YAFUATAYO ni masimulizi mafupi ya kipindi
kifupi cha Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari,
1964 yaliyoipindua serikali ya ubia ya chama cha
Zanzibar Nationalist (maarufu Hizbu) na kile cha
Zanzibar and Pemba Peoples Party (ZPPP).
Tunaangazia nini hasa kilitokea usiku wa
Jumamosi Januari 11, yaliyojiri siku ya pili yake
na mwezi mzima wa Januari, mwaka 1964 .
Tumeyakusanya masimulizi haya baada ya
kuzungumza na walioshiriki katika Mapinduzi
hayo ambao baadaye walisaidia kudhibiti
madaraka na kuunda taasisi zilizoziba pengo la
Serikali iliyopinduliwa ya Waziri Mkuu,
Muhammed Shamte Hamadi.
Usiku wa manane wa Januari 11, makada
wapatao 200 wa Umoja wa Vijana wa Afro-
Shirazi (Afro-Shirazi Youth League) walielekea
kwenye kambi ya polisi ya Ziwani, nje kidogo ya
mji huko Unguja.
Wakiongozwa na Yusuf Himid wapinduzi hao
hawakukabiliwa na upinzani walipofika Ziwani ila
waliikuta ghala ya silaha iko wazi na
wakazinyakua silaha na kukimbia nazo hadi
kwenye uwanja ulio nje ya jengo la Raha Leo.
Hapo ndipo palipokuwa makao makuu ya
Mapinduzi kwa siku chache na ndipo wapinduzi
walikokuwa wakipewa silaha. Studio za redio ya
Serikali pia zilikuwa hapo.
Moja ya sababu zilizoyafanya Mapinduzi
yafanikiwe haraka ni uamuzi wa viongozi wa
Serikali iliyopinduliwa Sheikh Muhammed
Shamte na Sheikh Ali Muhsin Barwani
kuwataka wafuasi wao wasitumie nguvu
kuyapinga.
Hivyo, mbali na mapigano yaliyozuka saa za
asubuhi ya Jumapili Januari 12, mbele ya
Steshini ya Polisi Malindi, hapajazuka mapigano
Unguja kati ya waliopindua na waliopinduliwa.
Pemba nako pia hakukuwa na upinzani
ijapokuwa kisiwa hicho kilikuwa ngome ya vyama
vya ZNP na ZPPP.
Wengi wa wapiganaji waliokuwa kwenye
Stesheni ya Polisi ya Malindi walikuwa wakuu wa
polisi Wakiingereza. Wakipigana na makada wa
Umma Party ambao ndio pia waliouteka uwanja
wa ndege, bandari pamoja na kituo cha
mawasiliano ya nje cha Cable & Wireless,
kilichokuwa kwenye jengo ambalo sasa ni Hoteli
ya Serena Mji Mkongwe.
Kwa hakika, kinyume cha baadhi ya watu
walivyoandika hapakutokea mauaji ya kimbari.
Aliyeanzisha uvumi huo alikuwa John Okello
aliyeandika kwenye kitabu chake kuhusu
Mapinduzi ya Zanzibar kwamba watu zaidi ya
elfu kumi waliuliwa. Okello aliongeza kwamba
aliamrishwa na Yesu Kristo kuwakomboa
Waafrika wa Zanzibar kutoka kwa wageni.
Tutamrejelea Okello na wengine waliokuwa Raha
Leo baadaye. Kwanza tukumbushe kwamba
mkesha wa Januari 12, mwaka 1964, Zanzibar
haikuwa na jeshi. Kulikuwa polisi waliokuwa
wakiongozwa na Waingereza. Wengi wa askari
polisi walikuwa raia wa Tanganyika. Serikali
iliyopinduliwa ilikataa kuandikiana mkataba wa
kijeshi na Uingereza kwa sababu ikihisi mkataba
kama huo utaonekana kuwa wa kikoloni.
Hatuwezi kusema ni nani hasa aliyepiga risasi ya
mwanzo au ya mwisho katika Mapinduzi.
Naitoshe tusemapo kwamba kwa vile hakukuwa
na upinzani, Serikali iliyokuwa madarakani
iliporomoka kama nyumba ya karata.
Tuwarejelee sasa waliokuwa Raha Leo, makao
makuu ya Mapinduzi kwa siku chache. Kwanza
tumuangalie Okello ambaye sauti yake ndiyo
iliyokuwa ikivuma kwenye Redio Zanzibar.
Hatuna uhakika nani alimpeleka Okello Raha
Leo. Wengine wanasema ni Yusuf Himidi.
Wengine wanasema ni Seif Bakari aliyetoa rai
atumiwe kutoa matangazo kwenye redio kwa
vile sauti yake ilikuwa na lafudhi ngeni ya
kutisha.
Uhakika tulio nao ni kwamba Okello alipotokea
Raha Leo na mabastola yake, Aboud Jumbe
alishtuka na akauliza: Nani huyu? Katokea
wapi?
Kijana huyo aliyekuwa na umri wa miaka 27
hakujulikana kabla ya Mapinduzi. Alikuwa mtu
asiyejua kuandika wala kusoma na akili zake
zikimtosha mwenyewe. Hakuwa na sifa za
uongozi na wala hakushiriki katika vuguvugu
lolote la kisiasa.
Akijibandika cheo cha kijeshi cha Field Marshall
ni yeye aliyetangaza kwamba serikali ya ZNP/
ZPPP imepinduliwa.
Kwa hakika, kazi hiyo ya kutangaza kufanikiwa
kwa Mapinduzi kwanza alipewa Ramadhan Haji,
mmoja wa wapinduzi. Lakini alikataa. Jina la
Okello lisingelisikika lau Ramadhan Haji
angekubali kutangaza kwamba Serikali
imepinduliwa na kwamba wapinduzi waliidhibiti
nchi.
Waliokuwa wakiongoza mambo Raha Leo tangu
Mapinduzi yaanze, hadi Jumatatu Januari 13,
walikuwa Aboud Jumbe, mmoja wa viongozi wa
chama cha Afro-Shirazi (ASP), Thabit Kombo
(Katibu Mkuu wa ASP) na Badawi Qullatein wa
Umma Party. Muda wote huo, Sheikh Abeid
Amani Karume (kiongozi wa ASP), Abdulrahman
Babu (mwenyekiti wa Umma Party) na Abdalla
Kassim Hanga (ASP) walikuwa Dar es Salaam.
Mnamo siku hizo hizo liliundwa Baraza la
Mapinduzi na Baraza la Mawaziri lililokuwa na
mamlaka kamili ya kuiendesha Zanzibar.
Mabaraza hayo mawili yalikuwa taasisi kuu za
Serikali ya kimapinduzi ya Jamhuri ya Watu wa
Zanzibar. Na sio ile iitwayo Kamati ya Watu
Kumi na Nne ambayo baadhi ya watu
wanasema kuwa ndiyo iliyoandaa Mapinduzi.
Okello akipenda kujigamba kwamba ndiye
aliyeyapanga na kuyaongoza Mapinduzi. Alikuwa
akitoa matamshi ya kushtusha na ya ajabu-
ajabu kwenye Redio Zanzibar. Kwa mfano, siku
moja alidai kwamba alipwe mshahara mkubwa
zaidi ya aliokuwa akilipwa Rais Karume. Siku
nyingine akasema kwamba kasri zote alizokuwa
akitumia sultani kupumzikia apewe yeye.
Kuna siku aliyotoa hukumu kwamba mzee
mmoja wa zaidi ya miaka 60 afungwe kwa
miaka 99. Alisema kama huyo bwana atakufa
gerezani basi mwanawe afungwe ili kuendeleza
kifungo na mwanawe akifa basi mjukuu wake
afungwe mpaka itimie miaka 99.
Nyakati nyingine aliwaonya watu wazitie moto
familia zao na wao wenyewe mpaka wafe kabla
ya majeshi yangu kuja. Alikuwa akitoa vitisho
visivyowahi kamwe kusikika Zanzibar.
Kuna siku alitangaza kwamba wakazi wa eneo
moja ambako alikuwa apite, wajipange foleni
barabarani wakiwa wamevaa chupi tu.
Okello alikuwa ni adha, kitisho, kichekesho na
fedheha kwa Zanzibar. Viongozi wapya wa nchi
walichoka naye na wakaamua kumchukulia
hatua. Salim Rashid, mmoja wa viongozi wa
Umma Party aliyekuwa katibu wa Baraza la
Mapinduzi anasema kwamba, kwanza
alilizungumza suala la Okello na Sheikh Karume.
Halafu akalizungumza na Brigadia Yusuf Himid
na mwisho yeye, Yusuf Himid na Kanali Ali
Mahfoudh wakalitafutia dawa.
Ilisadifu kuwa siku moja Okello alisafiri kwenda
Dar es Salaam akifuatana na Jaha Ubwa,
aliyekuwa katibu wake. Walipokuwa
wanatarajiwa kurudi Zanzibar, Karume, Yusuf
Himid, Salim Rashid na Ali Mahfoudh
walikwenda uwanja wa ndege kumsubiri.
Siku hiyo anaikumbuka vizuri Luteni Hashil Seif
aliyekuwa ofisa wa zamu kwenye kambi ya jeshi
huko Migombani karibu na uwanja wa ndege.
Alipigiwa simu akitakiwa aende kwa haraka
uwanja wa ndege. Hakuambiwa anaitiwa nini.
Alipofika ndipo alipoambiwa kwamba kuna
ndege ya Shirika la Ndege la Afrika ya Mashariki
iliyokuwa inakuja kutoka Dar es Salaam ndani
yake wakiwemo pia Okello na Jaha Ubwa.
Akaelezwa kwamba awaruhusu abiria wote
pamoja na Ubwa washuke, lakini amzuie Okello
asishuke. Halafu amwambie rubani ampeleke
Okello Kenya.
Hashil naye akampigia simu komredi mwenzake
Luteni Amour Dugheshina kumwita aende
uwanja wa ndege amsaidie. Maluteni wote
wawili walikuwa na bunduki za aina ya machine
gun.
Ndege ilipotua walipanda ndani ya ndege,
wakampokonya silaha Okello na kutekeleza
amri waliopewa. Rubani wa ndege alikasirika
sana. Uso wake ulighadhibika, utafikiri mnyama
aliyekosewa risasi, alieleza Hashil.
Lakini rubani hakuwa na la kufanya ila kuiwasha
ndege na kuelekea Kenya.
Huku nyuma Salim Rashid akampigia simu
Oginga Odinga, Makamu wa Rais wa Kenya,
kumuarifu kwamba wamemfukuza Okello na
wanamrejesha Kenya. Alifanya hivyo kwa
makosa kwa sababu kutokana na jina lake
akifikiri kuwa Okello ni Mjaluo kutoka Kenya.
Kumbe alikuwa mtu wa kabila la Acholi
aliyezaliwa Uganda na alikwenda Unguja kabla
ya kuhamia Pemba ambako alikuwa mwashi,
mtiaji rangi nyumba na mpasuaji mawe.
Swali la kujiuliza hapa ni; je, iwapo kweli Okello
alikuwa kiongozi mpendwa wa Mapinduzi
ilikuwaje wafuasi wake na wanamapinduzi
wenzake wasimtetee alipoadhiriwa uwanja wa
ndege na kufukuzwa nchini? Ilikuwaje
akafukuzwa kwa urahisi hivyo?
Kuna uzushi mwingi kuhusu kipindi hiki kifupi
cha historia ya Zanzibar. Kwa mfano, kuna
filamu ya kubuni ya Wataliana inayoonyesha
maiti chungu nzima za watu waliopigwa risasi.
Filamu hiyo ilikuwa na lengo moja tu; kuonyesha
ukatili na unyama wa Waafrika.
Hakuna ithibati yoyote kwamba watu waliouawa
katika siku za mwanzo za Mapinduzi walifika elfu
kumi. Ukweli ni kwamba jumla ya watu
waliouawa siku hizo haipindukii 200, katika
sehemu za mjini hawazidi 25.
Uzushi mwingine ni kwamba walipelekwa
Watanganyika, Zanzibar wakiwa na silaha
kwenda kupindua. Na si kweli kwamba
Mapinduzi yalikuwa na msisitizo wa kikabila.
Katika kipindi cha mwanzo cha Mapinduzi
msisitizo ulikuwa wa kitabaka. Nyimbo
zilizokuwa zikiimbwa kwenye Redio Zanzibar
zikiwazungumzia wakwezi na wakulima na
wafanyakazi kwa jumla na si makabila.
Mapinduzi ya Zanzibar yalianzisha taasisi mpya
za utawala zikiwa pamoja na Baraza la
Mapinduzi, Baraza la Mawaziri na ofisi ya Rais.
Taasisi hizo zilikuwa zifanye kazi kwa muda wa
mwaka mmoja tu kwa vile ilikwishaamuliwa
kwamba Januari 1965 pafanywe uchaguzi wa
kulichagua Bunge la Katiba, lililokuwa litunge
Katiba ya kudumu ya Zanzibar.
Baraza la Mapinduzi la Zanzibar pamoja na
Serikali mpya zilianza kwa ubia baina ya chama
cha ASP na Umma Party. Ingawa wanachama wa
ASP ndio waliofanya Mapinduzi waliutambua
mchango wa wafuasi wa Umma Party na hasa
mchango wa makada wao waliopata mafunzo ya
kijeshi nchini Cuba.
Vijana hao wa Umma walizitia wasiwasi serikali
za Marekani na Uingereza na kuzifanya ziamini
kuwa utawala mpya wa Zanzibar ulikuwa wa
kikomunisti. Dhana hiyo ndiyo iliyosababisha
kuchukuliwa hatua ya kuyachimba na
kuyagandamiza Mapinduzi ya Zanzibar
yaliyodumu kutoka Januari 12, hadi 26 Aprili,
mwaka