...ili ajibu tuhuma mbali mbali zinazomkabili za ufisadi
Tuna shaka na Mkapa
Tanzania Daima
JUMAPILI iliyopita, tuliandika tukimuomba Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa, avunje ukimya wake, ajitokeze kuzungumzia kashfa kubwa ya upotevu wa mabilioni ya fedha za Watanzania zilizochotwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) wakati akiwa kiongozi mkuu wa taifa letu.
Tulieleza imani yetu kwamba, Mkapa ndiye mtu muhimu, ambaye kauli yake inapaswa kusikika sasa akizungumza kuhusu kile anachokijua katika kashfa hii ya upotevu wa sh bilioni 133 kutoka Akaunti ya Kulipa Madeni ya Nje (EPA).
Tulieleza zaidi kuwa, pamoja na kutambua msimamo wa Mkapa tangu alipoondoka madarakani zaidi ya miaka miwili iliyopita sasa, wa kutotaka kuzungumza mambo yaliyotokea wakati akiwa madarakani, katika hili la upotevu wa mabilioni ya EPA, tulishauri kuwa anapaswa kubadili msimamo wake huo.
Kwamba ajitokeze, azungumze ili kulinda heshima yake na kuondoa shaka iliyoanza kujengeka dhidi ya wengi kuwa mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha urais wake ni kiini macho.
Kinyume chake, Mkapa amekuwa kimya, mengi yanazungumzwa dhidi yake na wenzake aliokuwa nao madarakani, lakini hakuna maelezo yaliyotolewa ya uhakika kuhusu hayo yanayozungumzwa.
Ukimya huu wa Mkapa umetufanya tuwe na shaka kwamba huenda haya yanayozungumzwa kuhusu yale aliyoyafanya wakati akiwa madarakani, yana chembe chembe za ukweli.
Shaka yetu hii inatokana na ukubwa wa tuhuma zinazomuandama, ambazo tunasema kwa kujiamini kabisa kuwa hazitofautiani sana na zilizowahi kuwaandama viongozi wengine wa Afrika, tukimtaja haraka Frederick Chiluba wa Zambia kama mfano wa kwanza, ambaye sasa anakabiliwa na mashtaka mahakamani.
Kwa sababu hiyo, tunapenda kueleza kuwa, ukimya wa Mkapa unatufanya tuwe na shaka kuwa, huenda tuhuma zilizotolewa kwamba wakati akiwa Ikulu alianzisha kampuni yake ya biashara inayotajwa kwa jina la ANBEM akishirikiana na mkewe, Anna Mkapa, ni za kweli.
Awali hatukutaka kabisa kuamini tuhuma hizi dhidi ya Mkapa, kwa kuzingatia kuwa sifa kubwa kwa kipindi kirefu akiwa madarakani, alikuwa akijulikana kama Mr. Clean, achilia mbali mkewe Anna ambaye alikuwa akitajwatajwa kujihusisha na biashara za hapa na pale.
Hatukuamini kwa sababu Mkapa alikuwa mwanafunzi mzuri wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambaye kwa kutumia ushawishi wake, alifanikisha Mkapa kwenda kukaa Ikulu baada ya kuwaaminisha Watanzania kuwa ndiye kiongozi aliyekuwa akifaa kwa wakati huo, kuongoza mapambano ya kuwakomboa Watanzania kutoka katika maisha magumu waliyokuwa nayo na kuelekea katika maisha yenye neema.
Shaka yetu inaongezwa na tuhuma kwamba mbali na kufungua Kampuni ya ANBEM, Mkapa huyu huyu, akishirikiana na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona, walisajili kampuni binafsi iitwayo Tanpower Resources na akaisimamia kununua asilimia 85 ya uliokuwa mradi wa umma wa makaa ya mawe, Kiwira mkoani Mbeya.
Kwamba, mbali na kufanya hivyo, Mkapa alikwenda mbali zaidi, alitumia wadhifa wake wa urais kuhahakisha kampuni yake hiyo inapata mkataba wa kuliuzia Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) megawati 200 za umeme katika gridi ya taifa.
Hizi ni tuhuma nzito sana kuelekezwa kwa kiongozi wa taifa la Tanzania, tena aliyeingia madarakani kwa msaada wa Baba wa Taifa hili, ambaye historia yake imetukuka kwa uadilifu.
Kwa dhati kabisa tunatamka kwamba, tuhuma hizi zinamfanya Mkapa kuwa rais wa kwanza katika historia ya taifa letu kufanya biashara akiwa Ikulu, mahali ambako palitajwa na Baba wa Taifa kuwa sehemu takatifu.
Hivyo basi, tunapenda kumshauri Mkapa kuwa iwapo ataendelea kuwa kimya, bila kujali ukubwa wa tuhuma zinazomkabili, na bila kujali heshima yake na heshima ya Baba wa Taifa aliyewaomba Watanzania wampe ridhaa ya kukaa Ikulu kwa sababu ni muadilifu, hakika, heshima aliyoondoka nayo madarakani inaweza kufutika kabisa.