Hata hivyo, sioni kwamba kitendo cha Zitto Kabwe kutangaza kuutaka urais kama ni kosa kwa sababu CHADEMA haijaweka rasmi utaratibu wa kuukataa utamaduni huu. Kwa kuwa utamaduni huu haujakataliwa rasmi kimfumo, haiwezi ikawa kosa mtu moja moja kuchagua kuutumia. Ndio maana Mzee Mtei kawataja watu wengine kadhaa, akiwamo yeye, kwamba nao wanaoutaka urais lakini hawajatangaza nia bado kwa hoja eti muda wa kufanya hivyo bado, kama vile ndani ya CHADEMA kuna muda rasmi uliowekwa wa kutangaza nia ya kugombea.Ni wazi basi kwamba hata wale wanaompinga na kumzomea Zitto Kabwe kuutaka urais wanaonyesha unafsi. Hawafanyi vile kwa sababu wana misingi fulani wanayoiamini juu ya namna ya kupata uongozi, la hasha. Hawa wanafanya hivyo kwa sababu ya aina ya pili ya unafsi, ambayo ni fitina.
Hawa wanajaribu kuonyesha kwamba Zitto Kabwe kafanya kosa kubwa kutangaza kugombea urais, lakini hawasemi ni kosa gani na amevunja kanuni gani ndani ya chama. Wengine wameenda mbali zaidi na kumuona Zitto kama ni msaliti ambaye amenunuliwa ili kukidhoofisha CHADEMA.
Hii ni fitina na ni aina mbaya kabisa ya unafsi na tabia inayojitokeza vile vile katika uliberali uchwara. Nina wasiwasi kwamba watu wanaompinga Zitto kwamba nao labda wana watu wanaodhani wanafaa kuwa marais na wanajaribu kumchonganisha Zitto na jamii, ili hatimaye njia yao ya kuusaka urais iwe nyeupe huko mbele.
Katika mfumo wa kidemokrasia za kiliberali kutangaza kugombea urais hakupaswi kuleta mzozo wala vurugu katika chama. Wakati mwingine kitendo cha Zitto ni jibu kwa wapinzani wa CHADEMA aina ya Samuel Sitta wanaojaribu kujenga taswira ya hovyo kwamba ndani ya CHADEMA hakuna wenye uwezo wa urais zaidi ya Dk. Slaa aliyegombea kwa mafanikio mwaka 2010.
Kwa hiyo, wakati huu ambapo CHADEMA haina mwongozo elekezi juu ya namna ya kuutaka urais, kutangaza kuutaka urais mapema ndio demokrasia yenyewe . Kwa hiyo tunapaswa kuwatia moyo wanachama wengine wenye matamanio ya urais watangaze wakati wowote na mahala popote wanapojisikia, wakati tukiweka misingi murua ya namna ya kupata mgombea mwafaka kwa wakati husika kutoka kwenye kundi la hao wanaojitangaza au wengine.
Kwa hiyo, wosia wangu wa leo ni kwamba kutangaza kugombea urais mapema hakupaswi kuleta mzozo au vurugu katika chama cha kidemokrasia kama CHADEMA. Ndiyo kusema hakuna sababu ya kupachika watu majina ya kifitina wanaotangaza kuutaka urais sasa na baadaye.
Muhimu ni kuweka mfumo utakaohakikisha kwamba CHADEMA hakizidiwi na nguvu za mfumo wa uliberali uchwara ambao umetamalaki nchini, ili hatimaye chama ndicho kiamue nani anakuwa mgombea.