1. Ni kitu gani majini?
Majini ni viumbe miongoni mwa viumbe vya Allah (SWT) wanatofautiana na binadamu na vile vile malaika . Lakini kuna sehemu kadhaa ambapo hushirikiana na binadamu katika sifa, sifa ya uhuru na uwezo wa kuchagua ‘baina ya haki na batili, makosa na usahihi, kheri na shari’. Tofauti iliyopo kati yao na binadamu ni ya kile kinachojulikana kama asili ya maumbile kwani maumbile ya majini yanatofautiana na maumbile ya binadamu.
2. Ni mada ipi walioumbiwa nayo majini?
Allah (SWT) ametufahamisha ya kuwa amewaumba majini kutokana na moto na hiyo ni katika aya tofauti mfano, Neno lake Allah ( S W T): "Na majini tumewaumba hapo mwanzo kutokana na moto wa upepo wenye joto kubwa" , Al- Hajar 27 . Na akasema katika aya nyingine katika sura ya Ar-Rahman, aya ya 15:
"Na akaumba majini kutokana na ( ncha ) ya ulimi wa moto" .
Vilevile Mtume (SAW) ameeleza kuhusu namna walivyoumbwa majini wakati aliposema: "Wameumbwa malaika kutokana na nuru, wakaumbwa majini kutokana na ulimi wa moto. Na wameumbwa binadamu kutokana na namna mlivyoelezwa." Hadithi hii imetolewa na Muslim kutokana na Bi Aisha (RA)
Hivyo basi asili ya kuumbwa majini kwa mujibu ya maelezo yaliyomo ndani ya Qur-an na Sunna za Mtume Muhammad (SAW) ni kwamba wameumbwa kwa moto. Hivyo jinni kwa asili yake ni moto. Lakini wameondoka kweye ile asili yao ya moto kama vile mwanadamu asili yake ni udongo, lakini mwanadamu alivyo si udongo, isipokuwa asili tu ndio udongo. Hivyo, majini nao wana asili tu ya moto lakini si moto wenyewe, kwani kuna ushahidi wa hadithi ya Mtume (SAW) ambayo inafahamisha kwamba majini si moto kama tunavyofahamu wa kuunguza isipokuwa ile ilikuwa tu asili ya maumbile yao. Na kuthibitisha kwamba majini hawapo tena katika yale maumbile yao ya asili ( moto ) ni tamko lake Mtume (SAW): "Hakika adui wa Allah (SWT) Ibilisi, alinitokezea na kijinga cha moto ili anichome nacho katika uso wangu." Imepokewa na An-Nasaiy. Vilevile Imam Ahmad amepokea kutokana na Mtume (SAW) kwamba kuna mtu alimuuliza Abdur-Rahman bin Khanbash: “Nini alifanya Mtume (SAW) wakati alipojiwa na mashetani?”. Alisema: “ Mashetani walimjia Mtume (SAW) kutokea majimbo fulani, wakamteremkia kutoka majabalini huku akiwepo Shetani na kijinga cha moto kwa ajili ya kumchoma nacho Mtume (SAW), akasema: 'Alitishika'. Jaabir akasema: 'Nami nilihisi hivyo hivyo ( kwamba .Mtume (SAW) atatishika )'. Akasema: 'Akawa anarudi nyuma'. Akasema: 'Akamtokezea Jibril (AS) akasema: 'Ee Muhammad sema', Mtume (SAW) akauliza,'niseme nini?' Akamwambia, 'Sema: Najilinda kwa maneno ya Allah (SWT) yaliotimia, maneno ambayo hafui dafu yeyote juu ya maneno hayo ikiwa ni mwema, mbaya kutokana na shari ya alichokiumba, na kudhurika na shari ya kinachoteremka kutoka mbinguni na shari ya kinachopanda. Na shari ya fitna za usiku na mchana. Na shari iliyopo ardhini na ile itokayo ardhini, Ee Rahman.' Na hapo ukazimika moto wa mashetani kwa uwezo wa Allah ( S W T)."
Hivyo basi tunapata kuelewa kutokana na hadithi hii kwamba lau kama majini wangekuwa wapo katika yale maumbile yao ya asili ( moto ) na kwamba wao wanaunguza, isingehitajika mmoja kati ya hao mashetani kubeba kijinga cha moto. Kwani ingetosha tu kuwa mkono wa shetani au kiungo chake chochote kinatosha kumunguza binadamu kama vile ambavyo mwanadamu huchomwa na moto akiugusa. Hivyo inaonyesha dhahiri kwamba ule moto walioumbiwa Majini umetapakaa katika maeneo yote ya umbile la majini na kuwa ni viumbe ambao hawaunguzi isipokuwa wao pia huungua kwa moto. Na bila shaka yoyote, Majini huwa wanakula na kunywa kama tulivyo sisi. Pia hukua kimaumbile kama akuavyo mwanadamu kwa kula na kunywa. Na katika vyakula vyao kuna ambavyo ni vya baridi na vya moto. Na kutokana na kuzaana kumewageuza wao kutoka kwenye ile mada ya moto walioumbiwa mwanzo na kuwa na sifa nne: (1) Joto (2) Baridi (3) Majimaji (4) Ukavu.
3. Ni lini yaliumbwa majini ?
Kuna kauli nyingi zinazozungimzia kuhusu hasa ni lini Allah (SWT) aliwaumba Majini, lakini kauli zote hizo hazina ushahidi wa Qur-an au Sunna za Mtume (SAW) hivyo sisi hatutozizungumzia . Hivyo tunaweza tu kusema kwamba, Majini waliumbwa kabla ya kuumbwa mwanadamu na hivyo ni kutokana na kauli yake Allah (SWT) aliposema, "Na tulimuumba mwanadamu kwa udongo mkavu unatoa sauti ( unapogongwa ), unaotokana na matope mepesi meusi yaliyovunda, na majini tuliwaumba kabla , kwa moto wa upepo wenye joto ( kubwa kabisa )", Al - Hijr 26 - 27 . Hivyo ameweka wazi Allah (SWT) katika aya hizi kwamba Majini yaliumbwa kabla ya mwanadamu.
4. Ni aina ngapi za majini?
Majini yapo aina tatu kama ilivyokuja katika hadithi za Mtume (SAW) ambapo imetajwa na Ibun Aby Dunia katika kitabu cha "Makaidish - Sheitaan" kutokana na Abud - Dardaa, kwamba Mtume (SAW) amesema: "Allah (SWT) amewaumba majini ya aina tatu: Aina ya kwanza ni majoka , nge na wadudu wa ardhini. Aina ya pili ni kama upepo hewani. Na aina ya tatu ni wale watakaohesabiwa kwa mabaya yao na mazuri yao."
1. Je majini wana miili?
Kwa wale wenye ujuzi na elimu ya maisha yao wametofautiana katika pande mbili kwa kauli mbili tofauti.
Kundi la mwanzo limeonelea kwamba hawa viumbe majini hawana maumbile kama tunavyofahamu miili ilivyo, bali ni mada iliyopo katika hali aliyoiumba Allah (SWT).
Kundi la pili linaonelea kwamba majini wana maumbile ya aina fulani fulani na wenye kauli hii nao wametofautiana. Kuna wanaosema kwamba maumbile yao ni kama kioo, 'transparent' ( ambapo ukiangalia unaweza kuona upande wa pili ), au ni maumbile yanayobadilika kuchukua sura mbali mbali na vile vile yawezekana pia kuwa wapo katika hali kama ya hewa ( hewani ).
Na kuna waliosema kwamba miili yao ni laini 'soft' mno kiasi kwamba si rahisi kuonekana na macho yetu, kutokana na udhaifu wa kuona tuliokua nao. Kwani Allah (SWT) angeweza kutupa uwezo wa kuwaona tungeliwaona. Na kile kinachofahamisha ulaini wa maumbile yao ni ushahidi uliopo katika Qur-an Tukufu katika neno lake Allah (SWT) aliposema: "Hakika yeye ( shetani ) pamoja na kabila lake wanakuoneni, hali ya kuwa ninyi hamwaoni" , Al-A'raaf 27. Haya ni baadhi ya maoni na ushahidi uliopokelewa. Hivyo sote tunatosheka na ushahidi kwamba macho yetu hayakupewa uwezo wa kuwaona, lakini wao wanatuona.
2. Je majini wana majina mengine?
Jawabu ni ndio; majini wana majina mbali mbali katika lugha ya kiarabu tutataja baadhi yake:
( a ) Jinni : Anapokusudiwa jinni tu. Na maana ya neno jinni ni kitu kisichoonekana au kilichofichika.
( b ) Aamir : Anapokusudiwa yule anaishi katika majumba ya watu.
( c ) Shetani : Anapokuwa na shari
( d ) Rauhaan : Yule anaewatokezea watoto
( e ) Afriit : Anapokuwa na nguvu za kupindukia
3. Je majini wana uwezo wa kujibadilisha?
Majini wana uwezo huo, tena uwezo mkubwa mno wa kujigeuza katika maumbile tofauti kama vile kuwa kama majoka, nge, farasi, ng'ombe, ngamia, kondoo na ndege. Na pia wana uwezo wa kujigeuza katika maumbile va kibinadamu.
4. Uwezo wa majini
Majini wana uwezo na nguvu ambazo ni zaidi ya alizonazo binadamu na miongoni mwa nguvu zao hizo ni ule uwezo wao mkubwa wa kusafiri. Na mfano wa haraka haraka ambao tungependa kuutoa ni ule wa ahadi ya mmoja kati ya Majini wenye nguvu, Afriit, alipomwahidi Nabii Suleyman (AS) katika baraza lake, kwamba angeweza kumletea kiti cha enzi cha Malkia wa Yemen kutoka huko mpaka pale walipo ambapo ni Palestina kabla ya Nabii Suleyman (AS) kuvunja kikao chake. Allah (SWT) amesema katika suratun - Naml aya ya 38, 39: "( Suleyman akakusanya mawaziri wake akasema): 'Enyi wakuu! Ni nani atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajakuja kwangu, hali ya kuwa wamekwisha silimu?' Mjasiri mmoja wa majini akasema: 'Mimi nitakuletea kabla hujainuka mahali pako hapo na mimi hakika ninazo nguvu na uwezo wa hilo na ni mwaminifu'" . Miongoni mwa nguvu zao pia ni ule uwezo wa kupaa mbali mbinguni kusikiliza habari. Na hiyo ilikuwa kabla ya kuja Mtume Muhammad (SAW).
5. Je majini hufa?
Hilo halina shaka kwani nao wanajumuishwa kwenye tamko la Allah (SWT) katika Qur-an, suratur- Rahman 26, 27: " Kila kilichoko juu yake ( ardhi na mbingu ) kitatoweka; na inabaki dhati ya Mola wako ( tu Mwenyewe ) Mwenye utukufu na heshima ". Na Mtume (SAW) amesema katika dua: "Najilinda kwa utukufu wako, ambapo hapana mwingine apasaye kuabudiwa kwa haki isipokua wewe ambaye hufi, lakini majini na watu wote wanakufa" , imepokewa na Bukhari. Hivyo, kutokana na ushahidi uliotangulia majini hufa kama wanavyokufa viumbe wengine lakini Iblisi yeye amepewa muda mrefu wa kuishi mpaka siku ya kiyama, kama inavyoeleza Qur-an Tukufu, Al-A'raaf 14, 15: "Akasema ( Shetani ), 'Nipe muda ( nisife ) mpaka siku watakapofufuliwa ( viumbe )'. Akasema( Allah SWT ), 'utakua ni miongoni mwa waliopewa muda ( lakini si mpaka wakati ulioutaja ).'"
6. Ni vipi wanavyotembea mashetani?
Katika hili Mtume (SAW) anatufundisha kwa kusema:
"Yeyote kati yetu asitembee na kiatu kimoja kwani shetani hutembea na kiatu kimoja."
7. Ni muda gani ambao wanatapanyika mashetani?
Wanatapanyika wakati unapoingia usiku na hiyo ni kutokana na uthibitisho wa hadithi ya Mtume (SAW) aliposema, "Unapoingia usiku au linapoingia giza wazuieni watoto wenu ndani, kwani mashetani hutapanyika wakati huo, litakapopita lisaa limoja baadaye muachilie, na fungeni milango na mumtaje Allah (SWT), kwani hakika shetani hafungui mlango uliofungwa." Imepokewa na Bukhari.
8. Wapi kipo kiti cha enzi cha Iblis?
Kiti cha enzi cha Iblis kipo baharini. Imepokewa na Imam Ahmad kutoka kwa Jabir kwamba Mtume (SAW) amesema, "Hakika Iblisi ameweka kiti chake cha enzi kwenye maji, kisha hutuma majeshi yake."
9. Mayoe ya Iblisi
Ametoa mayoe Iblisi mara nne:
( a ) Kapiga yoe wakati alipolaaniwa
( b ) Wakati alipotolewa kwenye pepo
( c ) Wakati alipopewa utume Mtume Muhammad (SAW)
( d ) Wakati ilipoteremshwa Suratul - Fatihah
10. Mambo aliyotangulia kufanya Iblisi kabla ya binadamu
( a )Iblisi ndiye aliyetangulia kulia kwa sauti
( b )Iblisi ndiye aliyetangulia kulinganisha ubora wa viumbe, yaani yeye ndiye wa mwanzo kujilinganisha na mwanadamu na kujiona bora.
( c )Naye ndiye aliyeanzisha nyimbo na kuimba
Je Iblisi alikuwa ni miongoni mwa majini au alikuwa ni Malaika?
Tamko ( Jinni ) limekaririwa katika Qur-an Tukufu mara ishirini na mbili. Hivyo, limetajwa pekee neno ( Jinni ) pasi na kuambatanisha na neno ( Insi ) mwanadamu mara nane katika sehemu tofauti, kuhusiana na kuambatanishwa kwa neno ( Insi ) mwanadamu na neno ( Jinni ) limetajwa mara kumi na tano ndani ya Qur-an Tukufu.
Iblis (LAA)
1. Je Ibilisi ni katika majini au malaikah?
Iblisi ni katika majini, kwani neno la Allah (SWT) katika suratul Baqarah, aya 34 , " isipokua Iblisi" linafahamisha kwamba alikua si Malaikah isipokuwa yeye alikua pamoja na Malaikah wakati ilipotolewa amri ya kumsujudia Adam (AS).
Kuna rai nyingi nyingine zinazodai kwamba Iblisi ni katika Malaikah, lakini zote hazina nguvu mbele ya neno lake Allah (SWT) aliposema: "isipokuwa Iblisi alikua ni katika majini akaiasi amri ya Mola wake." Al-Kahf 50. Vile vile ushahidi mwingine wa kuthibitisha ya kwamba Iblisi ni katika majini ni neno lake yeye Mwenyewe Iblisi alipokua akizungumza na Allah (SWT) aliposema :
"Umeniumba kutokana na moto, na kumwumba yeye ( Adam A S ) kutokana na udongo." Al 'Araf 12.
Na vile vile Iblisi ana watoto kinyume na malaika, na kwamba malaikah wao wapo kama vile walivyoelezea na Allah (SWT): "Hawamwasi Allah katika amri zake na wanatekeleza kila wanaloamrishwa." At-Tahrim 6. Izingatiwe kwamba malaikah wameumbwa kutokana na nuru, lakini majini wameumbwa kutokana na moto. Hivyo basi Iblisi ni katika majini wala si malaikah
2. Ni vipi anatakiwa mwislam kuamini kuhusiana na majini?
( a ) Wao ( Majini ) ni viumbe wa Allah (SWT), kama ambavyo Allah (SWT) aliumba malaika vile vile aliumba majini na watu
( b ) Qur-an Tukufu haikuelezea namna ya sifa ya ndani ya maisha ya majini isipokua tu vile walivyoumbwa kwa moto, na namna ya kuongea kwao na sisi kuongea nao na kuwasiliana nao
( c ) Lakini la kuzingatia mno ni kwamba Qur-an kwa nguvu zote inakataza watu kutaka msaada kutoka kwa majini au kuwategema, kuwaogopa n.k kwani atakaye wafanya kuwa ni wapenzi wasaidizi, na kuomba kinga kutoka kwao kinyume na Allah (SWT), Allah (SWT) atamdhalilisha huyo atakayefanya hivyo.
Majini ni viumbe miongoni mwa viumbe wa Allah (SWT) ambao wamepewa majukumu ya kiibada kama alivyopewa mwanaadam.