SEHEMU YA 24
Alistuka Atu na kujichekesha kabla hajakaa mkekani na kunisalimu.
"Jamani baby mbona ghafla hivyo?" alinena nami huku akiwa hajiamini amini pale chini nami sikutaka kumuonesha dalili zozote mbaya wala kustushwa na muonekano wake.
"Usijali baby nimekuja kukuona baada ya kusikia unaumwa lakini nashukuru kwa ninavyokuona tu upo poa eeh!"
"Mh! we acha tu baby niko poa jioni hii ndio nikawa nafanya maoezi ya kuzunguka mitaa ili kesho nianze safari ya kurudi kwetu nilikumiss sana mume wangu." Bila haya Atu alinena na muda ule simu yake iliwaka mwanga kuonesha ilikuwa inaita lakini haikutoa mlio zaidi ya kuvibrate. Aliitazama pasipo kuipokoea.
"Mbona hupokei baby?"
"Haah! achana nae Mery huyu wa chuo nikipokea ataanza maongezi malefu wakati sasa hivi niko nawe baby wangu." Alijibu Atuganile maneno ambayo nilihisi wazi kuwa ni uongo mtupu. Moyo uliniuma kwa kweli sio kidogo japo nilijitahidi kutabasamu na kuficha usoni.
"Hebu nione simu yako mamyto." nilijikuta uvumilivu ukinishinda na kutamani kuona ushahidi zaidi wa mke wangu kiasi gani amenichoka na kunisaliti mbali ya kutotaka kuwa nami tena.
"Jamani baby ya nini tena badala tuendelee na mazungumzo mume wangu."
"Sasa unaninyima mumeo simu ambayo nilikununulia mwenyewe?"
Nilimuuliza swali kwa sauti tofauti kidogo ambayo sikupenda itoke lakini iliniteleza kutokana na vuguvugu la joto hasira kuzidi kutafuna kifua changu.
"Haya basi isiwe ugomvi." Alinisogezea simu na kunyanyuka kuingia ndani akionesha wazi hakupenda hata kidogo. Sikujali zaidi ya kuanza kutazama 'inbox' ya ujumbe aliokuwa anatumiwa na upande wa ujumbe aliokuwa anatuma.
Asaaalaaaleeee! jamaniii! macho yalihakiki kile nilichokuwa nakisoma huku akili ikinukuu na moyo kusoma kimya kimya.
'Inbox' ya mke wangu zilijaa jumbe za mapenzi mapenzi tena kutoka kwa namba tofauti zengine zikiwa zimehifadhiwa kwa majina tofauti ya kuvutia. Miongoni mwa majina yaliyokuwa na jumbe nyingi yalikuwa MY MUME, MY LOVE SHEBBY, BABY T, MY JOHN, R BODABODA, na mengine ambayo hayakuseviwa majina zaidi ya namba tupu. Niliumizwa mno na jumbe nilizosoma huku nyengine zikionesha wazi kuwa mke wangu alikuwa akitembea nao kimwili kama huyo 'My Love Shebby' na 'My Mume' ambapo jumbe yake moja ilisomeka.
'Atu baby hakika wiki moja tu uliyonipa mapenzi umenifanya usiku wa jana kuuona mlefu sababu yako. Nakupenda sana sina budi kufanya hima nikuoe mpenzi ili nijifaidie raha zako kila siku.'
Niliumia sana hata kwa upande wake alivyokuwa ameujibu ujumbe huo akiahidi na kusisitiza.
'My love, wewe ndie kila kitu kwangu. Nakupenda sana natamani iwe kesho baby.'
Chozi lilinitoka ingawa sikuweza kulia. Muda huo wote mke wangu hajatoka tangia aingie ndani pindi aliponikabidhi simu yake iliyojaa uchafu.
Ujumbe mwengine waliokuwa wanatumiana ulikuwa wa aibu sana hata kuunukuu. Mke wangu alionesha kiasi gani kakubuhu kwenye mambo ya wanaume.
Sikuwa na hamu ya kuendelea kusoma jumbe zake zilizokuwa zinaninyima amani na kuniumiza moyo zaidi niliamua kuandika namba yangu kwenye simu yake kuona ameihifadhi kwa jina gani kama majina yote ya kimahaba yamehifadhiwa kwa namba nyengine?
Hapo ndipo nilipokutana na jina 'MJOMBA' likitokea kwenye kioo cha simu ya mke wangu pindi nilipoipiga namba yangu.
"Hapa sina mke." Moyo ulinambia na muda huo mama mkwe alikuwa asharejea pasipo kugundua na akawa amekaa mkekani akinitazama jinsi nilivyokuwa nimechoka machoni na kukosa nuru ya tumaini usoni.
"Baba! enhee vipi hali zako?" sauti ndiyo iliyonigutusha na kujieka sawa huku nikitoa kiitambaa na kuyakagua vizuri macho yangu yaliyokuwa yameshaanza kudondosha machozi mepesi mashavuni.
"Mama, hebu naomba tuambiane ukweli nini kinaendelea kuhusu mke wangu?" Uzalendo na uvumilivu vikanishinda. Swali nililomuuliza mama mkwe lilimfanya akae vizuri huku akiwa na nyuso ya mshangao.
"Kwanini baba umeuliza hivyo?"
"Hapana mama kuna nyendo siku baada ya siku ananionesha mwanao zinanisikitisha sana nahisi kama hakuwa tayari kuolewa nami."
"Mh! ina maana Atu ameshakuwa na tabia mbaya?"
"Mama, hebu tazama simu ya mwanao halafu kama mzazi hebu kaa upande wangu uyaone maumivu niliyo nayo." Kwa sauti ya mtetemo nilimpa simu mama Atu kusoma jumbe za mwanae alizokuwa anatumiana na hao wanaume zake awapendao.
"lool! tena afadhali babaake naye alikuja jana inabidi haya mambo tuyazungumze sasa."
Aliongea mama Atu na muda huohuo alimwambia yule mwanae mdogo aende akamwite baba yao mdogo yule aliyekuwa anaishi Iringa.
Alinyanyuka mama mkwe na simu mkononi kisha nae akaingia ndani alipokuwa mke wangu ambae aliganda kabisa huko pasipo kutoka. Sijui alikuwa anajifikiria nini au alikuwa anajipanga nini lakini hata mama mkwe naye alichelewa kutoka hadi waliposikia sauti ya baba akisalimiana nami pale nje mara baada ya kufika nao wakatoka huku Atuganile akiwa amebadilika kimavazi na kuvaa nguo za heshima.
"Enhe vipi baba maisha yenu salama?" alifungua maongezi baba mkwe baada ya kusalimiana na wote kukaa mkekani.
"Salama kiasi baba tunamshukuru Mungu."
"Mbona unanitisha ukiasi gani huo baba? tena ujio wako wa ghafla inaonesha kuna tatizo." Aliuliza baba mkwe na kabla sijamjibu mama mkwe alidakia na kuweka mambo wazi.
"Ni kweli baba Atuganile mtoto wetu ameshakuwa kikwazo kwa mumewe kwa maelezo ambayo hata mimi yamenishangaza sana nimjuavyo Atu tokea yungali tumboni na maadili yote tuliyompa lakini safari hii naona ameenda kutuaibisha na kututusi kwa mumewe. Hebu eleza baba kama ulivyonieleza."
Kauli ya mama mkwe ilinipa uhuru kiasi fulani lakini cha ajabu nilijikuta nikizungumza machache huku mengine hususani kuhusu jumbe za simu nikishindwa kumwambia baba zaidi ya matukio machache kama ya kupeleka bidhaa dukani, kuondoka pasipo kuaga na lile tukio la kutoroka. Sijui hata kwanini ulimi wangu ulikuwa mzito kuzungumza yale muhimu zaidi ya kunipa point.
"Sawa baba pole sana kwa namna moja. Enhee Atuganile mwanangu hebu nawe tueleze maisha yenu na kuhusu tabia zako alizozungumza mumeo."
swali liligeuka kwa Atuganile aliyekuwa ameinama muda wote huku akinitazama kwa macho makali pindi nilipokuwa nazungumza na kunibedulia midomo.
Alipopewa nafasi naye kweli aliitumia nafasi na kwa mara ya kwanza uso kwa macho niliweza kuyaona makucha ya Atuganile yule niliyekuwa namuona mpole, ana nidhamu, ana hekima, lakini kumbeeee daaaah! Atu alinimaliza mbele ya wazazi wake kwa maneno makali ya uongo uliokubuhu.
"Baba kiukweli tangia nimeolewa sikuwahi kuwa na maisha ya furaha hata siku moja zaidi ya siku ile ya harusi. Ilifika wakati nilijuta kwanini nimeolewa na pia nilijitahidi kuvumilia na kumtunzia siri mume wangu sikuwahi kuwaambia haya lakini sasa inabidi. Kwanza kabisa One mnamuona hapa tu baba lakini ni mlevi sana, kila siku alikuwa anarudi amelewa ndani hakuna amani matusi na kunipiga pasipo sababu za msingi. Pia simu yake muda wote anazungumza na wanawake nakutana meseji za wanawake zake na kipindi hiko mimi nimemsevu mume wangu yeye akawa amenisevu 'Shangazi' hapo ndipo nilipoumia zaidi na mimi nikamsevu 'Mjomba' kwenye simu yangu kama alikuwa hajui hata sasa hivi nikikuonesha nimefanya hivyo kwa hasira. Kuna mengine baba aliyokuwa ananilazimisha mume wangu kunifanyia naona hadi aibu kusema. Halafu anavyonihisi namsaliti ndipo ananiumiza zaidi baba muulizeni hata mwenyewe hadi ananioa amenikutaje? sikuwahi kuwa na mwanaume yoyote wala kujihusisha na mapenzi kama kweli nilikuwa na tabia mbaya mbona sikumsaliti kabla hajanioa halafu nije msaliti ndani ya ndoa kweli? Au yeye kunilazimisha kuniingilia kinyume nilipomkatalia ndio aliona sahihi? Eti simsikilizi?.."
"Baba? hapana wee Atuganile mke wangu muogope Mungu aaah!" nilijikuta uvumilivu ukinishinda na kuingilia kati.
"Sasa mbona mwenzio alinyamaza ulipokuwa unazungumza baba! muache mwenzako naye aseme amalize." Mama Atu alidakia kunikatisha huku baba Atu akitoa ishara ya mkono kumwambia Atuganile aendelee kusema.
"Mungu namuogopa sana ndio maana nasema ukweli. Kuhusu hata Chuo ilikuwa tabu kunipeleka hadi nikatoroka na ndipo alipokubali lakini hata ada ameshindwa kunilipia kumbe aliomba awe anatoa kidogo kidogo na kila nikienda chuo naulizwa na mwalimu na kujisikia aibu hata wengine wakinicheka. Nasoma kwa aibu pasipo uhuru na nikaambiwa kama chuo kikifunguliwa pasipo kumaliza ada basi nisiende. Mi nimechoshwa na tabia zake ingawa nilikuwa tayari kurudi kesho hata asingelikuja lakini maisha haya nimeyaweka moyoni yakiniumiza nikishindwa jua nifanyeje aaah!"
Aliongea huku akilia Atuganile. Moyo uliniuma kupita kiasi, machozi yakatabaruku uso wangu huku kamasi nyembamba nazo zikibisha hodi puani. Nilijuta kumfahamu Atuganile. Alinimaliza huku ananiangalia usoni pasipo kunihurumia hata kidogo. Alinionesha kiasi gani yeye jasiri kuliko hata muindaji aliyepania kumuua nyani muharibifu wa mazao. Nilitamani nami niseme yote sasa hata meseji zake za wanaume lakini wakati wangu ulishapita. Nilishachelewa na nikakosa pointi. Nilijutia hata kumfata pale. Kweli Mbwa koko anapokuwa kwao hupata nguvu ya kumbwekea hata Simba. Yaani leo hii Atuganile ananichinja hivihivi? Mimi yuleyule aliyeniita 'my everything?' Aaaaah! kosa langu lipi kubwa? wema wangu tangia akiwa bado shuleni? kumsomesha kabla hata kumuoa? upole wangu na hekima? upendo wangu wa dhati? ina maana kumpenda mtu kweli na kumuonesha ajue ni dhambi kwa watu? aaaah! Yako wapi mapenzi ya dhati? Niliyaona malipo ya wema wangu, thamani ya mke wangu, na ukarimu wangu vyote vikawa mizigo ya moto kwenye ndoa yangu. Hii ndio fadhila niliyooneshwa na mke wangu hata miezi sita ya ndoa bado. Yaani amesahau kwa muda mfupi hivi?
Baba mkwe alitikisa kichwa na kunitazama kabla hajazungumza.
Nafsi ilishakufa ganzi hata hamu ya kulala pale haikuwepo kabisa. Nilitamani nigeuze muda huohuo kwa gharama yoyote nirudi kwetu.
Lakini maneno aliyosema baba mkwe mdogo nayo mmmmh