Stuka

JF-Expert Member
Jul 19, 2022
214
686
UCHAMBUZI WA KIJANA MZALENDO, DEVID LEVI NKINDIKWA KUHUSU MGOGORO WA MKATABA WA BANDARI LEO TAREHE 22/7/2023

1. UTANGULIZI

MKATABA WA IGA BAINA YA TANZANIA NA EMIRATE YA DUBAI


Pamoja na Maoni na ushauri unaotolewa na wananchi kuhusu kufanya marekebisho ya Ibara zenye kasoro katika mkataba wa Bandari, lakini Serikali imeamua kukaidi na kukubali mkataba huu uanze kutekelezwa kama ulivyo pamoja na dosari zake zote zilizopo. Hili ni jambo la kusikitisha sana kwa nchi inayozingatia utawala bora na wa kidemokrasia, Tuunganishe nguvu pamoja na kwa gharama yoyote tukaupinge mkataba huu na kuishinikiza Serikali iufute.

2. MATAMKO YA VIONGOZI KUHUSU MKATABA TATA WA BANDARI

Hapa nataka niongelee Viongozi watatu (3) ambao wameonekana kuutetea hadharani na kwa nguvu kubwa mkataba huu licha ya changamoto zake ambao ni Dk. Tulia, Prof. Kitila na Chongolo.

(i) Dk. Tulia Ackson, Spika wa Bunge, ametoa matamshi ya kukashifu na kuwatukana wale wote wanaokosoa vipengele vya mkabata huo kwa kudai kuwa hawajawahi kupitisha hata t-shirt moja bandarini na kuwaita
wapumbavu huku akijinasibu kuwa yeye ni mtu mwenye elimu kubwa katika sheria.

Spika Tulia hana mamlaka ya kuwatukana wapumbavu watanzania na atambue kuwa hizi Bandari ni Maliasili ya Watanzania wote, lakini pia Kauli zake zinakwenda kinyume na Katiba na Sheria za nchi na maadili
ya Viongozi wa Umma zinazolinda thamani ya utu na kuheshimu uhuru wa kutoa mawazo.

Kwa Muktadha huu, Ndugu Tulia Ackson amepoteza sifa ya kuendelea kushika wadhifa wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo anayo Nafasi ya kujipima, kujitathmini na kujiuzulu kwa
hiari Nafasi ya Spika.

(ii) Prof. Kitila Mkumbo, Waziri wa Mipango na Uwekezaji, anadai kwamba watanzania waridhie mkataba huu kwani hata kama una kasoro ipo Nafasi ya kuuvunja huko mbeleni huku akitolea mifano ya Mikataba
Mibovu iliyowahi kuingiwa na ikavunjwa na Serikali ametolea mfano mkataba na City Water, Net group Solution na Mikataba mingine ya madini Kauli hizi amezitoa huku akijitapa kuwa yeye ni msomi wa
kimataifa.

Kiongozi huyu mwenye dhamana kubwa anaongea bila aibu huku akijua fika nchi yetu imeingia hasara kubwa kutokana na Mikataba Mibovu inayoingiwa na Serikali kama alivyoitaja Mwenyewe na mifano mingine
mingi kama Mkataba mbovu wa Symbion ambao Serikali imelipa zaidi Bilioni 360, malipo hewa ya IPTL zaidi ya Bilioni 340, Ndege yetu kushikiliwa Uholanzi kwa madai ya mabilioni ya Shilingi na Mikataba
mingine ya madini ambayo kwa ujumla imeliacha taifa na wananchi wake kuwa masikini na ombaomba.

Profesa Kitila Mkumbo Waziri wa Mipango na Uwekezaji ameanza vibaya na hawezi kuaminika tena mbele ya umma wa watanzania, unaacha kufanya maamuzi na kutoa ushauri kwa misingi ya kitaaluma,vigezo vya utafiti na uhalisia na badala yake unaongea kishabiki ili kufanikisha madili yaliyopangwa ya kuuza Bandari zetu kwa Mwarabu. KWELII. Umekumbwa na nini Profesa? Kama taifa tumeshaingizwa kwenye Mikataba Mibovu kiasi cha kutosha. Hatutakubali tena ushauri wa ovyo kama wa Prof. Kitila.

(iii) Daniel Chongolo, Katibu Mkuu wa CCM anasema ni wajinga wanaokosoa mkataba wa IGA kauli hii ni kinyume cha Katiba na Sheria za nchi na Miiko ya Viongozi wa CCM kuhusu kuheshimu utu na uhuru
wa kutoa maoni.

Kauli yake nyingine ni ile aliyoitoa kwenye Mkutano wa hadhara wa mikoa ya nyanda za juu kusini, uliofanyika jijini Mbeya tarehe 15.7.2023 ambapo alisema Serikali isihangaike kutoa Ufafanuzi juu ya mkataba huo
bali waachiwe wao Chama cha Mapinduzi kutoa Ufafanuzi na akaiagiza Serikali iharakishe kwenda hatua ya pili ya mchakato wa kuingia Mikataba ya utekelezaji.

Nataka nimkumbushe kwamba, Serikali inashauriwa kupitia vikao vya kikanuni na sio mtu binafsi, lakini pia Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) kilichofanyika Dodoma Tarehe 9/7/2023 kiliagiza Serikali itoe elimu na isikilize Maoni ya wananchi kuhusu mkataba wa Bandari. Maagizo yake ni kinyume na maagizo ya vikao halali vya Chama na pia sio kazi ya Chama Kuridhia Mikataba wala kuzunguka nchi nzima kutoa elimu ya mikabata iliyoingiwa na Serikali.

