Makapuku Forum

Makapuku Forum

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 42 AZIZ HASHIM
ILIPOISHIA:
Kwa akili yangu nilijua kwamba tayari kazi imekwisha, kumbe kulikuwa na kazi nyingine, nikaanza kutetemeka tena huku nikigeuka huku na kule kuwatazama wale watu ambao wote walikuwa na nyuso za furaha. Nilipogeuka upande wa kushoto, nilimuona mtu aliyenifanya nishtuke mno, nilifikicha macho nikiwa ni kama siamini.
SASA ENDELEA...

Alikuwa na Isrina, naye akiwa amevaa kama wale watu wengine wote waliokuwepo eneo lile. Alikuwa ametulia akinitazama kwa makini, ilionesha kwamba kumbe naye muda wote wakati yale mambo yakiendelea alikuwepo na alikuwa akinifuatilia hatua kwa hatua.
Nilishtuka kupita kiasi, nikageuka na kumtazama baba, naye akanitazama huku akitingisha kichwa kama ishara ya kuniambia ninachokiona ni kweli. Ni hapo ndipo nilipoelewa kwa nini mara kwa mara baba alikuwa akinikanya kuwa karibu na msichana huyo huku akiniuliza mara kwa mara kama najua ana malengo gani na mimi.
Nilijikuta kama kichwa kikiwa kizito, kwa tafsiri nyepesi, Isrina au Isri kama mwenyewe alivyokuwa akipenda kuitwa, alikuwa akifahamiana vizuri na baba kwa sababu wote walikuwa jamii moja. Bado sikutaka kuamini kama Isrina naye anahusika na hayo mambo, nilijaribu kuvuta kumbukumbu ya siku niliyokutana naye kwa mara ya kwanza.
Bado sikuwa na majibu ilikuwaje mpaka tukapanda basi moja, ilivyoonesha ni kama kukutana kwetu hakukuwa bahati mbaya bali ni jambo ambalo lilipangwa. Sasa kama anafahamiana na baba, kwa nini hataki kabisa niwe karibu naye? Kwa nini anamchukia? Nilijiuliza maswali mengi yasiyo na majibu.
Nikiwa bado naendelea kujiuliza maswali mengi yasiyo na majibu, yule babu ambaye baba aliniambia anaitwa Mkuu, alinishika mkono baada ya kuona nimepigwa na butwaa. Licha ya uzee wake na mwili wake kuchoka, Mkuu alikuwa na nguvu kwelikweli, akanivutia kwake na kuanza kutembea na mimi kuelekea pale katikati nilipokuwa nimelazwa kwa mara ya kwanza.
Mara nilishtuka kuona wanaume wanne, wakitoka kule pembeni na kusogea mpaka pale tulipokuwa, wakiwa wamebeba jeneza. Sikuelewa lile jeneza ni la nini lakini kwa jinsi walivyolibeba, ilionesha kama lipo tupu.
Walilisogeza mpaka pale jirani na kuliweka chini, wakasimama wakiwa ni kama wanasubiri maagizo kutoka kwa Mkuu huku wote wakinitazama. Niligeuka na kumtazama baba, akawa ni kama ananipa ishara kwamba nisiogope, nikageuka na kumtazama Isri, bado alikuwa amenikazia macho muda wote, nikashusha pumzi ndefu na kumgeukia Mkuu.
Alitoa kichupa kutoka kwenye mkoba wake wa ngozi aliokuwa ameuvaa kiunoni, akakitingisha kisha akakifungua na kunipa ishara kwamba ninuse kilichokuwemo ndani. Nilipofanya hivyo tu, nilianza kupiga chafya mfululizo kutokana na ukali wa ile dawa iliyokuwa mle ndani ya kichupa.
Nikapiga chafya zisizo na idadi, mara nikaanza kuhisi kizunguzungu kikali, nikawa napepesuka, wale wanaume wakanishika ili nisianguke, Mkuu akanisogelea pale nilipokuwa nimeshikwa, akaninusisha tena na safari hii, hakukitoa haraka kile kichupa puani, nikaendelea kupiga chafya nyingi, mwisho giza nene likatanda kwenye uso wangu na mwili wote ukawa ni kama umekufa ganzi.
Licha ya hali hiyo, bado nilikuwa naweza kuelewa kinachoendelea ingawa sikuwa na uwezo wa kufanya chochote, nikasikia wakinilaza chini kisha lile jeneza likagongwagongwa na kitu kizito, nadhani walikuwa wakilifungua.
Nikiwa bado sielewi hatma yangu, nilishtukia wakininyanyua na kunilaza ndani ya jeneza. Sikuwa hata na uwezo wa kufumbua macho ingawa bado nilikuwa na fahamu zangu. Baada ya hapo, nilisikia tena jeneza likigongwagongwa juu yangu, nikajua mimi ndiyo nimewekwa kwenye jeneza.
Mara nilisikia tena lile pembe la ng’ombe likipulizwa kisha Mkuu akapaza sauti na kutamka haraka maneno ambayo sikuyaelewa, wale watu wengine wakaanza kuimba nyimbo kama za maombolezo, nikahisi lile jeneza nililowekwa ndani yake likinyanyuliwa na waliolibeba wakaanza kutembea.
Ilikuwa ni kama nipo kwenye ndoto lakini tofauti yake ni kwamba nilikuwa najielewa. Wale watu waliendelea kuimba huku nao wakionesha kuwafuata wale walionibeba kwenye jeneza. Wakatembea umbali fulani kisha nikahisi jeneza likishushwa chini huku wale watu wakiendelea kuimba.
Nikiwa sielewi nini hatima yangu, nilihisi kama jeneza linahamishwa tena na safari hii, lilikuwa kama linaingizwa kwenye shimo, mara nikashtukia vitu vizito vikianza kuangushiwa juu ya jeneza.
Kwa jinsi vilivyokuwa vikidondoka kwa vishindo, nilielewa moja kwa moja kwamba ulikuwa ni udongo, nikajiuliza ina maana wamenipeleka makaburini? Ina maana wananizika nikiwa hai? Sikupata majibu.
Vile vishindo viliendelea na muda mfupi baadaye, zile sauti za watu waliokuwa wakiimba nazo zilianza kufifia na baadaye zikatoweka kabisa, ukimya mkubwa ukiwa umetanda kila sehemu. Sikuelewa tena kilichoendelea kwani hata zile fahamu zangu, sasa zilinitoka kabisa.
Nilipokuja kushtuka, ilikuwa tayari kumepambazuka na licha ya yote yaliyotokea, nilijikuta nikiwa kwenye chumba changu, nikiwa nimelala kitandani, mwili wangu ukiwa hauna nguvu kabisa.
“Vipi unajisikiaje?” sauti ya baba ilinishtua, nikageuza shingo na kumtazama, alikuwa amekaa pembeni yangu, mkononi akiwa na bakuli la uji. Hata nguvu za kumjibu sikuwa nazo, pembeni pia alikuwepo baba yake Rahma ambaye uso wake ulikuwa na furaha.
Walisaidiana kuniinua kidogo upande wa shingoni, wakaniwekea mto na baba akaanza kuninywesha ule uji.
“Jitahidi kunywa ili upate nguvu,” alisema baba, nikajilazimisha hivyohivyo, kweli nikamaliza lile bakuli maana ni kweli tumbo nalo lilikuwa tupu kabisa.
“Inabidi uendelee kupumzika, leo hutakiwi kufanya shughuli yoyote mpaka utakapopewa maagizo na Mkuu,” aliniambia baba, nikatingisha kichwa kuashiria kukubaliana na alichokisema ingawa sikuelewa huyo Mkuu atanipaje hayo maagizo. Yaani nilivyokuwa nikijisikia, ni kama mtu aliyeumwa kwa kipindi kirefu sana na kusababisha mwili uishiwe nguvu kabisa kiasi cha kushindwa hata kujigeuza pale kitandani.
Waliinuka na kutoka, mimi nikapitiwa tena na usingizi mzito. Nikiwa usingizini, nilianza kuota ndoto ya kutisha, nilijiona nipo kulekule porini lakini tofauti na mara ya kwanza, safari hii tulikuwa tumebaki wawili tu, mimi na Mkuu. Akawa ananiambia ili nguvu zangu nilizopewa zianze kufanya kazi, ni lazima nitoe kafara na kafara hilo ndiyo utakuwa mtihani wangu wa kwanza.
Aliniambia kwamba wachawi wote, sifa ya kwanza ni lazima wawe na uwezo kuua na kwamba kadiri mtu anavyoua watu wengi zaidi ndivyo anavyopanda ngazi. Alisema maneno hayo kwa msisitizo kisha baada ya kumaliza, alicheka kicheko cha nguvu kilichokuwa kinasikika kama mwangwi kisha akayeyuka.
Kwa jinsi ndoto ile ilivyokuwa inatisha nilijikuta nikishtuka, kutazama nje bado ilikuwa mchana, mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kuliko kawaida. Kumbe pale wakati nashtuka, nilipiga kelele zilizomfanya baba na baba yake Rahma waje haraka kule chumbani kwangu.
Cha ajabu, nilipowahadithia nilichoota, hakuna aliyeonesha kushtuka, sanasana baba akapigilia msumari kwa kusema kwamba ile haikuwa ndoto bali ni Mkuu alikuwa akiwasiliana na mimi.
“Baba!” nilisema kwa mshtuko nikiwa bado palepale kitandani.
“Nini sasa.”
“Mimi niue mtu?” nilipotamka maneno hayo, baba alinionesha ishara kwamba nisipige kelele, wote wakanisogelea pale kitandani na kuniambia kwa sauti ya chini kwamba Mkuu akishatoa maagizo kwa mtu, kinachofuatia huwa ni utekelezaji tu na endapo mtu akishindwa kutekeleza alichoambiwa, anakufa yeye. Nilishtuka mno, nikamtazama baba, nikamtazama baba yake Rahma, wote walionesha kumaanisha kile walichokisema.
“Hapana! Hapanaaa,” nilisema kwa sauti ya juu, ikabidi baba anizibe mdomo maana alihisi naweza kuropoka mambo mengine na kuwafanya wasiohusika wajue.
“Huna haja ya kuogopa, zipo njia za kutimiza hicho ulichoambiwa bila kuonekana kama wewe ndiyo umefanya moja kwa moja, mbona sisi huwa tunafanya sana tu” alisema baba, macho yakanitoka.
Je, nini kitafuatia?
 
The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 43 AZIZ HASHIM
ILIPOISHIA:
“Hapana! Hapanaaa,” nilisema kwa sauti ya juu, ikabidi baba anizibe mdomo maana alihisi naweza kuropoka mambo mengine na kuwafanya wasiohusika wajue.
“Huna haja ya kuogopa, zipo njia za kutimiza hicho ulichoambiwa bila kuonekana kama wewe ndiyo umefanya moja kwa moja, mbona sisi huwa tunafanya sana tu,” alisema baba, macho yakanitoka.
SASA ENDELEA...

Aliondoa mkono wake mdomoni mwangu, akaniambia wameniamini ndiyo maana wameniunganisha kwenye jamii yao, akaniambia faida nitakazozipata ni nyingi na kubwa sana kwa hiyo sina sababu ya kuogopa kutimiza sharti lile dogo nililopewa.
“Sijawahi kuua mtu hata siku moja, nitaanzaje,” nilisema, baba akatabasamu na kumgeukia baba yake Rahma, wakacheka na kugongesheana mikono. Sikuelewa kwa nini wao wacheke wakati mimi nilikuwa kwenye hali mbaya kiasi hicho, hofu kubwa ikiwa imetanda kwenye moyo wangu.
“Unatakiwa ujue namna ya kudhibiti hofu yako, ukiwa mwoga hivi huwezi kufanya chochote,” alisema baba, baba yake Rahma akamuunga mkono, wakawa wananieleza kwamba mtihani niliopewa ni mdogo sana na endapo nitashindwa nitakuwa nimewaangusha sana na kila mtu atanicheka.
“Utathibitisha kwamba kauli yangu niliyoitoa juu yako ni sahihi.”
“Kauli gani?”
“Kwamba wewe bado una akili za kitoto,” baba alisema. Hakuna kitu nilichokuwa sikipendi kama kusikia kauli za namna hiyo kutoka kwa baba, nikajikuta morali fulani ukinipanda ndani kwa ndani, nikajisemea kwamba nitamuonesha kwa vitendo kama mimi siyo mtoto.
