Makapuku Forum

Makapuku Forum

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 4
ILIPOISHIA:
Niliondoka kazini nikiwa ni kama nimechanganyikiwa, sikuwa namjua Shenaiza lakini sijui kwa nini nilihisi kama matatizo yake yalikuwa yakinihusu sana. Nikiwa kwenye kituo cha daladala nikiendelea kusubiri usafiri, ujumbe mfupi uliingia kwenye simu yangu, ulisomeka:
“Mwenye simu hii amelazwa Hospitali ya Amana, Ilala. Hali yake ni mbaya, hawezi kuzungumza.”
SASA ENDELEA…
“Mungu wangu,” nilisema baada ya kumaliza kuusoma ujumbe huo. Nilijaribu kuipiga tena namba hiyo, ikapokelewa lakini sauti haikuwa ya Shenaiza, akaniambia yeye ni Rozina, nesi katika hospitali ya Amana na kwamba yeye ndiye aliyekuwa akimhudumia msichana huyo.
Nilimuomba anitajie wodi aliyolazwa msichana huyo, akaniambia niende tu nikifika hospitalini hapo nipige kupitia namba hiyohiyo atakuja kunipokea. Niliita bodaboda na kumuelekeza kukimbia kadiri awezavyo kuelekea Amana. Abiria wengine waliokuwa pale kituoni wakisubiri daladala, walibaki kunishangaa lakini mwenyewe sikujali.
Nikaondoka na bodaboda huku nikimhimiza kuongeza mwendo ili tuwahi kufika. Baada ya kuhangaika sana kwenye foleni, kama ujuavyo Jiji la Dar es Salaam nyakati za jioni, hatimaye tuliwasili Amana. Nikapiga namba ya Shenaiza ambapo yule nesi alipokea tena, nikamweleza kwamba tayari nilikuwa nimefika, akaniambia nimsubiri mapokezi.
Sikuwa hata naijua sura ya huyo Shenaiza mwenyewe kwa sababu hatukuwahi kuonana zaidi ya kusikia sauti yake tu kwenye simu.
Muda mfupi baadaye, alitoka nesi mmoja, mwembamba, mrefu mwenye rangi ya weusi wa asili, akaniuliza kama mimi ndiye niliyekuwa nawasiliana naye kwenye simu. Nilipomjibu kwamba ni mimi, aliniuliza nilikuwa na uhusiano gani na mgonjwa?
Nikamjibu kwamba mimi ni kaka yake, nikamuona akiguna huku akinitazama kwa macho ya udadisi. Sikuelewa kwa nini ananitazama hivyo, nikajikaza kiume na kuonyesha kutobabaika.
“Nifuate!” alisema huku akianza kutembea kuelekea wodini, na mimi nikawa namfuata. Tulipita kwenye korido na kutokezea kwenye wodi za wanawake, nikawa naangaza macho huku na kule wakati tukipita pembeni ya vitanda walivyolazwa wanawake wengi, tukapita na kwenda kwenye wodi iliyokuwa imejitenga peke yake. Yule nesi akafungua mlango na kunipa ishara kwamba niingie.
Japokuwa kulikuwa na vitanda vinne ndani ya wodi hiyo, ni kimoja tu kilichokuwa kimelaliwa na mgonjwa aliyeonesha kutokuwa na fahamu. Yule nesi alinipa ishara kwamba yule ndiyo mgonjwa mwenyewe, nilimtazama kwa mshangao nikiwa kama siamini macho yangu.
Hakuwa Shenaiza yule ambaye nilimjengea picha kichwani mwangu, alikuwa mtu mwingine tofauti kabisa kiasi cha kunifanya nihisi huenda nesi amekosea kunipeleka au hatukuelewana katika mazungumzo yetu.
