Makapuku Forum

Makapuku Forum

*LEO IWE SIKU YA MWISHO KWA KITI CHA SPIKA KUKANDAMIZA DEMOKRASIA NCHINI.*

*_By Malisa GJ,_*

Kwa muda mrefu sasa kiti cha Spika kimekuwa kikitumika kwa maslahi ya serikali. Mijadala mingi inayoonekana kuumiza serikali imekua ikizimwa bila sababu za msingi hata kama mijadala hiyo ina maslahi kwa taifa.

Bunge la 9 lililoongozwa na Samuel Sitta ndio bunge pekee ambalo kiti cha Spika kilikua imara, kikitenda kazi yake kwa haki bila woga wala upendeleo. Lakini bunge la 10 chini ya Anna Makinda lilionesha kupwaya na kiti kikijisahau na kujikuta kikifanya kazi za serikali.

Wengi walihoji tofauti ya kiti cha spika ktk bunge la 9 na bunge la 10, lakini mwandishi mkongwe Ndimara Tegambwage akatoa majibu kwny makala yake moja kuwa _"TULITAKA SPIKA TUKAPEWA MWANAMKE"._ Chama cha Mapinduzi kilikataa kuangalia sifa nyingine zote za muhimu wakaangalia jinsia. Hoja ikabadilika kutoka "Spika mwenye sifa na uwezo" ikawa "sasa hivi ni zamu ya mwanamke". Na ndipo alipopatikana Anne Makinda. Anyway; Ikawa usiku ikawa mchana miaka mitano ya Makinda ikapita.

Sasa ni bunge la 11 kiti kimeanza tena kufanya yaleyale ya bunge la 10. Kiti kinailinda serikali kuliko serikali inavyojilinda yenyewe. Hali hii imeanza kuwa kero kwa wabunge wa Upinzani na hata wale wa CCM. Labda ni kwa sababu Katiba ya sasa inaruhusi kiti kuamuliwa na serikali, ndio maana kinailinda.

Yani serikali ndio inaamua nani awe Spika na nani awe Naibu Spika, ndio maana kiti kinapwaya sana ktk kuhakikisha bunge linaisimamia serikali. Huwezi kumsimamia mtu aliyekuteua mwenyewe. Itz against cardinal principles of Law _(nemo judex in causa sua)_.

Ndio maana watu wanaikumbuka sana Rasimu ya Warioba maana ilipendekeza Kiti cha Spika kisitokane na chama chochote cha siasa. Leo tungekua na Spika ambaye sio CCM wala UKAWA wala chama chochote cha siasa pengine kungekua na nidhamu bungeni na haya tunayoyaona leo huenda yasingejitokeza.

Kwa muda mrefu kiti kimetumika kulinda chama tawala (CCM) na kulinda serikali (ya CCM) bila kujali maslahi ya nchi. Wahanga wakubwa wa maamuzi ya kiti wamekua ni wabunge wa upinzani, lakini leo wabunge wa CCM nao wameonesha mshikamano na kuweka maslahi ya taifa mbele kuliko maslahi ya chama chao. Kwa mara ya kwanza wabunge wa CCM wameanza kufikiri kwa maslahi ya nchi.

*Hoja Ya Wanafunzi wa UDOM*
Watu wengi wanaohoji nini kiini cha tatizo la wanafunzi wa UDOM? Wamefanya nini? Kwanini wamefukuzwa? Kwanini iwe usiku wa manane? Nini hatma yao?

*Majibu*
Mgogoro huu una historia ndefu kidogo. Miaka michache iliyopita aliyekua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Jakaya Mrisho Kikwete alizindua program maalumu ya kusomesha waalimu wa masomo ya sayansi ktk shule za sekondari nchini. Hii ilikua ni program maalumu ya kukabiliana na changamoto ya uhaba wa waalimu wa sayansi nchini.

Ilionekana kuwa wastani wa waalimu 8,000 wa masomo ya Sayansi wanaweza kusaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la ukosefu wa waalimu wa Sayansi nchini. Lakini hakukua na chuo cha waalimu chenye kuweza kudahili walimu wote hao. Hata wizara ingeamua kuwagawanya kwny vyuo vya ualimu vya diploma wasipata nafasi za kutosha.

