Wakati tukiwapongeza Wakenya kwa mafanikio yaliyopatikana na kuwapa pole kwa magumu yaliyowakuta yatupasa kujiuliza mafunzo gani tunayopata. Mafunzo hayo ni muhimu ili tujiepushe na kasoro zilizowafikisha hapo. Kwa maoni yangu, fundisho kubwa sana tuliloliona ni kuwa kuendeleza ukabila ni jambo hatari sana kwa taifa. Bahati nzuri, katika nchi yetu tatizo la ukabila halipo, lakini linaweza kuwepo tusipokuwa waangalifu kwa vile makabila yapo. Nawasihi, ndugu zangu, tusiwape nafasi wale wote wanaofanya vitendo vinavyoweza kuturudisha kwenye ukabila.
Lakini, kwa nchi yetu lililo hatari la kujiepusha nalo si la ukabila tu, lipo la udini na yapo masuala ya ubaguzi mwingineo. Kenya hawakuwa na tatizo la udini lakini la ukabila lilitosha kuivuruga nchi. Je, kama lingeongezeka na tatizo la udini ingekuwaje? Tufanye kila tuwezavyo tuhakikishe kuwa tunapiga vita kwa uwezo wetu wote vitendo, fikra au hata mwelekeo tu unaoweza kutugawa kwa misingi ya makabila yetu, dini zetu, rangi za ngozi zetu, maeneo tutokako na mengineyo. Wale wenzetu wanaotaka kutupeleka kubaya tusiwape nafasi. Tusivumilie kauli zao za uchochezi au matendo yao ya kibaguzi. Misingi iliyowekwa na waasisi wa taifa letu hususan hayati Mwalimu Julius Nyerere na hayati Abeid Amani Karume daima tuienzi. Tukiipuuza ole wetu.