na mwandishi maalum (Rai)
WIKI hii nimesoma Habari kadhaa kupitia magazeti, na nimesikiliza nyingine kupitia redio, huku nyingine nikiziona kwa macho yangu.
Kati ya niliyoyasoma limo hili la kutaka aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, ashitakiwe na wengine wanapendekeza afilisiwe.
Nimesoma hata kiongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM, akitokea huko Tanga, ameamua kusema Lowassa na mawaziri wote waliotuhumiwa wakajiuzulu wafukuzwe ndani ya chama.
Najua kila mtu ana uhuru wa kutoa mawazo yake, hivyo hawa wanaofanya hivyo wanautumia uhuru huo. Hata hivyo, nina kila sababu ya kuamini kuwa uhuru huo unapaswa kutumika vyema. Uhuru bila nidhamu unaweza kugeuka utumwa.
Fukuto, upepo na hali ya hewa tayari imechafuka. Neno ufisadi sasa limekuwa kifungua kinywa, chakula cha mchana na kinywaji wakipendacho wengi. Ni msamiati unaokua kwa kasi kubwa. Huko mitaani leo imefikia hata mwenye kumiliki line za simu mbili anaitwa fisadi.
Rais Jakaya Kikwete wakati anazungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam Februari, mwaka huu, alifafanua kwa kirefu kashfa ya Richmond. Alieleza kukerwa kwake, lakini kabla ya kuhitimisha akamtetea Lowassa. Akawambia wazee wa Dar es Salaam kuwa yaliyomkumba Lowassa ni ajali ya kisiasa.
Hii ndiyo hoja ninayotaka kuijadili leo. Msemo kuwa Baniani mbaya, lakini kiatu cheke dawa au mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, ndiyo msingi wa mjadala wangu.
Nilitaka kumjadili aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge, Dk. Harrison Mwakyembe, lakini pengine kwa kukaa kimya nimepata fursa ya kumfahamu, naye akapata fursa ya kukarabati kauli yake.
Mwanzo Dk. Mwakyembe alisema Richmond ni kampuni ya Waziri Mkuu, Edward Lowassa na swahiba wake Rostam Aziz. Hapa ilikuwa wakati anawasilisha Ripoti ya Kamati Bungeni. Alisisitiza kuwa ilihitaji moyo wa uzalendo wa hali ya juu mtu kuwataja viongozi hawa wawili.
Hata hivyo, wakati anafanya majumuisho baada ya michango ya wabunge, Dk. Mwakyembe kidogo alibadilika. Matambo na mbwembwe japo hazikuisha, ila yalipungua. Kwa hakika alikarabati kauli yake na kusema Lowassa na Rostam hakuna popote walipotajwa na Kamati yake kuwa wamiliki wa Richmond.
Napenda kuamini kauli hii ya Mwakyembe aliyoitoa wakati wa majumuisho ndiyo yenye kusimama. Kwa kwaida wakati tupo jeshini ilikuwa tukiambiwa kuwa amri zote ni halali, ila askari anapaswa kutekeleza ya mwisho. Niazime busara hiyo, kukubaliana na kauli ya mwisho ya Dk. Mwakyembe juu ya umiliki wa Richmond.
Sasa sitajadili mkanganyiko uliotokea na kumfanya Balozi Fulgence Kazaura aikane Kamati kwa barua aliyodai kuwa hajapata kuwaeleza maneno yaliyomfanya Mwakembe na wajumbe wengine wa Kamati Teule waamini kuwa Richmond ilikuwa kampuni ya Lowassa na Rostam.
Nasema hili nalo silijadili tena, kwani Mwakyembe tayari amekwishaweka kumbukumbu sawa, ila jambo moja tu niliseme. Najiuliza na nadhani wapo wengi wenye kujiuliza juu ya mkanganyiko wa maadili hasa unapokuja utendaji wa Kamati hizi.
Kwamba nafahamu Dk. Mwakyembe ni mwanasheria aliyebobea na mwandishi mwandamizi, hapo ndipo nazidi kupata shida kidogo. Kaka yetu huyu amefundisha na anaendelea kufundisha Watanzania wengi wa rika mbalimbali.
Kwamba katika mafundisho yake amekuwa akisisitiza suala la kuaminiana na kulinda vyanzo (confidentiality and anonymity). Na kwamba Daktari huyu wa sheria anajua kuwa maneno ya mitaani wengine wanapenda kuyaita ushu ushu (hearsays), kamwe hayawezi kusimama kama ushahidi mbele ya sheria.
Daktari wetu huyu ameamua kutunga kanuni mpya za uandishi na ushahidi mahakamani. Kwamba anonymity and confidentiality, kwake si muhimu tena na wala havina madhara kwa Kamati Teule nyingine zijazo, ikiwa ilitokea kwamba kweli aliumwa sikio. Kazaura tayari amekana kumuuma sikio, ila hili halijibiki.
Kwake daktari huyu, maneno ya mitaani anayoyaitwa kuumwa sikio, yana nguvu kuliko ushahidi wa kiapo! Namheshimu sana daktari huyu, na wala hapa simsimangi, ila najaribu kufikisha fikra zangu kwako wewe msomaji juu ya falsafa hii mpya.
Jingine ninalodhani halihitaji ujasiri kulisema ni hili la kutompa fursa ya kumhoji Waziri Mkuu, aliyejiuzulu ndugu Lowassa. Kwa hulka ya ubinadamu ni rahisi wajumbe wa kamati kujitetea, lakini hapo ndipo umimi (egoism) unathibitika.
Iwapo ningeazima maneno ya Biblia Takatifu, inasema mtende mwenzio sawa na utakavyo utendewe wewe. Na Biblia inasema kipimo hicho hicho ukitumiacho kumpimia mwenzio, ndicho kitakachotumika kukupimia haki yako mbele ya safari.
Hili nalo sipendi kulisemea sana kwani Jaji Mkuu mstaafu aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, Joseph Warioba, amelisemea vizuri. Hoja iliyotumiwa Kamati Teule kuwa ukubwa wa cheo cha Waziri Mkuu uliwazuia kumuhoji Lowassa inaacha maswali mengi.
Jaji Warioba anasema yeye akiwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, aliwahi kuhojiwa. Alikwenda mbali zaidi akafafanua kuwa hata Rais Ali Hassan Mwinyi, alipata kuhojiwa akiwa Rais.
Hapa ndipo pa kujiuliza. Ilikuwaje Kamati hii haikupata kumbukumbu hizi nyeti na kubaini kuwa kumuhoji Waziri Mkuu si jambo geni kwa Tanzania? Wapo wanaosema Kamati hii ilikuwa na ajenda ya siri, ila binafsi sipendi kuamini hivyo.
Nimesema tangu mwanzo kuwa masuala haya yamejadiliwa kwa kina na wadau mbalimbali. Ifahamike wazi kuwa simtetei Lowassa, Rostam wala Mwakyembe katika hili, ila nasimamia msingi wa hoja. Najiuliza nani msaliti kati ya Lowassa na hao waliomtenda au kutenda yaliyomfikisha alipo leo.
Hapo juu nilisema Rais Kikwete amesema yaliyompata Lowassa ni ajali ya kisiasa. Maneno ya Rais Kikwete, yanakwenda sambamba na hoja ya Dk. Ibrahim Msabaha, japo ilipuuzwa na Dk. Mwakyembe.
Msabaha alisema haya yamekwishatokea, lakini Bunge lijadili mwelekeo na hatima ya taifa siku za usoni, hasa yanapopaswa kufanywa maamuzi kwenye kipindi cha dharura.
Hoja hii wapo wenye kusema inaweza kushughulikiwa kwa kutumia utaratibu wa international shopping sawa na ilivyopendekeza TANESCO wakati wa mchakato wa kumpata mwekezaji wa umeme wa dharura.
Nasema hilo linawezekana, lakini kuna kila sababu ya kufikiria kuwa na utaratibu wa wazi jinsi ya kutatua matatizo ya kitaifa wakati wa dharura.
Ni kiongozi wa ajabu pekee, ambaye angeweza kukaa kimya kutokana na hali ya umeme ilipokuwa imefikia. Sheria ya manunuzi inataka siku 45 za kuitisha zabuni, ikiwa na maana kuwa zilihitajika siku 45 za kuitisha zabuni, huku taifa likizidi kutumbukia gizani.
Narudia, siwatetei Richmond katika hili wala yeyote awaye, ninachojadili ni hoja ya utaratibu wa kutumika wakati wa dharura utakaokubalika kwa jamii yote ya Watanzania pasipo mikwaruzano.
Watanzania tu wepesi wa kusahau mambo. Sitashangaa kukuta hata wakazi wa Kahama na Shinyanga nao wakiwa kwenye mkumbo. Lowassa aliyesifiwa kama mkombozi siku zilizopita, leo ndiye tunampiga mawe na kupendekeza asulubiwe.
Wananchi wa Kahama na Shinyanga Lowassa akiwa Waziri wa Maji na Maendeleo alidiriki kutofautiana na Wamisri kwa ajili yao kuvuta maji ya Ziwa Victoria kutoka Mwanza kwenda Kahama na Shinyanga. Ilihitaji kiongozi mwenye uwezo wa kufanya maamuzi, kitu alichofaha Lowassa na leo maji yapo Shinyanga!
Kama si Lowassa, viwanja vya mnazi mmoja vingekuwa maghorofo ya akina Baghdad. Tunajua Lowassa alivyosimama kidete bungeni mwaka 1994, na kuamuru uzio wa mabati uvunjwe uliokuwa umezungushiwa viwanja vya Mnazi Mmoja Dar es Salaam.
Lowassa huyu huyu alifuta umiliki wa viwanja vya tajiri mmoja anayetamba jijini Dar es Salaam, ambapo leo ndipo yamejengwa majengo ya PPF, International House na majengo mengine kadhaa.
Lowassa huyu huyu aliwafukuza nchini kampuni ya City Water mwaka 2005, waliposhindwa kutimiza masharti yaliyokuwamo kwenye mkataba. City Water walikwenda mahakamani, lakini hasilani hawakushinda kesi. Wakatakiwa kuilipa Serikali ya Tanzania sh bilioni 15.
Ni Lowassa huyu huyu aliyesimamia ujenzi wa shule za sekondari za kata. Hoja kwamba hazina walimu ni sahihi, lakini lipo swali la kujiuliza. Hivi kipi bora, kutokuwa na vyote viwili; shule na walimu au kuanza na kimoja?
Wapo wenye hoja sahihi kabisa kuwa Serikali ingeanza na kufundisha walimu kabla ya kujenga shule, lakini walimu hawa hawa iwapo wangehitimu na kukosa ajira, hoja hii hii ingegeuzwa na kudaiwa kuwa Serikali ilipaswa kujenga shule kwanza kabla ya kufundisha walimu.
Kwamba shule zinapokuwapo, kasi ya mahitaji ya walimu inakuwa na mashiko (real) badahala ya dhahania (imaginary). Hakuna safari isiyokuwa na hatua ya mwanzo.
Ni Lowassa huyu huyu aliyesimamia chakula cha njaa kikasambazwa kila tarafa, kata hadi kijiji. Ni Lowassa huyu huyu aliyepunguza foleni jijini Dar es Salaam kwa utaratibu wa njia tatu. Kwamba leo karibu barabara zote za jiji la Dar es Salaam zinapanuliwa kwa maelekezo yake.
Nimetangulia kusema kuwa kwa kipindi kirefu sikuweza kuandika makala yoyote kutokana na mazingira iliyowasilishiwa Ripoti ya Richmond. Kwamba mwanzo Dk. Mwakyembe aliamua kuwaeleza Watanzania kuwa Lowassa ni fisadi (by implication), lakini wakati wa majumuisho akakarabati kauli yake.
Hili la kukarabati kauli yake ndilo lililonifunua macho. Nikaanza kujiuliza maswali mengi. Nikajiuliza Dk. Mwakyembe alishindwa nini kutoa ufafanuzi huu kwamba Lowassa habanwi kwa ufisadi bali kwa uwajibikaji wa pamoja kama msimamizi mkuu wa shughuli za serikali, pale Lowassa alipojieleza na kufafanua alivyoonewa.
Dk. Mwakyembe alipobaini kuwa Lowassa alikuwa hajaisoma vyema ripoti hiyo kwa nini hakusimama kuweka kumbukumbu sawa kuwa hahusiki katika ufisadi bali kushindwa kwake kusimamia watendaji?
Kwamba Mwakyembe akiyajua hayo, alikaa kimya kwa siku nne mfululizo wabunge nao wakajadili hoja iliyopotoshwa, huku akijua kuwa wabunge wanajenga hoja katika dhana isiyo sahihi, hadi wakapendekeza Lowassa anyongwe, afilisiwe na matusi ya kila aina, ni aibu!
Mwakyembe alishindwa nini kusimama katikati ya mjadala na kuomba mwongozo wa Spika akafafanua hayo aliyoyasema kwenye majumuisho kwa nia ya kuepusha wabunge wasijadili hoja isiyo sahihi? Hapa kuna namna!
Lowassa ameonyesha uungwana wa hali ya juu. Yeye ameamua kujiuzulu wadhifa aliokuwanao. Ingawa jamii imekwishaamini hayo yaliyosemwa juu yake, bado anayo fursa. Alipokuwa Monduli, alieleza mchakato mzima ulivyokwenda na nani alifanya nini. Dk. Ibrahim Msabaha na Mwanasheria Mkuu, Johnson Mwanyika, hadi kesho hawajawahi kujibu hoja za Lowassa. Wanajua walichofanya.
Nimalizie makala hii, kwa kuchavusha fikra zetu. Rais Kikwete amesema yaliyomkuba Lowassa ni ajali ya kisiasa. Naamini Lowassa alipokuwa akifanya maamuzi mengi kati ya niliyoyataja hapo juu, tulimshangilia na kumsifia kama kiongozi shupavu.
Najua fika Tanzania ina kiu ya viongozi wenye kuthubutu. Viongozi wanaoweza kufikiri na wakatenda bila hofu. Lowassa ni mmoja wao. Siwezi kumsemea, natumaini yeye anayo maelezo mazuri katika hili, ila kuna kila dalili kuwa hakutendewa haki hata kabla ya Kamati Teule kuundwa. Swali ni je, utamaduni huu wa kumalizana unatupeleka wapi?