Michirizi ya Damu

Shunie

JF-Expert Member
Aug 14, 2016
152,998
453,871
MICHIRIZI YA DAMU 01- Nyemo Chilongani

GIZA, Misri
Zilisikika kelele kutoka ndani ya piramidi moja lililokuwa katika Mji wa Giza uliokuwa nchini Misri. Watu waliokuwa humo ambao asilimia kubwa walikwenda kutalii wakatoka huku wakikimbia kwani mbali na kelele hizo, piramidi hilo halikuwa la kawaida, lilikuwa linatisha kiasi kwamba hata watalii waliokuwa wakiingia, walishikana mikono kama njia mojawapo ya kutokutana kuuawa na majini yaliyosadikiwa kwamba yalikuwepo ndani ya piramidi hilo.

Mwanamke yule aliyekuwa amepiga kelele akatoka huku akitetemeka, kijasho chembamba kikimtoka, walinzi waliokuwa mahali hapo wakamsogelea kwa lengo la kutaka kufahamu kilichomfanya mpaka kupiga kelele kiasi hicho hadi kuwaogopesha watu wengine.
Walipomuuliza mwanamke huyo wa Kiingereza akawaambia kwamba aliiona maiti ndani ya piramidi hilo kitu kilichomtisha kila mtu.

“What?” (nini?) aliuliza mwanaume mmoja.
“A deadbody!” (maiti)
“Are you sure?” (una uhakika?)
“Yes!” (ndiyo) alijibu mwanamke huyo huku akiendelea kutetemeka kwa hofu.
Watu wote waliotoka ndani ya piramidi hilo wakaanza kumwangalia mwanamke yule, wengine hawakuridhika, wakamsogelea na kumuuliza kilichokuwa kimetokea ndani ya piramidi lile, hakuficha, aliwaambia wazi kwamba aliiona maiti ikiwa chini kitu kilichomfanya kupiga kelele na kukimbia.
“Siyo kwamba umeona mauzauza?” aliuliza jamaa mmoja.

“Kwani mauzauza siyajui? Nimeona maiti!” “Sasa kwa nini ulikuwa peke yako na wakati hairuhusiwi?” aliuliza mwanaume mwingine.
“Niliingia na mume wangu! Yeye alikwenda upande mwingine na mimi kwenda mwingine,” alijibu mwanamke huyo na mumewe kutokea hapo, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumkumbatia mkewe.

Walinzi waliokuwa hapo wakachukua tochi zao na kuingia ndani ya piramidi hilo, walitaka kuona kile alichokiona mwanamke huyo. Kwa miaka mingi, tangu karne ya ishirini ilipoingia hakukuwa na mtu yeyote aliyekufa ndani ya piramidi hilo japokuwa kulikuwa na tetesi za kuwepo kwa majini. Kama hakukuwa na mtu aliyekufa! Iliwezekanaje mwanamke huyo kuona maiti humo?
20180327_154530.jpg
 
MICHIRIZI YA DAMU-02

Wakaingia mpaka ndani, wakaanza kumulika huku na kule, wakaelekea kule mwanamke yule alipokwenda huku wakiwa makini kuangalia chini. Kama alivyosema mwanamke yule ndivyo walivyokuta, macho yao yakatua katika mwili wa mwanaume mmoja uliokuwa chini, ulichomwa visu mara tatu kifuani na tumboni, mbali na hivyo, maiti yake iliburuzwa na kuachwa michirizi ya damu pale chini.

Kila mmoja alishtuka, hawakuamini kile kilichotokea, ilikuwaje mwanaume huyo auawe ndani ya piramidi hilo halafu muuaji asionekane? Kitu cha kwanza kabisa, hawakuigusa maiti ile, wakatoka ndani na kuelekea katika kompyuta zao na kuangalia orodha ya watu walioingia ndani ya piramidi lile dakika chache zilizopita kwani hata maiti ile ilivyoonekana, haikuonekana kama iliuawa muda mrefu uliopita.

“Mmeangalia jina lake?”
“Hapana!”
“Hebu kampekueni, mnaweza kuona hata kitambulisho,” alisema mwanaume aliyeshika kompyuta mpakato na hivyo walinzi hao kurudi ndani ya piramidi lile huku watu wengine wakiwa nje na idadi kubwa ya watu ikizidi kuongezeka.