Hakuwa msichana wa Kitanzania kama nilivyokuwa nimemfikiria, alikuwa na mchanganyiko ambao siwezi kueleza moja kwa moja kama ni Mzungu au ni Mwarabu lakini alikuwa katikati ya jamii hizo mbili. Kiumri alionesha kuwa bado ni binti mdogo tofauti na nilivyomfikiria kwamba anaweza kuwa ni mwanamke mwenye kati ya miaka 25 hadi 30.
Alikuwa amelala tuli kitandani huku akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani, huku jicho lake moja likiwa limebadilika rangi na kuwa na weusi na wekundu kwenye ngozi inayolizunguka jicho kuonesha kwamba damu zilikuwa zimevilia kwa ndani. Pia mkono wake mmoja ulikuwa umezungushiwa bandeji kubwa kuanzia juu kidogo ya kiganja mpaka kwenye kiwiko cha mkono.
Dripu moja sambamba na chupa ya damu vilikuwa vikitiririka kwa kasi kuingia kwenye mishipa yake ya damu, nikajikuta nikipatwa na hali ambayo siwezi kuielezea kwa urahisi. Kwa kifupi, japokuwa bado sikuwa na uhakika kwamba yule ndiye Shenaiza tuliyekuwa tukiwasiliana naye, nilijikuta nikimuonea huruma sana kutokana na hali aliyokuwa nayo.
Nilitamani kujua nini kimemfika mpaka akawa kwenye hali hiyo. Nilitamani pia nimjue yeye ni nani na asili yake ni wapi hasa kwani hakuonesha kuwa Mtanzania japokuwa alikuwa akizungumza vizuri Kiswahili.
“Mbona unamshangaa sana? Kwani mlikuwa mnafahamiana kabla?” yule nesi aliniuliza baada ya kuniona hali niliyokuwa nayo, nilishusha pumzi ndefu na kuzugazuga, nikasogea pembeni ya kitanda cha Shenaiza na kumpa ishara kwamba tusogee pembeni ili tuzungumze zaidi.
“Samahani nesi, hebu nieleze nini kimetokea?”
“Nitakueleza lakini nataka na wewe unieleze ukweli, usije ukanisababishia matatizo kwenye kazi yangu, huyu ni nani kwako?”
“Nimeshakwambia kwamba ni dada yangu.”
“Hapana, siyo kweli! Hebu ngoja kwanza,” alisema huku akienda kuchukua simu iliyokuwa pembeni ya kitanda cha Shenaiza, akanifuata na kuniuliza kama simu yangu nilikuwa nayo, nikamjibu kwamba ninayo, akaniambia nipige namba ya Shenaiza. Nikatoa simu yangu na kutafuta namba yake kisha nikampigia.
“Unaona amekusevu vipi?” aliniuliza yule nesi huku akinionesha jina lililotokea kwenye simu yake, nikabaki nimepigwa na butwaa kutokana na jinsi alivyokuwa amenisevu.
Sikutaka kuendelea kumbishia yule nesi kwa sababu angeweza kupata sababu ya kukataa kunipa ushirikiano baada ya kuamini kwamba nilikuwa nikimdanganya, nikaamua kukubali yaishe, nikamuacha aamini kile mwenyewe alichotaka kukiamini (nitafafanua zaidi baadaye jinsi alivyokuwa amenisevu).
Baada ya kuelewana na nesi huyo, alianza kunieleza kwamba walimpokea mgonjwa huyo majira ya saa tisa za jioni baada ya kuletwa na wasamaria wema ambao walidai wamemkuta amepigwa na kujeruhiwa vibaya nje ya nyumba yao.
“Alikuwa akitokwa na damu nyingi huku pia akiwa na majeraha sehemu mbalimbali za mwili wake, ikabidi tumpokee hivyohivyo na kuanza kumpatia matibabu lakini mpaka sasa hakuna anayejua jina lake, ametokea wapi na nini kilichomsibu, tunasubiri labda akirejewa na fahamu au ndugu zake wakija ndiyo watueleze kilichotokea,” alisema yule nesi, nikashusha pumzi ndefu na kugeuka kumtazama Shenaiza pale kitandani.
Baada ya kumaliza kuzungumza na nesi, nilimuomba niende kukaa pembeni ya Shenaiza mpaka atakaporejewa na fahamu zake lakini aliniambia kuwa ni kinyume na taratibu za hospitali hiyo, akanitaka nikakae nje ya wodi na kama kuna chochote, atanipa taarifa lakini akasisitiza kwamba mgonjwa alikuwa anahitaji damu zaidi kwa sababu amepoteza nyingi, akanitaka kama nipo tayari kumchangia anielekeze nini cha kufanya.
Sikuwa na kipingamizi, nilikubali kumchangia damu, yule nesi akanichukua mpaka kwenye wodi nyingine ambapo alinitambulisha kwa madaktari wenzake na kuwaeleza kwamba nilikuwa nataka kumtolea damu mgonjwa wangu Shenaiza. Nikachukuliwa vipimo vya awali na baada ya kuonekana nilikuwa fiti, niliingizwa kwenye chumba kingine na kuanza kutolewa damu.
Nikiwa naendelea kutoa damu, niliendelea kujiuliza maswali mengi kuhusu Shenaiza yaliyokosa majibu. Kuna wakati nilijilaumu sana kukataa kuonana naye mapema kwani niliamini pengine ningeweza kumsaidia asipatwe na kilichomtokea. Hata hivyo nilijipa moyo kwamba sikuwa nimechelewa, nikawa namuombea kwa Mungu apone na kurudi kwenye hali yake ya kawaida.
Baada ya kumaliza kutolewa damu, nilirudi pale nje ya wodi na kukaa huku nikiendelea kutafakari mambo mengi. Tayari kigiza cha jioni kilishaanza kuingia lakini moyo wangu haukuwa radhi kuondoka hospitalini hapo, nilijiapiza kwamba hata ikibidi kukesha usiku kucha, nitafanya hivyo mpaka nifahamu kilichomsibu Shenaiza.
Ilipofika majira ya kama saa moja za jioni, yule nesi, Rozina alinifuata na kunipa habari ambazo zilinifanya mapigo ya moyo yanilipuke kuliko kawaida. Aliniambia Shenaiza amerejewa na fahamu na jambo la kwanza alilouliza ni kama nilikuwa nimempigia simu.
“Nimemwambia kwamba upo hapa nje, akaniomba sana akuone, lakini anazungumza kwa shida sana,” alisema nesi huyo, nikainuka na kuanza kumfuata harakaharaka kuelekea wodini.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
 
Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 5
ILIPOSHIA:
Aliniambia Shenaiza amerejewa na fahamu na jambo la kwanza alilouliza ni kama nilikuwa nimempigia simu.
“Nimemwambia kwamba upo hapa nje, akaniomba sana akuone, lakini anazungumza kwa shida sana,” alisema nesi huyo, nikainuka na kuanza kumfuata harakaharaka kuelekea wodini.
SASA ENDELEA…
Muda mfupi baadaye, tulikuwa pembeni ya kitanda alichokuwa amelazwa msichana huyo, nesi Rozina akaniambia ananipa dakika chache za kuzungumza na mgonjwa, akatoka na kufunga mlango wa wodi hiyo. Kwa muda wote huo, macho yangu yalikuwa juu ya uso wa msichana huyo ambaye naye alikuwa akinitazama, tukawa tunatazamana.
Tofauti na nilivyofika mara ya kwanza hospitalini hapo, safari hii niliweza kumuona vizuri msichana huyo. Kitu ambacho naomba nikiseme wazi, japokuwa alikuwa kwenye maumivu makali, akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani na jicho lake moja likiwa limevilia damu na kuwa jekundu, Shenaiza alikuwa na sura nzuri mno.
Nilijikuta nikivutiwa naye na kuendelea kumtazama, naye akawa ananitazama bila kusema kitu chochote mpaka nilipoamua kuvunja ukimya.
“Pole dada Shenaiza! Pole sana,” nilisema kwa sauti ya upole, kauli yangu ikawa kama mkuki ndani ya moyo wake kwani badala ya kujibu, alianza kuangua kilio kikali cha kwikwi, machozi mengi yakawa yanachirizika kupitia kwenye pembe za macho yake na kuishia kwenye shuka jeupe alilokuwa amelala juu yake.
Ikabidi nimsogelee zaidi na kumuinamia pale kitandani, kwa kutumia mkono wangu mmoja nikawa namfuta machozi huku nikiendelea kumpa maneno ya kumfariji, nikamuona naye akitoa mkono wake mmoja kwenye shuka na kuushika mkono wangu huku akiendelea kulia, akauvutia kifuani kwake huku akinitazama usoni.
Macho yake ni kama yalikuwa na sumaku kwani katika mazingira ambayo sikuyategemea, na mimi nilijikuta nikianza kulengwalengwa na machozi. Nilijikuta nikimuonea mno huruma msichana huyo na kuwa na shauku kubwa ya kutaka kusikia nini kilichomtokea.
Mpaka muda huo, hakuwa amefumbua mdomo wake na kuzungumza neno hata moja zaidi ya kuendelea kulia tu huku akinitazama kwa macho yaliyobeba ujumbe. Japokuwa na mimi nilijisikia uchungu sana, nilijitahidi kujikaza kiume na kuendelea kumbembeleza.
“Nashukuru kwa upendo wako ulionionesha, kumbe nilivyokuwa nimekutafsiri baada ya kusikia sauti yako mara ya kwanza nilipokosea namba yako ya simu nilikuwa sahihi kabisa,” alisema Shenaiza kwa sauti ya chini mno lakini iliyosikika vizuri kabisa masikioni mwangu.
“Usijali Shenaiza, nipo kwa ajili yako na nitaendelea kuwepo pembeni yako kwa shida na raha,” nilimwambia, kauli ambayo ilimfanya aachie tabasamu hafifu, akaubusu mkono wangu ambao muda wote alikuwa bado ameung’ang’ania.
Kilichonishangaza kwa Shenaiza, japokuwa ndiyo kwanza tulikuwa tunakutana kwa mara ya kwanza, tena akiwa kwenye maumivu makali, alionesha kama ana hisia fulani juu yangu kwa sababu siyo rahisi kumshika mkono kisha ukaubusu kwa mtu ambaye wala hujawahi kumuwazia akilini mwako.
“Halafu kumbe wewe ni kijana mzuri namna hiyo, kwa nini hujaoa mpaka leo,” alisema Shenaiza kwa lafudhi nzuri japo alionesha kuwa na maumivu, nikajikuta nikitabasamu na kukosa cha kumjibu.
“Kwani nini kimekutokea dada’angu?”
“Ni stori ndefu, ngoja nitakusimulia kila kitu nikipata nafuu lakini naomba umwambie na nesi kwamba sihitaji mtu yeyote ajue kwamba nimelazwa hapa, naweza kupata matatizo mengine bure. Naomba wewe ndiyo uwe mtu pekee wa kunisimamia mpaka nitakapopona,” alisema msichana huyo kwa sauti ya chini iliyoonesha bado yupo kwenye maumivu, nikawa natingisha kichwa kuonesha kukubaliana naye.
Kwa muda mfupi niliozungumza na Shenaiza, niligundua kwamba huenda ana jambo zito sana lililokuwa likiusumbua moyo wake na kweli alikuwa akihitaji mtu wa kumsaidia ingawa bado sikuwa najua ni nini kilichokuwa kinamsumbua.
“Nikuulize swali jingine?” nilimhoji, akatingisha kichwa kuonesha kukubali. Nilitaka kumuuliza kuhusu jinsi alivyokuwa amenisevu kwenye simu yake lakini nikahisi huenda nikam-boa kwa swali hilo.
“Uliza tu,” alinisisitiza baada ya kuona nasitasita.
“Kwa nini umenisevu vile kwenye simu yako?”
“Simu yangu? Mungu wangu, we umeonaje wakati hata simu yangu huijui,” alisema msichana huyo huku aibu za kikekike zikiwa zimetawala kwenye uso wake, akawa anakwepesha macho yake ili yasigongane na yangu, tabasamu hafifu likiwa limechanua kwenye uso wake.
Aliendelea kulikwepakwepa swali hilo lakini na mimi niliendelea kumbana hapohapo. Nilichokifanya, niliamua kuipiga namba yake na kwa kuwa simu yake ilikuwa pembeni ya kitanda chake ingawa mwenyewe hakuiona, muda mfupi baadaye ilianza kuita, namba yangu ikiwa imeseviwa ‘My Husband’! Akazidi kujisikia aibu za kikekike na mwisho akafunguka:
“Niliamua kukusevu hivyo kwa sababu ya matatizo yanayonikabili, naomba suala hilo tusilizungumze leo, ipo siku utanielewa,” alisema na kugeukia pembeni kuonesha hakuwa akitaka tuendelee kuzungumzia suala hilo, nikabadilisha mada haraka.
Kingine kilichonishangaza kwa Shenaiza, kila nilichokuwa namuuliza alikuwa akikwepa kunijibu, hakuna jambo hata moja ambalo nilitaka kulijua na akanijibu bila wasiwasi, nilipomuuliza anaishi wapi na anakaa na nani, alikwepa swali hilo kwa maelezo kwamba tutazungumza siku nyingine akiwa amepona.
Nilipomuuliza pia nini kilichomtokea mpaka akaumia hivyo mpaka kulazwa hospitalini hapo, bado hakuwa tayari kunieleza, kisingizio kikawa kilekile kwamba mpaka atakapopona ndiyo atanieleza kila kitu.
Kwa kuwa bado mwili wake haukuwa na nguvu hasa baada ya kupoteza damu nyingi kama alivyonieleza nesi Rozina, nilikubaliana naye. Nilipomuuliza kama angehitaji nini usiku huo kwa ajili ya chakula kwa sababu nilikuwa na uhakika kwamba hajala chochote, aliiambia nikamtafutie juisi tu, inamtosha.
Tayari nesi alishaingia na kunitaka nitoke kwani mgonjwa alikuwa akihitaji mapumziko ya kutosha, nikamwambia kwamba kuna vitu ameniagiza naenda kumnunulia nitarejea baada ya muda mfupi, nesi akaniruhusu huku akisisitiza niwahi kwani kuna muda ukishafika, watu wa kawaida hawaruhusiwi tena kuingia wodini.
Nilitoka haraka na kwenda kwenye maduka yaliyokuwa jirani na hospitali hiyo, nikamnunulia juisi maboksi mawili na keki laini ambazo niliamini atazipenda. Nikarudi wodini na muda mfupi baadaye niliruhusiwa tena kuingia wodini, nikamkuta Shenaiza ametulia pale kitandani, akionesha kuanza kupata ahueni kubwa. Aliponiona tu, tabasamu pana lilichanua kwenye uso wake, nikamsogelea mpaka pale kitandani, nikatoa maboksi ya juisi na keki na kuweka kwenye droo ya pembeni ya kitanda na kumtaka akijisikia ahueni ajitahidi kunywa.
Kwa kuwa muda nao ulikuwa umeyoyoma, nilimuaga kwamba narudi nyumbani lakini nitakuja kumtembelea asubuhi lakini alionesha kuwa mgumu kukubaliana na hilo.
Mara simu yake ilianza kuita mfululizo, akaishika na kutazama namba ya mpigaji lakini katika hali ambayo sikuielewa, aliiachia simu hiyo, ikadondoka chini na kufunguka betri ikaangukia kivyake, mfuniko kivyake na simu nayo kivyake. Akaanza kuangua kilio kwa uchungu huku akiniomba nimsaidie, nilibaki nimepigwa na butwaa.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom