Mauaji yaliyojaa utata

“Ni lazima twende huko, ni lazima huyu muuaji apatikane. Wasiliana na polisi wa Cambridge, inawezekana hayupo huko ila ni lazima tuweke mitego, mbali na hivyo, pelekeni picha zake kila kona, kwenye vituo vya habari na sehemu nyingine. Gideon, hakikisha mtu huyu anapatikana,”



Ahsante madame@S

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI
MAUAJI YALIYOJAA UTATA
Sehemu ya Kumi na Tisa.
Mauaji yale, yalikuwa yaleyale ambayo yalitokea kwa masupastaa waliopita. Walikufa vilevile, wengi walihisi kwamba walijidunga madawa ya kulevya lakini baada ya miili yao kuchunguzwa, wakagundua kwamba kulikuwa na mtu aliyeitwa Benjamin ambaye ndiye alikuwa amehusika katika mauaji yale.
Hawakujua kuhusu Paul lakini bado mioyo yao iliwaambia kwamba inawezekana muuaji alikuwa huyohuyo ambaye mpaka kipindi hicho hakuwa amepatikana japokuwa alitafutwa sehemu yote nchini Marekani.
Kuna watu wengine walihisi kwamba Benjamin aliondoka na kukimbilia Mexico, nchi iliyokuwa na wauzaji wengi wa madawa ya kulevya. Hakukuwa na dalili za kupatikana kwake, kila watu walipokwenda huku na kule, hawakupata kitu.
Taarifa juu ya kifo cha Paul zikaanza kutangazwa kila sehemu, watu waliambiana kwenye mitandao ya kijamii, kila mtu aliyezipata, hakuamini kama kweli aliyekuwa ameuawa alikuwa Paul, yule mcheza kikapu mwenye jina, sura nzuri aliyekuwa akifagiliwa na wasichana wengi.
“Hebu tuambie nini kilitokea,” alisema ofisa wa FBI ambaye alikuwa katika chumba cha mahojiano na msichana Maria ambaye muda wote alikuwa akilia tu. Pembeni mwa ofisa huyo, alikuwepo mwingine ambaye naye alivalia suti kama aliyokuwa nayo.
“Sikumuua Paul,” alisema msichana Maria huku akiyafuta machozi yake.
“Nini kilitokea?”
Hapo ndipo Maria alipoanza kusimulia kile kilichotokea, hakutaka kuficha kitu, alikamatwa na kitu pekee ambacho kingemuweka huru kwa wakati huo ni kuzungumza ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
“Kwa hiyo muuaji haumfahamu?” aliuliza ofisa mmoja.
“Hapana! Simfahamu kabisa.”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
Polisi hawakutaka kumuachia Maria, ilikuwa ni lazima kumshikilia kwani mshukiwa namba moja wa mauaji yale alikuwa yeye, akawekwa sero, huko, alikuwa akilia sana, alijuta hatua aliyochukua ya kuwa na Paul na kwenda naye katika hoteli ile.
Hapo ndipo lilipokuja jina la Benjamin. Aliwahi kusikia mastaa wengi wakiwa wameuawa na mtu aliyeitwa Benjamin, hakumfahamu mtu huyo na hakujua sababu iliyomfanya kuwaua mastaa. Alimchukia Benjamin ambaye kwa kipindi hicho, alikuwa adui wa nchi nzima, yaani Enemy of the State.
****
Walipanga kwamba siku inayofuata ilikuwa ni lazima kwenda kituyo cha polisi na kuwaeleza polisi juu ya kile kilichokuwa kikiendelea. Benjamin hakuwa muuaji, hilo ndilo ambalo lingeweza kuzungumzwa kwani pasipo kufanya hivyo, Benjamin alikuwa katika wakati mgumu.
Tayari Benjamin na Harry waliwasiliana na David na kumwambia juu ya kile kilichotakiwa kufanywa, yaani piga ua ilikuwa ni lazima wakutane katika kituo cha polisi kwani yeye ndiye alikuwa na mawasiliano ya Bwana Seppy, Dracula na watu wengine katika upangaji wa mipango yao ya mauaji.
Wakakubaliana lakini ilipofika saa nne usiku wakapata taarifa zilizowashtua kwamba supastaa wa mchezo wa kikapu, Paul McKenzie alikuwa ameuawa ndani ya chumba cha hoteli, mauaji yake yalikuwa yaleyale, yaani kama Todd, Carter.
Walichanganyikiwa, hata kama majibu ya vipimo vya mwili ule havikutolewa, walijua fika kwamba taarifa zingesema kwamba Benjamin ndiye aliyeua, yaani kama ilivyokuwa katika mauaji mengine.
Hilo ndilo lililowafanya hata ule mpango wao wa kwenda kituo cha polisi kuusitisha, ilitakiwa wajipange upya wajue ni kitu gani wangetakiwa kufanya kwani pasipo kufanya hivyo, mambo yangekuwa mabaya zaidi.
“Tufanye nini?” aliuliza Harry.
“Dah! Hapa nimechanganyikiwa. Hebu subiri kwanza, naomba dakika kama tano hivi peke yangu,” alisema Benjamin huku akionekana kuwa na mawazo mengi.
Harry akamuacha, Benjamin akasimama na kwenda chumbani, alihitaji muda wa kuwa peke yake kwani kulikuwa na mengi ya kujifikiria, hakutaka kukurupuka katika kufikiria ni kitu gani alitakiwa kufanya.
“Nini cha kufanya?” alijiuliza huku akitembea huku na kule.
Alikuwa akiishi kwa hofu, hakuwa na amani, alijua kwamba kila kitu kilichokuwa kikitokea, Bwana Seppy alijua kwamba ilikuwa siri, kwa sababu yeye mwenyewe hakuwa na furaha, ilikuwa ni lazima hata Bwana Seppy naye akae akiwa na hofu kama alivyokuwa yeye.
“Umefikiria nini?” aliuliza Harry baada ya kukaa kwa dakika kumi nzima.
“Sioni sababu ya Bwana Seppy kuwa na furaha na wakati mimi nina hofu, kwa nini naye asiishi na hofu moyoni mwake?” aliuliza Benjamin.
“Unamaanisha nini?”
“Nataka niwasiliane naye!”
“Ben! Umechanganyikiwa?”
“Hapana! Hii ni njia ya kwanza, lazima akae kwa presha, ajue kwamba ninajua kila kitu, yaani hapo ndipo tutafanikiwa, kwanza tutakusanya ushahidi wa kutosha kwani atafanya maamuzi ya ghaflaghafla kitu ambacho kinaweza kuwa ushindi mkubwa,” alisema Benjamin.
“Umefikiria nini mpaka kusema hivyo?”
“Wala usijali! Nipe muda, nataka kwenda kumpigia simu, nitatumia simu ya barabarani,” alisema Benjamin.
Jambo alilozungumza halikumuingia akilini kabisa, hakujua alimaanisha nini, hakuona kama kulikuwa na sababu ya kufanya kile alichotaka kukifanya ila kwa sababu yeye mwenye mhusika ndiye aliamua kufanya hivyo, hakuwa na jinsi.
Alichokifanya Benjamin ni kuchukua namba ya simu ya Bwana Seppy na kisha kuondoka nayo kwenda mtaani. Kwa sababu ilikuwa usiku wa saa tano hakukuwa na mtu yeyote aliyemtambua kwani mbali na mwanga hafifu pia alivalia kofia kubwa aina ya pama.
Hakutaka kutumia simu ya mtaani hapo, alijua kwamba mara watakapogundua simu ambayo ilitumika ilikuwa ni lazima kumtafuta kuanzia hapo. Alichokifanya ni kupanda basi na kwenda katika mji mwingine ambao ulikuwa mbali na hapo, kama kilimeta thelathini kutoka hapo.
Huko ndipo alipotafuta kibanda cha simu za mitaani, alikipata katika kituo cha mafuta cha Total, akakifuata na kuanza kupiga namba ya Bwana Seppy. Wala simu haikuita muda mrefu, ikapokelewa.
“Bwana Seppy hapa, nani mwenzangu?”
“Benjamin Saunders...” alijitambulisha Benjamin, Bwana Seppy aliyekuwa upande wa pili, akashtuka.
****
Bwana Seppy akahisi kama mtu akija kumkaba kooni mwake, alichanganyikiwa sana kusikia sauti ya Benjamin, mwanaume aliyekuwa akimsumbua katika kipindi chote hicho, mtu ambaye alitaka afe haraka iwezekanavyo.
Mwanaume huyo alizungumza kwa kujiamini, hakuonekana kuwa na wasiwasi wowote ule mpaka wakati mwingine Bwana Seppy kuhisi kwamba Benjamin alikuwa na ulinzi wa kutosha huko alipokuwa.
“Ni lazima ufungwe maisha yako yote, ni lazima unyongwe kwa mauaji unayoendelea kuyafanya,” alisema Benjamin kwa sauti ya juu iliyosikika vizuri masikioni mwa Bwana Seppy.
“Hahaha!” akabaki akicheka.
“Cheka, ni vizuri kucheka kwa sababu siku ya hukumu yako inakaribia,” alisema Benjamin.
“Nani atajua? Wewe ndiye muuaji, vipimo vya madaktari na polisi vimeonyesha alama za vidole vyako, unahisi nani atakuamini?” aliuliza Bwana Seppy kwa dharau.
“Uwepo wa fedha katika kila tukio!”
“Hilo linaweza kuwa ushahidi tosha?”
“Ndiyo!”
“Zina maana gani?”
Benjamin hakutaka kuchelewa, hapo ndipo alipomwambia mzee huyo maana ya fedha zile zilizokuwa zikiwekwa katika kila eneo la tukio la mauaji lilipofanyika.
Bwana Seppy akachanganyikiwa, hakuamini kama kungekuwa na mtu ambaye angegundua kile kilichokuwa kimetokea kwamba Benjamin agundue maana ya uwekaji wa fedha zile.
Hilo lilikuwa jambo la kwanza ambalo hakutaka mtu yeyote afahamu, si mke wake, hata Dracula mwenyewe ambaye alikuwa akimtumia katika mauaji hakumwambia maana ya kuweka fedha zile katika kila tukio la mauaji aliyokuwa akiyafanya.
Hakutaka kuzungumza kitu, alichokifanya ni kukata simu na hapohapo kumpigia simu Dracula, kitu cha kwanza kabisa kumuuliza ni mahali gani walipofikia tangu waanze kumtafuta Benjamin ambaye bado aliendelea kutafutwa kila kona.
“Ndiyo tunaendelea, kuna nini kwani?” aliuliza Dracula.
“Amenipigia simu!”
“Amekupigia simu?”
“Ndiyo! Hebu niambie ukweli! Hivi atapatikana kweli?” aliuliza Bwana Seppy, kwa kumsikiliza tu, alinekana kuchanganyikiwa, hakuwa sawa kama siku nyingine.
“Atapatikana tu! Tuvute subira.”
****
Baada ya kuzungumza na Bwana Seppy na simu kukatwa, Benjamin akatulia huku akimwangalia Harry, alikuwa akitabasamu tu, mbele yake aliyaona mafanikio makubwa, alikuwa akifanikiwa kwa kila kitu alichokuwa akikifanya.
Walichokifanya, usiku huohuo ulikuwa ni wa kutoka na kwenda katika kituo cha polisi, huko, wangezungumza ukweli juu ya kile kilichotokea kwani tayari ushahidi walikuwa nao.
Wakatoka na kuanza safari ya kwenda huko. Japokuwa walikubaliana kwenda huko saubuhi lakini wakaiona mbali, ilikuwa ni lazima ifanyike siku hiyohiyo.
Walitembea mitaani, Benjamin hakutaka kuuficha uso wake kwani hata kama angekamatwa, bado alikuwa akienda kituo cha polisi. Walipishana na watu wengi, cha ajabu kabisa watu hawakumgundua kutoka na mwanga hafifu hasa katika kipindi hicho cha usiku.
“Tukifika, ni kutoa maelezo, hata kama nitapelekwa mahakamani, nitaeleza ukweli,” alisema Benjamin huku wakiendelea kwenda huko.
Walitembea kwa mwendo wa haraka, wakati wakikaribia kufika, simu ya Harry ikatoa mlio kwamba kulikuwa na ujumbe ulikuwa umeingia, harakaharaka akaichukua simu yake na kuangalia nini kilikuwa kimeingia, ilikuwa ni habari iliyoingizwa kutoka katika programu ya Shirika la Habari la CNN ambayo ilieleza kwamba kulikuwa na mauaji yalikuwa yametokea katika Hoteli ya Scandnavia Hill.
“Hebu subiri...” alisema Harry.
“Kuna nini?” aliuliza Benjamin.
“Paul McKenzie ameuawa,” alisema Harry, Benjamin akashtuka.
“Unasemaje?”
Hawakutaka kuendelea na safari, walichokifanya ni kwenda pembeni na kuanza kuisoma habari hiyo. Kwa jinsi mauaji yalivyotokea, walijua fika kwamba mzee huyo ndiye aliyehusika kwani mauaji yale yalifanana sana na yale mengine yaliyowahi kutokea.
Walibaki wakiangaliana tu, hawakujua ni kitu gani walitakiwa kufanya kwani kwa jinsi hali ilivyoonyesha, basi polisi wangeanza kumtafuta tena kwa nguvu kubwa.
Hawakuwa na sababu ya kuendelea mbele, safari yao iliishia hapo na hivyo kurudi nyumbani. Vichwani mwao walikuwa na mawazo tele, walijua fika kwamba mara baada ya mwili ule kupimwa, ilikuwa ni lazima alama za vidole vya Benjamin vionekane kwa sababu ndivyo Bwana Seppy alivyokuwa akifanya kwenye kila staa aliyekuwa akiuawa.
“Kwa hiyo tufanye nini?” aliuliza Hans.
“Subiri, nafikiri mpaka asubuhi nitakuwa na majibu, wala usijali,” alijibu Benjamin.
****
Msako mkubwa wa Benjamin ulikuwa ukiendelea, kamera ziliongezeka mitaani kwa ajili yake, ilikuwa ni lazima apatikane kwani kitu alichokuwa amekifanya, hakikuweza kuvumilika, ilikuwa ni lazima akamatwe na kufikishwa katika vyombo vya sheria na kuhukumiwa kwa yale yote aliyokuwa ameyafanya.
Maofisa wa FBI walikuwa wakihangaika, walitoa uangalizi kwa watu waliohusika na kamera mpya za barabarani ambazo walikuwa wamezifunga ili kuhakikisha Benjamin anakamatwa na mambo mengine kuendelea. Watu waliowekwa kwa ajili ya kuziendesha kamera zile, kila siku hawakuona kitu, waliendelea kufuatilia kwa wiki nzima lakini hakukuwa na mtu aliyeitwa Benjamini, yaani hata dalili zake kuwepo sehemu fulani, hazikuwepo.
“Na jana uliangalia?” aliuliza Bwana Swan, kiongozi aliyepewa kusimamia kamera hizo mpya ambazo zilifungwa sehemu nyingi nchini Marekani na taarifa kupelekwa moja kwa moja makao makuu.
“Ndiyo!”
“Na hamjamuona?”
“Ndiyo! Ila bado tunaendelea...”
Hivyo ndivyo alivyoambiwa. Wakati mwingine aliona kama hakukuwa na umuhimu wa kuwa na watu hao kwani alijitahidi kuwapa maneno mengi ya kuwafanya waone kwamba kulikuwa na umuhimu wa kumkamata mtu huyo lakini hiyo wala haikusaidia kabisa.
Ilimuumiza, hakupenda kuwasimamia watu ndiyo kazi ifanyike, kwa kumwangalia, alionekana kuwa mwanaume mpole, na hivyo ndivyo alivyokuwa ila alipotaka kitu fulani kifanyike, alikuwa kwenye presha kubwa sana.
“Hebu angalieni kamera vizuri, haiwezekani sehemu nzima asionekane,” alisema Bwana Swan.
“Sawa mkuu!”
Hakukuwa na kitu kilichobadilika, yaliendelea kuwa yaleyale kwamba Benjamin hakuonekana. Hawakujua alikuwa watu, ilikuwa vigumu sana mtu kutafutwa na nchi nzima, FBI halafu asionekane, hilo lilikuwa jambo gumu sana.
Wakati mwingine walihisi kama Benjamin alikimbia nchi, akaenda kujiunga na kundi la Kiislamu la ISIS, wakati mwingine waliisi kwamba Benjamin alikwenda kujiunga na Kundi la Born To Kill la nchini Cuba, yaani kumkosa Benjamin nchi nzima lilikuwa jambo lisilowezekana kabisa.
“Bosi...njoo uone hii,” alisema kijana mmoja, alikuwa mbele ya kompyuta yake, tangu asubuhi hakuwa ameondoka ofisini, yeye ndiye aliyepambana kwa nguvu zote kumtafuta Benjamin kila kona.
Alianzia jijini New York, akaenda Washington, akaenda Los Angeles na sehemu nyingine kwa kutumia kamera zilizowekwa lakini kote huko hakuambulia kitu.
Dakika za mwisho kabisa, alimuona mtu kama Benjamin, alipouona uso wake, akatafuta picha ya Benjamin na kuambatanisha na picha ile aliyoiona kwenye kamera, maneno yaliyotokea ni 100 MATCH, yaani imefanana kwa asilimia mia moja, hapo akajiona kuwa mshindi, ilikuwa ni lazima kumpa taarifa Bwana Swan.
JE, nini kitaendelea?
Suala la internet limekuwa chachu lakini pia nipo bize kuandaa kitabu changu ambacho nakamilisha hatua za mwisho-mwisho.
Nadhani hii ndiyo itakuwa hadithi yangu ya mwisho kuandika mitandaoni, sitoandika tena bali nitakuwa natoa vitabu tu. Kama ambavyo mmekuwa mkiniunga mkono tangu mwaka 2012 huku, basi tuendelee kuungana mikono hata kwenye vitabu vyangu ambavyo vitakuwa na simulizi ambazo hamjawahi kuzisoma.
Asanteni.
 
Madame mwambie mwandishi asiwaze, tutamuunga mkono kwenye vitabu. Wengine huu ndo ulevi wetu
 
NYEMO CHILONGANI
MAUAJI YALIYOJAA UTATA
Sehemu ya Ishirini.
“Yupo wapi?”
“Nawaona vijana wawili wakiwa wamesimama, mmoja yupo ndani ya kibanda cha simu na mwingine yupo nje, Benjamin ni huyu aliyekuwa ndani, aliyekuwa nje simfahamu,” alisema kijana huyo aliyejiita Genius.
Alichokisema Bwana Swan ni kuunganishwa kwa kompyuta ile katika televisheni kubwa iliyokuwa ndani ya chumba hicho huku akimtaka kila ofisa wa FBI aliyekuwa humo ndani aangalie kile kilichokuwa kikiendelea.
Sehemu iliyoandikwa Location ikiwa na maana ya eneo ilionyesha kwamba ilikuwa ni Macberth 25W, sehemu ambayo ilikusanya watu wenye maisha ya kati katika Jiji la Boston, huko ndipo ambapo huyo Benjamin alipokuwa.
Kumuona tu hawakuridhika, waliamini kwamba wangeweza kutorokwa kwani huyo Benjamin hakuwa mtu wa kawaida hata kidogo. Walichokitaka ni kumfahamu mtu ambaye alikuwa naye, alikuwa nani na alikuwa akiishi wapi.
Hiyo wala haikuwa kazi kubwa, alichokifanya Genius ni kuivuta sura ya Harry, akaruhusu sura kadhaa zianze kupita katika kompyuta yake huku ikiitafuta sura ya mwanaume huyo aliyekuwa pamoja na Benjamin.
Ilikuwa kazi kubwa, kila mtu aliyekuwa ndani ya jengo hilo alikuwa kimya, Bwana Swan alibaki akiwa amesimama, mkono wake mmoja ulikuwa mfuko na mwingine aliupeleka katika shavu lake, alikuwa akifuatilia kwa ukaribu sana.
Zaidi ya sura milioni mbili zilipita kwa kasi kubwa mno, ndani ya dakika ishirini, kompyuta ikasimama katika sura moja na kujiandika 100 MATCH kwamba sura ya mtu huyo ilifanana na huyu aliyekuwa ametafutwa.
“Ni nani huyo?” aliuliza Bwana Swan, jamaa mwingine akachukua kalamu na karatasi.
“Anaitwa Harry Hoff, kijana mwenye asili ya Ujerumani, anaishi jijini Boston, nyuma namba 278 katika Mtaa wa Vivien View Barabara ya St. Peters, anasoma katika Chuo cha Kikuu cha Harvard,” alisema Genius, maelezo ya wananchi wote wa Marekani, data zao zilikuwa zimechukuliwa kutokana na vitambulisho wa taifa walivyokuwa wamepewa.
“Safi sana...ninahitaji maofisa kumi waende huko anapoishi Harry. Hakuna kuua, mnachotakiwa ni kuwapata wote wakiwa hai,” alisema Bwana Swan na maofisa wote kuitikia na hivyo kuanza kwenda huko.
****
Vivian hakuwa na raha, moyo wake ulikuwa na majonzi tele, hakuamini kile kilichotokea kwamba mpenzi wake alikuwa akitafutwa kila kona huku sababu kubwa ikiwa ni kufanya mauaji.
Alijua kwamba hakuwa muuaji bali kulikuwa na mtu ambaye alifanya mauaji, hakumfahamu na hivyo ndivyo alivyowaeleza maofisa wa FBI lakini hakukuwa na mtu aliyemuelewa.
Aliruhusiwa kwenda nyumbani, hakukukarika, kila alipokaa, alimkumbuka mpenzi wake tu. Maofisa wa FBI hawakutaka kumuacha, walihakikisha wanamfuatilia kila hatua.
Nje ya nyumba hiyo kulikuwa na gari lao, ndani ya gari hilo kulikuwa na kompyuta nyingi pamoja na kamera zilizokuwa na uwezo wa kupiga picha na kuona kile kilichokuwa kikiendelea ndani.
Mbali na hivyo, waliendelea kufuatilia mpaka mawasiliano ya simu zake, kuanzia ile ya mezani mpaka ya mkononi kwani waliamini kwamba msichana huyo alikuwa na nafasi ya kuwasiliana na mpenzi wake ambaye alikuwa akitafutwa kwa udi na uvumba kipindi hicho.
“Nini kinaendelea?” aliuliza Bwana Swan ambaye aliwagawa vijana wake sehemu mbalimbali.
“Bado tunaendelea kufuatilia, tunamuwekea ulinzi wa kutosha huyu msichana wake,” alijibu ofisa mmoja.
“Simu zake?”
“Tumeziwekea ulinzi pia.”
“Sawa.”
****
Maofisa wa FBI wakaelekea nyumbani kwa Harry, walikwenda na gari lao, ilikuwa asubuhi sana muda ambao waliamini kwamba hata watu hao hawakuwa wameamka, walitaka kuwavamia na kisha kumchukua mtu wao ambaye aliwatesa sana huku usiku uliopita tu akiwa amefanya mauaji katika hoteli moja huko Los Angeles.
Walifika katika nyumba hiyo huku wakiwa na bunduki zao mikononi mwao, waliamini kwamba wangeweza kumpata kwani kwa jinsi walivyoona siku iliyopita, wawili hao wangeendelea kuwa ndani ya hiyo nyumba na ilionyesha kwamba kwa kipindi kirefu Benjamin alikuwa mahali hapo ila tu hawakuwa wakijua hilo.
Walipofika nje ya nyumba hiyo, kitu cha kwanza kabisa walichokifanya ni kuizunguka nyumba hiyo na ndipo mmoja wao akaanza kuugonga mlango na kutaka kufunguliwa.
Nyumba ilikuwa kimya, japokuwa alipiga kelele na kusema “FBI, FBI” lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyefungua mlango. Hawakutaka kuendelea kubaki hapo ndani, walikuwa na hofu kwamba inawezekana Benjamin angekimbia hivyo walichokifanya ni kuingia ndani ya nyumba hiyo kwa kuuvunja mlango.
Bunduki zilikuwa mikononi mwao, walioingia hawakuwa wao peke yao bali kulikuwa na askari wa SWAT ambao kazi yao ilikuwa ni kuvamia sehemu zilizokuwa na hatari, yaani kule ambapo kulikuwa na watu waliokuwa na silaha nzito, walitumika hao kwa ajili ya kuwalegeza kwanza.
Ndani, hakukuwa na mtu, walijaribu kuingia humu na kule, walitembea huku na kule lakini hawakukuta mtu yeyote. Mwisho kabisa wakaamua kukifuata chumba kimoja, kilikuwa chumba cha Harry, walipokifikia, wakaingia ndani, hawakumuona Benjamin, mtu pekee waliyemuona humo alikuwa Harry.
“You are under arrest....” (Upo chini ya ulinzi...) alisema ofisa mmoja huku wote kwa pamoja wakimnyooshea bunduki Harry ambaye aliamka na kuanza kuwaangalia.
“What the hell is going on?” (Nini kinaendelea?) aliuliza huku akiwaangalia.
Hawakutaka kumjibu swali lake, walichokifanya ni kumshika na kumlaza chini kisha kumfunga pingu huku wakimtaka kuwaambia mahali alipokuwa Benjamin.
“Benjamin, I don’t know where he is,” (Benjamin, sijui yupo wapi) alisema Harry huku uso wake ukionyesha tabasamu pana.
“Tell us where he is,” (Tuambie yupo wapi)
“I dont know men, he left last night,” (Sijui jamani, aliondoka usiku uliopita) alijibu Benjamin, kwa kumwangalia tu, alionyesha dhahiri kwamba aliwadanganya.
****
Benjamin alikuwa kama mtu mwenye machale, usiku wa siku hiyo hakulala, alibaki macho huku akiwa na wasiwasi mno, alijua kama kulikuwa na kitu ambacho kingetokea hivyo asingeweza kulala kabisa.
Alikesha, mpaka mwanga unaanza kuchomoza asubuhi, alikuwa macho, akatoka kitandani na kwenda jikoni ambapo akaandaa kahawa na kisha kuelekea sebuleni kuangalia televisheni.
Kipindi hicho televisheni ndiyo ilikuwa faraja yake, hakuwa na cha kufanya, hakuwa na uhuru wa kufanya kitu chochote kile, alipokuwa kwenye televisheni, ndiyo ulikuwa muda wa kujua kitu gani kilikuwa kikiendelea katika ulimwengu aliokuwa akiuogopa.
Mara kwa mara alijiona kwenye televisheni, alikuwa mtu maarufu kwa sababu ya matukio yaliyokuwa yametokea. Watu wengi walihojiwa, kilio chao kilikuwa ni kumuona Benjamin akikamatwa na kufikishwa mahakamani na kisha kushtakiwa kwa makosa ambayo dunia nzima ilijua kwamba aliyafanya.
“Ila kwa nini huyu mzee anafanya hivi?” alijiuliza pasipo kupata jibu.
Akasimama, akaanza kutembea ndani ya sebule ile huku akiwa na mawazo lukuki, aliongea peke yake kama kichaa, akatoka pale alipokuwa mpaka katika dirisha kubwa, akafungua pazia na kuanza kuangalia nje.
Alitamani kuwa huru, aliwaona watu wakitembea barabarani huku wakiwa wamejiachia, alitamani na yeye kuwa vile lakini ilishindikana kabisa, hakuweza kuwa huru kama watu wale walivyokuwa huru kipindi kile.
Wakati akiwa amesimama katika dirisha lile ndipo alipoliona gari moja likija na kusimama karibu na eneo la nyumba ile barabarani. Kwanza akaanza kuwa na wasiwasi, hakutaka kujipa uhakika kwamba watu waliokuwa ndani ya gari hilo walikuwa watu wazuri, akagundua kwamba kulikuwa na kitu.
Hakutaka kuwa na wasiwasi mwingi, akasubiri kuona ni watu gani wangeteremka kutoka ndani ya gari lile. Wakati akiwa amelikodolea macho, likatokea gari jingine ambalo kwa ubavuni liliandikwa S.W.A.T.
Harakaharaka wanajeshi waliokuwa na mavazi yaliyoandikwa S.W.A.T wakatoka ndani ya gari lile, walikuwa na bunduki kubwa hasa AK 47 ambazo ndizo zilikuwa maalumu kwa kazi yao.
Mavazi yao, yalikuwa yale mazito ambapo tumboni mpaka kifuani walikuwa na vazi jingine lililokuwa na uwezo wa kuzuia risasi. Benjamin alipowaona watu hao, hakutaka kusubiri, alijua fika kwamba walikuwa mahali hapo kwa ajili yake.
Hakutaka kujiuliza, wanajeshi wale na FBI tayari walianza kuelekea kule ilipokuwa nyumba ile, aliamini kwamba kama angekwenda jikoni na kutoka nje kupitia mlango wa nyuma, angechelewa na hivyo kukamatwa, wazo pekee lililomjia kichwani ilikuwa ni lazima aingie ndani ya ‘chimney’.
Sebuleni hapo kulikuwa na sehemu maalumu ambayo nyumba nyingi za Marekani na Ulaya au hata sehemu zenye baridi kali huweka kama jiko kwa ajili ya kuchoma kuni na kuleta moto ambapo moshi wake ulipita katika bomba kubwa lililokwenda juu ya bati na kupotelea huko.
Yeye alitaka kuingia katika bomba hilo, halikuwa kubwa sana lakini lilitosha kwa mwili wake kuenea kwani hakuwa mnene ila alikuwa mrefu. Hakutaka kuchelewa, haraka sana akaelekea katika sehemu ile, kulikuwa na kuni, akazisogeza pembeni na kisha kuanza kujiingiza, hakuanza kukiingiza kichwa, alibinuka na kuanza kuiingiza miguu yake kwenda kwenye bomba lile kwa juu.
Ilikuwa kazi kubwa lakini haikumsumbua sana, hakuchukua sekunde nyingi, akafanikiwa kuingia ndani ya bomba lile na kutulia, masikio yake yalikuwa ni hapo sebuleni, tangu maofisa wa FBI walipoanza kuugonga mlango na kuuvunja, yeye alikuwa ndani ya bomba lile sebuleni pale huku akisikiliza kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Maofisa wa FBI walijua fika kwamba Harry alikuwa akijua mahali alipokuwa Benjamin ila hakutaka tu kuwaambia ukweli. Walichokifanya ni kumchukua na kumpeleka kituoni.
Huko wakamuingiza ndani ya chumba cha mahojiano na kuanza kuzungumza naye, walitaka aeleze ukweli mahali alipokuwa Benjamin, vinginevyo wangemfanya kitu kibaya.
“Nina haki ya kusikilizwa pia,” alisema Benjamin kwani tayari aliona maofisa wale walikuwa wamekasirika.
“Sawa. Benjamin yupo wapi?”
“Sijui! Kwani nyie wa nini?”
“Amefanya mauaji!”
“Hapana! Benjamin hakuwahi kuua,” alisema Harry.
“Usibishane na sisi, aliua na hata jana aliua pia,” alisema ofisa huyo.
“Jana kuna mauaji yalitokea huko Los Angeles, wote mnasema kwamba Benjamin ndiye aliyehusika, si ndiyo?” aliuliza Harry.
“Ndiyo!”
“Sawa! Kwenye maelezo yenu mlisema kwamba jana usiku mliniona nikiwa naye, ilikuwa saa tano usiku, si ndiyo?”
“Ndiyo!”
“Mauaji yalitokea saa nne na nusu, si ndiyo?”
“Ndiyo!”
“Sasa jamani! Huyo Benjamin awe ameua saa nne na nusu usiku, atatumia usafiri gani kutoka Los Angeles mpaka hapa Boston kwa mwendo wa nusu saa? Kwa ndege haiwezekani, alitumia usafiri gani sasa?” aliuliza Harry huku akiwaangalia maofisa wawili aliokuwa nao humo ndani.
“Labda niwaulize kitu kimoja. Nyie mnaamini Benjamin ni yupi? Yule aliyefanya mauaji huko Los Angeles au huyu aliyekuwa pamoja nami?” aliuliza Harry. Maofisa wakabaki wakiangaliana tu.
Alichokisema Harry kilikuwa ni ukweli mtupu. Kutoka Los Angeles mpaka hapo Boston ilikuwa ni mwendo wa saa moja na nusu kwa ndege, sasa ilikuwaje huyo Benjamin afanye mauaji Los Angeles halafu ndani ya nusu saa aonekane jijini Boston? Hilo likawapa wakati mgumu maofisa hao, hawakujua washike lipi, kama Benjamin alionekana hapo Boston majira ya saa tano usiku, je aliyefanya mauaji saa nne na nusu usiku huko Los Angeles alikuwa nani? Wakabaki na maswali kibao.
****
Dunia ilikuwa ikijiandaa kwa ajili ya kumuona msichana mrembo ambaye angeibuka kidedea katika Mashindano ya Miss Dunia ambayo kwa kipindi hicho yalitegemewa kufanyika jijini Texas nchini Marekani.
Watu walitaka kushuhudia ni msichana yupi angeibuka mshindi kwani wasichana wote ambao walitegemewa kushiriki walikuwa wale warembo, waliowavutia watu wengi nchini mwao.
Kila mtu anawa na uhakika kwamba msichana Angelica Sanchez kutoka nchini Mexico angechukua taji hilo lililokuwa likishikiria na mrembo kutoka nchini Venezuel, Maria alejandro.
Kwa kumwangalia, Angelica alikuwa msichana mrembo mno, alikwenda juu, hipsi zake zilionekana vilivyo, alikuwa na sura nzuri uliopendezeshwa na vishimo viwili vilivyokuwa mashavuni mwake. Muda wote, alikuwa kwenye tabasamu pana kana kwamba hakujua maana ya kukasirika.
Huyo ndiye alikuwa gumzo kipindi hicho. Tangu alipochukua taji la urembo nchini Mexico, kila mtu alitokea kumpenda, kampuni mbalimbali zinazojihusisha na mambo ya mitindo ikamtafuta, yeye alijiona mrembo, watu wengine wakamuona mrembo lakini makampuni hayo yaliona fedha.
Walijua kwamba kama wangemtumia msichana huyo katika matangazo yao mbalimbali, wangepata fedha nyingi, hivyo wakaingia naye mikataba mingi kwa kutegemea kuwa angeweza kuchukua taji hilo.
Mbali na Angelica, pia kulikuwa na msichana aliyeitwa Jenny Chu, msichana kutoka nchini China, alikuwa mrembo, alisoma na kuwa na PhD ya udaktari, hakuangalia elimu yake, alichokuwa akikiangalia kilikuwa ni masuala ya urembo tu, tangu zamani aliwaahidi wazazi wake kwamba kuna siku angekuwa mrembo wa dunia, na muda huo, aliona ndiyo kipindi chenyewe.
Kulikuwa na wasichana wengi, japokuwa wengi waliwafikiria wasichana hao warembo lakini wakasahau kwamba mbali na wasichana hao kulikuwa na msichana mmoja aliyekuwa mrembo mno, inawezekana kuliko wote hao, msichana huyo aliitwa Stacie Lawrence.
Kwa kumwangalia msichana huyo kutoka nchini Australia, alikuwa mrembo haswa, sura ya kitoto, lipsi pana kidogo, macho ya goroli, shingo ya upanga, aliumbika, alijua kutembea, yaani kwa kumwangalia harakaharaka, ingekufanya kudhani kwamba umekutana na mzimu wa mwanamke mrembo kuliko wote, Cleopatra.
Stacie hakuwa mzungumzaji, alikuwa kimya, alionekana kama kuwa na wasiwasi, hakuonekana kujiamini kabisa. Alikuwa msomi, alikuwa na PhD ya mambo ya uandishi, alitamani kusoma lakini pia alipenda sana mambo ya urembo na huo ukawa ndiyo muda wake wa kukamilisha kile alichokuwa akikiota kila siku.
Alimuogopa msichana Angelica kwa kuwa alitangazwa sana, hakuwa na uhakika kama angeweza kushinda kinyang’anyiro hicho, kila wakati alipokuwa akimuona Angelica, alitamani kumsogelea na kumsalimia kisha kumwambia kwamba alitamani sana kuwa kama yeye.
Hakujua watu walimfikiria vipi. Wasichana wengi waliokuwa katika kinyang’anyiro hicho walimpa ushindi, alionekana kustahili hata zaidi ya Angelica ambaye mara kwa mara alikuwa akipigiwa promo kutoka sehemu mbalimbali.
Wasichana wengine wakashindwa kujizuia, walimsogelea na kumwambiia wazi kwamba alikuwa mrembo, kila msichana alitamani kuwa kama yeye lakini kila alipoambiwa, aliwajibu kitu kimoja kwamba inawezekana hawakumuona Angelica.
“Unajua wewe mzuri sana,” aliambiwa na msichana Priscilia, mrembo kutoka nchini Italia.
“Nani? Mimi?”
“Ndiyo! U mrembo sana...”
“Hapana! Labda hujamuona Angelica...”
“Nimemuona lakini wewe, hakika unastahili kuwa mshindi katika shindano hili,” alisema msichana Priscilia.
Kwa kumwangalia, alionekana kutokutania, alimaanisha kile alichokuwa akikizungumza. Hiyo haikuwa kwa msichana huyo tu, alipoondoka walimfuata wasichana wengine na kumwambia jinsi alivyokuwa mrembo.
Alipoambiwa, alijisikia aibu, hakujiamini hata kidogo. Kwa Angelica, tayari alianza kuona wivu, jinsi wasichana wengine walivyokuwa wakimzungumzia Stacie, moyo wake uliuma kupita kawaida.
Walikaa kambini huku wakiendelea na mazoezi kama kawaida, saa zilizidi kukatika, siku zikaenda mbele mpaka siku ya tukio kufika. Kila mtu alitaka kuona msichana Angelica akichukua taji hilo na kuwa mrembo wa kwanza kushinda kutoka nchini Mexico.
Wakati Angelica akiendelea kuwa gumzo ndipo watu wakafanikiwa kumona msichana Stacie. Kwanza kila mmoja akashtuka, hawakuamini kile walichokiona, hawakuamini kama kulikuwa na msichana mwingine mrembo hata zaidi ya Angelica ambaye alikuwa gumzo.
Mioyo ya watu ikaanza kubadilika, ikatoka kwa msichana Angelica na kuhamia kwa Stacie, watu wakaanza kumtafuta katika mitandao mbalimbali, picha zake, urembo wake ukawadatisha sana, hakukuwa na aliyeamini kama dunia hiihii ingekuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa Stacie.
Watu wakaanza kutumiana picha za msichana huyo katika mitandao ya kijamii, kila mtu aliyemuona Stacie katika picha zile, alitaka kumuona uso kwa uso kwani mioyo yao ilikataa kabisa kwamba katika dunia hiihii, kipindi hikihiki kungekuwa na msichana mrembo kama Stacie.
“Ni lazima nitakwenda kutazama kinyang’anyiro,” alisema jamaa mmoja, alikuwa ameshika simu yake akimwangalia Stacie.
“Si ulisema hauendi!”
“Nitakwenda, nimebadili mawazo,” alisema jamaa huyo.
Watu walitaka kuona ushindani mkubwa kutoka kwa wasichana wawili warembo, mmoja kutoka nchini Australia na mwingine kutoka nchini Mexico. Kila kona, wawili hao walawa gumzo, japokuwa kipindi cha nyuma Angelica alikuwa akizungumziwa sana lakini katika kipindi hicho upepo ukabadilika kabisa, hakuzungumziwa Angelica peke yake bali alizungumziwa Stacie, tena kadiri muda ulivyokuwa ukizidi kwenda mbele, aliendelea kusikika zaidi.
“Unahisi nani atachukua ushindi?”
“Mmh! Wala sijui manake nishanchanganyikiwa!”
Watu walisubiri mpaka pale kinyang’anyiro kilipoanza. Mwana huo, watu walifuatilia kinyang’anyiro hicho kuliko vipindi vingine vyote, kila kona, watu walikuwa wakifuatilia katika televisheni zao na kitu kilichokuwa kikiwavuta zaidi ni urembo wa wasichana hao wawili.
Vipengele vyote vikapita na mwisho wa siku mshindi kutarajiwa kutangazwa. Katika tatu bora alibaki Stacie, Angelica na mrembo mwingine kutoka Afrika Kusini, ThandiMbokani.
Ukumbi mzima ulibaki kimya, mtu aliyetakiwa kutangaza matokeo, akasimama, akachukua matokeo kutoka kwa majaji na kisha kusimama, hakuanza na mtu wa kwanza, alianza na mtu wa tatu.
Lilipotajwa jina la Thandi, kila mtu alikaa kimya, walilitegemea hilo, walijua kwamba msichana huyo angeshika nafasi hiyo na mbili za juu zingekuwa kwa hao warembo waliowafanya watu wengi kujaa ndani ya ukumbi huo.
Mtangazaji, hakutaka kutangaza kwa pupa, alitaka kila mtu awe na presha mahali hapo, kwanza akarekebisha tai yake, akajikoholesha, akafanya mambo mengi yasiyokuwa na msingi ili kuwafanya watu kuwa na presha ndani ya ukumbi huo.
Kila mmoja alikuwa akimwangalia, mapigo yao ya moyo yalikuwa yakidunda sana, wote walikuwa na mshindi wao mioyoni mwao, walitaka kumsikia mtangazaji huyo alikuwa nani kwani kama ni urembo, wote walikuwa warembo japokuwa msichana Stacie alizidi kidogo.
Je, nini kitaendelea
 
Back
Top Bottom