VITA YA WACHAWI-4
ILIPOISHIA:
"Siwezi kuua mwanangu kwa ajili ya wazazi wako, Ambakisye wewe ndiye muamuzi wa mwisho kumbuka nimekataa wanaume wangapi kwa ajili yako, wazazi wangu wanajua wewe ndiye mume wangu, unafikiri watapokeaje taarifa hii? Nimewaficha tangu uliponieleza, nimekuwa nalia kila nikiwa peke yangu ili wazazi wangu wasijue kitu.
SASA ENDELEA…
"Ambakisye wazazi wangu nawajua, nikiwaeleza wanaweza kukufanya kitu kibaya, hebu kaa na wazazi wako waeleze kuwa mimi ndiye chaguo lako."
"Hawezi kukubali kwa vile tayari wameshapeleka posa, kilichobakia ni ndoa tu."
"Amba wazazi wako wasije kujilaumu kwa uamuzi wao wa kikatili, nikitoka hapa naenda kuwaeleza wazazi wangu."
"Sina jinsi, kawaeleze."
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana, giza nalo lilikuwa limeanza kuingia. Ambakisye na Atuganile walirudi kijijini, wakati huo mvua zilikuwa zimebaki za rasharasha.
***
Atuganile alirudi nyumbani kwao huku macho yamemvimba kwa kilio, alipofika nyumbani alimkuta mama yake yupo nje, baada ya kumsalimia aliingia ndani moja kwa moja chumbani kwake. Mama yake alishtuka na kuacha kazi zake na kumfuata, alipoingia chumbani alishangaa kumkuta mwanaye amekaa chini kichwa amekilaza kitandani mikono kichwani.
Kitendo kile kilimshtua sana mwanaye, kurudi amelowa, tena akiwa amechelewa bila kujua siku ile alikwenda wapi, japokuwa hawakuwa na wasiwasi kwa kujua yupo na mpenzi wake Ambakisye.
"Atu," alimwita kwa sauti iliyomshtua mwanaye ambaye alikimbiza mkono kwenye macho kufuta machozi.
"Abee mama," alijitahidi kuitika vizuri lakini sauti ilionesha alikuwa akilia.
"Kuna nini mwanangu, kwanza umeondoka alfajiri umerudi umenyeshewa na mvua, umefikia kulia, kuna nini?"
"Mama, hata sijui nikueleze nini unielewe."
"Niambie tu mwanangu nitakuelewa tu."
Atuganile alimueleza mama yake yote aliyoelezwa na mpenzi wake juu ya wazazi wa Ambakisye kumtafutia mtoto wao mchumba mwingine. Kauli ile ilimshtua mama yake na kutaka ufafanuzi zaidi.
"Wamemtafutia mwanamke mwingine, ulikataa kuolewa?"
"Hapana, anasema hata yeye alikuwa hajui kitu."
"Yeye kasemaje?"
"Japokuwa hakuafiki kitendo cha wazazi wake lakini hawezi kupinga."
"Na hali hiyo?" Alimuuuliza kuhusu ujauzito.
"Amenishauri niitoe."
"Akaja na mahala, usosye ulwanda? Ikulonda mwisukulu gwangu afwe?" (Hana akili, utoe mimba, anataka mkujukuu wangu afe?)
"Unasema wamesema wazazi wake?"
"Anatutania."
"Kweli mama, Jumapili walikwenda kutambulishwa ukweni."
"Mmh! Sawa, tuachie kazi hiyo naona hawatujui."
"Lakini mama msimfanye Ambakisye kama John."
"Wao si wamekuona hufai, basi tutaoneshana kazi."
(John ni mvulana aliyeanza naye mapenzi, lakini alikwenda jijini Dar na kupata mwanamke mwingine na kumuoa, alipoulizwa alionesha dharau. Haukuchukua mwaka, alipata ajali mbaya akiwa na familia yake iliyochukua maisha yao, ikiwa mkono wa wazazi wa Atuganile.) Mwanzo wa mapenzi kabla ya kumkubali alitaka kuhakikishiwa kuolewa.
Ambakisye alimhakikishia kumuoa ndipo Atuganile alipomkubali na penzi lao lilijulikana kijijini kwa kila mmoja kuamini wawili hao wataoana. Kukataliwa kwa Atuganile kulimchanganya sana na kuwa na wasiwasi na uamuzi wa familia kwa kuamini maisha na mpenzi wake yatakuwa hatiani.
Mama Atuganile alikwenda kwa mumewe aliyekuwa akirekebisha banda la nyumba sehemu iliyokuwa ikivuja mchana. Alimuomba waingie ndani, mzee Andendekisye aliingia ndani kumsikiliza mkewe, kwa vile nguo zilikuwa zimelowa maji alisimama wima kumsikiliza.
"Unasemaje mama Atu?"
"Leo familia ya Amangise imenikata maini," alisema akishika mkono kiunoni.
"Kuna nini?"
Alimueleza yote aliyoelezwa na mwanaye, baada ya kumsikiliza alisema:
"Aliyesema hayo ni wazazi au Ambakisye?" Alimuuliza mkewe.
"Ambakisye lakini yamesemwa na wazazi wake."
"Kwa vile kesho tulipanga kwenda kwao kwa ajili ya kuzungumzia hali ya mwenetu, nina imani kila kitu kitajulikana."
"Naona wamenisahau, nitaisambaratisha familia yote, nyumba ibakie gofu."
"Usiwe na haraka ya kufanya lolote, yote tutajua kesho."
"Yaani nilivyokasirika, Ambakisye jua la kesho asingeliona."
"Usiwe na pupa, twende kwanza tukawasikilize."
"Yaani bila wewe sijui ingekuwaje?" Mama Atuganile alisema huku akitweta.
Mama Atuganile jazba ilikuwa juu, siku zote mumewe alimshusha bila hivyo uamuzi wake huwa mbaya. Hata kifo cha John hakumshirikisha mumewe, alifanya mwenyewe, jibu lilikuwa baada ya tukio ndipo alipoielezea familia yake kuwa yeye ndiye aliyetenda.
Baada ya kukubaliana, alirudi chumbani kwa binti yake na kumueleza asiwaze sana kwani kesho wanakwenda kusikiliza kauli ya familia ya mzee Amangise.
****
Siku ya pili, mzee Andendekisye na mkewe walikwenda nyumbani kwao Ambakisye, walipofika walipokelewa vizuri. Kama zilivyo mila na desturi, walikaribishwa pombe ya chimpumu kwenye kopo kubwa la plastiki la lita moja.
"Jamani karibuni sana."
"Asante."
Baada ya kunywa kidogo, hawakutaka kupoteza muda, walisema kilichowapeleka pale.
"Jamani si wakaaji sana, kuna jambo limetuleta," alisema mzee Andendekisye.
"Ndiyo, jambo gani?" Aliuliza mzee Amangise.
"Nina imani unajua uhusiano wa vijana wetu wawili, Ambakisye na Atuganile."
"Ndiyo."
"Jana usiku kaja binti yetu kutueleza jambo ambalo kwa kweli limetushtua sana."
Je nini kitatokea?
tukutane siku ya kesho jioni.