SEHEMU YA 51
Hebu fikiria, nimetembea na wanawake wote unaowajua wewe! Weupe, weusi, wanene, wafupi, wembamba, warefu, wenye wowowo, vipotabo lakini kote huko, sikupata kitu chochote zaidi ya kumaliza pesa zangu na kukaribia kupata magonjwa.
Walipoondoka, nikamuita Salama na kumshukuru kwa ukarimu wake kwangu na kwa wageni wangu, akaniambia huo ulikuwa wajibu wake na wala hakutakiwa kushukuriwa, yaani ni sawa na daktari kumponya mgonjwa halafu umshukuru, hapana, ule ni wajibu wake, wapo hapo kwa ajili ya kazi ya kuwaponya wagonjwa.
Sikuwa na nafuu, niliendelea kuumwa lakini Salama alikuwa bega kwa bega. Wakati nikiwa naumwa hivyo, wanawake wangu, yaani michepuko ikawa inanitumia meseji kwamba walikuwa wakitaka pesa, yaani hata kunijulia hali walishindwa, hivyo nikaachana nao.
Mimi: Mke wangu! Siwezi kulala peke yangu, naogopa nitakufa.
Salama: Unatakaje?
Mimi: Tulale wote.
Salama: Kweli?
Mimi: Ndiyo!
Salama: Hapana, nimepazoea sebuleni mume wangu, kunanifanya nijisikie amani, huru, naomba niendelee kulala sebuleni.
Mimi: Hapana! Hautakiwi kulala sebuleni tena, wewe ni mke wangu!
Nimekutesa kwa mwaka mzima, siwezi kukubali kukutesa tena, naomba tulale wote.
Salama: Ila kumbuka wewe ni mgonjwa.
Mimi: Najua ila naomba tulale wote.
Kweli usiku wa siku hiyo, kwa mara ya kwanza nikalala na Salama. Sikutaka kufanya kitu, si unajua nilikuwa mgonjwa hoi, nilikuwa mpole tu. Salama hakunifanyia utundu wowote, muda wote alikuwa kimya, hakulala, aliuchukua mto, akauweka nyuma, akauegemea na kisha kunilaza katika mapaja yake.
Hata nilipokuwa nikishtuka usiku wa manane, nilipomwangalia, alikuwa macho akiniangalia tu.
Mimi: Mbona hulali? Saa nane hii?
Salama: Nakulinda, sitaki kulala kwa kuwa unahitaji ulinzi wangu mume wangu! Nisipokulinda mimi, nani atakulinda? Naomba nifanye wajibu wangu!
Nilibaki nikimshangaa, alikuwa mwanamke wa ajabu kabisa. Kama alivyosema, kweli alimaanisha, hakulala, alibaki akinilinda usiku kucha, nilimuonea huruma, alipoamka, kama kawaida akawa ananipetipeti mpaka hali yangu ilipoanza kutengemaa.