Mzimu unaotabasamu

Mzimu unaotabasamu

MZIMU UNAOTABASAMU-24

Davis alikuwa jijini Kampala nchini Uganda akiendelea na masomo yake, moyo wake haukuwa na amani, tangu siku ambayo alijua kwamba pacha wake aliuawa msituni walipokuwa wamekwenda, hakupata raha hata kidogo.
Hakujua kitu gani kilimfanya baba yake kuchukua uamuzi wa kuwapeleka msituni kule, kila alipotaka kumuuliza moyo wake ulisita na hivyo kubaki kimya, ukimya ambao aliamini kwamba ungedumu milele ndani ya moyo wake.
Maisha jiji Kampala nchini Uganda yalikuwa mazuri, aliishi shuleni alipokuwa akisoma, akili yake akaiweka katika masomo na kuachana na mambo ya kufikiria mambo mengine. Shuleni hapo alipokuwa akisoma, alikuwa muongeaji sana, alijenga urafiki na watu wengi kiasi kwamba Waganda wakaamini kwamba hakukuwa na watu waliokuwa wakiongea sana kama Watanzania.
Siku zikakatika, baada ya miaka sita akamaliza masomo yake na hivyo kuamua kwenda kusoma katika Chuo Kikuu cha Nairobi na kuchukua masomo ya biashara.
Ucheshi wake uliendelea kuwa vilevile, akajijengea marafiki wengi huku wengine wakitamani kuona wanakuwa naye karibu kila siku. Darasani alikuwa na uwezo mkubwa, alitoka katika familia yenye pesa hivyo kila kitu alichokuwa akikihitaji alikipata kwa haraka sana.
Japokuwa Davis alikuwa mcheshi, aliyezungumza na kila mtu chuoni hapo lakini hakuwa mtu wa wanawake kabisa. Alipendwa, kila mwanamke alitamani sana kulala naye lakini hilo lilishindikana kabisa.
Wanaume wengi wakamkejeli, walimtania na kumpa jina la Papa kwa kitendo chake cha kutotaka kuwa na mwanamke yeyote yule. Jina hilo likampa umaarufu mkubwa, mbali na kujulikana ndani ya chuo hicho pia akaanza kujulikana mpaka nje ya chuo hicho.
“Eti chalii, kwa nini hupendi manzi ya Nairobee?” aliuliza jamaa mmoja kwa lafudhi ya Kikenya.
“Sijaamua kuwa na mwanamke Oliatuu. Nikiamua, hata dada yako Arafa muweke mbali,” alisema Davis na kuanza kucheka.
Japokuwa kulikuwa na wanawake wengi waliokuwa wakimpenda, lakini msichana aliyekuwa amekufa na kuoza kwa Davis alikuwa Evelina. Huyu alikuwa msichana mrembo wa kimasai aliyekuwa akiishi Mombasa hapohapo nchini Kenya.
Alikuwa msichana mrembo, mwenye macho makubwa na vishimo katika mashavu yake. Umbo lake lilikuwa machachari, alipenda kusuka kichwani, miguu yake ilikuwa minene na kila alipotembea aliringa kama twiga.
Wanaume wengi walimpenda Eveline, wengi walimfuata na kumtongoza lakini hakukuwa na mtu aliyefanikiwa kulionja penzi lake. Alifuatwa na wanaume wengi lakini moyo wake ulikuwa kwa Davis tu.
Mwanaume huyo alimpagawisha, alimpenda kupita kawaida. Kila alipokuwa akimuona, moyo wake ulikufa na kuoza, hakuajiamini, kwake, mtu aliyekuwa ameuteka moyo wake alikuwa mwanaume huyo tu na hakutaka kusikia jambo lolote lile zaidi ya kuona akiuteka moyo wa mwanaume huyo na kuwa naye.
Aliogopa kumwambia, alijisikia aibu kubwa. Kwa sababu Davis alikuwa mchangamfu sana, kila alipokuwa, alihakikisha na yeye anakuwa mahali hapo na kuanza kumsikiliza kila neno alilokuwa akiliongea.
Alivumilia kwa siku nyingi lakini mwisho wa siku akaamua kumwambia ukweli. Hakutaka kuogopa tena, hakutaka kuona akiendelea kuumia moyoni mwake, alichokiamua ni kumfuata na kumwambia kuhusu hisiia zake, jinsi mapenzi yalivyokuwa yakimtesa usiku na mchana.
