Michirizi ya Damu

Michirizi ya Damu

SEHEMU YA 136

“Hapana!”
“Kwa hiyo namba yangu uliifuta?” aliuliza Fareed.
“Mmh! Sina uhakika! Wewe nani?”
“Naitwa Farida!”
“Yupi?”
“Yule wa Belleck!”
“Ooh! Yule wa mpumbavu?” “Ndiyo!”

Kwa sababu watu hao walikuwa wakichukiana, Fareed aliamini kwamba angeweza kufanya naye kazi kwa ajili ya kukamilisha kile alichokuwa akikihitaji.

Akamwambia mwanaume huyo kwamba walitakiwa kuonana na hivyo kama hatojali basi aende kuzungumza naye kitu ambacho kwa bilionea huyo hakukuwa na tatizo lolote lile.

Ndani ya saa moja tayari Bilionea William alikuwa mbele ya Fareed. Alimwangalia kwa umakini sana, alionekana kuwa mtu tofauti kabisa, hakuwa kama kipindi kilichopita, mwanaume mwenye muonekano wa kike, kwa kipindi hicho alikuwa mwanaume shupavu, mwenye mwili uliojazia.

Williams alibaki akimkodolea macho, hakuamini kama mwanaume aliyesimama mbele yake ndiye mwanaume yule aliyefahamiana naye kitambo.

Fareed akamwambia bilionea huyo kile kilichomleta Marekani, hakuja kula starehe bali alitaka kufanya kazi moja, kumuua Bilionea Belleck.
“Kwa nini tena?”

Akamwambia sababu kwamba aliamua kufanya hivyo kwa kuwa mwanaume huyo naye alitaka kumuua ila kwa msaada wa Mungu aliweza kumtoroka na watu wake.

Williams akafurahia, chuki aliyokuwa nayo kwa Belleck ilikuwa kubwa kiasi kwamba kwa kitendo cha kuambiwa kwamba mwanaume huyo alikuwa tayari kumuua halikuwa tatizo kabisa.

“Kwanza hayupo Marekani,” alisema William.
“Yupo wapi?”
“Paris nchini Ufaransa,” alijibu Williams.
“Ni lazima niende huko. Utanisaidiaje kufika?” aliuliza Fareed.

Ili apate msaada wa kufika Ufaransa ilikuwa ni lazima amwambie Williams ukweli kwamba alikuwa akitafutwa kila kona. Mwanaume huyo alibaki kimya, alitaka muda wa kujifikiria ni kwa jinsi gani angemtorosha Fareed kuelekea nchini Ufaransa.

Alikaa na kuwaza sana, jibu alilokuja nalo ilikuwa ni lazima kwa mwanaume huyo asafiri kwa kutumia ndege yake binafsi ambayo ingempeleka mpaka huko.

“You will take my flight,” (utachukua ndege yangu) alisema Williams.
 
SEHEMU YA 137

Hakuwa na uamuzi mwingine zaidi ya huo na safari ilitakiwa kufanyika usiku. Fareed akajiandaa na baada ya siku mbili, magari mawili ya kifahari yakafika hotelini hapo na kumchukua kisha kumpeleka uwanja wa ndege.

Moyo wake ulikuwa na hofu, hakuamini kama angefika salama huko kwani kila kona alikuwa akitafutwa na FBI ambao hawakutaka kuzisambaza picha zake, walimtafuta kimyakimya ili asishtukie kama anatafutwa kumbe mwenzao alikwishajua hilo kitambo.

Uwanja wa ndege, hakupitishwa mlango wa kawaida, ndege ilikuwa ni ya binafsi tena ya bilionea mkubwa duniani, hivyo hata mlango aliopitishwa ulikuwa ni wa VIP na ilikuwa vigumu kumgundua kwamba alikuwa yeye.

Mpaka anakaa katika kiti ndani ya ndege hiyo, akashusha pumzi ndefu, hakutegemea kama ingekuwa kazi nyepesi namna hiyo.

Huku nyuma, bilionea Williams alikuwa akifanya mawasiliano na watu wake waliokuwa Ufaransa, alitaka kupata data zote kuhusu bilionea huyo, kwamba alikuwa akiishi katika hoteli gani na ratiba yake ya siku ilikuwaje.

Hilo halikuwa tatizo kwa vijana wake, kwa kuwa walikuwa huko na mtu huyo alikuwa maarufu, wakapata data zote na kumtumia na hivyo na yeye kumtumia Fareed ambaye baada ya kuzipokea, akamshukuru Mungu.

“Sasa kazi itafanyika,” alimwambia Williams kwenye simu.
“Ukikamilisha! Nakuahidi kukupa dola milioni kumi.

Huyu mpumbavu ananinyima sana usingizi,” alisema William huku akiwa na uhakika kwamba ilikuwa ni lazima mwanaume huyo ammalize Bilionea Belleck.

Ila la zaidi, alitaka kuona bilionea huyo akifa na yeye kumuua Fareed kwani kama angemuacha, siri ingeweza kuvuja. Ili siri itunzwe ilikuwa ni lazima hata naye Fareed afe.
 
SEHEMU YA 138

Fareed hakujua mahali mwanaume huyo alipokuwa, ila aliambiwa kwamba angepewa maelezo yote kwani yale aliyopewa mara ya kwanza, yalibadilika kwani mtu huyo aliondoka Paris na hakukuwa na aliyejua kama alikwenda Monaco au Marseille.

Baada ya dakika hamsini akapigiwa simu na kuambiwa kwamba mwanaume huyo hakuwa hapo Paris bali alikuwa jijini Marseille katika Hoteli ya Melkizedeki ambapo alikuwa akilala huku kila siku akishiriki katika kikao cha matajiri.

Hilo halikuwa tatizo, haraka sana akaondoka hotelini alipokuwa, akachukua ndege na kuelekea Marseille ambapo ndipo aliambiwa mwanaume huyo alipokuwa.

Njiani, alikuwa akimuomba Mungu afike salama kwani alikuwa na hasira kali, asingeweza kumuacha mwanaume huyo akaishi kwani alikuwa miongoni mwa watu waliotaka kumuua kwa nguvu zote.

Walichukua dakika arobaini na tano tu mpaka kufika jiji humo ambapo akateremka na kuchukuliwa kwa gari mpaka katika hoteli moja na kutulia huko.

Ilipofika saa mbili usiku, wanaume wawili wakafika hotelini hapo na kuomba kuzungumza naye.

Hilo halikuwa tatizo, alipewa taarifa na Williams kwamba watu hao wangefika mahali hapo, na wao ndiyo ambao wangemwambia kuhusu Belleck ambaye hakujua alikuwa katika hoteli gani.

“Belleck yupo anakula raha, hivi tunavyoongea, keshokutwa anaondoka kurudi Marekani,” alisema mwanaume mmoja aliyejitambulisha kwa jina la De Leux.

“Sawa. Kingine?”
“Huwa anapenda sana kununua malaya mitaani! Tunajua sehemu ambayo hupenda kununua na pia tunajua hoteli anayokaa mpaka chumba alichokuwepo,” alisema De Leux.

“Haina shida! Ningependa nikutane naye na kufanya kazi yangu,” alisema Fareed.
Hakwenda huko kufanya jambo lolote zaidi ya kumuua bilionea huyo na kuondoka zake.

Wanaume hao wawili ndiyo walikuwa wachora ramani wakubwa, walikuwa wakienda hotelini hapo, wanaonana na wahudumu wa hapo, wakatengeneza urafiki wa kizushi kwa ajili ya kuwasaidia hapo baadaye.
 
Back
Top Bottom