Walipoingia humo, wakampekua mfukoni na kukuta ‘business card’ iliyomtambulisha kwa jina la Benjamin Keith, mwanaume wa Kimarekani aliyekuwa akimiliki kampuni kadhaa ikiwemo kampuni ya mavazi ya Cotton Keith.

“Kumbe ni Keith!” alisema mwanaume mmoja kwa mshangao.
“Ndiye nani?”
“Yule bilionea wa Kimarekani!”
“Unamaanisha yule mwenye utajiri wa dola bilioni kumi na mbili?” aliuliza mlinzi mwingine.

“Ndiyo!”
“Mh! Hebu nione hiyo kadi.” Akakichukua na kuanza kukiangalia, kama alichokiona mwenzake na yeye alikiona hivyohivyo. Kila mmoja alishangaa, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona, waliwafahamu sana matajiri, kila kona walipokuwa wakienda, walikwenda na walinzi wao, ilikuwaje Keith aende huko peke yake mpaka kuuawa? Kila walipojiuliza wakakosa majibu.

Wakatoka nje wakiwa na ile kadi na walipomuonyeshea jamaa aliyekuwa na kompyuta, akaangalia jina lile, akagundua kwamba Keith alikuwa ameingia ndani ya piramidi lile na msichana, mrembo aliyeitwa kwa jina la Maria Ogabugu aliyekuwa na asili ya Nigeria.
“Aliingia na mwanamke humu ndani,” alisema jamaa huyo.
“Hebu tuone.”
 
MICHIRIZI YA DAMU-03

Akaangalia kwenye kompyuta ile kwa lengo la kujiridhisha, kile alichoambiwa ndicho alichokiona kwamba bilionea huyo aliingia na mwanamke aliyejulikana kwa jina hilo ndani ya piramidi hilo.

Hawakujua mwanamke huyo alikuwa wapi kwani walikuwa na uhakika kwamba yeye ndiye aliyemuua Keith na kisha kukimbia.
Wakawasiliana na polisi ambapo baada ya dakika kadhaa wakafika na kuingia ndani ya piramidi lile. Wakaelekea mpaka kule kulipokuwa na maiti ile kisha kuiangalia. Ilionyesha kwamba hakuuawa muda mwingi uliopita, na hata kama muuaji alikimbia, hakuwa amefika Cairo.

Wakaupiga picha mwili ule kisha kuubeba kwa lengo la kuondoka nao ila kabla hawajaondoka, wakaona kipande cha karatasi kikiwa chini, kilikuwa kimezibwa na mwili ule, wakakichukua kikaratasi hicho kilichoandikwa kwa maneno machache kwa Kifaransa yaliyosomeka C'est fait yakiwa na maana ya kukamilika kwa jambo au ‘done’ kwa Lugha ya Kiingereza.

Hilo likaibua maswali mengi, hakukuwa na mtu aliyejua maana ya neno lile lililoandikwa. Mwili ukachukuliwa na kupelekwa hospitali ambapo familia yake ikapigiwa simu na kuambiwa kile kilichokuwa kimetokea.
 
MICHIRIZI YA DAMU-04

Taarifa hiyo ikawekwa kwenye mitandao ya kijamii na kutangazwa sana katika vituo vya televisheni na radio. Kila mtu aliposikia habari hiyo alishangaa, hawakuamini kama bilionea Keith aliuawa ndani ya piramidi nchini Misri kwani alikuwa mtu mwema ambaye kila mtu alijua kwamba angeishi miaka mingi kwa ajili ya kuendelea kuwasaidia watu masikini.

Serikali ya Marekani haikutaka kukubali, mawasiliano yakafanyika kwenda nchini Misri na kuwaambia kwamba wafanyaje kila linalowezekana mpaka muuaji huyo apatikane, kama walikuwa na uwezo wa kwenda sehemu yoyote ile, ilikuwa ni lazima mwanamke huyo akamatwe.
Lilikuwa ni agizo kubwa na gumu, hawakujua mahali alipokuwa muuaji hivyo polisi kwenda kuulizia katika piramidi hilo na kuambiwa kwamba bilionea huyo alikuwa na mwanamke wa Kinageria aliyeitwa Maria Ogabugu.

“Huyu mwanamke ndiye anayetakiwa kutafutwa na kupatikana haraka iwezekanavyo,” alisema kamanda wa jeshi la polisi jijini Cairo.

“Sawa mkuu!” Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuifunga mipaka yote ya nchi hiyo, uwanja wa ndege kukawekwa ulinzi wa uhakika, sehemu ya kivuko kwa kupitia katika mfereji wa Suez napo kukawekwa ulinzi mkubwa, kila kona, mpaka bandarini kote huko ilikuwa ni kulindwa kwa nguvu zote na kulipokuwa na askari wachache, wakaongezwa wengine kuhakikisha huyo mwanamke anayejulikana kwa jina la Maria Ogabugu hapiti kuondoka nje ya nchi hiyo. Iwe isiwe ilikuwa ni lazima kumatwa na kufikishwa katika mikono ya sheria.

Je, nini kitaendelea?
Je, mwanamke huyo ni nani na kwa nini ameua?
 
SEHEMU YA 05

Zilisikika kelele za mwanamke kutoka ndani ya chumba kimoja kilichokuwa katika Hoteli ya Melkizedek iliyokuwa ndani ya Jiji la Marseille nchini Ufaransa. Watu wote waliosikia sauti hiyo walishtuka, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, kwa jinsi sauti hiyo ilivyosikika, haikuonekana kuwa ya amani hata kidogo, ilionyesha kabisa kwamba kulikuwa na kitu kikubwa kilitokea.

Wateja wengine waliokuwa katika vyumba vingine wakatoka, walitaka kujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea. Walipotokea ukumbini, macho yao yakatua kwa msichana aliyekuwa mhudumu ndani ya hoteli hiyo akiwa amekaa pembeni kabisa akilia huku akitetemeka kwa hofu kubwa.

Hakukuwa na aliyejua kitu kilichomfanya msichana huyo mrembo kuwa katika hali hiyo. Wakamsogelea kwa lengo la kumuuliza lakini hakujibu kitu, alichokifanya ni kuwaonyeshea chumba kilichokuwa mbele yake ambapo baada ya watu kuufungua mlango wa chumba hicho, macho yao yakatua katika maiti moja iliyokuwa sakafuni.

Kila mmoja alishtuka, hawakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea. Harakaharaka simu ikapigwa kwenda kwa polisi na kwa meneja wa hoteli hiyo ambapo baada ya meneja kufika, akamuuliza msichana huyo ni kitu gani kilitokea lakini akawaambia hakuwa akijua, alimpelekea mteja kahawa lakini akakutana na maiti hiyo.

Baada ya dakika chache polisi wakafika mahali hapo. Kitu cha kwanza kilikuwa ni kuzungumza na msichana huyo ambaye maelezo yake alisema kwamba alikuwa na utaratibu wa kumpelekea kahawa mteja huyo kila inapofika jioni lakini kitu cha ajabu kabisa, jioni ya siku hiyo akakuta maiti ya mwanaume huyo ndani ya chumba hicho.

Kitu cha kwanza walichokitaka ni kumfahamu mtu ambaye alikuwa ndani ya chumba hicho na mwanaume huyo ambaye hawakujua alikuwa nani kwani alichomwa visu kadhaa shingoni mwake, damu nyingi zilimtoka, nyingine zikauziba uso wake na pale alipoanguka, aliburuzwa na hivyo kufanya michirizi ya damu kuonekana sakafuni.
 
SEHEMU YA -06

Walipokwenda mapokezini na kuangalia wateja walioingia, wakaliona jina la mwanaume huyo, aliitwa Belleck Peter, bilionea mkubwa aliyekuwa akimiliki kiwanda cha karatasi na viwanda kadhaa vya kutengeneza mbao vilivyokuwa nchini Marekani.

Kila mtu alishangaa, hawakuamini kama mtu aliyeuawa ndani ya chumba kile alikuwa Belleck. Alijulikana dunia nzima kutoka na utajiri wake mkubwa wa dola za Kimarekani bilioni 7 ambazo ni zaidi ya shilingi trilioni 14, aliheshimika na watu wengi walimuita kwa jina la Golden Angel ‘Malaika wa Dhahabu’ kwa jinsi alivyokuwa akiwasaidia watu wengi, hasa vituo vya watoto yatima na masikini waliokuwa wakilala mitaani.

“Is this Belleck I know?” (huyu ni Belleck ninayemfahamu?) aliuliza polisi mmoja huku akionekana kushangaa.
“Yeah! What has happened?” (ndiyo! Hivi ni kitu gani kimetokea?) aliuliza polisi mwingine.

Hakukuwa na aliyejua, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuwatafuta wasichana wote waliokuwa wamelala naye kwani kwa taarifa walizozikuta hotelini hapo ni kwamba tangu Belleck afike katika hoteli hiyo, kazi yake kubwa ilikuwa ni kubadilisha wanawake tu.

Msichana wa kwanza alikuwa Natasha, alichukuliwa kutoka katika mawindo yake ya usiku, wa pili alikuwa Stella na wa tatu alikuwa Neyonce. Wote hao walikuwa wakijiuza mitaani na mtu ambaye walifanya naye biashara yenye malipo makubwa alikuwa mwanaume huyo.

Kila mtu kwa wakati wake wakaingizwa ndani ya chumba cha mahojiano na kuanza kuulizwa kuhusu msichana huyo. Hakukuwa na aliyejua, kitu pekee walichokuwa wakikifahamu ni kwamba walinunuliwa na mwanaume huyo, wakafanya naye mapenzi na kisha kuondoka zao baada ya malipo kufanyika.

“Alors rien n'est arrivé ,” (kwa hiyo hakuna kilichotokea?) aliuliza polisi kwa kutumia Lugha ya Kifaransa.
“Rien ne se passe que le sexe,” (hakuna kilichotokea zaidi ya ngono)
 
SEHEMU YA 07

Walihitaji kufahamu ukweli. Taarifa zilisema kwamba mwanaume huyo alikaa hotelini kwa siku nne, na siku zote hizo alikuwa akilala na mwanamke hotelini lakini mpaka muda huo walikuwa wamefanikiwa kuzungumza na wanawake watatu tu, kulikuwa na mmoja alibaki, alikuwa nani? Walihitaji kumfahamu msichana huyo.

Wakaelekea mpaka hotelini na kuwauliza wahudumu. Wengi walikumbuka kwamba siku ya nne mwanaume huyo aliingia na msichana aliyekuwa amevalia nikabu na suruali ya jinsi, alikuwa na shepu bab’ kubwa na nyuma alionekana kujazia hasa, aliingia na bilionea huyo ndani ya chumba kile lakini hawakumuona alipokuwa ametoka, walihisi kwamba huyo ndiye alifanya mauaji.

“Ana muonekano gani?” aliuliza polisi.
“Ni mrefu, kwa muonekano wa macho yake, anaonekana ni mzuri sana, halafu anatembea kwa madaha kama twiga mbali na hayo, mwanamke huyo ana bomba moja kubwa sana kwa nyuma,” alijibu mhudumu mmoja wa kiume.

“Bomba ndiyo nini?”
“Kalio! Kajazia sana.”
“Na alipotoka hamkumuona?”
“Ndiyo! Ila alikuwa naye hotelini!”
Mpaka hapo polisi wakapata uhakika kwamba mtu aliyemuua biliona huyo alikuwa mwanamke ambaye wakati akiingia ndani na bilionea huyo alijitambulisha kwa jina la Victoria. Walitaka kumfahamu msichana huyo, baada ya kuondoka, alielekea mahali gani, na kama hakupitia pale mapokezi, alipitia wapi?

“Na hakuna mtu anayeweza kupitia mlango wa nyuma?” aliuliza polisi.
“Hakuna! Mlango wa nyuma ni kwa ajili ya wafanyakazi tu, tena inabidi uingize namba za siri ambazo zinajulikana kwa wafanyakazi tu,” alijibu msichana mmoja.
Waliwahoji wafanyakazi kadhaa ndani ya hoteli hiyo, kila mmoja alimwambia alichokuwa akikifahamu kuhusu kifo cha bilionea huyo. Wengine wakahisi kwamba alijiua, kwamba aliingia ndani ya chumba kile na kujimaliza mwenyewe kwa kuwa tu alikuwa na mawazo mengi kuhusu mkewe aliyefariki miezi mitatu iliyopita.

Hilo halikuingia akilini mwa polisi, walijua kabisa kulikuwa na mtu aliyemuua bilionea huyo na walihisi kabisa mwanamke huyo wa mwisho aliyeingia naye ndiye aliyefanya mauaji hayo.
 
SEHEMU YA 08

Kwa sababu ilikuwa ni hoteli kubwa na yenye kamera ndogo za CCTV, walichokifanya ni kuhitaji picha zilizorekodiwa, wakapelekwa huko kulipokuwa na video na kisha kuangalia kile kilichokuwa kimetokea.

Ni kweli walimuona mwanamke huyo akiingia na bilionea huyo hotelini, sura yake haikuonekana vizuri kwani alivalia vazi la wanawake wa Kiislamu, nikabu ambalo lilificha sura nzima na ni macho tu ndiyo yaliyokuwa yakionekana.

Wakaingia ndani ya chumba hicho ambapo baada ya saa nne, akatoka na kuondoka, hakupitia mlango wa mbele, akapitia mlango wa nyuma na kilichowashangaza sana polisi ni kwa namna gani mwanamke huyo kupita kwenye mlango huo na wakati hakuwa na namba za siri za kufungua mlango huo?

“Aliufungua vipi huo mlango?” aliuliza polisi huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Hata sisi hatujui!”
“Ni lazima kutakuwa na mtu alimpa namba ya siri!”
Wakati wakijadiliana hilo ndani ya chumba hicho kilichokuwa na kompyuta, mara simu ya mkuu wa polisi ikaita ambapo harakaharaka akaipokea na kusikiliza, aliisikia sauti ya mwanaume kwenye simu ambayo ilimwambia kwamba walikutana na kitu cha ajabu baada ya kuitoa maiti ya bilionea Belleck ndani ya chumba kile.
 
SEHEMU YA 09

“What is that?” (Kitu gani?) aliuliza.
“We have found a piece of paper written C'est fait on it,” (tumekuta kipande cha karatasi kikiwa kimeandikwa Imekamilika juu yake) alisema jamaa huyo.

“Is it surprising you?” (hicho ndicho kinachokushangaza?)
“It’s the same person who killed Cotton Keith in Giza, Egypt,” (ni mtu yuleyule aliyefanya mauaji ya bilionea Cotton Keith kule Giza nchini Misri) alisikika mwanaume huyo.

“What?” (unasemaje?)
“That it is sir.” (ndiyo hivyo mkuu!)
Walichanganyikiwa, ilikuwaje muuaji wa Belleck awe yule msichana aliyefanya mauaji kule nchini Misri na wakati mtu huyo alikuwa akitafutwa kila kona nchini humo?

Alishangaa. Hakutaka kutulia, haraka sana akatafuta namba ya simu ya mkuu wa polisi nchini Misri kupitia kitengo cha Interpool na kumuuliza kuhusu suala lile kama muuaji alikamatwa au la.

“Bado hatukumkamata!”
“Basi sawa.”
“Kuna nini?”
“Amefanya mauaji na huku pia.”
“Amefanya mauaji! Lini?”
“Leo hii!”

“Haiwezekani! Hakuna mtu anayeweza kuua kirahisi, ndani ya siku chache kama hizi,” alisema polisi mkuu kutoka nchini Misri.
“Ndicho kilichotokea! Ila nahisi tutampata japokuwa swali moja muhimu la kujiuliza, hivi kwa nini anaua mabilionea tu?” aliuliza polisi wa Ufaransa.

“Mmh! Kweli! Napata picha! Kwa nini mabilionea? Hii inamaanisha ndani ya siku chache zijazo kutakuwa na bilionea mwingine atauawa kama tu tusipofanya kazi ya ziada kumkamata?”

“Inawezekana! Hebu tusubiri. Ila nina uhakika kwa mauaji aliyoyafanya hapa, tutamkamata! Tena wiki hiihii na atatuambia kwa nini anauacha ujumbe huu kila anapofanya mauaji,” alisema polisi wa Ufaransa na kukata simu. Msako wa kumtafuta mwanamke huyo ukaendelea.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 10

“Where is the father?” (padri yupo wapi?) alisikika msichana mmoja akiuliza kanisani alipokwenda kwenye chumba kidogo kwa ajili ya kuzungumza na padri lakini bahati mbaya hakumkuta.
“He was right there,” (alikuwa huko)
“Where?” (wapi?) Watu walikuwa wakiulizana kanisani. Hakukuwa na watu wengi, kanisa zima lilikuwa na washirika watano ambao walikaa kwa kujigawa ndani ya kanisa hilo kubwa.

