HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-14
ILIPOISHIA:
Alielezewa yaliyotokea Kilasilo ya mpenzi wake kuchukuliwa kichawi na mamba ambaye alimchagua yeye peke yake katika kundi la watu.
Mungu wangu, inamaana ule mto una mamba?Hauna juzi ilikuwa ajabu ya mwaka, kibaya kingine mganga aliyesema atamrudisha alishikwa na mamba na kuzamishwa ndani ya maji na kuokotwa siku iliyofuata akiwa amekufa na kunyofolewa baadhi ya sehemu za mwili.
Mmh! Kazi ipo, nani aliyefanya hivyo?
SASA ENDELEA
Hajajua, ila nitaingia kazini kuangalia nani kafanya vile, nikimjua nitakachomfanya Mungu anajua, alijiapiza mzee Amanyisye.
Kwa hiyo nini kinaendelea?
Baba amesafiri leo kwenda Malawi kutafuta tiba kwa vile wanasema uchawi ule unatumika sana huko, alisema mmoja wa vijana waliokuja kuleta taarifa za kupotea kwa Bupe mchumba wa Ambakisye.
Nami nitamtafuta aliyefanya vile nikimjua nitamaliza familia nzima, alizidi kujiapiza mzee Amanyisye.
Sawa nimesikia, alisema Ambakisye kwa unyonge huku moyoni akifurahi kupotea kwa yule msichana lakini hakupenda afe.
Kuna kauli iliyotukatisha tamaa, mganga aliyekufa maji alisema kuwa siku ya jana ikipita hatutampata tena na tukimpata atakuwa ameishakufa, alisema kaka yake huku akitokwa machozi ya uchungu.
Wee waache si wameanza sisi tutamaliza, mzee Amanyisye aliendelea kujitapa kwa hasira.
Baada ya vijana walioleta taarifa za kupotea Bupe kuondoka, wazazi wa Ambakisye walikaa kikao cha faragha kulijadili lililotokea.
Mke wangu mi nina wasiwasi na familia ya Andendekisye!
Hata mimi nilikuwa na wazo hilo, inawezekana kabisa kitendo cha Amba kumpatia ujauzito mtoto wao ndicho kilichosababisha wafanye hivyo, mkewe aliunga mkono wazo la mumewe.
Na ile dawa tuliyompa aitege aliitega kweli?
Hata mimi nashangaa leo siku ya ngapi hatujapata majibu.
Hebu mwite.
Mama Ambakisye alimwita mwanaye kwa sauti ya juu.
Ambaaa!
Naam mama.
Hebu njoo.
Ambakisye aliyekuwa akimpa taarifa Atuganile aliyejifanya kushituka alimuacha na kwenda kumsikiliza mama yake.
Mpenzi nakuja.
Dah! Pole sana nenda ukawasikilize.
Atuganile alikuwa na hamu ya kujua familia ya mpenzi wake itapokea vipi kupotea kwa mchumba wa mtoto wao katika mazingira ya kutatanisha. Ambakisye alikwenda hadi kwa wazazi wake, alipofika alisimama mbele yao.
Naam.
Eti ile dawa ulimtegea Atu?
Ndiyo jana, halafu kitu cha ajabu alipotoka na kuruka ile dawa alipiga kelele na kuinama chini akishika mikono chini ya kitovu. Usiku alipolala kwao ile hali ilijirudia tena safari ile ilisababisha atokwe damu nyingi na kusababisha kupoteza ujauzito wake, Ambakisye alisema kwa masikitiko.
Mmh! waliguna wote.
Sasa mbona haikusaidia kitu?
Tulikuambia wale si watu wema lazima wameutoa kwa hasira kabla ya kuitega ile dawa, walitengeneza uongo.
Ila hata mimi sikubali aliyemuua mwanangu naye nitamsafiria Malawi, haiwezekani waniulie mwanangu asiye na hatia.
Ambakisye usirogwe kushiriki uchawi, wewe bado kijana mdogo kazi hiyo tuachie sisi wazazi ndiyo tunaweza kukabiliana nao, mzee Amanyisye aliwahi kumzima mwanaye kwa kujua bomu limetegewa ndani mwao.
Mmh! Sawa lakini ungeniacha tu.
Vita ya kichawi inataka uzoefu, ukienda kichwakichwa utapotea. Sasa hivi uchawi wa bure. Kwa vile nimeahidi kupambana nao basi niachie mimi kazi hiyo.
Sawa baba.
Basi kaendelee na kazi yako.
Ambakisye aliondoka na kuwaacha wazazi wake wakiendelea kuteta, alirudi hadi chumbani kwake na kupokewa na Atuganile aliyekuwa na hamu ya kujua mpenzi wake aliitiwa nini kwani hata uso wake ulijaa simanzi.
Amba kuna nini, mbona hivyo?
Mchumba niliyetaka kumuoa kachukuliwa na mamba katika mazingira ya kutatanisha, alimweleza mengine japo mwanzo hakumwambia.
Mungu wangu pole sana, Atuganile alijifanya kushtuka.
Si bure lazima kuna mkono wa mtu.
Lakini mpenzi usisikitike sana mimi mpenzi wako wa damu si nipo?
Sawa, lakini huoni kama wanaweza kutufikiria vibaya labda tumepanga kumpoteza ili tuendelee kuwa pamoja. Japo tuko pamoja lazima kipindi hicho uhusiano wetu usiwe wa wazi sana kuonana kwetu iwe usiku tu.
Sawa, lakini sikubali utafutiwe mwanamke mwingine kama amepotea au amekufa nasubiri ndoa yangu.
Hakuna tatizo, kama hivyo sitakubali kuchaguliwa tena mwanamke, Ambakisye alimuhakikishia mpenzi wake.
Nimefurahi kusikia hivyo, basi naomba utumie hii dawa ili tujue tatizo nini.
Mmh! Sawa, lakini lazima nizungumze na baba ili nijue ataniambiaje.
Amba kwa nini usitumie tu ili tujue kitakuwa nini kuliko kuwapa presha wazazi wako?
Hapana lazima nimwambie baba kwa vile ni mtu wangu wa karibu ili nijue atanisaidia vipi kabla ya kutumia dawa.
Bibi Tumwambilile tatizo lako aliliona na kusema ukitumia dawa hii ndani ya siku tatu kila kitu kitaenda vizuri.
Sawa, lakini hili ni jambo zito kwa vile toka nizaliwe halijawahi kunitokea, jana nilijua ni uchovu wa safari lakini leo imenijulisha kuwa hili ni tatizo.
Kwa hiyo dawa hii niirudishe?
Hapana, niachie ila lazima nimwambie kwanza baba nisije sema hali imekuwa mbaya.
Mmh! Sawa.
Atu kuna kitu gani kati yetu?
Kipi?
Kwa nini matatizo yametutokea kwa siku moja, huoni hapo kuna mchezo fulani tuliochezewa?
Mmh! Kweli kabisa mpenzi wangu siku uliposhindwa kufanya kazi usiku wake ndipo niliharibu ujauzito wangu.
Unafikiri ni kwa amri ya Mungu?
Hapana lazima kuna mkono wa mtu.
Hujamuuliza bibi Tumwambilile tatizo lako linatokana na nini?
Aliniambia nikifukua sana uchafu nitakutana na uvundo na chanzo cha moto mkubwa ni cheche.
Alimaanisha nini?
Nilimuuliza, aliniambia kwa vile nimepona haina haja ya kuchimba sana.
Na mimi?
Kaniambia utumie dawa hii utapona kabisa.
Sasa fanya hivi nitakupitia kwenu ili twende tukamchimbe bibi Tumwambilile, nina senti kidogo najua atakubali kutueleza.
Sawa, basi mi nitakusubiri, muda mzuri jioni nitakuwa nimemaliza kazi.
Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia Kesho....