MH. JESCA KISHOA ATIKISA BUNGE SWALA LA KASHIFA YA MABEHEWA.
Na Kilawa the Iron
Bunge limeamua kumsimamisha Mh Jesca Kishoa kwa madai ya kwamba kashindwa kuthibitisha juu ya swala la kashifa ya mabehewa. Huu ni udhaifu uliojidhihirisha bungeni.
Awali ya yote sina budi kumpongeza Mh Jesca Kishoa kwa kutudhihirishia kwamba viatu alivyokuwa akivivaa Mh Kafulila na yeye vinamtosha. Ameonesha wazi kwamba hayumbushwi na uzembe wa viongozi wa bunge.
Ikumbukwe kashifa hii ya mabehewa iliibuliwa na Mh Kafulila na alieleza mwaka jana(2015) kwa kina juu ya Riport ya PPRA na Mamlaka nyinginezo zenye ripoti ya kashifa ya mabehewa.
Katika hali isiyoyakawaida bunge letu limedhihirisha kwamba halina meno ya kuutafuna mfupa uliopo mbele yake na si kushindwa kutafuna mfupa tu bali hata mnofu uliopo bunge limeshindwa kuutafuna badala yake linang'oa meno
Kumtoa Jesca kishoa bungeni ni sawa na kung'oa meno ya mbele na meno chonge halafu ukabakiwa na meno ya Nyuma tu.
Nini kilipaswa kufanyika na bunge kabla ya maamuzi ya kumsimamisha Jeska Kishoa kuhudhuria bungeni kwa siku mbili?
Mosi, Bunge lilipaswa kuhakikisha serikali inaleta riport iliyopo kutoka mamlaka husika bungeni ili wabunge waisome na waijadili kwa kina ili waone ni wapi pakuisimamia serikali.
Pili,Bunge lilipaswa kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Mh Jesca Kishoa na Kafulila ili waweze kupata undani wa swala hilo na kuweza kulifanyia kazi bungeni kwa ufasaha.
Tatu, bunge lisifanye kazi ya kuitetea serikali badala yake lifanye kazi ya kuisimamia serikali. Bunge hili lifanye kazi kama mhimili unaojitegemea.
Nne, wabunge wote waache uvyama ndani ya bunge badala yake waoneshe ushirikiano mkubwa katika kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa mjibu wa katiba na sheria za nchi yetu.
Naamini katika hayo machache bunge linaweza kufanya kazi kwa ufasaha, linaweza kuisimamia serikali badala ya kufukuza wabunge wa upinzani.
Kwanini udhaifu huu wa bunge unajitokeza?
Mosi, Ni vigumu sana kesi ya ngedere kuhulumiwa na Nyani. Kiujumla washiriki wakuu wa kashifa za ufisadi wengi wao ndio viongozi wa bunge na ndio viongozi wa serikali hivyo hali hii inapelekea ugumu kuwajibisha serikali kwakuwa wahusika ni walewale wenye mamlaka.
Pili, Wabunge kuendekeza uvyama ndani ya bunge, chuki binafsi, ubinafsi n.k
Tatu, baadhi ya wabunge pia hawajui majukumu yao yaliyowapeleka pale, wanadhani wamekwenda kuunga mkono hoja na kupiga makofi na sio vinginevyo
Hayo yote yakifanyiwa ukarabati naamini bunge linaweza kuwa na usimamizi mzuri wa serikali, uwakirishi mzuri wa wananchi.
Msema ukweli ni adui wa watenda maovu.