“Unanipenda mimi?” aliuliza Davis, kwa kuwa alikuwa mtu wa utani sana, hata uulizaji wake ulikuwa wa masihara sana.
“Ndiyo!”
“Jamaniiii! Kwa hiyo nakutesa sana!”
“Ndiyo! Nahitaji uwe mpenzi wangu, ninakupenda mno David,” alisema Eveline huku akimwangalia David.
Hilo lilikuwa gumu kwake, aliyaogopa mapenzi, hakutaka kabisa kuona akiyapa nafasi mapenzi hayo, alitaka kubaki hivyohivyo, hakutaka msichana yeyote aingie ndani ya moyo wake kwa kuwa tu aliogopa kuumizwa.
Hakukubaliana na Eveline, mpaka chuo kinafungwa na kurudi jijini Dar huku msichana huyo akirudi Mombasa wakawa hawajakubaliana kuwa wapenzi.
Jijini Dar es Salaam waliendelea kuwasiliana, walizungumza sana kwenye simu, msichana huyo aliendelea kumsisitiza Davis awe naye lakini mwanaume huyo hakutaka kabisa kukubaliana naye, alimwambia kuhusu msimamo wake kwamba muda wa kuwa na mwanamke haukuwa umefika, kama kweli alimpenda alitakiwa kusubiri.
“Utatakiwa kusubiri,” alisema Davis.
“Mpaka lini?”
“Hapo nitakapoamua. Vuta subira Eveline,” alisema Davis, na maneno hayohayo ndiyo aliyokuwa akimwambia kila siku.
“Sawa. Haina shida! Nitakusubiri.”
***
David alikuwa ndani ya daladala iliyoanza kuondoka kuelekea Bagamoyo, alikaa dirishani, aliiwaona wanaume waliokuwa wakizungumza kwa mbali huku wakimwangalia yeye.
Moyo wake ukaogopa na kuhisi kwamba ile karatasi waliokuwa wameishika watu wale ilikuwa na picha yake. Alichokifanya, akainama, kuivua sura yake ya bandia halikuwa jambo gumu, ilikuwa imepachikwa tu. Kitendo cha kuinama huku akiwa ameuegemea mkono wake katika kiti cha mbele, akaanza kuivua pasipo mtu yeyote kugundua. Alipoona imetoka, akaitupa chini ya kiti cha gari na kutulia.
Ndani ya dakika moja tu, wanaume wale wakasimamisha daladala ile kwa lengo la kuingia ndani. Walimwambia dereva kwamba walimuona mwanaume yule aliyekuwa akitafutwa akiwa ndani ya gari lile.
“Jamani! Yaani nyie mmuone halafu abiria wote humu ndani wasimuone! Kweli?” aliuliza dereva lakini kwa kuwa vijana hao waling’ang’ania kuingia ndani ya gari, akawaruhusu.
Wakaingia, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuangalia katika kiti alichokalia David, ni kweli walimuona mwanaume yule akiwa katika kiti kile lakini walipoangalia tena, kulionekana kuwa mtu mwingine kabisa.
“Yupo wapi?’ aliuliza mwanaume mmoja.
“Alikuwa hapa. Eeh! Mbona kuna mwingine?” aliuliza jamaa mwingine.
Walichanganyikiwa, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea. Mwanaume aliyekuwa amekaa katika kiti kile alikuwa mwingine kabisa lakini nguo zake zilikuwa zilezile. Hawakujua kama wao walichanganya au la. Ilikuwaje aonekane mtuhumiwa lakini baada ya dakika kadhaa kuonekana mwanaume mwingine.
“Oya braza! Jamaa aliyekuwa hapo yupo wapi?” aliuliza jamaa mmoja huku akimwangalia David.
“Hakukuwa na mwingine zaidi yangu!”
“Hapana! Kulikuwa na huyu mwanaume!” alisema huku akimuonyeshea picha.
“Hapana! Nimekaa mimi tangu mwanzo,” alisema David.
Hawakutaka kuridhika, waliendelea kumwangalia kila abiria aliyekuwa ndani ya daladala hiyo lakini hawakufanikiwa kumuona mtu waliyekuwa wakimtafuta. Wakateremka na kuondoka huku wakiwa hawajui ni kitu gani kilikuwa kimetokea kwani mwanaume aliyekuwa katika picha ile walimuona akiwa ndani ya gari lile, ghafla baada ya kuingia, hakuonekana tena.
Kidogo David akashusha pumzi, akatulia na kujipa uhakika kwamba ilikuwa ni lazima kufika nchini Kenya kwa kuwa tu sura aliyokuwanayo ilikuwa nyingine kabisa, sura aliyozaliwa nayo ambayo hakukuwa na mtuu aliyekuwa akiifahamu.
Walichukua saa moja wakaingia Bagamoyo, hakutaka kupoteza muda, akawatafuta wavuvi na kuwaulizia kama kulikuwa na ngalawa yoyote ya kuelekea Mombasa.
“Siku hizi hakuna ngalawa kaka! Watu wanasafiri kwa jahazi!” alisema jamaa mmoja.
“Sawa. Mimi nataka kufika Mombasa, inakuwaje sasa?” aliuliza David.
Hilo halikuwa tatizo, alichokifanya mwanaume huyo ni kumwambia kuhusu jahazi ambalo lilitaka kusafiri kuelekea Mombasa kwa siri huku likiwa na watu waliokuwa na biashara zao za magendo.
Akatakiwa kulipa kiasi cha shilingi laki moja, hilo halikuwa tatizo, akalipia ana usiku wa siku hiyo akaunganishwa na watu wa jahazi na kuanza safari ya kuelekea Mombasa.
Bahari ilikuwa imetulia, hawakupata shida, walitumia saa kumi na nne mpaka kufika Mombasa huku wakiwa wamepitia Tanga. David akateremka na kuanza kuelekea katika hoteli ya Lion Kingi iliyokuwa hapohapo Mombasa pembezoni mwa bahari.
Akachukua chumba humo. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuwasiliana na mzee Armando na kumpa taarifa kwamba alikamilisha kazi aliyokuwa amepewa, alimuua Msuya pasipo kugundulika.
“Unasemaje?” alisikika mzee huyo huku akionekana kutokuamini.
“Nimekamilisha kazi yako mzee. Hakuna mtu atakayegundua. Ingia katika mitandao ya Kitanzania uangalie, utakutana na taarifa hiyo,” alisema David kwa sauti ya kujiamini.
Upande wa pili mzee huyo akafanya kama alivyoambiwa, alichokutana nacho humo kilikuwa kilekile, kulikuwa na habari iliyoripotiwa sana na vyombo vya habari kwamba bilionea huyo alikutwa amekuffa ufukweni.
Moyo wa Armando ukaridhika, akajikuta akitoa tabasamu pana na kuanza kurukaruka chumbani kwake. Mtu ambaye alimuhangaikia sana kwa kipindi kirefu amuue na kushindwa leo hii aliuawa na kijana aliyeamini kwamba angemsaidia huko mbele. Kwake, akamuona David kufaa kufanya kazi.
Katika daftari lake alikuwa na watu wengi waliotakiwa kuuawa kwa kuwa tu aligombana nao. Ukiachana na Msuya, kulikuwa na mtu mwingine aliyetaka sana auawe, huyo aliitwa Fabian Petrescu, mwanaume aliyekuwa raia wa Romania aliyekuwa akiishi nchini Ufaransa.
“Huyu ndiye anayefuata. Nitahakikisha nawamaliza wabaya wangu wote kupitia huyu David, naamini atafanikisha mipango yangu yote ya mauaji,” alisema mzee Armando.
Wakati akiwaza hayo bado David alikuwa hotelini, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, bado picha aliyokuwa msituni na baba yake ilikuwa ikizunguka kichwanai mwake, moyo wake ulimuuma, hakuacha kuwa na hasira dhidi ya baba yake huyo. Hakutaka kumuua, kila siku alipanga kumfanyia kitu kimoja ambacho kingemfanya kujutia kile alichokuwa amemfanyia.
Ilipofika majira ya saa kumi na mbili jioni, David akatoka kwa lengo la kutembea hapo Mombasa, alitaka kuzunguka mji huo baadhi ya sehemu kwa kuwa alijua kuwa alikuwa salama kabisa. Hakutaka kuchukua teksi, aliamua kutembea kwa miguu ili auone mji huo vizuri kabla ya kwenda Nairobi ambapo angechukua ndege na kuelekea Ujerumani.