Mbona hatukumuona Katibu Mkuu huyu akifanya ziara nchi nzima kuhusu kupanda kwa gharama za chakula na bidhaa nchini, tatizo la kukatika kwa umeme kwa zaidi ya miaka 2 na ugumu wa maisha nchini? Mbona hatukumuona akifanya ziara nchi kulaani wizi na ufisadi mkubwa uliotajwa kwenye Ripoti ya CAG ambapo matrilioni ya fedha yamepotea, dhuluma wanazofanyiwa wafugaji wa nchi hii, matatizo ya kuhamisha
wananchi wa Ngorongoro, kuanguka kwa bei za mazao kama Pamba na Alizeti na mengineyo.

leo hii Katibu Mkuu wa CCM anazunguka nchi nzima kutetea mkataba wa ovyo wa Bandari, Je ana maslahi gani binafsi katika Mkataba huu? Kiufupi Viongozi hawa niliowataja wameshindwa kujibu hoja zinazoibuliwa na
wananchi katika mkataba wa IGA na badala yake wanaishia kutukana na kujipata kuhusu elimu zao.

3. MKUTANO WA WAZIRI WA UJENZI, TIMU YA SERIKALI YA MAJADILIANO NA JUKWAA LA WAHARIRI KUHUSU MKATABA WA BANDARI TAREHE 14/7/2023

Nilifuatilia kwa makini mjadala huo ambapo asilimia 90 ya maswali 40 yaliulizwa na Wahariri wetu yalikosa majibu, Nichukue Nafasi hii kuwapongeza sana Wahariri wa vyombo vya habari kwa kuuliza maswali mazuri na ya kizalendo kwa niaba ya wananchi ambayo yameibua mambo mapya yaliyoacha maswali mengi
kwa umma wa watanzania. Kwa ufupi ni kama ifuatavyo,

(i) Mwanasheria wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Ndugu Mohamed Salum akijibu swali la Mhariri ndugu Nevil
Meena ambaye alitaka kujua nini kilichosababisha Serikali kupeleka kwa haraka Bungeni mkataba huo
bila kuwashirikisha wananchi kwenye hatua za awali? Mwanasheria wa Wizara Ndugu Salum alijibu kuwa mkataba baada ya kusainiwa Oktoba 25, 2022 ulipelekwa Bungeni Februari 2023 kwa ajili ya hatua za
uridhiwaji ambapo alisisitiza kuwa kabla ya Azimio halijapelekwa Bungeni lilipitiwa na Mfumo mzima wa Serikali ambao ni Wakurugenzi wote wa Sera na Mipango (DPP), Makatibu Wakuu wote chini ya mwenyekiti wao Katibu Mkuu Kiongozi (CS) na Baraza la Mawaziri ambapo Mhe. Rais ndiye Mwenyekiti ambapo wote kwa pamoja
waliridhia mkataba huo kwenda Bungeni. Majibu haya yanazua maswali mengi

(a) Je Kwanini Mheshimiwa Rais hakuutangazia umma kusudio la kuingia mkataba huo? Mkataba huu haukuwahi kufahamika hadi ulipovuja kwenye mitandao ya Kijamii Juni 2023, binafsi nimefuatilia
hakuna hata picha yoyote inayowaonyesha Viongozi wakisaini mkataba huo.

(b) Je Kwanini Spika wa Bunge Dk. Tulia Ackson hakulijulisha Bunge na watanzania kupokea pendekezo la Azimio la Kuridhia Mkataba wa IGA kati ya Tanzania na Dubai tangu alipokabidhiwa na Serikali Mwezi
Februari 2023? Mkataba huu umewafikia wananchi baada ya kuvuja kwenye mitandao Juni 2023 miezi 4 baadaye.

(c) Kama Spika alipokea Azimio hilo miezi 4 iliyopita nini kilichopelekea Spika huyo kutoa muda wa siku 1 kwa watanzania kufika Dodoma na kutoa Maoni? Vilevile upande wa wabunge walipewa masaa 5 tu kujadili na kupitisha Azimio hilo tarehe 10/6/2023 huku wabunge wengi wakikosa Nafasi ya kutoa Maoni yao ndani ya bunge.

Kwa ufupi maamuzi haya ya Serikali na Spika katika uwasilishaji na uidhinishaji wa mkataba huu ni kinyume cha Kifungu cha 12 cha Sheria za Umiliki wa Rasilimali na Maliasili Na. 5 ya Mwaka 2017, Sheria ya
TEITI ambacho kinataka ushirikishwaji wa wananchi na Bunge katika hatua zote na pia ni kinyume na Mkataba wa Umoja wa Mataifa.

(ii) Mhariri wa Gazeti la Mwanahalisi, Ndugu Saed Kubenea aliuliza kuhusu mkopo wa Benki ya Dunia uliyotumika kuboresha Bandari ikiwemo Kitengo cha TEHAMA, kasoro za utiaji saini mkataba, namna kampuni
za wazawa zitakavyoingia Ubia na DP World wa asilimia 35. Kwa ujumla maswali yote ya Mhariri huyu Mbobevu na Mbunge Mstaafu wa Ubungo Ndugu Saed Kubenea hayakupata majibu ya Serikali na badala
yake yamezua maswali mengi kwenye umma na kujiuliza kulikoni?

(a) Mgawanyo wa hisa wa asilimia 35 kwa makampuni ya wazawa ulipatikanaje, wakati feasibility study haijafanyika na mikataba baina ya TPA na DPW haijaisainiwa? Hivi ni vipengele vya mkataba wa HGAs na tumeshaambiwa Mikataba hii bado hawajaanza mazungumzo, Na hapa inanifanya niamini maneno ya Mheshimiwa Kubenea kwamba hawa wanaopigia debe mkataba huu mbovu ndiyo
wenye hisa za asilimia 35.

(b)Tathmini ya Mkopo wa Benki ya Dunia kupitia mradi wa uboreshaji wa Bandari (DMGP) haijafanyika na hakuna Maelezo ya kina yaliyotolewa kwenye Hotuba ya Waziri siku ya kuwasilisha Azimio Bungeni, Mfano eneo la TEHAMA ambapo Mheshimiwa Kubenea ameuliza, akijibu Mkurugenzi wa TPA, Ndugu Mbossa anakiri bayana
kuwa hajui scope ya mradi huo, sasa kama ndivyo, Serikali imewezaje kumpa DP World maeneo hayo yanayofanyiwa maboresho makubwa na Serikali kabla ya tathmini ya kina kufanyika?

