Nimekuwa nikitafakari kile kinachoendelea kufuatia tukio la vifo vya watu 20 vilivyotokea huko Moshi kwenye kongamano la Mtume Boniface Mwamposa "Bulldozer." Baada ya tukio hilo kumekuwa na maoni mengi na mitazamo tofauti kwa ujumla kutokana na jinsi ukio hilo lilivyotokea, nami nimeona nitoe mtazamo wangu juu ya jambo hili.
Chanzo cha vifo ni kipi hasa?
Hapa nimeona nichambue kwa kina tatizo hasa ni nini. Kumekuwa na mitazamo hasi kuhusiana na chanzo hasa cha vifo kiasi kwamba kumekuww na hasira kali juu ya imani ya baadhi ya watu.
1. Je vifo vimetokana na mafuta?
Ukitafakari kwa kina utaona hili si kweli. Mafuta hayakusababisha hivyo vifo kwa sababu hayuko hata mmoja aliyetumia mafuta hayo na kufariki. Mafuta hayo yamekuwa yakikanyagwa mara nyingi, kwa miaka mingi pasipo kuwa na madhara kwa watumiaji.
2. Je vifo vimesababishwa na mafundisho?
Ni muhimu kupima mafundisho kama ndio chanzo hasa cha vifo hivi. Kwamba kile kilichohubiriwa siku hiyo ndicho kilichopelekea watu kukanyagana hata vifo kutokea. Kama siku hiyo waliambiwa watakuokuwa wa kwanza kukanyaga mafuta watapokea upako kiasi cha kuwalazimu waamini kugombania nafasi ya kwanza basi hilo ni tatizo. Lakini kama fundisho lilikuwa ni kwamba kukanyaga mafuta tu ni kupokea baraka, basi haijalishi kama ni wa kwanza ama ni wa mwisho.
3. Je vifo vimesababishwa na mafundisho potofu?
Hili ni suala pana kwa sababu limelenga mambo ya kiimani. Nilishangaa jana pale nilipomsikiliza waziri Simbachawene akielezea jinsi ambavyo huwa anaangalia baadhi ya mafundisho na kujiuliza kama kuna Mungu pale. Siamini kama ni jukumu la waziri kupima wapi pana Mungu wa kweli na wapi hapana Mungu.
Mwenye jukumu la kupima usahihi wa mafundisho ni nani hasa linapokuja suala la imani? Nimesikia hoja yabkuwa na wahubiri wenye digrii ya teolojia. Je, ni sehemu gani kwenye Biblia ambapo Yesu alianzisha chuo cha teolojia ama kuagiza kianzishwe? Teolojia ni elimu ya kimfafanua Mungu KWA MTAZAMO WA ANAYEFUNDISHA. Hili ni tatizo. Tukifika hapo itabidi waprotestanti, wasabato, wakatoliki, moraviani, waanglikana na walutheri wakalishwe chini kuamua mafundisho yapi ni ya Mungu wa kweli. Itabidi tuamue teolojia ipi ni ya kweli na ndiyo hasa anayoikubali Mwenyezi Mungu.
Labda tujiulize mafundisho potofu ni nini? Hapo ndipo penye mgogoro na si vinginevyo. Sisemi haya kutetea mambo ya mafuta na maji ya upako, hasha. Nasema kwa sababu naona suala hili linachukua mkondo wa kidunia zaidi, kumpima Mungu kwa elimu ya kidunia wakati kumbe elimi ya Mungu wala haichangamani na hiyo.
4. Je, vifo vimesababishwa na usimamizi mbovu?
Nadhani hapa ndipo penye tatizo. Kilichotokea ni wazi kuwa ni usimamizi mbovu, ama uzembe kwenye kusimamia uendeshaji wa tukio la kukanyaga mafuta. Habari ya kwa nini watu wanaamini katika mafuta haina uhusiano hata kidogo na vifo hivyo. Ni sawa na kuhoji kwa nini watu wanaamini katika mkate na divai, ama katika kuchoma udi n.k. Tatizo liko kwenye utaratibu wa waamini kukipata kile wanachokiaminia.
Mambo ya kiimani yanabaki kuwa juu ya mhusika mwenyewe, hivyo ni ujinga kumwona anayeamininhayo kuwa mjinga. Nikutafuta kuwaingizia wengine imani yako kwa lazima, hivyo kuondoa maana ya uhuru wa kuabudu bila kuvunja sheria. Kama sheria imevunjwa, sio sheria ya kukanyaga mafuta bali sheria ya kushindwa kusimamia kusanyiko kwa usalama.
Hivyo basi hoja yangu imelenga kuonyesha kuwa sio sahihi kuanza kushambulia imani ya watu kwa vigezo vya nini sisi wengine tunakiamini, bali yatupasa kuwafundisha uzuri wa imani zetu na ubaya wa imani yao ili waamini habari zetu waachane na hayo yao.
Ni makosa makubwa kuwaaminisha wau kuwa tukio la mwamposa inashabihiana na lile la Kibwetee wa Uganda. Hii ni namna ya kutafuta kushambulia imani nyingine kwa mgongo wa nyuma na ndipo hoja za wenye imani tofauti zilipojikita. Mpaka sasa sielewi ni kwa vipi tukio la Moshi limefanana na lile la Kibwetere. Ni uongo na uzushi mkubwa wa wenye kuishambulia imani.
Nawasihi utafakari kwa kina tatizo lilipo, tuachane na mihemkoa bali tuwe wakweli kwani kweli itatuweka huru.
Sent from my SM-T355Y using Tapatalk