Tukiwa bado tunatafakari mabadiliko ya mara kwa mara ya baraza la mawaziri wa serikali ya awamu ya tano, hali inaonekana sio shwali ndani ya chama hicho.
Nasema hali sio shwari, kwani kila mtu amekuwa na hofu kubwa, hasa wale wadadisi ndani ya chama. Inavyoonekana kwamba sasa hivi JPM ameamua kuwafunga midomo CCM na yeyote atakayeibuka kusema kitu ambacho ni tofauti na fikra za mwenyekiti wa chama na Musiba et al, basi akumbuke kwamba, nafasi yake ndani ya chama itakuwa ni finyu sana.
Serikali zote, tangu ile ya kwanza, zimekuwa zikiwaona vijana kuwa ndio hazina ya chama na wamekuwa wakisaidia kuongeza ushawishi kwa vijana wenzao ambao hawako karibu na chama. Hatua hii imesababisha kujenga chama kwa kutumia imani ya vijana ambao ni zaidi ya asilimia 70 ya wapiga kura wote Tanzania.
Ndio maana, leo utaowaona akina George Kahama, Malechela, Mkuchika, Lukuvi ambao miaka ya 80 walikuwa vijana wakiendelea kuhudumu serikalini toka serikali moja kwenda nyingine na wamekuwa wakiheshimiwa hadi hivi leo.
Leo hii kuwavuruga Nape, Mwigulu, Makamba nk, ambao ni miongoni mwa vijana wenye ushawishi CCM, sio kitu kizuri na kinaweza kuharibu afya ya chama.
Tangu serikali ya tano ianze kutawala, wazee wamekuwa hawana chao. Hawana ushawishi tena na kila wakijaribu kusema kitu, basi wanaambiwa wanawashwa washwa. Tumeona baadhi wakipewa onyo na mwenyekiti kuwa wakae kimya. Huu sio ustaarabu kabisa ndani ya chama kwani historia inawanyonya awamu ya tano.
Hivi majuzi, tumeona bwana anayejiita Musiba akiendelea kuwadharirisha wazee wa chama kwa kuwakashifu hali iliyosababisha wazee hao kutoka hadharani na tamko ambalo limesababisha mjadala mkubwa miongoni mwa watanzania.
Ikumbukwe kwamba, mwaka 2015 kwenye sakata la kura za maoni CCM, hakuna aliyejua kwamba JPM atapenya kwani mchuano ulikuwa mkali sana. Bila wazee wa CCM, basi JPM asingepenya hata nafasi tano..leo hii huenda Membe, Makamba, ama wale akina mama wa Zanzibar ana Lowasa, mmoja wao angekuwa rais.
Maisha ya watanzania yamebadilika sana tangu serikali ya awamu ya tano iingie madarakani. Njia kuu za uchumi zimeharibiwa na fedha zote zimeenda kwenye mikondo ya serikali, ambayo kwa mbwembwe zinaishia kununua ndege, madaraja nk, vitu ambavyo havijengi kabisa social capital. Tujifunze kwa Nigeria.. imeendelea sana lakini gap la maskini na tajiri ni kubwa sana hali inayosababisha wanigeria wengi kukosa imani na nchi yao na wengine kukimbia nchi.
Kuna ukabila sana serikali hii ya awamu ya tano. Ukiangalia safu za wakubwa, wengi wao wanatoka kanda ya ziwa, na wengi ni watu wa karibu sana na Rais ambao kwa namna moja ama nyingine wamekuwa ni dhaifu katika kushughulikia maslahi ya watanzania na wamebaki kuimba mapambio kwa JPM.. kusifia kusiko na mwisho.
Kwa sababu hizi nne, ninaona muelekeo wa CCM sasa huenda ukawa mbaya kwani CCM wanajulikana jinsi wanavyozika vichwa vyao ardhini na pale wanapokugeuka hutaamini kwamba ndio wao
Marijani Kyomo
Maruku, Kagera