(c) Kwa mujibu wa kifungu cha 28 cha Mkataba wa IGA kinataka wanaoweka saini kwenye mkataba wawe wamepewa mamlaka kamili kutoka pande zote mbili, Swali hili la Mhariri nguli Kubenea halijajibiwa kabisa na Serikali kwani Naibu Katibu Mkuu Uchukuzi, Dk. Ally Possi hakujibu swali hilo na aliishia kueleza uzoefu wake
katika kupractise sheria Mahakamani.

(iii) Mhariri wa gazeti la Raia Mwema, Ndugu Joseph Kulangwa aliuliza swali kuhusu ulinzi wa ajira za watanzania katika Bandari alijibiwa na Mwenyekiti wa Timu ya Majadiliano, Ndugu Hamza Johari na Naibu
Katibu Mkuu Uchukuzi, Dk. Ally Possi kuwa suala hilo walivutana sana na DP World katika maslahi ya wafanyakazi na kwamba ajira za watanzania zitalindwa.

Majibu haya yanaleta mkanganyiko mkubwa na kuibua maswali mengi, majadiliano juu ya wafanyakazi yamefanyika lini wakati tunaambiwa feasibility study haijakamilika wala Mikataba midogo midogo ya HGAs
haijaingiwa? Kwa Maelezo haya inaonyesha wazi kuwa kila kitu kilishakamilika ila wananchi kwa sasa wanatuhadaa tu.

(iv) Mhariri Mwandamizi Mzee Salim Said Salim, aliyeuliza Serikali kupokea proposal ya Makampuni 7 kwa ajili ya uboreshaji wa Bandari kutoka nje ya nchi na akataka Serikali iweke hadharani proposal hizo ili umma upate uthibitisho kuwa DP World ilipatikana kupitia mchakato.

Waziri Profesa Mbarawa alisema kwamba Serikali ilipokea maombi ya Makampuni 7 kutoka maeneo mbalimbali Duniani. Majibu haya ya Serikali yanaleta mkanyanyiko mkubwa na haielezwi kwa kina mchakato
huo wa zabuni ulifanywa lini na Serikali?

(a) Ni njia gani ya Manunuzi iliyotumika kuyaalika hayo Makampuni 7? Serikali imeshindwa kuweka wazi na hata tarehe za Kuanza mchakato wa kuwapata wazabuni wala Tangazo la zabuni kama Mzee Salim
Said Salim alivyowaomba.

(b)Kama TPA ilifanya mchakato wa Manunuzi kumpata mwekezaji DP World ya Dubai, je nini kilichopelekea Serikali ya Tanzania na Serikali ya Emirate ya Dubai kuingia mkataba wa IGA?

(c) Wataalamu wa Timu ya Serikali ya Majadiliano, wanasema Mkataba wa IGA unaweka msingi wa awali wa Makubaliano ya ushirikiano katika undelezaji wa Bandari, kama ndivyo hivyo, kwanini tusingeishia kwenye MoU, Badala yake tukaenda kwenye mkataba wa IGA ambao unaifunga nchi yetu katika sheria za kimataifa. Nasema
tena IGA hii kwa jinsi ilivyo sasa ni hati ya mauziano (SALES AGREEMENT) ya Bandari zetu nchini.

(d)Serikali ilitumia utaratibu gani kuyaalika na kuyafanyia uchambuzi wa Makampuni 7 hadi kuipata Kampuni ya DP World wakati ikiwa haijafanya feasibility study ya aina yoyote ili kubaini mahitaji halisi
ya uwekezaji. Pia serikali ilikuwa haijafanya tathmini ya uboreshaji mkubwa wa Bandari unaondelea hivi sasa na utendaji wa Bandari kwa ujumla Kama Sheria ya Ubia (PPP) na Sheria ya Manunuzi (PPA)
zinavyotaka.

Kitendo cha Serikali kushindwa kujibu swali hili kwa ufasaha kama lilivyoulizwa na Mzee wangu Salim Said Salim ni uthibitisho kuwa Serikali iliamua kwa makusudi kuvunja sheria za nchi ili kufanikisha
Kampuni ya DP World kununua Bandari zetu.

(v) Mhariri Mwandamizi, Absalom Kibanda aliuliza kuhusu madai ya kukosewa Power of Attorney iliyompa mamlaka Waziri Profesa Mbarawa kwenda kusaini IGA kwa niaba ya Tanzania na Dubai lakini, Makamu Mwenyekiti wa Timu ya Majadiliano ya Serikali, Wakili Mussa

Mbura badala ya kujibu swali hilo alieleza Mamlaka ya Rais katika Ibara ya 33, 34 na 35 ya Katiba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kukosewa kwa PA kunaufanya mkataba mzima kuwa hauna Uhalali. (Null and
Void) kwani Rais wa Tanzania hana Mamlaka na Serikali ya Dubai.

Kama ya Timu ya Serikali iliyoshiriki hatua zote za kuandaa hadi kusainiwa kwa mkataba huo haina majibu hao wanaozunguka nchi nzima kupigia debe mkataba huu watafafanua nini zaidi. Kutokana na mapungufu hayo makubwa Nimeamua kuandaa Jedwali la maswali yalivyoulizwa na wahariri na majibu yaliyotolewa na Serikali ili kukata mzizi wa fitna. Jedwali hilo nimeliita JEDWALI NAMBA 1 na nimeambatisha katika tamko hili.

4. MAZINGIRA YENYE UTATA KUHUSU MKATABA WA BANDARI

Kuna mazingira yenye utata mkubwa na yanayoibua hisia na maswali mengi kutoka hatua ya MoU, kusainiwa na kuridhiwa kwa mkataba huu wa IGA, nitaongelea vipengele vitano kama ifuatavyo.

(a) Kampeni za wazi, Spika wa Bunge kuandaa ziara mwezi Februari 2023 ya wabunge 60 kutembelea maeneo ambayo DP World amewekeza na maeneo mengine Duniani ili kujifunza uwekezaji wa sekta binafsi katika uendeshaji wa bandari. Zoezi hili lilifanyika wakati mkataba haujatangazwa wala kufahamika kwa wananchi na wabunge wenyewe lakini pia ziara hiyo inatuhumiwa na wananchi kugubikwa na rushwa kubwa ili kulishawishi
Bunge kuipa upendeleo Kampuni ya DP World.

(b)Baadhi ya Viongozi na watendaji wa Nafasi za juu serikalini kuondolewa kwenye Nafasi zao bila Maelezo yoyote akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari, Eric Hamis aliondolewa tarehe 4/7/2022, Katibu
Mkuu Kiongozi Balozi Hussein Katanga na Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa, Kamishna Diwani Athumani ambao waliondolewa kwa pamoja tarehe 3/1/2023. Viongozi wote hawa waliondolewa ndani ya kipindi cha
mchakato wa MoU na Kuridhiwa kwa mkataba huu na Bunge.

(c) Kuchukua kipindi kirefu cha miezi 8 kuingia Mkataba tangu kusainiwa MoU na katika kipindi hicho Serikali haikufanya tathmini wala feasibility study kujua mahitaji na manufaa ya mradi.

(d)Kutangaza kufanyia marekebisho ya Sheria ya Manunuzi na Sheria za Ulinzi wa Rasilimali kabla ya kuingia Mikataba ya HGAs baina ya TPA na DP World.

(e) Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Mbarawa na timu ya Serikali ya majadiliano kuendelea kutoa Ufafanuzi wa Mkataba wa IGA badala ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Jaji Dk. Eliezer Mbuki Feleshi na Baba wa Mikataba na Baba Negotiation, Mhe. Profesa Palamagamba Aidan Mwaluko Kabudi. Viongozi hawa wamekaa kimya badala ya kujitokeza hadharani wawaeleze watanzania ukimya wao unasukumwa na nini?

5. VIFUNGU VYA MKATABA WA IGA

Dosari zilizomo katika Mkataba huu zimekosa majibu kutoka serikalini tangu zianze kuhojiwa na wananchi na zinaweza kupelekea nchi yetu kushtakiwa kimataifa kwa kuwa mkataba huu unakwenda kinyume na Mkataba wa Umoja wa Mataifa.

(i) Baadhi ya Viongozi na wataalamu wa wizara na Timu ya Serikali ya majadiliano wanasema haya ni Makubaliano tu ya awali ya nchi na nchi kwa ajili ya kuweka msingi wa Makubaliano na sio Mkataba, wanasema
hayo huku wakijua kwamba IGA ni Makubaliano yenye nguvu ya kisheria ambayo ni MKATABA na sio Makubaliano ya awali ya mashirikiano (MoU). IGA iliyoingiwa baina ya Tanzania na Dubai ina
nguvu ya kisheria ndiyo maana hata utaratibu wa namna ya kushtakiana, usuluhishi wa migogoro umewekwa katika Ibara 20 na Ibara ya 21, muda na utaratibu wa kuvunja mkataba umewekwa katika Ibara ya 23 ya Mkataba wa IGA.

Kwa hiyo maneno yanayotolewa kwamba haya ni Makubaliano ya awali ya nchi hizi mbili ni UONGO.

(ii) Madai yanayotolewa kuwa IGA haielezi utekelezaji wa mpango wa biashara na kwamba masharti ya mpango wa biashara yatawekwa kwenye Mikataba midogo midogo ya HGAs kati ya TPA na DP World
ambayo bado haijasainiwa, lakini ukisoma Mkataba huu kwa sehemu kubwa umeeleza namna Kampuni ya DP World itakavyofanya biashara na uwekezaji katika maeneo mbalimbali ya Bandari nchini, namna
itakavyopewa vivutio vya kodi, mashirikiano yake na TPA, haki ya kumiliki Ardhi na kutumia miundombinu wezeshi na maeneo huru ya uwekezaji kama ilivyo katika Ibara ya 4, Ibara ya 5, Ibara ya 6, Ibara ya 7, Ibara ya 8, Ibara ya 9, Ibara ya 10, Ibara ya 16, Ibara ya 18 ya Mkataba huu wa IGA.

Pia jukumu la nchi ya Dubai katika mkataba huu halijatajwa Mahali Popote isipokuwa majukumu yote yapo kwa DP World kwa hiyo sio kweli kwamba mkataba huu ni wa nchi na nchi bali mkataba huu ni wa Kibiashara baina ya nchi ya Tanzania na Kampuni DP World na hivyo sababu ya Tanzania na nchi ya Dubai kuingia mkataba wa IGA haijulikani hadi sasa.

(iii) Waziri Profesa Mbarawa anasema Kampuni 7 zilileta maombi ya kuendesha Bandari na baada ya mchakato ikapatikana Kampuni ya DP World, lakini ukisoma utangulizi wa Mkataba wa IGA unaeleza bayana kuwa DP World ilipatikana baada ya Mhe. Rais, Dk. Samia Suluhu Hassan kukutana na Mfalme wa Dubai na baadaye TPA na DP World kusaini MoU tarehe 28.2.2022 kwenye maonyesho ya Dubai Expo 2020 ya ushirikiano katika kuendeleza, kuboresha na kuendesha Bandari za Tanzania na baadaye kusainiwa Mkataba wa IGA tarehe 25.10.2022.

Waziri Mbarawa anaposema kwamba DP World ilipatikana kwa mchakato wa ushindani wa Makampuni 7 tofauti Duniani anataka kumdanganya nani wakati mkataba uko wazi na ameusaini yeye Mwenyewe kwa jina lake na saini yake. Ikumbukwe kuwa Kuchagua mwekezaji bila ushindani ni upendeleo na kinyume cha Sheria ya
Manunuzi ya Umma Na. 7 ya mwaka 2011 na Mkataba wa Umoja wa Mataifa Mwaka 1974, Ibara ya 2 Kifungu cha 2 (a).

(iv) Mkataba huu unakabidhi Bandari zetu zote za bahari, maziwa makuu, bandari kavu , maeneo huru ya uwekezaji, miundombinu wezeshi kwa DP World kwa mujibu wa Ibara ya 1, Ibara ya 2 na Ibara ya 4 ya
Mkataba wa IGA na si kama inavyoelezwa na Serikali kwamba Mkataba huu unahusu Bandari ya Dar Es Salaam pekee,lakini pia mkataba huu, unapora mamlaka ya nchi katika kulinda, kusimamia na kunufaika na maliasili na rasilimali zake kwa kuweka masharti ya nchi kuamuliwa katika rasilimali zake na Dubai Ibara ya 4

(2) ya mkataba, Mkataba kutokuwa na ukomo Ibara ya 23 (I), na zuio la kujitoa Ibara ya 23(4), kutumia Sheria na Mahakama za nje ya Nchi Ibara ya 20, kutoa haki ya kumiliki Ardhi Ibara ya 8, Kuweka usiri kwenye mkataba wa rasilimali Ibara ya 10.

Lakini pia kuingia mkataba ambao umelalia upande mmoja yaani hauna Win Win Situation na bila kufanya feasibility study ili kubaini mahitaji na manufaa kwa nchi, Mchakato huo ni kinyume cha Sheria ya Bandari
ya Na. 17 ya Mwaka 2004 na kinyume cha Kifungu cha 6, Kifungu cha 7 na Kifungu cha 11 cha Sheria ya The Natural Wealth and Resources (Permanent Sovereignty) Act no.5 of 2017, Sheria ya PPP na Mkataba
wa Umoja wa Mataifa Ibara ya 2 (I).

(v) Ibara ya 22 ya Mkataba wa IGA inazuia kufanya marekebisho ya baadhi ya vifungu vyenye kasoro mpaka pande zote mbili zikubaliane, kwa aina ya mkataba huu, rasilimali zitakazotumika ni za upande mmoja wa
Tanzania hivyo asipokubali Dubai maana yake rasilimali zetu zitaendelea kunyonywa na nchi yake na hii ni kinyume kabisa na kifungu cha 6 cha Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba
inayohusu Rasilimali na Maliasili za Nchi Na. 6 Mwaka 2017 (The Natural Wealth and Resources Contracts (Review and Re- Negotiation of Unconcianable Terms)

(vi) Mkataba huu unaathiri mahusiano ya Tanzania na nchi nyingine Duniani kwa kujifunga na nchi moja kuendeleza, kuboresha na kuendesha Bandari za Tanzania Ibara ya 19 na Ibara ya 27 ya Mkataba wa IGA, hii
ni kinyume na Sera zetu Kimataifa na pia ni kinyume na Mkataba wa Umoja wa Mataifa.

(vii) Mkataba huu pia haukuzingatia Sheria ya The Tanzania Extractive Industies (Transparecy and Accountability Act 2015) inayotaka michakato yote ikiwemo mikataba itangazwe kwa uwazi kwenye vyombo
vya habari na kushirikisha wananchi kikamilifu. Lakini pia kama nilivyosema mkataba huu haukusainiwa kikamilifu kama inavyotaka Ibara ya 28 ya Mkataba wa IGA. Kwa kifupi

(a) Power Of Attoney iliyompa mamlaka Profesa Mbarawa kusaini kwa niaba ya Tanzania imekosewa kwani Rais wa Tanzania hana mamlaka na Serikali ya Dubai,

(b)Aliyemshuhudia Waziri Prof. Mbarawa ambaye ambaye anayedaiwa kuwa ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi haijulikani mamlaka iliyomteua kufanya jukumu hilo, lakini pia jina lake
limefichwa,

(c) Eneo la kusaini anayedaiwa ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kuna saini mbili moja ya wino wa kijani na nyingine ya wino wa bluu, hali inayoonyesha kuwa kulikuwa na kughushi saini,

(d)Kwa upande wa Dubai aliyesaini Mamlaka iliyomteua, H.E Ahmed Mahboob Musabih ameficha jina na ameficha cheo chake,

(e) Shahidi aliyemhuhudia huyo H.E Mahboob ameficha jina na ameficha
cheo chake. Mkataba huu hauna Uhalali na umekosa msingi wa kisheria na ndiyo
maana nasema huu ni Mkataba FEKI.

6. MREJESHO KUTOKA KWENYE MITANDAO YA KIJAMII
KUHUSU MKATABA WA BANDARI


Baada ya kufanya mapitio ya Maoni ya wananchi kwenye mitandao mbalimbali ya Kijamii ya You Tube, Facebook, Instagram, Jamii Forums, Twitter, Maria Space, Club House, Sauti ya Watanzania na maeneo mengine nimebaini yafuatayo kwa uchache:-

(i) You Tube Channel ya Super News Tv, Uhondo Tv, Global Tv, na Kayuni Online Tv, tarehe 25.5.2023 zilichapisha Maoni ya Mbunge wa CCM, Luhaga Joelson Mpina aliyoyatoa wakati akichangia bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi akipinga mpango wa kubinafsisha Bandari ambapo hadi kufikia tarehe 17.7.2023 walio like ni watu 449,
watazamaji walikuwa 106,871 na waliotoa Maoni walikuwa watu 317 ambapo asilimia 97.6 walikataa mpango huo.

(ii) You Tube channel ya Mbeya Yetu Online Tv, iliyochapisha taarifa ya Dk. Tulia Ackson Spika wa Bunge, kuhusu Bandari Tarehe 13.7.2023 alipofanya ziara katika Shule ya Msingi Benson Mpesya ilikuwa na watazamaji 8,991, walio like ni watu 19 na waliotoa Maoni ni watu 201 kufikia tarehe 17.7.2023 ambapo asilimia 90.5 ya waliotoa Maoni wamepinga mkataba huo.

(iii) You Tube channel ya Jambo Tv, Ayo TV, Wasafi Tv, Global Tv iliyorusha Live Mkutano wa CCM kuzungumzia Mkataba wa Bandari uliofanyika Mbeya tarehe 15.7.2023 ambapo hadi kufikia tarehe 17.7.2023 watu walio like 25, watazamaji 15,277 na waliotoa Maoni ni watu 94 ambapo asilimia 99.8 walipinga mkataba huo.

(iv) You Tube Channel ya Jambo Tv, TBC online, The Chanzo Tv, Wasafi Tv, Global Tv, Azam Tv, iliyorusha Live Mkutano wa Waziri Profesa Makame Mbarawa, Timu ya Serikali ya Majadiliano na Jukwaa la Wahariri kuhusu Mkataba wa Bandari uliofanyika Tarehe 14.7.2023 hadi kufikia tarehe 17.7.2023 ulikuwa na like 205, watazamaji 79,953, watu walioandika Maoni yao ni 327 ambapo asilimia 99.7 ya Maonihayo walipinga mkataba huo.

(v) Mkutano wa Sauti ya Watanzania uliofanywa kwa pamoja baina ya Balozi Dk. Wilbroad Slaa, Wakili Boniface Mwabukusi, Wakili Peter Madeleka, Askofu Mwamakula na wenzao tarehe 12.7.2023 na kurushwa live na Jambo Tv, The Chanzo, Watetezi Tv, Kusaga Tv, Ayo Tv na Mgawe Tv ambapo inayonyesha kuwa like ni watu 914 na watazamaji walikuwa watu 174,252 na watu walioandika Maoni ni 720 ambapo asilimia 97.3 walikataa mktaba huo.

(vi) You Tube Channel ya Jambo Tv, ilirusha live Mkutano wa Maazimio ya Kamati Kuu ya CHADEMA kuhusu Bandari tarehe 14.7.2023 ambapo walio like ni watu 183, watazamani 40,764 na waliotoa Maoni walikuwa 91 ambapo asilimia 90 walikataa mkataba huo.

(vii) You Tube Channel ya Super News Tv, Uhondo Tv, Ayo Tv Tarehe 13.6.2023 ambapo channel hizo ziliweka video ya Mchango wa Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Aida Kenani akichangia Azimio la Bunge Bungeni siku ya Kuridhia Mkataba wa Bandari ambapo hadi kufikia Tarehe 17.7.2023 ambapo walio like ni watu 1,291, watazamaji walikuwa 245,503 na waliotoa Maoni walikuwa ni watu 886 ambapo asilimia 99 walikataa mkataba huo.

(viii) You Tube Channel ya Nyikani Tv, tarehe 8.6.2023 ilichapisha Maoni ya Wakili Boniface Mwabukusi akikosoa mkataba wa Bandari ambapo hadi kufikia tarehe 17.7.2023 walio like ni 1,300, watazamaji
walikuwa 122,302 na waliotoa Maoni walikuwa watu zaidi ya 1,000 ambapo asilimia 99 walipinga mkataba huo.

(ix) You Tube Channel ya Kanisa Katoliki Tanzania, tarehe 12.6.2023 ilichapisha Tamko la Viongozi wa Dini baada ya kusikiliza Serikali juu ya Mkataba wa Uwekezaji Bandarini ambapo hadi kufikia tarehe
17.7.2023 walio like ni 1,600, watazamaji walikuwa 312,817 na waliotoa Maoni walikuwa watu 1,200 ambapo asilimia 100 walipinga mkataba huo.

(x) Profesa Issa Shivji, Mzee Jaji Joseph Sinde Warioba, Mzee Joseph Butiku na Profesa Anna Tibaijuka ambapo waliripotiwa na You Tube Channel za Jambo Tv, Uhondo Tv, Global Tv, ITV Online, Wasafi
Tv, Mwananchi Digital ambapo kwa ujumla walio like ni 2,299, watazamaji 284,327 na waliotoa Maoni ni 1,570 ambapo asilimia 99 walipinga mkataba huo.

Kwa ushahidi huu wa takwimu kutoka katika mitandao michache ya Kijamii niliyoitaja inathibitisha kwamba watanzania zaidi ya asilimia 97.2 wamepinga mkataba huu bila kujali dini, kabila na itikadi ya Vyama. Lakini cha kushangaza ni kuona baadhi ya Viongozi wakiendelea kupingana na uhalisia huu, kuzua lawama,
kuwabambikia watu kesi na kuwatukana wananchi wanaokosoa mkataba huu.

7. HITIMISHO
Viongozi na Watendaji wa Serikali waliotuingiza kwenye mkataba huu mbovu wanaendelea kulazimisha na kuwaaminisha watanzania kuwa mkataba huu wa Bandari ni mzuri, ukiwasikiliza Viongozi hawa wanasema mkataba huu una nia njema na nchi yetu itapata manufaa makubwa.

Nia njema hiyo inapimwaje ikiwaSerikali iliacha misingi ya uwazi na Uwajibikaji na kuamua kuingia mkataba huo
kimya kimya bila kuujulisha umma wa watanzania,

Nia njema hiyo itapimwaje kwa Spika wa Bunge ambaye aliamua kuuficha mkataba huo kwa zaidi ya miezi 4 na baadaye kupelekwa Bungeni kinyemela bila kuwashirikisha kikamilifu wananchi kutoa Maoni yao na baadaye Spika huyo alipeleka mkataba huo Bungeni kujadiliwa na kupitishwa kwa masaa 5 tu licha ya unyeti wake, Pia upande wa Waziri mwenye dhamana ya Uchukuzi,

Nia njema hiyo itapimwaje kama Waziri huyo ameshindwa kuthibitisha ni utafiti gani uliofanywa, tathmini gani na sheria gani alizozitumia kufikia uamuzi wa kuingia mkataba huo.

Mkataba huu ni mbovu, watanzania tusiukubali kwa gharama yoyote ile, wananchi wengi katika majukwaa mbalimbali kwa zaidi ya asilimia 97.2 wameukataa mkataba huu,

Mheshimiwa Rais wangu Dk. Samia Suluhu Hassan, kuna gharama gani kuachana na mkataba huu, kuna gharama gani kuurudisha mkataba huu Bungeni ili kutoa Nafasi ya kutosha kwa wananchi na wabunge kuuchakata kwa kina zaidi mkataba huu.

Ni vema Nchi yetu iepuke kuingia Mikataba ambayo inaweza kuathiri utekelezaji wa miradi mikubwa inayotegemea Matumizi ya Bandari ikiwemo Ujenzi wa Bomba la Mafuta (East Africa Cruide Oil Pipeline -EACOP), Mradi wa Gesi asilia wa LNG, Ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa n.k.

Ikumbukwe kuwa Mheshimiwa Rais ameonekana mara kadhaa akilalamikia watendaji wa serikali kuingia Mikataba Mibovu inayoua nchi yetu na amekwenda mbali zaidi akaamua kuunda Tume ya Haki Jinai ambayo nayo imeenda kuibua Udhaifu mkubwa katika Usimamizi wa sheria nchini, lakini pia hata mtangulizi
wake Hayati Dk. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano alikuwa akichukizwa na kulalamikia Mikataba mibovu ambapo aliamua kuchukua hatua kadhaa ikiwemo kutungwa Sheria za Ulinzi wa Rasilimali za Nchi mwaka 2017.

Mheshimiwa Rais nini kinachofanya ushindwe kuamua? Mheshimiwa Rais
nakuomba amua leo, amua sasa kuufuta mkataba huu.

8. MWISHO

Kabla sijahitimisha, nichukue Nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru watanzania wote waliojitokeza hadharani kupinga mkataba huu, nachukua Nafasi hii kuwapongeza sana watanzania wenzangu wazalendo tuliosimama pamoja na kuungana kuukataa mkataba huu ambao maudhui yake unapora mamlaka ya nchi
na rasilimali za Taifa na kuwafanya wananchi kuwa manamba kwenye nchi yao
huru.

Naomba niwataje baadhi yao wakiwemo Umoja wa Viongozi wa Dini, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu, Mzee Anic Rwegarulila Kashasha, Askofu Maxmilian Machumu, Askofu Benson
Bagonza, Kadinali Policap Pengo, Dk. Rugemeleza Nshala, Wakili Boniface Mwabukusi, Profesa Issa Shivji, Mzee Joseph Sinde Warioba, Mzee Joseph Butiku, Profesa Anna Tibaijuka, Katibu wa Baraza la Maaskofu Katoliki, Padri
Dk. Charles Kitima, Askofu Bandekile Mwamakula, Mshindi Andrew Mhadhiri wa UDOM,

Wengine ni Mhe. Balozi Dk. Wibroard Slaa, Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe Mwenyekiti wa CHADEMA, bila kuwasahau waheshimiwa wetu wabunge wachache waliojitokeza hadharani kupinga mkataba huu ambao ni Mheshimiwa
Luhaga Joelson Mpina (CCM), Mbunge wa Jimbo la Kisesa, Mheshimiwa Aida Joseph Kenani (CHADEMA), Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini na Mheshimiwa Halima James Mdee (CHADEMA), Mbunge wa Viti Maalum.

Hata maandiko Matakatifu yanasema kupitia Kitabu cha Isaya 58:1 inasema Piga Kelele, Usiache, Paza Sauti yako Kama Tarumbeta, Uwahubiri watu wangu kosa lao na Nyumba ya Yakobo dhambi zao.

Lakini pia ukisoma Kitabu cha Mathayo 15:7-9 kinasema Enyi Wanafiki, ni vyema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu akisema, watu hawa huniheshimu kwa midomo, ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.

Nimalizie tena kwa kuchukua Nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza wapiganaji wote wa mstari wa mbele wanaopinga kuuzwa kwa Bandari zetu, Pia ninatambua Mkutano mkubwa wa hadhara ulioitishwa na JUKWAA LA SAUTI YA WATANZANIA Siku ya Jumapili wiki hii tarehe 23/7/2023 utakaofanyika viwanja vya Bulyaga Temeke, Dar es Saalam, naomba watanzania wote tujitokeze kwa wingi na siku hiyo tuweke msimamo wetu thabiti wa kuhakikisha maazimio ya Mkutano huo ndiyo utakuwa mwongozo wa kupigana kufa na kupona
kuhakikisha Bandari zetu haziuzwi. Waswahili wanasema USIPOZIBA UFA UTAJENGA UKUTA.

Asanteni sana kwa kunisikiliza, Mungu Ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania,
Mungu zinusuru Bandari zetu zisiuzwe.

David Levi Nkindikwa
Kijana MZALENDO
0685 446343
 

Attachments

  • MZALENDO BANDARI(1).pdf
    278 KB · Views: 15
Uchambuzi makini sana wa Kijana mzalendo..hao Kina Tulia, Chongolo, Kitila, Kabudi na AG watoke hadharani wajibu hoja hizo nzito zenye maslahi na nchi yetu, wasiendelee na mikutano ya kuwayumbisha wananchi na kuwapotosha kwamba mkataba ni mzuri kumbe kuna maswali mengi kiasi hiki.
 
MAZINGIRA YENYE UTATA KUHUSU MKATABA WA BANDARI

Kuna mazingira yenye utata mkubwa na yanayoibua hisia na maswali mengi kutoka hatua ya MoU, kusainiwa na kuridhiwa kwa mkataba huu wa IGA, nitaongelea vipengele vitano kama ifuatavyo.

(a) Kampeni za wazi, Spika wa Bunge kuandaa ziara mwezi Februari 2023 ya wabunge 60 kutembelea maeneo ambayo DP World amewekeza na maeneo mengine Duniani ili kujifunza uwekezaji wa sekta binafsi katika uendeshaji wa bandari. Zoezi hili lilifanyika wakati mkataba haujatangazwa wala kufahamika kwa wananchi na wabunge wenyewe lakini pia ziara hiyo inatuhumiwa na wananchi kugubikwa na rushwa kubwa ili kulishawishi
Bunge kuipa upendeleo Kampuni ya DP World.

(b)Baadhi ya Viongozi na watendaji wa Nafasi za juu serikalini kuondolewa kwenye Nafasi zao bila Maelezo yoyote akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari, Eric Hamis aliondolewa tarehe 4/7/2022, Katibu
Mkuu Kiongozi Balozi Hussein Katanga na Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa, Kamishna Diwani Athumani ambao waliondolewa kwa pamoja tarehe 3/1/2023. Viongozi wote hawa waliondolewa ndani ya kipindi cha
mchakato wa MoU na Kuridhiwa kwa mkataba huu na Bunge.

(c) Kuchukua kipindi kirefu cha miezi 8 kuingia Mkataba tangu kusainiwa MoU na katika kipindi hicho Serikali haikufanya tathmini wala feasibility study kujua mahitaji na manufaa ya mradi.

(d)Kutangaza kufanyia marekebisho ya Sheria ya Manunuzi na Sheria za Ulinzi wa Rasilimali kabla ya kuingia Mikataba ya HGAs baina ya TPA na DP World.

(e) Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Mbarawa na timu ya Serikali ya majadiliano kuendelea kutoa Ufafanuzi wa Mkataba wa IGA badala ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Jaji Dk. Eliezer Mbuki Feleshi na Baba wa Mikataba na Baba Negotiation, Mhe. Profesa Palamagamba Aidan Mwaluko Kabudi. Viongozi hawa wamekaa kimya badala ya kujitokeza hadharani wawaeleze watanzania ukimya wao unasukumwa na nini?

............................................

Hiyo ni sehemu ya uchambuzi wa Kijana Mzalendo David Levi Nkindikwa kuhusu mkataba wa Bandari.
 
Uchambuzi makini sana wa Kijana mzalendo..hao Kina Tulia, Chongolo, Kitila, Kabudi na AG watoke hadharani wajibu hoja hizo nzito zenye maslahi na nchi yetu, wasiendelee na mikutano ya kuwayumbisha wananchi na kuwapotosha kwamba mkataba ni mzuri kumbe kuna maswali mengi kiasi hiki.
Wote hawa wamepewa majumba Dubai
 
Upo uwezekano wa baadhi ya waliotajwa kuhusika na huu mkataba kuja kujibu maswali haya ndani ya mahakama.
 
MAZINGIRA YENYE UTATA KUHUSU MKATABA WA BANDARI

Kuna mazingira yenye utata mkubwa na yanayoibua hisia na maswali mengi kutoka hatua ya MoU, kusainiwa na kuridhiwa kwa mkataba huu wa IGA, nitaongelea vipengele vitano kama ifuatavyo.

(a) Kampeni za wazi, Spika wa Bunge kuandaa ziara mwezi Februari 2023 ya wabunge 60 kutembelea maeneo ambayo DP World amewekeza na maeneo mengine Duniani ili kujifunza uwekezaji wa sekta binafsi katika uendeshaji wa bandari. Zoezi hili lilifanyika wakati mkataba haujatangazwa wala kufahamika kwa wananchi na wabunge wenyewe lakini pia ziara hiyo inatuhumiwa na wananchi kugubikwa na rushwa kubwa ili kulishawishi
Bunge kuipa upendeleo Kampuni ya DP World.

(b)Baadhi ya Viongozi na watendaji wa Nafasi za juu serikalini kuondolewa kwenye Nafasi zao bila Maelezo yoyote akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari, Eric Hamis aliondolewa tarehe 4/7/2022, Katibu
Mkuu Kiongozi Balozi Hussein Katanga na Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa, Kamishna Diwani Athumani ambao waliondolewa kwa pamoja tarehe 3/1/2023. Viongozi wote hawa waliondolewa ndani ya kipindi cha
mchakato wa MoU na Kuridhiwa kwa mkataba huu na Bunge.

(c) Kuchukua kipindi kirefu cha miezi 8 kuingia Mkataba tangu kusainiwa MoU na katika kipindi hicho Serikali haikufanya tathmini wala feasibility study kujua mahitaji na manufaa ya mradi.

(d)Kutangaza kufanyia marekebisho ya Sheria ya Manunuzi na Sheria za Ulinzi wa Rasilimali kabla ya kuingia Mikataba ya HGAs baina ya TPA na DP World.

(e) Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Mbarawa na timu ya Serikali ya majadiliano kuendelea kutoa Ufafanuzi wa Mkataba wa IGA badala ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Jaji Dk. Eliezer Mbuki Feleshi na Baba wa Mikataba na Baba Negotiation, Mhe. Profesa Palamagamba Aidan Mwaluko Kabudi. Viongozi hawa wamekaa kimya badala ya kujitokeza hadharani wawaeleze watanzania ukimya wao unasukumwa na nini?

............................................

Hiyo ni sehemu ya uchambuzi wa Kijana Mzalendo David Levi Nkindikwa kuhusu mkataba wa Bandari.
Mtalia sana lakini hakuna cha maana mtakachoweza kukibadili. SSH ni kiongozi mzuri sana kwenye mikakati ya kiuongozi.

DP World hatakuwa wa mwisho pale bandarini. Tukumbuke kuna magati namba nane mpaka kumi na moja yanahitaji mwekezaji pia. Masuala ya uchumi wa bandari ndio yanayofanyika kivitendo hivi sasa, cha muhimu ni kujiongeza kielimu na sio kuishia kuziamini sana hizi siasa za mitaani zilizojaa majungu na upuuzi mwingi.
 
Back
Top Bottom