“Davie...Davie...Davie...” alisikia akiitwa kwa nyuma.
Akashtuka, hakuamini kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akimfahamu. Akageuka, macho yake yakatua kwa msichana aliyekuwa akija kwa kasi huku akiwa na tabasamu pana, alipomfikia, akamkumbatia kwa furaha.
“Why didn’t you tell me that you are coming?” (kwa nini hukuniambia kwamba unakuja?) aliuliza msichana huyo huku akiwa amemkumbatia. David alibaki akishangaa, msichana huyo alikuwa mgeni kabisa, hakumfahamu, sasa ilikuwaje amfuate na kumkumbatia kiasi kile kana kwamba alikuwa akimfahamu.
Hakutaka kumwambia kwamba alimfananisha, ili kwenda naye sawa naye akajifanya kumchangamkia na kumkumbatia, alichokitaka ni kujuua mwanamke huyo alimfananisha na nani.
“Why?” (kwa nini?)
“I am sorry! I was very busy!” (samahani! Nilikuwa bize sana) alisema David.
Msichana huyo akamwangalia David kwa macho yaliyoonyesha mapenzi yote aliyokuwa nayo, akamshika mkono na kumwambia waende sehemu fulani kwani kulikuwa na kitu alitaka kumuonyesha. David akakubali, akaanza kwenda naye huku huku kichwa chake kikiwa na mawazo lukuki kwamba msichana huyo alikuwa nani.
Akampeleka mpaka katika hoteli moja iliyoitwa Giraffe na kumwambia kwamba hiyo hoteli ilikuwa ya baba yake. David akafurahi tu lakini bado kichwa chake kilikuwa na maswali lukuki juu ya msichana huyo, alikuwa nani na alijuaje vipi kama aliitwa David?
 
MZIMU UNAOTABASAMU-25

Bado kichwa cha David kiliendelea kuwa na maswali mengi, hakumfahamu msichana yule, hakuwahi kumuona katika maisha yake, alijaribu kukumbuka kama alikwishawahi kuonana naye nchini Nigeria alipokuwa akisoma lakini hakukumbuka kama alikwishawahi kumuona msichana huyo.
Moyo wake ukawa na shauku kubwa ya kutaka kufahamu kuhusu msichana huyo na huyo mtu ambaye alikuwa amemfananisha. Muda wote aliokuwa akiongea, aliongea kwa furaha na kumchangamkia kana kwamba aliwahi kukutana naye kabla ya hapo.
Akaingizwa katika Hoteli ya Girrafe ambayo ilikuwa kubwa hapo Mombasa na kuanza kumtambulisha kwa baadhi ya wafanyakazi kwamba yule mtu aliyekuwa akiwaambia mara kwa mara alipokuwa chuoni ndiye huyo hapo.
“Kila siku nilikuwa nawaambia kuhusu wewe, wakatamani sana kukuona, ila leo, umekuja Mombasa, Mungu mkubwa,” alisema msichana huyo huku akionekana kuchangamka mno.
“Kwa hiyo walikuwa hawaamini kama wewe mpenzi wangu?” aliuliza David huku naye akionyesha ushirikiano wa kuonyesha tabasamu.
“Hawakuamini!”
“Nahisi sasa wameamini!” alisema David.
Msichana huyo hakutaka kuishia hapo, akamchukua David na kwenda naye nyumbani kwao, alikuwa na furaha tele, kitendo cha kumuona mwanaume huyo kilimchanganya na kuona kwamba huo ndiyo ulikuwa muda wa kumtambulisha kwa wazazi wake.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika katika Mtaa wa Kilindini hapo Mombasa. Gari likaegeshwa nje ya jumba moja kubwa na la kifahari. David alikuwa akishangaa, hakuamini kama msichana aliyekuwa amemfananisha na mtu ambaye hakumfahamu alitoka kwenye familia iliyokuwa na pesa nyingi kiasi hicho.
Wakaingia ndani ambapo wakawaona wazazi wa msichana huyo wakiwa kwenye kochi wametulia. Wakawasalimia na baada ya utambulisho, akaanza kuwaambia wazazi wake kwa undani kwamba huyo ndiye mpenzi wake aliyekuwa akisoma naye nchini Kenya.
