Makapuku Forum

Makapuku Forum

c934209e7ca50fef4975ffb6667eab74.jpg
 
Sehemu ya nne



...... . Ama kwa hakika urafiki tu wa German Machine ulinipa faida kubwa kuliko hata urafiki niliouweka kwa shule. Nilichokivuna kwa German Machine kilikuwa kikubwa kuliko nilichokivuna shule. Hakika ukikaa nae unaweza kufaulu mengi kwenye maisha kuliko aliyesoma. Lakini leo hii ndio hayupo! kwanini German umeenda mapemaa!
||*******||
Kumbukizi zilikatika kilio kikanishika. Sikuweza kujizuia kabisa nikajikuta nanyong'onyea miguu na kushuka chini taratibu. Watu wa huduma ya kwanza waliniwahi.
Ingawa miguu ilinisaliti nguvu ya kuubeba mwili lakini akili ilibaki na utimamu wake. Niliekwa sehemu ya wazi na watu wa huduma ya kwanza ambapo pia kulikuwa na watu wengine wakiwahudumia. Kweli German alipendwa na wengi. Kuahirishwa sherehe za sikukuu ya uhuru ilikuwa si suala dogo kwa Taifa. Hakika alikuwa lulu ya kipekee ambayo hutokea kwa nadra sana kwenye uso wa dunia.
Spika zilizofungwa uwanjani zilisafirisha sauti za kila muongeaji rasmi kwenye shughuli za msiba wa German Machine.
"Wapendwa katika bwana. Neno la Mungu linatukumbusha kuwa kifo si mwisho wa binaadamu bali ni hatua tu ya kuvuka kutoka kwenye ulimwengu wa kimwili na kurudi ulimwengu wa kiroho kwa baba yetu aliye mbinguni. Sisi sote ni wa kwake na kwake tutarejea. Hatupaswi kuhuzunika na kutia kufuru katika kazi ya Mungu ambayo milele haina makosa. Sisi tulimpenda lakini Mungu amempenda zaidi. Kitu cha msingi ni kumuomba bwana ampe raha za milele na itapofika zamu yetu atupokee kwenye falme ya baba. Tunajua kimwili hayuko nasi lakini kiroho mpendwa wetu bado tunaye. Sasa napenda kumkaribisha askofu ANTON SCHWARZ kutoka Ujerumani kwa sala maalum kabla hatujampisha msemaji wa familia kutusomea historia ya mpendwa wetu aliyelala kwenye usingizi wa milele. Asante."
Sauti hii ilinipa nguvu ya kusimama kwa mara nyengine baada ya kupatiwa huduma ya kwanza. Msemaji ambaye alikuwa mchungaji maarufu nchini nilimuona akimkaribisha askofu aliyesafiri kutoka Ujerumani kwaajili ya kuja kumzika German Machine. Kijana mdogo aliyezimika kabla hata kufika robo ya karne toka azaliwe laikini ameweza kulitikisa taifa na dunia kwa ujumla. Uwepo wa askofu yule sambamba na wageni wengine kutoka ulaya kwaajili yake, hakika ulizidi kunidhihirishia kuwa German Machine alichokifanya kitabaki kuwa kwenye kumbukumbu ya vizazi. Alisimama askofu Anton akiwa na mkalimani wake alianza kuongoza sala maalum ambapo uwanja mzima ulizizima utulivu. Kumbukizi zangu zilinirudisha tena mpaka siku ile nilipokuwa kwenye chumba cha German Machine nikishangaa michoro yake huku akinipa elimu ya mambo mawili, Hofu na Imani.
* * * *
||MIAKA 12 NYUMA||
"German hakika mambo unayonambia ni ya kushangaza sana. Wapi unajifunza hivi vitu? Mbona elimu hii hatukufundishwa, we unaitoa wapi?" Nilimuuliza huku nikimtazama kwa mshangao.
"Twaha, kujifunza ni kuamua. Elimu haiko darasani wala shule hazipo kwa ajili ya kuwapa watu elimu ingawa watu wengi wanaamini shule ndipo mahala inapotolewa elimu." Alichonambia safari hii kilinifanya nicheke na kumpinga.
"Hapana German. Hapo umeelewa vibaya na hiko usemacho ni uongo. Shule ndipo panapotolewa elimu na hakuna mtu mwenye elimu ambaye hakusoma." Nilimpinga kutoka moyoni. Lakini alinitazama na kusikitika kisha akaanza kuyachimba maneno yake yaliyonionesha kina cha maana yake ambayo ilinishinda ubishi.
