Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Innocent Bashungwa @innocentbash amewasilisha Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 ambapo moja ya mambo aliyoyasema kwenye hotuba yake ni kutoa rai kwa Vijana wote wanaopata fursa za kupata mafunzo ya JKT, kuzitumia stadi za kazi na maisha walizozipata kujiajiri na kujitegemea.
“Wizara kupitia JKT imeendelea kuwapatia Vijana wa Kitanzania mafunzo ya ukakamavu, stadi za kazi, kuwajengea uzalendo na umoja wa kitaifa, katika mwaka wa fedha 2022/23, mafunzo yamefanyika kwenye kambi mbalimbali za JKT kupitia Operesheni Jenerali Venance Mabeyo, Vijana 24,458 kwa mujibu wa sheria wamepatiwa mafunzo, kati yao 17,942 wa kiume na 6,516 wa kike”
“Aidha, Vijana 11,358 wa Kujitolea wamepatiwa mafunzo, kati yao 7,483 ni wa kiume na 3,875 ni wa kike, dhumuni la mafunzo yanayotolewa kwa Vijana ni kuwapatia ukakamavu, stadi za kazi, kuwajengea uzalendo na umoja wa kitaifa ili baada ya kumaliza muda wa mafunzo na kutumikia JKT, waweze kurejea majumbani kwao wakiwa raia wema, wazalendo na wenye uwezo wa kujitegemea na kulilinda Taifa”