SEHEMU YA 86
Fareed alifika nchini Marekani majira ya saa 10:30 jioni. Hali yake hewa ilikuwa ni baridi kali, katika sehemu kubwa ya Jiji la New York kulikuwa na theluji kitu kilichomfanya kuwa kwenye wakati mbaya mno.
Akaondoka uwanjani hapo kwa kuchukua teksi ambayo ilimpeleka mpaka katika Hoteli ya Queen Cleopatra ambayo haikuwa mbali sana kutoka katika uwanja huo. Alipofika, akakifuata kitanda na kutulia.
Bado kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, akili yake ilichanganyikiwa kupita kawaida. Maisha aliyokuwa amepitia yalikuwa machafu yaliyomfanya kulia sana.
Hakutaka kumwambia mtu yeyote kwamba aliamua kuyabadilisha maisha yake, hata Asteria alipokuwa akimtumia meseji kwa njia ya WhatsApp au hata kumpigia hukohuko hakuwa akipokea simu kwani alihitaji muda wa kuwa peke yake, Mungu ayasafishe maisha yake na kuishi maisha matakatifu.
“Nilisikia kwamba Yesu alikufa kwa ajili yetu wanadamu! Alisulubiwa ili tupate ukombozi, kwa kupigwa kwake, sisi tumepona. Mungu naomba unisaidie, uusafishe moyo wangu kwa damu ya Yesu,” alisema Fareed huku akiwa kitandani, hakuishia hapo, akatoka kitandani hapo, akapiga magoti na kuanza kusali kwa maneno aliyoyafahamu yeye kwani hakuwahi kuingia kanisani hata mara moja.
Sala yake ilichukua dakika tano, alikuwa akilia kwa uchungu mkubwa, aliuona upendo wa Mungu mpaka kumtoa mwanaye wa pekee kuja duniani kwa ajili ya maisha ya wanadamu lakini mwisho wa siku wanadamu hawakutaka kuyabadilisha maisha yao akiwemo yeye.
Alisikia hukumu kubwa moyoni mwake, alikuwa akilia na wakati mwingine alikipiga kifua chake kwa maumivu makali mno kwani hakuamini kama alikuwa amefanya uovu mkubwa kiasi hicho.
“Mungu! Naomba unisamehe! Mungu, mimi ni mwanadamu, nimekutenda dhambi, moyo wangu unalia, unahuzunika na kuumia, sikustahili kukutendea hay. Mungu! Nisamehe, usafishe moyo wangu,” alisema Fareed huku akiendelea kulia kama kawaida.
Siku hiyo ilikuwa ni siku ya kutubu dhambi zake, ulipofika usiku akalala huku akisubiri asubuhi ya kesho aende katika Kanisa la St. Peter ili kuungama dhambi zake kwa padri aweze kusamehewa.