"Twaha usiyatazame maneno kama yalivyo. Kumbuka nilipokwambia juu ya mambo mawili, Imani na Hofu. Bado hujajua kuyatumia ndio maana umewahi kupinga. Sasa nakupa hizi siri ambazo zimefichwa vitabuni hawakuandika tofauti ya SHULE na ELIMU. Na havikufichwa kwa bahati mbaya bali vimefichwa kwa makusudi na watu maalum wa kale waliovumbua shule. Wamefanya hivyo ili watu maalum wazidi kuwa wachache na ndio maana kina Johannes Kepler wamegundua sayari na mambo mengi ya anga katika karne ambazo hakukuwa hata na ndege za kwenda angani wala shule iliyofundisha mambo hayo. Unaweza kujiuliza Johannes Kepler alijuaje mambo ya umbali na jinsi sayari zinavyozunguka ikiwa elimu hiyo haikuwepo shuleni karne hizo? Je wapi aliitoa elimu hiyo? Na vipi kuhusu waliobuni hesabu ambazo tunafundishwa leo ikiwa hapo kabla hazikuwepo? Wapi waliitoa elimu ya ubunifu huo? Je, ushajiuliza mtu wa kwanza kusoma na kuandika alifundishwa na nani? Jiulize kwanza waliipata wapi elimu watu hao wa kale hata wakaja kubuni uwepo wa shule? Sasa nataka nikuthibitishie kuwa elimu haitolewi shule ingawa shule ndiyo sehemu inayoweza kuonesha wapi elimu ilipo ili ukaitafute. Lakini kama utaenda shule kuitafuta elimu hakika utaikosa kwa kuwa haiko huko." Aliongea kwa hisia German Machine na maneno yake hakika yalizidi kunishangaza.
"Sasa kama ni hivyo shule ni nini na kwanini tunaenda?" Nilimuuliza.
"Kaa kitandani nikuoneshe kitu." Alinambia nami nikajisogeza mpaka kwenye kitanda kidogo cha kamba kilichogubikwa na mkeka chakavu. Nilitulia nikimuangalia ambapo aliinama uvunguni mwa kitanda kuna kitu alikivuta.
"Twaha, naomba uniahidi hutoanika haya mambo kwanza." Alisema huku akitoa vibao viwili vilivyotengenezwa kwa pembe tatu kila kimoja.
"Nakuahidi sitomwambia mtu." Nilimuhakikishia ndipo aliponikabidhi kibao kimoja naye alibaki ameshika kile cha pili, kisha akaendelea kunidadavulia kuhusu shule na elimu.
"Nakupa siri iliyoweka tofauti ya Elimu na Shule ambayo wengi hawaijui. SHULE ni sehemu maalum kwa ajili ya kuwafunza watu matokeo ya uvumbuzi, tafiti, maono na mawazo ya watu waliofanikiwa kabla yao ambayo yamekusanywa sehemu moja ili kuzipa changamoto akili zao. Pia ELIMU ni matokeo ya pevuko la akili kuweza kutafiti na kupambanua mambo kwa kina na kuzalisha mawazo ya uvumbuzi hata kuleta mafanikio kwenye maisha ya mtu na vizazi. Sasa watu wenye elimu walizijenga shule ili waweze kuwaonesha wengine elimu zao na vipi walizichuma ili kuyatanua mawazo ya wengine wapate kutumia akili zao na wao wakachume elimu na kuzikusanya shule wapate kufanya muendelezo. Ndio sababu kama utaitumia shule kwa umakini utaiona wapi elimu ilipo na utaifata. Na kama ukiipata na ukaitumia vyema unaweza kuongeza kitu ndani ya shule ili wengine waweze kujifunza pia kupitia wewe." Alipomaliza nilishusha pumzi na kumwambia.
"German Machine wewe si mtu wa kawaida ujue vitu unavyonambia ni vigeni kabisa? Kwa hiyo naweza nisiende shule na nikaipata elimu?"
"Hiyo ni bahati inayoendana na mazingira. Ingawa shule haikupi elimu lakini kumbuka shule ndipo kwenye njia ya kukuonesha wapi elimu ilipo ili uifate ama uiache. Shule ni sehemu ya kuifunza akili yako na kuipa changamoto ipate utambuzi wa kuitafuta elimu ambayo iko nje ya pale. Na utapoipata elimu shule pia itakuhitaji ili iyatumie mawazo yako kuzichangamsha akili za wengine ili nazo zijitambue. Sasa kama hujaenda kabisa shule ili uipate elimu unatakiwa uishi kwenye misingi ile niliyokwambia awali ama upewe kipawa maalum na Mungu na si vyenginevyo."
"Na je, unaweza kusoma shule mpaka umemaliza na usiwe na elimu?"
"Kabisa Twaha. Unaweza kusoma hata ukafaulu masomo mengi lakini bado ukaikosa elimu kichwani mwako na matokeo yake ukawa limbukeni wa mawazo ya watu walioelimika ambayo yametumika kukufundisha tu. Muda ushaenda Twaha kwa leo tuishie hapa ila hiko kibao nilichokupa nenda kakisimamishe kwenye dirisha la nyumba yenu wakati wa asubuhi jua lichomozapo au jioni lizamapo kisha simama kwenye pembe ya chumba ukiwa umelipa kisogo dirisha chukua kioo kimulikie upande wa dirisha na uwe unatazama jua kwa jicho moja kupitia usawa wa kibao tu, Kuna kitu utaona." Alinambia German Machine baada ya kunipa chakula cha ubongo.
"Ni kitu gani nitaona?" Nilimuuliza lakini alinisisitiza nikafanye hivyo nitajionea mwenyewe kisha atanipa tafsiri ya hiko nitachokiona pindi tutapokutana siku nyengine. Daaah! ama kweli maajabu ya German Machine yataendelea kusafiri kwenye ndoto zangu daima. Alinisindikiza siku hiyo baada ya kutoka na kumuaga baba yake aliyekuwa pale pale nje amekaa mkekani ameegama kwenye nyumba yao. Kila hatua niliyopiga niliihisi sauti ya German Machine na maneno yake ambayo hayakuendana kabisa na muonekano wake achilia umri. Nilipofika nyumbani usiku mzima nilimfikiria na kukumbuka maneno yake. Kesho yake niliamka subuhi na mapema niliwahi kufanya kama vile alivyonambia huku nikiwa mwingi wa shauku kujua ni kitu gani amenambia nitaona. Daaah! Jua lilipoanza kuchomoza ukweli nilichokiona kupitia kile kibao alichonipa nilistaajabu mno. German ama kwa hakika ni Machine.......
 
Inayofuataa....



.......Nilipofika nyumbani usiku mzima nilimfikiria na kukumbuka maneno yake. Kesho yake niliamka subuhi na mapema niliwahi kufanya kama vile alivyonambia huku nikiwa mwingi wa shauku kujua ni kitu gani amenambia nitaona. Daaah! Jua lilipoanza kuchomoza ukweli nilichokiona kupitia kile kibao alichonipa nilistaajabu mno. German ama kwa hakika ni Machine.
Mambo yalianza asubuhi na mapema nilipoamka baada ya kupita usiku niliotamani uishe haraka ili nifanye kile nilichoelekezwa na German.
Nililielekea dirisha na kupandisha pazia. Jua lilikuwa ndio linachomoza. Haraka nilichukua kile kibao na kufanya kama nilivyoelekezwa. Nilirudi nyuma na kusimama huku mkononi mwangu nikiwa na kioo. Moja kwa moja nilianza kukodolea macho kioo kilichoonesha kile kibao cha nyuma yangu sambamba na dirisha. Lakini sikuweza kuona chochote cha ajabu. Kijua kilizidi kuchomoza na ndipo nikaanza kukata tamaa kwa kushindwa kung'amua kitu. Lakini nilipogeuka ndipo nilikumbuka German alisema kuwa napaswa kuziba jicho moja pia nisimame kwenye pembe ya chumba. Ndipo nilipofanya hivyo. Looool! ilikuwa kama sinema ambayo sikuwahi kuifikiria. Kadiri kioo kilivyomulikwa na jua kupitia dirishani pale kwenye kibao cha pembe tatu ndivyo niliona maajabu. Cha kwanza nilishangaa kuliona jua likiwa karibu mno kichogoni mwangu katikati mwa kile kibao huku mwangaza wake mwekundu ukizunguka pembe tatu. Cha pili nilistaajabu kujiona uso wangu ukiwa nusu upande ule niliojiziba jicho ukihama taratibu sana kufata muelekeo wa jua dirishani hali ya kuwa mwenyewe nilisimama tu. Bumbuwazi lilizidi baada ya dakika kadhaa mbele nilijiona kupitia kioo uso mzima ukiwa umeliziba jua katikati ya kile kibao cha pembe tatu dirishani huku miale ya jua ikimulika kila pembe nje ya pembe tatu. Nilibaki nimeganda nikijionea maajabu. Dakika zilivyozidi kukatika nilibumbaika kuona najiona uso wangu tu huku kile kibao dirishani kikiwa kimenihama na dirisha nikiliona kwa upande.
"KHA!" Nilistaajabu mabadiliko yale hali ya kuwa sikufanya mzunguko wowote zaidi ya kusimama palepale kwenye pembe ya upande wa chumba. Nilipojaribu kufumbua macho yote mawili nione vizuri lakini ajabu nilipofanya hivyo nilijikuta naumia macho kwa mwangaza wa jua pia sikuweza kujiona uso vizuri. Nilipojiziba tena jicho nilishangaa kuona dirisha limehama zaidi ya awali na sasa nyuma yangu niliposimama kwa asilimia kubwa nilikuwa nauona ukuta wa ndani karibu na dirisha. Ili kukiona kile kibao sasa ilinipasa nipige hatua kuufata usawa wa dirisha.
"Huyu mshikaji German Machine mbona ananistaajabisha na haya mambo? Eeeh!" Nilisema mwenyewe na kugeuka kurudi dirishani. Kutazama nje kulikuwa kumekucha na jua lilishachomoza lote na kupamba anga. Nilirudi kitandani na kujibwaga chali mawazo yakasafiri mpaka kwa kina German Machine.
"kujifunza ni kuamua. Elimu haiko darasani wala shule hazipo kwa ajili ya kuwapa watu elimu. SHULE ni sehemu maalum kwa ajili ya kuwafunza watu matokeo ya uvumbuzi, tafiti, maono na mawazo ya watu waliofanikiwa kabla yao ambayo yamekusanywa sehemu moja ili kuzipa changamoto akili zao. Pia ELIMU ni matokeo ya pevuko la akili inayoweza kutafiti na kupambanua mambo kwa kina na mawazo ya uvumbuzi hata kuleta mafanikio kwenye maisha ya mtu na vizazi. Ingawa shule haikupi elimu lakini kumbuka shule ndipo kwenye njia ya kukuonesha wapi elimu ilipo ili uifate ama uiache." Niliyanukuu baadhi ya maneno ya German Machine aliyonambia jana yake. Kidogo kuna picha ilianza kunijia juu yake. Moyo wangu uliamini kama yeye ni wa tofauti. Nilitamani nimuamshe shangazi kwa shauku nimwambie habari za maajabu ya rafiki yangu mpya shuleni lakini moyo ulisita baada ya kukumbuka ahadi ya German Machine kuwa nisiyaanike popote mambo yale kwanza. Nilishusha pumzi na kufurahi nafsini kumjua rafiki kama yeye. Hapo ndipo shauku ya kujifunza ilipozidi kunivaa.
"Hivi pale kilichotembea ni jua, uso wangu, kioo ama dirisha? Isije kuwa kile kibao ni cha mazingaombwe? Mhh! Kweli kujifunza ni kuamua. Kwa hili lazima nimpekenyue German anambie ukweli tu huenda baba yake alikuwa mwana mazingaombwe zamani naye karithishwa." Niliwaza na kuamua kutoka nje baada ya kumsikia shangazi akifagia mwenyewe uwanja.
"Shikamoo shangazi. Naomba pumzika siku hizi nipo nyumbani kazi hizi nitafanya mimi." Nilimsihi shangazi yangu baada ya kumsalimu huku nikimpokea fagio mikononi mwake. Alitabasamu na kuniacha nifagie. Nyumbani niliishi na shangazi tu ambaye alinilea baada ya wazazi kufariki. Asubuhi hiyo nilifanya kazi bila kuhimizwa hadi ya kuosha vyombo nikijua namfurahisha shangazi ili nipate ruksa yake ya kwenda kijiji cha pili kule kwa kina German Machine. Na kweli baada ya kuchemsha magimbi na kunywa chai nilimuomba shangazi kwenda huko naye akanikubalia ingawa alinisisitiza nisichelewe kama jana yake.
"Nitawahi shangazi sikai sana." Nilimuaga na kuondoka kwa furaha. Shauku yangu ilikuwa kuwahi kwa kina German. Maswali yaliyojengeka kichwani mwangu yalikuwa mengi kwa kile nilichokiona. Naikumbuka sana siku ile kwa jinsi nilivyotembea kwa haraka bila kuchoka. Kiu ya kujifunza na kujua mambo ilinikamata vyema na German Machine nilimuona ndiye maji yenyewe ya kutuliza kiu yangu.
||*******||
"Kweli alistahili kuwa German Machine! mpaka sala yake imefunguliwa na askofu toka Ujerumani? Eeeeh! Mungu kwanini watu wema hawadumu? Aaaaaah! jamaniiiii German...!" sauti ya mwanamke iliyoshiba sikitiko ilisikika pembeni yangu. Mawazo ya zamani yalinitoka na kugeuka kumtazama mwanamke huyo. Alikuwa ni dada mmoja mnene kiasi amesimama akitazama kule kwenye jukwaa maalum ambapo sala ilikuwa inaendelea kuombwa na askofu Anton Schwarz. Nilipomtazama vizuri yule dada akili ilinambia kuwa namjua. Nilifikiria kidogo wapi nilimuona ndipo haraka nikamkumbuka vyema kabisa.
"Tina..Tina!" Nilimwita kwa sauti ya chini yenye mkauko wa kilio cha muda mrefu. Aligeuka kunitazama ndipo tulipokutanisha macho naye akanikumbuka.
"Aaaaaah! TWAHA!" Alitabasamu na kuniita jina langu huku akiwa haamini. Uchungu ulimkaba na kujikuta akichutama na kuuficha uso wake huku akilia kwa sauti na kuombeleza.
"Twahaa yuko wapi German wetu? Twaha..! German anatuuma jamani Mungu kwanini amemchukua mapema hiviiiii! Aaaaah.... Twaha sikuzoea kukuona peke yako lakini wapi Germaan Machine. Mungu baba mrudishe Germaaan uuuuuuuu Jamaniii ameondoka bado dunia inamuhitaajii! Mungu kwanini umemchukua kipindi hiki jamaniiii eeeeeh!" Alilia Tina nami nikachuchumaa kumfariji ingawa pia alinitonesha kidonda kibichi moyoni mwangu. Tulikuwa eneo lile lililotengwa na watu wa huduma ya kwanza.
"Jikaze dada presha yako iko chini la sivyo tutakuhamisha hapa ukizimia kwa mara ya pili!" sauti ya mtoa huduma ilisikika mara alipoinama naye kumnyamazisha Tina. Maneno ya yule dada wa huduma ya kwanza yalinifanya nibaini kuwa Tina alishazimia awali na ndio maana aliletwa upande ule. Nilijitahidi kumtuliza Tina nikijua wazi lazima awe na uchungu wa pekee. Yeye ndiye alikuwa mtu wa kwanza kabisa kusimama na kutusihi tumpongeze German Machine miaka ya nyuma na tukiwa darasani baada ya kufaulu mtihani aliopewa na mwalimu mkuu hata kurudishiwa dictionary yake ya kijerumani. Hakika Tina ndiye alinipa ujasiri wa kusimama pia na kugonga dawati huku nikilitaja jina la German na kulifanya darasa zima lifate mkumbo. Leo hii tumekutana tena kwa machungu kumuaga yule tuliyempongeza huku tukijua ndio hatutaonana tena. Hakika iliuma sana. Aaaaaah! maumivu na uchungu ulizidi nilipoyakumbuka maneno yake German siku ile nilipomtenga kwa kutaka ataje jina lake halisi. Maneno ambayo leo nimeyaamini kwa kuona maana. Nikiwa namfariji Tina sauti ile ya German ilirejea akilini mwangu.
"Kumbukeni kuwa jina halina uhai ila kupitia uhai wako unaweza kulifanya jina likaishi milele. Jina linaloitikwa na moyo wangu ni German Machine." Nilijikuta nami nikianza kulia kwa sauti wakati Tina ameanza kunyamaza. Katikati ya kilio maneno yalinitoroka kumwambia Tina.
"Hakika Tina! Hakikaaa ameweza German. Hakika ameweza kulipa uhai jina lake baada ya kifo chake. Hakikaaa ameweza aaah! Hakika jina lake litaishi milele...Eeee Mungu mueke pema sitamani kulia mimiii" Nililia na kukaa chini kabisa baada ya nguvu za kuchutama kuingia ganzi miguuni. Daaah! Sitakusahau German Machine. Ulichotwambia darasa la sita kuhusu jina ndivyo imekuwa kwa jina lako. GERMAN MACHINE Ama kweli maneno huumba.
....
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom