Bajaji zinazidi kutikisa miji mingi 👇👇👇👇👇👇👇👇😂👇👇👇👇👇👇👇Mgomo wa daladala umerudia tena jijini Arusha, huku madereva wa magari hayo wakimwomba Rais Samia Suluhu Hassan aingilie kati mgogoro uliopo kati yao na madereva wa pikipiki za matairi matatu maarufu kwa jina la Bajaj.
Mgomo huo unafanyika leo Agost 14 ikiwa ni mara ya tatu mfululizo, ukiwemo mgomo uliofanyika Julai Mosi na mwingine ukafuatia wa Julai 3 mwaka huu, ambapo madereva daladala wamekuwa wakishinikiza kuondolewa kwa usafiri wa bajaji katika barabara wanazohudumu kwani zinawanyima biashara.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, mmoja wa madereva daladala Herman Elias amesema katika mgomo wao wa pili, Mkuu wa mkoa wa Arusha John Mongela aliitisha kikao cha madereva hao na kusikiliza madai ya daladala na Bajaji na kuahidi kuchukua hatua ya utatuzi.
"Mkuu wa mkoa alisema atatusaidia kuondoa Bajaji kwenye ruti zetu lakini hadi leo hakuna kinachoendelea, sasa tumeamua kusitisha huduma watoe hao wanaowakumbatia" amesema.
Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa, John Mongela akizungumzia na Mwananchi leo amesema kuwa bado timu yake inashughulika na utatuzi na baadae wataweka wazi kilichofanyika.
"Sio suala kubwa kubwa kama inavyochukuliwa, na timu yangu iko kazini kuhakikisha tatizo linapata Suluhu hivyo subirini mtapata taarifa nzuri baada ya mda," amesema.
Uongozi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (Latra) Mkoa wa Arusha ulipotafutwa kuhusu suala hilo, haukuwa tayari kuzungumzia.
Hata hivyo, mwezi mmoja uliopita Ofisa Mfawidhi wa Latra, Amani Mwakalebela alisema wanaandaa utaratibu wa kuhakikisha wanazihakiki bajaji za ndani ya jiji a Arusha na kuzipunguza.
Amesema kuwa ndani ya Arusha kuna zaidi ya bajaji 2,000 zinazofanya kazi, wakati zilizosajiliwa hazizidi 350.
(Imeandikwa na Bertha Ismail)
#mwananchiupdates
#tunaliwezeshataifa