Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imepata kibali cha ajira 547 kutoka Ofisi ya Rais Utumishi za wataalamu wa kada mbalimbali za afya wanaokidhi vigezo vya kuajiriwa chini ya wizara hiyo na taasisi zake.
Tangazo hilo la ajira limetolewa jana Jumatano Mei 12, 2021 na katibu mkuu wa Wizara ya Afya, Profesa Abel Makubi.
Amesema ajira hizo ni utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na Serikali akibainisha kuwa ajira hizo zinajumuisha nafasi 473 zitakazoratibiwa na wizara wakati nafasi 74 zitaratibiwa na sekretariati ya ajira.
“Wataalamu 74 wa kada mbalimbali wataajiriwa katika maabara kuu ya Taifa na wataalamu 473 wa kada mbalimbali wataajiriwa katika hospitali za kanda za KCMC, Mbeya, Bugando na Benjamini Mkapa, hospitali za rufaa za mikoa na vyuo mbalimbali vilivyopo chini ya wizara ya afya,” amesema.
Profesa Makubi amesema wataalamu 473 chini ya uratibu wa wizara ambao watanufaika na nafasi hizo ni pamoja na madaktari wauguzi, wafamasia, wateknolojia wa dawa, wateknolojia wa maabara, wateknolojia wa mionzi, wateknolojia wa macho, watoa tiba kwa vitendo, maafisa afya mazingira, wasaidizi wa afya, makatibu afya, maafisa istawi wa jamii na maafisa lishe.
“Ajira hizo (473) zitajaza nafasi zilizoachwa wazi na watumishi waliokoma utumishi kutokana na sababu mbalimbali. Waombaji wanasisitizwa kuzingatia maelekezo yote yatakayotolewa na vyanzo rasmi vya taarifa za ajira na utaratibu kupitia tovuti
www.moh.go.tz kwa kiunganishi (ajira.moh.go.tz). Maombi ni kuanzia Mei 12 hadi 25, 2021,” amesema.