HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-17
ILIPOISHIA:
Najuta mpenzi wangu kukubali kitu nisichokijua, Atuganile alisema huku akilia kilio cha majuto.
Ambakisye alimbembeleza mpenzi wake na kumuomba waendelee na safari yao ya kwenda kumuona bibi Tumwambilile.
SASA ENDELEA...
Walikubaliana kuondoka kwenda kwa bibi kwa kupitia kilabuni kwa Mwangibile kununua chimpumu ya lita mbili na kwenda nayo.
Walikwenda hadi kwa bibi Tumwambilile, walipofika walikuta hakuna mtu ila mlango upo wazi na katikati ya mlango kulikuwa na paka mweusi.
Kwa vile Atuganile alikuwa amepazoea pale, walipofika alimwita kwa sauti ya juu huku akiingia ndani na kumuacha Ambakisye nje.
Bibiiii Tumwa.
Alimpita yule paka mweusi mlangoni na kuingia mpaka ndani na kuendelea kuita mpaka chumbani lakini hakukuwa na jibu la mtu, ilibidi atoke nje alipokuwa amesimama mpenzi wake na kumuita kwa sauti ya kukata tamaa.
Mmh! Hayupo.
Sasa atakuwa amekwenda wapi?
Hata najua, lakini mlango upo wazi inaonesha hayupo mbali.
Basi tumsubiri.
Mmh! Labda yupo nyuma ya nyumba.
Kamuangalie.
Atuganile alizunguka nyuma ya nyumba ya bibi Tumwambilile lakini vilevile hakumuona, alirudi na kumueleza mpenzi wake.
Hata nyuma ya nyumba hayupo.
Basi tumsubiri lazima atakuwa karibu.
Walisogea pembeni kwenye gogo na kukaa kumsubiri bibi Tumwambilile, paka aliyekuwa mlangoni alitoka alipokuwa amesimama na kuzunguka nyuma ya nyumba.
Baada ya dakika moja alitokea bibi Tumwambilile nyuma ya nyumba akiwa amejifunga kaniki nyeusi mabega nje.
Wajukuu zangu karibuni.
Kwanza walishtuka kwa vile muda mfupi hakukuwa na mtu, kisha waliitikia kwa pamoja.
Asante bibi shikamoo.
Marahaba, karibuni wapenzi.
Asante.
Nakuja, alisema huku akiingia ndani.
Baada ya kuingia ndani walijikuta wakitazamana na kila mmoja alinyanyua mabega juu. Baada ya muda alitoka bibi Tumwambilile akiwa amebadili nguo na kujifunga kitenge na kingine kujitanda juu. Alikaa kwenye kizingiti cha nyumba yake na kuwafanya Atuganile na mpenzi wake wasogee kwa kubeba kipande cha gogo cha kukalia.
Karibuni wapenzi leo naona mpo pamoja, bibi alisema huku akiachia tabasamu la kizee.
Asante bibi, waliitikia kwa pamoja.
Leo jua litawaka usiku Ambakisye kuja kwangu.
Hapana bibi, huwa napita lakini sikuoni.
Mmh! Kuna kipi kimewaleta jioni?
Bibi kama tulivyozungumza nimeona leo nije na mwenzangu.
Tulizungumza nini?
Kuhusu matatizo yetu.
Kwani nilikuambiaje?
Ulisema nisiyachimbue sana kwa vile tumeshapona.
Kipi kimebadilika?
Hali ya mwenzangu ndiyo bado inatuchanganya.
Nilikuambia nini kuhusu tatizo lake?
Ile dawa niliyopewa na mama hakutumia alisema mpaka azungumze na baba yake, jioni tulipokutana alinieleza walienda kwa Mwakasanga, Atuganile alijisahau kuwa alimwambia mpenzi wake kapewa na bibi Tumwambilile.
Yule mganga? bibi Tumwambilile aliuliza.
Ndiyo.
Ehe.
Basi kule sijui walielezwa nini na kupewa dawa nyingine ambayo kaanza kuitumia leo, kaambiwa baada ya siku tatu arudi kujua anaendeleaje. Ameniomba nije kwako ili utusaidie tujue tatizo lipo wapi.
Sasa mbona unamuongelea kama yeye hana mdomo, bibi Tumwambilile alimgeukia Atuganile aliyeongea kwa niaba ya mpenzi wake.
Amba hebu mwambie bibi ili atusaidie.
Bibi nafikiri hakuna nitakachosema tofauti na aliyoyasema mpenzi wangu. Ni kweli bibi hali yangu ni mbaya na inaonekana kabisa matatizo yetu wazazi wetu wanahusika kwa asilimia kubwa kwa kutupa dawa kwa kutudanganya matokeo yake imekuwa madhara kwetu.
Bibi nina imani wewe ni msaada mkubwa kwetu hebu tupe ukweli wa tatizo hili, japo hupendi tuchimbue lakini mambo mengi yapo wazi kwa vile kuna siri kubwa kwa wazazi wetu.
Kwani mlipokwenda kwa Mwakasanga alisemaje?
Alimwambia baba kuwa alipiga naye kapigwa.
Alipiga nini na kapigwa nini?
Inaonekana kutoka kwa ujauzito wa Atu, ulitoka katika familia yangu na mimi ndiye niliyemuua mwanangu bila kujua. Na hii hali niliyonayo inatoka katika familia ya mpenzi wangu naye aliniuliza bila kujua kama hali hii itanitokea. Pia alimuuliza kama ilikuwa wanalipa kisasi alijibiwa kuwa upande wa pili ndiyo wanajiandaa kulipa kisasi sasa sijui kisasi cha nini na kisasi gani.
Alimwambia kuwa vita ya familia mbili haitapata mshindi zaidi ya kubakisha magofu, suluhu ni familia mbili kukaa chini kumaliza tofauti zake. Kwa hiyo bibi naomba msaada wako.
Msaada upi?
Kwanza kupata ukweli ya ninayowaza juu ya wazazi wetu, kipi kilipigwa toka pande zote. Na mwisho naomba kama yote ninayo yawaza yapo sawa basi wewe ndiyo usimame katikati kuiokoa vita ambayo naamini haina mshindi zaidi ya kufa wote.
Itaendelea kesho............