JanguKamaJangu
JF-Expert Member
- Feb 7, 2022
- 2,308
- 5,460
Akisoma hukumu ya kesi hiyo namba 53 ya Mwaka 2023, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Njombe Matilda Kayombo, amesema mshtakiwa amekutwa na hatia katika makosa sita, matatu yakiwa ni ubakaji na matatu yakiwa ni makosa ya ulawiti anayodaiwa kutenda Mei 16 hadi 23, 2023 katika Mtaa wa Kihesa Kilimani Mkoani Njombe.
Hakimu Matilda ameeleza kwa mahakama imemtia hatiani baada ya kusikiliza ushahidi uliotolewa na mashahidi saba, wakiwemo waathirika wa matukio, Taarifa ya uchunguzi wa Daktari, uongozi wa Serikali ya Mtaa pamoja na Jeshi la Polisi.
Juma Msemwa anadaiwa kutenda makosa hayo kwa nyakati tofauti, baada ya kuwahadaa Wanawake watatu na kisha kuwafungia katika nyumba aliyokuwa anaishi katika Mtaa wa Kihesa, kisha kuwalawiti na kuwabaka kwa zamu usiku na mchana, zoezi lililoenda sambamba na kuwaingiza magunzi ya mahindi na matango katika sehemu za siri.
Taarifa zilizosaidia kukamatwa kwake zinaelezwa na mahakama kuwa zilitolewa na mmoja kati ya wanawake aliokuwa amewateka, ambaye alifanikiwa kutoroka na kupiga yowe kwa majirani ambao walivamia nyumbani kwa Juma na kukuta Wanawake wengine wawili wakiwa ndani.
Aidha, vilevile kulikutwa mfuko ukiwa na dawa za kienyeji, huku mahakama ikieleza kuwa sehemu ya ushahidi uliotolewa ulibainisha mtuhumiwa baada ya kuhojiwa alikiri kwamba alifanya matukio hayo akiwa anatekeleza maagizo ya mganga aliyemtaka abake Wanawake na Watoto.
Waendesha mashtaka wakiongozwa na Magdalena Whelo na Elicy James waliiomba mahakama kutoa hukumu kali kwa mtuhumiwa ili iwe funzo kwa jamii yote ikizingatiwa kwamba matukio ya ubakaji na ulawiti yamekuwa yakiongezeka Mkoani Njombe.
Mahakama imeeleza baada kujiridhisha na ushahidi uliotolewa imemhukumu Juma Msemwa kutumikia miaka 30 jela kwa kila kosa, katika makosa yote sita yaliyomtia hatiani, ambayo ni kinyume na kifungu cha sheria namba 130 kifungu kidogo cha kwanza na cha pili (e) sambamba na kifungu kidogo cha kwanza cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Kifungu namba 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2022.
Hata hivyo pia adhabu hiyo ya kifungo imekwenda sambamba adhabu ya faini ambapo Juma Msemwa anatakiwa kulipa fidia ya fedha kiasi cha Shilingi Milioni moja, kwa kila muathirika wa makosa aliyoyafanya.