Ni vita ya biashara ya Marekani dhidi ya China, au ya Marekani dhidi ya dunia?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG211390997455.jpg



Ni karibu miaka sita tangu Marekani izushe mgogoro wa kibiashara kati yake na China, na kuubazita mgogoro huo jina la vita ya biashara kati ya China na Marekani, wakati uhalisia wake ni vita ya biashara ya Marekani dhidi ya China iliyoanzishwa na aliyekuwa Rais wa Marekani Bw. Donald Trump, ambayo mrithi wake Bw. Joe Biden ameindeleza japo sio kwa kupaza sauti na kugonga vichwa vya habari kama alivyofanya mtangulizi wake.



Bila kujali Marekani imechagua kutumia jina gani kuuita mgogoro huu, na bila kujali kama vita hiyo inaendeshwa kwa sauti au kimyakimya, matokeo yake yanaendelea kuwa wazi. Aliyekuwa Rais wa Marekani Bw. Donald Trump alikuwa akiilenga China mara kwa mara kwenye majukwaa ya kisiasa, na kuchukua hatua mbalimbali za kikodi na zisizo za kikodi (tariff and non-tariff barriers) kuzuia bidhaa kutoka China kuingia kwenye soko la Marekani, na kujitapa kuwa huo ni ushindi. Lakini haikuchukua muda kabla ya wananchi wa Marekani kuanza kumgeuka na kumlaumu kwa kupandisha gharama za maisha kwa watu wa kawaida nchini Marekani.



Kelele za wanasiasa wa Marekani kuhusu biashara na China zimepungua, lakini vitendo vya uhasama wa kibiashara dhidi ya China bado vinaendelea.



Japo serikali ya Joe Biden sasa imekanusha kwamba inatekeleza sera ya decoupling, lakini halisi ni kwamba inajitahidi kudhoofisha mafungamano yake ya kibiashara na China, sera ambayo ni tamu masikioni mwa wanasiasa wa mrengo wa kulia, lakini ni chungu kwa wenye viwanda na wawekezaji wa magharibi waliowekeza nchini China, na ni mbaya kwa wateja sio tu wa Marekani, bali pia wa nchi nyingine za magharibi na hata dunia nzima.



Ukweli kwamba China ni kituo muhimu cha uzalishaji duniani haupinguiki, kwani China ina msingi imara wa sekta ya viwanda kutokana na nguvu kazi yake kubwa kuwa ni vijana wenye elimu na utaalamu, gharama nafuu za uzalishaji, mtandao mzuri wa usafishaji wenye ufanisi na gharama nafuu kufikisha bidhaa kwenye soko, na hata faida kubwa kwa mashirika na makampuni ya nchi za magharibi kutokana na uwezo mkubwa wa kifedha wa tabaka la kati la China. Mfano mzuri ulitolewa na jarida la The Diplomat la Machi 23 mwaka huu, unaonesha kuwa kampuni ya Apple inashindwa kutekeleza hiyo sera ya decoupling, kutokana na kuwa haiwezi kuhamishia shughuli zake kutoka China kwenda nchi nyingine, kutokana na kuwa bado hakuna nchi yenye mazingira yanayofanana na China yanayoweza kuivutia kampuni hiyo.



Ukweli ni kwamba China ina msingi mkubwa wa uchumi unaoweza kuhimili vizuizi mbalimbali vinavyowekwa na Marekani dhidi yake, kibaya zaidi ni kwamba kuna nchi nyingi duniani ambazo sekta zake za uzalishaji zinategemea minyororo ya ugavi iliyoungana na China. Kituo cha utafiti wa sera za uchumi cha Ulaya chenye makao yake mjini Paris, kilitoa takwimu zinazoonesha madhara ya vizuizi vya Marekani kwa nchi nyingine kilichoyaita “bystander effect” na kuzitaja Israel, Colombia, Misri na Ukraine kuwa nchi ziliothirika zaidi kutokana na vizuizi vya Marekani.



Kibaya zaidi ni kuwa wapambanapo mafahari wawili ziumiazo ni nyika. Ukweli ni kuwa vizuizi vya Marekani dhidi ya China haviitikisi China, na badala yake vinaiimarisha China. Pamoja na kuwa hatua hizi za Marekani ni sawa na kujipiga risasi mguuni, inawezekana wananchi wake wana uwezo wa kuvumilia machungu ya ongezeko la bei kwa baadhi ya bidhaa . Lakini ubaya wake ni kuwa kuna nchi nyingine nyingi duniani zinazoathiriwa na hatua zinazochukuliwa na Marekani, na matokeo yake ni kuwa watu wake wanaumia lakini hawana uwezo wa kupaza sauti au kuchukua hatua. Hali hii inaonaoyesha kuwa Marekani sio kama tu inajaribu kuilenga China, lakini kuilenga China matokeo yake ni madhara kwa nchi nyingi duniani
 
Back
Top Bottom