SEHEMU YA 80
Belleck alikuwa ametulia, masikio yake yalikuwa kwenye simu yake, alitaka kufahamu kile kilichokuwa kikiendelea nchini Ufaransa, alitaka kujua kama tayari Fareed alifanyiwa upasuaji na kutolewa kwa kete za madawa ya kulevya au kitu hicho hakikuwa kimefanyika.
Alisubiri sana, tangu Fareed afikishwe ndani ya hospitali, aliambiwa kwamba angepigiwa simu na kupewa kila kitu kilichokuwa kimeendelea lakini mpaka saa moja na nusu bado hakuwa ametaarifiwa kitu chochote kile.
Alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilitokea, hakutaka kuvumilia, hapohapo akachukua simu yake na kupiga upande wa pili, simu ilipopokelewa, akaambiwa kila kitu kilichokuwa kimetokea.
“Kwa hiyo Dk. Wtason hayupo?” aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Ndiyo mkuu!”
“Atatuchelesha, ingieni ndani na mmuue kisha zitoeni hizo kete, hakuna haja ya kuendelea kumsubiri muda wote,” alisema Belleck na kukata simu.
Ilikuwa ni amri, vijana hao hawakutaka kuendelea kumsubiri daktari huyo, walitaka kufanya kile walichokuwa wameambiwa. Fareed alikuwa ndani ya chumba kile, haikuwa kazi kubwa kuingia na kumuua kisha kulipasua tumbo lake na kuzitoa kete alizokuwa amezimeza.
Wakaufuata mlango kwa lengo la kuufungua, haukufunguka, ulionekana kufungwa kwa ndani. Kwa kuwa hiyo haikuwa hospitali kubwa sana, hakukuwa na wagonjwa wengi wala madaktari hivyo kuanza kuupiga mlango huo kwa lengo la kuuvunja na kuingia, tayari walipewa agizo kwamba mtu huyo auawe hivyo hawakuwa na msalie mtume.
*
*
“What are you doing?” (mnafanya nini?) lilisikika swali kutoka kwa mwanamke aliyekuwa nyuma ya watu hao waliokuwa wakijaribu kuuvunja mlango ule wa chumba alichokuwemo Fareed.
Vijana wa Belleck wakageuka nyuma na kumwangalia mtu aliyewauliza swali hilo. Alikuwa nesi wa hospitali hiyo, kibonge, aliyevalia gauni refu jeupe huku kichwani akiwa na kikofia kidogo cha kilichoonesha kwamba alikuwa muuguzi.
Bastola zilikuwa mikononi mwao, kitendo cha mwanamke huyo kuziona bastola hizo, hakutaka kubaki mahali hapo, akaanza kukimbia huku akiwaita polisi kwani alijua kwamba watu hao hawakuwa watu wazuri hata mara moja.