“Endelea kupumzika mpaka mwili upate nguvu, tutakuja baadaye kukuelekeza nini cha kufanya,” alisema baba, wakatoka na kuniacha nimelala palepale kitandani. Kwa nje nilisikia wakifunga mlango kwa funguo, nikabaki nashangaa kwa nini wananifungia?
Sikuwaza sana kuhusu hilo la mlango, bado nilikuwa na mawazo mengi juu ya hatma yangu na ile kazi niliyokuwa nimepewa. Sikuwahi kudhani hata siku kwamba eti na mimi naweza kuwemo kwenye orodha ya wachawi, tena wanaoua na kula nyama za watu wasio na hatia.
Ni kweli kuna kipindi nilikuwa nikitamani kuwa na nguvu kama za baba lakini nilichokuwa nikikijua ni kwamba nguvu zake zilikuwa ni za kutibu watu na kufanya yale yasiyowezekana tu, sikujua kuwa gharama zake ni kubwa kiasi hicho.
Sikupata jibu mtihani mkubwa uliokuwa mbele yangu ningeuvuka vipi, sikujua ni kwa kiasi gani moyo wangu utakuwa na hatia kwa kuyakatisha maisha ya mtu asiye na hatia. Kuna wakati nilikuwa nikitamani kama nitoroke na kuelekea kusikojulikana lakini kila nilipokuwa nikifikiria vile vitisho nilivyokuwa napewa, nilijikuta nikikosa ujanja.
Nilipokumbuka na kauli za baba za kunidharau, nilijikuta nikizidi kuchanganyikiwa, sikuelewa nini itakuwa hatma yangu. Basi niliendelea kuwaza na kuwazua pale kitandani, mwili ukaanza kupata nguvu taratibu, saa zikawa zinazidi kuyoyoma.
Mida ya jioni baba alikuja tena, akafungua mlango na kuingia akiwa na bakuli lililokuwa na supu ya kuku wa kienyeji. Akaniwekea vizuri na kuniambia niinuke mwenyewe pale kitandani. Kwa kuwa safari hii nilikuwa na nguvu, niliinuka mwenyewe na kukaa kitako.
Akanisogezea lile bakuli na kunipa. Nililipokea huku mikono ikitetemeka, nikaanza kuinywa supu ile kwa pupa. Muda mfupi tu baadaye, bakuli lilikuwa tupu. Ile njaa niliyokuwa nayo sasa ilikuwa imepungua na nilijihisi kuwa na nguvu kama zamani.
“Hebu jaribu kusimama mwenyewe,” baba aliniambia wakati akikusanya mifupa na kuiweka kwenye lile bakuli, nikajishikilia kwenye kingo za kitanda na kusimama. Bado miguu haikuwa na nguvu vizuri lakini niliweza kusimama, akaniambia nizunguke mle ndani, kweli nikaweza.
“Safi sana, sasa umekuwa mwanaume kamili,” aliniambia huku akinielekeza kuendelea kupumzika mpaka usiku. Nilirudi kitandani na kujilaza, kidogo nikawa najisikia vizuri, baba akatoka na kufunga tena mlango kwa ndani.
Kiukweli nilikuwa nimemkumbuka sana Rahma, sikujua anawaza nini juu yangu maana siyo kawaida tukae wote nyumba moja halafu tusionane siku nzima. Nilitamani japo nipate muda mfupi wa kuonana naye, nimweleze kinachonitokea maishani mwangu maana angeweza kuhisi kama labda simpendi tena na ndiyo maana nimebadilika.
Muda ulizidi kuyoyoma na hatimaye giza likaingia, mara nikasikia mlango ukifunguliwa. Walikua ni baba na baba yake Rahma, waliingia na kuwasha taa, wakanisogelea mpaka pale kitandani.
“Vipi unaendeleaje?”
“Naendelea vizuri.”
“Safi, sasa inatakiwa tuondoke kuna mahali tunaenda kukuonesha sehemu tunapochimba dawa zetu za kufanyia kazi,” baba aliniambia, nikainuka na kukaa vizuri.
