumtazama David, akamuuliza

"Kama hufahamu sababu ya wewe kuwa na urafiki na Aman Collence inakuwaje unafanya naye kazi ya uuzaji wa madawa ya kulevya ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu?"

Lilikuwa ni swali lepesi kwa David lakini majibu yaliendelea kumfunga kwa binti yule wa kiarabu

"Maisha yangu ni magumu sana, ugumu wa maisha yangu na ushawishi wa Aman ulionihitaji nimsaidie kusambaza biashara ya madawa ya kulevya ya baba yake ndivyo vilivyosababisha nikaingia ndani ya mkondo huo. Mimi sio muhusika kabisa lakini Aman aliahidi kunisaidia kimaisha endapo nikimsaidia kazi yake, hakika alifanikiwa kunipata sawa sawa. Sikuwa na pingamizi kwa sababu nina uhitaji mkubwa wa fedha"

Majibu ya David yalizidi kutengeneza maswali katika kichwa cha binti wa kiarabu, binti yule akauliza haraka

"Unamaanisha humfahamu baba yake na Aman? Namaanisha mzee Collence"

David alikubali kwa kichwa akimaanisha hamfahamu kabisa baba yake na Aman, mzee aliyeaminika ndiye mkuu wa genge la madawa ya kulevya. David alifafanua kwa mdomo kuwa yeye yupo kwenye ngome ambayo inaongozwa na Aman, ngome ambayo Aman ndiyo sauti ya mwisho na hawajawahi kumuona mzee Collence katika ngome hiyo japokuwa Aman huwasisitiza kuwa mzee huyo asiyeonekana ndiye bosi wao. David alifafanua zaidi kuwa kwa muda mfupi aliokaa katika ngome hiyo ameona ugumu na uimara wake kwa sababu ina ulinzi mkali na endapo mtu msiye muhusika akigundulika eneo lile hupigwa risasi au kunyong'wa kinyama.

Maneno ya David yalimuingia vizuri binti wa kiarabu, hakika aliyaamini kwa asilimia kubwa kwa sababu walisha jaribu kuwatuma vijana wao kuingia ndani ya ngome hiyo kwa lengo la kuichunguza ili wapate taarifa kamili kabda hawajachukua maamuzi ya kuivamia lakini hawakurudi kamwe, hali iliyomaanisha waliuliwa kabda hawajakamilisha kazi iliyowapeleka. Hakika ngome ile ilikuwa ngumu kuingia kwa mtu asiyehusika.

Binti wa kiarabu akapata wazo, wazo aliloamini ni sahihi zaidi, akamtazama David usoni kisha akamwambia

"Unatakiwa kurudi ndani ya ngome ile, urudi kama mpelelezi wangu ili nifahamu kila kitu kabda sijapanga mashambuzi dhidi yao"

Ilikuwa ni kauli mbaya sasa katika masikio ya David, aliifikiria mara mbili mbili akaona hawezi kuifanya kazi hiyo kwa sababu kazi hiyo ilimaanisha kifo, ilimaanisha kuyaweka rehani maisha yake. Moyo wake ukasema hapana, lakini alipomtazama mtoto wake aliyekuwa kwenye mikono ya binti wa kiarabu alijikuta akipata jawabu lililokinzana na matakwa ya moyo wake. Aliamini akikataa kutimiza alichoambiwa anaweza kusababisha maafa ya familia yake, aliona bora yeye afe lakini sio mwanae na mpenzi wake Winnie.

ITAENDELEA
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: mwandishi.phiri

SEHEMU 08

Japokuwa giza lilikuwa totoro lakini halikumaanisha chochote katika akili ya David, alikuwa akitembea peke yake barabarani huku akiwa hana tofauti ya chizi, alikuwa akiongea peke yake, akijiuliza maswali na kujijibu mwenyewe. Akili yake ilikuwa ikiwaza namna atakavyofanikisha kazi aliyopewa na kuiwasilisha kwa binti wa kiarabu aliyempatia namba ya barua pepe yake baada ya kurudishiwa simu yake. Alifikiria kutokufanya kazi hiyo lakini aliamini akifanya hivyo atakuwa amemaanisha kifo cha mtoto wake na baadae kifo cha mpenzi wake na yeye pia. Alipoona hafiki aendapo akaamua kusimamisha pikipiki kisha akamwambia dereva

"Nipeleke Katubuka"

David aliamua aende kwa mpenzi wake kwanza kabda hajaianza rasmi kazi ya kifo, alitaka amuombe msamaha na kumuelezea kila kitu kisha kumuhakikishia kuwa lazima mtoto wao apatikane haraka iwezekanavyo. Pikipiki ilisimama nje ya nyumba aliyopanga David. Alimlipa dereva kisha dereva yule akatokomea barabarani kutafuta mteja mwingine. David alibaki akiitazama nyumba aliyopanga, alikuwa akipanga maneno ya kumuelezea mpenzi wake ili aeleweke. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha kuwa ilikuwa saa sita na robo usiku. Akijihakikishia kuwa mpenzi wake atakuwa amelala fofofo au kama atakuwa macho basi atakuwa kwenye dimbwi zito la mawazo juu ya mtoto wake. David aliingia mpaka uwani, palikuwa kimya kabisa, kila mpangaji alikuwa chumbani kwake akitafuta usingizi au akiwa amelala usingizi mzito. David aligonga dirisha la chumbani kwake huku akisema

"Winnie wangu, Winnie wangu nifungulie mlango"

Muda huo Winnie alikuwa macho huku kichwa chake kikiwaza hatima ya familia yake, macho yake mazuri yalikuwa yamevimba na mekundu kwa kilio alichopitia siku hiyo. Winnie alijihakikishia kuwa sauti aliyoisikia ikimuita ilikuwa ni sauti ya mpenzi wake, David. Akabaki akijiuliza

"Siku zote alikuwa wapi?"

Hasira zilimjaa akatamani asiitike wala asiinuke kwenda kufungua mlango lakini moyo ulikataa kabisa, moyo wa Winnie ulikuwa umehifadhi hisia za David, sasa kitendo cha kutomfungulia mlango kilimaanisha kupingana na hisia zake. Winnie aliyekuwa amevaa nguo maalumu za kulalia alijikokota toka kitandani pasipo kuitika kauli ya David, akafungua mlango kisha akarudi kitandani, hakusubiri David aingie, hicho hakukijali kabisa. David aliingia taratibu kisha akamtazama mpenzi wake aliyekuwa kwenye nyuso ya huzuni na hasira, moyo ukamuuma sana kujiona mkosaji mbele yake. David akaufunga mlango kisha akaanza kuvua nguo alizokuwa amevaa.

Wote walikuwa kimya sana. David alikuwa akiogopa kuanzia mazungumzo kwa sababu aliamini alikuwa na maswali mengi ya kujibu. Alipobakia ndani ya boksa, aliingia bafuni kuoga. Chumba chao kilikuwa na choo na bafu ndani. Alipotoka kuoga alimkuta mpenzi wake amekaa kitako tofauti na alivyomuacha, sasa aliamini umefika wakati wa maswali na majibu. Hakika alichokuwa akikiwaza kilikuwa tofauti na mpenzi wake. Bila hata salamu, Winnie alimwambia David

"Kesho naenda kwenu kumuelezea baba yako juu ya maisha yetu, nikitoka kwenu naenda nyumbani kukaa huko huko, yaani unabahati sana leo kunikuta hapa. Japokuwa nyumbani walinifukuza lakini nitaenda kuwabembeleza, nafikiri watanielewa vizuri. Siwezi kukaa na wewe pasipo mwanangu"

Kauli hiyo ilisikika vizuri katika masikio ya David, alitamani amwambie mpenzi wake ,hapana, lakini alijua atazua balaa lingine, bora akubaliane na hali. David alianza kumuomba msamaha mpenzi wake, alizunguka zunguka lakini mwisho wa siku ilimbidi amwambie ukweli wote, ukweli uliomuumiza sana Winnie. Hasira za Winnie zikageuka huzuni na huruma. Akamkumbatia mpenzi wake kisha akamuuliza

"Una uhakika gani kama waliomchukua mtoto wetu ni kitengo cha siri kinachopambana na wauza madawa ya kulevya?"

Swali hilo lilikuwa gumu sana kwa David kudhibitisha kwa sababu hata yeye alikuwa na mashaka juu ya wale watu. Awali Winnie alitamani kumwambia David asiendelee kujishughulisha kwenye makundi hayo ya kigaidi lakini uhai wa mtoto wake ulimsisitiza na kumlazimisha David kutafuta ufumbuzi. Winnie hakuchoka kumlaumu David kwa kujihusisha kwenye biashara ambayo alimkataza toka awali. David hakuchoka kuomba msamaha na kusisitiza kuwa hakuwa na namna nyingine ya kupata pesa kwa haraka zaidi ya kuingia kwenye uhalifu ule. Mwisho wa siku walikubaliana jambo la kuhakikisha usalama wa mtoto wao, walikubaliana lazima David arudi kwenye ngome ya kifo na afanye kila kitu alichoambiwa na kukiwasilisha kwa binti wa kiarabu. Winnie alimsisitiza David kuwa makini kwa sababu aliamini akigundulika hakuna adhabu nyingine atakayopewa zaidi ya kifo.

Walilala usingizi mzuri kama watu walioshinda vita. Ilipofika saa kumi na moja kasoro David alimuaga Winnie, waliagana kwa huzuni sana kwa sababu David alimuhakikishia mpenzi wake kuwa hatapata muda wa kwenda kumtembelea lakini alimuhakikishia kumpigia simu pindi apatapo nafasi. David alimsisitiza mpenzi wake asije kumpigia wala kumtumia SMS kwa sababu akifanya hivyo inaweza leta hali ya kutiliwa mashaka. David David alimwambia mpenzi wake kuwa aliambiwa lazima awe makini na kazi sio vitu vingine, familia itatumiwa pesa sio mambo ya kuongea ongea ovyo kwenye simu.Hakika waliohofia kudukuliwa kwa maongezi ya watu wao.

David alimkabidhi mpenzi wake kiasi kikubwa cha pesa alichopewa na binti wa kiarabu ili amuachie mpenzi wake atakachotumia kipindi ambacho atakuwa bize kutafuta taarifa na mambo mengine katika ngome ile ya kifo. Winnie alizishangaa pesa zile zilivyokuwa nyingi lakini David hakujali chochote. Alitoka ndani ya chumba chao na kuondoka zake. David aliamua kuondoka masaa hayo ili asije kuonwa na majirani zao
***********************

Yalikuwa yamepita masaa mawili tangu David apigishwe magoti na kijana aliyekuwa rafiki yake kipenzi, kijana aliyemshawishi kuingia katika biashara haramu ya madawa ya kulevya. Magoti hayo ilikuwa ni sehemu ya adhabu ya Kwanini alichelewa kurudisha taarifa ya mzigo aliotumwa kumpelekea kijana mwenye mwili wa miraba minne. Kichwani David alizidisha chuki dhiki ya Aman, kijana ambaye alikuwa rafiki yake wa muda mrefu. Hakuamini alivyokuwa akishurutishwa kama mtoto, alishindwa kubisha kwa sababu vijana zaidi ya nane mwenye miili iliyojengeka kwa mazoezi walikuwa ni sehemu ya ulinzi wa Aman. Aman alitembea kushoto mara kulia huku akiendelea kumuangalia David aliyekuwa akitetemeka kwa sababu magoti yake yalikuwa yameshatengeneza ganzi ya kutosha. Aman akamwambia David

"Tunapokuwa kazini hakuna habari ya urafiki, yakupasa kuchapa kazi kama ulivyoagizwa"

ITAENDELEA
 
Habari,

Leo nimepigiwa hesabu ya gharama ya uzalishaji wa Riwaya ya AFISA USALAMA. Hakika nikiuza kitabu kwa bei ya 10,000 nitakuwa sijafanya chochote. Nawaomba mni'support kwa bei ya 12,000. Kitabu ni kikubwa sana, kina page zaidi 330. Just imagine.

Nilifanya makosa kutangaza bei kabda ya kujua gharama za uzalishaji, siwezi kujilaumu bali ni ugeni katika tasnia hii ya uandishi.

Asante.
Kwanini usiuze soft copy km akina Patrick CK ?
 
SIMULIZI: UHAI WA MWANANGU
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890
INSTAGRAM: mwandishi.phiri

SEHEMU: 10

David alikosa majibu ya maswali yake, alibaki kamtolea macho Aman aliyekuwa mbele yake. Aman alielewa hali ya David akaamua kufafanua zaidi ili kumuweka David karibu na mawazo yake

"Kundi la wauza madawa ya kulevya tunalotaka kukuingiza kila siku linafanya mawasiliano na kundi letu mama lililo Afrika Kusini pasipo wao kujua kama kundi hilo na kundi hili ni kitu kimoja"

Aman aliendelea kuona mshangao wa David usoni kwake, mshangao uliomaanisha alikuwa haelewi chochote zaidi ya kusikia sauti inayoelezea. Amani alifafanua zaidi

"Baada ya kundi hilo lililo chini ya binti mwenye asili ya Uarabuni kufanikiwa kuchukua kila kitu toka mikononi kwetu, sisi tuliandaa mpango wa kulipiza kisasi na kuliteketeza kabisa kundi lake. Kuna mzee na vijana wangu waliopo Afrika Kusini ambao ndiyo huratibu biashara yetu toka huko mpaka hapa Tanzania. Vijana hao pamoja na mzee huyo waliweza kumuingiza mtegoni binti wa kiarabu akaanza kufanya nao biashara pia, ilikuwa rahisi kwa sababu binti wa kiarabu alikuwa akichukua mzigo wake toka nchi hiyo na jinsi mtego ulivyosukwa haikuwa rahisi kushituka".

David alikuwa makini sana kumsikiliza Aman, muda wote akiwa amepiga magoti. Aman aliona umuhimu wa David kuinuka, alimwambia ainuke kisha akae kwenye kiti cha plastiki kilichokuwa ndani ya eneo hilo. David akatimiza maagizo ya bosi wake. Aman akaendelea

"Japokuwa ilikuwa rahisi lakini haikuwa rahisi sana kumuaminisha binti wa kiarabu kukubali kufanya biashara na watu aliokuwa hawajui wala kuwafahamu awali. Hakika tuliandaa mpango wa kumuaminisha binti huyu jeuri. Tulifatilia nyendo za biashara zake tukagundua ratiba yake ya kuendea mzigo Afrika Kusini. Tuliandaa mpango wa watu wake watakaoenda kuchukua mzigo wa madawa ya kulevya Afrika Kusini wakamatwe na polisi. Tuliandaa polisi feki waliofanikiwa kuwakamata watu wa kundi lake wakiwa na mzigo wa madawa ya kulevya tayari kwa kuondoka kuelekea Tanzania.

Kitendo kile kilimaanisha jela tena ughaibuni, vijana wale walifadhaika sana. Walifungwa pingu kisha wakaingizwa kwenye gari la polisi feki tuliowaandaa lakini kabda gari lile halijaondoka mahala pale pa maficho ambapo hutumika kufanyia mambo ya kijangili na uuzaji wa madawa ya kulevya ghafla gari tatu zikiwa na mwendo kasi zilivamia eneo lile, zikafanikiwa kulizuia gari la polisi lililowateka vijana wa binti wa kiarabu. Walishuka vijana zaidi ya nane wakiwa na silaha za moto za kisasa. Polisi walishurutishwa kushuka ndani ya gari lile, polisi hawakuwa na jinsi walishuka kama walivyoamuriwa wakaambiwa wachague kufa au kutimua mbio. Hakuna polisi aliyejibu, muda huo walikuwa wakitimua mbio.

Vijana waliokamatwa na polisi awali wakawa mikononi mwa vijana walioenda kutoa msaada. Makundi yote mawili yalikuwa hayafahamiani kabisa kwa sura lakini vijana walioenda kutoa msaada walikuwa na taarifa za kutosha kuhusu vijana waliotoka nchini Tanzania. Mmoja wa vijana walioenda kutoa msaada akaongea

"Hakuna haja ya kujiuliza mara mbili, hamtufahamu hata kidogo lakini sisi tunafahamu kuwa ninyi ni Watanzania mnaojishughulisha na biashara ya madawa ya kulevya. Msihofu, hiyo ni biashara yetu pia"

Akapumzika kidogo akawatazama wenzake waliokuwa kimya huku wamevaa sura za kazi. Kijana yule akaendelea kutoa maelekezo kwa vijana waliookolewa toka mikononi mwa polisi

"Mpo kwenye mikono salama kabisa, wala msiwe na hofu yoyote. Nyie ni mwenzetu. Wote tuonafanya biashara za madawa ya kulevya tuna uaduni na polisi na Serikali kwa ujumla. Tuligundua polisi walifahamu nyendo zenu tukaamua kufatilia ili tutoe msaada endapo ukihitajika. Hakika tumefanikiwa kwa asilimia mia moja"

Japokuwa ufafanuzi uliendelea lakini vijana waliosaidiwa toka mikononi mwa polisi hawakuwaamini waliotoa msaada kwa sababu hawakupewa sababu za msingi za kusaidiwa na watu wasio wafahamu, vile vile hawakuachwa huru waondoke zao bali walichukuliwa wakapelekwa kwenye ngome ya waokoaji, ngome iliyo kama Casino kwa muonekano lakini ina siri nzito ndani yake. Ilikuwa ni ngome ya kitajiri yenye kila aina ya ufuska. Wacheza kamari, wasagaji, wanawake malaya wachezea fimbo pamoja na mambo mengine ya anasa yaliendelea kama kawaida.

Waliingizwa ndani ya Casino hiyo kisha wakaingizwa kwenye chumba cha siri, hata baadhi ya wafanyakazi wa Casino hiyo hawafahamu uwepo wa chumba hicho. Chumba hicho kinafahamika kwa watu wachache sana ndani ya kundi, watu ambao wanafahamu uwepo wa gwiji wa madawa ya kulevya ndani ya Casino hiyo. Chumba hicho kipo chini ya jengo la Casino, chumba cha chini. Mlango wa siri wa kuingilia chumbani humo unapatikana kwenye choo kimojawapo kati ya vyoo vya Casino hiyo. Sio rahisi mtu kufahamu uwepo wa mlango huo wa siri.

Chumbani humo walikutanishwa na mzee wenye umri zaidi ya miaka sabini, mzee alijitambulisha mbele yao kwa jina Masiya akimaanisha kuwa yeye ni mkombozi aliyeletwa duniani makusudi kuwatetea watu wanyonge na masikini. Aliwaeleza kuwa yeye ndiyo msambazaji nguli wa madawa ya kulevya barani Afrika. Hakika aliweza kujielezea kwa vijana wale. Mwisho wa siku, mzee Masiya aliwahakikishia ulinzi na usalama.

Siku iliyofuata aliwasafirisha kwa njia za panya zaidi ya njia walizokiwa wakizifahamu wakafanikiwa kufika Tanzania pasipo kipingamizi chochote. Hakika wakijihakikishia kuwa mzee yule ni nguli katika biashara ya madawa ya kulevya. Kilichowashangaza zaidi hawakuporwa mzigo wao wa madawa ya kulevya wala fedha nyingi walizokuwa nazo bali waliongezewa ulinzi na usalama wa safari yao.

Mzee yule alikuwa wa ajabu sana vichwani mwao. Walijiuliza

"Inakuwaje muuza madawa ya kulevya akuache uondoke na madawa pamoja na pesa nyingi kiasi hiki?"

Lakini walipoufikiria utajiri wa mzee yule waliamini aliamua kuwaachia tu kwa sababu alijiita mtetezi wa wanyonge na masikini. Taarifa za mzee yule walimfikishia bosi wao, binti wa kiarabu. Zilikuwa taarifa za kumshitusha lakini baada ya kuwasiliana na mzee Masiya kupitia mawasiliano aliyowapa vijana wake hofu ya binti wa kiarabu iliisha kabisa. Hapo ndipo urafiki wa kazi kati ya binti wa kiarabu na mzee Masiya ulipoanza, walifanya biashara ya kuaminiana sana, biashara isiyokuwa na mambo ya kiswahili. Mzee Masiya alimuhakikishia binti wa kiarabu kuwa anamjali kama mwanae wa kumzaa, hakika kauli hiyo aliidhibitisha kupitia uhusiano wao. Japokuwa wapo mbali na hawajawahi kuonana lakini wanawasiliana sana kama watu walio ndani ya mkoa mmoja. Binti wa kiarabu alifungiwa mzigo wake, ukapewa na ulinzi na kukwepa vipingamizi vyote kwa nguvu ya mzee Masiya.

Biashara ilileta hali ya uaminifu zaidi ya undugu, uaminifu huo ulijengwa na binti wa kiarabu dhidi ya mzee Masiya, akahitaji kufahamiana zaidi. Binti wa kiarabu alimuomba mzee Masiya waweze kuonana nchini Tanzania, aende maana amemuandalia zawadi anayohisi itamfaa lakini mzee yule alimsisitizia binti wa kiarabu kuwa umri wake ni mkubwa sana, hashauriwi kusafiri safiri ovyo maana akifanya hivyo anahatarisha afya yake. Lakini mzee Masiya akamwambia binti wa kiarabu kuwa atamtuma kijana wake aende kumpokelea zawadi hiyo.

Kauli hiyo ilikuwa nzuri katika masikio ya binti wa kiarabu lakini aliomba kitu kingine zaidi, binti yule alimwambia mzee Masiya

"Ningependa mwanao angebakia ndani ya kundi langu ili tukafanya biashara vizuri zaidi, uwepo wake kwangu utarahisisha mambo mengi ambayo yatakuhitaji wewe"

Kauli hiyo ilimaanisha kijana wa mzee Masiya aende nchini Tanzania kuchukua zawadi ya baba yake kisha arudi nchini Tanzania kujiunga na kundi la binti wa kiarabu ili wafanye kazi kwa ukaribu zaidi. Kauli hiyo ilikuwa tamu sana masikioni mwa mzee Masiya, aliona amepata mwaya wa kumuingiza kijana wetu katika himaya ya binti wa kiarabu. Mzee Masiya alinielezea kila kitu, akaniambia nimuingize kijana makini katika himaya ya binti wa kiarabu ili tuweze kumsambaratisha. Kijana huyo amepatikana, kijana huyo ni wewe David. Lazima uingie kwenye himaya ya binti wa kiarabu kama mtoto wa mzee Masiya. Hakika Nasra alikuwa hajui alikuwa akisukiwa mtego siku nyingi, mtego ulioandaliwa ili kumsambaratisha yeye na kundi lake. Sasa amenasa mtegoni"

Baada ya Aman kumaliza kutoa ufafanuzi, sasa David alilitambua jina la binti wa kiarabu kuwa ni Nasra lakini utambuzi wa jina hilo haukumsaidia chochote wakati huo, yeye aliufikiria mpango ulioandaliwa, mpango wa kumuingiza kwenye imaya ya Nasra kama mpelelezi kisha akafikiria kazi aliyopewa na Nasra, kazi aliyomuweka mtoto wake dhamana. David alibaki njia panda.

Upande wa pili Nasra alikuwa akimsubiria kwa hamu mtoto wa mzee Masiya, aliamini akimpata mtoto huyo utakuwa ni mwanzo mzuri wa safari yake ya matumaini. Akatabasamu baada ya kuona anaweza kuua ndege wawili kwa wakati mmoja.

ITAENDELEA
Screenshot_20210808-184548_Facebook.jpg
 
Back
Top Bottom