“Ooh! Ndiye yule Davis uliyekuwa ukituambia Eveline?”
“Ndiyo! Davis Gideon Matimya,” alijibu Eveline.
Kitendo cha kusikia jina la Davis tu moyo wa David ukamlipuka, alimfahamu mtu huyo, alikuwa ndugu wake wa damu ambaye alipelekwa naye msituni na baba yao kwa lengo la kuuawa. Hakuamini kama ndugu yake huyo alikuwa hai, kumbukumbu za kila kitu kilichokuwa kimetokea kule msituni kikaanza kurudi tena kichwani mwake hali iliyomfanya kuwa na maumivu makali.
Alizungumza kwa uchangamfu mkubwa, walipomaliza, akaaga na kuondoka. Eveline hakutaka kumuacha, akaondoka naye mpaka hotelini. Muda wote huo Eveline alihisi kwamba mwanaume huyo aliyekuwa akizungumza naye alikuwa Davis, alimwambia mambo mengi ya chuoni na ili kumfanya msichana huyo aamini kwamba alikuwa yeye, alikuwa akimsapoti kwa kila kitu alichokuwa akikizungumza.
Kitu kilichokuwa moyoni mwa Eveline ni kufanya mapenzi na David tu. Moyo wake ulimpenda, alimwambia hivyo tangu wakiwa chuoni, kwake, alikuwa tayari kwa kila kitu. Wanaume walimpenda sana lakini wote hao kwake hawakupata nafasi, mtu aliyekuwa akimpenda kwa moyo wa dhati alikuwa huyo aliyekuwa mbele yake.
Hakujua kama huyo hakuwa yule aliyekuwa akimfahamu, kila alipomwangalia, aliamini kwamba alikuwa mwenyewe kabisa na hata wakati mwingine alipokuwa akimshika, hakukuwa na utofauti, mwanaume huyo alifanana mno na ndugu yake ambaye kipindi hicho alikuwa jijini Dar es Salaam.
“Ninakupenda sana Davis! Nilikwambia hilo tangu chuoni, siwezi kukuficha, upendo wangu kwako hauna mipaka,” alisema msichana huyo kwa sauti nyororo kabisa chumbani.
Hapohapo akaanza kuvua nguo zake, alianza na brauzi, akavua suruali yake ya jinzi na kubaki na nguo ya ndani, akaanza kumsogelea David pale kitandani na kutaka kulala juu yake.
“Unafanya nini?’ aliuliza David huku akionekana kushtuka.
“Ninakuhitaji. Ninakuhitaji Davis,” alisema msichana huyo kwa sauti nyororo kabisa, tena ile ya kumtoa nyoka pangoni.
“Hapana Eveline! Siwezi kufanya mapenzi na wewe!”
“Kwa nini? Hunipendi?”
“Si kwamba sikupendi.”
“Ila?”
David hakujibu kitu, akanyamaza na kumwangalia msichana huyo machoni. Ni kweli alikuwa mrembo, alipendeza na alivutia hasa lakini hakuona kama hilo lingemfanya kukubaliana naye na kufanya naye mapenzi.
Aliamini kwamba alikuwa mpenzi wa ndugu yake, hakujua watu hao walikubaliana vipi, hakujua ni kitu gani kingetokea kama tu angediriki kufanya naye mapenzi. Alimkatalia pasipo kumwambia sababu, Eveline hakutaka kukubali, usiku wa siku hiyo aling’ang’aniza sana wafanye mapenzi lakini msimamo wa David ulikuwa palepale kwamba hakutaka kufanya kitendo hicho.
Hilo likamuumiza mno msichana huyo, akakasirika na kuondoka kurudi nyumbani huku akiwa na kinyongo moyoni. Hakukuwa na siku ambayo aliumia kama siku hiyo, njia nzima alikuwa akilia mpaka alipofika nyumbani, hakutaka kusikia kuhusu mwanaume huyo, aliumia mno moyoni mwake kiasi kwamba hakuona kama kungekuwa na sababu nyingine ambayo ingempelekea kutamani kuwa na mwanaume huyo.
Wakati akiwa chumbani kwake humo, majira ya saa 5:30 usiku akasikia simu yake ikianza kuita. Huku akionekana kuwa na uchovu, akaichukua na kuangalia kioo. Alishangaa kuona mpigaji akiwa ni Davis, kilichomchanganya zaidi ni ile namba aliyokuwa akitumia, ilikuwa ni namba yake ya Tanzania, ilikuwaje atumie namba hiyo na wakati alikuwa hapo Mombasa nchini Kenya. Akaipokea huku akiwa na shauku ya kutaka kujua kilichotokea.
“Halo!” akaita kwa sauti ndogo.
“Halo Eveline. Samahani mamii kwa kutokukupigia simu tangu asubuhi. Nilikwenda Morogoro kidogo kuna ishu nilifuatilia sasa hivi ndiyo naingia Dar,” alisikika Davis kwenye simu. Eveline akashtuka.
“Unasemaje?”
“Mbona umeshtuka sana.”
“Wewe si nimekuacha hotelini?”
“Hotelini? Muda gani?”
“Dakika arobaini zilizopita.”
“Mimi?”
“Ndiyo! Wewe!”
“Hotelini wapi?”
“Hapana Mombasa.”
“Mimi na Mombasa wapi na wapi? Kwanza sijawahi kufika huko. Halafu nitafikaje kimyakimya hivyo?” aliuliza Davis maswali mfululizo.
Eveline alichanganyikiwa, hakujua kilichoendelea. Alikumbuka kabisa kwamba alitoka kuzungumza na Davis hotelini na kumng’ang’aniza kufanya mapenzi lakini mwanaume huyo alikataa, sasa ilikuwaje ampigie simu na kumwambia kwamba alikuwa Dar es Salaam?
Hakutaka kubaki nyumbani, alihitaji kufahamu ukweli, kama yule mtu wa hotelini hakuwa Davis, alikuwa nani? Akaingia ndani ya gari lake na kuanza kurudi kule, alipofika, akaelekea mapokezi na kuhitaji kwenda kumuona mgeni aliyefikia katika chumba namba 88.
“Subiri tumpigie simu!” alisema dada wa mapokezi.
Simu ikapigwa, Eveline alikuwa na presha tele, alikuwa na dukuduku moyoni mwake, alihitaji kujiridhisha kwamba yule mwanaume aliyekuwa naye hotelini alikuwa Davis au mtu mwingine. Simu ilipigwa na kuita sana, haikupokelewa, mhudumu akapiga zaidi na zaidi lakini majibu yalikuwa yaleyale kwamba simu haikupokelewa.
“Hapokei simu. Bila shaka amelala!”
“Sawa. Naomba niende kumuona!”
“Kumuona haiwezekani! Huwezi ukafika chumbani kwa mteja pasipo kupewa taarifa,” alijibu mhudumu huyo.
Eveline akaenda katika kiti na kutulia. Alikuwa na kimuemue cha kuonana na David, alitaka kufahamu ukweli wa kile kilichokuwa kikiendelea. Alisubiri pale kwa dakika ishirini, alipoona kwamba hakukuwa na uwezekano wa kumuona akarudi pale mapokezi na kuanza kuongea na yule dada.
“Samahani! Nahitaji chumba,” alisema huku akimwangalia usoni.
“Chumba? Sawa.”
Hilo ndilo lililobaki. Alijua kwamba alizuiliwa kwenda kule ghorofani kuonana na David hivyo kitu chepesi kabisa ambacho kingemfanya kwenda huko kwa urahisi zaidi ni kuchukua chumba. Akapewa ufunguo na kuanza kupelekwa katika chumba ambacho alitakiwa kukitumia kwa usiku huo.
Wakati akipita katika chumba namba 88, alitamani kuugonga mlango na kuingia ndani lakini ilikuwa vigumu kufanya hivyo. Akapelekwa mpaka katika chumba namba 95 na kuambiwa kwamba hicho ndicho kilikuwa chumba chake kutokana na ukubwa wa pesa aliyokuwa amelipia.
“Nashukuru.”
Akaingia ndani na kumsikilizia mhudumu. Alipoona ameondoka tu, haraka sana akatoka na kwenda katika chumba kile na kuanza kuugonga mlango akitaka kufunguliwa.
Ni kama ndani hakukuwa na mtu, aliugonga na kuugonga lakini hakukuwa na mtu aliyeufungua. Alishindwa kuelewa kama mwanaume huyo alikuwa ndani ya chumba hicho au la. Akajaribu kuusukuma, mlango haukufunguka. Hakutaka kuacha, akaendelea kuugonga.
“Nani?” aliisikia sauti ya David.
“Mimi hapa.”
“Nani?”
“Mhudumu.”
“Nikusaidie nini mhudumu?”
“Nimekuletea chakula cha usiku.”
“Kwani tunatakiwa kula mara ngapi kwa usiku manake ulikwishaniletea, au umesahau?”
“Nimekuletea na soda pia.”
“Ila uliniletea na juisi, nikanywa na kushiba, au umesahau dada mhudumu?” aliuliza David aliyekuwa ndani.
“Naomba unifungulie.”
“Hilo si tatizo, unatakiwa kuniambia unahitaji nini ili nikufungulie.”
“Kuzungumza na wewe.”
“Kuhusu nini?”
“Kuhusu Davis. Unamfahamu huyu mtu?”
“Ndiye nani? Simfahamu mtu yeyote. Nakwenda kuoga kwanza, nitakuja kukufungulia,” alisikika David.
“Sawa.”
Ili kuogopa kushtukiwa, haraka sana Eveline akarudi chumbani kwake na kutulia. Kichwa chake kiliendelea kuwa na maswali mengi juu ya mwanaume huyo. Alichanganyikiwa, hakuamini kama alikuwa na uwezo wa kuwafananisha watu wawili namna ile, alikuwa na uhakika kwamba mtu aliyekuwa amemuona alikuwa Davis kwani kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, kucheka na kila kitu alikuwa na uhakika kwamba alikuwa yeye.
Baada ya dakika kumi, akainuka na kuelekea katika chumba cha mwanaume yule na kuanza kugonga. Mara hii hakuitikiwa, hakusikia kitu chochote kutoka chumbani, alipoona kimya sana, akakishika kitasa na kujaribu kufungua. Mlango ukafunguka, akaingia ndani, akajaribu kuangalia kila kona, hakumuona mwanaume huyo na sauti iliyokuwa ikisikika ni maji yaliyokuwa yakimwagika kwenye bomba la mvua bafuni.
Haraka sana akaenda huko, hakumkuta, akaangalia kila kona lakini mwanaume huyo hakuonekana. Akazidi kuchanganyikiwa zaidi. Akatoka na kuanza kuelekea chini kwa kasi ya ajabu, alipofika, akaanza kuangalia huku na kule lakini akamkosa mwanaume huyo.
“Yupo wapi? Kakimbia au?” alijiuliza lakini hakupata jibu.
Hakutaka kuridhika, alichokifanya ni kumpigia simu Davis na kuanza kuzungumza naye. Bado hakuamini kama walikuwa ni watu wawili, alichohisi ni kwamba mwanaume huyo alitaka kumchezea mchezo fulani tu.
“Niambie ukweli Davis..” alisema Eveline.
“Ukweli gani?”
“Kuhusu huyu mtu. Nina uhakika ni wewe, mbona unataka kunitesa hivi,” alisema msichana huyo.
“Eveline! Unazungumzia kuhusu nini? Mbona unanichanganya.”
“Umekuja huku Mombasa, halafu hutaki kuniambia,” alisema msichana huyo.
“Kuja Mombasa? Hapana! Sijaja huko.”
“Sasa huyu ni nani? Nimezungumza naye dakika kumi zilizopita hotelini, niambie huyu ni nani kama si wewe,” alisema Eveline.
“Si mimi! Nipo Dar, kama unaona nakudanganya, mbona hata simu inaonyesha kwamba ni code ya Tanzania! Eveline, umekutana na nani huko?” aliuliza Davis.
“Na wewe!”
“Mimi sijaja Mombasa.”
“Sasa huyu nani?”
“Ndiyo nikuulize wewe uliyekutana naye.”
“Hapana! Huyu ni wewe. Jinsi unavyoongea, unavyocheka mpaka kutembea. Huyu ni wewe Davis. Kwa nini unanifanyia hivi lakini?” alihoji msichana huyo.
“Si mimi! Utakuwa unaota Eveline kwa sab...” alisema Davis lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, Eveline akakata simu na kuanza kulia kama mtoto.
 
Bonge moja la arosto....nimekuwa teja wa kujitakia🤕🤕
 
Nikionaga jina Eric shigongo tu basi mzuka wote wakuendelea na kusoma simulizi huwa unaniisha
 
Back
Top Bottom