“Kwa mfano hiyo kazi uliyopewa, huwezi kuifanikisha kwa urahisi mpaka uwe na dawa na inabidi dawa hizo ukachimbe wewe mwenyewe, kwa hiyo sisi tunachokifanya ni kukuelekeza tu, mambo mengine utafanya mwenyewe ikiwa ni pamoja na kujifunza kwa vitendo,” alisema baba.
Sikuwa na cha kujibu zaidi ya kuinuka, nikataka kwenda kuoga lakini baba alinikataza, akasema sitakiwi kuoga kwa muda wa siku saba, nikashangaa sana. Aliniambia nivae nguo zangu tuondoke haraka maana tulikokuwa tukienda ni mbali.
Ilibidi nifanye kama walivyoniambia, nilivaa nguo zangu vizuri, baba akafungua mlango na kutangulia, kabla hajatoka aliniambia kwamba kila tunakoenda, sitakiwi kutangulia mbele wala kubaki nyuma, muda wote niwe katikati yao.
Sikuelewa maana ya maelekezo yake hayo ila nilitii, akatangulia, nikafuata halafu baba Rahma akafuatia nyuma. Nikiri kwamba baada ya yale yote yaliyotokea, nilikuwa nikiwatazama baba na baba yake Rahma kwa jicho tofauti kabisa. Hata sijui nieleze vipi lakini kwa kifupi nilikuwa nikiwatazama kwa jicho la tofauti.
Tulitoka moja kwa moja mpaka nje na nadhani hakuna mtu yeyote aliyetuona, tulitoka mpaka pale nje kabisa palipokuwa na maegesho ya Bajaj na bodaboda.
“Yule jamaa aliyekamatwa kwa mauaji ameachiwa? Sijui kama tutapona mtaa huu,” nilimsikia dereva bodaboda mmoja akiwaambia wenzake, akimaanisha mimi. Nilijua kwamba ananizungumzia mimi maana hata siku ile nilipokuja kuchukuliwa na polisi pale nyumbani, yeye ndiyo alikuwa kiherehere wa kuwasimulia wenzake kwamba eti mimi nimemuua mtu gesti.
Nilijikuta nimepandwa na jazba, nikatamani kama nimrukie na kumtandika makofi kwa hasira. Hakuna kitu ambacho huwa sikipendi kama dharau. Kumbe wakati nikifikiria nini cha kufanya, baba na baba yake Rahma walishajua ninachowaza.
“Hutakiwi kuwa na hasira zisizo na msingi, muache afurahishe mdomo wake,” alisema baba yake Rahma huku akinipigapiga begani. Nilishusha pumzi ndefu, baba akazungumza na dereva mmoja wa Bajaj, tukaingia na mimi nikakaa katikati.
“Tupeleke Ubungo,” alisema baba, safari ikaanza. Ubungo hapakuwa pageni kwangu kwani ndiyo sehemu ya kwanza kukanyaga tuliposhuka kwenye basi tukitokea Chunya. Basi tulienda mpaka Ubungo, tulipofika baba alimlipa dereva, tukavuka kwenye mataa ya kuongozea magari na kwenda upande wa pili mpaka kwenye stendi ya daladala.
Tulipanda kwenye gari moja, hata sijui linaelekea wapi, tukaenda kukaa siti ya nyuma kabisa, mimi nikiwa katikati.
“Kwani tunaenda wapi?”
“Tunaenda Kibaha,” alisema baba, nikashindwa kumhoji chochote maana hata huko kibaha kwenyewe sikuwa nakujua.
Baadaye gari liliondoka, ikiwa ni majira ya kama saa tatu za usiku, tukaenda mpaka tulipofika Kibaha, tukashuka na kuanza kutembea kwa miguu. Tulivuka barabara, nikaona kuna kibao kimeandikwa Tumbi Hospital, nimewahi sana kuisikia hii hospitali kwani mara nyingi ajali nyingi zinazotokea mkoa wa Pwani majeruhi au maiti huwa zinapelekwa Tumbi.
Basi tulianza kutembea kuifuata barabara hiyo, giza nalo likawa linazidi kuwa nene, tukatembea umbali mrefu, tulipofika kule juu kabisa, tuliiacha barabara ya lami na kuingia vichakani, nako tukatembea umbali mrefu sana, hatimaye tukatokezea kwenye eneo lililokuwa na vichana vifupivifupi.
Kwa kutumia tochi aliyokuwa nayo, baba alianza kumulika kwenye vile vichaka kama anayetafuta kitu, mimi na baba yake Rahma tukawa tunamfuata kwa nyumanyuma maana kama nilivyosema, mimi sikutakiwa kutangulia mbele wala kubaki nyuma kwa hiyo ilikuwa ni lazima tutembee watatuwatatu.
“Unauona huu mti, unaitwa mtunguja, huu ndiyo hutumika sana kutengeneza ajali za kichawi na unapatikana kwa wingi eneo hili na ndiyo maana huku kila siku unasikia ajali mbayambaya zinatokea maana wanafunzi kama wewe, huku ndiyo eneo la kujifunza kwa vitendo,” alisema baba huku akianza kufukua kwenye shina la mti huo mdogo.
“Sifa yake moja, huu mtu huwa unatoa damu,” alisema baba, akatoa kisu na kubandua sehemu ndogo ya ganda lake, nikashangaa kweli mti ukitoa vitu vilivyokuwa vikifanana kabisa na damu.
“Niangalie vizuri namna ya kuchimba maana tukitoka hapa inabidi na wewe ukafanye majaribio kama wenzako,” alisema baba. Muda huo ulikuwa ni kama saa sita hivi za usiku, giza nene likiwa limetanda kila sehemu.
Je, nini kitafuatia?
 
The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 44
ILIPOISHIA:
“Niangalie vizuri namna ya kuchimba maana tukitoka hapa inabidi na wewe ukafanye majaribio kama wenzako,” alisema baba. Muda huo ulikuwa ni kama saa sita hivi za usiku, giza nene likiwa limetanda kila sehemu.
SASA ENDELEA...

Huku nikitetemeka, nilianza kumtazama vizuri baba alivyokuwa akichimba, alikuwa akifukua shina la ule mti huku akiuzunguka, akitamka maneno fulani ambayo sikuwa nayaelewa. Baada ya kuuzunguka karibu mara saba, tayari alishakuwa ameifikia mizizi, akatoa kisu na kuanza kuichambua na kuikata mmoja baada ya mwingine.
“Hutakiwi kukata mizizi zaidi ya saba kwenye mti mmoja, na hutakiwi kuchimba mti ambao unaonekana tayari umeshachimbwa katika siku za hivi karibuni,” alisema baba, nikawa natingisha kichwa kumkubalia. Baada ya kumaliza, alinikabidhi tochi, akaniambia niutazame vizuri ule mti, nikaumulika vizuri.
“Sasa na wewe unatakiwa kutafuta mti kama huuhuu, ipo mingi lakini lazima uwe makini kutafuta wa kuchimba dawa,” aliniambia baba, basi nikaanza kumulika huku na kule, baba akiwa upande wa kushoto na baba yake Rahma upande wa kulia.
Muda mfupi baadaye, kweli nilifanikiwa kuupata lakini ulikuwa umezongwa na miiba mingi, baba akaniambia ni lazima niitoe kwanza miiba yote ndiyo nianze kuchimba, nilifanya hivyo na baada ya muda, nilikuwa nimepasafisha pale kwenye shina la mti huo.
Nikaanza kuchimba huku baba akinielekeza hatua kwa hatua, akaniambia kwa kuwa ndiyo kwanza naanza hakuna umuhimu wa kunuiza maneno kama alivyokuwa akifanya yeye bali natakiwa kuweka nia moyoni kwamba nahitaji damu kwa ajili ya kafara.
Nilifanya hivyo, nikawa naufukua ule mti na nilipozunguka mara ya saba, tayari mizizi ilikuwa ikionekana, baba akanipa kisu na kuniambia kwamba natakiwa kuchagua mizizi ya katikati, yaani isiwe mikubwa sana wala midogo sana na isizidi saba.
Nikakata wa kwanza, pale nilipokata pakawa panatoka yale majimaji kama damu, nikakata wa pili, wa tatu mpaka saba ilipotimia, shina lote likawa limelowa na yale majimaji ya ule mti kama damu.
“Haya fukia lakini hakikisha hiyo mizizi hauiweki chini, ishike vizuri,” aliniambia na kunielekeza kwamba wakati wa kufukia, natakiwa kwenda kinyume na vile nilivyokuwa nafukua, yaani kama wakati wa kufukua nilikuwa nauzunguka mti kwa kuelekea upande wa kulia, ninapofukia natakiwa kuanzia upande wa kushoto na hivyo ndivyo nilivyofanya.
Baada ya kumaliza, baba alisema tunapaswa kwenda kuziosha dawa zetu mtoni na kuzitengeneza vizuri. Sikuwa mwenyeji wa Kibaha na hata sikuwa najua kama kuna mto, nikawa kama bendera fuata upepo.
Tulitembea tukikatiza vichaka na mapori, hatimaye tukatokezea mahali palipokuwa na kama chemchemi hivi, pembeni kukiwa na bustani za mbogamboga nyingi, baba akatangulia mpaka pale kwenye chemchemi, kabla ya yote, alitoa kisu chake na kukata jani kubwa la mgomba, akalikata vipande vitatu, kimoja akanipa, kingine akampa baba Rahma na kingine akabaki nacho yeye.
Alitoa ile mizizi aliyoichimba, akaniambia nimtazame kwa makini anachokifanya, ilikuwa imebadilika rangi na kuwa nyekundu kama damu, akaanza kuiosha ikiwa juu ya jani la mgomba, akafanya hivyo kwa dakika kadhaa mpaka ilipobadilika rangi na kurejea kwenye rangi yake halisi ambayo ni kama kahawia fulani hivi.
Ilifika zamu yangu, na mimi nikafanya vilevile, nikaitoa mfukoni na kuiosha vizuri, kisha ikafika zamu ya baba yake Rahma ambapo baba alimtolea na kumpa mizizi yake, akaiosha kwa uzoefu wa hali ya juu kisha tukaondoka eneo hilo.
Hapakuwa mbali sana na barabara kwani hata kelele za magari yaliyokuwa yakipita kwa kasi kubwa tuliweza kuzisikia. Kadiri tulivyokuwa tukisonga mbele ndivyo hofu ilivyozidi kutanda kwenye moyo wangu.
Tulikatiza vichaka, mapori na mashamba ya watu na hatimaye tukawa tumetokezea barabara ya lami. Sikujua eneo lile linaitwaje lakini kwa mzunguko tulioupiga, kuanzia pale tuliposhuka kwenye gari, tulivyoelekea njia ya Tumbi na baadaye kuingia porini kisha kurudi barabarani, nilijua kwamba si mbali sana na pale tuliposhukia.
“Mtu yeyote akikusemesha hutakiwi kujibu chochote, eneo hili lina watu kutoka jamii mbalimbali ambao huwa wanapenda kupimana nguvu, umenielewa?” baba aliniambia, nikatingisha kichwa kuonesha kumkubalia.
“Leo ni zamu yako, kwa hiyo inatakiwa unisikilize kwa makini,” baba aliniambia, akasema kati ya ile mizizi saba, mmoja natakiwa kwenda kuufunga kwenye mti au jani lolote upande wa pili wa barabara, mwingine natakiwa kuuweka katikati ya barabara, mwingine natakiwa kuufunga upande ule tuliokuwepo, mmoja natakiwa kuutafuna na kuumeza na miwili natakiwa kubaki nayo mwilini, mmoja niweke kwenye mfuko wa kushoto wa suruali na mwingine niubane kwenye kwapa langu la kushoto kama kipima joto.
Yalikuwa ni maelezo marefu lakini nilijitahidi kuwa mwelewa maana nilikuwa na shauku kubwa ya kuona nini kitatokea. Kweli baada ya hali kutulia, kwa maana kukiwa hakuna gari kutoka upande wowote, nilivuka barabara kinyumenyume mpaka upande wa pili.
Kwa kutumia uzi mweusi alionipa baba, niliufunga ule mzizi kwenye tawi moja la mti mdogo uliokuwa pale pembeni ya barabara, nikarudi tena kinyumenyume mpaka katikati ya barabara na kukaa chini kabisa, nikaweka ule mzizi kisha nikajiburuza kwa makalio kinyumenyume mpaka pale baba na baba yake Rahma walipokuwa wamesimama.
Nikasimama na kusogea kwenye kimti kingine kidogo kilichokuwa kando ya barabara, usawa wa kile nilichokifunga, nikaenda kufunga ule mzizi kwa kutumia ule uzi kisha kinawasogelea akina baba ambao walikuwa wakinitazama kwa makini kuhakikisha sikosei hatua hata moja.
“Safi sana,” alisema baba kisha akaanza kuniuliza kama mpaka hapo nimeshaelewa ni gari linalotokea upande gani ndiyo litapata ajali. Sikuwa naelewa chochote. Akaniambia kwa sababu nimesota kwa makalio kutokea katikati ya barabara kuelekea upande wa kushoto wa Barabara ya Morogoro, gari litakalopata ajali litakuwa ni linalotoka Dar es Salaam kuelekea upande wa Morogoro.
Sikuelewa anamaanisha nini, ikabidi nitulie kuona nini kinachoenda kutokea. Tulisogea pembeni kabisa, umbali wa kama mita mia moja hivi, vichakani kabisa, tukakaa kwa kukunja miguu na kutengeneza duara. Kulikuwa na mbu wengi lakini wote walikuwa wakiishia kutuzunguka tu, hata sijui kwa nini hawakuwa wakituuma.
“Nataka ufumbe macho halafu utulie huku ukitafuna huo mzizi mmoja, nitakachokuuliza unijibu,” baba aliniambia, nikafanya kama alivyoniambia. Cha ajabu, nilipofumba macho tu, japokuwa tulikuwa mbali kidogo na barabara, niliweza kusikia sauti za magari na pikipiki vikipita kwa kasi, cha kushangaza zaidi, niliweza kusikia hata sauti za madereva na abiria, nikashtuka sana.
Nikiwa nimeendelea kutulia, japokuwa nilikuwa nimefumba macho, kadiri nilivyokuwa nikizidi kutafuna ule mzizi ndivyo nilivyoanza kuona taswira ya kila kilichokuwa kikiendelea barabarani utafikiri nilikuwa nimesimama pembeni ya barabara, tena nikiwa nimefumbua macho.
“Unaona magari mangapi?”
“Mengi tu.”
“Yanayoelekea upande wa Morogoro ni mangapi?”
“Ni matatu.”
“Ambalo lipo nyuma kabisa lina abiria wangapi?”
“Abiria mmoja ambaye ni mtoto na dereva mwanamke.”
“Safi, hiyo ndiyo kazi yako ya leo, likazie macho hilo gari kwa nguvu na likikaribia hapo ulipo fumbua macho ghafla halafu tena hicho kilichopo mdomoni mwako,” alisema baba, kweli nikawa nalitazama gari hilo.
Lilikuwa ni gari dogo na ndani yake kulikuwa na watu wawili tu, dereva mwanamke na mtoto, ilionesha ni kama ni wanafamilia wanarudi makwao. Sikuelewa nini kitawapata lakini kwa sababu ya shauku niliyokuwa nayo, nilijikuta nikifanya kile baba alichoniambia, nikafumbua macho ghafla na kutema mabaki ya ule mzizi, nikashtukia nimemtemea baba usoni.
Mara kikasikika kishindo kikubwa kule barabarani, kilichonishtua mno. Sikuelewa nini kimetokea pale kwa sababu nilipokuwa nimefumbamacho, nilikuwa najiona kabisa kwamba nipo barabarani lakini nilipofumbua tu, nilijikuta nikiwa nimekaa palepale tulipokuwa tumekaa na baba na baba yake Rahma.
Kitu cha mwisho nilichokumbuka, wakati nataka kufumbua machom nilimuona yule mwanamke aliyekuwa kwenye usukani, akikunya usukani gahfla kama aliyeona kitu cha hatari mbele na sasa anataka kukikwepa, ndipo kikafuatia kile kishindo.
“Nenda haraka, hakikisha unamtoa mtoto kwenye gari na kuja naye hapa, pale kwenye gari ulipomtoa utaweka hiki,” alisema baba huku akinipa kipande cha mgomba.
Je, nini kitafuatia?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom