Mwanamke wa makamo kutoka Ecuador aliyezinduka baada ya madaktari kutangaza kuwa amefariki, anapatiwa matibabu katika hospitali ya serikali ambayo ilitangaza kuwa amekufa siku mbili zilizopita, mtoto wake alisema Jumapili.
Video iliyotumwa kwenye Twitter inamuonyesha Bella Montoya, 76, kwenye jeneza likiwa wazi akipumua kwa nguvu huku wanaume wawili wakimsaidia.
Mtoto wake, Gilbert Balberán, alisema "alikuwa akipiga sanduku" kwa mkono wake wa kushoto baada ya kuamka kwa saa tano.
Balberán alilazimika kuomba mchango wa jeneza kwa familia maskini baada ya hospitali hiyo, kutangaza kuwa Montoya amekufa siku ya Ijumaa.
"Hata walitupa cheti cha kifo," alisema kwenye video iliyotangazwa na vyombo vya habari vya ndani.
Vyombo vya habari vya Ecuador viliripoti tukio hilo lisilo la kawaida, na vichwa vya habari vikisheheni ‘kufufuka’ kwa mwanamke huyo.
"Mama yangu amepata oksijeni. Moyo wake uko shwari. Daktari alimfinya mkono wake na akaitikia," Balberán alisema katika ripoti ya gazeti la El Universo.
"Wananiambia kuwa hii ni nzuri, kwa sababu ina maana kwamba anarejesha afya yake taratibu."
Montoya alilazwa hospitalini akiwa na kiharusi "na alikuwa hapumui kutokana na mapigo ya moyo kusimama, kwa hivyo daktari wa zamu alithibitisha kifo chake," Wizara ya Afya ya Ecuador ilisema katika taarifa yake Jumapili.
Wizara ilisema kuwa imeunda kamati ya kuchunguza tukio hilo na kwamba itasimamia uangalizi wa Montoya.
Balberán alisema alikuwa amemtembelea mama yake katika chumba cha wagonjwa mahututi siku ya Jumapili.
"Kidogo kidogo naelewa kilichotokea. Sasa namuombea tu afya ya mama yangu iwe bora. Namtaka awe hai na awe upande wangu," alisema