Na. KLHN News
Rais Kikwete amezungumza na Taifa katika utaratibu wake wa kuzungumza na wananchi kila mwishoni mwa mwezi. Hotuba yake hiyo iliyocheleweshwa ka karibu saa moja na nusu ilikuwa inasubiriwa kwa hamu na wananchi hasa kutokana na uzito wa mambo ambayo Rais alitarajiwa kuzungumzia.
Akizungumza katika hotuba hiyo ambayo ilionekana kuwa imerekodiwa Rais Kikwete alizungumzia mambo makubwa manne ambayo aliyatolea maelezo kwa kirefu. Hata hivyo jambo kubwa ambalo wananchi wengi walikuwa wanasubiri kulisikia ni hatua zilizochukuliwa dhidi ya makampuni na watu waliohusika na wizi wa fedha za EPA na kujua hatima ya uchunguzi mzima.
Pamoja na hilo suala jingine ambalo wananchi walikuwa wanasubiri kwa hamu ni msimamo wa serikali yake kuhusu suala ambalo linaonekana kuwagawanya wananchi kwa misingi ya dini. Suala hilo ni mpango wa Serikali ya Muungano kujiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu (OIC)
Akizungumzia suala la OIC ambalo alilipa umuhimu wa kwanza Rais Kikwete alisema kuwa mjadala wa OIC jinsi unavyoendeshwa sasa hivi ni mjadala usiofurahisha. Akielezea zaidi kutokufurahisha kwa mjadala huo Rais Kikwete alisema kuwa mjadala huo una sura ya malumbano baina ya waumini wa dini zetu kuu na kupandikiza chuki baina ya serikali
Kwa mujibu wa Rais msukumo wa kujiunga na taasisi hiyo zaidi unatoka Zanzibar ambayo ilikuwa imejiunga mwaka 1993 na kulazimika kujitoa miezi saba baadaye baada ya pingamizi toka serikali ya Muungano. Tangu wakati huo Zanzibar wamekuwa wanasubiri uamuzi wa Serikali ya Muungano. Kila wakati wenzetu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wamekuwa wanaliuzia suala hilo.
Hata hivyo akionekana kutofautiana na Waziri Membe Rais Kikwete alisema kuwa hakuna utafiti uliofanyika kuhusu suala la OIC na hivyo serikali bado inasubiri utafiti huo toka Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje. Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa haijakamilisha kazi yake ya utafiti na hivyo haijawasilisha Serikalini matokeo ya utafiti wao pamoja na mapendekezo yao kwa ajili ya kutafakariwa na kuamuliwa ipasavyo.
Hata hivyo kauli hiyo ya Rais inapingana na kauli aliyoitoa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje Mhe. Bernard Membe akizungumza Bungeni Augusti 22, 2008 ambapo akizungumzia suala la OIC alinukuliwa kusema kuwa sasa tumefanya utafiti wa kutosha na kugundua kuwa OIC ina faida kwetu na haina madhara, hivyo tunafanya mchakato wa kujiunga, lakini ni vema ikaeleweka wazi kuwa, Zanzibar wasingeweza kupata ridhaa ya kujiunga nayo kwa sababu si nchi katika uso wa kimataifa,
Ni kauli hiyo ya Waziri Membe ndiyo iliyosababisha wimbi la shutma na malalamikko ya Taifa kuburuzwa kwenda kujiunga OIC na wakati huo huo kupata pongezi kuwa wakati muafaka umefika wa kufanya hivyo kwani utafiti tayari umeshafanyika.
Rais alielezea msimamo wa serikali kuwa Serikali haijafanya uamuzi wowote kuhusu suala la OIC kwa vile hatujapokea mapendekezo yoyote kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Rais amewataka wananchi wawe na subira.
Kuhusu suala jingine ambalo limekuwa mwiba kwa serikali Rais Kikwete ameeleza kuwa kufuatia hotuba yake ya Augusti 21 aliagiza makampuni yaliyolipwa bilioni 90 kuhakikisha yanarudisha fedha hizo na yale ambayo yatashindwa kufanya hivyo yatachukuliwa hatua.
Leo ndiyo siku ya mwisho. Napenda kuwajulisha kuwa, taarifa nilizoletewa majira ya mchana leo(Ijumaa), ni kuwa kiasi cha shilingi 69,326,437,650 kati ya shilingi 90,359,078,804 zilikuwa zimerejeshwa. Hii ni sawa na asilimia 76.7. alisema Rais.
Aliwaambia wananchi kuwa leo (Jumamosi) taarifa zaidi itatolewa kuhusu kiasi halisi kilichorudishwa. Kutokana na kauli yake hiyo inawezekana hesabu hiyo isiwe sahihi. Wachambuzi wa suala hili la EPA wanaonekana kushangazwa na Rais kutaja namba ambayo siyo sahihi na masaa machache baadaye iliyo sahihi itolewe.
Kuhusu wale ambao hawakuitikia wito huo Rais Kikwete alisema kuwa ametoa maagizo kuwa Kamati (ya Mwanasheria Mkuu) ikabidhi majalada yao kwa Mkurugenzi wa Mashtaka mara moja, kwa hatua zipasazo za kisheria. Agizo hilo alilolitoa Rais ni sawasawa na agizo alilolitoa wakati wa kuunda tume ya Mwanyika pale alipomuagiza Mwanasheria Mkuu kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu na makampuni yote yaliyohusika na uhalifu huu. Haijaeleweka tofauti ya uelewa wa Agizo hilo la kwanza na la pili ni nini hasa kwa sababu ofisi ya DPP iko chini ya ofisi ya Mwanasheria Mkuu.
Uamuzi huo unahusu makampuni yale 13 kati ya ya 22 yanayohusishwa na wizi wa EPA. Kuhusu makampuni 9 yaliyosalia ambayo yanadaiwa kulipwa bilioni 40 Rais Kikwete alisema kuwa nasubiri taarifa yao mpya kuhusu maendeleo ya uchunguzi huo. Taarifa niliyopewa wiki mbili zilizopita zinaonyesha kuwa polisi wetu bado hawajapata majibu kutoka kwa wenzao
katika nchi walizoomba msaada. Hivyo, nakusudia kuwataka waendelee kufuatilia kwa wenzao ili hatua zipasazo ziweze kuchukuliwa.
Kwa maneno mengine uchunguzi kuhusu makampuni hayo bado haujaanza kwani Rais ndiyo amekusudia kuwatataka waendelee kufuatialia makampuni hayo 9. Makampuni hayo ni pamoja na kampuni inayodaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na Mbunge wa Igunga Mhe. Rostam Aziz, ya Kagoda Agricultural.
Hata hivyo Rais aliwahakikishia wananchi kuwa utaratibu wa kuzigawa fedha hizo kwenye sekta ya kilimo Umekamilika.
Mambo mengine ambayo Rais aliyazungumzia kwa kirefu ni pamoja na suala la madai ya walimu, mauaji ya Albino, na suala hali ya kiuchumi ya dunia