Nchi zinazoishutumu China kwa kuweka mtego wa madeni. Je, zilishakaa na kujiuliza tatizo halisi linaanzia wapi?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG111255071090.jpg


Wachina wana wazo moja kwamba ukitaka kuendelea na kukuza uchumi wa nchi basi lazima kuwe na miundo mbinu mizuri na imara. Wazo hili ndilo lililopelekea China kuziacha nyuma nchi nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zinaonekana ziko sambamba na nchi hii katika umasikini. Kupitia ujenzi na uboreshaji wa miundo mbinu, sasa China imekuwa nchi ya pili kwa ukubwa wa uchumi duniani. Wazo hili ndilo lilimfanya rais Xi Jinping wa China aone ni vyema na nchi za Afrika pia zikuze uchumi wake kupitia kujenga kwanza miundo mbinu, ndio maana alianzisha pendekezo la “Ukanda Moja, Njia Moja” si tu kwa lengo la kuzisaidia nchi marafiki za Afrika bali pia kuhakikisha zinakwamuka kwenye umasikini.

Kupitia pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja” na Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) nchi nyingi za Afrika zilianza kunufaika na uwekezaji kwenye sekta mbalimbali. Mikopo inayotolewa kupitia majukwaa haya imeboresha miundo mbinu ya Afrika, imekuza uchumi wa nchi za Afrika kutoka 0.176 hadi 0.300%, imeongeza mapato ya usafirishaji bidhaa katika nchi za nje; imefungua njia ya uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni; imeongeza kiwango cha watoto kwenda shule; imeongeza upatikanaji wa maji safi na salama ya kunywa na bila kusahau pia imeongeza nafasi za ajira kwa wenyeji.

Hata hivyo kuna baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikifumbia macho matokeo na mafanikio haya kwa watu wa Afrika, na kuamua kuishutumu China kwamba wakati inapoingia makubaliano ya miradi na nchi za Afrika huwa haiko wazi na hii hatimaye hupelekea nchi za Afrika kuingia kwenye mitego ya madeni. Kama hayo hayatoshi, vyombo vingine hata hufikia kusema kwamba China kwa makusudi mazima sasa imeamua kupunguza kufanya uwekezaji wake.

Nafikiri kabla ya kuanza kumlaumu mtu kwa lolote lile kwanza kabisa ni lazima kuchunguza kwa makini na kujua tatizo ni nini, limesababishwa na nani au na nini, na tatizo liko wapi. Kwa hapa labda kwanza ningeangalia kwa upande wa wakopaji. Nchi za Afrika zinapoamua kuanzisha mradi, kabla ya kwenda kuomba mikopo kwa ajili ya uwekezaji, pamoja na mambo mengine pia zinapaswa kuangalia eneo la uwekezaji, wanufaika wa uwekezaji ambao ni wananchi, wenyeji wa eneo la uwekezaji na hata gharama ya uwekezaji.

Lakini kilichopo ni kwamba baadhi ya nchi huwa zinatumia fursa hii ya uwekezaji kufanya ufisadi na kusahau taratibu nyingine zote muhimu katika uwekezaji. Ufisadi unafanya deni liwe la gharama kubwa sana na pia liwe vigumu sana kulipa. Nasema hivi kwasababu pesa nyingi huwa hazifiki kwenye miradi husika, huwa zinapotea katikati. Utakuta gharama zinazowasiliswa kwa wakopeshaji zinakuwa kubwa na baadhi ya wakati huwa hata mara dufu ya gharama halisi za mradi. Tutole mfano mradi unaogharimu dola laki tano za kimarekani unapokwenda kuwasilishwa kwa wakopeshaji basi gharama zake zinakuwa dola milioni moja za Marekani. Swali ni kwamba hizi dola laki tano zimeyoyomea wapi, jibu lake bila shaka tayari kila mtu analifahamu.

Wahusika wakishatafuna fedha za ufisadi, kawaida mzigo unaiangukia serikali ambayo inaonekana ndio mkopaji na hatimaye serikali hii inashindwa kulipa au kufikia tarehe ya mwisho ya kulipa deni. Hili ni jambo ambalo linasikitisha sana na linapaswa kushughulikiwa haraka iwezekanavyo.

China kwa upande wake haiwezi kuingilia kati na kufundisha nchi namna ya kuendesha nchi. Tunafahamu kuwa linapokuja swala la ufisadi China inakuwa makini na inapambana vikali sana. Na pia inapenda kuona ufisadi sio tu kwamba haufanyiki ndani ya nchi bali hata nje ya nchi hasa nchi inazoshirikiana nazo. Kwa maana hiyo ili kupunguza mizigo ya madeni kwanza nchi husika zinatakiwa kuondoa ulafi na ubinafsi. Na zinapoanzisha miradi basi lazima pande zote mbili yaani mkopaji na mkopeshaji ziwe wakweli na wawazi.

Ufisadi ni tatizo moja tu lakini kuna hili jingine ambalo pia linaendelea kushamiri kwenye uwekezaji wa miradi. Hapa nazungumzia kuanzisha miradi kwenye maeneo yasiyofaa na kuitelekeza kwasababu ya kutotumiwa na wananchi. Mathalan nchini Senegal walikuwa na mradi wa kuchimba kisima, maafisa wa serikali walikwenda kwenye eneo la mradi na kuchunguza eneo hili bila hata kuwashirikisha wenyeji ambao wanalijua eneno lao kwa undani. Baada ya mradi kuzinduliwa maafisa walirudi mjini, halafu walipokuja tena kuangalia mradi unaendeleaje baada ya miaka minne, matokeo yake wakagundua kuwa maji yameshindwa kutumika kwasababu wanakijiji wanasema maji ya eneo hilo hayawezi kunywewa kwani mahali hapo wamezika mababu zao. Tukumbuke kwamba serikali imeshachukua fedha za mkopo kwa ajili ya kuendesha mradi lakini mwisho wa siku maji hayatumiki, na inalazimika kulipa.

Hii ni mifano michache tu kati ya mingi sana inayotokea katika nchi zanazokopa. Kwa hiyo kabla ya kulaumu upande mmoja tu kwa kuweka mtego wa madeni ni lazima kuchunguza na upande mwingine kwanini unashindwa kulipa madeni haya kwa wakati licha ya kwamba baadhi ya wakati wanongezewa muda.
 
Andiko nzuri, japo mifano yako yote haipo specific. Kila kitu umezungumzia kwa ujumla. Ilitakiwa uzame ata kwende mradi mmoja tu. Utuambie ni pesa kiasi gani au dhamani ya pesa kiasi gani ilikopwa na mtililiko wakwe wote wa upigaji huku ukizitaja namba halisi mpaka mwisho.

Tofauti na hapo kutakuwa hakuna tofauti na story za vijiwe vya kahawa.
 
Back
Top Bottom