Hivyo basi Rais Kikwete kwa kushirikiana na mamlaka ya Elimu (TEA), Tume ya vyuo vikuu(TCU), Mamlaka ya elimu ya ufundi (NACTE) na wadau wengine wakafikia maazimio ya kudahili wanafunzi hao chuo kikuu cha Dodoma baada ya kufanyika assesment na kuonekana nafasi zipo za kutosha wanafunzi wote hao.

Lakini ili kuepuka kupata walimu "wasio na sifa" serikali ikaset standards za udahili, kwamba itakua ni kwa wahitimu wa kidato cha 4 waliopata daraja la kwanza hadi la tatu (division 1 hadi 3) na pia wawe wana ufaulu wa alama "A" au "B" katoka masomo ya sayansi. .

Lakini je unawezaje kumshawishi Mwanafunzi aliyepata Division 1 au 2 aende kusomea Ualimu wa sayansi ngazi ya Diploma? Wengi wana malengo tofauti na wangependa kuendelea na kidato cha 5 na hatimaye chuo kikuu kama "priority number 1".

Kwahiyo serikali ikaona njia rahisi ni kuwapatia mikopo ya 100% wanafunzi hao na kuwaahidi ajira pindi wamalizapo masomo. Kwa hali hii wakafanikiwa kuwashawishi hasa wale watoto wa maskini wasio na uwezo wa kujisomesha "private". Hawa wajajikuta wamekua wahanga wakuu wa mfumo huu.

Wakakubali kujiunga na Program hii maalumu kwa kuwa wana uhakika watapata mkopo na wamehakikishiwa ajira baada kuhitimu. Lakini wale watoto wa vigogo waliofaulu kwa division 1 na 2 hawakua na muda wa kupoteza kwny programu hii. Wakaenda kidato cha 5 na 6 kwenye shule nzuri za binafsi zenye kulipiwa mamilioni.

Watoto wa mama Ntilie waliofaulu vizuri wakadahiliwa UDOM tayari kuianza safari yao ya kuwa waalimu _(Diploma in Education - Special Program)_. Program hii ilizinduliwa na Rais Kikwete kwa pesa zilizoombwa bungeni kisheria. Bunge liliridhia kuwasomesha vijana hao kwa gharama za serikali ili wakafundishe O-level katika shule za serikali ktk kulabiliana na changamoto ya walimu wa Sayansi nchini. Programu hii ilienda vizuri tangu kuanzishwa kwake hadi serikali ya Magufuli ilipoingia madarakani.

*Kiini cha Mgogoro*
Serikali ya Magufuli ilipoingia madarakani kwanza ikasitisha kupeleka fedha kwenye program hii, hali iliyopelekea wahadhiri waliokua wakifundisha kukosa mshahara, posho na stahiki zao nyingine. Wahadhiri walipokosa mshahara wakagoma kufundisha, na hivyo kukaanza mgogoro kati ya wahadhiri, wanafunzi na serikali.

Punde si punde serikali ikasitisha mikopo kwa wanafunzi hawa kwa madai kuwa wanafunzi wa kidato cha nne hawana sifa ya kwenda chuo kikuu, na hata wakienda kwa "equivalent pass" hawastahili kupewa mkopo kwa mujibu wa sera ya mikopo.

Mgogoro ukawa mkubwa zaidi pale serikali ilipowafukuza kazi viongozi wakuu wa TCU eti kwa kudahili wanafunzi "wasio na sifa" chuo kikuu. Serikali ikastaajabu eti wanafunzi wa kidato cha 4 wamefikaje chuo kikuu na kupata mkopo asilimia 100%??

Serikali ikaenda Bodi ya Mikopo na kufukuza Watendaji wote walioshiriki kuwapa mikopo vijana hawa. Vyombo vya habari navyo vikaandika kishabiki bila hata kufanya utafiti eti "Wanafunzi vihiyo chuo kikuu waanza kukiona", wengine wakaandika "Waliowapa mkopo wanafunzi vihiyo wafukuzwa". Yani kila mwandishi akaandika lake kuonesha kufurahishwa na uamuzi huo wa serikali.

Lakini ni waandishi hawahawa walioandika miaka miwili iliyopita kuwa "Waliofaulu vizuri sekondari kupewa mkopo 100% kusomea ualimu wa sayansi". Leo vijana walewale waliotajwa kufaulu vizuri na serikali ya JK ikapongezwa kuwaanzishia program maalumu, ndio wanaitwa "vihiyo" na waandishi walewale waliowasifia.

Hivi mtu aliyepata division 1 au 2 na akafaulu masomo ya Sayansi kwa alama A au B miaka miwili iliyopita leo anakuaje "kihiyo??". Wanafunzi hawa waliofaulu vizuri masomo yao ya O-level wakaitwa "magenius" na kuombwa wakasomee ualimu leo wanaitwa "vihiyo" na serikali ileile.

Leo serikali ya chama kilekile iliyokuja na mpango huu, kupitia wizara ileile inawafukuza viongozi wa TCU waliowadahili wanafunzi hawa. This is typical unfair.

Mbaya zaidi hawakuishia hapo; wakakwenda chuoni na kusitisha mishahara ya wahadhiri. Hawakuishia hapo wakazuia mikopo ya wanafunzi hawa kutoka familia duni. Hawakuishia hapo, hatimaye jana usiku wakawafukuza wanafunzi hawa wasio na hatia.

Hakika nimeshindwa kuelewa kabisa jambo hili. Yani serikali ya JPM inataka dunia iamini kuwa serikali iliyopita ni nyingine kabisa na haina mazuri iliyoyafanya na ilikua inaongozwa wajinga?? Ina maana mtangulizi wake hakumueleza juu ya programu hii maalumu ya kuongeza idadi ya walimu wa sayansi nchini? Kama alielezwa mbona anafanya maamuzi kwa kukurupuka?

Yericko Nyerere anahoji kuwa; inawezekanaje Katika bunge lilelile na spika wa chama kilekile wanazuia hoja binafsi ya Mbunge Joshua Nassari aliyetaka bunge lijadili mgogoro huu na kunusuru hatari inayowakumba watoto wetu hapo UDOM?? Badala yake mbunge huyo ananyanyuliwa mzobemzobe na polisi na kutupwa nje ya lango la bunge.

Vijana hawa wamefukuzwa jana usiku na kupewa notice ya masaa 24 wawe wameondoka ndani ya eneo la chuo, huku magari ya polisi, na polisi wenye silaha, mabomu ya machozi na maji ya kuwasha wakiwa wamezingira maeneo ya chuo hicho tangu usiku.

Wamefukuzwa kama mbwa bila hata kusikilizwa. Wamelazimishwa warudi makwao bila kupewa hata nauli. Watarudije?

Baadhi ya wanafunzi kutokana na kuhofia usalama wao walifungasha mizigo yao na kwenda kujilundika stand ya mabasi Dodoma wakiwasiliana na ndugu zao wawatumie nauli. Polisi wakawavamia leo asubuhi na kuanza kuwapiga wakiwashinikiza waondoke Dodoma haraka. Lakini wataondokaje bila nauli? Kama serikali inajali utu kwanini isiwakodishie mabasi yawarudishe kwao? Mbona Mwalimu Nyerere alipowafukuza kina Samuel Sitta UDSM alitoa mabasi yaliyowapeleka hadi majumbani kwao? Serikali hii ya JPM inashindwa nini?

Mwanafunzi aliyeamua kujisitiri stand ya mabasi akihofia asije kufia chuoni peke yake, hana ndugu Dodoma, hana nauli ya kurudi kwao, anapiga simu kwa ndugu zake wamtumie nauli. Amelala kwa kusimama na kuumwa mbu hadi asubuhi inafika hajapata nauli. Polisi wanamkuta na kuanza kumpiga eti kwanini yuko stand na hataki kusafiri. Huu ni ukatili mkubwa sana dhidi ya binadamu.

Mahali pekee ambapo wanafunzi hawa wanaweza kupata haki yao kwa sasa ni Bungeni tu. Serikali imeshawakana wakati ndio iliyoanzisha hiyo programu. Maafisa wa TCU waliowadahili wameshafukuzwa. Viongozi wa Bodi ya Mikopo waliowapa mikopo nao wamefukuzwa. Tumaini pekee la maisha yao limebaki bungeni.

Halafu Mbunge Nassari analeta hoja ya kujadili suala hili kwa dharura Naibu Spika anakataa, anaagiza Polisi wamtoe nje Nassari. This is very unfair. Wanafunzi hawa wamekua "valnurable" na wako kwenye hatari nyingi ikiwa ni pamoja na kubakwa (kwa wale wa kike) au kufanyiwa vitendo vya kihuni hata kuuawa.

Wanahitaji msaada wa dharura ili waweze kujua hatma yao. Na mahali pekee pa kupata msaada huo ni bungeni, lakini Naibu Spika hataki. Anasema hoja hiyo siyo ya dharura. Huu ni unyama. Ni ukatili. Ni Ukosefu wa utu. Ni ushetani. Yani wadogo zetu wafie Dodoma halafu tuambiwe si dharura? Hivi huyu mama amezaa? Ingekua wanae ndio wapo kwenye mazingira hayo angefanya hivyo?

Kwanini tunawaadhibu watoto hawa kwa makosa ambayo hawajafanya. Kama ni kukosea basi aliyekosea ni JK na serikali yake, kwanini Magufuli awaadhibu hawa watoto wasio na hatia? Nini hatma yao? Wengine wako mwaka wao wa mwisho kumaliza elimu yao ina maana wamepoteza muda bure? Nani atawalipa muda waliopoteza?

Leo ni vijana hao hao kama wangeamua kwenda kidato cha tano wangekuwa wamemaliza form six mwaka jana na sasa wapo first year chuo kikuu na wengine wangekua wanasubiri kujiunga first year mwaka huu. Wapo waliokua na ndoto za kuwa maribani, madaktari, wahandisi lakini walijitolea maisha yao na kuamua kwenda kusomea ualimu kwa ajili ya Tanzania; licha ya kufaulu kwa division one na two. Leo wanafukuzwa kama mbwa na Polisi wenye silaha.

*SULUHISHO.!*

*_Suluhisho Namba1_*
Leo iwe siku ya mwisho kwa Naibu Spika kuhujumu demokrasia ndani ua bunge. Miezi mitano aliyohudumu imetosha kuonesha rangi yake halisi. Ameingia ktk orodha ya maspika waliofanya vibaya zaidi duniani tangu kumalizika kwa vita kuu vya pili vya dunia.

Kwahiyo ili kumsaidia inabidi Bunge lipige kura ya kutokua na imani nae. Afukuzwe katika kiti hicho ili iwe fundisho kwa wengine.

Wabunge wa upinzani wasign petition ya _"Vote of no Confidence"_ kwa Naibu Spika. Kwa mujibu wa Kanuni "petition" hiyo inahitaji kusainiwa na theluthi moja ya wabunge wote ili kura hiyo iweze kupigwa. Yani moja ya tatu ya wabunge wote.

Kwa sasa bunge lina wabunge 387 (Wakuchaguliwa kutoka majmboni ni 264, Viti maalum 115, Wakuteuliwa na Rais 07 plus AG na Naibu Spika). Theluthi moja ya 387 ni wabunge 129.

Hadi sasa Upinzani wana wabunge 119 (118 UKAWA + 1 ACT). Mana yake ni kwamba Wabunge wote wa UKAWA wakisaini "petition" ya kumuondoa Naibu Spika watapata signature 119 na hivyo watapungukiwa signature 10 tu kufikia akidi. Kwahiyo watahitaji wabunge 10 tu wa CCM wawaunge mkono ili "petition" hiyo ijadiliwe bungeni na kumpigia Naibu Spika kura ya kutokua na imani nae. Na kwa mshikamano wa leo nina uhakika signature 10 za CCM zitapatikana hata zaidi.

_*Suluhisho Namba2*_
Bunge lijadili kwa dharura changamoto hii iliyowakumba wanafunzi hawa na kwa pamoja lifikie maazimio yafuatayo;

*(a)* - Wanafunzi wote warudishwe chuoni na kuendelea na masomo,

*(b)* - Watendaji wa TCU na HESLB waliofukuzwa kazi kwa kuwadahili na kuwapa mikopo wanafunzi hawa warudishwe kazini mara moja,

*(c)* - Prof.Mlacha makamu mkuu wa UDOM Fedha na Utawala asimamishwe kazi mara moja kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yake,

*(d)* - Wahadhiri wote waliogoma walipwe mishahara yao na warudishwe kazini kuendelea kufundisha hawa vijana,

*(e)* - Ufanyike uchunguzi kuhusu udahili wa wanafunzi hawa na wale watakao onekana kudahiliwa bila sifa wasimamishwe masomo na sio kufukuza wanafunzi wote.

Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumepata siluhisho la kudumu la mgogoro huu.

*_Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli._*

*Malisa GJ* || _Your Partner In Critical Thinking.!_

Sent from my TECNO-Y6 using JamiiForums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom