SEHEMU YA 83
Hawakutaka kuona wakishindwa, waliamini kwamba kama wangemtafuta mtu huyo angepatikana hivyo kuingia mitaani na kuanza kumtafuta. Walitumia saa nne lakini hawakufanikiwa kumpata na muda wote huo Belleck alikuwa akiwasumbua kwenye simu kwa kutaka kujua kile kilichokuwa kikiendelea.
Walianza kwa kumficha lakini mwisho wa siku walipoona muda umekwenda sana na hawakumpata, wakaamua kumwambia ukweli kwamba Fareed aliwatoroka hospitali.
“Alitoroka?”
“Ndiyo!”
“Aliwatorokaje?”
Wakaanza kumwambia namna mtu huyo alivyowatoroka, alitaka kuwalaumu lakini baada ya kuambiwa mazingira yote jinsi alivyotoroka, akaridhika na kuona kwamba hata kama angekuwa yeye ilikuwa ni lazima kutorokwa kama ilivyokuwa kwa wenzake.
“Ila hakikisheni mnamtafuta hapo. Najua atakuwa hapohapo Marseille,” alisema Belleck huku akiwa na uhakika kwamba mtu huyo hakuwa ametoka hapo Marseille.
“Haina shida mkuu!”
**** Fareed alikuwa ndani ya chumba cha hoteli, moyo wake ulikuwa kwenye majonzi tele, siku hiyo hakujisikia vizuri kabisa. Aliyakumbuka maisha yake aliyokuwa amepitia, jinsi alivyokumbwa na pepo la ngono ambalo lilimfanya kushiriki mapenzi ya jinsi moja.
Moyo wake ulimuuma mno, ulichoma kiasi kwamba hadi machozi ya uchungu yakaanza kutiririka mashavuni mwake. Alijijua kwamba yeye alikuwa mkosaji, alijua kwamba Mungu alimuumba mwanaume kwa kuwa alikuwa na makusudi naye, hapo akagundua kwamba Mungu hakufanya makosa kumuumba mwanaume bali alikuwa na makusudi mengi.
Alijuta, siku hiyo alijikuta akianza kuyafikiria maisha yake, njia zake mbaya alizopitia, alilia kama mtoto chumbani mule. Nafsi yake ilimuhukumu, ilimwambia kwamba alichokuwa amekifanya kwa miaka yote halikuwa kusudio la Mungu bali la shetani ambaye aliamua kumtumikisha kupitia mwili wake.
Alitaka kubadilika, hakutaka kuendelea kumtumikia shetani, alitaka kubadilika na kuwa mtu mwingine kabisa. Tangu azaliwe, hakuwahi kwenda msikitini wala kanisani, hakujua yeye alikuwa dini gani, alijichagulia maisha yake kuishi hivyo hata alipotaka kuyabadilisha maisha yake.