Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 2,984
- 12,307
Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limenunua rasmi eneo la Urafiki na majengo yaliyokuwa chini ya Kampuni ya Urafiki wa Tanzania na China (Tanzania - China Friendship Textile CO LTD) Jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Mawasiliano kwa Umma wa Shirika la Nyumba la Taifa, Muungano Saguya ameyasema hayo wakati wa ziara ya kukagua maeneo mbalimbali ambayo sasa yatakuwa chini ya miliki ya NHC na kufafanua kuwa eneo hili linajumuisha nyumba, maghala, viwanja vya wazi, viwanda na mali nyinginezo.
Katika ziara yake, Saguya alielezea furaha yake na matumaini makubwa kuhusu hatua hii, akibainisha kwamba itasaidia kuboresha miundombinu na kuinua uchumi wa maeneo hayo na kuboresha mandhari ya jiji.
Amesema kuwa NHC, imelinunua eneo hilo lenye ukubwa wa zaidi ya ekari 50 kutoka kwa mnada wa wazi kikiwa na thamani ya zaidi ya shilingi bilioni tatu.
Eneo la Urafiki lina historia ndefu ya kuwa kituo muhimu cha viwanda na makazi, kikitoa mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania. Hivi sasa, NHC inapanga kufanyia maboresho makubwa eneo hili kwa kujenga miundombinu bora, nyumba za kisasa, na maeneo ya biashara ambayo yatavutia wawekezaji na wakazi wapya.
Shirika la Nyumba la Taifa linaamini kuwa mradi huu mpya utakuwa na manufaa makubwa kwa taifa kwa ujumla, na kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya makazi na maendeleo ya kiuchumi nchini. Katika mpango wa maendeleo ya NHC, eneo la Urafiki litawekewa mkazo maalum kwa ajili ya kuhakikisha kuwa linakuwa mfano bora wa maendeleo ya kisasa na endelevu.
Wabia wakuu wa kiwanda hicho ni Msajili wa Hazina na kampuni Kampuni ya Urafiki wa Tanzania na China (Tanzania - China Friendship Textile CO LTD).