Sawa,
Labda nitangulize kipande hiki kisha nipate feed back za watu. Wapi nibadilishe ama kipi niongezee maanake unajua tunaweza kutunga kitabu cha pamoja hapa?..mengi yaliyotangulia umewahi kunisikia nikiyasema siku za Bcstimes, TEF na mijadala iliyotangulia ya JF. Kisha lugha ya uandishi mjomba mimi bado kabisa sijaenda shule! ila nakuombeni jaribuni kuipata message!..naandika kama nanyoongea, kazi kweli kweli!
Hata hivyo itachukua miezi kukamilisha kwa hiyo tuanze na kipande hiki kulingana na mawazo yangu mimi binafsi - MJAMAA mimi!
Nimeondoa kichwa cha habari kinachotangulia.
UTANGULIZI
Kwa muda mrefu sana nimekuwa nikisumbuka kuelewa hasa dhumuni la nchi yetu na hasa nchi za kiafrika tulipodai uhuru wetu toka kwa mkoloni ikiwa matokeo ya uhuru huo umekuwa na matunda mabaya sana kwa raia wake kisiasa na kiuchumi. nachopenda kujiuliza kila mara ni kati ya maswali haya:-
Kiutawala:- Je, dhumuni hasa lilikuwa kumwondoa mtawala mlowezi na badala yake kumweka mzawa tukitumia falsafa inayofanana na nguvu ya milki iliyowekwa na mkoloni?
Kiuchumi:- Je, ilikuwa mategemeo ya wengi viongozi kubadilisha mkono wa mtawala wa uchumi toka mlowezi na badala yake kushikwa na mzawa pasipo kuwa na dira yenye malengo ya kumkomboa mwananchi kiuchumi ama tulitegemea kwamba zimwi likujualo halikuli likakwisha!..
Nini hasa maana ya neno UHURU ikiwa wananchi wengi wa nchi zilizo huru wamekuwa na maisha mabaya zaidi chini ya utawala wa mzawa. Adui mkubwa wa maendeleo ya mwafrika imekuwa mwafrika mwenyewe. Umaskini wa mwafrika umezidi kukua baada ya Uhuru na ujenzi wa matabaka baina ya wananchi kiuchumi umeshamiri zaidi ktk siasa zetu.
Leo hii imefikia kuwepo na watu wanaosema - Afadhali ya mkoloni!
Hili ni neno zito sana na lenye uchungu mkubwa kwa mwenye kufikiri, kwa sababu umaskini wa mwafrika ni maradhi ya kujitakia zaidi ya hali halisi na yawezekana kabisa kuwa UHURU wetu umetafsirika vibaya hivyo kupoteza malengo ambayo yalikusudiwa toka awali kwa sababu ya tamaa ya baadhi watu wachache walioshika ama wanaendelea kushika madaraka aidha kwa kuchaguliwa ama kuteuliwa.
Pamoja na maswali yote haya, sio rahisi kupata majibu yake ikiwa tutashindwa kutambua kwanza - Sisi tumetoka wapi na yapi yalikuwa malengo yetu! Kwa kifupi tumetoka wapi na tunakwenda wapi!..Nini madhumuni ya ubunifu wa falsafa ambayo ingetuongoza kama dira katika kila hatua ya maendeleo yetu. Nje ya hapo Uhuru kwa mwafrika utakuwa hauna tofauti kabisa na mabadiliko ya sura ya mtawala. Kiongozi mwafrika ni binadamu mwenye tamaa na hisia zote za kibinadamu kama watawala wengine na kuna kila sababu ya mtawala mwafrika kuwa mbaya sawa ama zaidi ya mtawala mgeni. Kwani mtawala mgeni hutegemea zaidi nguvu ya silaha kuendesha utawala wake wa mabavu, wakati mwenyeji anaweza jificha chini ya rangi yake kama mbwa mwitu aliyevaa ngozi ya kondoo.
Umaskini wa mwafrika ni maradhi ya kujitakia na yawezekana kabisa kuwa UHURU wetu umetafsirika vibaya toka mwanzo hivyo kupoteza kabisa dira ya uhuru huo. Hii vita kubwa ya kumkomboa mwafrika ktk Umaskini itawezekana tu ikiwa sisi tutaweza kutambua dira na malengo yetu na wapi tumekwama. Na Katika kuyatazama hayo ndipo tutaweza kuweka maazimio mapya, maazimio ambayo yataambatana na uboreshaji wa KATIBA katika vitengo muhimu vya UTAWALA, SHERIA na UWAJIBIKAJI kulingana na hitlafu zitakazo jitokeza.
Katika kifungu hiki nitazungumzia zaidi dira ya kitaifa kwa kuzingatia zaidi msukumo uliotufanya sisi kuchagua dira ya kitaifa baada ya uhuru kuwa ya UJAMAA na KUJITEGEMEA.
1. UJAMAA ikiwa na maana ya ujenzi wa UMOJA wa Watanzania wote ktk maendeleo na usatawi jamii hiyo.
2.KUJITEGEMEA ikiwa na maana ya ujenzi wa Uchumi wetu ili kutupa uwezo wa kuendesha maendeleo yetu bila kutegemea misaada toka nchi nyingine.
Haya ni maelezo ya uchache kama sababu za kimsingi ambazo zimetokana na historia ya nchi yetu, historia ambayo imetufanya tujifunze mengi mabaya na mazuri chini ya utawala wa mkoloni. Na kutokana na sababu hizo tulipata msukomo wa kupitisha dira hii ya kitaifa ambayo tuliijengea maazimio na mikakati ili tuweze kwenda mbele kama taifa huru. hayo Maazimio na Mikakati kwa kiasi ilitusogeza mbele lakini ilifika mahala tukakwama, hazikuweza kuzaa matunda tena kitaifa tofauti na madhumuni yaliyotangulia. Hapa nikiwa na maana kwamba kwa kiasi kikubwa Tanzania iliweza kujenga nguzo za ujenzi wa UJAMAA kiasi kwamba Tanzania ilikuwa moja ya nchi chache maskini duniani zilizosimamisha UJAMAA wa kweli baina ya wananchi wake lakini tulikuja shindwa baada ya nguzo hizo kuanza kuachia kutokana na kutokuwa na msingi mzuri wenye uwezo wa kubeba uzito wa jumba zima la UJAMAA na KUJITEGEMEA. Kushindwa kwa nguzo hizi kusimama, kumetokana na uzito mkubwa uliobeba kipengele cha pili cha dira yetu yaani KUJITEGEMEA. Kipengele ambacho wakati wote hakikupewa muda kutazamwa kwa makini zaidi ama kutenganishwa na imani yetu ktk siasa zilizokuwa zimetawala dunia. Ujamaa badala ya kuwa ni UMOJA wa wananchi wake ktk maendeleo ya pamoja ukajengwa kwa kuiga kiutendaji itikadi za wageni zenye malengo ya kujenga ama kuboresha bado uchumi wa dola zao. Baada ya Wakoloni kuondoka, mfumo mpya wa kiutawala ulivumbuliwa, utawala ambao ulizua falsafa mpya ya ujenzi wa makoloni ya kiuchumi kwa njia ya mawasiliano badala ya dola ama milki lakini bado nchi za kiafrika na nyingine maskini ziliendelea kuwa tegemezi wa falsafa za utawala huo wa Kibepari na Kimmunist.
Ukitazama kwa makini utakuta kwamba Wamarekani, Warusi, Wajarumani, Wareno, Wahispania, Wajapan, Wachina na Waingereza wote walisimama kama mataifa yenye kutaka kutawala, kudumisha na kulinda tawala zao nje ya mipaka yao kwa kutumia mawasiliano ya kiuchumi ambayo haitofautiani na dhumuni la mwanzo la dola ya mkoloni ambalo lilikuwa ni uwezo wao kumiliki uchumi wa nchi nyingine kwa kuweka utawala wa dola ndani ya nchi hizo kuhakikisha mafao ya nchi hizo yanarudi kujenga nchi zao.
Hii ndiyo azma kubwa ya siasa zote za nchi za Ulaya, azma ambayo ilikuja zua vita kubwa baina yao wakitutazama sisi kama ngo'mbe jike linalohitaji fahari wa kumiki zizi. Kila fahari akaingia na rangi zake, makeke na kila vitisho ambavyo vinaweza kumvutia ngo'mbe jike. Ni tofauti hizi za umilikaji wa uchumi nje ya mipaka yao ndio chanzo kikubwa kilichowasha vita zote kuu za dunia. Tofauti ambazo sisi tulikuja kuzikumbatia na kuzitangaza kwa kuzipigia debe hali misingi ya ujenzi wa rasimu na hata ilani yake haikuwa kwa manufaa ya nchi zetu au kuboresha mazingira yetu bali sisi kutumiwa kama watumishi watawaliwa mithiri ya mchwa wanavyojenga makazi yao kwa manufaa ya malkia. Ukimwondoa malkia mchwa hana maisha tena kwa hiyo uhai wake unategemea kuwepo kwa malkia ambaye ni unique ktk kizazi.
Tanzania na baadhi ya nchi maskini tukajikuta tukifuata mkondo wa Urusi bila kufahamu kwamba wao walijenga itikadi hii pingamizi kwa nchi za magharibi wakati wakizitawala nchi zote za USSR na ulaya ya mashariki kiuchumi na hata China wakizitawala nchi nyingi za Asia ya mbali kiuchumi. Kwa kifupi Ujamaa na Ubepari ni mifumo ya kiuchumi iliyojengwa ktk mazingira ya kuboresha nchi zao wakizitumia nchi maskini kama shamba la kuvuna kwa mapana ya mipaka kulingana na mbegu za kisiasa walizopandikiza. Ni katika kuiga hizi siasa Maazimio yasiyo kuwa na hesabu yalijengwa kwa kupotosha madhumuni yaliyotangulia kabla na baada ya uhuru. Matokeo yake tulipoteza kabisa dira na malengo yetu ya awali na kujitwika utumwa wa fikra za kupachikwa ambazo zimedumu hadi leo hii.
Tanzania imebaki kama uwanja mtupu uliojaa tope bila nyasi baada ya vita ya hao mafahari ambao bado hadi leo hii wanatafuta mabaki ya nyasi ktk malisho yao. Vita ya kwanza ya dunia na ile ya pili, zote zilitokea nchi zetu zikiwa bado chini ya utawala wa mkoloni isipokuwa vita hii baridi ya kisiasa kati ya Marekani na Urusi ndio vita pekee ambayo nchi zetu za kiafrika zimeweza kuusikia uzito wake kiuchumi kwa sababu vita hiyo imetukuta tukiwa huru na wenye kuwajibika ktk maendeleo ya nchi zetu. Matokeo ambayo yamekuwa jaribio jipya kwa nchi yetu kiasi kwamba tunadiriki kudai kuwepo kwa mabadiliko ya kiuchumi duniani hali ukweli umesimama kuwa ni mabadiliko ya kisiasa yaliyotangulia mabadiliko ya kiuchumi. Misingi ya kiuchumi iliyotumika zamani bado ni ile ile toka mkoloni isipokuwa hatukuchukua muda kutafakari mchango wa siasa hizo ktk uchumi wa nchi maskini kama kikwazo kikubwa kilichopotosha malengo ya awali ktk kudai uhuru wetu. Pamoja na mabadiliko yote, misingi ya kiuchumi bado inaendelea kutazama maslahi ya nchi za Ulaya. Hakuna tofauti kubwa za Kiuchumi kwa nchi maskini kati ya Ukoloni wa kilowezi na Ukoloni mamboleo ila mabadiliko yote ya kiuchumi yalitokana na ukweli kwamba nchi nyingi zilizokuwa zimetawaliwa kuwa huru. Sheria na masharti ya biashara yalipanuliwa zaidi kutokana na kuongezeka kwa teknologia na hasa kulinda soko kubwa la nchi hizo. Hata hivyo bado nchi maskini tunatumiwa kama tulivyokuwa tukitumiwa wakati wa Mkoloni, wakati wa vita baridi na leohii ktk mfumo mpya wa Ukoloni mamboleo.
Huko ndiko tulikotoka!..
Haya waungwana nasubiri dondoo zenu kabla sijaendelea! nadhani mnaelewa naelekea wapi mjamaa miye!