Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia, Dkt. Faustine Ndugulile amesema ukiangalia simu zinazopigwa kwenda nje au kuingia kutoka nje zimepungua...
Serikali inataka kuweka mfumo wa kutoza kodi simu za whatsapp zinazokwenda na kutoka nje ya nchi. Waziri Ndugulile amesema siku hizi watu wakitaka kuwasiliana na ndugu/jamaa zao nje ya nchi wanatumia whatsapp call badala ya simu za kawaida na hivyo kuikosesha serikali mapato.
Kwa mfano mtu akiunga bundle la internet la TZS 1,000/= anaweza kupigia ndugu zake wengi waliopo nje ya nchi na bado akabaki na bundle la kuperuzi mitandaoni. Lakini akitumia TZS 1,000/= kupiga simu za kawaida nje ya nchi hataweza kuwasiliana hata na mtu mmoja. Kwahiyo Ndugulile anaona dawa ni kuanza kutoza kodi simu za whatsapp.
My Take:
1. Kazi ya serikali ni kuboresha huduma kwa wananchi. Kwa hiyo wananchi wanapopata unafuu wa huduma serikali inatakiwa kufurahi. Serikali iliyosikitika kuona watu wanatumia gharama nafuu kuwasiliana na ndugu zao nje ya nchi ni serikali ya ajabu.
2. Serikali iache kuchuma mahali ambapo haijapanda. Whatsapp sio product ya serikali. Mark Zukerberg ameinvest teknolojia, ubunifu na fedha nyingi, lakini ameruhusu watu wapige simu bila kulipia kodi. Serikali ambayo haijakuwekea hata profile picture inataka kukutoza kodi. Upuuzi.
Ni kama serikali imeanza kuzoea kuchuma mahali ambapo haijapanda. Hata ukiagiza gari nje ya nchi unaweza kulipia $5,000 kwa Mjapani aliyetumia muda wake, nguvu na teknolojia kubuni gari hilo. Lakini likifika bongo serikali ambayo haijachangia hata tairi moja inakudai kodi 15M.
3. Serikali isijaribu kushindana na teknolojia. Hakuna aliyewahi kushindana na teknolojia akashinda. Serikali ikitaka watu walipie kodi simu za Whatsapp, watu watatumia application zingine kupigia simu ndugu zao, kama vile Viber, Talkhome, Yola, Dingtone, TalkU etc. Na bado kila siku zinabuniwa nyingine mpya. Serikali haiwezi kutoza kodi zote.
4. Serikali iache kutafuta vyanzo rahisi vya mapato vinavyomuumiza mwananchi. Mauritius inaingiza Trilioni 10 kupitia utalii wa fukwe peke yake, sisi tunaingiza Trilioni 1.7 kwa utalii wote kuanzia mbugani, mlima, hadi fukwe. Kwanini tusiwekeze zaidi kupata pato kubwa badala ya kuhangaika kutoza kodi simu za whatsapp?
Malisa GJ.