MBUNGE wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla (CCM), amejikanganya katika maelezo aliyoyatoa kukanusha tuhuma za kutumia vibaya misamaha ya kodi ya mamilioni ya shilingi kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Afya eneo la Uchama, wilayani ya Nzega.
Katika taarifa yake aliiweka kwenye mitandao ya kijamii na vilevile mazungumzo yake na gazeti hili kwa simu, Dk. Kigwangalla alitoa maelezo ya kukinzana ambayo yanatofautiana na yale yaliyoko kwenye nyaraka za kampuni yake ya Emergent Africa Ltd.
Wakati Kigwangalla akisema msamaha wa vifaa hivyo ni kwa ajili ya Ujenzi wa Chuo Cha Afya Nzega (kitakachoitwa International Institute for Health Tabora), nyaraka za TRA na Kituo cha Uwekezaji (TIC) zinataja kituo hicho kama Taasisi ya kisasa ya Kliniki ya Madawa, Afya ya Jamii na Elimu ya Biashara.
Sambamba na hilo, mbunge huyo anadai kuwa na hisa asilimia 40 na mkewe Dk. Bayoum Kigwangalla ana asilimia 11 wakati nyaraka za TIC zinaonyesha kuwa anamiliki asilimia 78 na mkewe 22.
Nyaraka hizo zinaonyesha kuwa kampuni ya Emergent Africa Ltd, ilisajiliwa TIC Septemba 27, 2011 na iliruhusiwa kupata misamaha hiyo kuanzia Septemba 2011 hadi Agosti 2014.
Hata hivyo, akizungumza na gazeti hili, Dk. Kigwangalla alishindwa kufafanua kuhusu utata wa nyaraka kutofautiana tarehe za kuagiza na kupokea bidhaa.
Wakati nyaraka nyingine zikionyesha kuwa manunuzi yalifanyika nchini China Oktoba mosi 2012, nyaraka za TRA zinaonyesha kuwa bidhaa hizo zilishaingizwa nchini tangu Aprili 14 mwaka huo, kupitia kampuni ya Innovative Freight yenye TIN 100-145-596, risiti namba 2012/0000002986.
Pia utata huo, unaonekana katika taarifa za Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ambazo zinaonyesha bidhaa hizo zilikaguliwa Machi 28, 2012 kwa fomu Na 40381.
Kuhusu hilo, Dk. Kigwangalla alisema, "Suala la tarehe ni suala dogo sana, na haliwezi kuathiri bidhaa zilizoingizwa nchini. Wewe unakimbilia kujadili tarehe tu, hilo hata watu wa TRA hawakuangalia tarehe bali bidhaa ndiyo maana wakaruhusu. Pengine tarehe zimekosewa China.
"Na wewe una uelewa mdogo wa mambo ya biashara nakuvumilia tu," alisema.
Dk. Kigwangalla alisema, "Niliwahi kuibiwa bidhaa na nyaraka za dukani, ingawa mke wangu alinizuia kuripoti polisi na sasa nitachukua hatua, we nenda katoe taarifa unayojua, mimi nitakuja tena kuongeza ufafanuzi. Sina uadui na wewe hata Mbowe, nitawashtaki mahakamani kadiri mnavyonichafua."
Aliongeza kuwa bidhaa zilizoingizwa tangu Aprili mwaka jana, hazijauzwa; kwamba ziko katika stoo Dar es Salaam kwani anasubiri kupata mkopo ili aweze kuzisafirisha kwenda wilayani Nzega.
Tanzania Daima ilidokezwa kuwa hata kampuni ya Innovative Freight Forwarders Co. Ltd iliyoshughulikia upakuaji wa mzigo huo na kuutoa bandarini haijalipwa hadi leo.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, meneja wa kampuni hiyo, Queen Mwasanguti, alisema: "Kwa kweli wewe ni mtu wa nne kuniulizia suala hilo, ni kweli sijajua kuna nini, ingawa ni kweli sijalipwa ila kila nikimuuliza Kigwangalla anasema yeye atakuja anikutanishe na vijana wake waliosimamia mizigo hiyo ili aweze kunilipa."
Aliongeza, "Bidhaa ziliingia ndio, sisi tulikabidhiwa nyaraka hizo unazotaja tukashughulikia mizigo hiyo kwa taratibu za kawaida, ingawa ni kweli ‘bill of lading' na ankara za manunuzi ya biashara zilitofautiana."
Kwa mujibu wa makubaliano kati ya kampuni ya Emergent Afica Ltd na TIC, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) iliombwa kuisamehe kodi kampuni hiyo ya Dk. Kigwangala vitu mbalimbali vyenye orodha toka namba 1 hadi 390.
Bidhaa hizo kwa uchache ni kompyuta 1042, mashine za kutolea kopi 12, Printa 12, mashine za kufungia (binding machines) 12, vikokotozi (calculators) 640, projekta 12, ‘video camera' 12, feni 30, vifaa vya simu, maboksi 28, jenereta moja, magari aina ya Toyota 13, malori matatu, Nissan Navarra Pik up nne, Mitsubishi Canter mbili na mabasi madogo manane.