HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-19
ILIPOISHIA:
Watu waliumia kutokana na tabia za Bupe kila mvulana alipenda awe mkewe, wengi waliamini mchezo ule umefanywa palepale kijijini kwa wivu wa kuolewa yeye na kuwaacha wasichana wengine. Kilasilo kila mtu alisema lake lakini mzee Ambokile alijua kila kitu.
SASA ENDELEA...
Kutokana na mwili kutoka kwenye maji hawakutaka kuuweka sana, walipanga mazishi yake siku ya pili asubuhi. Siku ya pili yalifanyika mazishi yaliyohudhuriwa na umati wa watu ambao waliguswa na msiba ule ambao nguvu za giza zilitawala na kutishia ndoa za wasichana wa Kilasilo ambao walikuwa mbioni kuolewa kwa kuamini nao watakufa kama Bupe.
Baada ya mazishi, jioni mganga alikuwa na mazungumzo na familia ya mzee Ambokile juu ya tukio lile.
"Jamani nimejitahidi kadri ya uwezo wangu, lakini nilikuwa napambana na jeshi la watu wengi. Bila hilo ningeweza kumtoa hai. Sasa baada ya tukio hilo kama wazazi mlikuwa mnasemaje?"
"Tunakusikiliza wewe."
"Mnamuachia Mungu au na nyinyi mnataka kurudisha kombora lilipotoka?"
"Kwa vile wamemkata binti yangu hivihivi na mimi nataka aliyefanya hivi basi naye akatike kama mwanangu," alisema mama Bupe kwa uchungu.
"Basi kazi hiyo kwangu ndogo sana," alisema mganga Msioka.
"Unasema wameshiriki zaidi ya mtu mmoja wote utawafyeka?"
"Kila aliyehusika hatabaki hai hata awe nani kwa dawa nitakayoifanya utaniambia, hata uwe ukoo mzima utapukutika ila kwa aliyehusika tu."
"Majibu lini?"
"Narudi leo Malawi, leo usiku silali nitakesha na kazi hiyo, asubuhi nalituma kombora, mpaka jioni mtasikia majibu ya kazi mliyonituma, kwa vile sehemu yenyewe mbali unaweza kwenda kusikilizia kumetokea nini."
"Tutashukuru maana wametuchukulia jicho letu, kama ikiwezekana fagia ukoo mzima."
"Ninyi si mmenipa kazi, basi kaeni kimya muuone moto wangu, mimi ndiye Msioka," mganga alijitapa.
Baada ya makubaliano, mganga Msioka aliondoka kurudi Malawi ili kurudisha kombora kwa mtu aliyeshiriki kumuua Bupe.
KIJIJINI IBUNGU
Siku iliyofuta taarifa zilifika kijijini Ibungu juu ya msiba wa mchumba wa Ambakisye aliyetolewa na mganga toka Malawi akiwa amefariki na mazishi kufanyika haraka siku iliyofuata kutokana na kuogopa mwili kuharibika.
Taarifa ile ilikuwa kama shubiri kwa mzee Amangise baada ya kusikia mazingira ya kifo cha mkwewe mtarajiwa, aliamini kabisa waliofanya hivyo ni familia ya mpenzi wa mwanaye.
Lakini hakuwa na jinsi zaidi ya kuzipokea habari zile na kuziacha kama zilivyo kutokana na maneno mazito aliyoyatoa mwanaye juu ya familia ya mpenzi wake kama kingewatokea chochote basi yeye angechukua uamuzi mzito juu ya familia yake.
Taarifa za kuonekana kwa Bupe akiwa amekufa zilimfikia Ambakisye ambaye alifurahia moyoni kwa kujua ndoa na Atuganile ipo karibu hasa baada ya familia yake kuonesha kubadilika na uamuzi wao mzito juu ya wazazi wenzao.
Alitoka na furaha hadi kwa mpenzi, Atuganile alipomuona alijawa na shauku ya kutaka kujua jana yake mpenzi wake kazungumza nini na wazazi wake.
"Karibu mpenzi wangu, yaani uso wako unaonesha kuna dalili njema."
"Ni kweli, hebu nipe kwanza kwenu ilikuwaje ili nami nikujuze yaliyojiri."
Atuganile alimweleza mpenzi wake jinsi alivyowachachafya wazazi wake mpaka wakabadili uamuzi na kufuata anachokitaka yeye.
Ambakisye naye alimueleza mtiti aliouanzisha kwao baada ya mpenzi wake kumsikiliza alimuuliza.
"Sasa Amba kama baba yako angeendelea kusimamia msimamo wake ungeondoka kweli?"
"Nilikuwa sitanii ningejua mbele ya safari lakini si kukaa nyumba ya wauaji wale."
"Sasa tutafanyaje ili familia zikae pamoja na kumaliza tatizo?"
"Si bibi Tumwambilile alisema atakaa nao kwa vile kazi kubwa tumemaliza itakuwa rahisi kulizungumza."
"Na kweli, unaonaje twende tukamwambie sasa hivi?"
"Poa, tena nina habari njema mpenzi wangu."
"Habari gani tena mpenzi?" Atuganile alishtuka.
"Bupe kapatikana..."
"Sasa hizo ndizo habari njema, yaani kumbe unanidanganya unanipenda kumbe mawazo yako yapo kwa Bupe?" Atuganile alimkata kauli mpenzi wake na kuliza wivu.
"Atu, mbona unanikata kauli kabla sijamaliza sentesi yangu."
"Kuna nini zaidi ya kunirusha roho, jana nimewakosea adabu wazazi wangu kwa ajili yako, kumbe kuna mtu unayempenda."
"Atu, tutakorofishana naomba uniache nimalize ninachotaka kukueleza."
"Haya sema."
"Bupe kapatikana juzi mtoni akiwa amekufa na kazikwa jana."
"Muongo unataka kuniongopee."
"Atu mpenzi wangu kipi utakachoniamini, kweli taarifa imefika nyumbani nasikia ametolewa ndani ya maji akiwa amenyolewa upande mmoja. Tena nasikia baba yake kasafiri mpaka Malawi kumfuata mganga kwani wa pale Kilasilo walichemka."
"Mmh! Unajua siamini."
"Ndiyo maana nikakuambia habari njema, sasa hivi ndoa nyeupe baada ya kuwatolea uvivu wazazi wetu."
Atuganile alifurahi kwa kurukaruka na kumkumbatia mpenzi wake baada ya kujua aliyekuwa akimpa presha amekufa.
"Sasa hivi nina uhakika wa kuitwa Mrs Amba," Atuganile alijishebedua.
"Basi tuwahi kwa bibi Tumwambilile."
Walikubaliana kwenda kwa bibi Tumwambilile kumwambia walipofikia na wazazi wao. Walikwenda taratibu huku wakizungumza:
"Mmh! Bado siamini kama utanioa."
"Kipi kitakachofanya nisikuoe ikiwa yule msichana amekufa."
Wakiwa wameacha barabara kuu na kuingia yenye majani ili kupita njia ya mkato, ghafla mbele yao alitokea nyoka mweusi walishtuka na kutaka kumkwepa kwa kuruka nyuma lakini nyoka yule aliruka na kutaka kumuuma Atuganile. Kwa vile alikuwa amemuelekea alijitahidi kumkwepa na kurudi nyuma lakini kwa bahati mbaya alijikwaa na kuanguka chini.
Nyoka yule alimgonga mguuni, alikuwa tofauti na nyoka wengine baada ya kumgonga Atuganile wakati akipiga kelele za kuomba msaada kwa maajabu yule nyoka, aliingia mdomoni na kuishia wote ndani ya mwili. Muda uleule Atuganile alibadilika rangi na kuwa mweusi, Ambakisye alichanganyikiwa na kushindwa kumsaidia mpenzi wake.
Itaendelea Kesho.............