Longa mzee wa shamba
Na Mwandishi wa HabariTanzania.com
Shairilo nimesoma, tena nimeburudika,
Umenena kwa hekima , na wazi umetamka
nami ni bora nkasema, uwazi tunautaka
hata waimbe ngonjera, bado hatuwaelewi.
Umeme kitendawili, nani amewajibika,
wamezitapanya mali, wazila wanavyotaka,
majumba ya serikali, wametupa kama taka
Kikwete atupe jibu,tumechoka na ngonjera.
Madini walishagawa, hii ya Mkapa kazi,
kasi mpya itagawa, hili twaliona wazi,
hawa watu gawa gawa, hii ndiyo yao kazi,
Kikwete hata Lowassa, jamani tupeni jibu.
Wala rushwa wanatesa, wanadaka vidagaa,
nyangumi hawajanasa, wabaki kutahadaa,
mara nyingi tumeasa,twajua watuhadaa,
Kikwete tupeni jibu, ngonjera zimetosha.
Juzi wametuambia, kuwa kuna kazi nzito,
nguvuni kuwatia, wauza unga vizito,
mara wanatuambia,wameishavuka mto,
Wameikimbia nchi, nani wa kulaumiwa?
Naona mauza uza,urongo umeshamiri,
umma wameuchuuza, kwa kughani mashairi,
umma umejituliza,unangoja bila shari,
Kikwete twaomba jibu, matatizo yamezidi.
Juzi nilikueleza, kuwahusu wahalifu,
umma walouumiza, wakaufanya uchafu,
wenyewe wametuliza, hawana uadilifu,
wangapi umefukuza wale wakuu wilaya?
Wale walopiga watu, wakanyanyasa mchana,
hatuwasamehi katu, hata kama mwajuana,
kwetu hawa siyo watu, hawana hata maana,
wale Ma DC wako, Lowassa wangoja nini?
Tukutajie majina, utadhani huwajui,
waliyatenda bayana, mchana na asubuhi,
hebu fanya la maana, tushakupa maudhui,
Wale Ma DC wako, Lowassa wangoja nini?
Zirejeshe nyumba zetu, zile mlizogawana,
kwani hiyo pesa yetu, ndiyo tulichangishana,
zirejeshe nyumba zetu, hili ndilo la maana,
maneno yafuatie, tushachoka na maneno.
Fukuza wabadhilifu, ambao tunawajua,
wale wenye hitilafu, twajua mnawajua,
wale walocheza rafu, hakika mnajijua,
Hebu tufanyie kweli, tumechoka na ngonjera.
Watuzomea jirani, walonga twalamba buti,
japo tuna kisirani, hoja yao madhubuti,
umma uko msambweni, mnaujaza kaputi,
Kikwete imeshatosha, sasa anza chapa kazi.
Longa mzee wa shamba, huu ni wajibu wetu,
Atatulipa Muumba,anayo malipo yetu,
wananchi twaamba,nanyi msilale katu,
tusimame tuwabane, hawa wanotudanganya.
Source:
http://www.habaritanzania.com/articles/1897/1/