Majangaaa Mbona Majangaaa! - 34-
"Hujui?"
"Sijui…" alijibu Eddy
"Mbona inaonekana kama vile umetoka kufanya kazi muda si mrefu?"
"Sikuelewi…" alijitetea Eddy.
"Unaonekana kama vile ulikuwa bafuni…"
"Ndiyo…"
"Lakini mbona nimewaona yule mtoto wa mwenye nyumba na Pat nao wakitoka bafuni?"
"Miye nilitoka kabla yao," alijitetea Eddy.
"Siyo kweli… miye nilitoka kukuangalia barazani hukuwepo, nikaja chumbani kwako, hukuwepo…nikaenda uani ndipo nilipowaona wao wakitoka kisha nikahisi mtu akitoka bafuni, nadhani ulikuwa wewe…" alisema Rehema.
Moja kwa moja Eddy akatengeneza picha kichwani mwake, akaamini kwamba mwanamke huyo alikuwa sahihi katika maongezi yake.
Lakini siku zote Eddy alikuwa amejifunza kitu kimoja tu, kukataa kitu chochote ambacho kingeweza kumfanya mtu amfikirie vibaya.
"Sasa kama umewaona wao wananihusu nini mimi?"
"Siyo kukuhusu, inawezekana ulikuwa nao bafuni…"
"Umenichoka sasa…" alisema Eddy huku akionesha hasira usoni mwake na kutoka katika mikono ya Rehema, akasimama na kuvaa bukta yake.
Ilimbidi kufanya hivyo ili kuweza kukwepa kuingia msambweni na Rehema kwa kuwa alihisi msichana huyo hakuwa na lingine zaidi ya wivu na kutaka kutimiziwa jambo hilo.
Aidha Eddy alifikiria kwamba asingekuwa na nguvu za kupiga naye shoo kwa kuwa muda mchache alikuwa ametoka kugonga shoo za nguvu.
"Sasa unaenda wapi?" Rehema aliuliza kwa jazba.
"Nitakaaje na wewe ambaye unanihisi vibaya hata kwa vitoto vinavyonuka haja ndogo?"
"Siyo hivyo, nilikuwa nikihisi tu kutokana na mazingira na wewe hujaniambia ulikuwa wapi mpenzi wangu…" Rehema alianza kupunguza wasiwasi wake.
"Sawa ndiyo unihisi na vile vitoto?"
"Basi rudi nikwambie kitu kingine."
"Kuhusu nini?"
"Kuhusu Queen, roho ya Eddy ikashtuka na kutaka kujua kuhusiana na msichana huyo.
"Kafanya nini?"
"Nilijua lazima hilo hutataka kulisikia tu."
"Tatizo lako wewe wivu umejaa, unanihisi kila mtu ni halali yangu… ndiyo maana unaniudhi," Eddy alitengeneza ndita za uongo usoni mwake.
"Basi usikasirike, ni kwamba Queen amekuja na mwanaume wake… wako chumbani kwao…"
"Mimi inanihusu nini?"
"Si mpenzi wako?"
"Mpenzi wa nani? Miye sijawahi hata siku moja kutoka na Queen wewe mawazo yako yanakutuma vibaya," alisema Eddy na kutoka nje.
Moja kwa moja, Eddy alitoka hadi barazani na kuwakuta Muddy na Queen wakiwa huku baada ya kutoka chumbani kwa msichana huyo.
Queen alipomuona Eddy akafurahi na kuona ni sehemu ya kuweza kuweka mambo yake sawa, akamwita na kumtambulisha kwa Muddy.
"Huyu ni shemejio anaitwa Eddy ni mgeni hapa nyumbani kwetu, anakaa chumba kile cha mwisho..." Queen alitoa utambulisho huo mfupi.
"Sawasawa nimefurahi kukufahamu bwana Eddy…" alisema Muddy.
"Na huyu ni Muddy, ni mpenzi wangu wa muda mrefu sana, hapa katikati alipotea kutokana na kuzuzuliwa na wasichana wa mjini," Rehema alimtambulisha Muddy kwa Eddy.
"Sawasawa, nami nimefurahi kukufahamu bwana Muddy karibu sana kwetu… ndiyo tumeanza maisha…" alihitimisha Eddy huku akishikana mkono na Muddy.
Wakati hayo yakiendelea Rehema alishatoka ndani na kushuhudia utambulisho huo.
Akabaki akishangaa na kujiuliza maswali mengi kama kweli Queen hajawahi kutembea na Eddy.
Siyo yeye peke yake, hata Pat, Mwamvita na Tabu nao walikuwa barazani hapo wakishuhudia kitendo hicho.
Wote walibaki midomo wazi, wakashangaa kwa nini Eddy anakubali kutambulishwa kwa mwanaume mwenzake.
Wote hao walikuwa na uhakika wa asilimia mia kwamba Eddy alishatembea na Queen, Pat mdogo wake Queen alijua hivyo, Mwamvita alijua hivyo na hata Tabu alilijua hilo.
Mbali na kujua hivyo, wote walikuwa wakijua kwamba tayari walishatembea na mwanaume huyo, maswali yakawavagaa akilini mwao na kushindwa kupata jibu.
Walikuwa wakijiuliza kwamba, Eddy alikuwa akikubali kutoka moyoni au alikuwa akiigiza?
Pamoja na Rehema naye kujua kwamba aliingia katika ugomvi na Queen kwa sababu ya Eddy lakini kidogo alifarijika na kuamini kuwa mwanaume huyo alikuwa mkweli.
Hakuona sababu ya kumhisi Eddy vibaya, aliamini kwamba kama Eddy angekuwa ametembea na Queen asingekubali kutambulishwa kwa mwanaume mwenzake.
Hapohapo Rehema akawa mpole, akafuta mawazo yote mabaya juu ya Eddy.
Akahisi hata kuhusu wale watoto, Pat na Mwamvita zilikuwa ni hisia zake tu.
Akapanga kuondoa tofauti zake na Queen huku akidhamiria kumuomba msamaha kwa ugomvi wao wa siku za nyuma.
"Eddy…" Rehema hakutaka kulaza damu hapohapo akamwita mwanaume huyo.
"Unasemaje?"
"Twende ndani tukaongee," alisema Rehema huku akimvutia ndani mwanaume huyo. Bila kinyongo Eddy akamfuata kama vile mbwa anavyomfuata chatu.
Kitendo hicho kilimfurahisha sana Queen kwa kuona kuwa ameweza kuwahadaa wote waliokuwa wakimfikiria vibaya juu ya Eddy, akatoka kumsindikiza jamaa yake.
"Samahani mpenzi wangu?" Rehema alijikuta akisema mara baada ya kuingia chumbani na Eddy.
"Samahani ya nini?"
"Kwa jinsi nilivyokuwa nikikufikiria vibaya, naomba unisamehe juu ya Queen..-."
"Ni hilo tu?" Eddy alihoji
"Na mengine yote nayo naomba unisamehe…" Rehema alijikuta akiwa mtumwa ghafla wa kufuta mawazo yake na kusadiki mawazo ya mtu mwingine.
"Na kuhusu Queen?" Eddy alisema huku akimkazia macho Rehema.
"Hata yeye niko radhi kumuomba msamaha pia…" alisisitiza.
Nini kiliendelea? Usikose kusoma Jumatatu.