Walishangaa, kitendo cha kutokumuona padri kanisani humo kiliwapa wakati mgumu wa kutokugundua mwanaume huyo alikuwa wapi kwani kwa siku kama hiyo, tena ya kuungama dhambi zao, ilikuwa ni lazima padri awepo ndani ya chumba kile cha kuungamia dhambi.
Hakukuwa na mtu aliyejua mahali alipokuwa ila hawakuwa na hofu hata kidogo kwani waliamini kwamba padri huyo angerudi kanisani hapo na mambo kuendelea kama kawaida.

Hilo lilikuwa kanisa kubwa jijini New York nchini Marekani. Watu wengi wa Kanisa la Roma walikuwa wakishiriki misa katika kanisa hilo kubwa, wengi walitoka nchini nyingine na kufika katika kanisa hilo ambalo lilikuwa la kwanza kutembelewa na Papa José Kentenich miaka ya 1880.
Siku ya kwanza ikapita lakini hakukuwa na mtu aliyefahamu mahali padri alipokuwa. Walikuwa wakishiriki misa lakini kanisa liliongozwa na padri msaidizi ambaye naye hakujua mahali padri mkuu alipokuwa.

Wakati siku ya tatu ikiwa imeingia ndipo kanisani kukaanza kusikika harufu mbaya. Ilikuwa ni harufu ya mzoga iliyokuwa ikiwasumbua, wengi walihisi kwamba inawezekana mzoga huo ulikuwa nje ya kanisa hilo lakini kila walipokaa, wakajua kabisa mzoga huo ulikuwa ndani ya kanisa hilo.

Hapo ndipo walipoanza kuchunguza, waliangalia huku na kule na mwisho wa siku kugundua kwamba mzoga huo ulikuwa ndani ya chumba kile cha kuungamia dhambi ambacho kiliruhusiwa kuingiwa na mtu mmoja tu ambaye ndiye padri.
 
SEHEMU YA 11

Hawakuwa na jinsi, kwa kuwa hiyo ilikuwa ni siku ya tatu bila padri kuonekana, wakazunguka upande wa nyuma na kuingia. Walichokutana nacho kiliwashtua kupita kawaida, waliiona maiti ya padri ikiwa sakafuni, ilikuwa imechomwa visu kadhaa shingoni na ubavuni huku ikianza kuharibika na kuutoa harufu mbaya na kali.

Picha iliyoonekana mahali hapo iliwasisimua sana kwani mbali na kuuawa, ilionekana kabisa kwamba mwili wake uliburuzwa na hivyo kuacha alama za michirizi ya damu kitu kilichowafanya kusisimka zaidi.
“Mungu wangu! Padri!” alisema jamaa mmoja huku akionekana kushtuka.
“Jamani! Nini kimetokea?” aliuliza msichana mmoja, naye mwenyewe kama alivyokuwa mwanaume yule, alichanganyikiwa.

Walichokifanya ni kupiga simu katika kituo cha polisi hapo New York katika Mtaa wa Brooklyn ambapo baada ya dakika kadhaa polisi wakafika na kwenda ndani ya chumba kile.

Harufu iliyokuwa ikitoka humo ndani, iliwashtua, ilikuwaje mtu afe ndani ya chumba halafu ichukue siku nyingi kiasi hicho mpaka kugundua, wakahisi kwamba kulikuwa na tatizo.

“Nani amefanya mauaji haya?” aliuliza polisi mmoja.
“Hatujui! Tulikuwa tukimtafuta sana padri lakini hatukumpata mpaka leo hii tumeuona huu mwili wake,” alisema mwanaume mmoja.
Mwili ukapigwa picha, polisi walihakikisha wanafanya taratibu zote zilizotakiwa kufanywa na wao kisha kuuchukua mwili kwa lengo la kuondoka nao.

Wakati wakiwa wameutoa mahali pale, wakakiona kipande cha karatasi pembeni yake, wakakichukua na kuanza kukisoma, kilikuwa kidogo kilichoandikwa maneno machache yaliyosomeka ‘It is done’ kwa maana ya kazi kukamilika.

Polisi walivyokiona kipande hicho cha karatasi walishtuka, hawakuamini kama kweli muuaji aliyekuwa amefanya mauaji katika nchi mbili, Misri na Ufaransa ndiye ambaye alifanya mauaji ndani ya kanisa hilo.

Wakapeana taarifa kwa njia ya simu kwamba kulikuwa na mauaji mengine yaliyokuwa yamefanyika na muuaji alikuwa yuleyule aliyeua kipindi cha nyuma kitu kilichowafanya watu wengi wawe na hofu juu ya muuaji huyo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom